Riwaya: KITISHO

Dam55

JF-Expert Member
Oct 8, 2015
5,592
11,831
FILM: KITISHO
MTUNZI: Richard MWAMBE

1
Mbowe club saa 1:23 usiku

RADI kali ilipasua anga na kufanya mchoro wa kutisha, mwanga wake ulilipoteza giza kwa sekunde kadhaa, kila kilichojificha kilionekana wazi.
Hakuna mtu hata mmoja aliyekuwa nje muda huo. Ni mvua kubwa na ngurumo za kutisha zilitawala kila kona, ilikuwa ni hali ya kuogofya sana. Mifereji na mito ya dhalura ilianzishwa na maji ya mvua hiyo.
Kama ilivyo ada katika jiji la Dar es salaam, barabara zote zilikuwa zimejaa maji, kama ukiwa dereva mgeni basi hutoweza kujua ni wapi barabara ilipo. Sehemu kubwa ya mji hasa katikati ya jiji gari nyingi ziliegeshwa kando ya barabara kusubiri mvua iishe lakini haikuwa hivyo kwani mvua ilikazana zaidi ya saa nne.

Wakati hayo yote yakiendelea, ndani ya ukumbi mkubwa wa starehe unaojulikana kama ‘Mbowe Club’ watu hawakuwa wakijua kama nje kuna mvua, disco liliendelea kwa nguvu zote, watu walicheza, wakanywa na kuburudika. Katika kaunta kubwa ya ukumbi huo kulikuwapo walevi kadhaa ambao tayari walikwishabadilisha lugha ya mawasiliano kutoka Kiswahili na kuwa Kiingereza.

Gina binti Komba Zingazinga alikuwa ni miongozi mwa watu wachache waliokuiwa wamesaliwa na akili zao na utashi pia, alikuwa akinywa kinywaji chake taratibu huku jamaa mmoja akijitahidi kumzengea zengea lakini asifanikiwe. Kila wakati alionekana kuitazama saa yake aliyoivaa mkononi na aliposhusha mkono aliinua ule uliokamata ile bilauri yenye kiuno iliyojaa mvinyo kutoka Dodoma. Baada ya kupiga funda moja kasha la pili aliiteremsha taratibu na kuiweka juu ya mbao mwororo iliyoifunika na kuipendezesha kaunta ya ukumbi huo. Macho yake yalikuwa yakizunguka huku na kule yakitazama au kutafuta kitu ambacho hata yenyewe hayakukijua.

Upande wa pili wa ukumbi huo, kwenye sakafu iliyojengwa juu kidogo na ili uifikie itakulazimu kuzikwea ngazi kadhaa, kulikuwako watu watatu, wawili wanaume na mmoja mwanamke. Mwanaume mmoja alikuwa na tambo kubwa lililojaa kimazoezi, enzi za utoto wetu tungeweza kumwita Pawa, lakini enzi hizi wanamwita Baunsa, yote hayo ni mabadiliko ya nyakati. Watu wale watatu walikuwa wakiongea jambo Fulani na meza yao ilikuwa imechakazwa kwa pombe kalikali na sahani za nyama zilizokuwa zikipishana, vyote hivyo vilimiminwa katika matumbo hayo matatu. Ilikuwa ni vigumu kusikia nini wanachokiongea kutokana na muziki mkubwa uliokuwa ukipigwa ndani humo. Kati ya kaunta alipokuwapo Gina na ule upande kulitenganishwa na kundi la vijana waliokuwa wacheza muziki huo kwa mitindo mbalimbali. Gina alihakikisha hapotezi macho yake upande ule kwani mwili wake ulikuwa ukisisimka mara kwa mara na hiyo kwake ilikuwa ni ishara ya hatari.

Dakika chache baadae alimuona Yule mwanamke akiinuka na kutoka katika vile viti, akitembea kwa mwendo wa ki-levi levi. Akamtazama na kujua mara moja kuwa alikuwa anaelekea chooni, Gina akajikuta akishuka kutoka kwenye kiti kirefu alichokuwa amekalia, akaigugumia pombe yake yote kinywani mwake, kasha akavuta hatua fupifupi akikumbana na walevi na wacheza muziki akaelekea kule alikokwenda Yule mwanamke.
Halafu nitamwuliza nini? Akajiuliza pa si na kupata jibu. Lakini aliendelea kuvuta hatua kuelekea kule chooni, akapinda kona ya kwanza na kuingia kwenye milango Fulani iliyokuwa ikielekea huko atakako, mbele kidogo alimuona Yule mwanamke akiingia katika moja milango ya vyoo vile. Gina; mkono wa kulia ukiwa nyuma ya suruali yake ndani kidogo ya jaketi lake, sikwambii alishika kitu gani, aliuendea ule mlango, mara ghafla akaanza kuhisi kitu kikimfinya mkononi mwake, ilikuwa ni saa kubwa ya mkononi, saa yenye uwezo wa kupokea nukushi, kupiga picha za mjongeo na mnato, yenye uwezo wa kurekodi sauti na pia unaweza kuitumia kama simu. Akainua mkono na kubofya kitufe Fulani kasha akasubiri kidogo. Wakati akisubiri kijimkanda hicho chembamba kikitoka kwenye saa yake, Yule mwanamake bado alikuwa chooni.
Mama yuko mahututi Shamba, Tena Saan Aisee! Uikuwa ni ujumbe uliosomeaka hivyo katika kile kijimkanda. Akakikata na kukitia mfukoni mwake kisha akaanza safari ya kutoka ndani ya Klabu ile, akili yake ilikwisha sahau juu ya Yule mwanamke, akapita mlangoni na kukumbana kikumbo na Yule mwanaume mwenye tambo kubwa, akielekea kule choo cha wanawake, Gina akasukumwa pembeni; na Yule bwana akapita.

Nje ya Klabu hiyo ndipo alipokutana na mvua ya kutisha, akapachua kikofia katika ukosi wa jaketi lake na kukivaa kisha akaliendea gari lake, mita kadhaa kabla hajalifikia akapiga breki na kuacha kinywa wazi, hakuamini anachokiona. Vioo vyote vya gari yake vilikuwa vimevunjwa, tairi hazina upepo na ndani kulijaa maji ya mvua. Wameiba? Akajiuliza, kisha kwa mwendo wa tahadhari akasogea kwenye lile gari, juu ya kiti cha dereva kulikuwa na bahasha ngumu ya khaki, akatazama huku na kule, alipojihakikishia usalama akaingiza mkono kwa minajiri ya kuichukua ile bahasha ijapokuwa ilionekana kulowana.
Daraja la sarenda saa 1:55 usiku.
BMW nyeusi iliyokuwa iking’azwa kwa mwanga wa radi, ilshuka katika barabar hiyo ya Kenyata kwa kasi sana ikitokea maeneo ya Masaki. Ilipofika katika makutano ya barabar hiyo na ile ya Ally Hassan Mwinyi mkabala na Ubalozi wa Ufaransa iliingia barabara kubwa bila kungalia usalama huku ikirusha maji juu kutokana na mvua kubwa iliyokuwa ikinyesha usiku huo.
Madam S alikuwa katulia kwenye usukani akiiongoza gari hiyo ya Mwingereza kwa umahiri mkubwa. Akakunja ushoto na kukanyaga mafuta kueleka mjini. Ilikuwa ni tabu kuona mbele kutokana na wingi wa mvua, barabara imejaa maji, umeme umekatika, ilikuwa ni shida juu ya shida. Madam S hakujali alilikanyaga daraja la Salenda na kuendelea mbele, lakini kabla hajalimaliza, hamad, kulikuwa a mwili wa mwanadamu uliolala barabarani huku mikono yake ikiwa imefungwa nyuma. Akaiyumbisha gari kuukwepa mwili huo, gari ikasota na kukosa muelekeo, akarudisha usukani kulia kuukwepa mwamba wa daraja, akaknyaga krachi na kuachia mafuta kasha akatoa gia ya tano na kushusha ya nne, kutahamaki gari yake ilikuwa ikihamia barabara ya pili, akakanyaga breki lakini ikashindwa kusimama, akaknyaga tena breki bado gari ilikuwa ikiendelea, ikapanda tuta lakutenga barabara, ikajipigia na kutua barabara ya pili, akili ikamrudia, akavuta breki ya mkono na ile BMW ikaserereka na kujizungusha.

Kishindo kikubwa kikasikika, BMW iligongana na Land Rover Defender, ikaangushwa pembeni. Madam S akajikuta kwenye pori la mikoko chini ya daraja la Salenda, akafyatua mkanda, akapiga kioo cha mbele kwa kukikanyaga kwa mguu, akatoka, akajipapasa na kukuta bastola zake zipo salama.
Damu zilizikuwa zikitiririka semu ya paji la uso juu kidogo ya jicho la kulia, wakati akijitahidi kusimama, radi kali ilipiga na kufanya mwanga mkubwa uliong’aza vichaka vyote, Madam S akaona mbele yake kama kivuli cha mtu aliyesimama nyuma yake. Akajua ni mawenge ya ajali tu, akageuka nyuma na mara ghafla akakutana na pigo la kitu kizito kilichotua katikati ya paji la uso, akayumba vibaya lakini mikono yake tayari ilikuwa imekwishachomoa bastola zake, kabla hajafyatua akafunikwa na gza nene lililomfanya ashindwe kuona chchote, akaanguka kama mzigo na bastola zikimtoka mikononi mwake.

Ofisi ya usalama wa taifa saa 2:00 usiku.

MAAFISA wa Idara ya Usalama wa Taifa walikuwa wakiendelea na shughuli zao kama kawaida usiku huo. Katika moja ya ofisi za jengo hilo, vijana wawili na msichana mmoja walikuwa bize kutazama luninga nyingi zilizowazunguka zinazoonesha maeneo mbalimbali muhimu ya Jiji la Dar es salaam. Kupitia luninga hizo waliweza kuona moja kwa moja kile kinachotokea kwenye maeneo hayo kama Uwanja wa ndege, Bandarini, Stesheni ya Treni, Uwanja wa Sabasaba, Makao makuu ya Rais na maeneo mengine mengi ambayo yamepewa umuhimu wa pekee kwa sababu hii au ile.

Avant, msichana mbichi wa miaka takribani thelathini hivi alikuwa katingwa kuangalia tukio la ajali iliyotokea daraja la Salenda, bado alikuwa anapata shida kujua hasa nini kinaendelea kutokana na ile picha kufichwa na mvua ilikua ikinyesha eneo hilo lakini kila ilipokuwa radi ikipiga ndipo alipoweza kuona kitu, baada ya dakika kadhaa alipuuza na kuendelea kutazama maeneo mengine.
Mubah akajikohoza kidogo na kumgutusha Avanti kutoka pale alipokuwa akitazama.

“Si ukapime, au Mama yako anajua?” Avanti akamtania Mubah.

“Unanianza we mrembo, mi nasubiri time hapa niingie viwanja!” Mubah akajibu, huku akitoka kwenye kiti chake na kukiendea kile alichoketi Avant, akasimama nyuma yake, machoye akiwa kayakaza kwenye ile luninga.

“Shiit! Avant, nini hicho?” akauliza huku akisogea jirani zaidi.

“Ajali, imetokea kama dakika kumi hivi,” Avant akajibu.

“Kwa nini usipige simu polisi wawahi kama kuna chochote cha kuokoa?” Mubah akahoji.

“Sasa Mubah, Salenda pale kituo kipo jirani wataenda tu,” akaeleza huku akimtazama Mubah usoni.

“Yaani wewe! Kitendo cha kuitega kamera pale hatukufanya kwa makosa, lile ni eneo nyeti sana, kama ni ajali lazima polisi wafike mapema ili kuondoa kilichopo, pale vipngozi asilimia 99 wanapita, ikiwa hujuma utalaumiwa wewe kwani ndio eneo lako la kutazama leo!” Mubah akalalamika huku akiliendea kabati dogo lililo hapo jirani.

Avant akainua simu na kubofya tarakimu Fulani Fulani kasha akatoa taarifa hiyo kituo cha polisi cha Salenda. Haikupita dakika tano tayari kupitia luninga yake aliweza kuona gari na nyendo za polisi eneo hilo bila kujali mvua iliyopo. Avant aliendelea kutazama huku akigonga gonga karamu yake.

§§§§§

Gina alivuta hatua na kuingia katika lango kuu la Ofisi Nyeti, Shamba, akabofya namba zake za siri, kasha akaweka kiganja chake juu ya kioo Fulani kilichopo mlangoni na baada ya hapo akafanya kama anachungulia, kijimwanga chekunfu kikapita kati ya macho yake na kitasa cha ule mlango kikafyatuka, akaufungua na kuingia ndani. Moja kwa moja akaingia chumba Fulani na kuvua jaketi alilovaa, akabadilisha nguo na kurudi katika hali ya ukavu, akatoka na kutembea mwendo mfupi kabla hajagonga mlango Fulani kwa mtindo wa pekee na mlango ule ukafunguliwa.

“Karibu Gina!” Dkt Jasmine akamkaribisha na nukta chache baadae akampatia kikombe cha kahawa.

“Hawajafika?” Gina akauliza.

“Hapana, we ndiye wa kwanza, leo sijui kuna nini, labda kwa sababu ya mvua,” Dkt. Jasmin akaeleza.
Gina akashusha pumzi ndefu, mazungumzo mengine yakaendelea huku wakiwasubiri wengine, kila mara walikuwa wakitazama saa zao, hakuna simu wa taarifa yoyote iliyokuwa ikifika katika nyumba hiyo, Gina na Jasmine wakaanza kupata wasiwasi. Jasmine akainua uso na kuitazama saa kubwa ya ukutani, ikamwonesha kuwa ni saa 3:15 usiku.

“Hapana Gina, hii sio kawaida, tuanze kuwatafuta mmoja baada ya mwingine,” Dkt. Jasmin akamweleza Gina, kasha wote wawili wakaenda kwenye chumba maalumu cha mawasiliano, ndani ya chumba hicho ambamo ndiyo ofisi ya kudumu ya Chiba wa Chiba kulijawa na makompyuta na luninga nyingi huku na kule, simu za upepo, za kawaida na zile za satellite zilikuwepo. Kila kitu kilikuwa kinafanya kazi kwani haikuruhusiwa kuzima chochote labda tu kama kuna matengenezo, kila mmoja akaketi katika kiti chake na kuanza kucheza na simu zao za siri zilizounganishwa moja kwa moja.
Hakuna simu ya mkononi iliyokuwa ikipatikana si ya Madam S wala ya nani, walipigwa na butwaa na kubwa simu za nyumbani zote zilikuwa zikiita bila kukoma hazikupokelewa. Gina akamgeukia Dkt. Jasmine.

“Oya Shost, hapa ni mguu kwa mguu nyumba moja baada ya nyingine tukapate kujua kilichojiri,” Gina akamwambia Jasmine kasha wote wakaingia vyumbani na walipotoka walikuwa katika mavazi ya kazi, kila moja alibeba silaha anazoamini zingemfaa usiku huo kwani hawakujua hatari itakayowakabili. Wakiwa katika harakati hizo ndipo Gina alipokumbuka ile bahasha.

“Nisubiri Jasmine!” akarudi kwenye kile chumba akaichukua ile bahasha, bado ilikuwa imelowa akaichana taratibu na kuitoa karatasi ya ndani kwa uangalifu.

“Nini Gina?” Jasmine akauliza.

“Hii bahasha niliiokota kwenye ari yangu lakini sikuwahi kuifungua ndani,” akamjibu.

Gina alibaki kakodoa macho baada ya kukutana na kichwa cha habari kikubwa kilichosomeka ‘KITISHO!’ kisha chini yake kuliandikwa sentensi moja tu
Mwisho wa zama zenu umefika, mtaongea na Mzee Ngurumo.
Maneno hayo yalizigonga kwa nguvu nyoyo za wadada hawa, wakabaki wakitazamana, wkageuza macho yao wakaitazama tena ile karatasi.

“Gina!” Jasmine akaita.

