Kanungila Karim
JF-Expert Member
- Apr 29, 2016
- 20,746
- 25,638
USIKU WA JANUARI 20, 2005
SIMULIZI YA KWELI
INNOCENT A. NDAYANSE
KUNA MATUKIO MBALIMBALI YA KUFURAHISHA, KUSIKITISHA NA HATA YA KUTISHA YATOKEAYO KILA SIKU DUNIANI. KATIKA SIMULIZI HII NINAKULETEA MTIRIRIKO WA TUKIO HALISI LILILONIKUTA MWANZONI MWA MWAKA 2005 NA KUZUA TAHARUKI KATIKA JAMII YA ENEO NILILOKUWA NIKIISHI.
NI TUKIO LILILOIBUA MASWALI MENGI NA HISIA TOFAUTI KWA WAKAZI WA ENEO HILO NA HATA WALE WALIOKUWA WAKIISHI MAENEO MENGINE, KILA MMOJA KWA UPEO WAKE WA KUFIKIRI.
SIMULIZI HII NI YA KWELI KWA ASILIMIA MIA MOJA, TOFAUTI KABISA NA HADITHI NYINGINE ZILIZOTANGULIA NA ZITAKAZOTUJIA SIKU ZA USONI.
TIRIRIKA NAYO…
* * ***
HUDAIWA kuwa kila mtu huwa na jambo ambalo nafsi yake imejikita zaidi. Hupenda sana kulifanya jambo hilo hata kama itamlazimu kutumia gharama za ziada.
Kuna anayependa kukaa vijiweni na kupiga stori. Mwingine ni mpenzi wa kunywa pombe. Mwingine hupendelea sana kutazama televisheni. Yupo aliyebobea katika michezo ya kamari. Na yupo ambaye yeye akili yake yote ni kwenye uhusiano wa mapenzi, leo yuko na huyu, kesho yuko na yule.
Ndiyo, kila mmoja ana kile ambacho roho yake hukipenda na huwa tayari hata kuvuruga bajeti yake na kubadili ratiba zake za siku ili tu airidhishe nafsi yake.
Mimi nilitokea kupenda kupiga gitaa tangu nikiwa na umri wa miaka 14. Niliipenda fani hiyo kwa kuwa nilikuwa siachani na kaka yangu ambaye tulikuwa tukipendana sana tangu utotoni kabisa. Aliitwa Barack Ambrosse Ndayanse.
Barack alikuwa mpenzi zaidi wa gitaa, labda zaidi yangu na alikuwa akipiga na rafikiye kipenzi, Ramadhani Zahoro ‘Bangwe’, wakitoroka darasani na kwenda kujificha kwenye shamba la mihogo na kuanza kupiga gitaa lililotengenezwa kwa zana hafifu za galoni.
Wakati huo tulikuwa tukiishi kitongoji cha Bangwe, mjini Kigoma. Kwa kuwa mara kwa mara nilikuwa nashinda naye, nilishawishika na mimi kujifunza kutekenya nyuzi za gitaa hilo la kiasili.
Mwanzoni mwa mwaka 1978, tukajiunga kwenye kwaya ya Kanisa la Anglikana Mwanga mjini Kigoma, usharika wetu na ambao baba yetu mzazi alikuwa Shemasi kanisani hapo.
Katika kipindi hichohicho, wakaja wanamuziki wawili kutoka katika kwaya iliyokuwa ikitikisa ukanda wa Afrika Mashariki, Mwanza Town Choir. Wanamuziki hao walikuwa wamekuja mjini Kigoma kwa ajira za Upanuzi wa Bandari na hivyo wakaamua kuwa wanakuja kanisani hapo kupiga magitaa.
Ni hapo ndipo mimi na Barack tulipogundua kuwa viwango vyetu vilikuwa duni sana na kuanza kujifunza kwa hao vijana waliotoka Mwanza.
