Simulizi: Viganja mashavuni mwangu

Simulizi: Viganja mashavuni mwangu

Abdallahking

JF-Expert Member
Joined
Mar 19, 2018
Posts
3,985
Reaction score
10,843
0.jpg



SIMULIZI HII IMEKAMILIKA
IMEANDIKWA NA : NYEMO CHILONGANI
CHANZO : BURE SERIES


SEHEMU YA KWANZA

Cassian alikuwa kimya, macho yake yalikuwa yakiangalia baharini huku mawazo yake yakiwa mbali kabisa. Moyo wake ulichoka, maumivu aliyokuwa akiyasikia moyoni mwake hayakuweza kuelezeka.
Alikuwa bilionea mkubwa, mwenye makampuni mengi, migodi ya dhahabu na kila kitu ambacho kingemfanya kustahili kuitwa bilionea. Alimshukuru Mungu kwa utajiri aliokuwa nao lakini tatizo lilikuwa moja tu, hakuwa na mtoto.
Hilo lilikuwa pigo kubwa katika maisha yake, wakati mwingine alikuwa akimuuliza Mungu juu ya kilichokuwa kimetokea. Kwa nini alimpa utajiri mkubwa na kumnyima mtoto? Utajiri ungekuwa na maana gani kama tu hakuwa na mtoto ambaye angekuja kuurithi baada ya yeye kufa?
Hakuwa na furaha hata kidogo, kila siku moyo wake ulichoma kama moto kiasi kwamba alimuonea aibu mkewe, hata kukutana naye wakati mwingine aliogopa kutokana na tatizo lililokuwa mwilini mwake.
Hapo ufukweni mawazo yake yalikuwa mbali kabisa. Alitulia ndani ya gari huku akionekana kuwa na mawazo lukuki, alikaa garini kwa dakika kadhaa ndipo akaamua kutoka na kuanza kutembea. Kwa jinsi alivyokuwa akiwaza mpaka wakati mwingine machozi yalikuwa yakimtiririka mashavuni mwake.
Aligombana na dada zake kwa sababu hakuwa na mtoto. Kipindi cha kwanza ndugu hao walifikiri kwamba mwanamke aliyekuwa akiishi naye ndiye alikuwa na matatizo lakini baada ya kupima katika hospitali tatu, zote zilionyesha yeye ndiye alikuwa na matatizo.
Hakutaka kuwaambia ndugu zake ukweli, alikuwa tayari kugombana nao na hata kuchukiana maisha yake yote lakini si kuwaambia ukweli kwamba tatizo la kutokupata mtoto lilisababishwa na yeye na si mpenzi wake kama walivyokuwa wakihisi.
“Kwa nini wanamuonea? Kwa nini hawataki kuniuliza ili wajue ukweli kwamba Evelyne hana tatizo?” alijiuliza huku machozi yakimtiririka mashavuni mwake.
Hayo ndiyo yalikuwa maisha yake ya kila siku. Moyo wake ulimuuma mno, hakuona thamani ya utajiri, bila kuwa na mtoto maisha yake yangekuwa hivyohivyo mpaka kifo chake na mali kubaki kwa ndugu zake.
Si kazini, si nyumbani au barabarani, kila alipokuwa Cassian alikuwa myonge, hakuwa muongeaji, wakati mwingine alihisi kabisa mwili wake ukianza kupungua kutokana na matatizo aliyokuwa nayo.
Alipenda kuwa na mtoto, kila alipowaona wanaume wenzake wakiwa na watoto barabarani moyo wake ulimuuma, alitamani kuona kama ingekuwa yeye, alitamani kuona naye akiwabeba watoto wake kama walivyofanya watu wengine.
Mpenzi wake ambaye alimchukulia kama mkewe, Evelyne ndiye aliyekuwa akimfariji kila siku, alimwambia kwamba hakutakiwa kukata tamaa na ipo siku ambayo Mungu angetenda muujiza na hatimaye kupata watoto.
Alimwangalia Evelyne machoni, aliyaona maumivu yake, aliona jinsi msichana huyo alivyokuwa akiumia kwa kuwa tu hakuwa na mtoto. Alimuona kuwa mwanamke mwenye uvumilivu sana, aliyevumilia maneno ya ndugu na wakati hakuwa na tatizo bali tatizo kubwa lilikuwa kwake.
“Pole sana mke wangu,” alisema Cassian huku akimwangalia Evelyne.
“Usijali mume wangu! Maneno ya watu huwa hayanisumbui hata kidogo! Mimi nimekupenda wewe, katika shida na raha hakika tutaendelea kuwa pamoja na kamwe sitokuacha,” alisema Evelyne maneno ambayo kwa Cassian yalionekana kuwa faraja kubwa.
“Ila sina uwezo wa kumpa mimba mwanamke!” alisema Cassian.
“Hata kama! Nimekupenda wewe mpenzi, mtoto ni majaaliwa ya Mungu,” alisema Evelyne huku akimwangalia mpenzi wake huyo machoni mwake.
Japokuwa mkewe alijitahidi sana kumfariji lakini hakufarijika, bado alijiona kuwa na mzigo mkubwa kichwani mwake. Alimuomba Mungu kila siku bila kukoma, maombi yake makubwa yalikuwa ni kupata mtoto.
Ni kama alimuona Mungu akiwa ameziba masikio, alijitahidi kufunga na kuomba lakini matokeo yalikuwa yaleyale kwamba hakupata mtoto. Hilo lilimuuma mno, alichokifanya ni kwenda kwa madaktari wengi pamoja na mkewe, katika kila hospitali aliyofika, aliambiwa kwamba alikuwa na tatizo kubwa katika mfumo wa utengenezaji mbegu, hazikuwa na nguvu za kumpa mimba mwanamke.
Kila aliposikia sehemu kuna mikutano ya injili, yeye alikuwa wa kwanza, wakati mwingine alimuacha Evelyne nyumbani na kwenda huko, alitaka kumuona Mungu akimtendea muujiza lakini alimuona Mungu kuchelewa kwani kwenye kila alipofanyiwa maombezi aliambiwa kabisa kwamba angepata mtoto lakini matokeo yalikuwa yaleyale, hakupata mtoto.
Maumivu hayakupungua moyoni mwake, alikuwa mtu wa majonzi na kulia kila siku. Hakuona thamani ya utajiri, wakati mwingine alimwambia Mungu kwamba alikuwa tayari kupoteza kila kitu lakini mwisho wa siku aje kuwa na mtoto lakini maombi yake yote hayo yalionekana kama si kitu mbele za Mungu.
“Mchungaji! Kwa nini Mungu hajibu maombi yangu?’ aliuliza Cassian huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Kuna siku atafanya jambo. Nakwambia kwamba kuna siku utapata uzao wako wa kwanza,” alisema mchungaji huku akimwangalia Cassian.
“Kweli?”
“Unachotakiwa ni kuamini. Uwe na imani hata kama ni ndogo kama mchanga, hakika Mungu atafanya jambo,” alisema mchungaji huku akimwangalia Cassian.
Aliteseka usiku, hakulala vizuri, kila wakati alikuwa akishtuka usiku na alipoyafumbua macho yake kitu cha kwanza kilikuwa ni mtoto tu. Evelyne alimuonea huruma, wakati mwingine msichana huyo aliinuka kutoka kitandani na kwenda sebuleni, huko alikuwa akilia kama mtoto, hakuamini kama alikuwa akipitia maisha yake, alimpenda sana Cassian, alitamani siku moja wawe na familia yao lakini jambo hilo lilishindikana kabisa.
Cassian alipokuwa akiamka na kumkosa mkewe kitandani, alimfuata sebuleni na kumkumbatia, alimfariji kwa kumwambia kwamba kuna siku wangepata watoto hivyo hakutakiwa kuwa na hofu hata kidogo.
“Kuna siku Mungu atatupa familia yetu! Usilie mpenzi, amini kwamba kuna siku tutakuwa na familia yetu,” alisema Cassian huku akiwa amemkumbatia Evelyne.
“Ninaamini mume wangu!” alisema Evelyne huku akilia kilio cha kwikwi.

“Shoga mwenzako najuta kwa nini sikuwa nikichoma sindano za kuzuia mimba! Yaani umalaya wangu huu leo unanifanya nikose mtoto! Nimetoa mimba nyingi, mwisho wa siku leo hii nakosa mtoto! Hivi kweli mimi wa kukosa mtoto?” aliuliza Evelyne huku akimwangalia rafiki yake, Mwajuma.
“Mmh! Shoga ila na wewe ulizidi. Kila ulipopata mimba, kazi ilikuwa ni kutoa tu, ona sasa, unamfanya mume wako akose amani, alie kila siku, kwa nini lakini? Tena hata sindano za kuzuia mimba ulikataa kuchoma, ” aliuliza mwajuma.
“Wewe acha tu. Kwanza hapa ninachokitaka ni kufunga naye ndoa tu ili hata kama kuna siku mambo yataharibika basi yaharibike tukiwa kwenye ndoa ili tugawane mali manake bila hivyo naweza kuachwa kibudu,” alisema Evelyne.
“Hilo kweli Eve! Siku mumeo akigundua kwamba hata tatizo lolote ni lazima atakuacha. Umemdanganya sana! Kila nikimwangalia namuonea huruma bilionea wa watu. Wewe mwanamke mbaya sana,” alisema Mwajuma na wote kuanza kucheka.
Mwajuma alikuwa shoga pekee wa Evelyne aliyejua kilichokuwa kikiendelea. Aliyajua maisha ya Evelyne tangu kitambo, walikua wote utotoni na kusoma pamoja. Katika maisha ya ujana waliyopitia wasichana hao yalikuwa ni maisha ya kujirusha na kila mwanaume aliyekuwa akipita mbele yao.
Waliendekeza ufuska, walitembea na kila mwanaume aliyeonekana kuwa na pesa. Walipenda maisha ya starehe kiasi kwamba wakati mwingine walikuwa wakijiuza katika mitandao ya kijamii wakitafuta pesa na kwenda nchi mbalimbali kutafuta mabwana.
Maisha yao yaliharibika, wanaume ndiyo waliokuwa wakiyaendesha maisha yao. Kutokana na kujiona mjanja zaidi, Mwajuma aliamua kujichoma sindano za kuzuia mimba ila kwa Evelyne, aliogopa kabisa kufanya hivyo. Evelyne alipokuwa akipata mimba, kitu cha kwanza kilikuwa ni kutoa. Mpaka anakutana na bilionea kijana, Cassian, alitoa mimba zaidi ya kumi na mbili.
Wakawa wapenzi, wakaanza kuishi pamoja. Kwa kuwa alimpata mwanaume mwenye pesa, Evelyne akatulia, akataka kujenga maisha na kutengeneza familia yake ila tatizo lilikuja pale alipogundua kwamba hatoweza kushika mimba kwa sababu mfuko wake wa uzazi (uterus) na ukuta uliokuwa ukishikilia mfuko huo (cervix) vyote vililegea na mimba isingeweza kukaa tena.
“Huwezi kushika mimba. Mfuko wako wa uzazi umeharibika vibaya kiasi kwamba hauwezi kuruhusu kijusi kutengenezwa,” alisema daktari kwa sauti ya huruma huku akimwangalia Evelyne aliyekuwa akilia pembeni ya rafiki yake.
Hicho ndicho kitu kilichomuumiza mno, hakuamini kama tabia yake ya kutoa mimba ndiyo ingemfikisha mahali hapo. Alilia na kujuta sana huku wakati mwingine akitamani muda urudi ili arekebishe pale alipokosea lakini hakuweza kuurudisha muda huo.
Alijua kabisa kwamba kama angemwambia mumewe kuwa tatizo alikuwa nalo yeye angemuacha na kutafuta mwanamke mwingine, hivyo alichokifanya ni kutumia pesa zake, kwa kila hospitali waliyotakiwa kwenda kesho, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumtuma Mwajuma huko, alionana na daktari aliyetakiwa kuwapima siku inayofuata na kumpa kiasi kikubwa cha pesa ili aseme kwamba mwanaume ndiye aliyekuwa na tatizo.
Huo ndiyo ulikuwa mchezo wao, walifanikiwa, Cassian hakujua kilichokuwa kikiendelea, kwenye kila hospitali waliyokuwa wakiingia, majibu yalitoka na kusema kwamba yeye ndiye aliyekuwa na tatizo kitu kilichomnyima furaha katika maisha yake.
Wakati hayo yote yakiendelea, Evelyne hakutaka kuonyesha kitu chochote ndani ya nyumba, alimuonyeshea Cassian mapenzi ya dhati kwamba alikuwa akimpenda hivyohivyo kumbe dhamira yake kubwa ilikuwa ni kufunga ndoa na mwanaume huyo ili hata kama kuna siku wangeachana basi wagawane mali.
“Nakuonea huruma mke wangu,” alisema Cassian huku akimwangalia Evelyne.
“Hutakiwi kunionea huruma mume wangu! Nilikwishakwambia kwamba mimi na wewe mpaka kifo kitutenganishe,” alisema Evelyne huku akimwangalia mwanaume huyo.
“Ila sina uwezo wa kumpa mimba mwanamke!”
“Hilo hutakiwi kujali! Nilikupenda wewe, nakupenda jinsi ulivyo, unaniheshimu, unanithamini, hivyo ni vitu pekee ambavyo kila msichana huvipenda kutoka kwa mtu wake,” alisema Evelyne, wakati akizungumza hayo, tabasamu lilikuwa likionekana kwa mbali.
Bado Cassian alikuwa na mawazo tele, kila siku alipokuwa akimwangalia msichana huyo alijiona mkosefu katika maisha yote. Msichana mrembo kama Evelyne alitakiwa kuwa na mwanaume mwenye uwezo wa kumpa mimba mwanamke si kama yeye.
Mwanamke huyo alimuonyeshea uvumilivu, hakujua kama yeye ndiye mwenye tatizo na si kama alivyofikiria. Kwa kuwa alikuwa amejitolea kumpenda maisha yake yote, kuishi naye basi akataka kufanya kile alichokihitaji, kufunga naye ndoa pasipo kugundua mbinu za mwanamke huyo zilikuwa ni kugawana mali.
Akamwambia kwamba alikuwa tayari kufunga naye ndoa, hiyo ilimpa furaha Evelyne ambapo baada ya kuwa peke yake, akachukua simu yake na kumpigia rafiki yake kipenzi, Mwajuma kwa lengo la kumpa taarifa hiyo.
“Vipi? Mbona asubuhi asubuhi?” aliuliza Mwajuma kwenye simu.
“Mambo yametiki!”
“Umepata mimba?”
“Hapana bhana! Ameniambia nianze kufanya mipango ya harusi,” alisema Evelyne huku akionekana kuwa na furaha tele.
“Kweli?”
“Kwa nini nikudanganye? Tuanze kufanya mipango shoga kabla huyu mpuuzi hajagundua lengo langu,” alisema Evelyne.
“Eeh! Unamuita mpuuzi tena!”
“Hahah! Sasa nimuiteje? Mwanamke wa kukudanganya tena kizembe namna hii! Huyu ni mpuuzi,” alisema Evelyne na kuanza kucheka.
Mipango ikaanza kusukwa, Evelyne akajitoa vilivyo, akawataarifu marafiki zake wote kwamba alikuwa akijiandaa kufunga ndoa na mwanaume wake wa ndoto. Hakufikiria mapenzi, kichwa chake kilifikiria pesa ambazo aliamini kwamba mara baada ya kuachana na Cassian basi angeweza kuzipata.
Marafiki zake wakampongeza, wengine wakamuonea wivu kwani hawakupenda kumuona akiolewa na mwanaume mwenye pesa kama yeye, kila mtu alitaka kuwa na mwanaume mwenye pesa kama Cassian.
Akawasiliana na marafiki zake waliokuwa Dubai, akawaambia wamuandalie shela kwani alitaka kuvaa vazi hilo kutoka nchini humo. Akawapigia simu marubani wake wa ndege ndogo ya mpenzi wake aliyokuwa akiitumia kwenda huku na kule, akawaagiza kwamba wajiandae kwani walitakiwa kuondoka kuelekea katika Visiwa vya Comoro kula fungate yao baada ya kufunga ndoa.
Siku haikuwa imefika lakini Dar es Salaam nzima walikuwa wakifahamu kilichokuwa kikiendelea. Evelyne alimpa taarifa kila mtu aliyekuwa akimfahamu, alitaka watu wote wajue kwamba alikuwa akienda kufunga ndoa na bilionea mkubwa Afrika Mashariki.
“Tuna wiki mbili tu! Kila kitu kipo tayari kwa upande wako?” aliuliza Cassian huku akimwangalia Evelyne.
“Ndiyo mpenzi! Hofu kwako!”
“Huku kwangu kila kitu kipo poa. Nimewasiliana na Mchungaji Sebastian Mark kutoka nchini Ufaransa, amejitolea kuja kutufungisha ndoa. Nimeandaa boti nzuri na ya kifahari ambayo tutafungia ndoa huko katikati ya bahari,” alisema Cassian huku akitoa tabasamu, japokuwa alikuwa na moyo wa furaha lakini suala la kukosa mtoto lilimkosesha amani.
“Kwenye boti?”
“Ndiyo!”
“Waooo! Jamani baba watoto...” alisema Evelyne na kumkumbatia mwanaume huyo.
Siku hazikuwasubiri, ziliendelea kukatika kama kawaida. Baada ya kubaki wiki moja, maandalizi yakachachamaa, Evelyne hakutulia, kichwa chake kilifikiria mali, kwa jinsi alivyokuwa na presha aliona kama watu aliowaweka kwenye kamati walikuwa wakimchelewesha.
“Mwajuma! Wamesemaje?” aliuliza Evelyne.
“Kila kitu kipo tayari! Hoteli imekwishaandaliwa huko Comoro! Fungate tu ndiyo inasubiriwa,” alijibu msichana huyo baada ya kumpigia simu.
“Nashukuru sana shosti!”
“Halafu kuna kitu umesahau! Hivi umewaalika wale madaktari ambao walikusaidia kuficha siri?” aliuliza Mwajuma.
“Mungu wangu! Nilikuwa nimesahau! Ngoja niandike meseji halafu niwatumie wote kwa pamoja,” alisema Evelyne na kuanza kuandika ujumbe huo.
Aliandika harakaharaka, akakumbuka kwamba alitakiwa pia kumpigia Cassian na kumpa taarifa kwamba tayari hoteli ilikuwa imeandaliwa kwa ajili yao. Mara baada ya kuandika ujumbe huo wa kuwashukuru madaktari kwa mchezo walioufanya, na kwa sababu jina la Cassian lilimkaa sana kichwani, kwenye kutuma, akamtumia na Cassian, anakuja kushtuka baada ya ujumbe huo kwenda huko.
“Mungu wangu! Nimemtumia na Cassian pia!” alisema Evelyne, hapohapo kwa kuchanganyikiwa, akadondosha simu. Mapigo ya moyo yakaanza kumdunda kwa nguvu.

