nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Wednesday, 06 June 2012 21:15 |
Geofrey Nyang'oro CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema) jana kilizindua vuguvugu la mabadiliko (M4C) katika Mkoa wa Lindi huku kikimtaka Mbunge wa Jimbo la Lindi Mjini (CUF), Salum Barwani kujiunga na chama hicho. Katika siku hiyo ya kwanza, Chadema kilimnasa aliyekuwa meneja wa kampeni wa mbunge huyo, Abdallah Madebe. Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe alisema mbunge huyo kwa sasa na wabunge wenzake wa CUF wamekuwa hawana sauti ya kutetea wananchi ndani ya Bunge kwa kuwa uongozi wa juu wa chama hicho umeungana na CCM. Mbowe alimkaribisha mbunge huyo baada ya wananchi wa Kata ya Nng'apa, kusema Barwani amefuatilia baadhi ya malalamiko yao ya muda mrefu lakini, juhudi zake zinakwamishwa na Mkuu wa Mkoa wa Lindi na madiwani wa Halmashauri ya Manispaa ya Lindi. Malalamiko mengine ya wananchi hao yalikuwa mfumuko wa bei, kukosa huduma za afya na wanafunzi kutozwa Sh20,000 kwa ajili ya ulinzi wa shule za Serikali. Mkazi wa Kata ya Ng'apa, Rashid Issa alimweleza Mbowe katika mkutano huo kuwa hajui hatima ya maisha yao kutokana na mfumuko wa bei unaojitokeza kila wakati huku wakiendelea kutozwa kodi katika vivuko vya mazao na fedha hizo kuishia mikononi mwa wajanja. Akijibu hoja hizo, Mbowe alisema maisha magumu kwa Watanzania ni matokeo ya sera mbovu za Serikali ya CCM katika kusimamia uchumi wa nchi. Akimzungumzia Barwani, Mbowe alisema katika mazingira ya sasa ya CUF, mbunge huyo hatakuwa na uwezo wa kuwasaidia wananchi kwa sababu viongozi wa juu wa chama hicho, akiwamo Mwenyekiti, Profesa Ibrahim Lipumba na Katibu Mkuu, Seif Sharif Hamad ndiyo wanaofanya uamuzi na ‘wamekiunganisha' chama hicho na CCM. "Sina ugomvi na Barwani, ni mbunge na tunafanya naye kazi vizuri, tatizo ni misimamo ya viongozi wake wakuu. Hawa ni tatizo kwake. Ninamshauri ajitathmini na huku kwetu mlango uko wazi, anaweza kuusukuma na kuingia kwa ajili ya kuwatetea wana Lindi," alisema Mbowe. Mbowe aliwataka wakazi wa Lindi kutowavumilia viongozi wazembe ambao hawawezi kuwaelezea kodi zao zimetumika vipi, wakati wao wanashindwa kupata huduma za msingi. Slaa na polisi Akizungumza katika mkutano uliofanyika katika Uwanja wa Ilulu mjini hapa, Katibu Mkuu wa Chadema, Dk Willibrod Slaa aliwataka polisi wasipate tabu ya kurekodi mikutano yao, bali fedha wanazonunulia kanda za kurekodia wazitumie kuboresha maisha yao. Dk Slaa alidai kwamba katika mikutano ya Chadema, askari wamekuwa wakijaa kwa wingi kwa lengo la kusikiliza yanayozungumzwa ili wawafikishie mabosi wao. "Ninyi askari mnanishangaza sana ufisadi umejaa kila sehemu, badala ya kushughulika nao ninyi mnakuja kurekodi ili mseme tunachochea vurugu..." alisema Dk Slaa.Alisema atakachoweza kuwasaidia askari ni kuhakikisha kuwa mishahara yao inaongezwa baada ya mwezi wa saba. Lema amshangaa Membe Kwa upande wake, aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema alisema Waziri wa Mambo ya Nje na Uhusiano wa Kimataifa, Bernard Membe amepoteza sifa ya kufikiria kuwa kiongozi wa nchi kutokana na kushindwa kuusaidia Mkoa wa Lindi kuondokana na umaskini. Alisema kama Membe angekuwa kiongozi makini, angetumia fursa yake ya kusafiri nje kila wakati kutangaza vivutio vya Mkoa wa Lindi na kuufanya uwe mji wa kitalii kama mikoa mingine inayosifika kwa utalii Tanzania. Mnyika awashtukia wabunge CCM Mbunge wa Ubungo, John Mnyika alisema kama Rais Jakaya Kikwete asipopeleka bajeti yenye kupunguza mfumuko wa bei katika Bunge lijalo, Chadema itahamasisha nguvu ya umma kumshinikiza afanye hivyo. Alisema kauli inayotolewa na wabunge wa CCM kuwa wataigomea Bajeti ijayo ni ya kujikosha mbele ya jamii kwa kuwa wanajua wazi kuwa hilo haliwezekani kulingana na katiba waliyonayo. "Hawa wanasema wataipinga Bajeti wakati wana hamu ya kupokea posho za bungeni mbona wanajidanganya kwa kuwa wakifanya hivyo Rais atavunja Bunge na kwa hofu ya matendo yao, wengi wanajua hawataweza kurudi hivyo hizo ni propaganda tu," alisema Mnyika. Sugu na ajira za vijana Mbunge wa Mbeya Mjini, Joseph Mbilinyi (Sugu) alisema wakati anaelekea Mtwara akiwa ndani ya ndege alijua mikoa hiyo ya kusini ni ya kupigiwa mfano kutokana na aina ya watu aliokuwa nao katika ndege, kwamba hata vijana wa Mkoa wa Lindi watakuwa wananufaika na rasilimali za mkoa huo. "Nilipotua nikawauliza kama vijana mnanufaika na gesi inayopatikana katika mikoa yenu? Cha ajabu mnaniambia kuwa mnachopata ni vifaa vya kukingia kifua tu." |