Edo Kumwembe: De Gea alivyosalitiwa na miguu badala ya mikono

Oldmantz

JF-Expert Member
Jan 24, 2023
430
996
MVINYO wa Nebiollo unaopatikana Italia ndio mvinyo ambao unasindikwa katika chupa kwa muda mrefu zaidi duniani. Miaka 20. Kadri unavyozeeka ndivyo unavyokuwa mtamu. Unanywewa na matajiri kama kina Sir Alex Ferguson.

Katika huu mchezo wa kihuni unaoitwa soka, wachezaji wanaolinda lango maarufu kama makipa wamepachikwa jina la mvinyo. Kwamba kadri wanavyoendelea kucheza ndivyo wanavyokuwa wazuri. Ndivyo wanavyokuwa watamu.

Juzi nilikuwa nasoma mahala kwamba katika umri wa miaka 45 kipa mkongwe wa Italia, Gianluigi Buffon (Gigi Buffon) amepokea ofa ya kwenda kucheza Saudi Arabia kwa dau la Pauni 25 milioni kwa mwaka.

Mpaka sasa Buffon anacheza katika klabu ya Parma ya Italia ambayo ipo Serie B.
Edwin Van De Sar aliichezea Manchester United mpaka alipotimiza miaka 37. Orodha hii ni ndefu. Makipa wengi bora wanaocheza katika timu kubwa huwa wanaachia kamba katika umri mkubwa. Wengi wanaondoka katika umri wa miaka 35 na kuendelea.

Bahati hii haijamtokea mchezaji anaiyeitwa David de Gea. Hapa miaka ya katikati aliibeba Manchester United vilivyo kiasi kwamba aliwahi kuwa mchezaji bora wa Manchester United kwa misimu mitatu mfululizo. United pia ilionekana kuwa hoi. De Gea akabakia kuwa jeshi la mtu mmoja.

Bahati mbaya kwa De Gea ni kwamba hapa katikati wametokea ‘wendawazimu’ wenye akili ambao ni wajuaji zaidi ambao wanataka kipa awe bora katika kutumia miguu wakati mwingine kuliko anavyoweza kutumia mikono yake. Jambo la kushangaza sana.

Wahuni hawa wanaongozwa na Pep Guardiola. Wanataka kipa awe hodari katika kuanzisha mpira kutoka nyuma. Hakuna kubutua. Ukirudishiwa hata kama kuna mchezaji wa adui hatua tatu kutoka ulipo bado unalazimika kujaribu kupiga pasi kwa wachezaji wako.

Lakini hata kama unataka kuanzisha mpira ulio salama na maadui wamekabia mbele, bado unalazimika kuanzisha kwa mabeki wako haohao halafu mpira uende taratibu kwa njia zake.

Kuna makipa wamebarikiwa kuwa na umiliki mkubwa wa mipira miguuni, De Gea sio mmojawao.

Kiwango chake cha kucheza michomo kipo palepale. Sawa kuna wakati anafungwa mabao ya kizembe lakini ni machache kuliko michomo mingi anayookoa ambayo inaiweka Manchester United mchezoni. Hata hivyo wamekuja wahuni wapya ambao wanatuambia De Gea hatumii miguu yake vizuri.

Wazungu wanatubabaisha sana. Wanatuyumbisha kadri wanavyojisikia. Zamani waliutengeneza mpira katika namna ambayo hata wachezaji wasiokuwa na vipaji vikubwa wangeweza kucheza. Hawa ndio kina Sol Campbell.

Siku hizi wanataka hata mabeki wacheze kama viungo. Rafiki zangu kina Sol Campbell, sijui Phil Neville walikuwa hawana umiliki mkubwa wa mpira mguuni. Kilichowaokoa ni uwezo mkubwa wa kukaba na kisha kuwapa mpira watu wenye vipaji.

Hawa kina Guardiola wanataka hata na wao pia wawe na uwezo mkubwa wa umiliki wa mpira. Wapokee mpira kutoka kwa kipa wakiwa karibu kabisa na kipa. Wamrudishie. Wapasiwe tena. Wageuke na kupiga pasi ya karibu huku timu ikisonga mbele. hakuna kubutua.

Sijui kama kina Sol Campbell wangeuweza huu mpira wa kisasa unaochezwa na kina William Saliba. Sijui. Lakini afadhali mambo haya yangeishia kwa wachezaji wa ndani. Yamekuja pia kwa makipa. Hapa ndipo katika umri wa miaka 32 tu De Gea ameagwa Manchester United.

