Dr Shika amekamilisha leo malipo ya bima kwa ajili ya kutumiwa fedha zake kutoka nchini Urusi



Dk Louis Shika, ambaye alijizolea umaarufu baada ya kushinda zabuni ya kununua nyumba tatu za kifahari kwa takriban Sh3 bilioni lakini akashindwa kulipa asilimia 25 ya fedha hizo, amedai ameanza mchakato wa kurejesha fedha zake zilizo nje ya nchi.


Dk Shika amedai leo Jumamosi Novemba 18,2017 kuwa amelipa dola 100 za Kimarekani (sawa na Sh220,000 za Kitanzania) kwa ajili ya bima ili aweze kutumiwa fedha zake nchini.


Waandishi wa habari waliokuwa katika ziara ya Naibu Waziri wa Uchukuzi na Mawasiliano, Atashasta Nditiye aliyeenda Shirika la Posta kuzungumza na wafanyakazi, walimkuta Dk Shika akiwa katika shirika hilo na walipozungumza naye alisema alifika hapo kwa ajili ya malipo.


Dk Shika, ambaye alishikiliwa na polisi kwa ajili ya mahojiano akituhumiwa kuvuruga mnada wa nyumba hizo za mfanyabiashara wa jijini Dar es Salaam, Said Lugumi, alisema ametumia shirika hilo kulipa fedha hizo za bima kwa benki moja iliyoko Bangkok, Thailand.


"Kama mnavyoona hii karatasi,” alisema akionyesha fomu ya malipo.
“Nimelipa dola 100 za bima ili kukamilisha fedha zangu zije na nilipie zile nyumba. Hili la bima lilikuwa ni muhimu sana."


Hata hivyo, moja ya nyumba hizo tatu ilishauzwa kwa mshindi wa pili kwenye mnada huo, wakati kampuni ya udalali ya Yono imesema itaendesha mnada mwingine kuuza zilizosalia.


‘Bilionea’ huyo hakueleza fedha alizolipia ni kwa ajili ya kuingiza nchini kiasi gani cha fedha.
Dk Shika amesema bado anaamini kwamba nyumba hizo atazimiliki ili kuwaziba mdomo wale wote wanaombeza kwamba hana fedha.
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…