Yatokanayo na Kamati Kuu ya CHADEMA-Tamko Rasmi la Chama

Regia Mtema

R I P
Nov 21, 2009
2,970
863
CHAMA CHA DEMOKRASIA NA MAENDELEO
(CHADEMA)

Taarifa kwa Umma kuhusu maamuzi ya Mkutano wa Kamati Kuu ya CHADEMA

Kilichofanyika Markham Hotel, Dar-Es-Salaam 19 Machi, 2011:


A: Utangulizi

Kamati Kuu ilifanya Kikao Maalumu siku ya Jumamosi, tarehe 19 Machi 2011 kwa mujibu wa Katiba ya Chadema, Ibara ya 6.2.2. Katika kikao hiki maalumu, pamoja na mambo mengine, Kamati Kuu ilipokea taarifa ya hali ya siasa na jamii hapa nchini, ikitilia manani zaidi taarifa ya maandamano yaliyofanyika katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa mwezi Februari/Machi 2011 na matukio yaliyojiri baada ya hapo, zikiwemo kauli mbalimbali zilizotolewa na viongozi wa Serikali na CCM kuhusu maandamano hayo. Baada ya mjadala wa kina, Kamati Kuu imeyatolea maoni na maamuzi mambo mbalimbali yaliyojadiliwa kama ifuatavyo:

B: Kuhusu Maandamano katika Kanda ya Ziwa


1.
Kamati Kuu imewapongeza kwa dhati Sekretariati ya Chama, viongozi wa Chama wa kitaifa na mikoa iliyopo katika Kanda ya Ziwa , na wapenzi na Wananchi wote wa Mikoa ya Kanda ya Ziwa, kwa kutekeleza kikamilifu na kwa ufanisi azimio la Kamati Kuu la kufanya maandamano katika Kanda ya Ziwa. Aidha Kamati Kuu imepokea Taarifa kuwa Maandamano hayo kwa ujumla yalifanyika kwa amani bila vurugu yeyote, jambo linalidhihirisha wazio kuwa “maandamano ya amani yasipoingiliwa na Vyombo vya dola yanaweza kufanyika kwa amani, na kuwapa fursa Watanzania kueleza hisia zao kwa Serikali yao bila uwoga wala hofu. Aidha , Kamati Kuu ilizingatia kuwa maandamano haya yalikuwa na malengo mahususi manne kama ifuatavyo:-

a)
Kuishinikiza serikali ya CCM kuachana na mpango wake wa kuilipa Kampuni ya Dowans Sh 94 bilioni kufuatia hukumu iliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Biashara (ICC).
b) Kuishinikiza serikali kuhakikisha kuwa mgao wa umeme na bidhaa mbalimbali inashuka na mgawo wa umeme unaisha ili kuwapunguzia wananchi adha ya ugumu wa maisha
c) Kushinikiza mamlaka husika kuhakikisha kuwa uchaguzi wa Meya Arusha unafanyika kwa mujibu wa sheria
d) Kutaka Waziri wa Ulinzi na Jeshi la Kujenga taifa awajibike kutokana na matukio ya milipuko ya mabomu katika maghala ya Jeshi Gongolamboto.

2.
Kamati Kuu imewapongeza wabunge wa CHADEMA kwa kutoa michango ya kifedha iliyofanikisha maandamano hayo kwa kuchangia jumla ya shilingi milioni 19. Aidha Kamati Kuu inawapongeza kwa dhati Wabunge wa Chadema, viongozi wote wa ngazi mbalimbali na wananchi wote ambao kwa hiari yao walishiriki kikamilifu katika maandamano hayo.

3.
Kamati Kuu ilipokea na kujadili kwa umakini tathmini ya maandamano yaliyofanyika Kanda ya Ziwa, pamoja na matamko yaliyotolewa na viongozi wa Serikali na CCM, wakiwemo Rais Kikwete, Mawaziri Membe, Wasira na Sophia Simba na Katibu wa Itikadi na Uenezi wa CCM John Chiligati. Mambo mawili yamejitokeza katika kauli za viongozi hawa:
a) Kwamba maandamano ya CHADEMA yanahatarisha amani ya nchi kwa kuchochea wananchi kuitoa serikali iliyopo madarakani kwa njia ya maandamano
b) Kwamba CHADEMA inafadhiliwa na mataifa ya nje kufanya maandamano hayo.

