singidadodoma
JF-Expert Member
- Nov 11, 2013
- 4,394
- 1,536

Jaji Lubuva.
Tume ya Taifa ya Uchaguzi inapenda kuutaarifu Umma wa Watanzania kuwa Uchaguzi wa Ubunge katika Jimbo la Kijitoupele – Zanzibar utafanyika mnamo tarehe 20 Machi, 2016.
Uchaguzi wa Mbunge katika Jimbo la Kijitoupele – Zanzibar ni mojawapo ya Majimbo yaliyoahirisha kufanya Uchaguzi tarehe 25 Oktoba, 2015 kutokana na hitilafu kwenye Karatasi za Kura.
Aidha, Tume inapenda kuwataarifu Wananchi kuwa Watendaji (Msimamizi wa Uchaguzi na Wasimamizi Wasaidizi wa Uchaguzi) walioteuliwa kipindi cha Uchaguzi Mkuu wa 2015 ndio watakaosimamia na kufanya shughuli za Uchaguzi huo. Uchaguzi huo wa Ubunge katika Jimbo la Kijitoupele hautakuwa na kampeni na Wagombea walioteuliwa kushiriki Uchaguzi ulioahirishwa mwezi Oktoba, 2015 ndio watakaoshiriki Uchaguzi huu.
Vituo vilivyotumika katika Uchaguzi wa mwaka 2015 ndiyo vitakavyotumika. Vituo vitafunguliwa saa 1.00 asubuhi na kufungwa saa 10.00 jioni. Watakaoruhusiwa Kupiga Kura tarehe 20/3/2016 ni wale ambao wameandikishwa na majina yao yapo katika Daftari la Kudumu la Wapiga Kura la Kituo na waje na Kadi ya Mpiga Kura.
Imetolewa na,
Jaji (Mst.) Damian Z. Lubuva
TUME YA TAIFA YA UCHAGUZI
MWENYEKITI
26/01/2016