Kikwete amekwama mara 7

Edson

JF-Expert Member
Mar 7, 2009
9,846
5,076
Naanza moja kwa moja

Kwanza

Mrisho Kikwete (kama Mwenyekiti wa CCM taifa) ameshindwa uongozi
jumla! Ameshindwa kukisimamia chama chake (CCM) katika kurudi kwenye “asili”
baada ya chama hicho cha “wakulima na wafanyakazi” kupoteza haiba yake (shakhsia
ya kisiasa) kwa kuvamiwa na mafia, majambazi na matapeli wa kisiasa.

Uongozi wa chama unayumba na hata wakati mwingine kushindwa kuchukua maamuzi ya moja kwa moja na yenye taathira chanya kwa mustakabali wa chama juu ya falsafa ya kukisafisha chama na kukirudisha mikononi mwa wanachama. CCM imeachwa mikononi mwa wanahisa wanayeitumia CCM kama “kampuni ya kibiashara.”
Kushindwa kwenye chama na kufeli kwenye medani ya kukielekeza chama kwenye
misingi ya ujenzi wa jamii ya watu waliyo sawa na huru ni matokeo ya aidha rais
kuwa sehemu ya mfumo uliyoshindwa wa chama au kuzidiwa ujanja (wa kimafia,
kijambazi na kitapeli) na baadhi ya wanachama kwenye “mtandao” aliyeutumia mwaka
2005 kufikia lengo la kushika mamlaka ya nchi baada ya kushinda kwa “kimbunga”
kilichotokana na matumizi makubwa ya fedha na propaganda ya ahadi za kinafiki!
Unafiki ulichukua sehemu kubwa ya “ahadi za uchaguzi” kama zilivyotumika
mwaka 2005 na kurudiwa tena mwaka 2010!


Pili

kuongoza si lelemama kwani si urembo wa kujionyesha kwenye hafla, dhifa
na sherehe za kitaifa na kimataifa, hasha! Uongozi ni menejimenti ya kupanga
mipango sanifu, usimamizi wa mipango makini, na upimaji muafaka wa matokeo ya
utekelezaji wa mipango ya maendeleo ya siasa, uchumi na jamii kwa ajili ya watu
na maendeleo ya watu hao.

Kwa hili, Rais Kikwete amekwama, atabaki kutazama macho, labda anaweza
kupongezwa kwa kufanikisha sherehe za Miaka 50 ya Uhuru wa Tanganyika kwa vile
“makomandoo” wa JWTZ waliweza kuvunja matofali kwa vichwa, siyo? Sidhani!
Tatu

sarafu ya Tanzania imeporomoka sana na wakati huohuo uwezo wa wananchi
wa kawaida kumudu maisha yao ya kila siku umeporomoka pia! Rais Kikwete
ameshindwa kutangaza “hali mbaya ya uchumi” na hata haonyeshi dalili ya
kukabiliana na matatizo ya kiuchumi.


Wananchi wa mijini na vijijini, wameendela kutaabika kwenye maisha magumu (na
ya msoto) ilhali viongozi wan chi wanatumia nafasi hiyo kuzunguka duniani na
hata kwenda kujipumzisha na kustarehe wakati nchi ingali kwenye maafa ya
kiuchumi, kijamii na kisiasa! Sidhani kama kwa viongozi weledi wangeweza kupata
usingizi katika hali kama hii!

Ushahidi unaonyesha kwamba wapo viongozi waliyewajibishwa kujiuzulu baada ya
kushindwa kufikia utashi wa wananchi wao. Tuchukue mifano ya Italia na Ugiriki
ambapo viongozi wa serikali za nchi hizo waliwajibika kuachia ngazi na kuwapisha
viongozi wengine wenye uwezo wa akili ya kutatua matatizo yanayozikabili nchi
hizo!

Kinyume chake, uongozi wa Rais Kikwete, umekuwa ukitumia nafasi hiyo
kujipamba na “sifa kama za makomandoo kuvunja matofali kwa vichwa ilhali
wananchi wakiteseka na maisha magumu kwa mfumuko wa bei za bidhaa za vyakula na
ukosefu wa nishati ya umeme na petroli. Hii ni hatari ya uongozi wa nchi
kukwama!