4.
Kamati Kuu imesikitishwa na kauli zilizotolewa na viongozi hao wa serikali na CCM, ambazo zinaashiria kuwa viongozi wa CCM hawajui maana na kazi za vyama vya upinzani. Na hii inaeleweka kwa kuwa hawajawahi kuwaza kuwa chama cha upinzani. Kamati Kuu inapenda umma uelewe kuwa:-

a)
Maandamano ya CHADEMA katika Kanda ya Ziwa yalifanyika kwa mujibu wa sheria na taratibu zote za nchi na yalikuwa na amani tele. Kamati Kuu inaipongeza Jeshi la Polisi pale ambapo haikuingilia pasipo lazima maandamano hayo kitendo ambacho kilikuza amani na utulivu katika maandamano.

b)
Malengo ya maandamano yalianishwa waziwazi kabla, wakati na baada ya maandamano hayo na kama yalivyotajwa hapo juu. Kauli za Rais Kikwete kwamba maandamano haya yalilenga kuiondoa serikali iliyo madarakani kwa njia zisizo za kidemokrasia ni uzushi na uwongo. Wasiwasi na hofu aliyo nayo Rais Kikwete ni kushindwa kwake kutekeleza yale aliyowahidi wananchi. Aidha, inawezekana kabisa Amani anayoamini kuvurugukika ni Amani ya CCM na viongozi wake ambao kwa miaka yote walizoea kuishi kana kwamba nchi ni mali yao badala ya kujiona “watumishi wa wananchi waliowachagua kuwaongoza”.

c)
Kamati Kuu imesisitiza kuwa CHADEMA ni chama cha kidemokrasia na kitaendelea kutafuta ridhaa ya wananchi ya kuunda serikali kwa njia za kidemokrasia na kwa mujibu wa sheria za nchi na wala haina dhamira ya kuiondoa Serikali kwa njia zisiozo za kidemokrasia.

d)
Operesheni zote za kisiasa za CHADEMA hugharamiwa kwa njia ya michango ya viongozi na wanachama pamoja na ruzuku ambayo chama hupokea kutoka serikali kuu. CHADEMA haijawahi na wala haina mpango wa kupokea fedha kutoka kwa mataifa ya nje kwa ajili ya kufanya maandamano. Madai yaliyotolewa na viongozi wa serikali na CCM kwamba maandamano haya yalifadhiliwa na nchi za nje ni uzushi na uongo yaliyotolewa kwa lengo la kukichafua chama mbele ya macho ya wananchi. Mbinu za kisiasa kama hizi ni chafu na haziwezi kuiponya CCM na magonjwa inayougua. Ukweli ni kwamba CCM imechokwa na wananchi na kuondoka kwake madarakani ni swala la muda tu.

5.
Kamati Kuu imewapongeza sana wananchi wa Kanda ya Ziwa kwa jinsi walivyojitokeza katika kushiriki maandamano ya CHADEMA. Kamati Kuu imewashukuru wananchi kwa imani waliyo nayo kwa CHADEMA na inawaahidi kuwa tutaendelea kutetea haki zao na kupigania maslahi ya Taifa kikamilifu bila woga wala hofu.

6.
Kamati Kuu imetambua kuwa Rais Kikwete ameanza kutekeleza,angalau kwa “maneno” madai ya msingi yaliyotolewa katika maandamano ya CHADEMA, ikiwemo kufikiria kuchukua hatua za kushusha bei ya sukari na gharama za umeme. Kamati Kuu inamhimiza Rais Kikwete na serikali yake wasiwe wazito wala wasione aibu wa kutekeleza yale yote ambayo CHADEMA inawashauri na yenye manufaa kwa nchi lakini wayatekeleze kwa ukamilifu na ufanisi badala ya kufanya ‘kiini macho’. Watanzania wana haki ya kudai “maisha Bora” kwa kuwa wameahidiwa muda mrefu na Serikali na ni wajibu wa Serikali kufanya hivyo kwa kuwa inawatoza kodi wananchi. Kodi ni lazima ziendane na huduma inayolingana, na Rasilimali za Taifa ni lazima kwanza ziwanufaishe wananchi wenyewe na si vinginevyo.

