nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
Na Danson Kaijage, Dodoma
CHAMA cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), kimesema kuwa kitasimamia uasi dhidi ya sheria mbovu zinazowalinda marais wabovu wastaafu, ambao wameliingiza taifa katika matatizo makubwa ya kiuchumi.
Msimamo huo ulitangazwa jana na Mwenyekiti wa taifa wa chama hicho, Freeman Mbowe, mjini hapa katika mkutano wa hadhara uliofanyika viwanja vya barafu kuwatambulisha wabunge wapya, Cecilia Pareso na Joshua Nassari.
Mbowe alisema sheria za kuwawekea kinga viongozi wa juu ambao wameshika madaraka ngazi ya juu ni mbovu na inasikitisha kuona serikali inatumia fedha nyingi za maendeleo kwa ajili ya kuwatunza watumishi wa ngazi ya juu ambao waliitia nchi hasara.
"Wapo viongozi ambao walitumia vibaya mali ya nchi lakini kutokana na kuwekewa kinga ya kutoshitakiwa bado wanaendelea kulipwa fedha nyingi pamoja na huduma mbalimbali kwa kutumia fedha za walipa kodi ambazo zingeweza kuwasaidia Watanzania katika masuala ya afya na elimu," alisema Mbowe.
Pamoja na kueleza nia hiyo, CHADEMA kimesema kitafanya maandamano makubwa jijini Mwanza mara baada ya kumalizika kwa kikao hiki cha Bunge, kupinga vitendo vya polisi mkoani humo kutetea uhalifu kwa kushuhudia kipigo cha wabunge wake wawili bila kufanya lolote.
"Tutakwenda Mwanza pamoja na wabunge wote wa CHADEMA na tutaandamana hadi kieleweke, tunataka kujua polisi wamepata wapi jeuri hii ya kutetea uhalifu," alisema Mbowe.
Akizungumzia suala la hatima ya aliyekuwa Mbunge wa Arusha Mjini, Godbless Lema, Mbowe alisema chama hicho tayari kimekata rufaa katika Mahakama ya Rufaa.
"Mazingira yaliyotumika kutengua ubunge wa Lema ni tatanishi. CHADEMA tunajua haki haiombwi, tumekata rufaa, tuna imani jopo la majaji litatoa uamuzi wa haki.
"Hata hivyo hatuogopi kurudi kwenye uchaguzi, tupo tayari, kwa sasa. Kamanda Lema anatembea mikoa yote kuwaeleza Watanzania kilichotokea na tumempa helikopita," alisema Mbowe.
Aliwataka wananchi wa Dodoma kuacha woga na kupigania mabadiliko ya kisiasa.
"Shughuli hii ni vita, hamuwezi mkaleta mabadiliko wakati mnaogopa polisi. Dodoma mmejaa woga…nawapongeza vijana wa UDOM, lakini Wagogo bado mmelala, nadhani mnajivunia mbunge mashuhuri mwenye misamiati ya matusi.
"Dodoma mnasubiri nini? Kuna vijana wengi, tukiitisha maandamano nani atatoka? Mniwie radhi kwa kauli hii. Tumezunguka nchi nzima maeneo mengine wamekuwa majasiri na ushindi umepatikana, nanyi mnapaswa kuamka," alisema.
Mbunge wa Kigoma Kaskazini, Zitto Kabwe, amesema siku za Chama Cha Mapinduzi (CCM) kukaa madarakani zinahesabika kutokana na wananchi kukichoka.
Alisema jambo hilo limedhihirika hivi karibuni katika uchaguzi mdogo wa Jimbo la Arumeru Mashariki ambako chama hicho kilitumia nguvu kubwa, lakini wananchi wamekikataa.
"Arumeru ni kielelezo kuwa Watanzania wamekichoka, pamoja na kutumia fedha nyingi na vigogo wao, lakini wananchi wamewakataa," alisema na kuongeza kuwa huo ni ujumbe ambao watawala wanapaswa kuupata.
Mbunge wa Musoma Mjini, Vincent Nyerere, alisema ingawa si mtabiri lakini anajua kuwa mwisho wa CCM kushika hatamu ni pale Mkurugenzi wa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (NEC) atakapotangaza uboreshaji wa daftari la kudumu la wapiga kura.
Alisema ingawa Arumeru CCM walitumia watu wazito pamoja na kutoa mkwara, lakini hawajaweza kuwahadaa wananchi hao na hatimaye kuipa ushindi CHADEMA.
Mbunge wa Ubungo, John Mnyika, alisema chama hicho hakipo tayari ‘kuuziwa' na Rais Kikwete wajumbe wa katiba kwenye ‘gunia' na ndiyo maana wanaendelea kuchambua wasifu wa kila mjumbe historia yake, uwezo wake, uadilifu wake na iwapo wamependekezwa kweli kama kipaumbele na makundi ya jamii.
Aliwataka wananchi wa Dodoma na maeneo mengine nchini kuendelea kuwaunga mkono kwenye azima ya kutaka sheria ifanyiwe marekebisho mengine kuhusu Bunge Maalumu la Katiba na mfumo wa kura za maoni.
"CHADEMA hatutakubali kura za maoni zisimamiwe na tume ya wachakachuaji wa uchaguzi, ambayo imekuwa ikilalamikiwa na wananchi na wadau wengine," alisema.
Aidha, aliwataka wanachuo na Watanzania kwa ujumla kuzingatia kuwa serikali imepeleka bungeni muswada wa sheria ya marekebisho mbalimbali ukiwa ndani yake una marekebisho ya sheria ya Bodi ya Mikopo yenye kukandamiza zaidi haki za elimu ya juu hususan kwa vijana kutoka kwa Watanzania wa kipato cha chini.
Kwa upande wake, Mbunge wa Mpanda Mjini, Said Arfi, mbali na kuwahimiza vijana kujiandikisha katika daftari la kudumu muda utakapowadia, pia amewataka wawe na tabia ya kupiga kura kuchagua viongozi wanaowataka, kwani kwa kuacha wanaendelea kuipa nguvu CCM.
Naye Mkurugenzi wa masuala ya Bunge wa chama hicho, John Mrema, alimtaka Profesa Shaban Mlacha wa Chuo Kikuu cha Dodoma kuacha kuwanyanyasa wanafunzi wa chuo hicho ambao ni wanachama wa chama hicho.
Alisema kamwe chama hicho hakitakaa kimya wakati wanafunzi wa chuo hicho wananyanyasika kwa sababu za kisiasa.