Kwa ujumla, hali ya uchumi wa wananchi wa kawaida wanaotegemea maisha ya
kudunduliza yamekuwa ya shida kwa vile shilingi imeota mbawa (na inaruka kwa
kasi ya ajabu).

Upatikanaji wa bidhaa za vyakula umekuwa mgumu na kwa bei ya juu kuliko
ilivyokuwa enzi za Awamu ya Tatu ya mzee Benjamin Mkapa!

Unga wa sembe, unga wa ngano, mchele, maharagwe (mboga ya taifa), sukari na
mavazi vyote kwa pamoja vimekuwa bei juu (na havikamatiki madukani).

Wananchi wamekuwa wakisubiri nafuu ya “maisha bora” kwa mwaka wa sita sasa;
kila siku afadhali ya jana! Uongozi wa nchi ni mwendo-mdundo, mbele kwa mbele,
unahesabu siku 2015 ifike!

Nne

jamii ya Tanzania imeanguka! Uongozi wa nchi umekuwa ukiiangalia jamii
kwa jicho la “dharau” kana kwamba wao (viongozi) wanaishi “mbinguni.” Angalia
huduma mbovu na zisizokidhi viwango za afya ya wananchi walalahoi hususan wa
mijini na wa vijijini!

Tazama shule za msingi za serikali zilivyotelekezwa na nyingine kuachwa
zijiendeshe kama walimu watakavyo. Kwa ujumla, watoto wa wananchi walalahoi na
wale malofa (wenzangu na mimi) wameachwa wajisomee na au wasomeshwe kwenye
mazingira dhaifu na yasiyo rafiki ilhali watoto wa vigogo na wenye nacho
wakisomeshwa kwenye shule za daraja la pili na la kwanza (zinaitwa English
Medium Schools).
Jamii imegeuzwa ya matabaka! Uongozi wa CCM na serikali yake unaangalia
kuongezeka kwa pengo baina ya maskini na matajiri wachache huku vigogo wa CCM na
serikali yake wakiendelea kushadidia uwepo wa matabaka hayo.


Kuzorota kwa afya ya jamii; kuparaganyika kwa mfumo wa elimu ya walalahoi na
maskini wa Tanzania kunatumika kama sehemu ya mkakati wa nguvu ya wenzo dhidi ya
kutawala siasa katika mfumo wa vyama vingi ambapo siasa inatumia fedha kufikia
malengo ya kupata uongozi wa serikali. Nje ya chama uongozi unaonyesha
unawatumikia wananchi ilhali, ndani yake ni ufisadi mtupu!

Tano

Rais Jakaya Mrisho Kikwete ameshindwa kupambana na ufisadi na vitendo
vinavyoambatana nao.

Mwanzo, wakati alipoingia madarakani Desemba 2005, nilidhani
angaliwashughulikia wala rushwa kwa kasi mpya ambao alidai “anawafahamu
isipokuwa alikuwa anawapa muda.”

Miaka mitano ilipita na kupituka hadi sasa ni 2012 hakuna hata ufisadi mkubwa
ulioshughulikiwa kikamilifu kwa kuonyesha mfano. Kuna kadhia kadha wa kadha za
ufisadi ambazo hazikushughulikiwa vema kama vile: Ufisadi wa ununuzi wa mitambo
ya kufua umeme wa dharura (uliyozaa kashfa ya Richmond); Ufisadi wa Akaunti za
Malipo ya Madeni ya Nje (EPA); Ufisadi wa Meremeta; Ufisadi wa Jairo; Ufisadi wa
Majengo Pacha (Twin Towers) ya Benki Kuu; na kadhalika!

Kwa mshangao wa wengi; hata kwa wahisani wanaotufadhili kwenye mipango yetu
ya maendeleo waliyehusika wengi kwenye kashfa hizo wanadunda na au wanaendelea
“kula bata” huku Rais Jakaya Mrisho Kikwete akionyesha “kwenda polepole” kama
“Mzee Kobe” ilhali nchi inatafunwa na wajanja wachache wanaojiandaa kujiingiza
kwenye uongozi wa chama na serikali kuanzia mapema 2012 (ndani ya CCM) na 2015
(Ikulu ya Magogoni).