Tuliendelea na fani hiyo na baada ya miaka mitatu tulikuwa katika viwango vilivyokubalika kwa wapenzi wengi wa muziki. Nakumbuka kuwa tulikuwa wepesi wa kusikiliza nyimbo zilizokuwa zikitamba miaka ile.
Baadhi ya nyimbo hizo ni Nyako Konya (Orchestre Mangelepa), Memi, Moni Afinda (Orchestra Kiam), Mikolo Mileki Mingi (Orchestre Veve) na nyingine nyingi za Kikongo.
Nyimbo za Tanzania, Usia wa Baba, Mwanameka na Betty za Dar International pia zilikuwa zikituteka kwa kiasi kikubwa. Kusikiliza sana nyimbo hizo kulikwenda sambamba na uigaji ili tuweze kupiga hatua.
Mara nyingi nilikuwa nikimsikia kaka yangu akisema, “Kama wao wameweza kwa nini sisi tusiweze?”
Mwaka 1985 tukawa tumekomaa zaidi, Baraki akiwa imara kwenye upigaji wa gitaa zito la besi na rythm ilhali mimi nikikomaa zaidi katika gitaa la solo kiasi cha kujikuta tukianza kupiga katika bendi moja iliyokuwa mjini hapo ya Super Kibisa Orchestra tukiwa na Ramadhani Zahoro ‘Bangwe.’
Hata hivyo, baadaye Ramadhani aliondoka Kigoma na kulivaa Jiji la Dar es Salaam, mimi na Barack na wanamuziki wengine tukabaki tukiliendeleza ‘sebene’ kwenye bendi hiyo na wakati huohuo pia tukiupiga muziki kwenye kwaya ya kanisa. Kwa sasa Ramadhani Zahoro ‘Bangwe’ ni mpigaji gitaa tegemeo wa Msondo Ngoma Music Band ya Dar es Salaam.
Kuanzia mwaka 1990, kasi ya kupiga muziki ikanipungukia kutokana na wingi wa majukumu. Miaka miwili baadaye nikaamua kubadili mazingira. Nikahamia jijini Dar es Salaam na nikawa napiga gitaa mara chache pale nilipoliona na nilipokuwa na nafasi ya kufanya hivyo.
Siku zikaenda, hatimaye nikajiunga na Kwaya ya Amkeni KKKT Usharika wa Kinondoni mwaka 1996. Hapo sikudumu sana kwa sababu zilezile za kubanwa na majukumu.
Mwaka 1997 mwishoni nikajiunga na Kwaya ya Vijana na Uinjilisti Hananasif Kinondoni, kwa maombi ya mwalimu mmoja aliyewahi kuniona nikipiga gitaa kule Usharika wa Kinondoni KKKT.
Hapa Hananasif nimekaa sana na kwa kuwa ndipo yalipokuwa masikani yangu nikajikuta nikirudi kwenye fani kwa kasi ya ajabu.
Mapenzi yangu kwa mpiga solo mahiri wa enzi za miaka ya 90, Alain Makaba wa Wenge BCBG yakairudisha ile ari yangu ya kupiga gitaa na hasa kwa kipindi kile Wenge walipoibua albamu ya Pentagone mwaka 1994.
Sasa nikarudi kwenye gitaa kwa nguvu kubwa. Kila wimbo uliopigwa na Alain Makaba nikawa nauiga kwa kiasi kikubwa. Kiwango kikapanda.
Mwishoni mwa miaka ya 1990, bendi ya African Stars ‘Twanga Pepeta’ ikazaliwa. Nakumbuka bendi hiyo ilikuwa inapiga muziki wake kwenye viwanja wa Leaders Club bureee! Kila Jumapili mchana!
Watu tukawa tunajimwaga hapo kila wikiendi na hasa kwa kuzingatia kwangu mimi pale palikuwa ni jirani sana na nyumbani. Mpangilio mzuri wa muziki wa Twanga, sanjari na upigaji wa Adolf Mbinga katika gitaa la solo vilinivuta sana na hivyo sasa nikawa nikibuni vyangu, nachanganya na vionjo vya ama gwiji Alain Makaba au mzalendo Adolf Mbinga hasa na wimbo wake wa ‘Kisa Cha Mpemba.’