Cassian hakuwa na furaha kabisa, moyo wake ulikuwa na mawazo tele. Kila wakati alikuwa akimfikiria mpenzi wake, Evelyne, alionekana kuwa mwanamke shupavu, mwenye uvumilivu ambaye alikuwa tayari kufanya kitu chochote kile lakini si kumpoteza.
Alijiona kuwa na bahati kubwa, hakuwa na mawazo kwamba kitu alichokuwa akikihitaji msichana huyo kilikuwa mali zake na si mapenzi kama alivyokuwa amefikiria.
Akampigia simu rafiki yake aliyeitwa Osman na kumwambia kwamba alitaka kuzungumza naye, alihitaji kuwa bestman wake katika harusi hiyo iliyokuwa imebakiza siku moja kabla ya kufungwa katika boti moja ya kifahari aliyokuwa akiimiliki.
Kwa kuwa lilikuwa jambo muhimu, hakutaka kuzungumza naye kwenye simu, alichokitaka ni kuonana naye na kumwambia kwamba walitakiwa kuonana Serena Hotel kwa ajili ya kuzungumza suala hilo muhimu.
“Serena ni mbali sana. Kwa nini tusionane hapa Manyema?” aliuliza Osman kwenye simu. Alichokuwa akikiangalia zaidi kilikuwa ni foleni kubwa ya magari.
“Ipo wapi?”
“Hapa Kinondoni! Makaburini Mkwajuni!” alijibu Osman maneno yaliyomfanya Cassian kushtuka.
“Yaani nije kuonana na wewe Kinondoni?”
“Ndiyo! Njoo bwana!”
“Poa. Ila ninahitaji ulinzi, nisije kudandiwa na wahuni,” alisema Cassian, hilo halikuwa tatizo, kila kitu kiliandaliwa.
Cassian akatoka ofisini kwake, alijua kwamba alikuwa akienda katika mitaa ya Kiswahili hivyo hakutaka kwenda na gari lake la kifahari la Jaguar bali akachukua gari la mfanyakazi wake, Opa na kwenda nayo huko.
Hakutaka kugundulika, alijua kwamba kama angefika mahali hapo na gari la kifahari kila mtu angelitolea macho na kuangalia kuona ni mtu gani angeteremka katika gari hilo.
Njiani, kichwa chake hakikutulia, bado alimfikiria Evelyne, alimuona kuwa mwanamke shupavu, mwenye moyo wa chuma ambaye alijitolea maisha yake kwa asilimia mia moja kuishi naye japokuwa hakuwa na uwezo wa kumpa mimba.
Hakuchukua dakika nyingi akafika mahali hapo. Akapaki gari lake na kuteremka. Kwa kuwa lilikuwa gari la kawaida, hakukuwa na mtu aliyelitolea macho.
Hakutaka kugundulika, hivyo akachukua miwani yake ya jua na kuvaa kisha kuanza kupiga hatua kwenye sehemu ya kulia chakula ambayo ilikuwa maarufu Kinondoni nzima kwa kupika ugali mzuri na nyama ya kuchoma.
“Karibu bwana. Umebadilika! Hiyo miwani kama komando,” alisema Osman, ndiyo ilikuwa kawaida yake, kila walipokuwa wakikutana, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumtania kutokana na muonekano wowote aliokuwa nao.
Wakakaa na kuagiza chakula. Macho ya Cassian hayakutulia, yalikuwa yakiangalia huku na kule, hakuonekana kujiamini, swali lililokuwa kichwani mwake ni nini kingetokea mahali hapo kama tu watu wangegundua kwamba alikuwa yeye.
Wakati akiangalia macho yake huku na kule, yakatua usoni mwa msichana mmoja, mrefu kidogo, msichana aliyekuwa na sura nzuri, kifua kidogo huku uso wake tu ukiwa na tabasamu la asili.
Cassian akabaki kimya, akamwangalia msichana huyo kwa muda. Aliuona uzuri wake lakini tatizo kubwa alilokuwa nalo ni umasikini uliokuwa ukimwandama.
Alibalia khanga moja iliyoonekana kuchoka, kwa ndani alikuwa na gauni lake refu na blauzi ya rangi nyekundu. Japokuwa alionekana kuwa masikini kwa muonekano wake tu lakini msichana huyo alikuwa mchangamfu mno, aliongea na wateja kana kwamba alikuwa akimjua kila mtu.
“Mbona unamwangalia sana Naseku?” aliuliza Osman mara baada ya kumuona rafiki yake akimwangalia sana msichana huyo.
“Naseku! Ndiye nani?”
“Si huyo msichana unayemwangalia. Ngoja nimuite aje kutuhudumia,” alisema Osman na hapohapo kumuita msichana huyo.
Bila hiyana, huku uso wake ukiwa kwenye tabasamu pana Naseku akaanza kupiga hatua kuelekea kule walipokuwa wanaume hao. Macho yake Cassian hayakutoka kwa msichana huyo, alikuwa akimangalia mpaka alipofika mahali pale.
Mapigo yake ya moyo yalikuwa juu, alisahau kwa muda kwamba nyumbani alimuacha msichana ambaye kila siku alimwambia kwamba alikuwa akimpenda kuliko wanawake wote katika dunia hii.
“Naseku! Kutana na mshikaji wangu huyu,” alisema Osman huku akimtambulisha Cassian kama rafiki yake. Cassian alipovua miwani na kumwangalia vizuri msichana huyo, Naseku akashtuka.
“Umeshtuka sana kumuona Cassian hapa kwenu. Ndiye huyo unayemuona! Hebu msikilize kwanza,” alisema Osman.
Cassian alibaki kimya kwa muda, alikuwa akimwangalia msichana huyo kwa mshangao. Hakuamini kama angekutana na msichana aliyekuwa mrembo kama alivyokuwa.
Umbo lake maridadi, sauti yakena sura yake ya kitoto vilimfanya kuishiwa nguvu na kumsifu Mungu kwamba alikuwa akijua sana kuumba.
“Unaitwa Naseku?” aliuliza.
“Ndiyo!”
“Bila shaka Mmasai?”
“Ndiyo!”
“Nimefurahi kukufahamu! Una chakula gani?”
“Ugali na nyama choma!”
“Huna baga au pizza?” aliuliza Cassian na wote kuanza kucheka kwani walijua kwamba alikuwa akitania.
“Tuna sandwich!” alijibu Naseku kwa utani, vicheko vikazidi.
“Naomba ugali na nyama choma.”
“Sawa.”
Wakati anaondoka, mwanaume huyo alibaki akimwangalia kwa nyuma. Naseku alikuwa mrefu mwenye umbo maridhawa lililomfanya Cassian kuchanganyikiwa.
“Kaka una mke!” alisema Osman.
“Mke au mchumba! Unataka kunibania nini?” aliuliza Cassian na wote kucheka mpaka kugongeana mikono.
Naseku hakuchukua muda, akapeleka chakula mezani pale na wanaume hao kuanza kula. Kila mmoja alikuwa na furaha, walikuwa wakizungumza mambo mengi kiasi kwamba hakukuwa na mtu aliyechoka.
Muda wote huo Cassian hakumwambia Osman kilichokuwa kimemfanya kupigia simu na kukutana, alitaka wamalize kula na ndipo wazungumze.
Wakati wakiendelea kula, mara simu ya Cassian ikatoa mlio uuliomaanisha kwamba kulikuwa na ujumbe mfupi uliokuwa umeingia kwenye simu. Haraka sana akaingiza mkono mfukoni na kuitoa simu hiyo.
Macho yake yakatua katika kioo cha simu hiyo na kuliona jina la Evelyne. Moyo wake ukapiga paa kwani kwa jinsi alivyokuwa akimpenda, kila alipokuwa akiona ujumbe wake moyo wake ulifarijika mno, hivyo akaufungua ujumbe huo na kuanza kuusoma.
Haukuwa ujumbe mrefu sana, aliposoma mstari kwa mstari, alijikuta akibadilika, hakuamini kama ujumbe ule ulikuwa umetoka kwa msichana aliyekuwa akimpenda. Ulikuwa ni ujumbe uliobeba maumivu mazito, hakuamini kile alichokiona, akashusha pumzi nzito kiasi kwamba mpaka Osman akashangaa.
“Vipi?”
“Osman! Osman! Osman!” alijikuta akiliita jina hilo bila kuzungumza lolote.
“Kuna nini?”
“Evelyne! Evelyne!” alisema Cassian huku akimpa simu rafiki yake huyo na kuanza kuusoma ujumbe huo ambao uliandikwa ‘Dokta! Nashukuru sana kwa kunifichia siri ya kutokushika mimba. Mume wangu hajui lolote, anahisi tatizo ni lake. Naomba uje kuhudhuria harusi yangu wiki ijayo. Nitakupa taarifa zaidi’
“Mungu wangu!” alijikuta akisema Osman huku akiiweka mezani simu hiyo.
Cassian alishindwa kuvumilia, machozi yakaanza kumtoka. Moyo wake ulisikia maumivu makali ambayo hakuwa ameyategemea hapo kabla. Kila siku alijua kwamba yeye ndiye alikuwa na tatizo la kutokumpa mimba mwanamke lakini kwa meseji ile ilionyesha kabisa kwamba hakuwa na tatizo lolote lile.
Lawama zake za kwanza zilikwenda kwa madaktari ambao aliwaamini na kuwaambia wampime, wao ndiyo waliomwambia kwamba mpenzi wake hakuwa na tatizo lolote lile bali aliyekuwa na tatizo alikuwa yeye.
“Cassian! Unatakiwa kutulia, yaani usifanye maamuzi yoyote mabaya,” alisema Osman huku akionekana kumfariji sana rafiki yake huyo.
“Osman! Yaani huyu malaya ananifanyia hivi? Yaani ananifanya nijione sina uwezo wowote wa kumpa mwanamke mimba! Yaani ananifanyia hivi mimi!” alisema Cassian huku akilia kwa uchungu mkubwa.
Hakuweza kuvumilia, akainuka na kuelekea ndani ya gari. Osman akasimama na kumfuata kulekule. Kila mtu aliyekuwa ndani ya mgahawa ule alibaki akiwashangaa, si wao tu bali hata msichana Naseku naye alikuwa akishangaa na hakujua ni kitu gani kilikuwa kikiendelea mpaka Cassian kuinuka na kuelekea ndani ya gari lake huku akionekana kuwa tofauti.
Kazi ilikuwa kwa Osman, alikuwa akimpoza rafiki yake huyo ambaye alionekana kuumia kupita kawaida. Alijua kwamba kwa hali moja au nyingine ilikuwa ni lazima kufanya jambo kama tu angekwenda nyumbani akiwa katika hali hiyo. Alikaa naye ndani ya gari na kumpoza sana na mwisho wa siku mwanaume huyo kurudi katika hali ya kawaida.
“Nifanye nini?” aliuliza Cassian.
“Kitu cha kwanza kabisa hutakiwi kuonyesha hali yoyote ya kuupata huu ujumbe!” alisema Osman.
“Sawa.”
“Kama ni furaha, muonyeshee, usimfanye ashtukie kitu chochote kile, halafu huo ujumbe wake ulioingia, ufute. Halafu kesho nitakupeleka katika hospitali ya swahiba wangu akakufanyie vipimo tena,” alisema Osman.
“Sawa. Nitashukuru!”
Hicho ndicho alichoambiwa, hakutaka kuonyesha tofauti yoyote ile. Hakutaka kuondoka muda huo, alikaa mpaka ilipofika usiku ambapo akajiandaa na kuelekea nyumbani.
Alipofika, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumkumbatia Evelyne kwa furaha tele, alimletea unafiki, hakuonyesha tofauti yoyote ile machoni mwake, kama ilivyokuwa juzi na jana ndivyo ilivyokuwa siku hiyo kiasi kwamba msichana huyo akahisi hakukuwa na jambo lolote baya na inawezekana ujumbe ule haukuenda, na kama ulienda basi hakuuona.
Wakati Cassian akiwa amekwenda bafuni kuoga, haraka sana Evelyne akachukua simu ya mpenzi wake huyo na kuanza kuangalia. Akaenda sehemu ya meseji na kuangalia katika uwanja wa kuwasiliana naye, hapo, hakukutana na ujumbe wowote mpya kuonyesha kwamba kumbe meseji hakuwa ameipata.
Kidogo moyo wa Evelyne ukarudi kwenye amani, furaha ambayo ilikuwa imepotea ikarudi tena. Cassian alipomaliza kuoga, akarudi chumbani, akamnyanyua Evelyne na kumtupa kitandani ambapo akaanza kumvua nguo moja baada ya nyingine na kuanza kufanya mapenzi.
Mpaka kufikia hatua hiyo msichana huyo hakujua kama mwanaume huyo alijua kila kitu, hali aliyokuwa amemuonyeshea siku hiyo ilikuwa kama siku nyingine, wakalala na siku iliyofuata Cassian kuaga kwamba anaelekea kazini lakini ratiba yake ya kwanza kabisa ni kuwasiliana na Osman ambaye akamwambia hospitali ya kwenda na kuonana huko.
Hawakutaka kuchelewa, moja kwa moja wakaingia ndani ambapo Osman akamwambia tatizo alilokuwa nalo rafiki yake huyo ambapo daktari huyo hakuwa na tatizo lolote lile zaidi ya kuanza vipimo.
“Huna tatizo lolote lile. Mbegu zako zina nguvu za kuzalisha hata watoto ishirini! Wewe tu,” alisema daktari baada ya saa kumi za kusubiri majibu.
“Kweli?”
“Ndiyo! Kwani kuna mtu alikwambia huna uwezo?”
“Ndiyo! Kwa hiyo mambo yapo poa?”
“Kabisa kabisa. Mwanaume ngangari kama chuma,” alisema daktari huyo huku akimpongeza Cassian kwa kumpigapiga mgongoni.
Wakati Cassian akiwa amekwishapata majibu yake, Evelyne akampigia simu Mwajuma na kumwambia kwamba alitaka kuonana naye. Wakaonana na kuumuhadithia kila kitu kilichokuwa kimetokea, jinsi alivyowaandikia meseji madaktari na kwa bahati mbaya kumtumia mpenzi wake.
“Una hatari sana!”
“Wewe acha tu! Lakini hakushtukia. Angejuaaaa! Nafikiri angenichinja usiku ule,” alisema Evelyne huku akionekana kuwa na furaha tele.
“Mmh! Umecheza kama Pele. Kwa hiyo!”
“Sasa hivi hata kutuma meseji za kijinga siwezi. Nisije kukosea tena. Ile haikwenda, nikirudia tu, inakwenda,” alisema msichana huyo pasipo kugundua kwamba Cassian alijua na alitaka kumfanyia mchezo hatari, kumkataa siku moja kabla ya harusi.

