Matatizo ya Watanzania yawaliza Wajapani

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
UPUNGUFU wa walimu wenye sifa katika shule za awali umemfanya mfanyakazi wa kujitolea kutoka Japan ambaye amemaliza muda wake, Norie Sasaki kutokwa na machozi wakati akielezea changamoto zinazoikabili Tanzania.

Sasaki, ambaye alikuwa mwalimu wa watoto wadogo katika Halmashauri ya Jiji la Mbeya, alikuwa akieleza changamoto alizoziona huku akitokwa na machozi jana walipotembelea Ofisi ya Rais Menejimenti ya Utumishi wa Umma kwa ajili ya kuagwa.

Mwalimu Sasaki, ambae aliambatana na wataalamu wenzake wanne waliokuwa wakifanya kazi za kujitolea katika maeneo mbalimbali ya elimu na afya kupitia Shirika la Ushirikiano wa Maendeleo la Japan (JICA), alisema bado Serikali ya Tanzania haijaweka mkazo katika elimu ya awali.

Alisema kutokuwepo kwa mkazo katika elimu hiyo, kunawajengea watoto misingi mibovu ya maisha.

Mwalimu Sasaki alisema katika miaka miwili aliyofanya kazi ya kujitolea katika Jiji la Mbeya, amekutana na changamoto nyingi ikiwemo ya uhaba wa walimu kutokana na kutokuwepo kwa vyuo vya ualimu wa elimu ya awali.

“Walimu wengi wa awali niliokutana nao walikuwa hawana sifa ya kufundisha kwa sababu hawakuwa na vyeti… msifikiri kazi ya kufundisha watoto ni rahisi, lazima mtu anayewafundisha awe na elimu ya kutosha,” alisema.

Kwa upande wake Sayaka Hosoyamada ambae alikuwa mwalimu wa kujitolea wa sayansi na hisabati katika Shule ya Sekondari Ndugu, mkoani Mwanza, alisema bado Tanzania inakabiliwa na uhaba wa walimu wa sayansi huku akielezea kuwa alilazimika kufundisha vipindi zaidi ya 30 kwa wiki.

Alisema changamoto nyingine ni umeme na maji ambayo ingawa shule yao ilikuwa karibu na ziwa, lakini walikuwa wakilazimika kuoga mara moja kwa wiki kutokana na ukosefu wa maji. Naye Noriko Komatsu, ambaye alikuwa muuguzi katika Hospitali ya Wilaya ya Nachingwea, mkoani Lindi alisema kuna upungufu mkubwa wa dawa na vifaa nchini pamoja na wataalamu wa afya na mara nyingine wagonjwa wamekuwa wakipewa dawa zilizomaliza muda wake.

Akiwaaga wataalamu hao, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, George Yambesi aliwashukuru kwa kujitolea na aliahidi kuwa Serikali itazifanyia kazi changamoto hizo kupitia wizara husika.
 
Back
Top Bottom