“Jasmine!” naye akaitikia na wote wakatoka na kuingia kwenye gari ya Jasmine na kuondoka eneo hilo.

§§§§§§

Kerege – bagamoyo saa 4:07 usiku

TOYOTA Hilux Double Cabins, iliingia taratibu getini na kuegeshwa karibu na bustani ya maua iliyotengenezwa ndani ya ngome kubwa iliyobeba jengo la kifahari kuliko fahari yenyewe. Walinzi kadhaa walionekana kwenye kona zake, hawakushughulika kabisa na gari hiyo bali kila mmoja alishika lindo lake.
Dereva akashuka na watu wengine kama watatu hivi wakashuka, wakazunguka nyuma na kufungua funiko kubwa la alluminium lililotengenezwa ili kufunika mzigo uliopo ndani yake.

“Washushe hao, kisha wapeleke Kuzimu,” mmoja wa wale vijana aliyekuwa ameketi mbele akawaagiza wenzake kasha yeye akazikwea ngazi kulielekea jengo hilo lililoendezeshwa kwa taa zenye marembo mbalimbali.
Sauti za viatu vyenye kisigino kigumu zilisikika zikitembea lakini aliyevaa hakuonekana, Bwana Mpaya alibaki kusimama na kutazama kule sauti ile ilikokuwa ikitokea na asione mtu zaidi ya giza lililomlaki isipokuwa aliposimama yeye mwanga ulikuwapo na kufaya nuru ya kupendeza. Kasha ukimya ukatawala na sauti nzito ikalipenya lile giza.

“Ndio Bwana Mpaya, karibu sana, natumaini umekamilisha nililokutuma, sivyo?” alikuwa ni Pancho Panchilio aliyeyafikia masikio ya Mpaya aliyekuwa amesimama katikati ya sebule pana lakini asimwone anayeongea naye, isipokuwa sauti tu.

“Ndiyo Boss, tumewaleta lakini hali zao ni mbaya sana,” akaeleza.

“Vizuri sana, nani na nani mmempata?” akauliza tena.

“Tumempata Boss wao na Mtaalamu wao wa kompyuta,” akajibu.

“Ha! Ha! Ha! Ha! Ha!” akacheka cheko la pesa.

“Ok, wape vijana posho yao kama nilivyokwambia kisha unitafutie kichwa cha Kamanda Amata, huyu hasa ndiye mwiba kwangu, nataka apotee kwenye uso wa nchi ili binadamu tule vizuri, kuna pesa ndefu sana nimeiandaa mkilikamilisha hili,” Pancho akiwa mafichoni mwake akakohoa kidogo wakati Mpaya alikuwa akitoka, “Sikia Mpaya, hakikisha ukimuua Kamanda Amata, mkate kichwa, kisha kiwiliwili mkichome moto na kichwa mniletee, mbwa wangu hawajala nyama siku nyingi sana, maana Yule ni shetani anaweza kujiunganisha tena halafu akaangusha balaa, kwa heri!”
Alipomaliza kusema hayo na taa ndani ya jengo lile zikazimika.

2
KAMANDA Amata akaitazama gari yake aia ya Subaru Forester jinsi ilivyochakazwa kwa risasi, akashusha pumzi ndefu.
Wadude hawa wangeniua! Akajisemea moyoni huku akijaribu kuiwasha nayo ikawaka, akairudisha barabarani na kushika njia ya kwenda mjini, alijipapasa mifukoni hakuiona simu yake, wala saa yake mkononi haikuwepo. Any way! Akajipa moyo. Huku akiendelea kuutafuta mji wa Dar es salaam, saa ya ndani katika gari yake ilimwonesha kuwa ni saa tano za usiku.
Gina sijui kama atanielewa, maana tulikubaliana saa moja na robo, labda nitamkuta! Akaendelea kuongea na nafsi yake, huku akiiacha Gongo la Mboto na kuitafuta Uwanja wa Ndege. Katikati ya safari yake akafungua redio ndani ya gari na kusikiliza kinachoendelea. Ilikuwa ni kituo kimoja cha redio binafsi kikirusha habari hiyo ya dharula iliyoyanasa masikio ya Amata usiku huo.

…Mwili wa Mheshimiwa huyo umekutwa sakafuni bila uhai na kitu kama matundu ya risasi yakionekana kifuani mwake. Jeshi la Polisi linaendelea na uchunguzi wake ili kuwakama waliohusika na mauaji hayo…

Amata akakanyaga breki kali na kuitoa gari barabarani kwani taarifa hiyo haikujitosheleza kwake, akaegesha gari pembeni na kutazama huku na kule hakuona mtu kupita eneo hilo, pembeni yake kulikuwa na bar iliyokuwa ikiendelea kuburudisha watu kwa vinywaji na vilaji, akashuka na kuiendea, alipofika tu akakutana na mwanadada mrembo aliyevalia nguo nyeupe juu na sketi nyeusi chini.

“Karibu kaka, karibu kiti,” Yule dada akamkaribisha Amata huku akifuta meza iliyokuwa hapo. Ijapokua haikuwa nia ya Kamanda kuketi, akajikuta amefanya hivyo, “Pole!” neon hilo likaupasua moyo wa Amata akamtazama Yule dada Mhudumu wa bar.

“Pole ya nini?” akauliza

“Una damu kichwani,” akamwambia.

“Shiit!” akang’aka na kujigusa, kweli akahisi maumivu na kitu kama jeraha.

“Asante sana!” akamjibu, “Unaweza kunisaidia simu yako?” akamwuliza.

“Haina salio lakini, halafu ni kisimu cha tochi,” akajibu kwa aibu.

“Naomba hivyo hivyo.”

Yule mwanadada akachomoa simu yake akampatia Amata. Ilikuwa ni simu iliyochakaa, iliyoonekana kupita katika mikono mingi ya watu mpaka kuifikia mikono hii ya huyu Mhudumu wa baa. Ilifungwa kwa mipira ya manati, betri lake lilishikiliwa na kipande cha mpira wa manati. Hakujali, aliitazama vyema kasha akaanza kubofya hapa na pale.

“Haina vocha hiyo!” Yule Mhudumu akaeleza tena.

“Usijali, kaniletee Bia baridi sana bila glass tafadhali,” Kamanda akamwagiza Yule dada lakini alilotaka yeye haikuwa bia ila zile dakika mbili za kubaki peke yake. Vidole vyake vikaanza kutomasa tarakimu Fulani Fulani na alipomaliza, akapumzika, wakati huo bia yake ilikuwa imefika, akaigusa, akamwonesha Yule Mhudumu alama ya dole gumba, kisha akabaki na hamsini zake.
Meseji iliyofuata katika simu hiyo ilikuwa ni kutoka katika kampuni moja ya simu nchini, Kamanda Amata alikuwa amechukua muda wa hewani kwa namna yao ya siri na sasa simu ile Kimeo ilipata uhai.
Akaanza kupiga namba za maswahiba wake wa kazi, Chiba; simu haikuita kabisa, Madam S vivyo hivyo, akaduwaa wa sekunde kadhaa, haikuwa kawaida kwa watu hao kuwakosa kwenye simu, akili ya Kamanda ikiruka chogo chemba. Mbele yake kulikuwa na luninga kubwa iliyokuwa ikionesha matukio mbalimbali ya Kitaifa na lile lililomvutia ni ajali ya Salenda, alisahau kupiga simu na kutazama tukio lile. Kamanda Amata alikaza jicho kutazama picha hizo lakini hakuzitilia maanani kwani wakati wa mvua ajali kama hizo ni za kawaida sana.

“Kaka hadi bia imepoa!” Yule Mhudumu alipita tena kwenye ile mea aliyokaa Amata.

“Oh, sorry,” akamjibu kasha akainua chupa na kujijiminia mafunda kadhaa, alipoishusha ilikuwa nusu tu.
Akaitazama tena ile simu akabofya tarakimu nyingine, akaweka sikioni, simu ikaita na kuita haikupokelewa kama ilivyokuwa kwa simu za nyumbani za Chiba na Madam S, akashusha pumzi. Nini kinaendelea? Akajiuliza. Akarudia kuipiga namba ya mwisho, akaweka simu sikioni, baada ya dakika moja ile simu ikakwapuliwa na sauti nyororo ya kike ikasikika tofauti na alivyotegemea.

“…Polisi Kituo cha Kati, nikusaidie nini?” ile sauti ikauliza.

“Mwenye Ofisi, Inspekta Simbeye yupo?” Kamanda akauliza.

“…Inspekta leo alitoka kama mida ya saa tisa alasiri, hajarudi bado…” Yule mwanadada akajibu.

“Alisema kuwa atarudi au aliacha maagizo yoyote?” Kamanda akauliza.

“…alisema tu kuwa angerudi kabla ya saa kumi na ni kawaida yake kutoka saa tisa na kurudi saa kumi kila siku, lakini leo mpaka sasa hajarudi…” sauti ile iliendelea kueleza.
“We umeingia kazini saa ngapi?” akamwuliza.

“…nimeingia saa nane nitatoka saa nne usiku… samahani lakini naogea na nani?” Yule mwanadada alipouliza hivyo simu ikakatika.
Ndipo Kamanda alipojikuta hayuko peke yake mezani, mbele yake kulikuwa na mwanamke mmoja aliyevaa vazi refu jeusi, hijab na kujificha uso wote isipokuwa macho. Kamanda Amata akamtazama mtu huyo kwa tuo, akainua chupa yake na kupiga funda la mwisho, alipoishusha ilikuwa haina kitu ndani.

“Kwa nini unapenda kudhalilisha dini ya watu? Unaingia baa na vazi kama hilo?” Kamanda akaanza uchokozi, lakini Yule mtu hakujibu kitu, alikuwa akimwangalia tu. Jinni au! Akajiwazia, kabaridi ka haja kakapita kutoka utosini mpaka unyayoni.

§§§§§§
GINA aliegesha gari mita mia mbili hivi kutoka katika lango la kuingilia nyumba ya Madam S kule Masaki, akateremka na Jasmine akafanya vivyo hivyo, kisha wote wawili wakarudi taratibu wakiachina nafasi ya mita kadhaa katikati.
Lango la mbele lilikuwa limefungwa, Gina alitazama huku na huko hakuona hata dalili ya binadamu kupita myaa ule, isipokuwa manyunyu tu ya mvua yalikuwa yakimnyurunyuta mwilini mwake. Akajipapasa katika kiuno cha suruali yake na kufatua kijipini chenye ncha mbili zilizojikunja kwa mtindo wa pekee, kishapo akachukua kipini kingne kutoka kwenye kibanio cha nywele zake, akatanguliza kile chenye ncha mbili katika tundu la funguo ya lango hilo, akachukua kile cha tatu na kukitumbukiza kati, akafanya manuva kidogo tu, kitasa kutoka Uingereza kikafyatuka na kuuruhusu lango lile kuwa wazi.
Skunde mbili zikapita, ya tatu na ya nne bila Gina kuingia ndani ya wigo ule mkubwa, akatazama tena usalama, bado barabara ilikuwa tupu, hakumuona Jasmine, moja kwa moja akajua kuwa kwa vyovyote keshajiweka katika kona maalum ya kumlinda swahiba wake. Akaingia ndani ya wigo huku bastola yake aina ya Winchester ikiwa mkononi. Akatembea kwa hadhari kubwa huku na huko akitazama hakuona mtu. Hatua tatu kuelekea mlango wa nyumba hiyo, ndipo alipoona kitu kilichomshtua sana, akasimama mapigo ya moyo yakimwendea kasi kifuai mwake.

Mbele yake kulikuwa na mwili wa Binadamu uliolala chali ukiitupa mikono yake huku na huko, hakuwa na uhai. Gina akajiweka tayari kwani aliona huo unaweza kuwa mtego kwake, akatazama jumba la Madam S, taa za ndani zilikuwa zikiwaka kwa mwanga wa kupendeza, ina akajikuta anaishiwa nguvu, akainua mkono wake na kuizungusha saa yake kwa namna ya pekee kasha akaisogeza karibu na kinywa chake.

“…Jasmine …” akaita, hakupata jibu, akazidi kuingiwa na wasiwasi. Dina akatulia pembeni ya ule mwili, akahisi kama kuna mtu anayekuja nyuma yake, akakamata bastola yake barabara, liwalo na liwe, akageuka ghafla tayari kwa shambulizi, hakuna mtu.
Shiit! Akajisemea. Akauruka ule mwili na kuufikia mlango wa nyumba ile kubwa, akatoa gloves mfukoni na kuivaa, kisha akashika kitasa kwa mkono wa kushoto uliokuwa na gloves akaingia ndani ya sebule pana, iliyomlaki bila hiana. Kila kitu kilikuwa katika utulivu wa hali ya juu sana, hakukuonekana kama kulikuwa na purukushani yoyote ndani ya nyumba hiyo, akajivuta kuelekea chumba cha Madam S, akaufikia mlango na kuujaribu, ulikuwa umefungwa. Akatumia hila ileile na kuufungua. Hata chumbani kulikuwa tulivu kabisa, hakukuwa na ishara yoyote iliyoonesha kama kulikuwa na pambano la kufa na kupona.

Akaenda pembeni mwa kitanda upande wa kichwani, akachuchumaa na kubonya vijinamba Fulani vya kificho ambavyo kwa mtu wa kawaida huwezi kuvigungua mpaka mmiliki akuoneshe. Droo moja ikafunguka na ndani yake ikajifunua kompyuta kubwa ika simama mbele yake, Gina akatikisa kichwa juu chini, kwani alijua kama hiyo kompyuta haipo mahala pake basi hali ya Taifa iko hatarini. Alikumbuka maneno ya Madam S siku alipomkaribisha nyumbani kwake kwa mara ya kwanza.

….heri mimi nife lakini hii kompyuta ibaki. Nikifa au nikipotea kabla hamjatangaza kifo change hakikisheni mnang’oa kompyuta hii na kuikimbiza Shamba kisha mtangaze matanga. Siri yote ya Taifa hili ipo hapa, mipango yote mibaya na mizuri ipo humu, watu wote wabaya na wazuri wapo humu…

Gina alijikuta analia machozi peke yake, nifanyeje, niondoke nayo? Akajiuliza, nitaifikisha Shamba salama? Akajiuliza bila majibu. Gina alijikuta kachanganyikiwa, hajui la kufanya, aichukue au aiache, kichwani mwake alielewa kuichukua kompyuta hiyo ina maana kuwa Madam S kafa au katoweka, na je kama kuna wanaotaka na wameshindwa kuipata hatoweza kuwa kawarahisishia kazi?

Ulikuwa ni mgongano mkubwa wa mawazo kati ya roho, moyo na ubongo wake, akaamua kuiacha. Akabofya tena zile tarakimu na ile kompyuta ikajirudisha ndani taratibu na kujigia mahala pake. Gina akashusha pumzi ndefu, akaitazama bastola yake na kunyayuka taratibu, akaufuata mlango na kutoka akiufunga nyuma yake.

ITAENDELEA.

SEHEMU YA PILI

SEHAMU YA TATU

SEHEMU YA NNE

SEHEMU YA TANO
 
RIWAYA: KITISHO
MTUNZI: richard MWAMBE


Ulikuwa ni mgongano mkubwa wa mawazo kati ya roho, moyo na ubongo wake, akaamua kuiacha. Akabofya tena zile tarakimu na ile kompyuta ikajirudisha ndani taratibu na kujigia mahala pake. Gina akashusha pumzi ndefu, akaitazama bastola yake na kunyayuka taratibu, akaufuata mlango na kutoka akiufunga nyuma yake.