Evelyne alikuwa na presha kubwa, alitaka kuona akifunga ndoa na mwanaume huyo bilionea ili aweze kufanikisha ile adhma yake aliyokuwa ameipanga. Alimpigia simu Mwajuma na kumwambia kwamba alitaka harusi yake iwe bab’kubwa hivyo kuendelea kuwaambia watu wengine.
Akaona hiyo haitoshi, akazungumza na waandishi wa habari wa mitandaoni na magazetini, aliwalipa kiasi kizuri cha pesa kwa ajili ya kutangaza harusi hiyo ambayo ingefanyika siku ya Jumamosi inayofuatia.
Waandishi hao na wale waliokuwa na kurasa zao katika mitandao yao wakaanza kuwataarifu watu wengi kwa kuposti matangazo kuhusu harusi hiyo kubwa ambayo ilitarajiwa kufanyika hivi karibuni.
Ni ndani ya siku chache tu, gumzo kubwa katika mitandao ya kijamii ilikuwa harusi hiyo, kila mtu alitaka kuona ni kitu gani kingetokea kwani kwa jinsi ilivyokuwa ikitangazwa kwenye mitandao hiyo, kila mmoja akahisi kwamba ingekuwa harusi kubwa na ya kifahari hata zaidi ya ile ya Beckham alipomuoa Victoria.
“Hii harusi kiboko! Inafungwa ndani ya boti!” alisema jamaa mmoja huku akionekana kushtuka sana, hakuamini kama kungekuwa na Mtanzania ambaye angeamua kufunga ndoa ndani ya boti ya kifahari badala ya kanisani.
“Kaka hiyo ni pesa. Unachotakiwa ni kuiamkia pesa, hilo tu,” alisema jamaa mwingine.
Wakati hayo yote yakiendelea, Cassian hakuwa na furaha hata kidogo, alikuwa mtu wa mawazo tele, alipokuwa akikaa ofisini kwake, hakuamini kama Evelyne angemfanyia mambo kama yale aliyomfanyia lakini wakati mwingine alibaki akimshukuru Mungu kwa muujiza alioufanya.
Alikuwa na kila kitu, alikosa mtoto tu, alikata tamaa kwa kuhisi kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa kila kitu lakini mwisho wa siku daktari akabainisha kwamba hakuwa na tatizo lolote lile kitu kilichomfanya kumshukuru Mungu sana.
Mapenzi yote aliyokuwa nayo kwa Evelyne yakaanza kupotea na chuki kuanza kuingia moyoni mwake. Alihitaji kuwa peke yake, alihitaji kuwa na msichana mwingine, asingeweza kuendelea kukaa na msichana huyo, alitaka kumuondoa maishani mwake na kumuingiza mwanamke mwingine.
Alimuumiza mno, hakutaka kumuacha hivihivi pasipo kumuumiza kama alivyokuwa amefanya. Alipanga kumuacha siku moja kabla ya kufunga ndoa. Alijua jinsi Evelyne alivyokuwa akihaha huku na kule kuhakikisha kwamba harusi inafungwa haraka iwezekanavyo hivyo alichokitaka ni kumuumiza kwa kukataa kumuoa msichana huyo.
Akapanga na Osman kila kitu ambacho walitakiwa kufanya, ilikuwa ni lazima Cassian apange kwenda kulala na msichana huyo hotelini siku moja kabla ya kufunga ndoa hiyo halafu amtelekeze hukohuko na kuondoka hotelini hapo, hilo wala halikuwa tatizo lolote lile, wakapanga hivyo na kukubaliana na mwanaume huyo kwamba hicho kilitakiwa kufanyika haraka sana.
Bado Cassian hakutaka kuonyesha tofauti yoyote kwa Evelyne, alimuonyeshea mapenzi ya dhati kwamba bado alikuwa akimpenda mno, kila alipokuwa naye, uso wake ulikuwa na tabasamu pana na muda wote alikuwa akikenua japokuwa moyoni mwake kulikuwa na maumivu makali.
Hakuacha kumsisitiza msichana huyo kufuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea, alimharakisha sana kwani siku zilibaki chache na kama asingeweza kukamilisha kwa kipindi kifupi basi kila kitu kingeharibika.
“Waandishi umewaandaa kuja harusini?” aliuliza Cassian huku akimwangalia mpenzi wake huyo.
“Ndiyo! Tena niliwasiliana na waandishi wa habari wa BBC nao wamesema watakuja,” alisema Evelyne huku akionekana kuwa na furaha tele.
“Safi sana. Nakupendea hapo tu. Hakuna mwanaume asiyependa kuwa na mwanamke mwenye kasi ya kufanya mambo kama wewe mpenzi,” alisema Cassian, hapohapo akamvuta msichana huyo na kumkumbatia.
Uso wake ulikuwa tofauti na kile kilichokuwa moyoni mwake, alikuwa na hasira kali, alimchukia mno msichana huyo japokuwa hakutaka kumuonyeshea ni jinsi gani alikuwa na chuki kali dhidi yake.
“Nakupenda mpenzi!” alisema Cassian huku akimwangalia Evelyne usoni.
“Nakupenda pia mume,” alisema msichana huyo.
Siku ziliendelea kukatika, ilipofika Ijumaa, Cassian akampigia simu Osman na kumwambia kwamba siku hiyo ndiyo ilikuwa ya kufanya mpango waliokuwa wameupanga. Akamwambia kwamba kila kitu walichokuwa wamekubaliana kilikuwa juu ya mstari na kilichobaki kilikuwa ni wajibu wa kufanya hicho walichokuwa wamepanga.
Ilipofika majira ya saa moja usiku, Cassian akampigia simu Evelyne na kumwambia kwamba siku hiyo walitakiwa kulala hotelini ili asubuhi wajiandae na harusi iliyokuwa imepangwa kufanyika siku hiyo.
Hilo halikuwa tatizo, kwa kuwa alimwamini sana Cassian na aliamini kwamba hakuwa akifahamu kitu chochote kile, akaondoka nyumbani na kuelekea katika Hoteli ya Twiga iliyokuwa Masaki na kukutana huko.
Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kukumbatiana kwa furaha, wakaenda bafuni kuoga, walipomaliza, wakatupana kitandani na kuanza kuvuana nguo. Akilini mwa Evelyne aliyaona mapenzi mazito ya mwanaume huyo, aliamini kwamba kusingekuwa na mwanamke yeyote ambaye angemtoa katika ulimwengu wake.
Walipomaliza kufanya mapenzi, simu ya Cassian ikaanza kuita, alipoliona jina la Osman wala hakujiuliza, akaipokea simu ile na kuanza kuzungumza naye.
“Umekwishafika? Ndiyo...ni kesho...ooh! mchungaji ndiyo amefika! Umempeleka hoteli gani? Serena...safi sana...anataka kuniona...basi sawa nakuja...” alisema Cassian na kukata simu.
“Nani?”
“Osman! Anasema kwamba mchungaji Mark ameingia kutoka Ufaransa! Hivyo anataka nikamuone mara moja,” alisema Cassian.
“Sawa. Ila usichelewe kurudi mpenzi!”
“Usijali!” alisema Cassian, hakuishia hapo tu, akamvuta Evelyne na kumbusu mfululizo kisha kuondoka.
Msichana huyo akabaki na amani moyoni mwake, hakuamini kama kweli siku inayofuata ndiyo ilikuwa ya kufunga ndoa na kuwa mke halali wa mwanaume huyo. Alikuwa na tamaa ya utajiri, alijitahidi kuficha siri ambayo hatimaye alijua ndiyo ilikuwa imedumu pasipo kugundulika mpaka hapo alipokuwa akitaka kufunga naye ndoa.
Hapohapo akampigia simu Mwajuma, akajisifia sana kwamba alikuwa mwanamke wa shoka aliyemkamata vilivyo Cassian na mwisho wa siku kutaka kufunga naye ndoa huku akiwa amemdanganya vya kutosha kuhusu kuzaa watoto.
“Shoga kesho ndiyo naanza safari! Nikitoka hapo, ni kuleta vituko, akiniacha kesi inakwenda mahakamani tunagawana utajiri,” alisema Evelyne huku akionekana kuwa na furaha ya ajabu.
“Jamani shoga mpaka nakuonea wivu! Unakwenda kuuchukua ubilionea hivihivi!” alisema Mwajuma.
“We acha tu! Ndiyo tayari nishatajirika!” alisema Evelyne.
Cassian akashuka mpaka chini ya hoteli, akaingia ndani ya gari lake na kuondoka mahali hapo. Mtu wa kwanza kuzungumza naye alikuwa mlinzi wa nyumbani kwake, akamwambia kwamba Evelyne hakutakiwa kuingia ndani ya nyumba hiyo na kama angemruhusu kuingia basi angemchukulia maamuzi magumu mno.
Mlinzi huyo hakuleta ubishi, alimheshimu bosi wake, tena baada ya kuona kwamba mlinzi mmoja asingetosha, Cassian akapiga simu mpaka katika kampuni ya ulinzi ya Knight na kuwaambia kwamba alihitaji ulinzi wa watu watano nyumbani kwake ambapo bila tatizo lolote walinzi watano waliokuwa na bunduki wakaelekea huko.
“Osman upo wapi?” aliuliza Cassian.
“Nyumbani!”
“Hebu twende Albert Lounge tukale bata kidogo!” alisema Cassian huku akiendesha gari kwa kasi kuelekea Albert Lounge. Msasani kwa ajili ya kuonana na mshikaji wake huyo.

