CHAMA Cha Mapinduzi (CCM) kimekiomba Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kukutana na kufanya maamuzi ya pamoja yatakayosaidia kuzuia ulipaji wa tuzo kwa Kampuni ya kufua umeme ya Dowans.Katibu wa Halmashauri Kuu ya CCM (NEC), Itikadi na Uenezi, Nape Nnauye, alisema kwa kuwa sakata la malipo ya Dowans linawagusa Watanzania wote itakuwa vema iwapo CHADEMA itakubali kukaa meza moja na wao ili kujadiliana namna ya kupata njia muafaka ya kuzuia malipo hayo.Akijibu maswali ya waandishi wa habari katika ofisi ndogo za CCM, Lumumba jijini Dar es Salaam jana, Nnauye alisema kama CHADEMA wana nia ya dhati ya kutaka Dowans isilipwe, basi waunganishe nguvu bila kujali tofauti za kiitikadi katika suala hilo linalogusa uhai wa taifa.CHADEMA ni lazima wajue maandamano si njia ya kudai kila jambo
sisi tunasema ni vema tukae pamoja ili tujadili suala hili kisheria kwa sababu nasi tunaunga mkono msimamo wa serikali kupinga malipo haya, alisema mwanasiasa huyo.Alisema CHADEMA watafanya jambo jema na la msingi ikiwa wataungana na Tanesco kupinga tuzo hiyo kwa kuwasaidia ushauri wa kisheria kuliko wanavyotaka kufanya maandamano ya nchi nzima.Akizungumzia kauli hiyo ya CCM, Katibu Mkuu wa CHADEMA, Dk. Willibrod Slaa, alisema ingawa wazo la Nape ni zuri, limekuja likiwa limechelewa, hivyo akakishauri chama hicho tawala kuungana na chama chake katika maandamano yao.Serikali iliyopo madarakani imetokana na wananchi kwa mujibu wa Ibara ya 8 ya Katiba ya Tanzania. Kama kweli wana nia hiyo, nawashauri kwanza sote tushiriki katika maombolezo ya kitaifa ya Oktoba 14 kama wanaharakati walivyosema, na waje tuandamane kwa pamoja, akiwamo Sitta na wenzake ambaye amesema anayaunga mkono, alisema Dk. Slaa.Kiongozi huyo wa CHADEMA alisema msimamo wao kwa sasa ni kuwahimiza Watanzania kuwaunga mkono wao na wanaharakati katika maandamno hayo.Lakini la pili na kubwa, tunaitaka serikali kuwakamata wote waliohusika kuingiza taifa katika ufisadi huu wafilisiwe ili mali zao zifidie deni hilo. Kama Nape na CCM yake wana uchungu na Watanzania, waungane nasi kuhakikisha fedha hizo hazilipwi na wahusika wanakamatwa, alisema Dk. Slaa.