Wajumbe wa Kamati ya Bajeti wameibana serikali na kufanikiwa kupunguza zaidi ya Sh. bilioni 200 katika Bajeti Kuu ikiwamo matumizi ya anasa.
Katika kikao hicho kilichoanza tangu juzi, wajumbe hao wamepunguza maeneo ya anasa na safari za Rais zaidi ya Sh. bilioni 15 kwa mwaka 20/14/15.
Vyanzo vyetu vya habari vya kuaminika vilisema kuwa Rais mwaka huu (2013/14), alipangiwa bajeti ya Sh. bilioni 15, lakini ametumia karibu Sh. bilioni 50.
Chanzo hicho pia kilisema wajumbe wamepambana na kuipunguzia Ikulu Sh. bilioni 11.
Kilisema matumizi ya anasa kama kununua samani za ofisi na safari za mara kwa mara zisizo za lazima, ndizo zinazosababisha matumizi kuongezeka.
"Tumechoka kuona matumizi ya anasa huku wizara muhimu zinazogusa maisha ya wananchi zikikosa pesa," kilisema chanzo hicho.
Aidha, alisema mwaka huu wa fedha Rais alitengewa Sh. bilioni 50, lakini wajumbe walichachamaa na kuondoa Sh. bilioni 11.
"Fedha zilizoondolewa zinapelekwa kwenye kilimo, afya na hasa suala la MSD," kilisema chanzo hicho.
Alisema Wizara ya Afya iliomba Sh. bilioni 145, lakini serikali ikaitengea Sh. bilioni 45 tu.
"Sisi tumepambana mpaka zifike Sh. bilioni 95," alisema.
Aidha, chanzo hicho kilisema wajumbe wamepambana ili kuongeza posho za madiwani zifikie zaidi ya Sh. bilioni tano na mifuko ya maendeleo ya vijana ifikie zaidi ya Sh. bilioni 10.
"Serikali walikuwa hoi na usiku huu wanakwenda kukutana kwenye kikao na JK," kilisema chanzo hicho.
Hadi tunakwenda mitamboni wajumbe hao walikuwa bado wakiendelea na kikao hicho.