Na mwandishi wetu
Mazungumzo ya Rais Jakaya Kikwete na Rais George W. Bush wa Marekani, yamezua mtafaruku nchini Kenya, hasa baada ya kubainika kuwa moja ya ajenda katika mazungumzo hayo, ilikuwa ni kuyumba yumba kwa hali ya kisiasa nchini humo.
Magazeti ya Kenya yamewakariri maafisa wa serikali ya nchi hiyo, wakilaumu vikali hatua ya Rais George Bush kuzungumzia hali ya kisiasa Kenya bila kuwahusisha viongozi wa serikali waliopo New York waliohudhuria mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.
Ujumbe wa Kenya katika mkutano huo unaongozwa na waziri wake wa mambo ya Nje, Raphael Tuju, ambaye anatarajia kulihutubia Baraza la Umoja wa Mataifa Septemba 27.
Habari za kuwapo kwa ajenda hiyo katika mazungumzo ya Rais Kikwete na Rais Bush zilitolewa na Mkurugenzi wa Masuala ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, Dk Cindy Courville.
Rais Kikwete ni kiongozi pekee aliyepewa nafasi ya kuonana na Rais Bush kutoka nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara na alifanya mazungumzo hayo katika hoteli maarufu ya Waldorf Astoria jijini New York Jumanne wiki hii.
Jana magazeti Kenya yalimkariri Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Moses Wetang'ula, akilaumu uamuzi wa Bush kuzungumzia suala hilo, huku akiwaacha viongozi wa serikali ya Kenya ambao pia wapo New York kuhudhuria mkutano huo.
"Tutatuma ujumbe wa kidiplomasia kupinga kwa nguvu zetu zote tabia hii ya ajabu na dharau dhidi ya watu wa Kenya. Hapa kwetu hakuna mzozo wa kisiasa. Tunataka tupate ufafanuzi kama kweli jambo hili lilijadiliwa na marais hawa au kauli hiyo ilitolewa kwa bahati mbaya," alisema Wetang'ula, alipozungumza na gazeti la Daily Nation la jana.
Wetang'ula alisisitiza kuwa Kenya ni moja ya nchi za kupigiwa mfano barani Afrika kutokana na utulivu wa kisiasa uliopo na kwamba kamwe nchi yake haijawahi kufikia kiwango hicho kilichochoea mazungumzo kati ya Rais Kikwete na Rais Bush.
Alisema kinachotokea sasa ni kwamba nchi yake inajiandaa kwa ajili ya uchaguzi mwakani na kwamba kinachotokea hakiwezi kutajwa kuwa ni hali mbaya ya kisiasa nchini humo.
"Hakuna mgogoro wala mzozo wowote wa kisiasa hapa. Tunaamini kuwa Rais Mwai Kibaki, kwa kutumia nafasi yake katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, atalizungumzia suala hili atakapokutana na Rais Kikwete," alisema.
Mbali na kuandika habari hiyo, gazeti la Daily Nation pia liliandika tahariri kulaani mazungumzo hayo, likisema wananchi wa Kenya wamebebeshwa mizigo mizito kutokana na uhusiano wa serikali yao na ile ya Marekani.
Tahariri hiyo ilisema uamuzi wa viongozi hao wawili kuzungumzia hali ya kisiasa Kenya ni dalili ya kuonyesha dharau za wazi kwa nchi hiyo, hasa ikizingatiwa kuwa ujumbe wa serikali ya Kenya ulikuwapo New York, lakini haukuitwa na Bush katika mazungumzo hayo.
Tahariri hiyo inamtaja Rais Bush kama kiongozi wa ajabu kwa kuwa hivi karibuni, alipokea hati za utambulisho kutoka kwa Balozi wa Kenya nchini Marekani na katika hafla hiyo, akaisifia Kenya kuwa ni moja ya nchi yenye utulivu mkubwa wa kisiasa barani Afrika.
Imesema habari hizo za uongo zinazotolewa dhidi ya Kenya ndizo zinazoifanya serikali ya Marekani iwe inatoa maonyo ya kila mara kwa watalii wa Kimarekani wanaofika Kenya na Afrika Mashariki na hivyo kuzorotesha juhudi za kuinua uchumi wa nchi.
"Nchi yetu imepata madhara makubwa kutokana na magaidi kuiona kuwa rafiki wa karibu wa Marekani na mamia ya watu wetu wamekufa kutokana na hali hiyo. Lakini kila tunachokisikia kila siku ni kwamba utawala wa nchi yetu umejaa ufisadi au upumbavu au vyote viwili. Ukiwa na marafiki wa aina hii unahitaji kuwa na maadui kweli?" inasema sehemu ya tahariri hiyo.
Kwa mujibu wa Dk Courville, Kikwete na Bush pia walizungumzia hali ya kisiasa katika nchi za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo pamoja na uhusiano wa kisiasa na kiuchumi kati ya nchi hizo mbili. Hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Rais Kikwete kufanya mazungumzo na kiongozi huyo wa taifa kubwa duniani tangu aliposhika madaraka Desemba 21 mwaka jana.
Kutoka Mwananchi
Mazungumzo ya Rais Jakaya Kikwete na Rais George W. Bush wa Marekani, yamezua mtafaruku nchini Kenya, hasa baada ya kubainika kuwa moja ya ajenda katika mazungumzo hayo, ilikuwa ni kuyumba yumba kwa hali ya kisiasa nchini humo.
