Mtambuzi
Platinum Member
- Oct 29, 2008
- 8,810
- 15,398
Ilikuwa ni siku ya Ijumaa ya Agosti 31, 2012, majira ya saa nne asubuhi niko ofisini, nikiendelea na kazi zangu kama kawaida. Nilikuwa na jukumu la kakamilisha ripoti yangu ya mwishoni mwa juma.Nikiwa bado naendelea na kazi zangu kivivu vivu mara nikashikwa na shauku ya kutembelea Jamii Forum ili kuangalia kama kuna maoni katika uzi wa kesi za Ijumaa niliouweka usiku wa manane. Nilipofungua katika Jukwa la MMU nikakutana na habari iliyonishtua sana. Haikuwa nyingine bali ni taarifa ya msiba wa mke wa Mwanajamii Forum mwenzetu KakaKiiza.
Muweka taarifa Bwana Kiresua aliweka namba ya simu ya KakaKiiza ili iwe rahisi kwa wale watakaotaka kuwasiliana naye iwe ni rahisi kwao kuwasiliana naye. Sikufanya ajizi nilinyanyua mkono wa simu ya mezani huku mikono ikinitetemeka nilipiga ile namba ya simu. Lakini cha kushangaza simu ile ilipokelewa na mwanamke. Kwa kuhisi kwamba anaweza kuwa ni jamaa yake nilimuomba niongee na KakaKiiza.
Mwanamke yule alionekana kushangaa na kuniambia kwamba hamjui mtu mwenye jina lile. Nilimuuliza ile simu ni ya nani (maana nilihisi huenda haya majina tunayotumia hapa JF hayafahamiki kwa jamaa zetu). Alinihakikishia kwamba ile simu ni ya kwake na hamjui huyo mtu ninayemtafuta. Nilijua nimekosea namba, na huenda ilitokana na kitete cha kupiga simu haraka haraka bila kuangalia namba kwa makini.
Niliangalia namba kwa makini safari hii na simu ilipokelewa na KakaKiiza mwenyewe na baada ya kujitambulisha nilimpa pole ya kuondokewa na mkewe kisha nikamuuliza juu ya taratibu za mazishi. Alinijulisha kwamba bado hawajapanga lolote, lakini aliniahidi kunipa taarifa rasmi hapo watakapokaa kikao cha familia na kupanga namna ya kuhifadhi mwili wa marehemu mkewe. Niliagana naye na kumuahidi kwamba siku inayofuata yaani Jumamamosi nitamtembelea nyumbani kwake.
Siku iliyofuata majira ya saa sita mchana nilimpigia simu na akanielekeza mahali ulipokuwa msiba ambapo ni Tegeta mwisho eneo maarufu kama Kwa Majura. Ingawa barabara ya Tegeta ina foleni, lakini nashukuru niliwahi kufika na kukutana na mfiwa, KakaKiiza. Baada ya kujitambulisha, tulikaa pembeni na kuzungumza na hapo ndipo aliponieleza kile kilichotokea hadi mkewe we kufariki.
Alinieleza kwamba mkewe alianza kujisikia vibaya hapo mnamo Agosti 23, 2012. Lakini hakuonekana kama amezidiwa, kwani alikuwa na ujauzito wa miezi 6, na kuumwa kwake alikuchukulia kama matatizo ya ujauzito tu. Waliondoka nyumbani huku mgonjwa akitembea mwenyewe na kungia kwenye gari ambapo alimpeleka katika hospitali ya TMJ.
Walipofika akapata matibabu na kurejea nyumbani. Ilipofika tarehe 26, Agosti mkewe aliamua kwenda kwa mama yake mzazi maeneo ya Tegeta. Lakini alipofika alianza kujisikia vibaya na pia alikuwa anasikia kizunguzungu, hivyo mama yake akamuwahisha katika hospitali ya jirani iitwayo MICO ambapo alitundikiwa dripu. Siku iliyofuata yaani tarehe 27 Agosti alimrudisha mkewe katika hospitali ya TMJ kwa ajili ya matibabu zaidi. Walipofika hapo TMJ, mgonjwa alichukuliwa vipimo na baadae wakamhamishia katika Hospitali ya Muhimbili.
Alipofikishwa hapo, vipimo vilionyesha kuwa alikuwa na upungufu wa damu na sukari ilipanda kwa kiwango kikubwa, hivyo ikabidi aongezewe damu na kupewa matibabu mengine. Mgonjwa aliendelea na matibabu na hali yake ilonyesha kuimarika. siku ya alhamisi jioni ya tarehe 30 Agosti KakaKiiza alimuaga mkewe na kumweleza kwamba siku inayofuata yaani Ijumaa atachelewa kufika hapo hospitali kidogo kutokana na mambo fulani fulani aliyokuwa ayafanye kabla ya kwenda kumuona, kwani hali ya mgonjwa ilikuwa imeimarika na alijua dhahiri kwamba ataruhusiwa siku hiyo ya Ijumaa.