ITAENDELEA
 
SEHEMU YA PILI

Muda ulikuwa ukisonga mbele, msichana Evelyne alikuwa ndani ya chumba cha hoteli, mara kwa mara alikuwa akimpigia simu Mwajuma na kuzungumza naye, alikuwa akimtambia kwamba hatimaye alikuwa akienda kufanikiwa kwa kile alichokuwa amekipanga.
Cassian alikuwa na utajiri mkubwa, makampuni mengi ambayo aliamini kwamba kama wangekuwa mume na mke kisha kuachana basi akaunti yake ingesoma zaidi ya bilioni kumi za Kitanzania.
Hakuwa radhi kuona akikikosa kiasi hicho cha pesa na ndiyo maana alipambana kuhakikisha anaolewa na kufanya uchafu huo akiwa ndani ya ndoa. Hapo chumbani, kichwa chake kilikuwa kikifikiria mambo mengi, alitaka kuona kila kitu kikienda harakaharaka kama alivyokipanga, alitaka kuona asubuhi ikiingia, aende saluni na mpambe wake na baadaye aende kwenye boti ambayo walitakiwa kufungia ndoa.
Aliiamini simu aliyopigiwa Cassian na kuambiwa kwamba tayari mchungaji kutoka nchini Ufaransa alikuwa amekwishaingia nchini na kilichokuwa kimebaki kilikuwa ni kufunga ndoa tu.
Pale chumbani hakutulia, kila wakati alikuwa akiishika simu yake na alipoona muda unazidi kwenda na mwanaume wake harudi chumbani hapo, akaanza kumpigia simu.
Hakukuwa na majibu yoyote yale, simu ilikuwa ikiita tu lakini haikuwa ikipokelewa. Alishindwa kujua kulikuwa na tatizo gani lakini kila alipofikiria kwamba alikwenda kumpokea Mchungaji Mark, alihisi kwamba mwanaume huyo huyo alikuwa bize katika kufanya mazungumzo na mchungaji.
Muda ulizidi kusogea, mpaka inaingia saa tisa usiku wa manane bado majibu yalikuwa yaleyale. Hilo kidogo likaanza kumtia hofu na kitu kimoja na cha kwanza kilichomjia kichwani mwake ni kwamba Cassian alikuwa amepata ajali mbaya.
Akahisi mwili wake ukipigwa ganzi, hakutaka kuona hilo likitokea, kitu alichokuwa akikihitaji ni kuona akifunga ndoa naye na hata kama angepata ajali na kufa, basi kitu hicho kitokee wakati wakiwa ndani ya ndoa.
“Mpenzi nina wasiwasi,” alisema Evelyne, alikuwa amempigia simu Mwajuma.
“Wasiwasi wa nini tena?”
“Cassian. Aliondoka kwenda kuonana na Mzungu ambaye ndiye atakuwa mchungaji wa kesho. Hajarudi mpaka sasa hivi,” alisema Evelyne.
“Aliondoka saa ngapi?”
“Tangu saa tatu usiku!”
“Mmh! Lakini usijali! Inawezekana kaenda sehemu kunywa. Si unajua wanaume,” alisema Mwajuma.
Maneno ya rafiki yake huyo hayakumuingia kichwani, bado alikuwa na hofu kwa kuhisi kwamba kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea upande wa pili.
Muda ulizidi kusogea, hakupata usingizi, ilikuwa ni heri kukosa kitu chochote kile lakini si kuikosa ndoa ambayo iliutesa moyo wake, ndoa ambayo aliamini piga ua ilikuwa ni lazima kuyabadilisha maisha yake.
Ilipofika saa kumi na moja na kuona kimya, hakutaka kuendelea kubaki hospitali, haraka sana akatoka na kuanza kwenda katika hospitali zilizopo karibu, alihisi kwamba mwanaume wae huyo alikuwa huko. Alikwenda kwenye hospitali tatu lakini huko hakufanikiwa na ndipo akapata wazo la kwenda nyumbani kwa Cassian.
Hakuchukua muda mrefu akafika nyumbani hapo. Hali aliyoikuta ikamtia hofu, nje kulikuwa na walinzi kadhaa waliokuwa na bunduki, hakujua sababu ya watu hao kuwa mahali hapo, kitendo cha wao kuwa hapo kikampa majibu kwamba kulikuwa na tatizo, inawezekana Cassian alikuwa amekamatwa na polisi.
“Unakwenda wapi wewe mwanamke?” aliuliza mlinzi mmoja huku akimsogelea Evelyne.
“Naingia kwangu!”
“Humu kwako?”
“Ndiyo!” alijibu huku akimwangalia mlinzi yule.
“Nyumba yako hii?”
“Ni kwa mume wangu mtarajiwa, na leo tunafunga ndoa!” alijibu Evelyne kwa mbwembwe zote, alikuwa akimwangalia mlinzi huyo kwa jicho la dharau, jicho lililoonyesha moyo wake kusema ‘nikiingia ndani utanikoma mshenzi wewe’.
“Wewe si ndiye Evelyne?”
“Ndiyo!”
Wale wenzake waliokuwa pembeni waliposikia jina hilo, nao wakajisogeza kule alipokuwa msichana huyo na kumwangalia. Evelyne alishangaa, hakujua kitu kilichokuwa kikiendelea mahali hapo, akahisi kulikuwa na tatizo.
“Hutakiwi kuingia humu!” alisema jamaa mwingine.
“Siruhusiwi kuingia humu?”
“Ndiyo!”
“Na nani?”
“Huyo unayejidaia ni mpenzi wako!”
“Cassian?”
“Ndiyo!”
“This is insane! I got get inside,” (huu ni uwendawazimu! Inabidi niingie ndani) alisema Evelyne kwa Kiingereza cha harakaharaka.
“No! You have to leave!” (hapana! Unatakiwa usepe) alisema mwanaume mwingine, hakuishia hapo, akaanza kukoki bunduki yake.
Mara ya kwanza msichana huyo alifikiri ni utani lakini baada ya kuwaona watu hao wakimwangalia huku wakionekana kumaanisha walichokuwa wakimwambia, akahisi kabisa hapo hakukuwa na utani wowote ule. Akanywea ila kitu pekee kilichomjia kichwani ni kwa sababu gani Cassian hakutaka aingie ndani.
Akaona hilo halitoshi, akawaomba walinzi hao wamuitie mlinzi wa kila siku nyumbani hapo, hilo halikuwa tatizo, mlinzi huyo akafika na kuanza kuzungumza naye.
“Jamaa ndiyo aliagiza usiingie ndani! Hata huu ulinzi umeongezwa kwa ajili yako,” alisema mlinzi huyo kitu kilichompelekea Evelyne kuhisi kama akimwagiwa maji ya baridi kabisa.
Machozi hayakutaka kusubiri, hapohapo yakaanza kumtoka na kutiririka mashavuni mwake, akaanza kusikia maumivu makali, hakuamini kile kilichokuwa kikiendelea, alihisi kwamba alikuwa ndotoni akiota kila kitu kilichokuwa kikiendelea mahali hapo.
Hiyo ilimaanisha kwamba Cassian hakutaka kuwa naye, ilimaanisha kwamba hakukuwa na ndoa tena, yaani alichwa siku ya harusi. Lilimuumiza moyoni, alitamba sana kwamba alikuwa akienda kuolewa, mitandaoni, gumzo lilikuwa ndoa hiyo, kila kona ilizungumziwa harusi hiyo.
Akarudi ndani ya gari, kabla ya kuondoka akalalia usukani, mbele yake akayaona maisha yake yakiwa yamejaa giza, hakujua sababu iliyomfanya Cassian kuchukua uamuzi ule na wakati mpaka mara ya mwisho mwanaume huyo alipokuwa akiagana naye alionyesha sura ya tabasamu, penzi zito lilionekana kupitia macho yake, sasa iweje abadilike ghafla hivyo?
Akaanza kuifikiria mitandao ya kijamii, alitumia kiasi kikubwa cha pesa kutamba huko, kama kila mtu alikuwa akijua kwamba alikaribia kufunga ndoa na mwanaume huyo siku hiyo ilimaanisha kwamba hata hapo alipoachwa kwenye mataa basi kila mmoja angejua kwamba ameachwa solemba.
Alilia sana, hakutaka kumpigia simu Mwajuma na kumwambia, alichokifanya ni kuwasha gari na kumfuata huko. Mawazo juu ya Cassian yalikuwa makubwa mno, hakuamini kama kweli mwanaume huyo alimuacha katika kipindi kigumu kama hicho.
Aliendesha gari huku akiwa na mawazo hayo ya kuachwa yakimsumbua kichwani mwake. Kila alipokuwa akipita na kupishana na watu, aliona kama wote hao tayari walijua kama aliachika.
Alipofika Sinza Makaburini, akakata kulia ambapo aliendesha mpaka katika nyumba moja iliyokuwa na wanawake wengi kwa nje, akasimamisha gari na kuwafuata wanawake hao, akawasalimia na kuingia ndani.
Alikijua chumba alichokuwa akikaa Mwajuma, moja kwa moja akaelekea mpaka katika chumba hicho na kugonga, mlango ukafunguliwa na msichana huyo ambapo baada ya kumuona tu, akaanza kulia.
Mwajuma alishangaa, ilikuwa ni asubuhi sana hata kutoka ndani hakuwa ametoka, alijiuliza sababu ya msichana huyo kulia namna hiyo, alionekana kuumia, alionekana kuwa na kitu moyoni mwake, ilikuwaje alie kwa uchungu namna ile na wakati siku hiyo ilikuwa ni ysiku ya kufunga ndoa na bilionea mkubwa Afrika Mashariki.
Alijaribu kumbembeleza anyamaze lakini Evelyne hakunyamaza, alikuwa akilia mfululizo, tena kilio kikali kilichojaa kwikwi. Aliendelea kulia kwa dakika ishirini nzima ndipo akanyamaza na kuanza kumwambia Mwajuma kilichokuwa kimetokea.
“Haiwezekani!” alisema Mwajuma huku akimwangalia rafiki yake huyo.
“Ameniacha! Cassian ameniacha,” alisema Evelyne huku kila wakati akiyafuta machozi.
Huo ndiyo ulikuwa ukweli, aliumia mno moyoni mwake, kilichokuwa kimetokea hakukiamini, aliona kila kitu kilichokuwa kikiendelea kama ndoto fulani ambapo baada ya dakika chache angeshtuka kutoka usingizini.
Hawakujua sababu ya Cassian kuchukua uamuzi wa ghafla namna hiyo kwani usiku uliopita tu alikuwa na furaha tele na alimuonyeshea msichana huyo mapenzi yote, sasa iweje abadilike namna hiyo?
“Au ile meseji uliyomtumia ndiyo chanzo?” aliuliza Mwajuma.
“Hapana! Haikumfikia?”
“Una uhakika? Kwako ilionyeshaje? Kama meseji haikwenda inakuonyeshea kwa kuweka kialama chekundu, sasa kama ile ilikwenda, kwa nini kialama hakikuonekana?” aliuliza Mwajuma maswali ambayo yalianza kumpa jibu Evelyne.
“Mmh!”
“Nahisi meseji aliipata ila aliifuta na hakutaka kukuonyeshea dalili zozote zile!” alisema Mwajuma huku akimwangalia msichana huyo.
“Inawezekana!”
“Kwa hiyo utafanyaje?”
“Nimeaibika Mwajuma. Cassian ameniumiza. Kwa pesa nilizokuwa nazo kwenye akaunti yangu, nitazitumia hata zote kumuua mwanamke yeyote atakayekuwa naye, kama kuumia, na yeye aumie kwa kumuua msichana ampendaye!” alisema Evelyne huku akionekana kuwa na hasira kali.
“Wewe tu! Na mimi nitakusaidia. Ukiua kwa kisu, nitaiweka maiti kwenye gunia, sitokuacha ila huyu mbwa lazima tumkomeshe,” alisema Mwajuma huku naye akionekana kuwa na hasira sana kwani mafanikio ambayo angeyapata rafiki yake yangekuwa sawa na mafanikio yake.