C: Maandalizi ya Ziara na Maandamano katika Kanda ya Nyanda za Juu Kusini

7. Kamati Kuu imeiagiza Sekretariati ya ya Kamati Kuu ya CHADEMA kuendelea na maandalizi ya ziara ya kuwashukuru wananchi na maandamano katika mikoa ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, kwa kuanzia na Mkoa wa Mbeya. Kamati Kuu imeagiza kuwa maandamano haya yafanyike kuanzia Tarehe 04 Mei 2011. Katika ziara na maandamano ya Mikoa ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini, mambo yafuatayo yatafanyika:
a) Kuwashukuru wananchi kwa kura za urais, ubunge na udiwani
b)Kuendelea kuishinikiza serikali kuchukua hatua zaidi katika kupunguza adha ya gharama za maisha kwa wananchi. Hususani, ziara na maandamano ya Kanda ya Nyanda za Juu Kusini yatatumika kushinikiza kushushwa kwa bei za bidhaa muhimu za unga, mchele, umeme, mafuta, sukari na maharage. Bidhaa hizi zinatumika na wananchi wa kawaida. Kamati Kuu inaitaka Serikali itambue kuwa hakuna masoko au maduka ya wananchi wa kawaida tofauti na masoko ya vigogo. Hivyo tofauti kubwa ya kipato huwaathiri zaidi wananchi wa kawaida na hivyo ni jukumu la serikali kuhakikisha makali ya maisha kwa wananchi wake yanapungua bila kisingizio chochote kile.

D: Uchaguzi wa BAVICHA

8. Kamati Kuu imepitisha Ratiba ya Uchaguzi mdogo wa Baraza la Vijana kwa nafasi mbalimbali ngazi ya taifa, kama ifuatavyo:
a) Fomu za kugombea zitaanza kusambazwa mikoani kuanzia tarehe 23 Machi hadi 03 Aprili 2011
b) Wagombea wataanza kuchuka fomu za kugombea kuanzia tarehe 04 Aprili 2011 na tarehe ya mwisho ya kurudisha fomu ni tarehe 26 Aprili 2011.
c) Uchaguzi utafanyika katika Mkutano Mkuu wa BAVICHA uliopangwa kufanyika tarehe 28 May 2011.

E: Kuhusu Taarifa ya Vitisho vya Kuuawa kwa Dk Slaa na Viongozi

9. Kamati Kuu imepokea kwa masikitiko na tahadhari kubwa taarifa ya kuwepo kwa njama za mauaji dhidi ya Dk Slaa na viongozi wengine wa kisiasa hapa nchini iliyotolewa na Naibu Waziri wa Ujenzi, Mheshimiwa Dk Harrison Mwakyembe. Kwa kuzingatia nafasi ya mlalamikaji na ukina wa taarifa iliyotolewa, kuna kila sababu za kuichukulia tuhuma hizi kwa umakini na uzito unaostahili.

10.
Kamati Kuu imelitaka Jeshi la Polisi kuharakisha uchunguzi wa tuhuma zilizotolewa na kutoa taarifa kamili kwa umma mapema iwezekanavyo. Aidha, Kamati Kuu imelitaka Jeshi la Polisi kuhakikisha usalama wa Dk Slaa pamoja na viongozi wengine waliotajwa katika taarifa ya Dk Mwakyembe.Aidha, Kamati Kuu imesikitishwa na ukimya wa Serikali kwa ujumla kwa jambo kubwa kama hilo linalohusu maisha ya viongozi, wakati inahistoria ya kuwa na haraka ya kutoa kauli katika matukio ambayo hayana maslahi kwa umma.