Nikaendelea kuwa bora katika fani hiyo huku pia nikifanya kazi ya ajira katika Kampuni ya Uchapishaji Vitabu ya HEKO.
USIKU JANUARI 20, 2005
HII ilikuwa ni siku, kama siku nyingine ambazo niliamka na kwenda kwenye shughuli zangu za kila siku. Kwa siku hii nilizungukia mitaa ya katikati ya jiji ambako nilikuwa nafuatilia oda ya biashara kwa wafanyabiashara wakubwa wa maduka ya vitabu.
Ilipofika jioni, kitu kama saa 11 hivi nikawa nimesharudi Kinondoni na moja kwa moja nikaelekea kanisani kwa ajili ya mazoezi ya kwaya. Mazoezi yalimalizika saa moja usiku. Kijigiza kilikuwa kimekwishaitawala anga.
Baada ya mazoezi nilitoka na rafiki yangu, Kimambo aliyekuwa akiishi Kinondoni Shamba. Nilikuwa nikimsindikiza na tulikuwa na mazoea ya kuzungumza hili na lile hususan kuhusu kwaya kila tumalizapo mazoezi.
Siku hiyo, mara tulipomaliza mazoezi nilichoropoka hadi nyumbani ambako hakukuwa mbali. Nikavua viatu na kuvaa kandambili kwa kuwa siku hiyo sikuwa natarajia kwenda mbali.
Nikarudi eneo la kanisa ambako nilimkuta Kimambo akiwa nje ya uzio akizungumza na wanakwaya wengine huku akinisubiri.
Kabla hatujaondoka akaja rafiki yangu mwingine wa ‘kufa na kuzikana,’ Willy. William Jacob Kalumila. Huyu alikuwa ni mwalimu wa kwaya na nilizoeana naye kwa kiasi kikubwa na kuwa marafiki wa karibu zaidi kwa kuwa alikuwa akifundisha nyimbo zenye mwelekeo nilioupenda.
“Kocha vipi, tupandishe Mkwajuni?” Willy aliniambia.
Kwa kuwa tayari Kimambo alikuwa amenisubiri kwa muda mrefu, nikaona haitakuwa vizuri kumwacha na kuambatana na Willy. Kimambo angeona nimemdharau. Hivyo, kwa ustaarabu nikamjibu Willy, “Hapana kocha. Leo ngoja nimpe tafu mzee wa Kinondoni Shamba.”
Willy hakujali, tukaagana.
Mara tu nilipofika Kimambo alisitisha maongezi na kuniambia, “Inno, twen’zetu.”
Tukaondoka taratibu, tukipiga stori kuhusu mazoezi ya siku hiyo. Tukapita jirani na Shule ya Msingi Hananasif katika eneo lililokuwa na miti mingi iliyoongeza nguvu ya giza kwa kuwa hakukuwa na nyumba zilizokuwa kando ya barabara.
Tukawa tunapita Mtaa wa Ngano, mtaa uliokuwa umepandwa miti mingi iliyounda kivuli kizito mchana na kutengeneza giza la kuogofya usiku.
Mazingira yale tulikwishayazoea, hivyo hatukuwa na wasiwasi wowote. Tukawa tukitembea taratibu huku tukizungumza.
Hatimaye tuliuacha Mtaa wa Ngano, tukashika Mtaa wa Wakulima.
Mbele kidogo tukawa tunapita katikati ya makaburi. Tulipofika mwisho wa eneo la makaburi, tukawa kando ya Barabara ya Kinondoni, eneo lililojulikana na linalojulikana mpaka sasa kwa jina la MWEMBEJINI.
Hapo tulikuta mchanganyiko wa watu. Walikuwepo waliokuwa kituoni wakisubiri daladala na wengine kwa harakaharaka unaweza kuwaita ‘vibaka’ au ‘mateja’ kwani walikuwa ni vijana wanne wakizunguka-zunguka tu kituoni hapo huku wakizungumza kwa sauti zenye mikwaruzo inayokera, sigara na bangi zikivutwa bila ya wasiwasi.
Mimi na Kimambo hatukuwajali kama ambavyo nao hawakutujali. Mara kwa mara watu wa aina ile huwa eneo lile wakivizia daladala lililojaa ili waingie na kubanana na abiria na matokeo yake abiria ‘hulizwa.’ Au huvizia abiria atakayeteremka na kuzubaa-zubaa na wao huwa wepesi kwa kumpora chochote chenye manufaa kwao.
Magari mengi yalikuwa yakipita barabarani muda huo yakitokea katikati ya jiji hivyo ikatulazimu kusubiri. Mara daladala kutokea mjini likafika. Lilikuwa limejaa pomoni. Ile kusimama tu vijana wale nao wakasogea mlangoni kama abiria wa kawaida. Konda alipoteremka na kuwapisha abiria wateremke, vijana hawa waliokuwa chini wakawa wamesogea zaidi mlangoni.
Ndipo kilipotokea kituko. Mwanamume mmoja ambaye alikuwa amevaa nadhifu alipoteremka na kuanza kuvuta hatua akija upande huu wa Barabara ya Wakulima, alifuatwa na vijana wawili na haraka mmoja akampiga ngwara, jamaa akaenda chini kama gunia la mashudu tii!
Kabla hajajitetea, mikono ya vibaka wale ikawa imekwishatalii mifukoni mwake na kutoka na pesa na simu kisha hao wakakimbilia makaburini.
Yule jamaa aliyevamiwa alichanganyikiwa. Tukamsogelea na kumnyanyua. Tukamsihi aende tu nyumbani kwa kuwa vibaka wale wameshatokomea. Akaondoka huku akiilalamikia simu yake aliyodai kuwa kainunua siku tatu zilizopita kwa bei ya kutisha katika duka moja Mtaa wa Samora, katikati ya jiji.
Tulimwonea huruma lakini hatukuwa na namna ya kumsaidia. Mimi na Kimambo tulivuka barabara na nikaendelea kumsindikiza.
“Tuingie pale kwenye kantini tunywe maziwa moto,” Kimambo aliniambia mara tulipokuwa upande wa pili wa barabara.
Sikuwa na sababu ya kukataa. Nikamjibu, “Poa tu.”
Tukaingia. Akaagiza maziwa moto na keki mbili. Tukanywa taratibu huku tukiendelea kuzungumzia uboreshaji wa muziki wa gitaa, fani iliyokuwa inayateka maongezi yetu kila tunapokuwa pamoja.
Nusu saa baadaye, kama saa 2 hivi, tuliagana, yeye akaenda kwake ambako kwa hapo hakuwa mbali sana na mimi nikaanza safari ya kurejea nyumbani Hananasif. Kumbuka, nilikuwa nimetoka nyumbani nikiwa nimevaa makubadhi tu miguuni na sikutarajia kuwa ningetembea mpaka huko Kinondoni Shamba.
Hata hivyo, nilijifariji kuwa kwa giza lililokuwapo isingekuwa rahisi kila mtu kubaini kuwa nimevaa nini miguuni. Sikujali. Nikaanza kuvuta hatua, nikavuka barabara huku nikiwa nimekifungua kijiredio changu kidogo aina ya Panasonic nikisikiliza muziki.
Wakati niko eneo la katikati ya makaburi, nikimulikwa na mwangaza mkali kutoka kwenye taa kubwa zilizolizingira jengo moja lenye ofisi nyeti sana serikalini, mara nikakutana mwanamke mnene kiasi, mweupe akiwa amevaa gauni pana lakini lenye mvuto. Nuru ya taa za jengo hilo ilimmulika vizuri mwanamke huyo na kuuweka bayana uzuri wa sura na umbo lake.
TUTAONANA TENA SAA KUMI JIONI.....NIENDELEE KUKUJUZA KILICHOJIRI***
SIMULIZI YA KWELI
INNOCENT A. NDAYANSE
KUNA MATUKIO MBALIMBALI YA KUFURAHISHA, KUSIKITISHA NA HATA YA KUTISHA YATOKEAYO KILA SIKU DUNIANI. KATIKA SIMULIZI HII NINAKULETEA MTIRIRIKO WA TUKIO HALISI LILILONIKUTA MWANZONI MWA MWAKA 2005 NA KUZUA TAHARUKI KATIKA JAMII YA ENEO NILILOKUWA NIKIISHI.
NI TUKIO LILILOIBUA MASWALI MENGI NA HISIA TOFAUTI KWA WAKAZI WA ENEO HILO NA HATA WALE WALIOKUWA WAKIISHI MAENEO MENGINE, KILA MMOJA KWA UPEO WAKE WA KUFIKIRI.
SIMULIZI HII NI YA KWELI KWA ASILIMIA MIA MOJA, TOFAUTI KABISA NA HADITHI NYINGINE ZILIZOTANGULIA NA ZITAKAZOTUJIA SIKU ZA USONI.
TIRIRIKA NAYO…
* * ***
HUDAIWA kuwa kila mtu huwa na jambo ambalo nafsi yake imejikita zaidi. Hupenda sana kulifanya jambo hilo hata kama itamlazimu kutumia gharama za ziada.
Kuna anayependa kukaa vijiweni na kupiga stori. Mwingine ni mpenzi wa kunywa pombe. Mwingine hupendelea sana kutazama televisheni. Yupo aliyebobea katika michezo ya kamari. Na yupo ambaye yeye akili yake yote ni kwenye uhusiano wa mapenzi, leo yuko na huyu, kesho yuko na yule.
Ndiyo, kila mmoja ana kile ambacho roho yake hukipenda na huwa tayari hata kuvuruga bajeti yake na kubadili ratiba zake za siku ili tu airidhishe nafsi yake.
Mimi nilitokea kupenda kupiga gitaa tangu nikiwa na umri wa miaka 14. Niliipenda fani hiyo kwa kuwa nilikuwa siachani na kaka yangu ambaye tulikuwa tukipendana sana tangu utotoni kabisa. Aliitwa Barack Ambrosse Ndayanse.
Barack alikuwa mpenzi zaidi wa gitaa, labda zaidi yangu na alikuwa akipiga na rafikiye kipenzi, Ramadhani Zahoro ‘Bangwe’, wakitoroka darasani na kwenda kujificha kwenye shamba la mihogo na kuanza kupiga gitaa lililotengenezwa kwa zana hafifu za galoni.
Wakati huo tulikuwa tukiishi kitongoji cha Bangwe, mjini Kigoma. Kwa kuwa mara kwa mara nilikuwa nashinda naye, nilishawishika na mimi kujifunza kutekenya nyuzi za gitaa hilo la kiasili.
Mwanzoni mwa mwaka 1978, tukajiunga kwenye kwaya ya Kanisa la Anglikana Mwanga mjini Kigoma, usharika wetu na ambao baba yetu mzazi alikuwa Shemasi kanisani hapo.
Katika kipindi hichohicho, wakaja wanamuziki wawili kutoka katika kwaya iliyokuwa ikitikisa ukanda wa Afrika Mashariki, Mwanza Town Choir. Wanamuziki hao walikuwa wamekuja mjini Kigoma kwa ajira za Upanuzi wa Bandari na hivyo wakaamua kuwa wanakuja kanisani hapo kupiga magitaa.
Ni hapo ndipo mimi na Barack tulipogundua kuwa viwango vyetu vilikuwa duni sana na kuanza kujifunza kwa hao vijana waliotoka Mwanza.
Tuliendelea na fani hiyo na baada ya miaka mitatu tulikuwa katika viwango vilivyokubalika kwa wapenzi wengi wa muziki. Nakumbuka kuwa tulikuwa wepesi wa kusikiliza nyimbo zilizokuwa zikitamba miaka ile.
Baadhi ya nyimbo hizo ni Nyako Konya (Orchestre Mangelepa), Memi, Moni Afinda (Orchestra Kiam), Mikolo Mileki Mingi (Orchestre Veve) na nyingine nyingi za Kikongo.
Nyimbo za Tanzania, Usia wa Baba, Mwanameka na Betty za Dar International pia zilikuwa zikituteka kwa kiasi kikubwa. Kusikiliza sana nyimbo hizo kulikwenda sambamba na uigaji ili tuweze kupiga hatua.
Mara nyingi nilikuwa nikimsikia kaka yangu akisema, “Kama wao wameweza kwa nini sisi tusiweze?”
Mwaka 1985 tukawa tumekomaa zaidi, Baraki akiwa imara kwenye upigaji wa gitaa zito la besi na rythm ilhali mimi nikikomaa zaidi katika gitaa la solo kiasi cha kujikuta tukianza kupiga katika bendi moja iliyokuwa mjini hapo ya Super Kibisa Orchestra tukiwa na Ramadhani Zahoro ‘Bangwe.’
Hata hivyo, baadaye Ramadhani aliondoka Kigoma na kulivaa Jiji la Dar es Salaam, mimi na Barack na wanamuziki wengine tukabaki tukiliendeleza ‘sebene’ kwenye bendi hiyo na wakati huohuo pia tukiupiga muziki kwenye kwaya ya kanisa. Kwa sasa Ramadhani Zahoro ‘Bangwe’ ni mpigaji gitaa tegemeo wa Msondo Ngoma Music Band ya Dar es Salaam.
Kuanzia mwaka 1990, kasi ya kupiga muziki ikanipungukia kutokana na wingi wa majukumu. Miaka miwili baadaye nikaamua kubadili mazingira. Nikahamia jijini Dar es Salaam na nikawa napiga gitaa mara chache pale nilipoliona na nilipokuwa na nafasi ya kufanya hivyo.
Siku zikaenda, hatimaye nikajiunga na Kwaya ya Amkeni KKKT Usharika wa Kinondoni mwaka 1996. Hapo sikudumu sana kwa sababu zilezile za kubanwa na majukumu.
Mwaka 1997 mwishoni nikajiunga na Kwaya ya Vijana na Uinjilisti Hananasif Kinondoni, kwa maombi ya mwalimu mmoja aliyewahi kuniona nikipiga gitaa kule Usharika wa Kinondoni KKKT.
Hapa Hananasif nimekaa sana na kwa kuwa ndipo yalipokuwa masikani yangu nikajikuta nikirudi kwenye fani kwa kasi ya ajabu.
Mapenzi yangu kwa mpiga solo mahiri wa enzi za miaka ya 90, Alain Makaba wa Wenge BCBG yakairudisha ile ari yangu ya kupiga gitaa na hasa kwa kipindi kile Wenge walipoibua albamu ya Pentagone mwaka 1994.
Sasa nikarudi kwenye gitaa kwa nguvu kubwa. Kila wimbo uliopigwa na Alain Makaba nikawa nauiga kwa kiasi kikubwa. Kiwango kikapanda.
Mwishoni mwa miaka ya 1990, bendi ya African Stars ‘Twanga Pepeta’ ikazaliwa. Nakumbuka bendi hiyo ilikuwa inapiga muziki wake kwenye viwanja wa Leaders Club bureee! Kila Jumapili mchana!
Watu tukawa tunajimwaga hapo kila wikiendi na hasa kwa kuzingatia kwangu mimi pale palikuwa ni jirani sana na nyumbani. Mpangilio mzuri wa muziki wa Twanga, sanjari na upigaji wa Adolf Mbinga katika gitaa la solo vilinivuta sana na hivyo sasa nikawa nikibuni vyangu, nachanganya na vionjo vya ama gwiji Alain Makaba au mzalendo Adolf Mbinga hasa na wimbo wake wa ‘Kisa Cha Mpemba.’
