Chachu Ombara
JF-Expert Member
- Dec 11, 2012
- 6,160
- 11,228
Vyombo vya usalama mkoani Tabora vimewakamata watu sita kwa tuhuma za kutoa rushwa ya fedha kwa baadhi ya watu wanaosadikiwa kuwa ni wajumbe wa uchaguzi wa kura za maoni za Chama Cha Mapinduzi (CCM), kuelekea uchaguzi wa wagombea wa madiwani na wabunge ndani ya chama hicho unaotarajiwa kufanyika Agosti 4, 2025.
Akizungumza na waandishi wa habari Agosti 3, 2025, Mkuu wa Mkoa wa Tabora Paulo Chacha amesema kuwa tukio hilo lilitokea usiku wa manane katika Wilaya ya Nzega, ambapo watuhumiwa walinaswa wakigawa fedha zinazokadiriwa kuwa zaidi ya shilingi milioni 16 ndani ya gari.
Watuhumiwa waliokamatwa wamemtaja mmoja wa wagombea wa ubunge katika jimbo la Nzega kama mhusika mkuu wa kutoa fedha hizo, ambaye kwa sasa ametoweka huku akiendelea kusakwa.
Ameongeza kuwa zaidi ya watu 40 wengine bado wanasakwa kwa tuhuma hizo huku akitoa wito kwa wagombea wote kujiepusha na vitendo vya rushwa, akisisitiza kuwa vyombo vya dola vimejipanga kushughulikia yeyote atakayekiuka sheria au taratibu za uchaguzi.
Katika Jimbo la Nzega, wagombea sita wa CCM wanachuana kuwania kuteuliwa kupeperusha bendera ya chama hicho katika Uchaguzi Mkuu wa Oktoba 2025.
Chanzo: Jambo Tv