SEHEMU YA 2

KAWE – saa 4:02 usiku

LAND CRUISER ya polisi ilikuwa nje ya lango kubwa la nyumba ya Mheshimiwa Mbunge wa jimbo la Miroroso, wananchi wasio na dogo nao walijumuika nje ya nyumba hiyo wakikodoa kodoa macho kushangaa tukio hilo lisilo la kawaida. Hakuna aliyejali mvua ya rasharasha iliyokuwa ikiendelea kunyesha, watu walijikusanya kwa kujikunyata kutazama.
Ndani ya jumba hilo kulikuwa na Polisi waliovaa kiraia wenye bunduki kubwa kubwa wakiwa wanatembea hapa na pale, mwili wa marehemu Mbunge ulikuwa ndani ya chumba chake cha kulala. Polisi waliokuwa huko chumbani wakifanya taratibu zao za uchunguzi walikuwa wamekamilisha kazi yao, walitoka sebuleni na kuwapisha vijana wachache kutoka idara ya dharula ya kampuni binafsi ambayo husambaza gari za wagonjwa mitaani kwa minajiri ya kusaidia hali za dharula kama hizo.

Waliufunga sawia mwili wa Mheshimiwa katika mfuko maalumu na kuupakia kwenye machela yenye magurudumu, kasha wakaisukuma kuelekea kwenye gari yao iliyokuwa imeegeshwa pembeni tu mwa jumba hilo. Vilio vilisikika, wananchi wakalia na kuomboleza, walimpenda Mheshimiwa, ijapokuwa alipojenga jumba lake haikuwa jimboni mwake lakini bado alitoa misaada ya hali na mali kwa waliomzunguka.

“Alikuwa shujaa, kwa vyovyote wametumwa kumuua,” mwombolezaji mmoja alisikika akisema huku akifuta machozi yake.

Baada ya zoezi hilo ndipo Wananchi waliruhusiwa kuingia ndani na kuanza msiba huo. Hakuna aliyeamini kabisa juu ya lililotokea.
Lakini ilibaki hivyo kuwa Mbunge wa jimbo la Miroroso aliuawa na watu wasiojulikana.

§§§§§§

Kamanda Amata aliwekwa kati ya watu wawili huku mmoja na huku mwingine, mbele yake kulikuwa na mwingine tena ukiacha dereva aliyekuwa akiongoza gari hiyo. Wote walivaa maguo yaliyowaficha miili na sura zao. Hakuna aliyeongea; ile gari ilipita daraja la Salenda na kufuata uelekeo wa kwenda Mwenge, baada tu ya kupita daraja hilo, ikakunja kulia na kufuata ile Kenyata Drive, ilipomaliza maofisi ya Mabalozi iliiacha ile ya kwenda Coco Beach na kukunja kushoto, nyumba ya nne mbele ikasimama.

“Usilete makeke yako ya kipumbavu, tunataka kompyuta anayotumia boss wako basi,” akaambiwa na kuteremshwa chini, wakauendea mlango mkubwa na kuufungua, Kamanda Amata akatangulia mbele na wale jamaa wakamfuata nyuma, wote watatu walkuwa na Shot Gun mikononi mwao.
Wakatembea taratibu na kuipita ile maiti pale nje, moja kwa moja wakaingia ndani ya sebule, mmoja wao akasimama nje ya mlango wa sebule kuweka usalama, mwingine akabaki sebuleni na wa mwisho akaenda na Amata mpaka chumba cha Madam S.

“Usilete ujanja wako, tunajua kuwa ni wewe tu unayeweza kuitoa hiyo kompyuta hapo, haya fanya hivyo,” akamwambia huku akiwa kasimama umbali wa mita kama mbili hivi. Kamanda Amata akaiendea ile droo na kuingza mkono wake mahala Fulani, akapapasa anavyojua yeye, mara ile droo ikajivuta mbele na kufunguka, hakuna kompyuta! Yule mjinga akabaki katoa macho, akashangaa mahala pale hakuna kompyuta waliyokuwa wanaitaka ilhali wao walikuwa na uhakika kuwa ipo hapo baada ya kufanya uchunguzi wa kina.

“Haipo?” akauliza.

“Si unaona mwenyewe haipo!” Kamanda akajibu.

“Imeenda wapi?” akarusha swali la kijinga.

“Mimi na wewe tumeingia pamoja sasa nitajuaje ilipokwenda?” Kamanda akajibu kwa swali. Kama kuna kosa alilolifanya Yule mtekaji na atalijutia kuzimu ni ktendo cha kwenda kuhakikisha kwa macho kuwa Kompyuta ile haipo pale. Kamanda Amata kama umeme, kutoka pale alipokuwa amechuchumaa kuitoa ile Kompyuta, alijikunjua na kutawanya miguu yake sentimeta mbili kutoka usawa wa sakafu, Yule mjinga alipigwa ngwala kutoka upande wa nyuma na kujibwaga akitanguliza kisogo, yowe na kishindo vilimshtua Yule wa sebuleni akaja kwa kasi. Kamanda Amata alijirusha upande wa pili wa chumba na risasi zilizotoka katika bunduki ya Yule mtu wa pili zikachimba sakafu.
Kabla Yule bwana hajajiweka sawa, mwendo wa sekunde moja tu aliyoitumia kufanya shabaha ya pili dhidi ya Kamanda Amata, alijikuta akipaishwa juu na kujibwaga kama mzigo sakafuni tayari damu ilikuwa ikimtoka kama bomba. Amata alishuhudia hilo kwa haraka sana hakuelewa nini kinatokea.
Wamegeukana? Akajiuliza.

“Upo salama Kamanda Jitokeze!” sauti ya Gina ilimrudishia matuamaini. Kamanda Amata akajitokeza mzima mzima, lo! Domo la shot gun lilikuwa likimtazama umbali wa mita tatu tu kutoka pale alipo.

“Umeharibu utaratibu, nilikwambia usifanye makeke yoyote sasa wewe umekiuka kanuni, namuua huyu Malaya wako kasha naondoka na wewe,” sauti ya mtekaji ilisikika. Kamanda Amata akaona sasa mchezo usio rasmi unaanza kwani hakuwa na taarifa yoyote juu ya hii hatari.

“Umeshasema Malaya, we muue tu, hana thamani kwangu!” Kamanda akajibu.

“Leo hana thamani kwako wakati kila siku unamlala nyumbani kwako!” Yule mtekaji akaendele kuropoka, maneno ambayo yalimtia hasira Gina, akajaribu kukukuruka lakini hakuweza kutoka kwani kono la mtekaji lilimbana koo na akajihisi kukosa pumzi. Kamanda Amata alaimtazama Gina anavyoteseka, akawasiliana naye kwa macho, gina alielewa kitendo alichokifanya Kamanda.

Gina aliachia mkono wake kutoka kwenye ule wa Mtekaji lakini bado alikuwa kabanwa kwa kabala, akajizungusha na kukamata uume wa mtekaji huyo, akaubana kwa nguvu na kuuzungusha ghafla. Yule mtekaji akapiga kelele za maumivu, akamwachia Gina akabaki katoa macho ya kutisha, Gina akaendelea kuuzungusha huku amezikamata na korodani zake, Yule mtekaji akaanguka chini, Gina hakumwachia mpaka alipohakikisha kamtoa roho.

“Asante Gina!” Kamanda akamshukuru wakakumbatiana.

“Kompyuta Gina,” Kamanda akamwambia.

“Usiwe na shaka, nimekwishaitoa muda mrefu, wakati naondoka ndipo nilipoona hiyo gari inakuja, nikajibana hapo kwenye kochi kubwa upande wa nyuma hamkuniona. Niliposikia kile kishindo huko chumbani mlipo, nikajua kumekucha, nikamwona huyu wa sebuleni akija kwa kasi huko ndani, name nikajitokeza kumwahi kabla hajaleta madhara, ndipo nikamfumua bichwa lake, lakini sikujua kama kuna mwingine huku nje ndo huyu mpumbavu akanibana kabala. Pole sana Kamanda, nafurahi kukuona, Idara imetikiswa!” Gina alieleza kinachojiri.

“Gina haina haja ya kukaa hapa, twende tukajipange juu ya hili,” Kamanda akamwambia huku wakitoka. Walipofika karibu na geti, Gina akauchukua begi kubwa alilokuwa amelificha hapo wakatoka nje.

“We ulikujaje hapa?” kamanda akamwuliza.

“Shiiit!” Gina aling’aka baada ya kugeuka na kutoiona gari aliyokuja nayo. Akageuka kwa Kamanda na kumtazama usoni.

“Dr. Jasmine!” akamwambia huku chozi likimtoka. Amata akamtazama na kisha akaliendea lile gari walilokuja nalo na wale watekaji, akaingia, bahati nzuri halikuhitaji ufunguo, lilikuwa ni la kubonya tu nalo likawaka, wakaingia barabarani kuondoka.

KUZIMU – shimo la mauti

Kilikuwa chumba kikubwa chenye vijichumba vingi vidogo kwa vikubwa, kwa ujumla kilitisha kwani mafuvu ya vichwa vya binadamu yalipambwa ukutani kama mapambo ya kawaida, taa nyekundu kwa buluu ndizo zilizong’aza eneo hilo la kutisha, kulikuwa na friji kubwa mithiri ya chumba cha kuhifadhia maiti. Sehemu nyingine kulikuwa na stoo iliyohifadhi kila aina ya vikorokoro vya kutisha maalumu kwa ajili ya kutesea, kunyongea, na hata kuulia kabisa.
Chumba hiki kilijengwa chini kabisa ya jumba la kifahari la Mhindi Pancho Panchilio eneo la Kerege njia ya kwenda Bagamoyo, hakuna aiyejua kinachoendelea. Kwa nje lilikuwa ni jumba linalovutia kuliangalia, asilimia kubwa ya wananchi wa eneo hilo hawakuwahi kumjua wala kumwona mmiliki wa kasri hilo, ni watoto tu waliopenda kusemajumba lile ni la wanyonya damu kutokana na mambo kadhaa waliyokuwa wakiyaona, mara watu wameletwa huku nyuso zao zimefungwa vitambaa vyeusi na mambo kadha wa kadha kiasi kwamba ilipelekea watoto wa kitongoji hicho kukaa mbali na jumba hilo.
Lakini tofauti na watu wazima, wao waliwachapa fimbo watoto wao waliokuwa wakisema maneno hayo kutokana na kwamba kutoka ndani ya jumba hilo waliweza kupelekewa maji safi kwa mabomba maalum yaliyounganishwa na pampu kubwa na yenye nguvu, hivyo waliondokana na kero ya maji ya kunywa.

Mwili wa Madam S ulibwagwa chini kama roba la chumvi, haukuwa na uzima wowote.
Kibosho, akaangalia hali ya chumba kizima walichouhifadhi mwili huo, aliporidhika nacho akatikisa kichwa juu chini na kuwageukia watu wake.

“Ulinzi wa nguvu zaidi ya ule wa Ikulu, sawa?” akaagiza.

“Sawa Mkuu!” wakajibu. Akawaacha na kutoka, akaelekea chumba kingine, akakuta vijana wakimsulubu vikali Chiba wa Chiba huku akiwa ananing’inia kwenye minyororo, mwili wote ulitota damu, hakutamanika, hakuangalika. Kibosho alisimama mlangoni.

“Karibu sana kuzimu!” akamwambia Chiba aliyekuwa hawezi hata kuinua uso, “Wewe ndiye kinara wa kuvuruga mitandao ya watu sivyo, sasa utakuwa binadamu wa kwanza kushuhudia kifo chako mwenyewe baada ya kuwaona wenzako wote wako hapa, mbuzi nyie, nani aliwadanganya kuwa mna uwezo wa Kijasusi wa kuitisha Dunia? Sasa leo mtapambana na Shetani nah ii ndiyo himaya yake,” akaongeza kusema kisha akageuka kando akawatazama vijana wake walioonekana wana uchu wa kuua.

“Na Yule bibi, mfungeni kama huyu, lakini msimtese mpaka azinduke kama bado hajafa ili mateso yote ayashuhudie kwa akili na ufahamu wake, nimekuja hapa kwa kazi moja tu,” akamgeukia Chiba “Kuua!” akamaliza na kutoka huku akifuatiwa na vijana watatu wenye misuli ya ajabu. Chiba akiwa katika ile minyororo hakufanya lolote zaidi ya kutulia tu na kusubiri kuona nini kinaendelea.

§§§§§

Kamanda Amata waliitelekeza ile gari eneo la Hoteli ya Sheratoni na kisha wao kutembea kwa miguu mpaka ilipo ofisi ya Madam S. ilikuwa tayari imepita saa tano usiku, walinzi wakawapokea na kuwaruhusu kupita kwani walishazoea kuwa muda wowote watu hao huwa wanaingia ofisini. Moja kwa moja jicho la Kamanda Amata likaenda kwenye maegesho na hakuliona gari la Madam S, wakaingia ofisini na kuketi katika viti vyao kwa namba zao, kwani katika ofisi hiyo kila moja alikuwa na kiti chake kadiri ya namba zao za kikazi. Ukimya ulichukua nafasi kati yao, hakuna aliyeongea kwa sababu wakiwa hapo ni Madam S huwa anasema alichowaitia.
Kamanda Amata akamgeukia Gina.

“Gina, hili eneo si salama kwa sasa!” akamwambia.

“Yaani mi sina amani na eneo lolote, hata kitanda change nakiogopa, natamani kutoroka,” akajibu.

“Kutoroka! Sio suluhisho,” Kamanda akamwambia huku akinyanyuka na kufungua jokofu lililowekwa vinywaji vya kila aina, akatoa Konyagi ndogo na kuketi kitini, akachanganya na Sprite kisha akanywa taratibu. Gina alionekana kuwa mwenye mawazo mengi sana. Wakiwa katka ukimya huo mara simu ya mezani ikaita kwa fujo. Kila mmoja aliitazama hakuna aliyeipokea, baada ya kukerwa na kelele ya chombo hicho Kamanda Amata akaiinua na kuiweka sikioni bila kuongea.

“Kamanda Amata”, kisha cheko zito na la dharau likafuata, “…leo mtaishi kama digidigi, na nitawafuata popote mlipo mpaka nihakikishe nawamaliza, kwa taarifa yako, kibibi chako ninacho hapa nusu mfu, na wengine wawili, mmoja tayari ni marehemu kama unataka kumwona nenda kwenye vichaka vya Gongo la Mboto njia panda ya kwenda kwenye makaburi ya Wachina… tuachane na hilo, naihitaji hiyo kompyuta usiku huu… nipe kompyuta nikupe marehemu wako ukazike…”
Hasira ya Kamanda Amata ikawaka juu ya huyo asiyemwona,

“…kama unaitaka hii kompyuta njoo uichukue!” akamjibu.

“…Nataka uniletee wewe mwenyewe kwa mkono wako au huyo Malaya wako ambaye pamoja nawe mmeshanipotezea watu wangu watatu, kama hamtaki basi nitaichukua mwenyewe…” ile sauti ikaendelea.

“Acha uoga wewe! Kama unajiamini jitokeze tupambane, atakayeshinda atachukua kompyuta!” Kamanda akaongea kwa jazba, tayari konyagi ilishaanza kufanya kazi ichwani.
Yule mtu wa upande wa pili akacheka sana kisha akaendelea

“…sifanyi hiyo michezo ya kitoto, lakini nakuhakikishia kuwa nitaipata hiyo kompyuta, na nitazichukua roho zenu wote sita kabla ya jua kuchomoza,” akapiga mkwara.

“Na mimi nakuhakikishia kuwa nitakuwa nimekwisha kutoa roho yako na vibaraka wako kabla ya jua kuchomoza, shetani wewe!” alipomaliza kusema hayo, akainuka kitini.

“Unaenda wapi Kamanda?” Gina akauliza.

“Huyu mshenzi keshanitia wazimu, nitahakikisha namjua usiku huu huu na namng’oa koromeo lake, hawezi kufanya dharau na kitengo nyeti kama hiki, huyu hafai kuishi,” Amata aliongea kwa hasira.
Gina naye akasimama wima na lile begi lenye kompyuta mkononi, “Na hii je? Maana inaonekana wana uchu nayo,” akamwambia Amata.

“Tia kwenye sefu salama hapo hata uje na kifaru huwezi kuitoa,” akamweleza.

“Sijui namba za kufungulia,”

“Oh, sorry!” Kamanda akaichukua ile kompyuta na kuingia kwenye kijichumba kidogo kisha akaiweka mahala salama na kutoka na lile begi, akafungua kabati linguine na kutoa kompyuta iliyofanana na ile lakini ilikuwa mbovu siku nyingi, akaipachua hard disk na kulichukua lile ganda tupu akalitia kwenye begi, kisha wakatoka na kuchukua gari mojawapo iliyo kwenye maegesho.

“Gina, upo vizuri? Akili ipo sawa?” Kamanda akamwuliza. Gina hakujibu, alionekana kujawa na hofu kuu, Kamanda akamwangalia na kumwuliza tena.

“Gina, unakumbuka The Art f War?” akamwuliza.

“Hapana Kamanda!” akajibu. Kamanda Amata akatikisa kichwa baada ya jibu hilo.

“Gina wewe ni mwana usalama na haya mambo umejifunza chuoni hutakiwi kusahau mama, sawa?”

“Sawa!”

“Sikiliza Sun Tzu aliandika ‘Jifanye mchovu unapokuwa na nguvu na jifanye una nguvu unapokuwa mchovu’, hata mimi Gina ninaogopa maana simjui adui yangu kasimama wapi, lakini lazima na mimi nimtishe hiyo ndiyo Art Of War,” Kamanda alimtoa hofu Gina.

“Nimekuelewa Kamanda, sasa tunapambana vipi na huyu hayawani?” Gina akauliza. Kamanda akabaki kimya kwa muda, kisha akamgeukia Gina.

“Gina, naomba nisikujibu, na wala usinambie unachofikiria, unajua kwa nini?” akamuuliza.

“Hapana!” akajibu.

“Art of War inasema ‘Ifanye mipango yako iwe siri, isipenyeke kama giza la usiku, na unapojitokeza jitokeze kwa nguvu kama radi’ sio maneno yangu nia Sun Tzu na daima huwa napenda kufuata maneno yake ndiyo maana unaona hapa nilipo,” alipotaka kupachika ufunguo kwenye switchi ya gari Gina akamdaka mkono.

“Kamanda! Hayo uliyosema si ajabu hata adui anayajua,” akafungua mlango na kumvuta Kamanda nje, kisha wakaelekea getini na kutoka nje mpaka barabarani.

“Naona sasa umeanza kujua unalotakiwa kufanya, vizuri sana Gina!” Kamanda akampongeza kisha wakaingia kwenye tax na kutokomea.

Breki ya kwanza ilikuwa mje ya ukumbi wa Jiji mkabala na bandari ya boti za Zanzibar, wakalipa na kisha wakapotelea gizani.

ITAENDELEA.
 
Karibuni twende pamoja tupate burudani hii murua kabisa, usichelewe itakapofika mwisho itafutwa hapa
 
RIWAYA: KITISHO
MTUNZI: richard MWAMBE


“Kamanda! Hayo uliyosema si ajabu hata adui anayajua,” akafungua mlango na kumvuta Kamanda nje, kisha wakaelekea getini na kutoka nje mpaka barabarani.
“Naona sasa umeanza kujua unalotakiwa kufanya, vizuri sana Gina!” Kamanda akampongeza kisha wakaingia kwenye tax na kutokomea.
Breki ya kwanza ilikuwa mje ya ukumbi wa Jiji mkabala na bandari ya boti za Zanzibar, wakalipa na kisha wakapotelea gizani.

SEHEMU YA 03

Katika kaunta ya kituo cha Polisi cha Kati, kulikuwa na PC wawili na WP mmoja, Kamanda Amata na Gina walikwea ngazi na kusimama mbele yao. Wale Polisi mara moja walimtambua Gina na kusimama imara kwa kumpa heshima yake ya kijeshi.

“Inspekta Simbeye, ameonakana tena huku?” Gina akauliza.

“Yupo afande, amekuja muda si mrefu,” Yule WP akajibu.

“Naomba tumwone!” Gina akasema hayo huku tayari ameshaanza safari ya kuifuata ofisi hiyo.
Inspekta Simbeye alionekana kuzeeka ghafla kwani mashavu yake yalikuwa yameshuka kiasi kwamba Kamanda Amata alitamani kucheka.

“Shikamoo mzee!” Amata alianza kwa kuamkia kama kawaida akikutana na Inspekta huyo.

“Sina haja ya shikamoo yako, nakupigia simu Amata hupatikani kwa nini?” akauliza kwa hasira.

“Inspekta, kama ulivyowakosa wengine wote na mimi pia usingeshangaa, hata mimi sina mji wa kupokea, hali ni mbaya, nilikutafuta ulikuwa umetoka,” kamanda akajibu.

“Kamanda Amata! Ni nani huyu anayetufanya sisi wapumbavu kiasi hiki, Mheshimiwa Mbunge wa Miroroso ameuawa usiku wa leo, ni masaa mawili tu yalopita,” kabla hajaendelea Kamanda akamkatisha.

“Na hilo hasa ndilo limenileta kwako, nilitaka kujua ni nani aliyeuawa maana nimesikia tua lakini sikujua ni nani aliyeuawa!”

“Ni Mbunge wa Miroroso,” Simbeye akajibu.

“Ok, nimeelewa Inspekta, sasa picha inaanza kujijenga taratibu na itakamilika tu,” Kamanda akajibu.

“Huu umekuwa usiku mbaya sana, siwezi kulala kwa kuwa kifo cha huyu Mbunge kimekuja wakati mambo haya ya vita vya Ufisadi mliyopambana nayo huko Uswizz bado hayajapoa, na huyu Mbunge ndiye alikuwa mstari wa mbele kabisa katika kuyafichua, je huu si mnyororo mmoja?” Inspekta akaonesha wazi hofu yake.

“Nimekupata Inspekta, naomba niondoke kisha tuwasiliane dakika arobaini na tano zijazo,” Kamanda akajibu kisha akaondoka na kufuatiwa na Gina.

HOSPITALI YA TAIFA MUHIMBILI- SAA 6:47 USIKU

KAMANDA Amata akifuatana na Gina waliingia moja kwa moja chumba cha kuhifadhia maiti cha hospitali hiyo, wakamkuta Daktari akiendelea na uchunguzi. Wakiwa wanaongozwa na muuguzi waliingia ndani ya chumba hicho. Walipofika wakaonesha vitambulisho vyao kwa Yule daktari, hivyo hakuwatilia shaka.

“Karibuni sana!” akawakaribisha.

“Asante!” Gina akawa wa kwanza kujibu.

“Sijui niwasaidie nini? Maana nimechoshwa na maswali yenu yanayofanana,” Yule daktari akauliza huku akiwa amesitisha kuendelea kufanya uchunguzi.

“Nataka kujua maraehemu amekufaje?” Kamanda akauliza.

“Amepigwa risasi,” akajibu daktari.

“Ngapi?” Gina akawahi.

“Mbili za kifuani,” akajibu.

Kamanda Amata akasogea jirani na kutazama yale majeraha yalivyojipanga, moyo wake ukapiga chogo chemba, yalikuwa mithiri ya yale ya Frederick Masawe na Petit kule Uswizz, akatazama kwenye paji la uso la marehemu akaona alama ndogo ya risasi nyembamba iliyopenye bila uharibifu.

“Daktari, nah ii je?” akauliza. Yule Daktari akasogea na kwa kutumia kurunzi yake maalumu akagundua tundu hilo, wakamgeuza marehemu na kisogozi wakakuta matone machache ya damu.

“Amepigwa risasi tatu,” Kamanda akaeleza, “Asante Daktari, tulitaka kujua hilo tu,” wakamwacha na kuondoka zao.

“Kamanda hii kazi nyingine sasa,” Gina akamwambia Amata.

“Usijali Gina, hii kazi lazima imalizike usiku huu, kimya kimya mpaka kitaeleweka, leo nataka tufanye kazi hii ngumu mi na wewe tu, jua likichomoza tujue nini tumefanya na dunia ya pili isijue nini kimefanyika, usiogope, Art Of War iliyoandikwa na Sun Tzu inasema ‘Nenda taratibu kama upepo na muwe karibu kama miti. Shambulia kama moto na uwe imara kama Mlima’” Kamanda akamwambia Gina huku wakitoka nje ya chumba hicho.

“Twende nyumbani kwanza tukachukue dhana za kutosha kisha tuingie rasmi kwenye mpambano, tufanye haraka kabla watu wetu hawajapata madhara zaidi, Gina, piga simu Polisi Mabatini waambie kuna mwili wa marehemu kule Gongo la Mboto ili waende kutazama, na kama adui alitegemea kutunasa huko atapambana na vijana wa khaki,” Kamanda alimwambia Gina na mara baada ya Gina kufanya hivyo, wakaingia kwenye Tax.

“Kinondoni makaburini tafadhali!” Kamanda akamwambia dereva tax, kisha wakaondoka eneo hilo. Baada ya kuuacha Mtaa wa Mindu na kuchukua barabara ya Umoja wa Mataifa ndipo kamanda alipogundua kuwa kuna gari ikiwafuata, akamtazama dereva ambaye alionekana hajui chochote, walipopita shule ya Sekondari Tambaza ile gari ikawapita kwa kasi na kuwazuia kwa mbele.
Watu watatu walishuka kwa kasi kwenye ile gari, mikononi wakiwa na Shot Gun, waliishambulia ile tax kwa risasi na kuichakaza vibaya.
Kamanda Amata alimvuta dereva na kumsweka chini, mtawanyiko wa vyoo uliwafanya kushindwa kufanaya lolote, Gina alishuhudia lile begi likinyakuliwa na alipotaka kulitetea alipigwa na kitako cha bunduki akarudi chini, wale jamaa wakaondoka kwa kasi na gari yao wakapotelea katika mitaa ya Upanga.

Kamanda Amata akajinyanyua na kutoka nje, akamtoa Gina kisha Yule dereva ambaye alikuwa katika hali mbaya, hakuguswa na risasi lakini hofu ya milio ya zile mashine ilimfanya kuachia mkojo bila kujijua.
Kamanda Amata akachomoa kadi moja ya kibiashara na kumpatia Yule kijana, “Kesho jioni unitafute!” kisha yeye na Gina wakapotea eneo lile kabla Polisi hawajafika.
Walipokuwa wakikimbia, Gina alikuwa akiishiwa nguvu kila muda ukienda.

“Kamanda, Kamanda! Nakufa!” alilalamika.

“Jikaze Gina!” akamhimiza lakini hali haikuwa nzuri, Gina akaanguka chini. Kamanda akamtazama vizuri akaona mchaniko mkubwa a kichwani na damu zikimvuja eneo moja la mgongo karibu na nyonga, ilikuwa ni risasi iliyompata barabara katika eneo hilo.

“Shiiitttt!”

Akatazama huku na kule, akaona gari ikija kwa mbali, akamweka Gina chini na kuizuia kwa kuingia barabarani, hakuuliza, alimbeba Gina haraka na kumwingiza kwenye gari.

“Nifikishe Mtaa wa Upanga Seaview haraka!” akaamuru.

“Aliyekwambia hii tax ni nani?” Yule deeva akajibu kijeuri huku akizima gari na kuchomoa ufunguo. Kamanda Amata hakuwa na muda wa kupoteza, alfungua mlango akazunguka upande wa dereva, akafyatu lock na kumvuta nje, akamtupia barabarani kisha akakaa kwenye usukani, akachomoa kadi yake ya benki na kuivunja katikati, akaislaidi, katikati yake pakatokea ufunguo mdogo wenye meno mawili akaupachika kwenye swichi ya gari n kuiwasha kisha akaingia barabarani na kumwacha Yule mmiliki wa gari akipiga kelele.

§§§§§

SAA saba na nusu usiku ilimkuta Kamanda Amata katika jumba kubwa lililojengwa kandokando ya bahari ya Hindi huko Upanga, akaegesha gari mahala pake kisha akamtoa Gina ambaye tayari alikuwa amekwishapoteza fahamu.
“Usife Gina, usife tafadhali, subiri kidogo Gina!” kamanda alikuwa akiongea kama aliyechanganyikiwa huku kambeba Gina katika mikono yake akielekea ndani ya jumba hilo.
Dr. Khadrai alikuwa mlangoni akimwangalia kijana huyo ambaye wamekutana mara chache sana katika harakati za maisha yao.

“Karibu Amata, pole sana!” akamkaribisha na kumwongoza moja kwa moja mpaka kwenye chumba maalum ambacho kilishehenu kila aina ya kifaa tiba unachokijua, akamwonesha kitanda pa kumlaza Gina. Dr. Khadrai akamtazama Gina harakaharaka kisha akamtazama kamanda Amata. Akavuta mashine yake kubwa na kuchukua trei iliyojaa vikorokoro kisha akaanza kazi yake ya kitabibu, kwa kumsafisha Gina majeraha na kumtoa risasi iliyokuwa imenasa ndani. Kamanda Amata hakuwa na muda wa kusubiri.

“Daktari, maadam yuko mikononi mwako, naomba niende, kama kuna shida yoyote naomba unitaarifu kwa namba hizi,” akampa namba za Gina, kisha yeye akachukua simu mbili za Gina, akachukua saa na kumwachia simu moja ndogo ambayo si rahisi kwa mtu mwingine kuitumia kwa jinsi ilivyo.

“Amata usiwe na wasiwasi, huyu hajadhurika sana, akiamka tu nitakwambia,” kisha akaendelea na kazi yake.

KEREGE – saa 7:35 usiku.

PANCHO Panchilio alishusha siga alilokuwa amelipachika kinywani mwake na kulibana kwenye kibompoli maalumu cha kuzimia dubwasha hilo. Akainua macho yake na kutega masikio akisikiliza michakacho ya miguu ya mtu aliyekuwa akitembea sebuleni. Kwa jinsi alivyoijenga nyumba yake hiyo, yeye aliweza kumwona kila mtu lakini wale watu hawakuweza kumwona yeye nah ii iliwafanya kusikia sauti daima na kutokuona sura ya bosi wao.

“Karibu sana!” sauti yake ikaijaza sebule yote.

“Mkuu tumefanikiwa kuipata kompyuta uliyotuagiza Mkuu!,” Yule mtu akasema.

“Vizuri sana, sikufanya kosa kabisa kuwachagua ninyi watu makini katka kazi hii, je wale hayawani wawili mmewapata?” akauliza.

“Hapana hatujawapata lakini bila shaka wamefia kwenye gari waliyokuwa wakiitumia kwani tumeishambulia kwa risasi za kutosha,” akajibu, mara hakusikia kitu zaidi ya ukimya uliofuwatiwa na sonyo refu.

“Fanculato!” akatukana, “Kwa nini msihakikishe kama amekufa? Yule bwana ni hatari sana, hakikisheni mnapata habari zake usiku huu, naitaka roho yake kabla hakujapambazuka, potea!” akamukuza.
Pancho Panchilio alikuwa amekodi vikosi viatatu kwa nyakati tofauti na vyote kuvipa kazi moja tu ya kukisambaratisha kikosi cha TSA kuanzia Madam S mpaka wa mwisho. Mipango ya kazi hiyo ilipangwa kitaalamu sana na ilitumia mbinu za hali ya juu, mpaka dakika hiyo alikuwa tayari amefanikisha kwa asilimia sitini ya kile alichokidhamiria, nab ado muda wake bado ulikuwa unaruhusu kumalizia asilimia zilizobaki. Alihakikisha vikosi vyake hivyo havijuani na wala havikutani lakini vyote alikuwa amevipa kazi ileile kwa saa zilezile za kutekeleza lakini muda tofauti wa kufanya kazi.

Hakuona hasara sana kwa kupoteza vijana watatu usiku ule yeye aliishupalia dhamira yake tu ndio maana alikodi watu hao.
Kikosi cha kwanza kiliongozwa na Kibosho, Kanali wa jeshi aliyehasi na kupotea pasikojulikana, sasa alirudi baada ya kuitwa na Mhinidi huyo kwa kufanya kazi kama hizo. Kikosi cha pili kiliongozwa na mtu mmoja hatari kutoka nchi jirani aiyejulikana kama Kaburu na kikosi cha tatu kiliongozwa na mpiganaji aliyebobea kwenye taaluma ya kuua bila kukusidia huyu alikuwa ni mtaalmu wa kucheza na kifo mbele ya binadamu yeyote Yule, ni jambazi la kimataifa kutoka Kigoma, alijulikana kama Naima.

Hawa wote walipewa kazi kwa nyakati tofauti na wenyewe hawakujuana kama wana kazi moja kwa maana kila mtu hiyo ilikuwa ni siri kwake. Walipewa saa kumi na mbili za usiku tu kukamilisha kazi hiyo ngumu. Nao waliwasaka wabaya wao kwa hali na mali kuhakikisha wanamfurahisha bosi wao, malipo waliyopewa ni makubwa na yaliwapa jeuri ya kufanya hivyo.
Usiku huo kwao, ulikuwa usiku wa kazi.

3
KAMANDA Amata alikuwa kachanganyikiwa akili kwa namna moja au nyingine, alikuwa akiona kama ndoto inayotokea mbele yake, hakuamini kama wamewahiwa namna hiyo na kwa kasi ya ajabu, alijiuliza kila wakati ni nani mwenye uwezo wa kuwanasa namna hiyo, hakupata jibu zaidi ya hapo aligundua kuwa kwa vyovyote ni watu hatari wanaojua nini wanafanya na kwa wakati pia alielewa watu hao wamepewa kazi kwa muda maalumu hivyo nay eye kama ilimpasa kuwa saidia wenzake alitakiwa ajipe muda maalum na muda wa kazi yake uwe mdogo kuiko muda wa adui zake pia ucheze ndani ya muda wa adui zake. Alitikisa kichwa kana kwamba kuna mdudu akimtembea kwenye ubongo wake, akaitazama saa yake, saa zinayoyoma kwelikweli.

Ilikuwa inakaribia saa nane usiku alipokuwa akifungua geti la nyumbani kwake, akaingia na kulifunga nyuma yake, kisha akasimama kidogo kuangalia nini kinaendelea huku na kule, kwa macho yake makali aliweza kuona ua moja kubwa likitikisika kidogo, akaelewa wazi kuwa mtikiso huo lazima kuna kitu na si wa upepo kwani hali yah ewe ilikuwa imetulia sana na haikuwa na upepo. Damu ikamtembe haraka mwilini, hakufanya lolote, akauendea mlango wa nyumba kubwa na alipoufikia alikuta karatasi iliyoning’inizwa mlangoni, kisu chembamba chenye makali kuwili kilitumika kuishikia hiyo karatasi pale mlango.

Mwisho wa zama zenu umekwisha, mtaongea na Ngurumo.
Ulikuwa ujumbe uliosomeka katika karatasi hiyo pale juu. Akakikamata kile kisu na kukichomoa kwa nguvu, akakibusu, akaiokota ile karatasi na kuishika mkononi kisha akaingia ndani na kuuacha mlango wa nyumba yake bila kuufunga makusudi tu. Moja kwa moja akakiendea chumba chake na kufungua kabati kubwa lililokuwa mbele yake. Akavuta fulana yake nyeusi kaba shingo ya mikono mirefu akaivaa ikitanguliwa na vesti nyeusi pia. Kizibao cheusi chenye mifuko mingi ya kuwekea zana mbalimbali kikafuata juu yake, na zana zake zikapachikwa, bastola nne zilizosheheni risasi zikakaa mahala pake, visu vidogodogo vikawekwa mahala pake, paketi za risasi zikawekwa mahala pake, Shotgun mbili zikabanwa mahala pake nazo zikiwa zimetimia. Akakusanya vikolokolo vya kutosha kwa pambano hilo ambalo hakujua ni nani haswa anakwenda kupambana naye.

Akiwa kasimama kwenye kioo, anajiweka sawa, akahisi vinyweleo vyake vikisimama, mwili ukamsisimka, akajua kuna jambo, akalisubiri huku akijifanya hajui lolote.
Palepale kwenye kioo alimuona mtu akiingia kwa minyato kumfuata, Kamanda alitamani kucheka kwa sababu hata kama alikuwa akinyata wakati yeye alikuwa akimuona kwenye kioo ni kazi bure. Akamsubiri amkaribie ili ajue nini cha kumfanya. Yule mtu akajiandaa kwa waya aliokuwa kaufunga kutoka mkono hu mpaka ule mwingine.
Anataka kunikaba, Kamanda akawaza. Kisha kwa kasi ya ajabu akageuka na guu lake lenye nguvu likatua kichwani mwa Yule mtu, akajibwaga na kujibamiza kwenye mwamba wa kitanda, yowe la maumivu likamtoka, kabla hajafanya lolote akamnyanyua na kumpa kichapo kikali, alipohakikisha kuwa hali aliyokuwa nayo hawezi fanya lolote akamkalisha chini na kumwegemeza ukutani, akamtikisa na kumtazama usoni.

“Nani bosi wako?” akamwuliza.

“Si-si-simjui!” akajibu kwa tabu.

“Unaniletea utani siyo?” akamwuliza kwa ukali.

“Kweli simjui, mi natumwa tu na kulipwa ujira mkubwa wa kunitosha, kwa hali ya nchi yetu nakubali kufanya kazi yoyote kwa malipo yoyote,” akajieleza.

“Nafikiri hunijui sawa sawa sasa utanijua!” Kamanda akamwambia kisha akamkamata korodani zake na kuziminya kwa nguvu.

“Aaaaaiiiiggggghhhh…. Niache, niache nitasema,” akalia kwa uchungu.

“Sema, nani bosi wako, nani aliyekutuma kuja hapa?” kamanda akauliza sasa kwa ukali zaidi.

“Kweli kaka sim-ju-jui…” akajibu huku akijigeuza geuza.
Kabla Kamanda hajauliza linguine, akashuhudia povu jeupe likitoka kinywani mwa Yule mtu.

“Shiiit! Limejiua,” akang’aka kwa sauti, akaanza kumpekua.
Katika moja ya mfuko wa suruali yake akatoa simu ya mkononi, zaidi ya hapo hakuona chochote cha maana. Akaitazama ile simu, akaenda kwenye kitabu cha majina akakuta majina matano tu, la kwanza kabisa likamvutia, lilikuwa limeandikwa kwa jina moja tu ‘Naima’, kisha akaliangalia la pili na la tatu. Akaamua kuanza kampeni na jina hilo la kwanza.

Akaperuzi upande wa ujumbe mfupi, akakutana na ujumbe kutoka kwa Naima uliotumwa ndani ya dakika kumi zilizopita lakini ulionekana kutojibiwa.

‘…Akifika nijulishe nije nimalize kazi…’

Ujumbe ulisema hivyo.
Lilifikiri litaniweza, sasa naanza na Naima, kawaza na kuamua kuujibu ule ujumbe.
Kamanda Amata akaujibu ule ujumbe, kisha akaburuza mwili wa Yule mtu na kuubwaga katika mlango wan je kisha yeye akalitoa pikipiki lake na kuliegesha nje kabisa, akisubiri kuona kinachoendelea.
Akiwa nje ya nyumba yake, juu yapikipiki lake kubwa akasubiri kimya nje kabisa ya nyumba yake.
Dakika tano hazikupita, mwanga wa taa za gari ukaonekana ukijitokeza katika kona ya barabara na kuelekea mtaa huo ilipo nyumba ya Kamanda Amata. Ilikuwa Ford Ranger nyeusi, haikuwa na namba za usajili, ikasoge polepole na kuegeshwa karibu kabisa na lango la nyumba hiyo, watu watatu wakashuka, mmoaj kati yao alikuwa mwanamke, alionekana ndiye akiongoza wengine, aliwapanga, mmoja alimwamuru abaki langoni, yeye na mwingine aliyeonekana pande la jitu waliingia ndani.

§§§§§
Naima na lile jitu moja kwa moja waliingia getini na kutembea kwa mainyato huku silaha zikiwa mikononi mwao. Wakiwa wanajigawa kiufundi zaidi kuuelekea mlango, walishangazwa na ukimya uliotawala, lakini hawakujali. Lilikuwa ni lile pande la mtu lililotangulia kuuendea mlango, kabla halijafika likajikwaa kwenye kitu kama gogo.

“Aah!” likajivuta na kujibwaga mbele. Lilipogeuka nyuma likaona mwili wa binadamu, “Shiit! Amemuua,” akasema kwa sauti.

“Nani amemuua?” Naima akauliza, kisha akashusha silaha yake na kusogea pale ulipo ule mwili, akaugeuza, na kuchomoa kijikaratasi kilichopachikwa kinywani mwa marehemu.

…Naanza na wewe…

Naima akageuka huku na kule asione mtu, anaanza na mimi! Hata kama Naima alikuwa ni muuaji mzuri kitaaluma lakini alijikuta akishikwa na ubaridi wa ghafla. Wakaingia ndani wakatafuta huku na kule hawakuona mtu zaidi ya redio kubwa iliyokuwa ikipiga muziki laini wa ‘Killing me softly’ akasonya na kutoka nje. Wakabeba mwili wa mwenzao na kutoka nao. Wakaubwaga katika nyuma ya pikap yao na kufungia. Kisha nao wakaingia garini na kuondoka.

ITAENDELEA…
 
RIWAYA: KITISHO
MTUNZI: richard MWAMBE

Naima akageuka huku na kule asione mtu, anaanza na mimi! Hata kama Naima alikuwa ni muuaji mzuri kitaaluma lakini alijikuta akishikwa na ubaridi wa ghafla. Wakaingia ndani wakatafuta huku na kule hawakuona mtu zaidi ya redio kubwa iliyokuwa ikipiga muziki laini wa ‘Killing me softly’ akasonya na kutoka nje. Wakabeba mwili wa mwenzao na kutoka nao. Wakaubwaga katika nyuma ya pikap yao na kufungia. Kisha nao wakaingia garini na kuondoka.

SEHEMU YA 04

§§§§§§
Kamanda Amata akawasha pikipiki lake, bila kuwasha taa, akaingia barabarani na kuwafuata taratibu, wakaikamata barabara ya Kinondoni na kuvuka daraja la Salenda kisha wakaelekea mjini, moja kwa moja mpaka Mbowe Club, wakaegesha gari na kuteremka kisha wakapotelea ndani.
Kamanda Amata akaingia baada yao na kuhakikisha hawapotezi katika himaya ya macho yake, akaketi katika moja ya viti vya kaunta na kuagiza glass moja ya Whisky akachanganya na sprite baridi kisha akawa anakunywa taratibu.
Wale jamaa wakaketi mahala Fulani wakijadiliana jambo lakini wakionekana kuwa na wasiwasi, kila mara Naima alionekana kuisoma ile karatasi na kuiweka tena mfukoni. Mara lile jitu la miraba mine likanyanyuka na kutoka mahala pale likamwacha Naima na mwingine mmoja. Kamanda Amata alipogeuka hakuliona lile jitu limeingilia kona gani, akili yake ikazunguka mara mbili, akateremka katika kile kiti na kujichanganya katikati ya watu waliokuwa wakiburudika na uziki katika ukumbi huo. Dakika kadhaa baadae akaliona lile jitu pale kaunta likinga’aang’aa macho, likabeba vinywaji na kuelekea kule lilikokaa tangu mwanzo, yote hayo Kamanda Amata alikuwa akiyatazama kutoka katika kundi la watu wale. Alipoona kuwa hakuna aliye na yeye alirudi tena kaunta na kuagiza kinywaji, lakini hakuweza kukimaliza baada ya kumwona Naima akinyanyuka kitini na kuelekea nje, Kamanda Amata naye akatoka na kumfuatilia mwanadada huyo.
Naima alisimama kati ya magari na kuweka simu yake sikioni kisha akaendelea kuongea na aliyekuwa upande wa pili.
Naima akiwa anaendelea kuongea na simu alihisi ubaridi ukimgusa maeneo ya shingoni, akashtuka akataka kugeuka.

“Tulia!” sauti nzito ya Kamanda Amata ikapenya sikioni mwake. Naima akatulia kama alivyoamuriwa, “Nilikwambia nitaanza na wewe, na ndiyo sasa naanza,” akaongeza.

“Weweni nani?” Naima akauliza kwa sauti yake nyororo inayoweza kumnyong’onyesha mwanaume yeyote Yule rijali.

“Mimi ni Yule mnayenitafuta, Kamanda Amata, na nataka unambie watu wangu wako wapi?” Kamanda akaongeza swali kisha akatulia. Naima naye alitulia bila kujibu, akitafakari la kufanya. Baada ya sekunde kadhaa, uamuzi aliofuanya haukuwa mzuri hata kidogo. Aligeuka na pigo kali kwa Kamanda Amata, lakini Kamanda aliliepa kiufundi huku bastola yake ikimtoka mikononi. Naima aliruka sarakasi kwa minajiri ya kuiwahi le bastola lakini kabla hajafika alijikuta akipokea teka la nguvu mbavuni na kutupwa upande wa pili, akajiinua haraka na kusimama wima kumkabili Amata. Amata alijiweka sawa mwili wake na kumwendea kama mbogo, Naima alijiweka sawa na kuvamiana na Amata, kama Kamanda alifikiri mwanamke huyo anapigika kirahisi alikosea, mapigo matatu ya haraka yalimwingia Kamanda akajikuta anapoteza netweki, akajaribu kujitutumua lakini akajikuta amedhibitiwa ka mikono imara ya mwanamama huyo.

Naima alijirusha hewani kama jani la mkorosho na kuachia dabo kiki za maana zilizotua sawia kifuani mwake na kumpeleka chini.
Kisha Naima akatua chini kwa miguu miwilia akimtazama Kamanda Amata akigalagala chini.

“Ha ha ha ha niliambiwa kuwa Amata ni mwanamume wa chuma kaa mbali naye! Chuma kiko wapi hapa? Na sasa nakuua kwa mkono wangu kwani nimeahidiwa pesa nyingi sana kama roho yako nikiipeleka kwa bosi wangu,” Naima aliongea kwa kujiamini huku akiiweka sawa mikono yake tayari kumshushia pigo la mwisho kijana huyo. Alipomjia kumvamia alimshuhudia Kamanda Amata akijirusha kutoka chini kwa mtindo wa ajabu na guu lake la kulia likatua chini ya kidevu cha Naima, akanyanyuliwa na kubwagwa upande wa pili meno kadhaa yakimtoka.

“Mpo chini ya ulinzi!” sauti kali ikasikika upande mwingine. Kamanda alipotupa jicho akaona polisi eneo hilo, akaruka sarakasi na kutua upande wa pili wa gari, akajibana sehemu ambayo kutokana na nguo zake hakuweza kuonekana, akitazama linaloendelea.
Amata alishuhudia wale polisi wawili wakichezea kichapo cha maana kutoka kwa Naima, wakishindwa kujitetea hata kwa ngumi moja kwani kipigo kilikuwa cha sekunde kadhaa lakini kikali.
Huyu mwanamke ni balaa! Akajisemea, upo muda wake nitamtia mkononi tu, akajisemeana kusonya.

KEREGE – saa 8 usiku.

KIKAO cha dharula kiliitishwa ndani ya kasri la Pancho Panchilio, watu watatu walingia ndani ya jumba hilo kupitia milango tofauti kiasi kwamba hata walinzi tu hawakuweza kuwaona wageni hao. Walijikuta ndani wakiwa waneketi katika mtindo wa duara na Yule kinara wao akiwa mbele pa si na kuonekana. Wote waliketi kimya kabisa wakisubiri mkuu wao aongee.
Akajikohoza kidogo kutengeneza koo lake, kisha akafungua kikao hicho kisicho rasmi.

“Wajumbe mtashangaa nimewaita ghafla usiku huu, lakini lengo ni kuwapa taarifa ya kile kinachoendelea mpaka sasa,” Pancho alianza.

“Ndio tunakusikiliza,” mjumbe mmoja akaitikia.

“Vikundi vyetu vimefanya kazi kubwa sana na vimefanikiwa kuwakamata watu watatu, yaani namba moja, namba tatu na namba nne, na hali zao ni kifo muda wowote,” akaendelea.

“Ndiyo hata mimi nilikwishasema kuwa, hawa wakikamatwa ni kuwaua tu na maiti zao tunateketeza kwa moto ili kupoteza ushahidi,” Mjumbe mwingine akaongeza.

“Lakini sasa kuna kikwazo kimoja,” Pancho akatulia hapo.

“Kikwazo gani tena?” akauliza mjumbe.

“Namba moja wao ndiyo anyelete shida na kati ya watu wetu tuliowapa kazi kumbukeni ni vikosi vitatu mashuhuri, watu wane wameshapoteza maisha kwa mkono wake,” akawapa ujumbe uliowashtua kidogo.

“Unasema!” Mjumbe mmoja akaonekana kuanza kuchanganyikiwa.

“Habari ndiyo hiyo! Hivi sasa vijana wapo mtaani wanamsaka mshenzi huyo, mmoja kati ya hao tumemuua yupo katika machaka ya Gongo la Mboto ambako huko pia tumemkosakosa Amata ijapokuwa vijana wetu walilishambulia vikali gari lake lakini alitoweka.”

“Huyo siyo binadamu ni shetani, kwanza mi siku zote sijawahi kumwona japo nimefanya juu chini nimwone japo kwa sekunde moja, namsoma tu vitabuni,” mjumbe ambaye ni mzee kuliko wote aliongeza na wote wakacheka.

“Sasa tunafanyaje?”

“Vikosi vyetu vipo kazini, bado vinasakana na huyo Amata, hwa tulio nao nafikiri ni kuwamaliza kuwaweka hapa ni hatari kwani wakipata nguvu madhara yake ni makubwa,” Pancho akashusha pumzi, “Ila hapa kuna habari njema,” aliposema hayo wote wakakaa sawa.

“Tumeipata kompyuta mama, ile ambayo anatumia boss wao Yule bibi,” akawaambia.

“Eewaaaa hilo nalo neon asee!”

“Sasa ina neno fungushi ndiyo tatizo (password), maana humu ndimo kuna siri zote za hawa jamaa, nilikuwa nawasubiri kwa pamoja tuamue la kufanya,” akaeleza.

“Ni kutumia nguvu tu kupata hiyo password, wenyewe wanaijua, sasa wape kazi vijana watumie nguvu ili kupata hiyo password tujue kilichomo, hawawezi kutupanda kichwani,” Mjumbe mzee akatoa wazo.

§§§§§
Taarifa za kupatikana kwa mwili wa Scoba zilimfikia Kamanda Amata, nguvu zilimwishia kabisa hakuwa hata na la kufanya. Aliitazama saa yake mkononi ilikuwa saa nane na uchafu wake, muda unayoyoma, hakujali aliliwasha pikipiki lake na kuelekea hospitali ya jeshi Ukonga ambako aiambiwa mwili huo umehfadhiwa kwenye chumba maalum.
Hakuamini alipomkuta Scoba kalala kimya huku madaktari wakijaribu kupigania uhai wake wa mwisho. Kamanda Amata alisimama mlangoni na kisha akarudi nje, akajinaamia kwenye ukuta machozi yakimtoka.
Akachomoa mfukoni simu yake na kuiweka sikioni, akamsubiri mtu wa upande wa pili ajibu.

“Ndiyo konokono vipi?” sauti ile ikauliza.

“Konokono anahitaji miguu ya kutembea!” kamanda akaeleza kwa lugha waliyoelewa wenyewe.

“Mwambie aje kuchukua!” akajibiwa na simu ikakatika.
Kamanda Amata akapiga namba nyingine na kuisikiliza.

“Hello!” sauti ikaita.

“TSA namba moja anaongea!” akajibu lile itikio.

“Unasema nani a-a-naonge-a” kigugumizi kilimshika mtu wa upande wa pili.

“TSA namba moja ninaongea, Mkuu naomba tuonane ofisini kwako usiku huu, haraka sana,” Kamanda akatoa amri.

“Kuna nini Namba moja?” akauliza Mkuu wa Usalama wa Taifa Bwana Hosea.

“We naomba tuonane tutajua hapohapo kuna nini…”

“Ok! Copy and paste,” Hosea akajibu huku akikiacha kitanda na kumbusu mkewe Techla aliyekuwa kazama usingizini, kalala fofofo.

USALAMA WA TAIFA – saa 8:40 usiku.

MKUU wa kitengo cha Usalama wa Taifa, Bwana Hosea aliwasili katika jengo hilo na kupokelewa na walinzi, kila mmoja alishangaa kumwona mtu huyo usiku mnene kama huo, kuja kwake halikuwa tatizo, tatizo ni kuja ghafa na bila taarifa. Hakuongea na mtu, alipita moja kwamoja katia sebule kubwa ya kupokelea wageni.

“Mkuu mbona hivyo vipi?” Avanti alimtupia swali walipokutana koridoni.

“Salama tu, upo nani ofisini?” akamuuliza.

“Nipo na Muba,” akajibu.

“Ok, kuna lolote la ajabu mliloliona? Au taarifa mliyoipata?” akamwuliza.

“Ni ajlia iliyotokea Salenda, lakini tumeishaianyia kazi, na mauaji ya Mheshimiwa Mbunge wa Miroroso,” Avant akamweleza.

“Ok, nitawaona baadae kama nitawahitaji,” akamwambia huku akiiendea ofisi yake.
Dakika moja tu baada ya yeye kuingia katika jingo hilo, pikipiki kubwa la Kamanda Amata lilifika getini.

“Jitambulishe!” ilikuwa sauti ya mlinzi.
Kamanda Amata, akataja namba yake ya siri inayomtambulisha kikazi badala ya kitambulisho. Ukimya ukachukua nafasi kisha geti likafunguliwa naye akaingia. Akaegesha pikipiki lake na kuuendea mlango mkubwa, moja kwa moja ofisini kwa Hosea. Akamkuta Mkuu huyo akiwa ametulia kitini na bastola yake kaiweka uchi mezani.

“Karibu Namba moja!” akamkaribisha kwa hofu sana.

“Asante Mkuu! Samahani kwa kukusumbua maana imebidi umwache shemeji,” akamtania.

“Usijali, ndiyo kazi zetu hata yeye anajua, niambie Namba moja, vipi usiku huu, maana hujawahi fika ofini kwangu zaidi ya mwaka mmoja sasa,” akaanza kumhoji.

“Mkuu hali ni mbaya! Ni Kitisho!” kamanda akaanza namna hiyo.

“Unasema?” akauliza.

“Nasema idara ina hali mbaya!” akakazia.

“Kamanda Amata, TSA 1, nini tatizo?” Hosea akauliza.

“Mkuu, Madam S hajulikani alipo, Chiba, Dr. Jasmine wote hawajulikani walipo, Gina yuko mahututi kwa Dr. Khadrai, Scoba naye habari yoyote inaweza kutokea,” Kamanda akaeleza na kuangusha chozi.

“Kamanda Amata…!” Hosea akanyanyuka kitini na kuliendea dirisha kubwa la ofisi yake, alionekana wazi kuchanganyikiwa na taarifa hiyo, akajishika kiuno, akatikisa kichwa, akajipigapiga kichwani mara kadhaa kana kwamba analazimisha kukumbuka kitu, akasonya na kugeuka alipo Kamanda Amata.

“Eti unasemeje? Ina maana wametekwa au wameuawa?” akauliza tena kama hakusikia aliloambiwa.

“Siwezi kujua kama wametekwa au wameuawa! Ila wametoweka, na hapa unaponiona ninatafutwa kwa ubani na uvumba,” Kamanda akaeleza.
Mara hodi katika mlango wa ofisi hiyo ikabishwa.

“Ingia!” Hosea akaitikia, “Vipi, usiku huu sasa!”

“Samahani Mkuu, kuna taarifa hapa ambayo ungeikuta asubuhi lakini maadam upo ni muhimu kuiona tena haraka iwekanavyo,” Mubah akakabidhi karatasi ndogo kwa Hosea kisha yeye akaondoka. Hosea akaitazama kwa makini, akairudiarudia kuisoma kama haielewi.

“Japokuwa si kazi yako lakini tazama hii taarifa,” akampa Kamanda Amata, akaipokea na kuisoma, moyo ukamlipuka, akaanza kuhema kwa nguvu.

…Moja ya gari zenu imepata ajali leo wakato wa mvua kubwa katika daraja la Salenda, ndani ya gari hajapatikana majeruhi wala maiti, tunaomba ushirikiano wenu…

Ilikuwa ni sehemu ya taarifa hiyo, Kamanda Amata akashusha ile karatasi na kuiweka mezani.

“Naomba niwe na haraka!” akamwambia Hosea.

“Bila shaka kamanda!” akamjibu. Amata akachukua simu ya ofisini kwa Hosea na kuzungusha tarakimu kadhaa kisha akaweka sikioni.
Akaongea na mtu aliyemtaka kisha akaishusha simu na kuiweka mahala pake.

“Kamanda, njoo huku!” Hosea akamwambia kisha wakatoka na kuelekea chumba cha mawasiliano.
Wakaingia katika chumba kipana ambacho kilikuwa na kila aina ya mawasiliano ikiwe zile kamera za mabarabarani na sehemu nyeti Dar es salaam.

“Nyie, hii ajali imetokea saa ngapi?” Hosea akauliza.

“Saa moja kama na nusu hivi Mkuu!” Mubah akajibu.

“Sasa, saa moja mpaka sasa nane, na mnajua gari iliyopata ajali ni ya kwetu, eh! Mubah, Avant mlikuwa mnafanya nini humu ndani…?” Hosea aliongea kwa hasira, Mubah na Avant wakabaki kimya huku Mubah akimtazama Avant kwa chini.

“Hebu rudisha nyuma nione hiyo picha kwanza!” Kamanada akaomba. Avant akafanya hivyo na ile picha ikafika mahala pake, Kamanda Amata akashuhudia ile gari ikiacha njia na kupanda tuta la katikati kisha ikajipiga mwambani na kupinduka vibaya kabla ya kutumbukia kwenye mikoko chini ya daraja. Akairudiarudia kama mara tano hivi, kisha akamgeukia Hosea.

“Vipi?”

“Hii ni gari pekee ya Madam S japo siioni vizuri kutokana na mvua lakini bila shaka, tazama hapa, hapa, hii ni BMW umeona ee?” akamwonesha vizuri Hosea.

“Nyie vijana muwe makini nyie! Siku nyingine nitawafaya, sasa unajua kwa kuchelewa kupata hii taarifa meshaliweka pabaya Taifa na ninyi kazi yenu ni kuangalia usalama wa Taifa, nipigieni simu wakati wowote ule nitakuja kazini,” Hosea alilalama.

“Samahani boss, siku niliyopiga simu mkeo Techla alinitukana eti mi ni hawara wako,” Avant alilalamika.

“Avant haya ni mambo ya kazi achana na mke wangu! Sawa?” akafoka na kutoka ofisini. Wakasimama kwenye korido yeye na Kamanda Amata wakijadilia jambo.

“Sasa Mkuu, yaani hapa muda hautoshi, lazima kwanza niione hiyo gari kisha nijue la kufanya, na mimi nahusisha matukio haya na lile la mauaji ya Mbunge,” Kamanda akaeleza.

“Hapo umenichanganya kidogo!” Hosea akamwambia Kamanda.

“Nilikwenda kukagua maiti ya Mheshimiwa, mauaji yake yamefanana kabisa nay a wale waliouawa Uswizz, mlenga shabaha alifanya vile vile, kumbuka huyu Mbunge ni Yule mwenye kelele za kuibua mambo bungeni hasa sakata hili la kutorosha mapesa nje ya nchi,” kamanda akaeleza kwa undani mambo mbalimbai anayoyatilia mashaka.

Hosea, Mkuu wa idara ya Usalama wa Taifa wa nchi akabaki kinywa wazi, akajishika kidevuni hasijue la kufanya.

“Ok Kamanda, sasa ulikuwa unasemaje?” Hosea akarudisha mazungumzo nyuma.

“Mkuu kwanza nilikuwa nakupa hiyo taarifa na unajua taarifa zetu huwa ni salama kwa kuziongea ana kwa ana,” akamweleza.

ITAENDELEA
 
RIWAYA: KITISHO
MTUNZI: richard MWAMBE


“Nilikwenda kukagua maiti ya Mheshimiwa, mauaji yake yamefanana kabisa nay a wale waliouawa Uswizz, mlenga shabaha alifanya vile vile, kumbuka huyu Mbunge ni Yule mwenye kelele za kuibua mambo bungeni hasa sakata hili la kutorosha mapesa nje ya nchi,” kamanda akaeleza kwa undani mambo mbalimbai anayoyatilia mashaka.
Hosea, Mkuu wa idara ya Usalama wa Taifa wa nchi akabaki kinywa wazi, akajishika kidevuni hasijue la kufanya.

SEHEMU YA 5

“Ok Kamanda, sasa ulikuwa unasemaje?” Hosea akarudisha mazungumzo nyuma.

“Mkuu kwanza nilikuwa nakupa hiyo taarifa na unajua taarifa zetu huwa ni salama kwa kuziongea ana kwa ana,” akamweleza.

“Idara, imepata taarifa kama ulivyoileta, sasa wewe endelea na harakati zako, na mi hapa nawaita vijana wangu usiku huu, ili kuanza uchunguzi wa kina nitakutaarifu muda wowote nikipata lolote, nawe unitaarifu muda wowote ukipata lolote, kama kuna mahala utahitaji nguvu nafikiri una kibali cha kuomba jeshi la polisi muda wowote sivyo?” Hosea akunguruma.

“Ndivyo!” Kamanda akajibu.

“All the best!”

KITUO CHA POLISI SALENDA – saa 9:11 usiku

GARI ya Madam S haikutazamika mara mbili, kwa ujumla ukiitazama ni kama imegeuzwa nje ndani; ndani nje, vyoo vyote hakuna, injini iko nje na mengine mengi. Kamanda Amata akaitazama kwa kina, akaikagua hapa na pale kwa utaratibu maalum sio kama ule wa polisi wa haraka haraka, yeye aliangalia kimoja kwa kingine. Akakagua magurudumu na kisha akatulia kimya.
Akiwa katika kuangalia ndani ya gari hiyo ndipo alipoona kitu cha pekee kabisa, heleni, heleni ambayo yeye anaifahamu sana, akaiokota akaitia mfukoni mwake. Kisha akamgeukia polisi aliyekuwa naye mahala hapo.

“Twende eneo la tukio!” akamwamuru.
Yule WP aliyekuwa zamu akajiweka tayari kwa safari fupi ya usiku huo, wakapiga hatu mbili.kamanda akamsimamaisha.

“We WP! Tunakoenda huko unafikiri kupo salama? Hata kama hamruhusiwi kubeba silaha, mimi nakwambia kachukue silaha,” akamwambia kwa ukali.
Dakika mbili baadae Yule WP alikuwa na SMJ iliyoshiba vyema, wote wakakaa juu ya pikipiki kubwa aina ya BMW wakaelekea darajani.
Mikoko mingi ilikuwa imekatika huku na kule, kwa ujumla palisambaratika.

“Mlikuja wangapi?” Kamanda akamwuliza.

“Tulikuja watatu,” Yule WP akajibu.

“Hamkukuta mtu hapa, majeruhi wala maiti?” akauliza.

“Hatukukuta,” akajibu.

“Njoo hapa!” Kamanda akamwita, kisha akamwonesha alama za miburuzo.

“Unaona hii, huyu ni mtu kaburuzwa kutoka hapa ilipoangukia gari mpaka kule juu labda, na hizi ni alama za viatu vya huyo aliyemburuza,” akamweleza. “Tazama hiki kioo cha mbele, hii ni risasi, kioo cha ajali hakiwezi kupasuka namna hii, kwa hiyo ajalia hii kabla haijatokea dereva alipigwa risasi,” akaendelea kumjuza.
Baada ya kuridhika na hapo wakarudi kituoni.

“Wote mlilikuwepo ajalini?” akauliza tena.

“Hapana walikuwapo watatu tu,” akajibiwa.

“Naomba wote waliokuwepo wafike hapa haraka!” akaamuru. Sekunde tu. Askari watatu wakasimama mbele ya Kamanda Amata akiwemo Yule WP.

“Vueni viatu!” akawaamuru. Nao wakavua na kuviweka pembeni.
Akavichukua kimoja kimoja na kuvigeuza chini kuangali soli za viatu hivyo, akawarudishia. Kisha akawashukuru na kuondoka kituoni hapo, alipovuka tu daraja la Salenda, mbele ya ubalozi wa Ufaransa akasimamisha pikipiki lake, akaichukua ile heleni na kuipachua katikati kisha akaipachika sikioni kama earphone.
Kwanza akasikia miruzi mikali, kisha utulivu ukafuata na sauti ya Madam S ikasikika kwa mabli kidogo.

…Nataka wote tukutane ofisini, Shamba, Chiba na mimi tumepata ujumbe wa kitisho, hili sio la kupuuzia, (ukimya ukatawala) nimetoka nyumbani, naelekea shamba, ofisi za Ubalozi, Daraja la Salenda…

Kisha ikasikika sauti ya maumivu, na kelele ya kishindo kikubwa kilichojirudia mara kadhaa.

…Angalieni kwa chini, ndani ya gari, fanyeni haraka. Atakuwa amekufa huyu! Sawa tu, mchukueni hivyo hivyo…
Akasikia sauti ya kitu kama kijiwe kikianguka kisha ukimya ukatawala. Kamanda Amata akashusha pumzi ndefu, akaitoa ile earphone na kuiweka tena kama heleni kisha akaiweka mfukoni, pepo wa hasira akampanda, akapiga kiki moja na pikipiki lile likakubali sheria, akaingiza barabarani na kuchukua barabara ya Kinodoni, kisha akakunja ile ya Kawawa akaambaa nayo mpaka Kigogo akatobolea Tabata akasonga mbele.

GEREZA LA UKONGA- saa 10:01 alfajiri.

MBELE ya Kamanda Amata kulikuwa askari Magereza mmoja aliyekuwa zamu usiku huo, baada ya kuwasiliana na Mkuu wa gereza na kuwasili pale, wote kwa pamoja wakakaa ndani ya chumba kidogo kwa mazungumzo ya kikazi.

“Ndio bwana!” Yule Mkuu wa gereza akaanzisha mazungumzo.

“Asee Mkuu, nahitaji kuona rekodi ya wageni wanaomtembelea Kanayo O. Kanayo na Mahmoud Zebaki, hilo tu!” Kamanda akatoa ombi lake.
Punde si punde ikaletwa rekodi karibu ya mwezi mzima, kila mtu alitembelewa mara nyingi na mkewe isipokuwa tu kwa Mahmoud Zebaki, huyu zaidi ya mkewe alikuwa akitembelewa na mtu mwingine aliyejiandikisha kwa jina la Ravi Kumar, Amata akatikisa kichwa. Akatazama juu huku na kule.

“Mna kamera za usalama hapa gerezani?” akauliza.

“Ndiyo zipo,” Mkuu wa gereza akajibu.

“Naomba nione rekodi yake ya tarehe 21 May mwaka huu,” wakanyanyuka wote na kupita kwenye ujia mrefu mpaka ofisi nyingine ndogo ambako walimkuta kijana mmoja mwenye cheo cha koplo, akafanya hivyo walivyoomba.
Tarehe ile mwezi ule saa ile, akaonekana mtu mwenye asili ya Kihindi akiingia katika chumba cha kuongelea, kisha Mahmoud Zebaki akaja pale wakafanya mazungumzo mafupi kama dakika tano tu. Kamanda Amata alikuwa akiangalia midomo yao na matendo yao, walipokuwa wakiagana. Mahmoud aliiweka mikono yake juu ya mbao iliyokaa kama meza katikati yao ijapokuwa walitenganisha na nondo, na Yule Mhindi akaweka juu yake na kuiondoa. Kamanda Amata akatazama sana kitu hicho na kukirudisha nyuma mara kadhaa akagundua kuwa kabla ya Ravi kuweka mikono juu ya mikono ya Mahmoud kuna kitu alikuwa akikisoma au kukiangalia kwa makini. Kisha akaondoka na kumwacha Mahmoud akiwa na tabasamu pana.
Walipoangalia tukio la siku nyingine walimuona Ravi akifuatana na mke wa Mahmoud na mazungumzo yao yalikuwa yalionekana wazi hayakuwa ya Kiswahili bali lugha Fulani kama si Kihindi basi ni Kibangla.

“Asante Mkuu!” Kamanda akashukuru.

“Umeridhika? Ni wajibu wetu kulinda Taifa, mimi na wewe,” Yule Mkuu wa gereza akamweleza Kamanda Amata.

“Ni kweli, nikiwa na shida yoyote juu ya haya nitakutaarifu,” akamjibu.

“Bila shaka, muda wowote karibu sana,” wakaagana na Kamanda Amata akaondoka. Kamanda Amata akashika njia na pikipiki lake kuelekea mitaa ya Msasani ambako nyumba ya Mahmoud Zebaki ndiko iliko na familia yake yote iko huko, akiwa njiani akapiga simu kwa kutumia simu ileile ya Gina kwa Inspekta Simbeye, akaomba askari watatu wenye kibali cha upekuzi na gari haraka sana, akapatiwa.
Saa kumi na moja alfajiri alikuwa tayari amewasili Msasani Peninsula na ile gari ilikuwa tayari iko pale.

“Mko kamili?” akawauliza.

“Ndio afande!” wakajibu.

Wakagonga na kuingia ndani ya jumba hilo, walinzi hawakuwa na tatizo baada ya kuona serikali imefika hapo. Wakagonga mlango mkubwa na mfanyakazi wa ndani akatoka.
Walipouliza kuhusu mama mwenye nyumba wakajibiwa hayupo lakini kwa kuwa walikuwa na kibali cha upekuzi na walipita kwa Mjumbe wa shina ambaye alifuatana nao upekuzi ukaanza, nusu saa iliwachukua polisi wale kupekuwa nyumba huku wote waliobaki wakiwa wameanyang’anywa simu zao za mikononi, hakuna kibaya walichokipata isipokuwa kitabu cha kumbukumbu kilichoonesha kuwa Yule mama amekwenda Zanzibar likizo yeye na watoto wake. Ndani ya kijitabu hicho pia baada ya kupekuwa sana wakakuta namba za simu za watu mbalimbali ikiwemo Ravi Kumar, na namba hiyo iliandikwa tarehe 21 May. Kamanda Amata aaliendea likitabu likubwa la TTCL linaloitwa Yellow Page na kutafuta jina hilo mpaka akalipata, na kugundua mtu huyo anakoishi, Mtaa wa India kitalu namba 453RF, wakaagana na Mjumbe wa shina na kuondoka zao mpaka mtaa huo, haikuwa tabu kufika ghorofa ya tatu na kumkuta bwana huyo akiwa hoi kwa usingizi.

“Nyie taka nni kwagu, usiku hii bana!” Ravi alalamika. Kamanda Amata hakuwa na shaka naye kwani picha aliyoiona ni ilele iliyosimama mbele yake.

“Mchukueni huyo, tuondoke naye,” Kamanda akaamuru.

“Jamani mmi nafanya nini nyinyi? Manonea sana raia nyie bana, acheni mimi tawapa pesa jingi sana mfungue maduka!” akalalama.

“Kelele!” Kamanda akamkoromea kisha wakampakia kwenye gari ya polisi mpaka kituo cha kati. Wakamwifadhi chumba maalum.

§§§§§

KEREGE

“SASA mtataja password au hamtaji? Tunajua kama ninyi mnaijua ofisi nzima na sisi tunataka kuwasha hii kompyuta,” John the Killer ‘JoKi’ akiwa na mjeledi mkononi mwake alikuwa akimuhoji Chiba aliyekuwa hoi kwa kipigo huku mikono na miguu yake ikiwa imefungwa kwa minyororo imara. Kila alipoiangalia ile kompyuta Chiba alshikwa na woga wa kutaja password, kwa maana alijua wazi kuwa akitaja tu basi siri za za idara zimemwagika.
Upande wa pili Madam S alikuwa amerudiwa na fahamu lakini bado akajifanya amepoteza fahamu akiskiliza kila kinachoendelea, damu iliyoganda usoni kwa majeraha ya vioo, maumivu makali ya mkono na mguu yalimfanya ajikute anashindwa kustahimili hali ile, aliwaza sana alipogundua kuwa wale jamaa wameikamata ile kompyuta na vijana wake wote alishawaambia ni heri kufa kuliko kutaja hiyo password.

“Anhaaa! Bibi ameamka, verygood!” JoKi akavuta hatua mpaka kwa Madam S, akatikisa kichwa chake, kisha akamkanyaga kwa nguvu kwenye mguu wake ulioonesha kila dalili ya kuwa umevunjika kwa jinsi ulivyovimba.

“Aaaaaiiiiggghhhh! Ms**ge wewe!” Madam akapiga yowe la uchungu na kutoa tusi, JoKi akamtandika teke la usoni, Madam S akajigonga ukutani kwa kisogo na kutulia bado kwenye ile minyororo, kwa kuwa alikuwa hajafungwa miguu yake na alijiinua kwa kutumia nguvu ya mikono kwa kujiegemeza na ile minyororo, alijisungusha hewani na kumtandika teke JoKi, lililomsukuma na ye akajibamiza ukutani na kupasuka kwenye paji la uso.
Mtesi mwingine akampiga na shoti ya umeme Madam S akapiga kelele na kutulia.
JoKi akajipapasa usoni na kukuta damu zikimwagika, akamtazama Madam S kwa hasira sana, “Umefanya jambo baya sana mwanamke! Utajuta leo nakwambia!” JoKi akauzungusha mjeledi wake na kumcharaza vibaya Madam. Chiba alishindwa la kufanya.

“Mwachee!” akapiga kelele kutoka pale chini. Wale jamaa wakaanza kucheka kwa kejeli, “Ipo saa yenu, na haiku mbali, mtajuta kuiona siku ya leo,” akaongea huku akiuma meno.

“Tutajuta saa ngapi ilhali alfajiri hii nyote mnauawa?” mmoja wao akasema.

“Hata kama mkituua, nawaapia mtajuta kuiona siku ya leo!” Chiba aliendelea kusisitiza.

“Kelele wewe, nguruwe jike we!” JoKi akafoka. Na wakati huo huo watu wane wakaingia ndani ya chumba kile wote wakiwa wamevaa maguo meusi na soksi usoni; ni macho tu yaliyokuwa yakionekana.

“Karibuni wazee!” JoKi akakaribisha.

“Madam S, na kikosi chako, serikali ilkutuma kufuatilia nyendo za watu au kulinda usalama wa Taifa dhidi ya hila za Mabeberu?” mmoja wao akauliza.

“Beberu lenyewe ndio wewe!” Madam S akajibu kwa taabu kidogo lakini waliayaelewa maneno yake.

“Unajibu utumbo! Madam ! unakitaka kifo kabla ya wakati wake sio, subiri subiri bado nusu saa ya kukuua kwanza utimize haja yetu moja tu kisha tunakuua ili upumzike na mateso haya,” mwingine akadakia.

“Inaonekana mnanifahamu vema sio? Mimi siogopi kifo, nishakutana na kifo zaidi ya mara mia tano sasa hicho unachosema wewe wala sikiogopi, lakini naomba mniue kabla sijawaua ninyi,” akaongea kijeuri.
Kosi kali likatua shavuni, la pili, la tatu, la nne, kisha sonyo kali likafuata, “Acha ujeuri, usibishane na Mkuu!” Yule mtu wa pili akamaliza alilolifanya.

“Yote yatarudi kama usiponiua sasa!” madam akamwambia Yule bwana.
Jasmine akaletwa ndani akiwa na kamba mikononi na tambala chafu lililoshindiliwa kinywani, akasukumiziwa mle chumbani.

“Wawili wameshakufa,” Yule bwana aliyezungumza mwanzo akamwonesha picha ya mwili wa Scoba. Madam S akaangusha chozi, “Hakika mtalipa roho ya huyo mtu kwa gharama kubwa!” akalalama.

“Never!” Yule bwana akajibu.
Madam S akamtemea mate usoni, “Never say never again!”.

“Huyu mwanamke jeuri mpeni disprini kwanza!” amri ikatolewa, umeme ukawashwa na shoti zikamchapa Madam S takriban sekunde thelethini.

“Stop!” ikatolewa amri ya pili, umeme ukazimwa,

“Nilishawaambia, ukifuata nyayo zap aka utapotea, sasa ninyi ni manunda na sasa mtapotea hakika,” sauti yenye lafudhi ya kihindi kwa mbali ikasikika kutoka kwenye soksi jeusi lililomfunika mtu huyo.

“Haya nataka password ya hii kompyuta!” ile sauti ya kihindi ikaendelea. Alipoichukua ile kompyuta kutoka kwa kijana mmoja ndipo Chiba alipoiona kwa uvunguni na kugundua kuwa kompyuta ile si yenyewe, akamtazama Madam S, akajikohoza mara tatu kwa mtindo wa pekee, Madam akaelewa kuwa ule ni wito akamtazama Chiba, Chiba akayazungusha macho yake kwa namna ya ajabu huku akibana na kuachia kope zake, Madam S akaelewa anachoambiwa kuwa kompyuta ile ni feki.
Akawatajia password ya hiyo kompyuta, wale jamaa wakaanza kuifungua, ilipoanza kufunguka wakafurahi sana na kuondoka zao.

“Tunarudi muda si mrefu kuwaua!” mmoja wao akasema.
Wakaondoka zao.

ITAENDELEA....
 
Riwaya nyingine no hizi hapa
 
 
 
 
 
Kitabu kimya Cha HARUFU YA KIFO kutoka kwa Richard Mwambe bado kipo madukani usikose burudani hiyo, ni moja Kati ya riwaya kali sana za kijasusi.
 
RIWAYA: KITISHO
MTUNZI: richard MWAMBE


“Nilikwenda kukagua maiti ya Mheshimiwa, mauaji yake yamefanana kabisa nay a wale waliouawa Uswizz, mlenga shabaha alifanya vile vile, kumbuka huyu Mbunge ni Yule mwenye kelele za kuibua mambo bungeni hasa sakata hili la kutorosha mapesa nje ya nchi,” kamanda akaeleza kwa undani mambo mbalimbai anayoyatilia mashaka.
Hosea, Mkuu wa idara ya Usalama wa Taifa wa nchi akabaki kinywa wazi, akajishika kidevuni hasijue la kufanya.

SEHEMU YA 5

“Ok Kamanda, sasa ulikuwa unasemaje?” Hosea akarudisha mazungumzo nyuma.

“Mkuu kwanza nilikuwa nakupa hiyo taarifa na unajua taarifa zetu huwa ni salama kwa kuziongea ana kwa ana,” akamweleza.

“Idara, imepata taarifa kama ulivyoileta, sasa wewe endelea na harakati zako, na mi hapa nawaita vijana wangu usiku huu, ili kuanza uchunguzi wa kina nitakutaarifu muda wowote nikipata lolote, nawe unitaarifu muda wowote ukipata lolote, kama kuna mahala utahitaji nguvu nafikiri una kibali cha kuomba jeshi la polisi muda wowote sivyo?” Hosea akunguruma.

“Ndivyo!” Kamanda akajibu.

“All the best!”

KITUO CHA POLISI SALENDA – saa 9:11 usiku

GARI ya Madam S haikutazamika mara mbili, kwa ujumla ukiitazama ni kama imegeuzwa nje ndani; ndani nje, vyoo vyote hakuna, injini iko nje na mengine mengi. Kamanda Amata akaitazama kwa kina, akaikagua hapa na pale kwa utaratibu maalum sio kama ule wa polisi wa haraka haraka, yeye aliangalia kimoja kwa kingine. Akakagua magurudumu na kisha akatulia kimya.
Akiwa katika kuangalia ndani ya gari hiyo ndipo alipoona kitu cha pekee kabisa, heleni, heleni ambayo yeye anaifahamu sana, akaiokota akaitia mfukoni mwake. Kisha akamgeukia polisi aliyekuwa naye mahala hapo.

“Twende eneo la tukio!” akamwamuru.
Yule WP aliyekuwa zamu akajiweka tayari kwa safari fupi ya usiku huo, wakapiga hatu mbili.kamanda akamsimamaisha.

“We WP! Tunakoenda huko unafikiri kupo salama? Hata kama hamruhusiwi kubeba silaha, mimi nakwambia kachukue silaha,” akamwambia kwa ukali.
Dakika mbili baadae Yule WP alikuwa na SMJ iliyoshiba vyema, wote wakakaa juu ya pikipiki kubwa aina ya BMW wakaelekea darajani.
Mikoko mingi ilikuwa imekatika huku na kule, kwa ujumla palisambaratika.

“Mlikuja wangapi?” Kamanda akamwuliza.

“Tulikuja watatu,” Yule WP akajibu.

“Hamkukuta mtu hapa, majeruhi wala maiti?” akauliza.

“Hatukukuta,” akajibu.

“Njoo hapa!” Kamanda akamwita, kisha akamwonesha alama za miburuzo.

“Unaona hii, huyu ni mtu kaburuzwa kutoka hapa ilipoangukia gari mpaka kule juu labda, na hizi ni alama za viatu vya huyo aliyemburuza,” akamweleza. “Tazama hiki kioo cha mbele, hii ni risasi, kioo cha ajali hakiwezi kupasuka namna hii, kwa hiyo ajalia hii kabla haijatokea dereva alipigwa risasi,” akaendelea kumjuza.
Baada ya kuridhika na hapo wakarudi kituoni.

“Wote mlilikuwepo ajalini?” akauliza tena.

“Hapana walikuwapo watatu tu,” akajibiwa.

“Naomba wote waliokuwepo wafike hapa haraka!” akaamuru. Sekunde tu. Askari watatu wakasimama mbele ya Kamanda Amata akiwemo Yule WP.

“Vueni viatu!” akawaamuru. Nao wakavua na kuviweka pembeni.
Akavichukua kimoja kimoja na kuvigeuza chini kuangali soli za viatu hivyo, akawarudishia. Kisha akawashukuru na kuondoka kituoni hapo, alipovuka tu daraja la Salenda, mbele ya ubalozi wa Ufaransa akasimamisha pikipiki lake, akaichukua ile heleni na kuipachua katikati kisha akaipachika sikioni kama earphone.
Kwanza akasikia miruzi mikali, kisha utulivu ukafuata na sauti ya Madam S ikasikika kwa mabli kidogo.

…Nataka wote tukutane ofisini, Shamba, Chiba na mimi tumepata ujumbe wa kitisho, hili sio la kupuuzia, (ukimya ukatawala) nimetoka nyumbani, naelekea shamba, ofisi za Ubalozi, Daraja la Salenda…

Kisha ikasikika sauti ya maumivu, na kelele ya kishindo kikubwa kilichojirudia mara kadhaa.

…Angalieni kwa chini, ndani ya gari, fanyeni haraka. Atakuwa amekufa huyu! Sawa tu, mchukueni hivyo hivyo…
Akasikia sauti ya kitu kama kijiwe kikianguka kisha ukimya ukatawala. Kamanda Amata akashusha pumzi ndefu, akaitoa ile earphone na kuiweka tena kama heleni kisha akaiweka mfukoni, pepo wa hasira akampanda, akapiga kiki moja na pikipiki lile likakubali sheria, akaingiza barabarani na kuchukua barabara ya Kinodoni, kisha akakunja ile ya Kawawa akaambaa nayo mpaka Kigogo akatobolea Tabata akasonga mbele.

GEREZA LA UKONGA- saa 10:01 alfajiri.

MBELE ya Kamanda Amata kulikuwa askari Magereza mmoja aliyekuwa zamu usiku huo, baada ya kuwasiliana na Mkuu wa gereza na kuwasili pale, wote kwa pamoja wakakaa ndani ya chumba kidogo kwa mazungumzo ya kikazi.

“Ndio bwana!” Yule Mkuu wa gereza akaanzisha mazungumzo.

“Asee Mkuu, nahitaji kuona rekodi ya wageni wanaomtembelea Kanayo O. Kanayo na Mahmoud Zebaki, hilo tu!” Kamanda akatoa ombi lake.
Punde si punde ikaletwa rekodi karibu ya mwezi mzima, kila mtu alitembelewa mara nyingi na mkewe isipokuwa tu kwa Mahmoud Zebaki, huyu zaidi ya mkewe alikuwa akitembelewa na mtu mwingine aliyejiandikisha kwa jina la Ravi Kumar, Amata akatikisa kichwa. Akatazama juu huku na kule.

“Mna kamera za usalama hapa gerezani?” akauliza.

“Ndiyo zipo,” Mkuu wa gereza akajibu.

“Naomba nione rekodi yake ya tarehe 21 May mwaka huu,” wakanyanyuka wote na kupita kwenye ujia mrefu mpaka ofisi nyingine ndogo ambako walimkuta kijana mmoja mwenye cheo cha koplo, akafanya hivyo walivyoomba.
Tarehe ile mwezi ule saa ile, akaonekana mtu mwenye asili ya Kihindi akiingia katika chumba cha kuongelea, kisha Mahmoud Zebaki akaja pale wakafanya mazungumzo mafupi kama dakika tano tu. Kamanda Amata alikuwa akiangalia midomo yao na matendo yao, walipokuwa wakiagana. Mahmoud aliiweka mikono yake juu ya mbao iliyokaa kama meza katikati yao ijapokuwa walitenganisha na nondo, na Yule Mhindi akaweka juu yake na kuiondoa. Kamanda Amata akatazama sana kitu hicho na kukirudisha nyuma mara kadhaa akagundua kuwa kabla ya Ravi kuweka mikono juu ya mikono ya Mahmoud kuna kitu alikuwa akikisoma au kukiangalia kwa makini. Kisha akaondoka na kumwacha Mahmoud akiwa na tabasamu pana.
Walipoangalia tukio la siku nyingine walimuona Ravi akifuatana na mke wa Mahmoud na mazungumzo yao yalikuwa yalionekana wazi hayakuwa ya Kiswahili bali lugha Fulani kama si Kihindi basi ni Kibangla.

“Asante Mkuu!” Kamanda akashukuru.

“Umeridhika? Ni wajibu wetu kulinda Taifa, mimi na wewe,” Yule Mkuu wa gereza akamweleza Kamanda Amata.

“Ni kweli, nikiwa na shida yoyote juu ya haya nitakutaarifu,” akamjibu.

“Bila shaka, muda wowote karibu sana,” wakaagana na Kamanda Amata akaondoka. Kamanda Amata akashika njia na pikipiki lake kuelekea mitaa ya Msasani ambako nyumba ya Mahmoud Zebaki ndiko iliko na familia yake yote iko huko, akiwa njiani akapiga simu kwa kutumia simu ileile ya Gina kwa Inspekta Simbeye, akaomba askari watatu wenye kibali cha upekuzi na gari haraka sana, akapatiwa.
Saa kumi na moja alfajiri alikuwa tayari amewasili Msasani Peninsula na ile gari ilikuwa tayari iko pale.

“Mko kamili?” akawauliza.

“Ndio afande!” wakajibu.

Wakagonga na kuingia ndani ya jumba hilo, walinzi hawakuwa na tatizo baada ya kuona serikali imefika hapo. Wakagonga mlango mkubwa na mfanyakazi wa ndani akatoka.
Walipouliza kuhusu mama mwenye nyumba wakajibiwa hayupo lakini kwa kuwa walikuwa na kibali cha upekuzi na walipita kwa Mjumbe wa shina ambaye alifuatana nao upekuzi ukaanza, nusu saa iliwachukua polisi wale kupekuwa nyumba huku wote waliobaki wakiwa wameanyang’anywa simu zao za mikononi, hakuna kibaya walichokipata isipokuwa kitabu cha kumbukumbu kilichoonesha kuwa Yule mama amekwenda Zanzibar likizo yeye na watoto wake. Ndani ya kijitabu hicho pia baada ya kupekuwa sana wakakuta namba za simu za watu mbalimbali ikiwemo Ravi Kumar, na namba hiyo iliandikwa tarehe 21 May. Kamanda Amata aaliendea likitabu likubwa la TTCL linaloitwa Yellow Page na kutafuta jina hilo mpaka akalipata, na kugundua mtu huyo anakoishi, Mtaa wa India kitalu namba 453RF, wakaagana na Mjumbe wa shina na kuondoka zao mpaka mtaa huo, haikuwa tabu kufika ghorofa ya tatu na kumkuta bwana huyo akiwa hoi kwa usingizi.

“Nyie taka nni kwagu, usiku hii bana!” Ravi alalamika. Kamanda Amata hakuwa na shaka naye kwani picha aliyoiona ni ilele iliyosimama mbele yake.

“Mchukueni huyo, tuondoke naye,” Kamanda akaamuru.

“Jamani mmi nafanya nini nyinyi? Manonea sana raia nyie bana, acheni mimi tawapa pesa jingi sana mfungue maduka!” akalalama.

“Kelele!” Kamanda akamkoromea kisha wakampakia kwenye gari ya polisi mpaka kituo cha kati. Wakamwifadhi chumba maalum.

§§§§§

KEREGE

“SASA mtataja password au hamtaji? Tunajua kama ninyi mnaijua ofisi nzima na sisi tunataka kuwasha hii kompyuta,” John the Killer ‘JoKi’ akiwa na mjeledi mkononi mwake alikuwa akimuhoji Chiba aliyekuwa hoi kwa kipigo huku mikono na miguu yake ikiwa imefungwa kwa minyororo imara. Kila alipoiangalia ile kompyuta Chiba alshikwa na woga wa kutaja password, kwa maana alijua wazi kuwa akitaja tu basi siri za za idara zimemwagika.
Upande wa pili Madam S alikuwa amerudiwa na fahamu lakini bado akajifanya amepoteza fahamu akiskiliza kila kinachoendelea, damu iliyoganda usoni kwa majeraha ya vioo, maumivu makali ya mkono na mguu yalimfanya ajikute anashindwa kustahimili hali ile, aliwaza sana alipogundua kuwa wale jamaa wameikamata ile kompyuta na vijana wake wote alishawaambia ni heri kufa kuliko kutaja hiyo password.

“Anhaaa! Bibi ameamka, verygood!” JoKi akavuta hatua mpaka kwa Madam S, akatikisa kichwa chake, kisha akamkanyaga kwa nguvu kwenye mguu wake ulioonesha kila dalili ya kuwa umevunjika kwa jinsi ulivyovimba.

“Aaaaaiiiiggghhhh! Ms**ge wewe!” Madam akapiga yowe la uchungu na kutoa tusi, JoKi akamtandika teke la usoni, Madam S akajigonga ukutani kwa kisogo na kutulia bado kwenye ile minyororo, kwa kuwa alikuwa hajafungwa miguu yake na alijiinua kwa kutumia nguvu ya mikono kwa kujiegemeza na ile minyororo, alijisungusha hewani na kumtandika teke JoKi, lililomsukuma na ye akajibamiza ukutani na kupasuka kwenye paji la uso.
Mtesi mwingine akampiga na shoti ya umeme Madam S akapiga kelele na kutulia.
JoKi akajipapasa usoni na kukuta damu zikimwagika, akamtazama Madam S kwa hasira sana, “Umefanya jambo baya sana mwanamke! Utajuta leo nakwambia!” JoKi akauzungusha mjeledi wake na kumcharaza vibaya Madam. Chiba alishindwa la kufanya.

“Mwachee!” akapiga kelele kutoka pale chini. Wale jamaa wakaanza kucheka kwa kejeli, “Ipo saa yenu, na haiku mbali, mtajuta kuiona siku ya leo,” akaongea huku akiuma meno.

“Tutajuta saa ngapi ilhali alfajiri hii nyote mnauawa?” mmoja wao akasema.

“Hata kama mkituua, nawaapia mtajuta kuiona siku ya leo!” Chiba aliendelea kusisitiza.

“Kelele wewe, nguruwe jike we!” JoKi akafoka. Na wakati huo huo watu wane wakaingia ndani ya chumba kile wote wakiwa wamevaa maguo meusi na soksi usoni; ni macho tu yaliyokuwa yakionekana.

“Karibuni wazee!” JoKi akakaribisha.

“Madam S, na kikosi chako, serikali ilkutuma kufuatilia nyendo za watu au kulinda usalama wa Taifa dhidi ya hila za Mabeberu?” mmoja wao akauliza.

“Beberu lenyewe ndio wewe!” Madam S akajibu kwa taabu kidogo lakini waliayaelewa maneno yake.

“Unajibu utumbo! Madam ! unakitaka kifo kabla ya wakati wake sio, subiri subiri bado nusu saa ya kukuua kwanza utimize haja yetu moja tu kisha tunakuua ili upumzike na mateso haya,” mwingine akadakia.

“Inaonekana mnanifahamu vema sio? Mimi siogopi kifo, nishakutana na kifo zaidi ya mara mia tano sasa hicho unachosema wewe wala sikiogopi, lakini naomba mniue kabla sijawaua ninyi,” akaongea kijeuri.
Kosi kali likatua shavuni, la pili, la tatu, la nne, kisha sonyo kali likafuata, “Acha ujeuri, usibishane na Mkuu!” Yule mtu wa pili akamaliza alilolifanya.

“Yote yatarudi kama usiponiua sasa!” madam akamwambia Yule bwana.
Jasmine akaletwa ndani akiwa na kamba mikononi na tambala chafu lililoshindiliwa kinywani, akasukumiziwa mle chumbani.

“Wawili wameshakufa,” Yule bwana aliyezungumza mwanzo akamwonesha picha ya mwili wa Scoba. Madam S akaangusha chozi, “Hakika mtalipa roho ya huyo mtu kwa gharama kubwa!” akalalama.

“Never!” Yule bwana akajibu.
Madam S akamtemea mate usoni, “Never say never again!”.

“Huyu mwanamke jeuri mpeni disprini kwanza!” amri ikatolewa, umeme ukawashwa na shoti zikamchapa Madam S takriban sekunde thelethini.

“Stop!” ikatolewa amri ya pili, umeme ukazimwa,

“Nilishawaambia, ukifuata nyayo zap aka utapotea, sasa ninyi ni manunda na sasa mtapotea hakika,” sauti yenye lafudhi ya kihindi kwa mbali ikasikika kutoka kwenye soksi jeusi lililomfunika mtu huyo.

“Haya nataka password ya hii kompyuta!” ile sauti ya kihindi ikaendelea. Alipoichukua ile kompyuta kutoka kwa kijana mmoja ndipo Chiba alipoiona kwa uvunguni na kugundua kuwa kompyuta ile si yenyewe, akamtazama Madam S, akajikohoza mara tatu kwa mtindo wa pekee, Madam akaelewa kuwa ule ni wito akamtazama Chiba, Chiba akayazungusha macho yake kwa namna ya ajabu huku akibana na kuachia kope zake, Madam S akaelewa anachoambiwa kuwa kompyuta ile ni feki.
Akawatajia password ya hiyo kompyuta, wale jamaa wakaanza kuifungua, ilipoanza kufunguka wakafurahi sana na kuondoka zao.

“Tunarudi muda si mrefu kuwaua!” mmoja wao akasema.
Wakaondoka zao.

ITAENDELEA....

Kali sana.. Sijapita muda huku maana Hadithi zinaanzaga tu. Shukrani.
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom