Lycaon pictus
JF-Expert Member
- Jan 31, 2021
- 7,310
- 12,859
Asili na habari za Wachaga
Wachaga walikuwa ni moja ya makabila ya kwanza kwanza kabisa Tanzania kukutana na kupata ustaarabu wa Kizungu. Hilo limefanya kuwa kabila ambalo historia yake imeandikwa na kutunzwa zaidi. Sasa historia yao imejaa damu hasa, kuisoma tu lazima usikie harufu ya damu. Sijui kama makabila mengine nayo walichinjana namna hii(historia zao hazijatunzwa kama ya Wachaga). Nilichogundua baada ya kusoma kitabu hiki ni kuwa 1. Kilimanjaro ilikuwa tajiri hata kabla ya wazungu. 2. Utajiri wa Kilimanjaro ndiyo ulifanya watu wachinjane sana kuugombania. 3. Mangi Meli ni Mangi mdogo sana kwenye historia na inawezekana alikuwa kibaraka wa wadachi, kulikuwa na Mamangi hasa.
Kitabu hiki Asili na Habari za Wachaga kiliandikwa mwaka 1932 na mtafiti wa masuala ya wenyeji aliyeitwa Charles Dundas. Jisomee mwenyewe.
DIBAJI
KWA Wamangi, wazee na watu wa Kilimanjaro, Salamu ! Habari hizi za kale za kabila la Kichaga zilitungwa kwa maneno niliyoambiwa na wazee wa kila umangi. Maarifa niliyoyapata kwao ya kabila lenu yalinisaidia sana katika kuiendesha nchi kwa desturi za sheria zenu, na kusudi maarifa hayo yasipotee na kusahauliwa na ninyi na watoto wenu, nimeyaandika katika kitabu. Natumaini kitasaidia kuhifadhi haki katika nchi yenu mliyoirithi kwa babu zenu, kiwafanye mwone kiburi na upendo kwa nchi yenu, na kiwafanye mwatii Wamangi wenu na kutumainia mambo ya mbele. Tabia hizi mtaziona katika watu ambao habari zao zimesimuliwa kitabuni humu, na mkizifuata, mtawastahili babu zenu, na kuwasifu kwa ushujaa waliokuwa nao ambao uliuhifadhi urithi wenu. Pia, mtasoma mumu humu habari za mambo maovu na ya upuzi yaliyofanywa na watu wabaya, maana mambo kama hayo yamo katika habari za kila nchi.
Kumbukeni sana ya kuwa mambo mema na mabaya yaliyofanywa na watu huandikwa na kukumbukwa kwa miaka mingi baada ya kufa kwao.
Nawapeni kitabu hiki kiwafundisheni, na tena kiwe ukumbusho wa miaka ile niliyokaa miongoni mwenu, na kiwe alama ya upendo nilio nao kwenu.
Natumaini ya kuwa habari za sasa na za baadaye za nchi yenu zitakuwa za amani na usitawi, na kama hatuonani tena, kitabu hiki kiwe alama ya urafiki kati yetu.
Nataka kuwashukuru sana Nathanael Mtui na Joseph Merinyo walionisaidia sana katika kukitunga kitabu hiki.
Natia sahihi yangu, nikikitaja cheo kile cha heshima mlichonipa.
CHARLES DUNDAS,
Wasahuye-O-Wachaga (Elder of Kilimanjaro).
ASILI NA HABARI ZA
WACHAGA
SEHEMU YA KWANZA
SURA YA KWANZA
ASILI YA KABILA LA WACHAGA.
WACHAGA
SEHEMU YA KWANZA
SURA YA KWANZA
ASILI YA KABILA LA WACHAGA.
TANGU asili Wachaga si watu wa kabila moja, wala asili yao haitoki Kilimanjaro. Tukirudi nyuma na kuchungulia habari za asili ya koo mbali mbali zilizoko sasa, tutaona ya kuwa babu zao walikuja vikosi vidogo vidogo kutoka nchi nyingine nyingine hata wakafika Kilimanjaro. Pengine mtu tu na nyumba yake walifika, au pengine mtu peke yake, akaja akasimamisha ukoo au Kishari. Walikuja katika nyakati mbali mbali; kuna waliofika miaka mia kadhawakadha iliyopita, na wengine waliofika si zamani sana. Sasa yapata vizazi 20 vimepita tangu watu wa kwanza katika hao walipohamia Kilimanjaro; kwa hivi twaweza kuhesabu kuwa miaka 500 au 600 imepita tangu wakati huo hata hivi leo.
Wazee hao wote wa zamani waliotangulia kuhamia huko walikuwa karibu wote Wakamba, Wataita, Wapare, Washambala, Wamasai, na Wandorobo, lakini waliokuwa wengi zaidi ni Wakamba, Wataita na Wamasai, na katika hawa pia waliokuwa wengi sana ni Wakamba. Basi Wakamba na Wataita walifika kutoka kaskazini na mashariki ya Kilimanjaro, na kwa hivyo, upande wa mashariki na wa kaskazini wa mlima ulifikiwa na hao watu wa kwanza. Tangu nyakati hizo, koo nyingi nyingine zimeingia na kukaa kuuzunguka mlima. Nyingi zimegawanyika katika sehemu sehemu, na vita vya siku nyingi vilivyofuata vilifanya watu kuhamahama sana. Husemwa ya kuwa hao waliotangulia kufika katika nchi ya Kilimanjaro walipofika, waliwakuta washenzi wengine waliokuwa wakikaa mwituni wanaokumbukwa hata sasa kuwa ni Wakonongo au Watarimba. Sasa hawaonekani kabisa, maana labda walifukuziwa mbali au kuangamizwa na wageni waliokuja nyuma yao. Husemwa kuwa walikuwa watu wadogo sana wenye vichwa vikubwa, na hujipatia chakula chao kwa kuwinda; na ingawa hii ni hadithi tu, twaweza kusadiki ya kuwa walikuwa mbilikimo. Watu wengi wa namna hiyo walikuwapo katika Afrika, na baadhi yao wapo hata leo katika sehemu nyingine nyingine, na huonekana hasa katika nchi zenye misitu mikubwa mikubwa. Siku hizo yadhaniwa kuwa mitelemko ya Kilimanjaro ilikuwa imefunikwa na mwitu mkubwa uliotambaa mpaka chini uwandani, maana nchi yote inayokaliwa na Wachaga sasa ilifyekwa na watu hao waliotangulia kufika huko, ambao hawakuweza kabisa kulima mpaka walipokwisha kufyeka nafasi. Mwitu huo ulikuwa mkubwa na wa kushikana sana, hata mara nyingi watu wa ukoo huu hawakuwa na habari za watu wa ukoo mwingine, na kwa hivyo hawakujua kuwa walikuwapo watu wengine wanaokaa mlimani; basi kwa muda mrefu kila ukoo ulikaa peke yake, wala hawakuungana ila kwa taratibu kidogo kidogo hata wakawa jamaa kubwa wanaokaa mahali pamoja.
Kila ukoo ulikuwa na mkuu wake, au mzee, na ndiye aliyetawala ukoo. Mara nyingi koo mbili tatu hupigana, na pengine ukoo mmoja hushindwa na kulazimishwa kukubali utawala wa ule ulioshinda. Hivi basi, nguvu ya ukoo huo huwa nyingi, ndipo hupigana na wa tatu, na ushindapo, nguvu yake na mali huzidi kuongezeka, na vivyo hivyo mpaka ukoo mmoja hutawala koo nyingi; na mkubwa wao huwa Mangi. Basi kwa namna hiyo baada ya kupita muda mkubwa nchi yote ya Kilimanjaro iligawanyika na kutawaliwa na Wamangi mbali mbali. Wakuu hao walipigana wao kwa wao, pengine mkuu mmoja huwashinda wengi wengine, na kuwaweka chini yake. Hatimaye wakuu wengineo wachache walipigana ili wapate ukubwa wa kutawala mlima wote, na mambo yakaendelea hivyo mpaka siku za Wazungu zilipofika, ndio walioyakomesha mapigano hayo yote.
Katika kitabu hiki tutasoma habari jinsi Wamangi wengi walivyoinuka, na jinsi walivyotawala na kuzilinda nchi zao au jinsi walivyoshindwa; basi hapo tutafahamu jinsi watu walivyokuwa mashakani kabla ya kuja Wazungu, na jinsi walivyofaidiwa na utawala wao.
Kabla hatujaanza habari za Wachaga, lazima tuangalie jinsi Wachaga walivyogawanyika katika sehemu mbali mbali za utawala. Kuanzia upande wa magharibi twaona: Shira (iitwayo na Wazungu Kibongoto), Machame, Kibosho, Kindi, Uru, Mbokomo, Moshi. Nchi hizi tutaziita Kilimanjaro ya magharibi, au Kiboo. Tukiendelea kuuzunguka mlima, tutaona nchi iitwayo Vunjo; nayo ni milki ya Kirua, Kilema, Marangu, Mamba na Msae (ambayo sasa ni sehemu ya Mwika) na Mwika. Kutoka hapo twaona nchi ya upande wa mashariki ya Kilimanjaro inayoitwa sasa Rombo. Jina hili latokana na mkuu maarufu Horombo au Orombo. Katika nchi hii ziko milki hizi: Mengwe, Mriti, Keni, Mkuu, (hata hivi karibuni Chimbili ilikuwamo) Mrau, Kirua, Machati, Olele na Useri (hata hivi karibuni Ngasini ilikuwamo). Nchi yote ya Rombo hapo zamani iligawanyika katika nchi kubwa tatu, yaani Chimbili, Mkulya, na Useri.
Hivi, zamani nchi ya Uchaga iligawanyika katika sehemu kubwa tatu kufuatana na pande tatu zilizomo katika sehemu ya mlima inayoweza kukaliwa na watu. Tutaona ya kuwa katika habari za zamani za kabila, wakuu wa kila sehemu hizi walipigana wao kwa wao, lakini hapana aliyeweza kuruka sana mpaka wa sehemu yake ya nchi. Baadaye walipokuwa wakuu wenye nguvu nyingi, pengine wengine hujiunga pamoja, na kupigana na sehemu moja au mbili nyingine. Basi yafaa tukumbuke majina haya: Kiboo, Vunjo na Rombo. Rombo ina sehemu tatu, ndizo Chimbili, Mkulya na Useri.