Wakati ule mikono ikiwa lulu kuliko miguu, De Gea alikuwa roho ya Manchester United. Aliwaweka roho juu mashabiki wa Manchester United wakati ule alipotakiwa na Real Madrid. Hali hiyo haipo tena na miguu imemsaliti De Gea.

Kuanzia sasa katika umri huu wa miaka 32 De Gea alipaswa kuwa mtamu zaidi ya mvinyo. Bahati mbaya kuna mpira wa kisasa umeingia na De Gea hayupo vizuri. Inadaiwa kwamba hata mashambulizi ya mara kwa mara ambayo United imekuwa ikishambuliwa chanzo chake tunaambiwa kwamba kinatokana na De Gea kubutua mpira mara kwa mara.

Hata Kombe la Dunia pale Qatar, De Gea aliachwa na kocha wake, Luis Enrique kwa sababu hizi hizi. Hawa ndio makocha wa Kihispaniola ambao wamekuja kutubadilishia mpira kutoka katika ule mpira ambao tuliuzoea na kuupenda.

Hawa kina Pep wamekuwa wahuni katika kila eneo. Pep ndiye alikuwa kocha wa kwanza timu yake kucheza bila ya mshambuliaji huku washambuliaji wakiwa nje.

Kamuulize David Villa akiwa na Barcelona. Kuna wakati alikuwa anasugua benchi huku Cesc Fabregas akianza kama mshambuliaji.

Tazama mfumo mwingine ambao wanatuletea sasa hivi
Mlinzi wa kushoto anaingia katikati ya uwanja na kucheza kama kiungo. Pale Arsenal, Mikel Arteta amefundishwa tabia hii na Pep. Zinchenko anaingia katika kucheza kama kiungo kama Arsenal ina umiliki wa mpira.

Matokeo yake mmoja kati ya walinzi bora wa pembeni waliokuwa wanakuja juu, Kieran Tierney anakaa benchi. Kisa? Sio mzuri sana katika mfumo huo. Kama ingekuwa katika mfumo wa kawaida naamini kwamba Tierney ni bora zaidi ya Zinchenko.

Hiki ndicho kinachomtokea De Gea kwa sasa. Manchester United wametoa ofa ya kumchukua kipa wa Inter Milan, Andre Onana. Kisa? Ni mzuri katika matumizi ya miguu. Siamini kama Onana ni mzuri sana katika michomo kushinda De Gea.

Hatimaye rafiki yetu De Gea anaondoka zake. Kwangu anabaki kuwa mmoja kati ya makipa bora kuwahi kuwaona katika uso wa ulimwengu. Bahati mbaya mpira wa kisasa umemuondoa katika timu kubwa mapema. Anaweza kwenda kucheza kwa baadhi ya makocha ambao hawaamini sana katika falsafa za kina Pep. Tatizo naanza kuona makocha wengi wakiamini falsafa hizi.

Kitu pekee ambacho siwezi kumlaumu ni pale ambapo ataamua kwenda kwa Waarabu kufuata noti zake. Ameshinda mataji mengi ambayo mchezaji anatamani kuyashinda. Hakuna kikubwa alichobakiza. Huu ni muda wa kwenda kuchota noti za Waarabu.

Kila la heri kwake. Hatukutegemea kama angeondoka kirahisi Manchester United katika umri wa miaka 32. Wana bahati rafiki zetu kina David Seaman, Peter Schmeichel na wengineo ambao hawakujaribu uwezo wa miguu yao. Labda sio ajabu wasingedumu muda mrefu katika klabu ambazo walitamba nazo kwa muda mrefu.

CREDIT: MWANASPOTI
 
Pep alikuja na offensive GK Claudio Bravo alikiona.

Hii ngoma ingemkuta wodi klasi Magwaya Onana angeona matendo makuu ya Beki Ghali.

Dave saves aachane na wahuni.
 
Kwa jinsi Eric ten hag anavyo wa treat vibaya ma legend wa Manchester United sijui kama atakuwa na mafanikio makubwa kama watu wanavyotarajia alianza na Ronaldo akafuata David degea sasa hivi kibao kimegeuka kwa Maguire.
 
SIDHANI.

KOCHA anasafisha timu yooote.

ALTETA ALIWATIMUA AKINA AUBEMEYANFG, OZIL, LAKAZET NK.
 
Back
Top Bottom