Nikaendelea kuwa bora katika fani hiyo huku pia nikifanya kazi ya ajira katika Kampuni ya Uchapishaji Vitabu ya HEKO.
USIKU JANUARI 20, 2005
HII ilikuwa ni siku, kama siku nyingine ambazo niliamka na kwenda kwenye shughuli zangu za kila siku. Kwa siku hii nilizungukia mitaa ya katikati ya jiji ambako nilikuwa nafuatilia oda ya biashara kwa wafanyabiashara wakubwa wa maduka ya vitabu.
Ilipofika jioni, kitu kama saa 11 hivi nikawa nimesharudi Kinondoni na moja kwa moja nikaelekea kanisani kwa ajili ya mazoezi ya kwaya. Mazoezi yalimalizika saa moja usiku. Kijigiza kilikuwa kimekwishaitawala anga.
Baada ya mazoezi nilitoka na rafiki yangu, Kimambo aliyekuwa akiishi Kinondoni Shamba. Nilikuwa nikimsindikiza na tulikuwa na mazoea ya kuzungumza hili na lile hususan kuhusu kwaya kila tumalizapo mazoezi.
Siku hiyo, mara tulipomaliza mazoezi nilichoropoka hadi nyumbani ambako hakukuwa mbali. Nikavua viatu na kuvaa kandambili kwa kuwa siku hiyo sikuwa natarajia kwenda mbali.
Nikarudi eneo la kanisa ambako nilimkuta Kimambo akiwa nje ya uzio akizungumza na wanakwaya wengine huku akinisubiri.
Kabla hatujaondoka akaja rafiki yangu mwingine wa ‘kufa na kuzikana,’ Willy. William Jacob Kalumila. Huyu alikuwa ni mwalimu wa kwaya na nilizoeana naye kwa kiasi kikubwa na kuwa marafiki wa karibu zaidi kwa kuwa alikuwa akifundisha nyimbo zenye mwelekeo nilioupenda.
“Kocha vipi, tupandishe Mkwajuni?” Willy aliniambia.
Kwa kuwa tayari Kimambo alikuwa amenisubiri kwa muda mrefu, nikaona haitakuwa vizuri kumwacha na kuambatana na Willy. Kimambo angeona nimemdharau. Hivyo, kwa ustaarabu nikamjibu Willy, “Hapana kocha. Leo ngoja nimpe tafu mzee wa Kinondoni Shamba.”
Willy hakujali, tukaagana.
Mara tu nilipofika Kimambo alisitisha maongezi na kuniambia, “Inno, twen’zetu.”
Tukaondoka taratibu, tukipiga stori kuhusu mazoezi ya siku hiyo. Tukapita jirani na Shule ya Msingi Hananasif katika eneo lililokuwa na miti mingi iliyoongeza nguvu ya giza kwa kuwa hakukuwa na nyumba zilizokuwa kando ya barabara.
Tukawa tunapita Mtaa wa Ngano, mtaa uliokuwa umepandwa miti mingi iliyounda kivuli kizito mchana na kutengeneza giza la kuogofya usiku.
Mazingira yale tulikwishayazoea, hivyo hatukuwa na wasiwasi wowote. Tukawa tukitembea taratibu huku tukizungumza.
Hatimaye tuliuacha Mtaa wa Ngano, tukashika Mtaa wa Wakulima.
Mbele kidogo tukawa tunapita katikati ya makaburi. Tulipofika mwisho wa eneo la makaburi, tukawa kando ya Barabara ya Kinondoni, eneo lililojulikana na linalojulikana mpaka sasa kwa jina la MWEMBEJINI.
Hapo tulikuta mchanganyiko wa watu. Walikuwepo waliokuwa kituoni wakisubiri daladala na wengine kwa harakaharaka unaweza kuwaita ‘vibaka’ au ‘mateja’ kwani walikuwa ni vijana wanne wakizunguka-zunguka tu kituoni hapo huku wakizungumza kwa sauti zenye mikwaruzo inayokera, sigara na bangi zikivutwa bila ya wasiwasi.
Mimi na Kimambo hatukuwajali kama ambavyo nao hawakutujali. Mara kwa mara watu wa aina ile huwa eneo lile wakivizia daladala lililojaa ili waingie na kubanana na abiria na matokeo yake abiria ‘hulizwa.’ Au huvizia abiria atakayeteremka na kuzubaa-zubaa na wao huwa wepesi kwa kumpora chochote chenye manufaa kwao.
Magari mengi yalikuwa yakipita barabarani muda huo yakitokea katikati ya jiji hivyo ikatulazimu kusubiri. Mara daladala kutokea mjini likafika. Lilikuwa limejaa pomoni. Ile kusimama tu vijana wale nao wakasogea mlangoni kama abiria wa kawaida. Konda alipoteremka na kuwapisha abiria wateremke, vijana hawa waliokuwa chini wakawa wamesogea zaidi mlangoni.
Ndipo kilipotokea kituko. Mwanamume mmoja ambaye alikuwa amevaa nadhifu alipoteremka na kuanza kuvuta hatua akija upande huu wa Barabara ya Wakulima, alifuatwa na vijana wawili na haraka mmoja akampiga ngwara, jamaa akaenda chini kama gunia la mashudu tii!
Kabla hajajitetea, mikono ya vibaka wale ikawa imekwishatalii mifukoni mwake na kutoka na pesa na simu kisha hao wakakimbilia makaburini.
Yule jamaa aliyevamiwa alichanganyikiwa. Tukamsogelea na kumnyanyua. Tukamsihi aende tu nyumbani kwa kuwa vibaka wale wameshatokomea. Akaondoka huku akiilalamikia simu yake aliyodai kuwa kainunua siku tatu zilizopita kwa bei ya kutisha katika duka moja Mtaa wa Samora, katikati ya jiji.
Tulimwonea huruma lakini hatukuwa na namna ya kumsaidia. Mimi na Kimambo tulivuka barabara na nikaendelea kumsindikiza.
“Tuingie pale kwenye kantini tunywe maziwa moto,” Kimambo aliniambia mara tulipokuwa upande wa pili wa barabara.
Sikuwa na sababu ya kukataa. Nikamjibu, “Poa tu.”
Tukaingia. Akaagiza maziwa moto na keki mbili. Tukanywa taratibu huku tukiendelea kuzungumzia uboreshaji wa muziki wa gitaa, fani iliyokuwa inayateka maongezi yetu kila tunapokuwa pamoja.
Nusu saa baadaye, kama saa 2 hivi, tuliagana, yeye akaenda kwake ambako kwa hapo hakuwa mbali sana na mimi nikaanza safari ya kurejea nyumbani Hananasif. Kumbuka, nilikuwa nimetoka nyumbani nikiwa nimevaa makubadhi tu miguuni na sikutarajia kuwa ningetembea mpaka huko Kinondoni Shamba.
Hata hivyo, nilijifariji kuwa kwa giza lililokuwapo isingekuwa rahisi kila mtu kubaini kuwa nimevaa nini miguuni. Sikujali. Nikaanza kuvuta hatua, nikavuka barabara huku nikiwa nimekifungua kijiredio changu kidogo aina ya Panasonic nikisikiliza muziki.
Wakati niko eneo la katikati ya makaburi, nikimulikwa na mwangaza mkali kutoka kwenye taa kubwa zilizolizingira jengo moja lenye ofisi nyeti sana serikalini, mara nikakutana mwanamke mnene kiasi, mweupe akiwa amevaa gauni pana lakini lenye mvuto. Nuru ya taa za jengo hilo ilimmulika vizuri mwanamke huyo na kuuweka bayana uzuri wa sura na umbo lake.
TUTAONANA TENA SAA KUMI JIONI.....NIENDELEE KUKUJUZA KILICHOJIRI***
