DC kwenye maombi na waganga wafukua uchawi

kilimasera

JF-Expert Member
Dec 2, 2009
3,068
268
MKUU wa Wilaya ya Mbozi mkoani hapa, Gabriel Kimolo ameshiriki katika maombi ya kukemea uchawi katika shule ya msingi ya kijiji cha Chindi, huku waganga wajadi walioalikwa kwa kazi hiyo, wakichimbua uchawi uliofukiwa shuleni hapo.

Kiongozi huyo alilazimika kushiriki katika maombi hayo huku waganga wa jadi nao wakitumia utaalamu wao, baada ya walimu wa shule hiyo kuacha kazi kutokana na madai ya kulogwa.

Baada ya kumalizika kwa maombi hayo na kazi ya waganga, Kimolo ambaye alihudhuria maombi hayo akiwa na Mkurugenzi wa Halmashauri ya Wilaya ya Mbozi, Levison Chilewa na viongozi wa dini, alitoa mwito kwa walimu hao kurejea kwa kuwa hawatalogwa tena.

Wakati maombezi yakiendelea shuleni hapo, waganga hao walikuwa wakichimbua vitu ambavyo vinadaiwa kutumika kuwaloga na kuwatesa walimu hao ambavyo ni pamoja na
tunguri dawa zilizofukiwa katika maeneo ya shule hiyo.

“Shule zitakapofunguliwa Jumatatu ijayo, naomba walimu wote 12 warudi na kuanza kazi, isipokuwa mwalimu mmoja aliyetajwa kushiriki mchezo mchafu wa kuwasumbua watumishi wetu, huyo tutamuondoa,” alisema Kimolo.

Hata hivyo Kimolo hakufafanua wapi atapelekwa mwalimu aliyetajwa hadharani kuwaloga wenzake na kusababisha adha katika shule hiyo, wananchi na serikali.

Lakini Chilewa alisisitiza kuwa mwalimu huyo hatarejea kufanya kazi shuleni hapo, ila kuna
utaratibu unafanyika wa kumhamishia mahala pengine.

Wiki iliyopita kiongozi wa mila wa wanyamwanga, Chifu Chipwasi Mkoma wa sita, aliwataja hadharani watu watatu akiwemo mwalimu aliyefundisha muda mrefu shuleni hapo (majina yanahifadhiwa) kuhusika na vitendo vilivyosababisha walimu hao kuacha kazi kwa hofu ya usalama wa maisha yao.

Chifu huyo kwa mamlaka aliyonayo, alitoa tamko maalum mbele ya Kamati ya Ulinzi na Usalama ya Wilaya ya Mbozi na mkusanyiko wa wananchi kwamba hali ya usalama wa anga katika eneo hilo itakuwa salama salimini.
 
Back
Top Bottom