Nadhani kama Rais Kikwete amekalia “kuti kavu;” sidhani kwa sababu anadhani,
“acha nimalize muda wangu niwaachie” ni falsafa halali kwa kiongozi wa nchi,
sidhani!

Sita

ninapomtazama Rais Kikwete kama Mwenyekiti wa CCM, naona kama amekwama!
Kama kiongozi asiyekuwa na satwa ya kuchukua maamuzi magumu na yenye taathira
kubwa chanya amezungukwa na wapambe na au washauri wenye hila, nia mbaya, choyo
na uroho hali inayomfanya kiongozi huyu kushindwa kuthubutu.

Sidhani kama anaweza kuchukua uamuzi wa kuwaadabisha na au kuwasulubu wapambe
na au “washikaji” wake wanaomfanya aonekane kama kiongozi anayepwaya kwenye
nafasi zote za uongozi na menejimenti ya chama chake (CCM) na nchi kadhalika.

Manabii wa ufisadi wamemng’angania na yeye (kama Rais wa Nchi) amezingirwa na
mafuriko ya ufisadi wa kimfumo na wa ndani ya mfumo! Hata wakati mwingine
“mipango” ya ufisadi kufanywa na wenye dhamana ya uongozi na menejimenti ya
serikali, yaani wizarani na Ikulu (kwa Katibu Mkuu Kiongozi).

Saba, na mwisho napenda nizungumzie suala la kushindwa kuilinda na kuihifadhi
Katiba ya Jamhuri ya Muungaano wa Tanzania (JMT) ya 1977 (2005).

Kwa mujibu wa Ibara ya 33(1), Tanzania itakuwa na Rais wa Nchi (ambaye kwa
sasa ni Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete); na yeye (Jakaya Mrisho Kikwete)
atakuwa Rais wa Nchi na Mkuu wa serikali (kama ilivyo kwa Ibara ya 33(2) ya
katiba hiyo).
Kwa maana yoyote iwayo, Rais wa Nchi kama mkuu wa serikali ndiye mlinzi
anayetakiwa kuihifadhi na kuilinda Katiba ya JMT ya 1977 (2005). Mheshimiwa
Jakaya Mrisho Kikwete ameshindwa kuihifadhi na kuilinda Katiba ya JMT ya 1977
(2005) kwa kuacha “ivunjwe” huku yeye akiangalia mambo yaende kama yalivyo!


Nadhani, kwa jinsi mimi nionavyo, huku ni kufeli kwa jinsi yake kwa kingozi
mwenye dhamana ya ulinzi na uhifadhi wa Katiba ya JMT ya 1977 (2005) kuacha
katiba aliyoapa “kuilinda” na kuihifadhi” ikivunjwa mbele ya macho ya wananchi
na uongozi wa kisiasa! Sipati maelezo ya kufafanua kwa nini hatua za makusudi na
za kiutendaji hazikuchukuliwa juu ya uvunjifu wa sheria mama.

Hata kama dhamira ya kuvunjwa kwa katiba ilikuwa nzuri na yenye ujenzi wa
mujtamaa na mustakabali murua wa uendeshwaji wa siasa; kulikuwa na sababu ya
matumizi ya hekima na busara ya uongozi katika kufikia muafaka kwa mizani ya
uhuru, haki na usawa.

Pamoja na kupongeza maafikiano ya kuleta “utulivu wa kisiasa” visiwani (Pemba
na Unguja) kufuatia kuundwa kwa Serikali ya Umoja wa Kitaifa (SUK) baina ya CCM
na CUF kulikuwa na haja na ulazima wa kufikiria utashi wa kisheria juu ya
mustakabali huo kwa mtazamo wa Katiba ya JMT ya 1977 (2005) kwa kuzingatia
marekebisho makubwa yaliyofanywa kwenye Katiba ya Zanzibar ya 1984. Kwa ujumla,
marekebisho ya Katiba ya Zanzibar ya 1984 yamevunja Katiba ya JMT ya 1977 (2005)
na kwa vyovyote vile hakuna hoja inayoweza kuchukuliwa dhidi yake.

