Tanzania katika Soka la Kimataifa, Tunakosea Wapi?

Magehema

JF-Expert Member
Aug 11, 2008
428
27
Kwa wale wataalamu wa mapishi watakubaliana na mimi kwamba uzuri au utamu wa chakula unategemea kwa kiasi kikubwa utaalamu wa mpishi wa chakula husika na jinsi gani anavyotumia viungo husika kuandaa chakula.

Ni ukweli kwamba unga uliotokana na mahindi ya kusaga huweza kutumika kupikia ugali na unga huo huo huweza kutumika kupikia uji, ni suala la kipimo cha unga na uwiano wa maji ndilo litakaloamua kama kinachopikwa ni uji au ni ugali.

Mbali na mfano huo hapo juu, kwa upande mwingine mchele huweza kutumika kupikia wali na mchele huo huo huweza kutumika kupikia pilau, kinachotofautisha wali na pilau ni aina ya viungo vinavyotumika katika mapishi husika.

Lengo la makala haya sio kutoa mafunzo ya upishi bali ni kuonyesha ni kwa namna gani “kitu kamili” au “mfumo kamili” unavyoumbwa na mifumo midogo midogo katika hali ya kuhusiana, kuingiliana na kikubwa zaidi kutegemeana.

Kwa mfano wa pilau ili pilau liweze kuwa pilau ni lazima kwanza kabisa kuwepo na mchele, mbali na mchele ni lazima kuwepo na chumvi na viungo mbali mbali, maji ya kupikia, mafuta, jiko pamoja na mpishi mwenyewe, hivi vyote kwa pamoja ndio vinazalisha pilau.

Kwa upande mwingine tunaweza kujifunza katika mfano mwingine; sote tunafahamu kwamba kazi ya msingi ya polisi ni kulinda raia na mali zao, maana yake ni kwamba uwepo wa polisi kisheria unasababishwa na hofu kwamba miongoni mwetu kama raia tupo ambao tunaweza kutishia usalama wa raia wenzetu na mali zao, hivyo basi uwepo wa tishio hilo ndio uhalali wa uwepo wa polisi!

Kwa dhana hiyo hiyo ya kuwepo kwa tishio hilo ndio kunapelekea uwepo wa mahakama, kwa maana kwamba iwapo kutakuwa na wavunja amani ni jukumu la mahakama kuwashughulikia kwa mujibu wa sheria baada ya polisi kufanya kazi yao ya upelelezi na kuwafikisha watuhumiwa katika chombo hicho cha kutoa haki.

Mwendelezo huu wa kutegemeana unaweza kuishia katika ngazi ya mahakama iwapo chombo hicho cha kutoa haki kitaona mtuhumiwa hana hatia, hata hivyo katika mazingira tofauti na hayo nguvu ya mahakama inakuwa imeishia katika kutoa hukumu tu, hapo sasa ni jukumu la magereza kuchukua wajibu wake na kuhifadhi wafungwa kwa mujibu wa hukumu ya mahakama!

Kwa maana hiyo tunaona wazi kwamba mfumo wa utoaji haki kwa mujibu wa mfano hapo juu unategemea uwepo wa mtuhumiwa, polisi, mahakama na magereza, na kila chombo kitafanya kazi kwa mujibu wa sheria na mamlaka yake, iwapo kimojawapo kitakosekana kitapelekea vingine kukosa uhalali au kushindwa kufikia malengo.

Itakuwa ni vurugu tupu na kinyume cha sheria na huo mfumo hautaweza kufanya kazi mathalan magereza itakapoamua kutoa hukumu kwa watuhumiwa au polisi kujigeuza mahakama au mahakama kufanya kazi ya polisi ya kukamata watuhumiwa.

Vivyo hivyo kwa upande wa soka letu ili liweze kukua na kufikia pale ambapo kila mmoja wetu anatamani linahitaji ushirikiano na umoja wa wadau wote muhimu na kila mdau atimize wajibu wake bila kuingilia wajibu wa mdau mwingine.

Ni ukweli usiopingika kwamba kila mdau ana umuhimu wake katika kuendeleza soka lakini pia kuna wadau ambao ni muhimu zaidi ya wadau wengine na pia kuna wadau ambao inabidi wawe na majukumu na wajibu mkubwa zaidi ya wadau wengine.