F: Kuhusu swala la Meya wa Arusha

11. Kamati Kuu imepokea taarifa kuhusu hatua zilizochukuliwa na serikali katika kutatua mgogoro wa Arusha kwa kuzingatia maazimio yaliyotolewa na Kamati Kuu katika kikao chake kilichopita. Kwa kuzingatia kuwa serikali ya CCM imeziba masikio katika kusikia busara zilizotolewa na watu mbalimbali juu ya namna ya kutatua mgogoro wa umeya Arusha, ikiwemo kufanya uchaguzi wa meya kwa kuzingatia sheria na kanuni. Hivyo basi, Kamati Kuu kwa mara ya mwisho inaitaka Serikalii kumaliza mgogoro wa umeya wa Arusha ndani ya siku 21. Baada ya muda huu kwisha, CHADEMA haitakuwa na uwezo tena wa kuwazuia wananchi wa Arusha kudai uchaguzi wa meya wao kwa njia ya nguvu ya umma. Serikali isiendelee na kung’ang’ania kuwa wasioridhika waende mahakamani kwani Serikali inafahamu fika jinsi kupitia TAMISEMI na Mkurugenzi wa Manispaa ya Arusha ilivyopindisha Taratibu za Uchaguzi huo na hivyo kuuvuruga Makusudi na kuufanya uwe batili “ab initio”. Kitendo cha Serikali kuvuruga kwa makusudi Uchaguzi na kusukumiza swala mahakamani haliwezi kukubalika katika Demokrasia ya kweli. Kamati kuu inasisitiza kukataa kutengeneza “precedence” ya namna hiyo, kwani ni kiashiria mbaya kwa chaguzi zote zijazo iwapo itaachiliwe iendelee tu.

G: Kuhusu tatizo la umeme hapa nchini

12. Kamati Kuu imejadili kwa kina tatizo sugu la umeme hapa nchini na kuzingatia yafuatayo:

i)
Sekta ya nishati na madini, ikiwemo umeme, hapa nchini imegubikwa na rushwa na ufisadi mkubwa ukihusisha viongozi wa juu wa Serikali na CCM tangu mwaka 1991, wakati wa IPTL ambayo inaendelea kuitafuna nchi hadi leo. Wakati huo ikumbukwe kuwa Rais Kikwete alikuwa Waziri wa Nishati. Aidha, hali hiyo ya uzembe na ufisadi imefanya taifa kushindwa kujiondoa kwa wakati kukabiliana na upungufu wa umeme na nishati nchini.

ii)
Serikali imeshindwa kutekeleza mipango ya muda mrefu ya kulipatia taifa umeme wa uhakika. Badala yake, na hasa waziri wa nishati wa sasa, imekuwa ikitoa taarifa zenye lengo la kuwahadaa wananchi badala ya kuwaambia wananchi ukweli kuhusu upatikanaji wa umeme hapa nchini. Kwa mfano, tangu mwaka 2005 serikali ya Kikwete imekuwa ikiahidi kuwa tatizo la mgao wa umeme litakuwa historia lakini leo tatizo la mgao wa umeme limekuwa kubwa maradufu zaidi katika kipindi hiki. Hivyo basi, Kamati Kuu:

a)
imemtaka Waziri wa Nishati na Madini kuwajibika kisiasa kwa kuwa amepoteza sifa za kushikilia nafasi aliyo nayo kwa kushindwa kusimamia sekta ya umeme kwa ufanisi. Inashangaza Rais naye kushindwa kuchukua hatua, badala yake naye anaendelea kuimba wimbo huo huo.

b)
imeitaka Serikali kupitia upya haraka mikataba ya umeme hapa nchini ambayo imeliingiza taifa katika fedheha na hasara kubwa, ikiwemo mikataba ya IPTL na Songas,Artimas,Tanpower Resources /Kiwira, ikiwa ni pamoja na kuchukua hatua za kishera na kinidhamu patakapobainika uzembe au ufisadi wowote kwa wote wanaohusika, kwa mikataba iliyoisha lakini ambayo iliingiza nchi katika hasara kubwa

c)
imeitaka Serikali kuachana na mpango wake wa kukodisha mitambo ya kuzalisha umeme wa dharura kwani hatua hiyo ni kuliingiza taifa katika hasara ingine kubwa pasipo tija. Badala yake, Serikali inunue na kuwekeza kwa wakati katika mitambo mipya ya kuzalisha umeme inayotumia nishati nafuu hususani inayopatikana ndani ya nchi kama vile gesi, makaa ya mawe, upepo nk. Aidha serikali iongeze kasi zaidi katika utekelezaji wa miradi mingine mathalani Kiwira, Stiggler’s Gorge, Ruhudji nk ambao unasuasua kutokana na udhaifu wa kiuongozi na udhaifu wa maamuzi.

d)
imeitaka Serikali isijiingize katika bishara ya aina yeyote na Kampuni ya Dowans. Badala yake, itumie sheria zilizopo katika kutaifisha mitambo hiyo kwa kuwa michakato yake kuanzia hatua za awali ilihusisha ukiukwaji wa sheria na taratibu.

H: Mambo Mengine

iii) Kamati Kuu imepokea kwa masikitiko taarifa ya tukio la mabomu huko Gongolamboto. CHADEMA imeendelea kumhimiza Waziri wa Ulinzi awajibike kisiasa kwa kushindwa kuchukua hatua thabiti katika kuhakikisha kuwa milipuko ya mabomu katika kambi zetu za jeshi haijirudii. Aidha, Kamati Kuu inasikitishwa na ukimya wa Serikali katika kutoa Taarifa kwa umma tangu matukio ya Mbagala na sasa Gongo la Mboto, na pia ukimya wa Serikali kutokutoa agizo la kuchukua hatua za haraka kukaguliwa kwa maghala yote ya Silaha nchini. Hatuhitaji kusubiri hadi maafa mengine yatokee ndipo tuchukue hatua.

iv)
Kamati Kuu imepokea kwa masikitiko taarifa ya janga la tsunami iliyotokea Japan ambayo nayo imesababisha milipuko wa mitambo ya nyukilia, ambayo kwa pamoja yamesababisha maafa makubwa ya kibinadamu na mali nchini Japan. Kamati Kuu inatoa salamu za rambirambi na pole kwa Waziri Mkuu wa Japan, Mheshimiwa Naoto Kan na wananchi wa nchi hiyo.Kamati Kuu imeagiza Sekretariat ya Kamati Kuu kuangalia uwezekano wa kutoa msaada wowote kusaidia ndugu zetu wa Japan ambao wameathirika na maafa hayo. Kutoa ni moyo na si utajiri na chochote hicho kiwadsilishwe na uongozi wa Chama kwa Ubalozi wa Japan haraka iwezekanavyo kama ishara ya wanachadema, wapenzi na wananchi kwa ujumla kushirikiana na ndugu zetu wa Japan ambao kwa muda mrefu wamejitolea kwa hali na mali katika kusaidiana na Watanzania katika maendeleo na majanga mbalimbali.

v)
Kamati Kuu imepokea taarifa juu ya uamuzi wa Serikali wa kuandaa muswada mpya wa Sheria ya Manunuzi. Kamati Kuu imezingatia kuwa lengo kuu la muswada huu wa sheria mpya ya manunuzi ni kuiwezesha serikali na taasisi zake kuweza kununua bidhaa zilizokwisha tumika (second hand), jambo ambalo limezuiliwa katika sheria iliyopo sasa. Kuruhusu ununuzi wa mitambo chakavu ni kutoa fursa kwa ufisadi kushamiri. Hivyo basi, Kamati Kuu inapinga mabadiliko ya sheria ya manunuzi katika vipengele visivyozingatia kuziba mianya ya ufisadi na kusababisha matumizi mabaya ya rasilimali za umma.

vi)
Kamati Kuu imepokea taarifa kuhusu azima ya serikali kuwekeza katika uchimbaji wa Uranium kama moja ya masuala yatakayozingatiwa katika bajeti yake ya mwaka ujao wa fedha. Kamati Kuu imeishauri serikali kuwa makini na jambo hili kwa kuzingatia athari za nyukilia katika sehemu mbalimbali duniani. Kamati Kuu imeishauri serikali kutengeneza kwanza sera ya uvunaji na utunzaji wa madini ya Uranium kabla ya kuanza uchimbaji wake.

