nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
AWATAKA WATUMISHI WAMUOMBEE ASIADHIRIKE
na Daniel Mwita
​
SIKU mbili baada ya Rais Jakaya Kikwete kuwaapisha mawaziri wapya, aliyekuwa Waziri wa Viwanda na Biashara aliwaaga wafanyakazi wa wizara hiyo kwa majonzi huku akilalamika kuwa amengolewa uwaziri kwa kosa lisilomhusu.
Chami ambaye ni Mbunge wa Moshi Vijijini, alitoa kauli hiyo jana wakati akizungumza na watumishi wa wizara hiyo mara baada ya kukabidhi ofisi kwa Waziri mpya, Dk. Abdallah Kigoda.
Huku akionyesha huzuni kubwa na kuumizwa moyoni na uamuzi wa Rais Kikwete kumngoa madarakani, Dk. Chami aliwaomba watumishi hao wamwombee kwa Mungu ili asiaibike zaidi huko aendako.
Ndugu zangu niombeeni sana kwa Mungu asiniadhiri kama ilivyotokea sasa ili niweze kufanikiwa huko ninakokwenda na ni matumaini kwamba kila mmoja wenu atafanya hivyo, alisema Dk. Chami kwa huzuni kubwa.
Waziri huyo wa zamani ambaye kwa miezi kadhaa iliyopita alikuwa nchini India kwa matibabu, alisisitiza kuwa ameadhibiwa kwa makosa ambayo hakuhusika nayo kwa kuwa hajawahi kufanya ubadhirifu wowote wa mali za umma katika kipindi chote cha uongozi wake.
Alisema anatambua fika kwamba yeye ni mwadilifu katika nyanja zote kwenye wizara hiyo, lakini alisisitiza tena na tena kwamba ameadhibiwa kwa makosa ambayo hakuyatenda.
Kutokana na kauli yake ya kuhuzunisha, mtumishi mmoja wa kike ambaye alikataa kutaja jina lake, alimfariji na kumtia moyo waziri wake huyo wa zamani kwa kusema kuwa kama anaamini kwamba aliwatumikia Watanzania kwa uaminifu, Mungu atakuwa pamoja naye, huku akinukuu mfano wa Ayubu katika kitabu cha Biblia.
Kwa kuwa tunaamini kwamba wewe ulikuwa mtumishi mwaminifu, Mungu atakuwa pamoja nawe hatakuadhibu na kutolea mfano wa Ayub kwenye kitabu cha Biblia kwamba aliadhibiwa kwa makosa ambayo hakustahili, lakini Mungu aliruhusu iwe hivyo. Mungu atakusaidia, hatakuacha, alisema mtumishi huyo huku wenzake wakitikisa vichwa kuashiria kumuunga mkono.
Mbali ya kuzungumzia kusikitishwa na kungolewa kwenye uwaziri kwa kuonewa, Dk. Chami aliwapa wosia watumishi hao kuacha tabia ya majungu na kusemana kazini kwani vitu hivyo ni hatari katika maeneo ya kazi na vinaleta mahusiano mabaya kazini.
Mimi ninaondoka kwenye wizara hii, ninyi nyote ni mashahidi kuwa mimi sikuwahi kutuhumiwa kwa kosa lolote, ila imenilazimu kuondoka kwa sababu ya uajibikaji wa kisiasa, naomba niseme kitu kimoja kwenu na nadhani mkikitilia mkazo mtaweka mahusiano mazuri kazini, tabia ya watu kupinduana sio nzuri maana kuna wakurugenzi wasaidizi wanaotaka kuwa wakurugenzi hivyo wanapika majungu ili wakurugenzi waondolewe na wao washike nyadhifa hizo, alisema Dk. Chami.
Aliwataka kuwa wadilifu hasa katika swala zima la fedha, ambapo alisema endapo watendaji mbalimbali wa serikali watazingatia nidhamu ya fedha za umma, wizara nyingi zitakuwa na maendeleo makubwa.
Hata hivyo gazeti hili lilipomtaka afafanue kama kuna ubadhirifu wowote wa fedha za umma umefanyika katika wizara hiyo alikana na kusema anachofanya ni kusisitiza uajibikaji wenye tija kwa watumishi wa umma.
Chami na Naibu wake, Lazaro Nyalandu, ambaye kwa sasa amehamishiwa Wizara ya Maliasili na Utalii, walikuwa kwenye mgogoro mkubwa unaotokana na mitazamo tofauti ya kikazi hususan suala la Mkurugenzi wa Shirika la Viwango nchini (TBS), Charles Ekelege.
Katika sakata hilo, Chami alikuwa anamkingia kifua mkurugenzi huyo anayekabiliwa na tuhuma nzito zikiwemo za utendaji mbovu wa shirika hilo, huku Nyarandu akitaka bosi huyo wa TBS asimamishwe kupisha uchunguzi dhidi yake.