Kwa mtazamo wangu wachezaji ni wadau wakubwa na wa kwanza kwa umuhimu na wajibu wa kipekee katika kukuza na kuinua kiwango cha mpira wetu, ni jukumu la wachezaji wetu kujitambua, kujithamini na kuona kwamba bila wao hakuna sababu yoyote na watu kwenda viwanjani au kuangalia mechi katika luninga.

Wachezaji bila makocha ni sawa na meli bila nahodha, kwa mantiki hiyo makocha wana mchango mkubwa sana katika kumlea na kumjenga mchezaji kwa mafunzo sahihi kwa lengo la kumwandaa ili kuweza kushindana na kupata mafanikio.

Wadau wengine kwa umuhimu ni serikali; ni jukumu la serikali kutunga sera zitakazosaidia kuboresha na kuinua soka na michezo yote kwa ujumla, ni wajibu wa serikali kuhakikisha viwanja vya wazi kwa ajili ya matumizi ya michezo vinalindwa na pia kupunguza kodi ya vifaa vya michezo ili watanzania wengi zaidi waweze kumudu kununua.

Mbali na hayo ni jukumu la serikali kuandaa mazingira ambayo shule zetu za msingi na sekondari zinakuwa na walimu wenye sifa za kufundisha michezo mashuleni kwa watoto wetu na ikibidi kutoa ruzuku kwa shule za binafsi zenye michepuo ya michezo.

Ukiachana na serikali wadau wengine muhimu katika kufanikisha azma ya kuinua soka letu ni shirikisho la soka Tanzania [TFF]; hapa nazungumzia uongozi wa soka, hawa ndio waratibu wakuu wa mpira katika nchi hii, ndio waasisi na wasimamizi wa utekelezaji wa dira na dhamira ya wapi tunataka kwenda katika soka la nchi yetu.

Kwa upande mwingine vilabu ni wadau muhimu katika kuifikia ndoto na dira ya TFF kwa sababu wao ndio wanaishi na wachezaji, kuwalea na kuandaa timu kwa ujumla.

Wadau wengine wenye nafasi kubwa ya kuendeleza soka letu ni vyombo vya habari; hivi ndio vinaamua ajenda ya kujadiliwa na jamii siku hadi siku, vyombo hivi vikitumika vizuri vinaweza kujenga na kusaidia kukua kwa soka letu, kwa upande mwingine vyombo hivyo vinaweza pia kutumika kubomoa soka letu!

Wadau wengine muhimu ni pamoja na waamuzi [marefa], wadhamini pamoja na wazazi/walezi wa wachezaji, sote tunafahamu kwamba marefa kazi yao ni kusimamia na kutafsiri sheria za soka, kwa upande mwingine wazazi wa wachezaji wana jukumu la msingi la kuwalea vijana wao katika suala la lishe na nidhamu, bila kuwasahau wadhamini ambao watasaidia kifedha!

Ukiangalia kwa makini wadau wote muhimu ambao wanahitajika kushirikiana ili soka letu likue wapo, swali la kujiuliza ni kwanini tumeshindwa kuuendeleza mpira wetu, je kila mdau anatimiza wajibu wake ipasavyo?

Tuanze na Serikali

Sote tunakubaliana kwamba soka linachezwa uwanjani, je kuna viwanja vingapi vya wazi ambavyo vilikuwa vinatumika kwa michezo sasa hivi vimegeuzwa matumizi na kuwa garage bubu au maghala; katika hilo hilo la viwanja ni shule ngapi za umma za msingi na sekondari zina viwanja vye michezo? Katika mazingira kama hayo tunategemea hao watoto wacheza wapi huo mpira?

Je kuna walimu wangapi wa michezo qualified katika shule zetu za umman za msingi na sekondari, na je kuna shule ngapi zenye vipindi na ratiba serious za michezo kama ilivyokuwa miaka 30 iliyopita?

Tuwaangalie wachezaji wetu

Je ni wachezaji wangapi wa Tanzania wanaocheza mpira leo ambao wamepata misingi na mafunzo sahihi ya soka katika umri sahihi?.

Je wachezaji wetu wanajielewa kwa kiasi gani, je ndoto walizonanzo katika soka zinawiana na uwekezaji, jitihadi, nidhamu na bidii ya wachezaji husika? Ni kweli kwamba kila mmoja wetu anatamani kufanikiwa lakini sio wote wanatimiza na kutekeleza kanuni muhimu za kufanikiwa!

