gimmy's
JF-Expert Member
- Sep 22, 2011
- 3,311
- 3,341
Zoezi la kubomoa nyumba zilizojengwa kwenye maeneo yasiyo ruhusiwa kisheria linatarajiwa kuhamia mkoani Arusha wakati wowote kuanzia sasa na wananchi wakiwemo waliojenga kwenye vyanzo vya maji wameshaanza kupewa taarifa.
ITV imeshuhudia kazi ya kuweka alama kwenye nyumba zilizojengwa kwenye vyanzo vya maji katika wilaya ya Arumeru zikiwekewa alama na wananchi wakitakiwa kuanza kuzibomoa wenyewe ili kunusuru mali zao.
Hata hivyo baadhi ya wananchi hao wameiomba serikali kutumia vyombo vyake kuwawajibisha watendaji wa serikali waliochangia na kuruhusu maeneo yasiyoruhusiwa kisheria kujengwa na ikiwezekana walipe hasara inayojitokeza kwani wamefanya hivyo wakiwa wanajua wazi kuwa ni kosa.
Baadhi ya viongozi wa kata ikiwemo ya Kerai, Bw John Edward ambaye ni diwani pamoja na kukiri kuwepo kwa watendaji wanaoshiriki kuwasababishia wananchi hasara ameitaka serikali kuangalia namna ya kuwasaidia wananchi ambao walikuwepo kwenye maeneo hayo kabla ya sheria kupitishwa.
Arumeru ndio wilaya yenye vyanzo vya maji vinavyotegemewa na asilimia kubwa ya wananchi wa jiji la Arusha, na wilaya za jirani ikiwemo Monduli na Longido na ni miongoni mwa zinazokabiliwa na tatizo kubwa ya uharibifu wa mazingira.
================
Arusha. Zaidi ya wakazi 3,000 wa Kata ya Kiranyi Wilaya ya Arumeru mkoani hapa, wameamriwa na Mamlaka ya Bonde la Pangani kwa kushirikiana na Mamlaka ya Maji ya Mji Mdogo wa Ngaramtoni kubomoa nyumba zao kwa kujenga kwenye chanzo cha maji.
Meneja wa Mamlaka ya Maji Mji Mdogo wa Ngaramtoni (Ngauwsa), Clayson Kimaro alisema nyumba ambazo zimewekwa alama ya X zinazotakiwa kubomolewa kwa kuwa ziko ndani ya mita 60 kutoka kwenye chanzo hicho ambacho kwa mujibu wa sheria hazipaswi kuwapo.
Alisema wakazi hao wamekiuka Sheria ya Mazingira namba 20 ya mwaka 2004 na Sheria ya Usimamizi wa Rasilimali Maji namba 11 ya mwaka 2009 inayozuia maendelezo ya ujenzi na kilimo kwenye eneo la mita 60 kutoka kingo za maji.
Ofisa wa Bonde la Pangani mkoani Arusha, Joel Lao alisema kulinda vyanzo vya maji ni wajibu wa kila mwananchi kama inavyotamkwa kwenye Sera ya Maji ya mwaka 2002 na kazi ya mamlaka ya bonde hilo ni usimamizi wa sheria.
Alisema athari za kuwapo kwa shughuli za kibinadamu kwenye vyanzo vya maji zinaweza kuvikaviusha na kusababisha magonjwa ya milipuko yanayosababishwa na maji machafu kutiririkia kwenye vyanzo vya maji.
Baadhi ya wakazi hao, Hashim Kassimu na Mwanamkuu Shabani walisema unalenga kuwarejesha katika umaskini kutokana na kudunduliza fedha na kujenga makazi yao sehemu hiyo.
“Umaskini unatunyemelea upya. Tunaanza upya maisha,” alisema Kassimu.
Diwani wa Kata ya Kiranyi, John Seneu alisema wakazi hao wanaodaiwa kuvamia eneo hilo walinunua na kupata vibali kutoka Serikali za vijiji na wengine walizaliwa maeneo hayo, hivyo Serikali itumie busara kufanya uamuzi.
Chanzo: Mwananchi
Last edited by a moderator: