Penzi la wizi katika tamthilia ya Wabrazili na mauaji ya kutisha…!

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,398

daniela.jpg
Hayati Daniella Perez
Daniella Perez 2.jpg
dperez3.jpg
093401.jpg

f42b1798ec20100409011630.jpg
Muuwaji Guilherme de Padua
02-dani-reportegens-para-recordar-novelas-e-famosos-54.jpg
nnnnnnnnnnnn.jpg
Mtuhumiwa kizimbani

Mapenzi, haiba, uzinzi, kutoka nje ya ndoa na mauaji vyote hivyo ni chachu ya tamthiliya za Wabrazili ambazo zimeteka hisia za watu wengi, na si kwa Brazil tu bali pia Duniani kwa ujumla. Kwa nchi kama Brazili ambayo ina idadi ya kutosha ya watu wasiojua kusoma na kuandika….. Lakini karibu kila nyumba ya mwananchi wa nchi hiyo ikiwa na TV, tamthiliya kama Next Victim na Exploding Hearts zilikuwa ndio zinazoongoza kwa kutazamwa na watu wengi nchini humo.

Lakini tangu mwaka 1992 yalipotokea mauaji ya mwigizaji maarufu wa tamthiliya nchini humo Daniella Perez, tasnia hiyo imekumbwa na kizungumkuti kilichosababisha tasnia hiyo kuonekana kioja. Mcheza Ballerina wa zamani binti aliyekuwa na miaka 22 wakati huo Daniella Perez alikuwa ndio yuko kwenye kilele cha umaarufu wakati huo akiigiza tamthiliya maarufu ya Corp e Alma (Body and Soul), tamthiliya ambayo ilitungwa na mama yake aitwae Gloria Perez ambaye ni mtunzi maarufu wa tamthiliya nchini humo. Kwa wale wasiojua, Ballerina ni mchezo wa dansi usiohusisha maneno wala mziki.

Katika tamthiliya hiyo ya Body and Soul Daniella alicheza kama Yasmin, binti mwenye hisia kali za mapenzi yasiyotabirika. Ilikuwa ndio tamthiliya yake ya kwanza kucheza na ilimsababishia kuwa maarufu nchini humo. Alikuwa ni binti mbichi, tajiri na aliyekuwa na ndoa imara na iliyokuwa na amani. Alifunga ndoa na mwigizaji mwenzie aliyejulikana kwa jina la Raul Gonzala.

Ilikuwa ni usiku wa Desemba 28, 1992, muda mfupi baada ya kurekodi tamthiliya hiyo ya Body and Soul ambapo kijana aliyeigiza naye kama mpenzi wake ndio alikuwa amevunja uhusiano naye kama sehemu ya mwendelezo wa tamthiliya hiyo. Mara baada ya kumaliza kurekodi sehemu hiyo ya tamthiliya, Daniella alikutwa ametupwa kwenye eneo la kutupa taka akiwa amekufa jirani kabisa na studio za Globo TV katka jiji hilo la Rio De Janeiro. Alikuwa ameuwawa kwa kuchomwa na mkasi sehemu mbalimbali mwilini mwake.

Siku iliyofuata Polisi wa jiji hilo la Rio De Janeiro walimkamata mcheza filamu mwenzie maarufu aitwae Guilherme de Padua pamoja na mkewe aliyejulikana kwa jina la Paula de Thomaz. Wote wawili walishtakiwa kwa mauaji ya Daniella. Tamthiliya ni biashara kubwa sana nchini Brazil ambayo huwaingizia wafanyabishara wa tasnia hiyo mamilion ya dola kila mwaka kutoka katika makampuni mbalimbali yanayorusha vipindi hivyo hususan Globo TV ya nchini humo.

Watengenezaji wa Tamthiliya hiyo ya Body and Soul hawakuiacha tamthilia hii iishie hewani kutokana na tukio hilo, walitaka kuunganisha tukio hilo na tamthiliya hiyo ili kuweka uhalisia.
Wakati wa mazishi ya Daniella ambayo yalihudhuriwa na maelfu ya wapenzi waliokuwa wameshtushwa na mauaji hayo Globo TV walirusha mazishi hayo moja kwa moja kupitia Television ya taifa hilo ili wapenzi ambao hawakupata fursa ya kuhudhuria mazishi hayo wapate fursa ya kushiriki msiba huo mzito. Kila ushahidi mpya uliokuwa ukipatikana kutokana na upelelezi wa kesi hiyo, Globo TV ilikuwa ipo kuhakikisha hawakosi mwendelezo wa tukio hilo. Na hata kesi hiyo ilipokuwa inaanza kusikilizwa, Globo TV ilipata ruhusa ya mahakama kurusha moja kwa moja usikilizwaji wa kesi hiyo kila siku ilipokuwa ikisikilizwa.

Ilikuwa kama ni mwendelezo wa tamthiliya hiyo, ambao haujawahi kushuhudiwa nchini humo, na mchezaji kiongozi (Stealing) wa tamthiliya hiyo alikuwa ni Guilherme de Padua. Huyu alikuwa ni mchezaji wa kusasambua (Stripper) wa zamani katika klabu za usiku nchini humo aliyegeuka kuwa mwigizaji wa tamthiliya, wakati huo akiwa na miaka 23. Alikuwa ndio amepata nafasi ya kucheza sehemu kubwa ya Tamthiliya hiyo akiigiza kwa jina la Bira, kijana mwenye tabia ya kubadilika badilika (moody) na mwenye wivu kupindukia juu ya mpenzi wake Daniella aliyecheza kama Yasmini.

Waigizaji wenzie katika tamthiliya hiyo walidai kwamba, de Padua alikuwa ameibeba tabia aliyokuwa akiigiza katika tamthliya hiyo katika maisha halisi, na alionekana kujawa na hofu ya kuachwa na mwigizaji mwenzie yaani Daniella. Usiku huo wa mauaji ya Daniella, de Padua alionekana dhahiri kuudhiwa na kipande kile cha filamu alichorekodi cha Yasimin na Bira uhusiano wao kuvunjika, yeye akiwa anaigiza kama Bira na Daniella akiwa anaigiza kama Yasimin katika tamthiliya hiyo ya Body and Soul. Wakati wa kurekodi kipande hicho de Padua alionekana kuwa zaidi ya mwigizaji kwani alionekana kuchukizwa na kitendo hicho dhahiri.

Msimamizi mkuu wa kurekodi tamthiliya hiyo (Director) alidai kumuona de Padua akiondoka katika eneo walilokuwa wakirekodia huku machozi yakimtoka. Baadae aliondoka bila kuongea na wasimamizi wa kurekodi tamthiliya hiyo na waigizaji wenzie. Muda mfupi baadae Daniella anakutwa akiwa ameuawa.

Baada ya kukamatwa siku iliyofuata baada ya mauaji hayo akiwa kama mtuhumiwa mkuu wa mauaji hayo, de Padua alikiri kuhusika na mauaji hayo. Hata hivyo masaa machache baadae alibadilisha maelezo yake aliyokiri awali kuhusika na mauaji hayo, na badala yake alimnyooshea vidole mkewe Paula De Thomaz, binti mrembo aliyekuwa na miaka 25 wakati huo. Paula de Thomaz binti kutoka katika familia yenye uwezo katika jiji hilo la Rio de Janeiro, alikuwa ndio ameolewa na de Padua na kudumu katika ndoa yao kwa miezi saba tu kabla ya mauaji hayo ya Daniella, pia alikuwa ni mjazito wa miezi mitatu.

De Padua alidai kwamba De Thomaz ndiye aliyemchoma Daniella kwa mkasi mpaka akafa, kutokana na wivu wa mapenzi, baada ya kugundua kwamba Daniella alikuwa na uhusiano wa siri wa kimapenzi na yeye de Padua kwa miezi kadhaa. kwa upande wake De Thomaz alikanusha madai hayo. Lakini hata hivyo baadae iliripotiwa kuwa De Thomaz alikiri kuhusika na mauaji hayo wakati alipokamatwa. Ilichukua miaka minne kabla ya siri nzito kufichuka wakati wa kusikilizwa kwa kesi hiyo. Kipindi hicho kesi ya Daniella Perez ilikuwa ni maarufu nchini humo, ikiwa inaangaliwa na watu wengi nchini humo kupitia matangazo ya Television.

Katika nchi ambayo utafiti uliofanywa mwaka 1991 ulionyesha kwamba kati kesi zaidi ya 4,000 zinazohusisha vitendo vya unyanyasaji wa kijinsia vinavyofanywa na wanaume dhidi ya wake zao au wapenzi wao, ni kesi mbili tu ndizo zilihukumiwa. Haraka sana kesi ya Daniella ilitumika kuhamasisha wananchi kupiga kelele dhidi ya vitendo hivyo. Kuanzia mwaka 1992 nchi hiyo ilishuhudia maandamamo ya wanawake wakitaka haki itendeke katika kesi hiyo ya Daniella, na pia waliitaka serikali ibadili mfumo wa sheria ambao unawawezesha wanaume kukwepa hukumu za vitendo vya kikatili wanavyowafanyia wanawake.

Mama yake Daniella alijikuta akiongoza kampeni ya kitaifa ya kutaka kubadilishwa kwa adhabu ya miaka 30, ndiyo iwe ya kiwango cha juu cha makosa ya mauaji ya kukusudia. Alifanikiwa kukusanya sahihi zaidi ya milioni kutoka kwa watu waliokuwa wakimuunga mkono. Watu wengi kutoka katika jamii ya Wabrazili walijikuta wakimuunga mama huyo mkono katika kampeni hiyo na hata wanasiasa walishurutishwa na wananchi wa nchi hiyo kutoa maoni yao juu ya kesi hiyo.
Wakati huo huo Guilherme de Padua akiwa rumande akisubiri kusikilizwa kwa kesi yake alisema kwamba, ametunga kitabu ambacho amekipa jina la, “The Story Which Brazil Does Not Know” kitabu ambacho kitathibitisha ukweli kwamba yeye hana hatia na alimlaani mkewe kwa kuhusika na mauaji hayo. Hata hivyo uchapishwaji wa kitabu hicho ulisitishwa na mahakama mpaka hapo shauri lao, yeye na mkewe De Thomaz litakapoisha kusikilizwa.

De Thomaz aliendelea kusisitiza kwamba hana hatia. Mnamo mwaka 1993 alijifungua mtoto wa kiume akiwa rumande na mtoto huyo alichukuliwa na wazazi wa De Thomaz kwa uangalizi. Mwaka mmoja baadae De Thomaz alipewa talaka na mumewe de Padua. Akihojiwa na gazeti moja maarufu nchini humo Paula De Thomaz alidai kwamba, de Padua amemuuwa Daniella na sasa anataka kuharibu maisha yake, ya wazazi wake na mtoto wake.

Hatimaye mnamo Januari 22, 1997, ikiwa ni maiaka minne tangu Daniella auawe, kesi ya Guilherme de Padua ilianza kusikilizwa ambapo chumba ambacho kilitumika kusikilizwa kesi hiyo kilifurika waanndishi wa habari na wengine walikuwa wakiirekodi kesi hiyo kwa kamera za video. Kwa muda wa siku nne wananchi wa nchi hiyo walikuwa wakiangalia TV ya Globo ili kuona yatakayoibuliwa katika shauri hilo na kuujua ukweli. Nje ya mahakama hiyo kulikuwa na TV Screen kubwa nyingi mbazo zilikuwa zikionyesha mwenendo wa kesi hiyo ambapo wananchi wengi walikusanyika nje wakifuatilia kesi hiyo iliyovuta hisia za wananchi wengi nchini humo. Wakati huo huo makundi ya watu waliokuwa wakipinga mauaji hayo, yalikuwa yakiendelea na kampeni zao nje ya mahakama hiyo.