Mpaka ufikia usiku alikuwa anawasiliana na mkewe na hakuonyesha dalili kwamba amezidiwa. Ilipofika asubuhi alimpigia simu mkewe ili kumjulia hali pamoja na kumweleza kwamba anaedelea vizuri lakini alimsisitiza awahi hosptalini. KakaKiiza alikata shauri kuwahi hospitalini kama alivyoagizwa na mkewe. Alipofika alimkuta mkewe akiwa amezidiwa, alikuwa amewekewa oksijeni huku daktari na wauguzi wakijitahidi kumuhudumia kwa kila hali kwani ilionekana wazi kwamba mkewe anapigania roho yake.
Ni kweli, pamoja na juhudi kubwa za Daktari pamoja na wauguzi mkewe Subira (Juliana) Alfred Mwamasso alifariki majira ya saa tatu asubuhi ya Ijumaa ya tarehe 31, Agosti 2012 mbele ya macho yake. KakaKiiza na mkewe walidumu kwenye ndoa yao kwa miaka 12 na walijaaliwa kupata watoto wawili wote wa kike. Wa kwanza anaitwa Ellen ana miaka 10 na anasoma darasa la 5 na wa pili aitwae Adelaide ana miaka 6 na yuko darasa la 1. Wote wanasoma katika shule ya St. AnneMarie. Hayo ndiyo yalikuwa maelezo ya KakaKiiza kuanzia pale mkewe alipoanza kuumwa hadi mauti yalipomkuta.
Niliwasiliana na baadhi ya wana JF nilipokuwa hapo msibani na wengi waliahidi kufika hapo msibani ili kumfariji mwana JF mwenzetu. Mwana JF mwingine niliyewasiliana naye alikuwa ni NATA, nilipomweleza juu ya msiba huo, kwa bahati mbaya yeye alikuwa nje ya mji, lakini alituma mchango wake kwa njia ya Tigo Pesa na mimi nikauwasilisha kwa mfiwa. Napenda kuchukua nafasi hii kumshukuru NATA kwa moyo wake wa upendo.
Mazishi ya marehemu Subira (Juliana) Alfred Mwamasso, yalifanyika jana siku ya Jumatatu ya tarehe 3 Septemba 2012 katika makaburi ya Kinondoni majira ya saa kumi jioni, yakitanguliwa na mazishi ya kichanga chake kilichofia tumboni kilichokuwa na jinsia ya kiume ambacho kilizikwa katika makabuti ya Muhimbili majira ya asubihi. Nilibahatika kuhudhuria mazishi hayo na pia nilibahatika kukutana na mwana JF mwenzangu bwana Nicas Mtei. Niliambiwa kwamba walikuwepo wana JF wengine, lakini kutokana na shughuli za mzishi, wengi hatukupata fursa ya kuonana.
Ni kweli Shemeji yetu, dada yetu, shangazi yetu au rafiki yetu ametutoka na tutaendelea kumkumbuka daima.
Napenda kuchukua nafasi hii kumuombea KakaKiiza kwa Mwenye enzi Mungu ampe moyo wa subira hasa katika kipindi hiki kigumu cha kuondokewa na mkewe kipenzi. Najua ameguswa sana na msiba wa marehemu mkewe, na ni vigumu sana kwake yeye kuamini kuwa mkewe hayupo tena duniani, lakini ni vyema akubaliane na hali halisi, kwani kazi ya Mungu daima haina makosa. Namuomba mwenyezi mungu ailaze roho ya marehemu Subira (Juliana) Alfred Mwamasso mahali pema peponi …….. amina.
Naomba waraka huu usichukuliwe kama ni waraka wa shukurani kutoka kwa KakaKiiza, kwani kwa maelezo yake nilipozungumza naye jana, aliahidi kwamba akipata muda atakuja humu Jamvini kutoa shukrani zake za dhati kwa wadau wote walioshiriki kwa njia moja ama nyingine katika kipindi kigumu tangu alipoondokewa na mkewe mpenzi. Kwa sasa anahitaji muda zaidi wa kupumzika na kutafakari mustakabali wa maisha yake na familia yake aliyoachiwa na marehemu mkewe.
Kwa wale watakaopenda kuwasiliana na KakaKiiza namba yake hii hapa: 0752 30 78 78.
Pia mnaweza kutuma rambirambi zenu kwa M-Pesa kupitia namba hii, kwa wale wenye kutaka kufanya hivyo.