TWENDE TUKAPIME KABLA HATUJAOANA

Idd Ninga

JF-Expert Member
Nov 18, 2012
5,136
4,298
1)Nakutazama machoni,mtoto umeumbika
Mimi hoi taabani,kwa sifa unasifika
Tena hivi karibuni,ndoa yetu itafika
Twende kwanza tukapime,kabla hatujaoana.

2)Wewe ninakuamini,hilo linatambulika
Ili tuwe salimini,kupima twalazimika
Tofauti na zamani,magonjwa yaongezeka
Kwanza twene tukapime,kabla hatujaoana.

3)Majibu yetu moyoni,ni sisi tutayaweka
Tujitoe mashakani,sote tuje salimika
Hivi sasa duniani,mambo yamebadilika
Kwanza twende tukapime,kabla hatujaoana.

4)Waage kwenu nyumbani,wasije kukasirika
Uwaambie kwanini,afya enda chunguzika
Watakwelewa namini.tena watafurahika
Kwanza twende tukapime,kabla hatujaoana.

5)Tujiondoe shakani,shaka isije tufika
Tukawepo taabani,huku tunataabika
Tena nani nimwamini,ka si wewe malaika
Kwanza twende tukapime,kabla hatujaoana.

SHAIRI -TWENDE TUKAPIME
MTUNZI-idd Ninga wa Tengeru Arusha
+255624010160
iddyallyninga@gmail.com

 
Back
Top Bottom