Wakati wa kusikilizwa kwa kesi hiyo ndipo ilipojulikana ni kwa namna gani mapenzi ya siri kati ya Daniella Perez na de Padua yalivyopelekea waigizaji hao kufikia hatua ya mmoja kumuua mwenzie. Jose Filho, Mwendesha mashtaka katika kesi hiyo alielezea kwamba, de Padua alionekana kujawa na hofu ya kuachwa na mwigizaji mwenzie yaani Daniella, ambaye alikuwa na uhusiano naye wa siri mbali na walivyokuwa wakiigiza katika tamthiliya hiyo ya Body and Soul. Mwendesha mashtaka huyo aliendelea kusema kwamba kwa jinsi alivyokuwa na ukaribu na Daniella katika kuigiza tamthiliya hiyo ndivyo alivyozidi kuwa na wivu dhidi ya waigizaji wenzie na hofu ya kuachwa na Daniella kutokana na mafanikio aliyoyapata pamoja na umaarufu wake. Pia alikuwa na hofu kwamba penzi lao la wizi linaweza kujulikana.

Mwendesha mashtaka huyo aliendelea kubainisha pale mahakamani kwamba, yote hayo ndiyo yaliyomsukuma de Padua hadi kufikia hatua ya kufanya mauaji hayo, baada ya kurekodi kipande kile cha tamthiliya hiyo ambacho Daniella na de Padua waliaachana kama sehemu ya tamthiliya hiyo ambayo ilitungwa na mama yake Daniella mwenyewe.

Usiku wa siku yalipofanyika mauaji hayo, hapo mnamo Desemba 28, 1992, baada ya kurekodi sehemu ya tamthiliya hiyo, de Padua aliondoka hapo katika studio za Globo TV, na kuendesha gari lake hadi nyumbani kwake katika viunga vya Copacabana ambapo ndipo anapoishi yeye na mkewe De Thomaz. Baada ya kubadilisha namba ya gari lake kwa kuondoa namba halisi ya gari hilo LM 115 na kuweka OM 115, kwa kuibandika kwa gundi, de Padua aliendesha gari lake kuelekea upande wa studio za Globo TV ambapo alipanga kuonana na Daniella katika kituo kimoja cha mafuta. De Padua Alisindikizwa na mkewe katika safari hiyo.

Kulingana na maelezo ya mwendesha mashtaka, alisema kwamba, baadae de Padua alikutana na Daniella hapo katika kituo cha mafuta ambapo alipofika alipigwa na kitu kizito kichwani akapoteza fahamu. Alimpakia kwenye gari lake na kisha akiwa na mkewe De Thomaz. Inasadikiwa aliendesha gari hilo hadi sehemu iliyojitenga pembezoni mwa mji huo ambapo mmoja wao au wote kwa pamoja walimchoma kwa mkasi mara 18 kifuani na kumkata kooni kwa kutumia mkasi huo. Baadae waliutelekeza mwili wa Daniella.

Mwendesha mashtaka alisema kwamba mauaji hayo ni sehemu ya vioja vya mapenzi ambavyo vilikuwa vimeikumba ndoa ya de Padua na De Thomaz ambao inasemekana wote wawili walikuwa kila mmoja kaandika katika mfumo wa tattoo jina la mwenzie katika sehemu zake za siri. Katika utetezi wake de Padua aliendelea kujitetea kwamba mkewe ndiye aliyetekeleza mauaji hayo kwa sababu ya wivu. Alidai kwamba ni yeye aliyempiga Daniella na kitu kizito kichwani, na hiyo ilikuwa ni katika juhudi zake za kuwatenganisha mkewe na Daniella ambao walikuwa wanapigana kwa sababu yake. Alisema kwamba mkewe De Thomaz ndiye aliyemchoma Daniella kwa mkasi kifuani mara kadhaa wakati huo Daniella akiwa hajitambui mpaka akafa. De Padua alidai kwamba hakuona jinsi tukio zima la mauaji hayo lilivyofanyika. Lakini alishindwa kutoa sababu za yeye kutoona tukio hilo la mauaji lilivyofanyika.

Pia alikanusha madai kwamba alimteka Daniella na badala yake akasema kwamba Daniella alikwenda mwenyewe kwenye eneo la tukio. Akimtetea de Padua wakili wake aliyejulikana kwa jina la Paulo Romalho aliiambia mahakama kwamba mteja wake hakuwa na sababu ya kumuuwa Daniella. Na de Padua alipoulizwa kuhusu uhusiano wake wa kimapenzi na Daniella, alikanusha kuwa na uhusiano na mwigizaji huyo, lakini alidai kwamba ukaribu wake na Daniella ilikuwa ni kutaka kuwa karibu na mama yake yeye Daniella ambaye ndiye mtunzi wa tamthiliya ya Body and Soul waliyokuwa wakiigiza aitwae Gloria Perez, kwa lengo la kutaka amsaidie kuendeleza kipaji chake.

Hata hivyo kulitokea utata mkubwa katika kesi hiyo maarufu baada ya mashahidi ambao awali walikiri kumuona de Padua akimteka nyara Daniella katika kituo cha mafuta, kudai kwamba hawakumbuki kile walichokiona. Shahidi mmoja aliyetajwa kwa jina la Hugo da Silveira akitoa ushahidi wake alidai kwamba alimuona Paula de Thomaz katika eneo la tukio lakini alishindwa kueleza kwa usahihi wajihi wa De Thomaz. Pia shahidi huyo alishindwa kulitambua gari la de Padua ingawa aliliona na hata kunakili namba za gari hilo.

Kwa upande wa Paula De Thomaz, yeye aliendelea kukanusha kuhusika na mauaji hayo na alisema kwamba alikuwa kwenye manunuzi wakati huo wa mauaji katika duka moja maarufu katika jiji hilo la Rio De Janeiro liitwale Barra Shopping Mall ambapo alishushwa na mumewe. Pia alidai kwamba anao mashahidi wengi lakini wamekuwa na hofu kujihusisha kutoa ushahidi katika kesi hiyo iliyojizolea umaarufu.

Mnamo Januari 24, 1997, baada ya siku tatu za kusikiliza ushahidi wa kesi hiyo, jopo la Majaji waliokuwa wakisikiliza kesi hiyo walikesha usiku kucha wakipitia kesi hiyo kwa umakini mkubwa.
Mnamo siku ya Jumamosi, ya Januari 25, 1997 Guilherme de Padua alikutwa na hatia ya mauaji ya kupanga (Premeditated Murder) kwa kumuuwa Daniella Perez. Alihukumiwa kifungo cha miaka 19 jela, na kwa sababu alishatumikia miaka 4 akisubiri kusikilizwa kwa kesi yake hivyo alitakiwa atumikie miaka 15 jela. Jaji aliyemhukumu Jose Geraldo Antonio alimwelezea de Padua kama mtu hatari na wa kuogopwa katika jamii.

Kesi ya pili iliyomuhusu Paula de Thomaz, iliisha kusikilizwa kwake mnamo Mei, 1997, De Thomaz alikutwa na hatia ya kumsaidia mumewe kutekeleza mauaji hayo. Na yeye alihukumiwa kifungo cha miaka 15 jela.

Wakati huo huo Gloria Perez mama wa Daniella Perez akizungumzia kifo cha mwanae alisema kwamba,anaona kama vile ile tamthilia aliyoiandika alikuwa anamuandalia binti yake kifo.

Hapa chini nimeambatanisha youtube kuhusiana na mauaji hayo:





 
Last edited by a moderator:
Leo Ijumaa kama ilivyo ada, nimekuja na kesi hii iliyotokea huko nchini Brazil ambapo mapenzi kati ya wasanii wanaoigiza katika tamthiliya, yalivyoleta balaa kubwa na kusababisha mmoja kuuawa.

Ni kesi ambayo ilitikisa tasnia ya uigizaji nchini humo na ilileta changamoto hata kwa serikali ya nchi hiyo na kulazimika kutazama upya sheria zake zinazowakandamiza wanawake. Nimeweka simulizi hii makusudi ili kuonyesha ni kwa namna gani sanaa isipoambatana na maadili inavyoweza kusababisha watu kudhuriana au hata kutoana roho.............

Naamini wote tutajifunza kupitia simulizi hii.....................nawatakia weekend njema.
 
Kumbe leo Ijumaa ,,nimekutumia namba yangu unitumie ka mpesa ..
Asante mtambuzi kwa simulizi zako
Nitasoma baadae kidogo
 
Kumbe leo Ijumaa ,,nimekutumia namba yangu unitumie ka mpesa ..
Asante mtambuzi kwa simulizi zako
Nitasoma baadae kidogo
Haya nimeona na nimeshatuma M$-Pesa$................
Ukisoma hiyo baadae basi usisahau kuweka mtazamo wako hapa.......................Usije kaifananisha na ya Kanumba maana nakujua wewe.................LOL
 
Asante sana Mtambuzi nimeisoma yote na kuimaliza uwe na weekend njema..
Ila huyu muuaji na wife wake lol bado nafikilia kwa kina
 
Haya nimeona na nimeshatuma M$-Pesa$................
Ukisoma hiyo baadae basi usisahau kuweka mtazamo wako hapa.......................Usije kaifananisha na ya Kanumba maana nakujua wewe.................LOL


hahaha hii ya kanumba ni new epsode
Mala Freemason
Mala alikiuka masharti
Mala Ugonvi wa kimapenzi
Mala ....oooh,..
Niongezee basi M-pesa uliyotuma haitoshi kwa weekend..Cantalisia akinikuta hapa ha ha
 
Mkuu Mtambuzi story nzuri sana hii kuwa fundisho kwa jamii yetu.

Pamoja na watu wote kujifunza madhara ya mapenzi ya wizi lakini pia wahusika wa tasnia ya sanaa wanatakiwa kujifunza sana hapa.

Jambo kubwa na la mwisho hii ni changamoto kwa serikali pamoja na vyombo vyake vya dola katika kufanya upelelezi na kuuwakilisha mahakamani ili mahakama nazo zitoe hukumu za haki. Katika nchi yetu bado tuko nyuma sana katika suala la upelelezi.
 
Yes Gustavo! Kwakweli huyu kaka na mkewe nimeshindwa kuelewa kabisa.

1.Huyu kaka alionyesha kuchukia baada ya kuigiza kama ameachika

Ok yawezekana aliona kabisa kuwa huo ndio utakuwa mwisho wa kupata wakati wa kukutana na huyo dem mara kwa mara au ndio mwisho kabisa.

Na kwa vile yeye alikuwa ameoa inawezekana yule binti alikuwa na boy friend,
Jamaa akacheck akaona kwa nini wengine wakafaidi?

2. Yawezekana mkewe alishajua na wakapanga kummaliza!

Mh dunia hii!
Lkn kidogo inautata kama ya Kanumba
 
mh, mkuu mtambuzi kwanza shukrani mbele,
kuhusu hao jamaa mi nashindwa kuelewa kwa sababu sioni sababu ya mke kumsaidia mumewe kuua, dah, binadamu bwana kweli wanan vituko, ila inawezekana jamaa alimcorrupt mkewe, afu si tumeambiwa alishaanza kubeba uhusika kwenye maisha ya kawaida....wabongo jifunzeni sasa!!!!!!!!!1
 
hahaha hii ya kanumba ni new epsode
Mala Freemason
Mala alikiuka masharti
Mala Ugonvi wa kimapenzi
Mala ....oooh,..
Niongezee basi M-pesa uliyotuma haitoshi kwa weekend..Cantalisia akinikuta hapa ha ha

Hivi nyie watu mbona mnaomba watu pesa kwa upendeleo? Plz niombe na mimi FirstLady1
 
Last edited by a moderator:
Kwa kweli wangepata second chance ili waweze tutatulia utata kama huu
Kile kitabu alichotuinga muuaji kikazuiwa kuchapishwa na mahakama......................Mpaka leo hakijatoka...........!
 
Kile kitabu alichotuinga muuaji kikazuiwa kuchapishwa na mahakama......................Mpaka leo hakijatoka...........!

Kwanini walikizuia, kilikuwa kikipotosha?

Nadhani jamaa aliua kwa mwendelezo wa ile movie yao
inaelekea alichukulia serious ile kuachwa kwenye movie na kamfume dume akaamua kummaliza!

Yaani sipati picha kabisa!
 
Back
Top Bottom