Je maandalizi ya kimwili na kisaikolojia yanatoa fursa kwa wachezaji wetu kutoa ushindani nje ya mipaka yetu?

Je kuna role model ambaye anaweza kuwa hamasa na matamanio ya wachezaji wetu kutaka kufanikiwa katika soka?

Shirikisho la Soka/Uongozi wa Soka

Je TFF imeweza kuwa na ubunifu wa kutosha katika kusimamia mpira wa Tanzania?

Je TFF imetumiaje nafasi yake ili kuhakikisha vilabu vinakuwa na timu serious za vijana ukiachana na hizi za ujanja ujanja ambazo tumekuwa tukiziona.

Je TFF imekuwa ikiwekeza kwa kiasi gani katika timu za Taifa za vijana U17, U 23 nk?

Je TFF imekuwa ikijifunza nini kutoka kwenye FAs ambazo zimefanikiwa katika soka hasa kwa wenzetu ambao ambao kwa kiasi fulani mazingira yanafanana?

Je ligi zinazosimamiwa na TFF zina ubora na ushindani wa kutosha ambao mwisho wa siku wachezaji wanaoshiriki ligi hizo watakuwa wameandaliwa vya kutosha kushindana nje ya mipaka?

Vilabu vyetu vipi?

Je vilabu vyetu vinaendeshwa kwa weledi kwa maana ya kuandaa timu zetu [seniors na juniors], na kufanya uwekezaji wa miundo mbinu au tunategemea football fitina?

Je kauli za klabu zetu kuhusu dira na dhamira zao katika kuendeleza soka zinaendana na kuakisi matendo yao? Waingereza wanasema do they walk the talk?

Na vyombo vya habari je?

Je vyombo vya habari vinatimiza wajibu wake ipasavyo katika kujenga na kuinua soka au wamekuwa mstari wa mbele katika kubomoa soka letu?

Wazazi/walezi nao vipi?

Wachezaji wote waliopo wana wazazi au walezi wao, je nini mchango wao katika malezi ya kimwili na kisaikolojia kwa watoto wao? Tumekuwa na wachezaji wenye vipaji vya hali ya juu lakini wasiokuwa na nidhamu hata kidogo; umewahi kujiuliza wazazi au walezi walihusika kwa kiasi kufikia hali hiyo?

Tumewahi kujiuliza ni kwanini wachezaji wa kizazi hiki wana maumbo madogo madogo ukilinganisha na wale wa miaka 20 iliyopita? Je wazazi katika hilo wanahusikaje, je suala la lishe hapo lina nafasi yoyote?

Waamuzi wetu wewe unawaonaje?

Marefa ndio wanatafsiri sheria uwanjani na wao ndio wenye maamuzi ya mwisho kuhusu tafsiri ya sheria za soka uwanjani, je tunao waamuzi ambao wanakidhi mahitaji ya soka la karne ya 21?

Ni waamuzi wangapi wa Tanzania wana sifa na uwezo wa kuchezesha mashindano ya kimataifa kwa umakini?

Ni waamuzi wangapi ambao hutanguliza mahaba yao badala ya sheria wanapokuwa uwanjani? Tumewahi kujiuliza ni kwa kiasi maamuzi mabovu yanasababisha kudumaa kwa soka letu?

HITIMISHO

Kuna sababu nyingi sana zinazochangia kudumaa kwa soka letu, sababu hizo ni pamoja na wadau kutokutimiza wajibu wao ipasavyo, kuendesha mambo kwa mazoea na kutaka mafanikio ya haraka bila kufanya uwekezaji wa kutosha katika maeneo sahihi. Kwa mantiki hiyo suluhisho ni lazima liguse mfumo mzima wa uendeshaji wa soka letu, lazima wadau wote wanaohusika watimize wajibu wao na kuheshimu wajibu wa wadau wengine. Tukiendelea na mazoea ya kudhani tatizo la mpira wetu ni kocha tu au benchi la fundi tutakuwa tukifanya kazi ya kubadilisha makocha na benchi la ufundi na mwisho wa siku hakuna mabadiliko yoyote ya kimsingi yatakayopatikana! Tatizo letu ni la kimfumo kwa hiyo ni lazima ile mifumo midogo midogo inayounda mfumo kamili ifanyiwe kazi.


Alamsiki.
 
Hatuna sports academy za maana, kidongo chekundu ndo vile tena imekuwa academy ya kuuza sura
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom