Babu mwenye watoto 80, wake 8, awajengea shule

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,013
Babu mwenye watoto 80, wake 8, awajengea shule

2007-12-24 10:30:52
Na Amina Mollel, Arusha

Meshuko Mapi (80), maarufu kama mzee Laibon, mkazi wa kijiji cha Esilalei, Tarafa ya Makuyuni, Wilaya ya Monduli, mkoani Arusha ambaye ana wake wanane na watoto 80, ameamua kujenga shule yake binafsi ya msingi kwa ajili ya kuwasomesha watoto wake hao.

Hata hivyo, ameiomba serikali na mashirika mengine, kumpiga jeki kukamilisha ujenzi wa shule hiyo kwa kuwa pia itawachukua na watoto wa jamii nyingine wa Kimasai kijijini kwake.

Shule hiyo inatarajiwa kuanza kuwachukua wanafunzi mapema mwakani.

Bw. Mapi anaomba watu wamsaidie kukamilisha ujenzi wa madarasa mawili ambayo tayari ameanza kuyajenga.

Alitoa ombi hilo mwishoni mwa wiki baada ya kutembelewa na Nipashe kwa mahojiano maalum.

Alisema ameamua kujenga shule hiyo ili watoto wake wote waweze kupata elimu hasa kwa kuzingatia kuwa, jamii ya Kimasai wengi wao hawaithamini elimu.

``Ni kweli kwamba sisi Wamasai wengi wetu hatuthamini elimu na kwa kuwa nimezaa watoto wengi nahitaji pia wapate elimu ili kwanza wasaidie wadogo zao na pia wanisaidie na mimi pia hasa ukizingatia kuwa mimi sijasoma,`` alisema mzee Laibon.
Alisema kuwa, awali Waziri Mkuu, Bw. Edward Lowassa, alimsaidia Shilingi milioni moja.

Mzee Laibon anayesifika na kuheshimika na jamii ya Wamasai ambaye pia ni mganga wa jadi, alisema shule hiyo itakapo kamilika atawahimiza watoto wake wote wasome bila kuchagua jinsia na kwamba hata wale waliokwishaoa atawashauri pia wanapopata muda warudi darasani kuongeza elimu.

Aidha, aliongeza kuwa ingawa shule hiyo ameijenga yeye binafsi pia watoto wengine kutoka katika jamii ya wamasai wataruhusiwa kusoma.

Mzee Laibon alisema atawahimiza wamasai wenzake watilie mkazo elimu kwa watoto wao bila kuchagua jinsia hasa ukizingatia kuwa watoto wengi kutoka katika jamii hiyo na hasa wakike hawapati elimu kutokana na wazazi wao kuwaozesha katika umri mdogo.

Alisema changamoto kubwa inayomkabili sasa na kumuumiza kichwa ni jinsi ya kupata vitabu vya kufundishia pamoja na walimu watakaokuwa tayari kujitolea kuwafundisha watoto wake na watakao kuwa tayari kuishi kijijini hapo.

Alisema kwa sasa amepata walimu wawili ambao wamejitolea kuwafundisha watoto wake kutoka Shule ya Sekondari Makuyuni ambayo awali majengo yake yalitumika kama kituo cha jeshi ambacho kipo jirani na nyumbani kwake.

Aliwashukuru wasamaria wema wanaojitokeza kumsaidia na kumpa ushauri hasa Waziri Mkuu, Bw. Edward Lowassa, ambaye ndiye aliyeweka jiwe la msingi la ujenzi wa shule yake.

Wengine aliowashukuru ni Shule ya Msingi ya Manyara Range na raia mmoja wa Marekani ambaye alimtaja kwa jina moja la Bw. Karry kuwa amejitolea kuwalipa walimu hao Sh. 40,000 kama posho.

SOURCE: Nipashe
 
Back
Top Bottom