Wandugu nimesoma makala haya kwenye tovuti ya Shirika la Habari Vijijini Tanzania
Shihata
Igunga na fumbo la imani vijijini
Na Mwandishi Wetu, Igunga
VUMBI, upepo na baridi ni mambo unayotakiwa kuyazoea uwapo katika Wilaya ya Igunga.
Jioni moja katikati ya Julai mwaka huu, nateremka kwenye basi nikitokea jijini Dar es Salaam. Ni miaka mingi sasa imepita sijakanyaga ardhi hii ya Igunga.
Hali hiyo inanifanya kuwa makini sana kujaribu kuangalia ramani ya kipindi kilichopita na uhalisia wa mambo kwa nyakati hizi.
Nipo hapa kwa kazi moja tu ya kusaka ukweli wa hisia za wananchi vijijini mara baada ya Rostam Azizi ambaye ni mwanachama wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), kutangaza kuacha ubunge na ujumbe wa Halmashauri Kuu ya chama hicho.
Naingia katika jimbo hili, nikiwa nimeshasoma magazeti na kusikiliza redio pamoja na kuona taarifa mbalimbali kupitia runinga zikihabarisha kuhusu Rostam na uamuzi wake wa kuuacha ubunge.
Ikasikika kwamba kuna wanachama kadhaa waliangua kilio na wengine kuzirai baada ya kupata taarifa ya Rostam kujiuzulu ubunge.
Maswali yanakuwa mengi kwenye kichwa changu. Natafakari wakati wa kupanda basi pale Ubungo jijini Dar es Salaam kwamba huyu Rostam hasa kafanya lipi kubwa kwa wanavijiji hawa wa Igunga? Nakuwa na shauku ya kufika ili nipate kuona kwa macho ya mwili.
Kwa vile nimeingia jioni sana, nafasi pekee kwa wakati huo ni kusaka sehemu ya kuweka ubavu usiku, mlo wa moto baada ya safari ndefu.
Macheo yako upenuni, naamua kufanya zoezi kwa kutembea walau nione huu mji ukoje. Nashangaa kuona kuwa mitaa ya Igunga imejaa vumbi. Hakuna lami labda uende Barabara Kuu iendayo Singida.
Nyumba nyingi ni za tembe na hata zile zilizoezekwa kwa bati ziko katika hali duni. Unaweza kuyaita magofu ukiweza. Lakini wapiga kura wamo ndani yake. Wanaishi!
Hapa ndipo alipoliliwa Rostam? Najiuliza na kujipa jibu kwamba huenda nina papara. Kwa hiyo navuta subira na kurejea kwenye loji ili nipate kifungua kinywa na baadaye namsaka mwenyeji kwa ajili ya kunidokeza mawili matatu.
Hii ndiyo hali halisi na wala hakuna Igunga nyingine
unachokiona ndicho kilichopo. Yaliyomo yamo, anasema kwa kejeli kijana ambaye alinisaidia kwa kiasi kikubwa kuifahamu wilaya hii.
Jua tayari liko utosini, nami nishaingia katika Kijiji cha Mbutu. Kuna vijana pale Mbutu mjini wanacheza pool. Hawa ni wa kisasa, hawana muda wa kuchunga ngombe wala punda. Lakini unapowagusia kuhusu maendeleo ya kijiji chao wanasema hatima yao kwa sasa imo mikononi mwao na si kwa wanasiasa.
Kwanini wanasema hivyo? Kubwa ni kwamba wamekata tamaa. Mbunge aliyejiuzulu ananyooshewa vidole kwamba kwa kiasi fulani kawatelekeza. Shule hazina madawati, walimu na vifaa vya kufundishia.
Mita kama 300 mbele kuna kibao kilichosemeka Shule ya Msingi Mgondamvelo iliyo chini ya Halmashauri ya Kijiji cha Mbutu, majengo si ya kuridhisha kama zilivyo shule nyingi wilayani humo.
Hatua chache kutoka hapo kuna nyumba ya tembe. Mafiga matatu yamezunguka moto unaolekea kuzimika. Hii ni dalili kwamba kuna kitu kimetoka kupikwa hapo.
Yupo mama wa makamo, namsogelea na kumsalimu. Lakini lugha zinapishana. Yeye anajibu kwa Kinyamwezi na ananiacha hoi. Shukrani zimwendee mwenyeji niliyeongozana naye, anajitolea kuwa mkalimani.
Mama huyo anaweka wazi kuwa kuwapo au kutokuwapo kwa Rostam, binafsi haoni faida yake.
Tumekuwa tukihamasishwa kumpigia kura kila wakati lakini hali ndiyo kama hii. Haya ndiyo maisha yangu. Ni taabu kila leo, anasema mama huyo ambaye hata hivyo anagoma kutaja majina yake.
La maana sasa waje wengine tuone watatuletea kitu gani. Lakini je, alimpigia kura ya ndiyo mbunge aliyejiuzulu? Hapana, anasema. Kura sikumpa hata hivyo kwa matokeo tunayoyaona hata wenzangu ambao hawakuniunga mkono wana nafasi ya kufanya uamuzi mwingine tofauti.
Ukiachana na mwanamama huyo, kwa ujumla jimbo sasa liko shakani.
Vijiwe vingi Igunga mjini vinazungumzia uchaguzi mdogo unaotarajiwa kufanyika. Vijana wanaonekana kutaka mabadiliko.
Hii ni kauli ya Jumanne Paul. Chadema wanaweza kuingia nasi tukawapa kura za ndiyo. CCM imeshatuburuza vya kutosha kuna ulazima wa mabadiliko.
Sisi tuko huku vijijini, tunataka huduma za jamii. Tunalima pamba na mazao mengine lakini usafiri ni mgumu wakati wa mavuno. Hii maana yake ni kwamba umasikini ni janga letu kila siku.
Rostam aliingia bunge kwa mara ya kwanza mwaka 1994 baada ya uchaguzi mdogo uliotokana na kifo cha aliyekuwa mbunge wa jimbo hilo, Charles Kabeho.
Katika miaka ya hivi karibuni, Rostam, Edward Lowassa na Andrew Chenge wamekuwa wakitajwa kuhusika na vitendo vya kifisadi.
Rostam alitangaza uamuzi wa kuachana na ubunge katika Ukumbi wa Sakao, uliopo mjini Igunga wakati akizungumza na wazee wa CCM wa jimbo hilo. Alisema atabaki kuwa mwanachama wa kawaida wa CCM.
Hakusita kusema pia kuwa uamuzi wake umetokana na wanasiasa uchwara wanaoendesha siasa za kupakana matope baada ya Mwenyekiti wa chama hicho taifa, Rais Jakaya Kikwete, kuleta kaulimbiu ya kujivua gamba.
Rekodi zilizopo ofisini kwake zinaonyesha kuwa miongoni mwa mafanikio yaliyofikiwa ni kuwapo kwa umeme na taa barabarani, mfuko wa afya ya jamii kwa kila kaya, zahanati kila kijiji na shule nyingi kuliko idadi ya kata zilizomo kwenye wilaya.
Rostam ambaye ni msomi anayeshikilia shahada ya uchumi amekuwa mbunge wa jimbo hilo kwa miaka 18.
Ameondoka bungeni huku wananchi wake wengi wakiwa katika lindi la umasikini.