Magazeti ya Kenya yamewakariri maafisa wa serikali ya nchi hiyo, wakilaumu vikali hatua ya Rais George Bush kuzungumzia hali ya kisiasa Kenya bila kuwahusisha viongozi wa serikali waliopo New York waliohudhuria mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa.
Ujumbe wa Kenya katika mkutano huo unaongozwa na waziri wake wa mambo ya Nje, Raphael Tuju, ambaye anatarajia kulihutubia Baraza la Umoja wa Mataifa Septemba 27.
Habari za kuwapo kwa ajenda hiyo katika mazungumzo ya Rais Kikwete na Rais Bush zilitolewa na Mkurugenzi wa Masuala ya Afrika katika Wizara ya Mambo ya Nje ya Marekani, Dk Cindy Courville.
Rais Kikwete ni kiongozi pekee aliyepewa nafasi ya kuonana na Rais Bush kutoka nchi za kusini mwa Jangwa la Sahara na alifanya mazungumzo hayo katika hoteli maarufu ya Waldorf Astoria jijini New York Jumanne wiki hii.
Jana magazeti Kenya yalimkariri Naibu Waziri wa Mambo ya Nje wa Kenya, Moses Wetang'ula, akilaumu uamuzi wa Bush kuzungumzia suala hilo, huku akiwaacha viongozi wa serikali ya Kenya ambao pia wapo New York kuhudhuria mkutano huo.
"Tutatuma ujumbe wa kidiplomasia kupinga kwa nguvu zetu zote tabia hii ya ajabu na dharau dhidi ya watu wa Kenya. Hapa kwetu hakuna mzozo wa kisiasa. Tunataka tupate ufafanuzi kama kweli jambo hili lilijadiliwa na marais hawa au kauli hiyo ilitolewa kwa bahati mbaya," alisema Wetang'ula, alipozungumza na gazeti la Daily Nation la jana.
Wetang'ula alisisitiza kuwa Kenya ni moja ya nchi za kupigiwa mfano barani Afrika kutokana na utulivu wa kisiasa uliopo na kwamba kamwe nchi yake haijawahi kufikia kiwango hicho kilichochoea mazungumzo kati ya Rais Kikwete na Rais Bush.
Alisema kinachotokea sasa ni kwamba nchi yake inajiandaa kwa ajili ya uchaguzi mwakani na kwamba kinachotokea hakiwezi kutajwa kuwa ni hali mbaya ya kisiasa nchini humo.
"Hakuna mgogoro wala mzozo wowote wa kisiasa hapa. Tunaamini kuwa Rais Mwai Kibaki, kwa kutumia nafasi yake katika Jumuiya ya Afrika Mashariki, atalizungumzia suala hili atakapokutana na Rais Kikwete," alisema.
Mbali na kuandika habari hiyo, gazeti la Daily Nation pia liliandika tahariri kulaani mazungumzo hayo, likisema wananchi wa Kenya wamebebeshwa mizigo mizito kutokana na uhusiano wa serikali yao na ile ya Marekani.
Tahariri hiyo ilisema uamuzi wa viongozi hao wawili kuzungumzia hali ya kisiasa Kenya ni dalili ya kuonyesha dharau za wazi kwa nchi hiyo, hasa ikizingatiwa kuwa ujumbe wa serikali ya Kenya ulikuwapo New York, lakini haukuitwa na Bush katika mazungumzo hayo.
Tahariri hiyo inamtaja Rais Bush kama kiongozi wa ajabu kwa kuwa hivi karibuni, alipokea hati za utambulisho kutoka kwa Balozi wa Kenya nchini Marekani na katika hafla hiyo, akaisifia Kenya kuwa ni moja ya nchi yenye utulivu mkubwa wa kisiasa barani Afrika.
Imesema habari hizo za uongo zinazotolewa dhidi ya Kenya ndizo zinazoifanya serikali ya Marekani iwe inatoa maonyo ya kila mara kwa watalii wa Kimarekani wanaofika Kenya na Afrika Mashariki na hivyo kuzorotesha juhudi za kuinua uchumi wa nchi.
"Nchi yetu imepata madhara makubwa kutokana na magaidi kuiona kuwa rafiki wa karibu wa Marekani na mamia ya watu wetu wamekufa kutokana na hali hiyo. Lakini kila tunachokisikia kila siku ni kwamba utawala wa nchi yetu umejaa ufisadi au upumbavu au vyote viwili. Ukiwa na marafiki wa aina hii unahitaji kuwa na maadui kweli?" inasema sehemu ya tahariri hiyo.
Kwa mujibu wa Dk Courville, Kikwete na Bush pia walizungumzia hali ya kisiasa katika nchi za Burundi na Jamhuri ya Kidemokrasi ya Kongo pamoja na uhusiano wa kisiasa na kiuchumi kati ya nchi hizo mbili. Hii ilikuwa ni mara ya kwanza kwa Rais Kikwete kufanya mazungumzo na kiongozi huyo wa taifa kubwa duniani tangu aliposhika madaraka Desemba 21 mwaka jana.
Kutoka Mwananchi