Kuna masuala mawili ya kuhoji hapa; na lazima majibu yake yatapelekea kwenye
usiri mkubwa wa “dharau” na “ ubabe” ndani ya muafaka wa muungano!
Jakaya Mrisho Kikwete, kama Rais wa Awamu ya Nne, aliwahi kutoa ahadi ya
“kuushughuikia mgogoro wa kisiasa baina ya CCM na CUF Zanzibar.” Hata hivyo,
Kikao cha CCM cha Butiama ambacho ujumbe wa Zanzibar ulihudhuria ukiongozwa na
aliyekuwa Rais wa Zanzibar (2000 hadi 2010) Abeid Aman Karume ulidai kwamba
“Zanzibar hakuna mgogoro.”


Hadi pale wawili (Aman Abeid Karume na Seif Sharif Hamad) walipokutana na
kukubaliana “muafaka wa wawili.” Makubaliano ya Maalim Seif Sharif Hamad na Aman
Abeid Karume ndiyo yaliyozaa mabadiliko ya Katiba ya Zanzibar ya 1984 na kuundwa
kwa SUK baada ya Uchaguzi Mkuu, Oktoba 2010.

Katiba ya JMT ya 1977 (2005) imevunjwa! Tazama Ibara ya 105 ilivyovurugwa na
kuchezewa! Hivi, Rais wa Nchi (JMT) ambaye ndiye mlinzi na mhifadhi wa katiba
hiyo hajui hili?

Na kwa nini hasa iwe kwake juu ya uvunjifu huu na yeye (kama Amiri Jeshi
Mkuu) mwenye mamlaka ya kulinda JMT amemezwa na SUK? Au tuseme, Zanzibar inaweza
kufanya vyovyote itakavyo kwa maslahi yake bila kufuata utaratibu wa sheria
zilizokubaliwa?

Kulikuwa na ugumu na au uzito gani kubadilishwa Ibara 105 ili kutoa nafasi
kwa Zanzibar (kama nchi) kufanya mambo yake bila songombingo la kikatiba?

Ukiachilia mbali kuvunjwa kwa Ibara ya 105 ambayo kuvunjwa kwake ndiko
kulikowezesha kuundwa kwa SUK kulikoshadidiwa na mabadiliko ya kumi ya Katiba ya
Zanzibar ya 1984; kuna uvunjwaji mkubwa wa Katiba ya JMT ya 1977 (2005) ambao
ndio msingi wa maisha ya wananchi wa Tanzania.

Kwa ujumla, kama tulivyosawiri na kuona kwenye nukta ya kwanza, ya pili, ya
tatu hadi ya saba juu ya kukwama kwa Rais Kikwete kwenye uongozi jumla;
menejimenti ya siasa, uchumi na jamii; kushindwa vita dhidi ya ufisadi; na
kushindwa kuilinda na kuihifadhi Katiba ya JMT ya 1977 (2005) kuna kushindwa
kustawisha hali za maisha ya wananchi.

Huku ni kushindwa kukubwa kwenye nchi inayotegemea uongozi wa kisiasa kama
Tanzania. Kwa ujumla na kwa msisitizo wake, Ibara ya 8(1) (b) inabainisha wazi
kwamba, “lengo kuu la serikali litakuwa ustawi wa wananchi.”

CCM, kama chama kinachoongoza serikali na Rais Kikwete akiwa mwenyekiti wake
wa taifa, kimeshindwa kutoa malengo, kutekeleza, kusimamia malengo, na kupima
matokeo ya utekelezaji wa malengo ya kiuchumi katika kuboresha hali za maisha ya
wananchi.

Ustawi wa wananchi wa Tanzania kiuchumi umedorora kwa kiasi kikubwa; na hali
ya uchumi na mapato ya wananchi wengi wa Tanzania ni dhaifu na taabani!

Maisha ya wananchi wengi wa mijini na vijijini yamekuwa ya kuishi kwa
utegemezi wa kilimo cha kujikimu ambacho hakina tija kubwa na au hata mazao
yanapokuwa ya kutosha uwezo wa miundombinu haukidhi mahitaji jumla ya wakulima.

Upande wa wafanyakazi wa kada za kawaida na wale wa kada za chini wamekuwa
wakiishi kwa kutegemea ujira wa mshahara ambao hauwezi kukidhi hata bajeti
(makadirio ya matumizi) ya siku kumi za mwezi!

Kwa ujumla, hali ya ustawi wa maisha ya wananchi wa Tanzania kwa asilimia
zaidi ya 70 ni mbaya na hairidhishi. Rais Jakaya Mrisho Kikwete kwa hili
amefeli; na zaidi amevunja katiba ambayo ameapa kuilinda na kuihifadhi.

Mwisho(saba)

, nadhani wakati umefika kwa hatua za makusudi na za kimkakati
kuchukuliwa katika kurekebisha hali hii ya kushindwa kwa uongozi na menejimenti
ya nchi katika kufikia utashi wa wananchi. Ustawi wa wananchi ndio jukumu la
kwanza kwa serikali yoyote duniani na kwa jinsi yoyote iwayo, hakuna serikali
inayoweza kubaki kwenye mamlaka ya kuongoza watu kama inavunja misingi ya
utawala, uongozi na menejimenti ya uhuru, haki na usawa kwa uadilifu na insafu
ya kuongoza.

Ni ukweli usiopingika kwamba, “uongozi unahitaji akili, uwezo wa maarifa,
ustadi wa kuongoza, na maadili ya kuongoza.” Si kila anayetafuta uongozi anaweza
kuwa kiongozi mweledi; ni vema na haki kwa muungwana kusema nimefeli! Na kwa
jinsi hii, JK amefeli mara saba kwa mpigo!
 
ungefupisha maneno tusome wengi. sina comment sijamaliza kusoma ninachoona tu ni kama una chuki binafsi na Jk au uko chama cha upinzani au mwanaharakati
 
huna jipya ni yale yale na kibwagizo kilele na waimbaji walewale. aliyekutuma mwambie angoje hadi 2015 atapata maumivu makali moyoni kama hataki kukubaliana na hali halisi kwamba Jk ndiye Rais wake ama kama alimpa kura au hakumpa kura.
 
umepotea njia Jk ndiye Rais wako utake usitake huna jinsi ni kumpa tu ushirikiano ili nchi yetu isonge mbele.
 
ni kama umetumwa na yule aliyeshindwa kupata Urais mwaka 2010 na mkaapa kwamba nchi haitatawalika kweli tunaona kazi yenu.
 
Aibu!
Kuna mtu aliuliza swali hivi hakuna watu wa TISS wanaoitakia mema nchi hii?

wewe mwenyewe ni TISS kwa ajili ya ulinzi wa nchi yako ukisubiri TISS walioajiriwa rasmi kuna siku utajuta pale utakapokuwa umeuzwa kwa senti tano. Ulinzi wa nchi ni wa kila mmoja wetu.
 
natamani kukuchapa viboko 12 ukamwonyeshe yule unayelala naye kitanda kimoja. Ukamwambie umepigwa kwa sababu ya kejeri zako kwa mkuu wa nchi. waliokutuma wanaitamani Ikulu kawaambie watabweka sana Jk ndiye huyo Rais wao.
 
Nidhani kakwama kwenye safari zake baada ya kuishiwa mafuta kumbe.......
 
umepotea njia Jk ndiye Rais wako utake usitake huna jinsi ni kumpa tu ushirikiano ili nchi yetu isonge mbele.

Ni kweli JK ni Rais wa TZ lakini madhaifu yake lazima yasemwe. Mimi naona amebaki Rais wa kuhani misiba na kutoa pole. hata kwa watu chini ili jamii imuone yuko karibu na wananchi. kiuchumi ni 0
 
Hii ndiyo shida ya kununuliwa kwa vijisenti na watu ambao kifikra wamejichokea baada ya kukosa Urais kwa kipindi kirefu. Aiseee, hata mpangilio wako hauna mashiko... Ungempa kwanza aliyekutuma afanye editing!
 
Huku mwisho umerudia saba mara mbili au ulimaanisha nane? Lakini pia uliyoyaandika mwishoni yapo mwanzoni... Umeniharibia siku kabisa! Argh!
 
Back
Top Bottom