Donatila
JF-Expert Member
- Oct 23, 2014
- 8,247
- 25,191
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), Dk. Willibrod Slaa, akihutubia wananchi wa kijiji cha Ludewa Wilaya ya Kilosa mkoani Morogoro katika mkutano wa Operesheni Delete CCM uliofanyika katika Uwanja wa Shule ya Msingi Ludewa juzi
Katibu Mkuu wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chedema) Dk. Willibrod Slaa, amemuweka njia panda Mkuu wa Wilaya ya Kiteto mkoani Manyara, Martha Umbulla, baada ya kumuomba Rais Jakaya Kikwete amfukuze kazi kwa madai ameshindwa kuzuia mapigano ya wafugaji na wakulima ambayo hadi sasa yamesababisha vifo vya watu zaidi ya 10.
Akizungumza katika mkutano wa hadhara uliofanyika kijiji cha Mvuha mkoani Morogoro, alisema kama Rais Kikwete hatamchukulia hatua Mkuu huyo wa wilaya wananchi wanaoona damu ikimwagika hawawezi kumwelewa.
Dk. Slaa aliwaomba wakulima na wafugaji kuacha kupigana na kuuana wakigombea ardhi badala yake waiwajibishe Serikali ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) kwa madai ndiyo chanzo cha migogoro ya ardhi inayoendelea nchini.
"Migogoro ya ardhi inayoendelea nchini ni matokeo ya serikali ya CCM kushindwa kuwajibika ipasavyo hasa katika kuweka mipango mizuri ya matumizi ya ardhi ambayo ni majukumu ya serikali za mitaa," alisema.
Dk Slaa ambaye jana alianza ziara ya chama hicho iliyopewa jina la ‘Operesheni Delete CCM' akimpokea Mwenyekiti wa Chadema Taifa, Freeman Mbowe, alisema kutoka na chama tawala kushindwa kuweka sera nzuri za ardhi hivyo imefika wakati kwa wananchi kuchukua hatua ya kufanya mabadiliko.
Alisema kuwa umwagikaji wa damu huo usipodhibitiwa na migogoro hiyo kutafutiwa ufumbuzi wa kudumu, Serikali itakuwa imeshindwa moja ya majukumu yake ya msingi ya kulinda raia wake na mali zao.
"Tunavyozungumza hivi sasa kuna matukio ya kutisha yametokea huko Kiteto, Siha, Malinyi na kwingine,wakulima na wafugaji…ninyi wote ni Watanzania. Nawaomba sana muendelee kuishi kama ndugu kama ilivyokuwa huko nyuma," alisema.
"Haya ni matokeo ya Serikali kushindwa majukumu yake. Ni matokeo ya sera za CCM kushindwa. Mipango na matumizi mazuri ya ardhi, ili ardhi ya mifugo ijulikane na ardhi ya kilimo ijulikane na matumizi mengine ni kazi za serikali za mitaa kupitia halmashauri," alisema.
Dk. Slaa alisema chanzo cha mauaji yanayoendelea Kiteto ni baadhi ya wanasiasa wanaoongoza wilaya hiyo akiwamo Mkuu wa Wilaya, Mwenyekiti wa Halmashauri ya Wilaya na mbunge ambao wameshindwa kuwajibika ipasavyo.
CHANZO: NIPASHE