Kwa upande wake, Nyalandu alitoa waraka uliombebesha mzigo waziri wake, Dk. Chami, akisema alimpa ushauri wa kumsimamisha kazi Ekelege kupisha uchunguzi wa Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), lakini hakutekeleza.
Katika barua hiyo ya Februari 10, mwaka huu, kwenda kwa Chami, alimweleza kuwa wabunge walikuwa wanashuku kuwa mkurugenzi huyo alitoa taarifa zisizo sahihi.
Kikao cha briefing cha CAG na waheshimiwa wabunge, TBS imeshutumiwa kuhusiana na ukaguzi wa magari nje ya nchi na mchakato wote unaohusiana na suala hilo, inasomeka dokezo hilo la Nyalandu.
Alisema wabunge walioshiriki katika ziara ya nchi za Hong Kong na Singapore wametoa madai kuwa Mkurugenzi Mkuu wa TBS aliwadanganya juu ya kampuni zinazofanya ukaguzi wa magari na bidhaa nyingine nje ya nchi na wakatoa madai kuwa TBS imetoa taarifa tofauti na yale waliyoyaona katika ziara.
Dk. Chami alikiri kupokea ushauri huo lakini, akasema wakati anautoa kulikuwa hakuna tuhuma zozote za kamati kuhusu Ekelege.
Ushauri ulikuwa mzuri lakini Ekelege ni mteule wa Rais hivyo huwezi kwenda kwa Rais kumtaka amwondoe wakati hakuna taarifa yoyote inayoonyesha tuhuma zake. Kuna njia mbili za kumsimamisha: kwanza, kumshauri Rais na pili hizo ripoti dhidi ya Ekelege zipelekwe kwenye Bodi ya Wakurugenzi ya TBS na baada ya hapo wakitoa maazimio ndiyo waziri anaweza kwenda nayo kwa Rais, alisema Dk. Chami.
Rais Kikwete wiki iliyopita alifanya mabadiliko makubwa katika Baraza la Mawaziri kwa kuteua wapya watatu na manaibu 10 huku akiwaacha sita.
Pia aliwapandisha manaibu mawaziri wanne kuwa mawaziri kamili na kuwahamisha wizara mawaziri wanane na manaibu waziri sita, huku mawaziri na manaibu waziri 22 wakibaki katika wizara zao za awali.
Kutokana na mabadiliko hayo, idadi ya mawaziri na manaibu wao sasa imeongezeka kutoka 50 katika baraza la awali hadi 55. Mawaziri kamili wameongezeka kutoka 29 hadi 30 huku manaibu waziri wakiongezeka kutoka 21 hadi 25.
Mawaziri ambao wamengolewa na wizara walizokuwa wakiziongoza kwenye mabano ni Mustafa Mkulo (Fedha), Dk. Hadji Mponda (Afya na Ustawi wa Jamii), William Ngeleja (Nishati na Madini), Dk. Cyril Chami (Viwanda na Biashara), Omar Nundu (Uchukuzi) na Ezekiel Maige (Maliasili na Utalii).
Panga hilo la mabadiliko liliwakumba pia Manaibu Waziri wawili, Dk. Lucy Nkya (Afya na Ustawi wa Jamii) na Dk. Athumani Mfutakamba (Uchukuzi).
Mawaziri wapya walioteuliwa na wizara zao kwenye mabano ni Mbunge wa Handeni, Dk. Abdallah Kigoda (Viwanda na Biashara), Mbunge wa Kalenga, Dk. William Mgimwa (Fedha) na Mbunge wa Kuteuliwa Profesa Sospeter Muhongo (Nishati na Madini).
Walioteuliwa kuwa Manaibu Waziri ni Mbunge wa Rufiji Dk. Seif Suleiman Rashid (Afya na Ustawi wa Jamii), Mbunge wa Kibakwe, George Simbachawene (Nishati na Madini), Mbunge wa Bumbuli, January Makamba (Mawasiliano, Sayansi na Teknolojia), Mbunge wa Buchosa, Dk. Charles Tizeba (Uchukuzi) na Mbunge wa Mvomero, Amos Makala (Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo).
Wengine ni Mbunge wa Makete, Dk, Binilith Mahenge (Maji), Mbunge wa Shinyanga Mjini, Stephen Maselle (Nishati na Madini Madini), Mbunge wa Viti Maalumu, Angela Kairuki (Katiba na Sheria) na Wabunge wa Kuteuliwa Janet Mbene na Saada Mkuya Salum wote Fedha.
Naibu Mawaziri waliopandishwa na kuwa mawaziri kamili wamo, Christopher Chiza (Kilimo, Chakula na Ushirika), Dk. Harrison Mwakyembe (Uchukuzi), Dk. Fenella Mukangala (Habari, Vijana, Utamaduni na Michezo) na Khamis Kagasheki (Maliasili na Utalii).