vii)
Ili kukabiliana na tatizo la njaa linaloikabili nchi kwa sasa na mwaka ujao, Kamati Kuu imeitaka serikali kuhakikisha kuwa inaweka mpango maalumu katika bajeti ijayo ili kuhakikisha kuwa bei za bidhaa muhimu za chakula, na hasa bei za unga, mchele, sukari, maharage nk zinashuka kwa pamoja na mambo mengine kuongeza uzalishaji na ufanisi wa soko la ndani.

viii) Kamati Kuu imesikitishwa kupanda kwa kasi kwa deni la taifa kwa kiwango cha kufikia Dola la Marekani 11,041.8 milioni. Deni hili limeongezeka kwa asilimia 18 ndani ya mwaka mmoja. Kamati Kuu imewataka wabunge wa CHADEMA kuibana serikali kueleza chanzo cha kupanda kwa deni la taifa katika kipindi hiki cha utawala wa Rais Kikwete. Aidha kamati kuu imetahadharisha kuhusu dhamira ya serikali ya kutaka kuongeza matumizi ya mikopo ya kutoka nje yenye gharama kubwa (non concessional external financing) ambapo serikali inapanga kuchukua dola za kimarekani milioni 525 hali ambayo itachangia zaidi kuongeza deni la taifa wakati ambapo kuna vyanzo vingine vya ndani vya mapato ambavyo bado havijatumika ipasavyo.

Dk Willibrod Peter Slaa
Katibu Mkuu
 
Ni vema kama unaweza kuiweka moja kwa moja wengine tunatumia simu zinasumbua 2 download files plse
 
Acheni utani attachment haipo, hata kwenye kompyuta haionekani. Regia iweke fasta nina usongo, Invisible help her
 
Shukran sana Mh. Regia, taarifa tumeipata na kwa kuangalia yaliyomo ni Agenda zilezile ambazo Chadema wamekuwa wakizisemea.

Swali hapa ni kwa nini KIKAO MAALUMU? Ratiba ya kawaida ya vikao vya Chama ikojo kwamba labda isingefanyika wakati wa kikao cha kawaida?
 
.......Kutoa ni moyo na si utajiri na chochote hicho kiwasilishwe na uongozi wa Chama kwa Ubalozi wa Japan haraka iwezekanavyo kama ishara ya wanachadema, wapenzi na wananchi kwa ujumla kushirikiana na ndugu zetu wa Japan ambao kwa muda mrefu wamejitolea kwa hali na mali katika kusaidiana na Watanzania katika maendeleo na majanga mbalimbali.


Hivi serikali ya ccm imewapa nini Wajapan zaidi ya pole?
 
Taarifa ni nzuri ingawaje imejadili mambo mengi mno na kukosa IMPACT inayotakiwa. Ni vizuri kwenye vikao kujadili mambo mengi, lakini summary ikae kwenye issue muhimu kama nne, ili mkazo ueleweke, otherwise inakuwa vigumu KUWEKA WEIGHT kwenye mambo lukuki.

Issue ya UMEYA WA ARUSHA, naomba sana pamoja na rafu zote zilizofanyika, lakini sasa kama Chama, CHADEMA wamove on. Sijapenda pale ambapo taarifa inasema baada ya siku 21, nguvu ya umma inaweza kutumia ( This is SERIOUS) na kwa kweli inaweza kuleta Fujo na vurugu ambazo zitaprove CCM RIGHT kuwa chadema wanataka kuvunja amani.

In truth, hata kama uchaguzi ukifanyika leo wa Umeya wa Arusha as long as # ya madiwani imekamilika kwa CCM kuwa na zaidi na TLP(MREMA kuwa mkononi mwa JK) CCM ITASHINDA.

Umeya wa Arusha sio muhimu kiasi hicho, madiwani wa Chadema wafanye kazi ya kutetea wananchi, na Chadema wawaeleze wananchi wa Arusha uchaguzi ujao wachague madiwani wengi wa Chadema ili kupata Umeya.
 
Thanks for the document ingawaje natarajia tu kuwa kuna mkakati wa ufuatiliaji na utekelezaji wa Tamko hilo.

All blessings from God should guide this official statement
 
17 Reactions
Reply
Back
Top Bottom