Cassian aliamshwa na alamu ya simu yake, haraka sana akashtuka kutoka usingizini, mwili wake ulikuwa umechoka kwani usiku uliopita alichelewa kulala kutokana na kwenda baa kunywa huku akiwa na rafiki yake, Osman.
Akaanza kuangalia huku na kule, hakuwa sawa, akayapeleka macho yake katika saa yake ya ukutani ambayo ilimuonyesha kwamba tayari ilikuwa ni saa 12:00. Akapeleka mkono wake pembeni kwa lengo la kumgusa mpenzi wake, Evelyne, alikuwa amesahau kile kilichotokea usiku uliopita, alipomkosa, kumbukumbu zake zikamjia kwamba aliachana na msichana huyo.
Hapo ndipo mawazo juu ya Evelyne yalipoanza kurudi kichwani mwake. Alijiona shujaa, alifanya kitu ambacho kwa wanaume wengine wasingeweza kufanya, alipoteza muda wake, alilia kwa kuwa aliumia sana lakini baadaye, kila kitu kilichokuwa kimetokea hakikuwa kama kile alichokuwa amekifikiria.
Wakati akiwaza hayo, picha ya msichana mmoja ikaja kichwani mwake, hakuwa msichana mwingine zaidi na Naseku. Alimkumbuka binti huyo wa kimasai, jinsi alivyokuwa mrembo, umbo matata ambalo lilitosha kumfanya mwanaume yeyote duniani kuwa kwenye mhemko mkubwa.
Akatoa tabasamu, kwa jinsi alivyokuwa, alihisi kabisa kwamba msichana huyo alistahili kuwa mke wake, alikuwa msichana masikini, aliyetafuta maisha kwa kuwa mhudumu katika mgahawa uliokuwa Kinondoni, hakutaka kujali kwa kuwa alikuwa na pesa, aliamini kwamba angeweza kumbadilisha na kuwa na muonekano mzuri kama ilivyokuwa kwa Kim Kardashian.
Hakuwa amezoeana naye, ila aliamini kwamba kama angemtumia rafiki yake, Osman ingekuwa rahisi kuonana na msichana huyo kisha kuzungumza naye. Hapohapo pasipo kuchelewa akaichukua simu yake na kumpigia rafiki yake huyo.
“Vipi mzee mzima?” ilisikika sauti ya Osman kwenye simu.
“Poa tu! Una nafasi leo?” aliuliza Cassian.
“Yeah! Hasa kwa mtu kama wewe ukiuliza hivyo! Kuna ishu?” aliuliza Osman.
“Ndiyo! Nataka unipeleke kwa yule msichana!”
“Msichana gani?”
“Naseku!”
“Duh! Mpaka jina lake umelikariri! Wewe noma!”
“Hahaha! Itawezekana?”
“Haina shida!”
Huyo ndiye mtu aliyekuwa akimfikiria muda huo, taswira ya Naseku ilipomjia kichwani, ilimkaa vilivyo. Alitabasamu na muda mwingine kutoa kicheko cha chini. Aliamini kwamba kama angezungumza na msichana huyo basi angeweza kukubaliana naye na kuwa mpenzi wake.
Akajiandaa, alipomaliza, akaondoka zake kuelekea ofisini. Njiani, alikuwa akiangalia huku na kule, kila alipowaangalia watu aliokuwa akipishana nao, moyo wake ulikuwa na furaha kwani alihisi kila mtu aliyekuwa akimwangalia alijua kilichokuwa kimetokea kati yake na msichana aliyetokea kumchukia mno, Evelyne.
“Bosi! Karibu sana,” alimkaribisha sekretari wake huku akiwa na tabasamu pana.
“Ahsante sana!”
“Na leo kumbe unakuja kazini!”
“Kwa nini nisije sasa?”
“Si unakwenda kwenye harusi!”
“Harusi gani?”
“Jamani! Yaani umesahau?”
Cassian hakujibu kitu zaidi ya kutoa tabasamu na kuingia ofisini kwake. Moyo wake ulikuwa na furaha tele, alijisikia amani kuliko siku nyingine. Alijua kwamba Evelyne alichanganyikiwa lakini hilo hakutaka kujali.
Kila mfanyakazi alishangaa, wengi waliamini kwamba siku hiyo ilikuwa ni siku ya harusi ya bosi wao. Wanakamati walikamilisha ripoti yao, wakatengeneza ratiba lakini kilichowashtua ni kumuona bosi wao akiwa ofisini, ilikuwaje awe mahali hapo na wakati siku hiyo ilikuwa ni ya kufunga ndoa na Evelyne.
Kila mmoja alikuwa na maswali mengi, alilijua hilo, alichokifanya ni kutoka na kuanza kuzungumza nao. Aliwaambia kwamba hakukuwa na harusi, aliahirisha kila kitu baada ya msichana yule kumdanganya.
“Alikudangany? Kivipi?” aliuliza mfanyakazi mmoja.
“Alinifanya nijue sina nguvu ya kumpa msichana mimba!”
“Kumbe unazo?”
“Tena nyingi! Naweza kujaza hata mbuga ya wanyama!” alisema Cassian na wote kucheka kwa sauti.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa kuvujisha kile kilichokuwa kimetokea. Kila mfanyakazi aliyeipata, akachukua picha ya Evelyne na kuiweka mtandaoni, kama alivyokuwa ametamba sana katika mitandao ya kijamii ndiyo hiyohiyo iliyotumika kumchafua.
Waandishi wa habari hawakuwa mbali, baada ya kuipata taarifa hiyo, kitu cha kwanza kilikuwa ni kumpigia simu Evelyne, simu yake iliita bila kupokelewa mpaka pale ilipozima.
Mitandaoni kila sehemu stori kubwa ilikuwa ni kuachwa kwa msichana Evelyne, wengi walimsikitikia kwa kuona kama kile kilichotokea alikuwa ameonewa huku lawama zao nyingi zikiwa kwa Cassian ambaye alikuwa akiheshimika kila kona nchini Tanzania.
Baada ya kuwekwa sababu ya watu hao kutokufunga ndoa, kila mmoja akabadilisha moyo wake na kuanza kumchukia msichana huyo. Posti mbalimbali zikawekwa katika mitandao ya kijamii wakikilaani kitendo alichokifanya msichana huyo, wengine walimdhihaki, wengine walimcheka kwa kumwambia kwamba mbwembwe zote alizokuwa amezifanya mitandaoni kumbe hakuwa na uwezo wa kushika mimba.
“Halo halo! Mwanamke mtu mzima hata aibu hana,” alisema msichana mmoja aliyekuwa saluni akisukwa, mkononi alikuwa na simu yake ya Tecno, muda wote alikuwa akicheka tu.
Tanzania nzima ikajua kilichokuwa kimetokea, mbwembwe zote zikaisha na hakukuwa na harusi tena. Wale waliokuwa wamejiandaa, wakapewa taarifa kwamba kitu kama hicho kisingekuwepo tena.
“Mwajuma! Nitamuua Cassian! Nitamuua Cassian,” alisema Evelyne huku akionekana kuumia mno, kilichokuwa kikiendelea katika mitandao ya kijamii kilimuuma kupita kawaida.
Wakati yeye akihuzunika na kulia, upande wa pili Cassian alikuwa na mpango wa kuonana na msichana Naseku. Alihakikisha kwamba ni lazima afanye kila liwezekanalo kumpata msichana huyo.
Wakakubaliana kuonana na Osman sehemu na baada ya hapo kuanza kuelekea katika mgahawa ule. Hawakuchukua muda mrefu, wakafika huko ambapo macho ya Cassian yalipotua kwa msichana Naseku, moyo wake ukapiga paaa!
Wakafuata meza moja na kukaa hapo. Macho yake hayakutoka kwa Naseku, alikuwa akimwangalia tu, siku hiyo alionekana kuwa tofauti, alionekana mzuri zaidi ya siku ya kwanza alipomuona mahali hapo.
Kama kawaida yake ndani alivalia gauni lake refu huku kwa nje akiwa na khanga iliyofubaa. Alimwangalia, kichwani alisuka mabutumabutu, kwa kifupi alionekana msichana mshamba mwenye umasikini mkubwa.
“Leo nahitaji wali na nyama,” alisema Osman baada ya Naseku kufika mezani hapo.
“Sawa. Kaka hapo?”
“Nahitaji kuzungumza na wewe tu!” alisema Cassian na Naseku kuanza kucheka kwani alihisi kama utani fulani.
“Hahaha!”
“Naseku! Ninahitaji kuzungumza na wewe!” alisema Cassian huku akimwangalia msichana huyo, mtazamo wake ulibadilika, hakuonekana kuwa na utani hata kidogo kwa kile alichokuwa akikizungumza. Kidogo Naseku naye akatulia.
“Kuzungumza na mimi?”
“Ndiyo!”
“Kuhusu nini?”
“Usijali! Mimi si mtekaji! Naweza kuzungumza na wewe?” aliuliza Cassian.
“Mmh!”
“Dakika kumi tu!”
“Nyingi sana! Au baada ya kazi!”
“Haina shida!”
“Sawa.”
“Unatoka saa ngapi?”
“Saa moja usiku!”
“Nitakufuata!”
Hiyo ndiyo ilikuwa shida yake siku hiyo, hakuwa na haja ya kula chakula ila alikuwa tayari kulipia kiasi chochote cha pesa mahali hapo. Alibaki akimwangalia Naseku, msichana huyo mpole alikuwa akitembea kwa mwendo wa taratibu, alionekana kuwa na hofu, alimfahamu Cassian, alikuwa mwanaume mwenye pesa, alipojiangalia yeye, hakujiona kuwa na pesa yoyote ile, sasa kwa nini mwanaume huyo alitaka kuzungumza naye?
Hakufikiria ishu ya kimapenzi hata mara moja, alijiangalia jinsi alivyokuwa, maisha yake na hata jinsi alivyokuwa akivaa, hakustahili hata kumgusa Cassian si kuwa mpenzi wake tu. Kila alipokuwa akiwahudumia wateja, alipomwangalia Cassian, naye mwanaume huyo alikuwa akimwangalia vilevile.
Baada ya Osman kumaliza kula, wakaondoka, njiani, Cassian alikuwa na mawazo tele, kichwa chake kilivurugika, mawazo yakamuingia, alikuwa akimfikiria msichana huyo kuliko kitu chochote kile.
“Ninataka nimuoe Naseku!” alisema Cassian huku akimwangalia Osman.
“Umuoe Naseku?”
“Ndiyo!”
“Mhh!”
Alimaanisha, aliondoka mpaka nyumbani kwake, alikaa kidogo na kurudi tena kulekule kazini kwa kina Naseku huku saa yake ikimwambia kwamba tayari ilikuwa ni saa 12:26 jioni. Alipofika hapo, akamuulizia msichana huyo na kuambiwa kwamba aliondoka.
Moyo wake ukamuuma, aliumia kupita kawaida, alihisi kudharauliwa, hakutaka kukubali, kwa jinsi alivyotokea kumpenda msichana huyo, hakuwa radhi kuona akilala pasipo kuzungumza naye. Akauliza alipokuwa akiishi, akaambiwa kwamba ni Tandale Kwa Mkunduge.
“Ninakwenda sasa hivi!”
Akaondoka mgahawani hapo mpaka huko. Alipofika, akaulizia na akaelekezwa mahali msichana huyo alipokuwa akiishi. Alipoteremka na kuifuata nyumba hiyo, alipoiona tu akashindwa kuvumilia, machozi yakaanza kumtoka, hakuamini kama msichana aliyekuwa akimpenda kwa moyo wa dhati alikuwa akiishi katika nyumba mbovu kama hiyo.
Ilikuwa nyumba yenye ukuta uliochoka, bati lenye kutu ambalo lilikuwa na matairi ya gari, kulikuwa na kila aina ya uchafu katika paa la nyumba hiyo, mbali na vyote hivyo, mlango wake ulikuwa mbovu kiasi kwamba kama ungeuegemea tu basi ungeanguka nao mpaka ndani.
Alibaki nje huku akiwa amesimama tu, hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya kama ni kwenda kugonga au kusubiri mpaka msichana huyo atokea.
Huku akiwa mahali hapo na mawazo mengi, akamuona msichana akija kule alipokuwa huku akiwa na ndoo ya maji kichwani mwake. Akamwangalia msichana huyo vizuri, hakutaka kujipa maswali mengi kwamba alikuwa nani, alikuwa Naseku.
“Naseku!!!” aliita huku akianza kumfuata msichana huyo ambaye aligeuka, alipomuona Cassian, akashtuka.
“Cassian!”
“Naam!”
“Umefuata nini?”
“Nimekufuata wewe!”
“Umenifuata mimi?”
“Ndiyo!”
“Hadi nyumbani?”
“Ndiyo!”
“Nani alikwambia ninapoishi!”
“Kazini kwako! Naweza kukaa nawe sehemu kuongea na wewe?”
“Hapana! Nataka kwenda kupika. Mama yangu ni mgonjwa, inatakiwa nimpikie!” alisema Naseku huku akimwangalia Cassian.
“Anaumwa nini?”
“Ni habari ndefu.”
“Habari ndefu ambayo haisimuliki?”
“Cassian! Naomba uondoke. Kaka yangu mkali sana, akikuona hapa, atakushikia panga!” alisema Naseku.
“Anishikie panga! Mimi?”
“Cassian! Naomba uondoke. Tutaonana kesho kazini! Nakuomba,” alisema Naseku.
“Kuondoka siondoki!”
“Oscar atakukuta!”
“Acha anikute! Kama kunikata mapanga, bora anikate lakini hapa siondoki! Kama ni treni ishafika Kigoma,” alisema Cassian, hapohapo akaenda kibarazani kwa kina Naseku na kukaa kabisa.
Naseku hakujiamini, alikuwa akiogopa, alimjua kaka yake, alikuwa mtemi Tandale nzima, alikuwa mtu wa kushika panga, hakupenda kuona mwanaume yeyote akimmendea dada yake, alijua wanaume wengi walikuwa wadanganyifu.
Aliwakata mapanga wanaume wengi, walimuogopa na kumuona Naseku kama ukoma, hakukuwa na mtu aliyemsogelea. Naseku alimwambia hilo Cassian lakini hakutaka kujali, hakutaka kusikia kitu chochote kile, kwake alichokuwa akikitaka ni kuzungumza na msichana huyo tu.
Wakati Naseku akiwa amepeleka ndoo ya maji ndani, mara Oscar akaanza kuonekana kwa mbali, kama kawaida yake alikuwa akija kwa kasi ya ajabu, alikwishatoa onyo kwamba hakutaka kumuona mwanaume yeyote nyumbani kwao, kitendo cha kumuona Cassian alijua kabisa alifika nyumbani hapo kwa ajili ya dada yake tu.
Alipomfikia Cassian, hakutaka kuuliza alikuwa nani, akalipandisha shati lake, akatoa panga. Watu wote waliokuwa wakimuona wakajua kabisa kwamba Oscar hakuwa akitania, hakuwa na historia ya kurudisha panga pasipo kufanya kazi.
Cassian alibaki akimwangalia mwanaume huyo aliyeonekana kuvimba kwa hasira. Hapohapo akamrushia Cassian panga, bila kukwepa lilikuwa likimpiga kichwani.
“Umekwepa! Unajiona ninja!” alisema Oscar na kuanza kumsogelea tena, kitendo cha Cassian kukwepa panga lake ilionekana kuwa kama dharau kwani tangu awe mtemi wa mtaa, hakukuwa na mtu aliyewahi kulikwepa panga hilo.

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA TATU


Bila Naseku kuingilia kati basi hali ya Cassian ingekuwa mbaya mahali hapo. Oscar alionekana kukasirika, ilikuwa ni afadhali kucheza na maisha yake lakini si kucheza na dada yake huyo aliyeonekana kuwa kila kitu.
Watu waliokuwa pembeni baada ya kuona Naseku amemzuia mwanaume huyo nao ndiyo wakaingilia na kumzuia. Oscar alikuwa akiongea peke yake huku akiwataka watu hao wamuachie ili amuonyeshee mwanaume huyo kwamba alikuwa mtu hatari aliyekuwa akiheshima katika mtaa huo.
Muda wote huyo Cassian hakuongea kitu, alibaki akiashangaa tu, mambo aliyokuwa akiyafanya mwanaume huyo yalimshangaza lakini akazuia hasira zake kwani kama angeamua kumpoteza kijana huyo, ilikuwa ni kuongea mara moja tu na wasingemuona tena katika dunia hii.
“Mbona mnanishika! Mbona mnagombelezea bhana?” aliuliza Oscar huku akiwa ameshikwa huku na kule.
“Tulia kwanza! Utaua!”
“Mimi nataka niue sasa! Hawa mbung’o ni kuwaua tu! Kwenda kwao kuwapigia misele dada zao hawataki! Jamani si mniache! Mbona mnanishika kama mtoto wenu,” alisema Oscar huku akionekana kuwa na hasira sana.
Naseku ndiye aliyemtuliza zaidi kaka yake na kumwambia kwamba mwanaume huyo hakuwa mtu mbaya, alikuwa mtu mzuri ambaye alifika mahali hapo si kwa lengo la kumtongoza kama walivyokuwa wanaume wengine bali alikuwa hapo kwa ajili ya kumsaidia mama yao.
Kidogo hilo likamfanya Oscar kutulia. Mama yao alikuwa mgonjwa ndani, alikuwa akisumbuliwa na mgonjwa wa miguu kuvimba, alikuwa kitandani mwaka wa pili, kipindi cha nyuma walikuwa wamesumbuka kumpeleka hospitalini lakini kikafika kipindi wakatulia kwani hawakuwa na msaada wowote wa kifedha.
Kidogo Naseku ndiye aliyeonekana kuwa msaada, yeye ndiye aliyekuwa akitafuta pesa kwa ajili ya kumsaidia mama yake na hata kununua chakula cha humo ndani.
Oscar hakuwa akijali, alichokuwa akikiangalia kilikuwa ni ulevi tu. Alikuwa mvuta bhangi na mtafunaji mirungi maarufu hapo Tandale. Maisha yake yaliishia hapo, alijua kabisa kwamba mwisho wa kila kitu ilikuwa ni lazima kufa.
“Kwa hiyo yupo hapa kumsaidia bi mkubwa?” aliuliza Oscar.
“Ndiyo! Wewe kila mtu unayemuona unadhani kaja kunifuata mimi!” alisema Naseku huku akimwachia kaka yake aliyeonekana kunywea.
Hiyo ndiyo ikawa salama ya Cassian. Mpaka kufikia kipindi hicho hakukuwa na mtu aliyegundua kwamba alikuwa yeye. Pale alipokuwa kulikuwa na giza, alizibwa uso na giza lililokuwepo mahali hapo kwani hata Cassian mwenyewe hakumuona vizuri usoni.
Akachukuliwa na kuingizwa ndani, alishangaa kwamba ni kwa namna gani watu walikuwa wakiweza kuishi katika nyumba mbovu kama hiyo. Alibaki akishangaa kila kitu, kulikuwa na harufu mbaya humo ndani, hakukuwa na sakafu ya simenti, kulikuwa na ndoo za maji zilizotobokatoboka.
Hakutaka kujali sana, akapelekwa mpaka katika chumba alichokuwa amelala mama yake Naseku, alikuwa juu ya kitanda huku akiwa amewekewa chandarua kilichokuwa kimetonokatoboka na sehemu nyingine kilikuwa kimeshonwa.
Alichokiona, akashindwa kuvumilia, machozi ya uchungu yakaanza kutiririka mashavuni mwake. Aliumia mno moyoni mwake, mwanamke yule aliyekuwa kitandani alikuwa akiteseka, pale alipokuwa, hakukuwa na kitu kingine alichokuwa akikisubiria zaidi ya kifo tu.
“Tatizo nini?” aliuliza Cassian ambapo Naseku akaanza kusimulia kila kitu huku machozi ya uchungu yakianza kumtoka.
Ilikuwa ni stori mbaya iliyouchoma mno moyo wake. Hakuamini kama kungekuwa na mwanamke ambaye alikuwa amepitia maisha ya kumuumiza kama alivyokuwa amepitia mama yake Naseku.
Mwaka wa pili mfululizo mwanamke huyo alikuwa akiteseka, hakuwa akisimama, wala kutembea, maisha yake yalikuwa kitandani hapo kitu kilichoonekana kumtesa kila siku.
Walimpeleka hospitali lakini baada ya kuambiwa kwamba matatizo yake yangetibiwa kwa shilingi milioni kumi, wakakata tamaa na mwisho wa siku kumuweka ndani wakisubiri siku ifike na kufariki dunia.
Huruma nyingi ikamuingia Cassian kana kwamba aliyekuwa kitandani akiugua alikuwa mama yake wa kumzaa. Hakutaka kuona mwanamke huyo akiendelea kuteseka, kwa kuwa alikuwa akimpenda binti yake kwa moyo wa dhati hakuwa na jinsi kumsaidia mwanamke huyo kwa kuamini kwamba ingekuwa rahisi kwa Naseku kuamini kwamba alikuwa akimpenda.
“Nitamsaidia mama,” alisema Cassian maneno yaliyomfanya hata Oscar kushtuka.
Hayo ndiyo yalikuwa maneno yake, hakutaka kusubiri, hapohapo akachukua simu yake na kumpigia kijana wake ambaye alimtaka kufika hapo mara moja kwa kumpa maelekezo kupitia Oscar. Ni ndani ya dakika kadhaa, kijana huyo akafika nyumbani hapo akiwa na gari ambapo moja kwa moja wakamchukua na kuondoka naye.
Huo ndiyo ulikuwa mwanzo wa maisha yake na msichana Naseku, aliahidi kumsaidia mwanamke huyo, akapelekwa hospitalini ambapo huko matibabu yakaanza kufanyika.
Mwanamke huyo hakuamini kama Cassian alikuwa akimsaidia kwa kiasi hicho, moyo wake ulifurahia na alitamani kusikia mambo mengi kuhusu mtu aliyekuwa akimsaidia.
Kwa kuwa Cassian alitaka kumuonyeshea Naseku kwamba alikuwa akimpenda kwa moyo wa dhati, akawataka kwenda kuishi kwenye jumba lake jingine lililokuwa Mbezi Beach na ile nyumba yao iliyokuwa Tandale kuvunjwa na kuanza kujengwa upya.
Kila mmoja alishangaa, waliijua familia hiyo, ilikuwa miongoni mwa familia choka na masikini iliyokuwa Tandale, sasa iweje nyumba yao ivunjwe na kujengwa upya na wakati hawakuwa na uwezo wowote ule, wengi wakahisi kwamba ilikuwa imeuzwa.
“Mh! Jamani! Hata Oscar haonekani! Hii nyumba waliiuza au?’ aliuliza mwanamke mmoja huku akiangalia mafundi waliokuwa wakiifanya kazi kwa nguvu kubwa, usiku na mchana walikuwa wakihangaika nayo kuhakikisha ndani ya mwezi mmoja kila kitu kiwe kimekamilika.
“Hata mimi mwenyewe nashangaa! Ila tutajua yote hayo,” alisema mwanamke mwingine, hao wawili walikuwa nje wakisukana, kazi yao ilikuwa ni kuongea umbeya, kuwaangalia wakina nani wamepita na nani siku nzima ili wawaseme.
Wakati hayo yote yakiendelea Cassian hakuwa amemwambia Naseku jambo lolote lile, aliamua kunyamaza kwanza, alitaka kuona kwanza akimfanyia mambo mengi mwanamke huyo kama ishara ya kumuonyeshea kuwa alikuwa akimuhitaji kupita kawaida.
Siku zikaendelea kukatika, kule alipokuwa amewaweka, aliwaita wafanyakazi, Oscar na Naseku wakapelekwa katika shule ya kujifunza kuendesha gari na kuwanunulia magari.
Maisha yalibadilika haraka sana, hawakuwa wakiamini walichokuwa wakikipitia, wakati mwingine walihisi kama ni ndoto ambapo baada ya muda fulani wangeamka na kujikuta wakiwa kitandani.
Maisha yalikuwa ya raha, hakukuwa na kulia tena, hakukuwa na machozi tena na baada ya miezi miwili, mama Naseku akapona ugonjwa wa miguu na nyumba ile waliyokuwa wakitengenezewa ikamalizika kabisa.
“Naseku!” aliita Cassian baada ya kipindi kirefu kupita, siku hiyo alitaka kumkumbushia msichana huyo juu ya kile alichokuwa amemwambia nyuma.
“Abee!”
“Umependeza sana! Hakika ninauona uzuri wako kwa sasa. Siwezi kujuta kukuchagua wewe,” alisema Cassian huku akitoa tabasamu pana.
“Nashukuru sana!”
“Kuna kitu nahitaji kukwambia!”
“Kitu gani?”
“Kilekile cha siku zote kwamba ninakuhitaji sana! Ninahitaji nikuoe! Nimekaa na kukufanyia haya yote, ulistahili, ulitakiwa kuwa na maisha ya furaha, ufute machozi yako, uondoe maumivu makali moyoni mwako,” alisema Cassian.
Siku hiyo hakutumia nguvu sana, ilikuwa ni kama kumsukuma mlevi katika mteremko wa mlima. Msichana huyo akakubali kuwa mpenzi wake na hatimaye baada ya mwezi mmoja wakafunga ndoa na kuwa mume na mke.
Ilikuwa ni furaha kubwa kwa kila mmoja, Naseku yule, msichana masikini hatimaye maisha yake yalikuwa yamebadilika na kuwa bilionea mkubwa. Kwa Cassian hicho ndicho kitu alichokuwa akikihitaji, moyo wake ulikuwa na furaha tele, alitaka kuoa na kupata mtoto na mabya zaidi kipindi hicho hakuwa akijua chochote kile kuhusu Evelyne aliyekuwa amemuacha kwa maumivu makali.
“Mume wangu! Sijaziona siku zangu,” alisema Naseku huku akimwangalia Cassian.
“Unasemaje?”
“Sijaziona siku zangu!”
“Hebu rudia tena kwanza! Unasemaje?” aliuliza Cassian huku akionekana kutokuamini.
Wiki mbili tu zilitosha kuonyesha kwamba Naseku alikuwa mjauzito. Cassian hakuamini, kila wakati alikuwa akimwangalia mke wake, hakuamini kama kweli hatimaye alikuwa akienda kuitwa baba.
Alikuwa makini, alihitaji kumpenda mke wake kwa mapenzi ya dhati, alihitaji kumpa kila kitu alichokuwa akikiihitaji. Baada ya miezi minne wakaenda kupima ili kuona jinsi ya mtoto aliyekuwa naye Naseku tumboni.
“Hongereni sana! Mkeo ana mimba ya watoto mapacha,” alisema daktari huku akimwangalia Cassian.
“Unasemaje? Mapacha? Wa kiume wa kike?” aliuliza Cassian huku akionekana kutokuamini.
“Wa kiume.”
“Nashukuru sana!”
Hiyo ndiyo ilikuwa furaha yake, hakuacha kwenda kliniki na mkewe, mara kwa mara walikuwa wakienda huku wakati mwingine wakitumia utra-sound kuangalia jinsi watoto walivyokuwa tumboni mwa mke wake.
Siku ziliendelea, wakati Naseku akiwa amefikisha miezi saba ya ujauzito wake ndiyo hali ya tofauti ikaanza kuonekana kwa mapacha hao. Siku hiyo walikwenda kupima kama kawaida, kuwaangalia watoto waliokuwa tumboni kuona walikuwa wakiendeleaje. Baada ya kuwapiga picha, dokta alionekana kuwa tofauti na siku nyingine na hata ile karatasi ngumu ambayo ingeonyesha jinsi watoto walivyokuwa tumboni hakutaka kuwaonyeshea.
“Kuna nini?” aliuliza Cassian.
“Mmh!” aliguna tu daktari.
“Hebu tumabie kuna nini! Hebu nione hiyo karatasi,” alisema Cassian huku akijaribu kuichukua karatasi hiyo ngumu kutoka mkononi mwa daktari.
“Subiri kwanza!”
Cassian hakutaka kukubali, hapohapo akampokonya daktari karatasi ile ngumu na kuanza kuiangalia. Macho yake yalipotua kwenye karatasi ile hakuamini alichokiona, ghafla tu machozi yakaanza kumtoka, akapiga magoti chini na kuanza kulia kama mtoto.
“Mume wangu kuna nini?” aliuliza Naseku huku akimwangalia mume wake, naye mwenyewe alitaka kuiona karatasi hiyo, cha kushangaza mumewe akamzuia, hakutaka kuiona.
“Hapana! Hebu niambie kuna nini! Watoto wamekufa au? Lakini mbona nawasikia wakichezacheza! Niambie kuna nini,” alisema Naseku huku akihitaji kuiangalia karatasi hiyo ambayo Cassian hakutaka kabisa kumuonyeshea kwa kuamini kwamba angeumia sana kitu ambacho hakutaka kuona kikitokea.

Naseku hakutaka kuelewa kitu, aliamini kabisa kulikuwa na tatizo kwa watoto wake na hivyo kutaka kuangalia kile kilichokuwa kimepigwa tumboni mwake, hali ya watoto wake kwani alichohisi ni kwamba walikuwa wamefariki dunia.
Bado Cassian alikataa, msimamo wake ulikuwa uleule, alijua kwamba kama mke wake angekiona kile kilichokuwa kimetokea kwa mapacha wake basi angeumia kupita kawaida.
Naseku hakukubali, bado alihitaji kuona tena huku akilia kabisa kitu kilichomfanya Cassian kumpa karatasi ile ngumu na kuangalia kilichokuwa kikiendelea.
Hakuamini, watoto wake mapacha waliokuwa tumboni mwake walikuwa na kila dalili za kuungana. Moyo wake ulimuuma mno, hakuamini alichokuwa akikiangalia lakini wakati mwingine alihisi kwamba hata kama wangeungana, bado wangeweza kuwatenganisha kwa kuwa tu walikuwa na pesa.
Hiyo ndiyo hali iliyokuwa imetokea, kila mmoja alihuzunika mno, mioyo yao iliuma, ilichoma kupita kawaida. Wakakumbatiana na kumshukuru Mungu kwa kuamini kwamba kila kitu kilichokuwa kikitokea, Mungu alikipanga na kamwe hakukuwa na mtu wa kufanya vinginevyo.
Mara kwa mara walikuwa wakifika hospitalini hapo kwa ajili ya kuangalia watoto wao ambao bado hawakuwa wamezaliwa, Cassian alikuwa na muda mwingi wa kuangalia picha za mapacha walioungana kama watoto wake ambao hawakuzaliwa, alitaka kuangalia maisha yao, waliishi vipi na hata mavazi yao yalikuwaje.
Hapo ndipo akaamua kuwafuatilia mapacha wa aina hiyo, Abby na Brittany Hansel waliokuwa wakiishi nchini Marekani. Kila alipoziangalia picha za mapacha hao moyo wake ulimuuma, hakuamini kama kweli Mungu aliamua kumpa watoto wa namna hiyo na wakati alikuwa amemuomba kwa kipindi kirefu mno.
“Mungu! Kama Abby na Brittany wanaishi, nina uhakika hata watoto wangu wataishi pia,” alijisemea Cassian huku akiangalia picha za mapacha hao, hakuishia hapo tu bali aliangalia za wengine wengi ambao wote kwa pamoja walimgusa sana moyoni mwake.
Siku zikaendelea, Naseku hakuonekana kuwa na furaha, muda mwingi alionekana kuwa na huzuni mno. Mama yake alitumia muda mrefu kumtia moyo, hakuataka kumuona akiwa kwenye hali hiyo kila siku.
Ukiachana na mama yake, pia Cassian alikuwa na kazi kubwa ya kumfariji, alimsisitizia kwamba kila kitu kiilichokuwa kikiendelea ni kwamba Mungu alipanga iwe hivyo, hakutaka kumkatisha tamaa, inawezekana katika mapacha hao kungekuwa na rais wa Tanzania.
“Hutakiwi kulia mpenzi,” alisema Cassian huku akimwangalia mke wake aliyekuwa kwenye maumivu makali.
“Inaniuma sana!”
“Ni bora kupata watoto kuliko kukosa kabisa. Usihuzunike, kuwa na mapacha walioungana si kwamba ndiyo mwisho wa kuishi, bado maisha yanaendelea kama kawaida mke wangu,” alisema Cassian huku akimkumbatia mke wake huyo.
Siku na miezi ziliendelea kukatika mpaka Naseku alipofikisha miezi tisa na hivyo kujisikia uchungu na kwenda kujifungua katika Hospitali ya Ocean Road.
Siku hiyo Cassian alikuwa na presha kubwa, hakuamini kama angekwenda kuwa baba. Moyo wake ulibadilika, huzuni kubwa aliyokuwa nayo tangu agundue kwamba mke wake angejifungua mapacha walioungana ikatoweka na furaha ya ajabu kumuingia moyoni mwake.
Alikuwa nje ya chumba cha kujifungulia akiwa na wazazi wake, hakukaa chini, alikuwa amesimama huku kila wakati mikono yake ikiwa imekutanishwa kana kwamba alikuwa akisali.
“Dad! I am going to be a father, can you believe that?” (nakwenda kuwa kuwa baba, unaweza kuamini hilo baba?) aliuliza Cassian huku akiwa na tabasamu pana usoni mwake.
“I am so proud of you my son!” (najivunia wewe sana kijana wangu)
“They are conjoined twins. It doesn’t matter, I just want to see them,” (ni mapacha walioungana. Haijalishi, ninataka kuwaona tu) alisema Cassian huku kila wakati akiusogelea mlango wa chumba kile na kutegesha sikio lake.
“Come and give me a hug,” (njoo unikumbatie) alisema mama yake ambaye alisimama na kukumbatiana na kijana wake.
Waliendelea kusubiri mpaka baada ya dakika hamsini ambapo mlango ukafunguliwa na daktari kuwaambia kwamba walishindwa kufanya kazi yao ndani kwani ilishindikana kabisa Naseku kujifungua kwa hali ya kawaida kwani watoto hao walikuwa wawili kwa pamoja na njia ilikuwa ndogo.
Hawakuwa na jinsi, wakakubaliana na hali iliyokuwepo hivyo Naseku kujifungua kwa njia ya upasuaji kitu ambacho kilifanikiwa kwa asilimia mia moja. Moyo wa Cassian ukawa na furaha tena, hakuamini kama kweli siku hiyo aliitwa baba baada ya miaka mingi kupita.
Hawakuruhusiwa kumuona Naseku wala watoto siku hiyo, waliambiwa wasubiri mpaka siku mbili zipite ndiyo wangepewa nafasi ya kuwaona watoto hao.
Nyumbani, hakukukalika kwa amani, muda wote Cassian alikuwa akitamani kuwaona watoto wake. Aliwaita watu wa kudesign nyumba na kuweka katika staili ya kitoto na kumkaribisha mke wake, nyumba ilipendeza, kulikuwa na kila kitu ambacho mtoto alitakiwa kuwa nacho, kitanda kikubwa, midoli na vitu vingine vingi.
Hakwenda kazini, muda mwingi alikuwa akishinda hospitalini kuliko hata nyumbani. Baada ya siku mbili, akaruhusiwa kumuona mke wake, macho yake yalipotua kwa mwanamke huyo tu, uso wake ukawa na tabasamu pana, alimwangalia, alikuwa mwanamke aliyemfanya kujiona mwanaume aliyekamilika, akamsogelea mahali pale na kumshika mkono, hapohapo Naseku akafumbua macho yake na kuangaliana.
“Mke wangu...” aliita Cassian huku akimwangalia mke wake aliyekuwa akitabasamu tu.
Moyo wake ukafarijika, akajisikia amani moyoni mwake kuliko kipindi chochote kile. Hapohapo manesi wakamletea watoto wake waliokuwa katika chumba kingine kabisa, alipowaona, japokuwa walikuwa wameungana maeneo ya kichwani, upande wa kulia kwa mtoto mmoja na kushoto kwa mwingine lakini moyo wake ulisikia furaha ya ajabu ambayo hakuwahi kuisikia kabla.
“Watoto wangu!” alisema Cassian huku akiwachukua, machozi ya furaha yalikuwa yakimtoka.
Walikuwa watoto wazuri wa kiume waliochukua sura yake, walikuwa wadogo lakini aliwaona jinsi alivyokuwa amefanana nao. Alitabasamu, alicheka kwa furaha, akamuinamia mke wake na kumbusu shavuni.
“Nashukuru kwa kunipa watoto na kunifanya niwe mzazi,” alisema Cassian huku akimwangalia mkewe, alishindwa kumshukuru vipi mke wake huyo.
Naseku hakujibu kitu chochote zaidi ya kuachia tabasamu pana. Moyo wake ulifurahia, aliwapenda watoto wake, hakuangalia namna walivyokuwa, kwake, hao walikuwa kila kitu katika maisha yake.
Waliendelea kukaa hospitali hapo kwa siku mbili zaidi na ndipo wakaruhusiwa huku Cassian akiwa amewapa watoto wake majina ya Walter na Walker.
Walikuwa na sura nzuri, kila mtu aliyekuwa akifika nyumbani na kuwaangalia, alidiriki kusema kwamba Walter na Walker walikuwa na sura nzuri mno. Kila mtu akawapenda, watu wengi wakasikia habari zao na kutaka kwenda huko kuwaona.
Wengine walimfuata Cassian na kumshauri kwamba alitakiwa kutumia kiasi cha fedha kuwapeleka watoto hao nchini India kwa ajili ya kutenganishwa lakini alikataa, katika maisha yake aliamini kitu kimoja tu kwamba Mungu anaporuhusu jambo fulani kutokea, huruhusu kwa kusudi maalumu.
“Kuungana si tatizo! Mungu aliamua iwe hivyo, kwa nini sisi wadamu tupingane naye?” aliuliza Cassian kila alipokuwa akiambiwa mambo ya kuwatenganisha watoto wake.
Walikuwa watoto wenye afya tele ambao waliungana vichwa vyao. Kwa jinsi walivyokuwa wameungana, hata kama Cassian angekubaliana na kila mtu kwenda kuwatenganisha ingeshindikana kabisa kutokana na watoto hao kuchangia ubongo.
Pale walipokuwa wameungana kulikuwa na mishipa mikubwa, mingi iliyokuwa ikipitisha damu, kitendo cha kuwatenganisha kilimaanisha kwamba ni lazima mishipa hiyo ikatwe na sehemu ya ubongo ambao walikuwa wakitumia pamoja iondolewe kitu ambacho kingemaanisha kifo chao.
Lilikuwa jambo gumu mno kuwatenganisha, Cassian alikubaliana na kila kitu, alikuwa tayari kuwaona watoto wake wakiendelea kukua kwenye hali ile kuliko kuwatenganisha au kuwaua wote.
Watoto waliendelea kuwa kwenye uangalizi mkubwa mpaka baada ya kufikisha miezi miwili ambapo wazazi hao wakaamua kuanza kutafuta mfanyakazi kwa ajili ya kuwaangalia watoto hao.
Kitu cha kwanza kabisa walitaka kwenda kijijini kuchukua msichana wa kuwaangalia watoto hao lakini baada ya siku nne, Cassian akapigiwa na mjomba wake, Marcus ambaye alimwambia kwamba angewapa mfanyakazi mzuri kwa ajili ya kukaa na watoto hao.
“Anajua kutunza watoto?” aliuliza Cassian.
“Hilo si swali! Alimtunza Jackson na Careen mpaka walipoanza kuongea,” alijibu mjomba huyo, wakati huo walikuwa wakiongea uso kwa uso.
“Nashukuru sana! Naomba uniitie huyo msichana, nitamlipa kiasi chochote kile,” alisema Cassian.
“Hakuna shida.”
***
Ilikuwa ni rahisi kwa Evelyne kusahau kila kitu kilichotokea katika maisha yake, kusahau tarehe ya siku yake ya kuzaliwa, kuwasahau watu waliomtendea mabaya kuliko kumsahau Cassia na mambo yote aliyokuwa ameyafanya.
Ilikuwa ni aibu kubwa, hakutoka ndani, kila alipokuwa chumbani kwake alikuwa mtu wa kulia tu, alihuzunika, aliumia moyoni mwake na wakati mwingine alihisi kwamba ilikuwa ni afadhali kujiua kuliko kuendelea kuishi.
Rafiki yake, Mwajuma ndiye aliyekuwa karibu naye, yeye ndiye aliyekuwa akimbembeleza usiku na mchana na hata msichana huyo alipotaka kufanya maamuzi magumu ya kutaka kujiua, Mwajuma alikuwa akimuokoa, alifanya hivyo mara tatu kwa nyakati tofauti.
Alimchukuia Cassian, aliilaani siku aliyokutana na mwanaume huyo, aliwachukia wanaume wote duniani hata kama wengine hawakumfanya kile alichofanyiwa na Cassian. Alilia sana, alihuzunika mno na moyo wake kuchomwa na kitu cha moto kilichokuwa na ncha kali.
Siku zikakatika, alijiapiza kwamba ilikuwa ni lazima kulipiza kiasi kwa Cassian, kama alikuwa amemuumiza kwa staili ile na yeye ilikuwa ni lazima kumuumiza kwa pigo lenye maumivu kama lile.
Kwa mwaka mzima alikuwa chumbani, ni mara chache tu ndizo alizokuwa akitoka ndani, tena usiku, kila alipokuwa akipita kwenye mitandao ya kijamii, watu walimcheka, walimdhihaki kwa kile kilichokuwa kimetokea na hivyo moyo wake kubaki na kidonda kikubwa ambacho hakudhani kama kuna siku kingekuja kupona.
Mwajuma ndiye aliyekuwa akifuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea, yeye ndiye aliyemwambia Cassian kwamba alikuwa amepata mwanamke mwingine, wa uswahilini, asiyejua hata thamani ya dola ya Kimarekani kwa pesa ya Kitanzania.
Moyo wake ulichoma zaidi, kidonda kikatoneshwa, maumivu yakaongezeka, alizidi kulia na kuomboleza kila siku. Siku zikaendelea kukatika huku Mwajuma akimletea kila kitu kilichokuwa kikiendelea, mpaka aliposikia kwamba mke wa Cassian, Naseku alikuwa amejifungua mapacha walioungana, kidogo moyo wake ukajisikia nafuu kwa kuona kwamba machozi aliyokuwa amemwaga kwa ajili ya mwanaume huyo hatimaye Mungu alikuwa amemlipia.
“Mungu amenilipia, na bado ataendelea kunilipia,” alimwambia rafiki yake, Mwajuma pasipo kujua kwamba huo ulikuwa ni mpango wa Mungu kwa watoto hao kuwa katika hali hiyo.
“Tena sana. Chozi la mwanamke haliendi bure,” alisema Mwajuma pasipo kujua kwamba siku zote machozi ya mwanamke malaya kama walivyokuwa yalikuwa yakienda bure, yaani kama kumwaga maji mtaroni kutoka kwenye ndoo chafu.
Wakajifariji sana, wakazungumza maneno yao ya kujipa nguvu na kujiaminisha kwamba kila kitu kilichokuwa kimetokea kilikuwa ni mpango wa Mungu. Baada ya siku miezi miwili watoto kuzaliwa, Evelyne akapata wazo jingine kwamba hata kama Mungu alikuwa amemlipizia kwa mwanaume huyo kupata watoto walioungana ilikuwa ni lazima kufanya jambo, kuwateka na kuwaua ili Cassian aumie, alie kama alivyokuwa akilia.
Hakujua ni kwa namna gani angeweza kuwapata watoto hao. Cassian alikuwa bilionea, mwenye ulinzi mkubwa ambaye kila kona nyumbani kwake kulikuwa na walinzi waliokuwa na bunduki, alijifikiria sana na baada ya kumtuma Mwajuma kumchunguza kwa undani zaidi, akagundua kwamba familia hiyo ilikuwa ikitafuta mfanyakazi wa ndani wa kukaa na watoto.
“Unasema kweli?” aliuliza Evelyne huku akionekana kutokuamini.
“Ndiyo shoga yangu!”
“Hii ndiyo nafasi yangu!” alijisemea.
Alikuwa na pesa, akaunti yake ilikuwa na milioni tisini, alichuma pesa hizo kwa Cassian, zilikuwa ni zaidi ya milioni mia moja na ishirini ila kwa matumizi ya mwaka mzima zikabaki hizo.
Alitaka kutumia sehemu ya pesa hizo kumuumiza Cassian, kitu alichokifanya ni kuwatafuta vijana watatu kutoka katika Kundi la Fogo lililokuwa na maskani yake Tandale na kuwaambia kwamba alitaka kuona watoto wa mzee mmoja wakitekwa.
“Mzee gani?”
“Anaitwa Marcus!”
“Anaishi wapi?”
“Mbezi Beach.”
“Hakuna shida.”
Akawaelekeza namna ya kuwapata watoto hao, haikuwa kazi kubwa, akawaelekeza shule waliyokuwa wakiishi, gari lililokuwa likielekea shuleni kuwachukua, gari hilohilo lilitakiwa kutekwa.
Ilikuwa ni kazi ndogo sana, watu hao waliokuwa na bastola ambao walitumwa kufanya kazi hiyo kwa malipo ya shilingi milioni kumi wakaanza kufuatilia, ni ndani ya siku mbili tu, tayari watoto wake, Jackson na Careen wakatekwa na hivyo kupigiwa simu.
“Jamani naomba msiwaue,” alisema Mzee Marcus huku akionekana kuogopa.
“Wala usijali! Ukifanya tunachokitaka, hawatokufa, ila usipokifanya, tutaviweka vichwa vyao kwenye boksi na kukutumia,” alisikika mwanaume upande wa pili wa simu.
“Jamani naomba msifanye hivyo! Nitawapendi kiasi chochote cha pesa,” alisema Mzee Marcus.
“Hatuhitaji pesa, tunahitaji kuonana na wewe. Ukishindwa, tunawaua, au ukiwapa taarifa polisi, ndiyo kabisa tunawatumbukiza kwenye pipa la tindikali na hutoona hata maiti zao,” aliskika mwanaume huyo.
“Basi sawa. Tuonane, tuyapange na tutakuachia watoto wako wakiwa wazima wa afya,” alisema mwanaume huyo.
“Wapi?”
“Tandale Sokoni, kesho saa saba mchana, pembeni ya kijana anayeuza mihogo, utamuona amevaa fulana iliyoandikwa Big Man kifuani. Zingatia muda, ukichelewa, tusilaumiane. Saa saba mchana kumbuka,” alisema mwanaume huyo na kukata simu.

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA NNE.


Mzee Marcus alikuwa kwenye mawazo mengi, hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya. Alihisi kwamba watu hao walihitaji pesa lakini wazo hilo lilifutika kichwani mwake kwani kama kweli walikuwa wakihitaji pesa ilikuwa ni lazima wamwambie kwamba alitakiwa kwenda na pesa zao kabisa.
Siku iliyofuata mapema tu alifika Tandale Sokoni, kulikuwa na watu wengi na ilikuwa vigumu kwa mtu kama yeye kugundua ni mahali gani walipokuwa wakiuza mihogo. Akaulizia mahali kulipokuwa kukiuzwa mihogo, akaambiwa na kwenda huko.
Macho yake yalikuwa yakiangalia huku na kule, aliogopa, kulikuwa na watu wengi kiasi kwamba hakujua mwema alikuwa yupi na mbaya yupi. Alipoendelea kuangalia huku na kule macho yake yakatua kwa mwanaume aliyekuwa akiuza mihogo ambaye alivalia fulana ya Bluu iliyoandikwa Big Man kifuani.
“Yule pale.”
Akaanza kumsogelea kijana yule na kumsalimia. Ilionekana kama kijana yule hafahamu kitu chochote kile, kwani baada ya kuitikia salamu ile, akaendelea na mambo yake kama kawaida.
Mzee huyo alisimama kwa dakika kadhaa, mara mwanaume mmoja akafika mahali hapo akiwa na pikipiki, akaisimamisha na kumwambia apande ili aondoke naye.
“Watoto wangu wapo wapi?” aliuliza hata kabla ya kupanda kwenye pikipiki ile.
“Wewe twende! Au hutaki?” aliuliza mwanaume huyo, haraka sana mzee huyo akapanda na kuondoka mahali hapo.
Mwendo ulikuwa ni wa kasi, wakaondoka kwa kupitia barabara iliyokuwa ikielekea Kwa Mtogole, walipofika kwenye msikiti wa Bi Mtumwa, wakachukua njia upande wa kulia na kwenda sehemu ambayo ilikuwa na kibanda cha wauza mkaa.
Walikwenda kwa mwendo wa kawaida mpaka wakaingia kwenye kichochoro ambacho ilikuwa ni vigumu sana kuona kama pikipiki ingeweza kupenya, wakaingia na kwenda mbele ambapo ikasimama mbele ya nyumba moja chakavu, wakateremka.
Akaingizwa ndani ya nyumba hiyo, akakutana na vijana watatu waliokuwa na bastola, wakamuamrisha kukaa chini na kumwambia kwamba kulikuwa na kitu alichotakiwa kufanya.
Wakamwambia kwamba watoto wake walikuwa wazima kabisa na ili kumridhisha wakamuonyeshea picha za watoto hao ambao walikuwa wamefungwa vitambaa.
“Naomba msiwaue,” alisema mzee huyo huku akitetemeka.
“Hilo si tatizo! Unachotakiwa ni kufanya tunachotaka ukifanye,” alisema mwanaume mmoja.
Wakaanza kumwambia kile walichokuwa wakikihitaji. Alihitajika kumwambia Cassian kwamba atafute dada wa kufanya kazi za ndani ambaye huyo ndiye angekaa na watoto aliokuwa amewapata na msichana huyo hakuwa na sababu ya kumtafuta kwani walitaka kumpa wao wenyewe.
“Jamaniiii!”
“Kama hutaki basi tuwaue!”
“Naomba msiwaue!”
“Basi fanya tulichokwambia!”
Wakamwambia zaidi jinsi hali ilivyotakiwa kufanywa. Hakutakiwa kubisha, ili watoto wake wawe salama ilikuwa ni lazima kufanya kile ambacho watu hao walimtaka kukifanya. Wakakubaliana na kuondoka huku akiacha namba ya simu.
Siku iliyofuata, akapata ugeni, alikuwa msichana mwenye sura mbaya ambaye ndiye huyo aliyetakiwa kutumwa kwa Cassian kwa ajili ya kufanya kazi za ndani kumbe lengo kubwa likiwa ni kuwateka watoto hao na kwenda kuwaua.
Akampigia simu Cassian, aliongea naye kwa kirefu, akamsifia msichana huyo kwamba alikuwa mtu safi, aliyewalea watoto wake mpaka kukua. Cassian hakuwa na hofu, alimwamini Mzee Marcus na hivyo kuhitaji kuonana na msichana huyo.
Alipomuona tu, kwa jinsi alivyokuwa, akahisi kwamba kweli huyo alikuwa mfanyakazi wa ndani na hivyo kumkaribisha kwa mikono miwili.
“Unaitwa nani?”
“Sikujua!”
“Ooh! Sawa. Karibu sana mama!” alimkaribisha Cassian.
Hakukuwa na mtu aliyegundua kwamba mwanamke huyo alikuwa mbaya, wakatokea kumwamini, kila siku ilikuwa ni lazima wampe majukumu yote ya kuwalea watoto hao kitendo kilichomfanya kuwa karibu na watoto hao.
Kila siku asubuhi walikuwa wakiondoka kuelekea katika majukumu yao, nyumbani alikuwa akibaki msichana huyo na watoto hao tu pamoja na walinzi waliokuwa wakilinda mahali hapo.
Siku zilikatika, watoto wao walikuwa furaha yao kubwa, waliendelea kuwapenda, na kila siku walipokuwa wakirudi, kitu cha kwanza kilikuwa ni kuwajulia hali.
“Oh! My kings!” (Oh! Wafalme wangu) alisema Cassian huku akiwaangalia, hapohapo akaanza kuwamwagia mabusu mfululizo.
Wakati hayo yote yakiendelea Evelyne alikuwa akifuatilia kwa karibu, mara kwa mara alikuwa akiwapigia simu watu hao na kuwauliza ni kitu gani kilichokuwa kikiendelea. Aliwalipa pesa zote na kilichokuwa kikisubiriwa ni kimoja tu, watoto hao watekwe na kuwaua kwa mikono yake.
“Mmefikia wapi?” aliuliza Evelyne.
“Hadija yupo ndani ya nyumba!”
“Sawa. Amekwishawateka?”
“Wewe unataka watekwe lini?”
“Hata kesho!”
“Haina shida!”
Kule ndani alipokuwa, msichana yule alikuwa na simu yake ndogo ambayo hakukuwa na mtu yeyote aliyekuwa akiiona, hiyo ndiyo aliyokuwa akifanya mawasiliano na wenzake waliokuwa wamempa kazi hiyo.
Aliambiwa kitu gani alitakiwa kufanya. Mipango ilikuwa imekamilika na kilichokuwa kikisubiriwa ni yeye kuwateka watoto hao na kuondoka nao.
Siku ambayo alitaka kufanya tukio hilo, akasubiri mpaka Cassian na mkewe waondoke nyumbani, walipofanya hivyo, saa 3:00 asubuhi akaelekea chumbani kwao, akachukua ufunguo wa gari aina ya Range SUV nyekundu na kwenda kufungua.
Mlinzi mmoja aliyekuwa mahali hapo alishangaa, haikuwa kawaida kwa mfanyakazi huyo kufungua mlango wa gari lolote lile, hakutaka kusubiri kuambiwa, akamfuata msichana huyo kwa lengo la kuzungumza naye.
“Sikujua!” aliita mlinzi huku akimsogelea.
“Naam kaka!”
“Vipi tena?”
“Vipi kuhusu nini?”
“Mbona unafungua gari. Kuna lolote?” aliuliza mlinzi huku akimwangalia msichana huyo.
“Nataka niwapeleke hospitali. Mama aliniachia maagizo nifanye hivyo!” alisema Sikujua.
“Uwapeleke hospitali! Eeh! Tangu lini umeanza kuwapeleka hospitali?” aliuliza mlinzi huyo huku akionekana kushangaa sana.
Sikujua hakutaka kujibu hilo, akatoka hapo, akaingia ndani ambapo akawachukua watoto hao, akawaingiza ndani ya gari na kuondoka nao.
Mlinzi alibaki akiashangaa. Kwanza hakuamini kama msichana huyo alikuwa akiwapelekea hospitalini lakini kilichomshangaza kabisa, iliwezekanaje msichana kama Sikujua ambaye kwa muonekano tu hakuonekana hata kujua kupiga honi ya gari awe anaendesha gari?
“Mmh!” aliguna mlinzi.
Hakutaka kubaki kimya, alichokifanya ni kumpigia simu Cassian. Mwanaume huyo aliyekuwa ofisini alipoona simu ya mlinzi wa getini ikiingia, akaanza kuogopa, haikuwa kawaida, akili yake ilimwambia kwamba inawezekana kulikuwa na tatizo limetokea nyumbani.
Kabla ya kuipokea akaanza kujiuliza maswali mengi yasiyokuwa na majibu kwamba kabla ya kuondoka nyumbani kulikuwa na jambo baya gani lililokuwa limetokea nyumbani? Hakuna! Sasa kwa nini mlinzi huyo alikuwa akimpigia simu? Kulikuwa na nini? Akapiga moyo konde na kupokea simu.
“Hamisi! Kuna nini?”
“Eti ulimwambia Sikujua awapeleke hospitalini watoto?” lilikuwa swali la kwanza kabisa, swali ambalo lilimshtua mno Cassian.
“Unasemaje?”
“Sikujua kawapeleka watoto hospitalini. Kachukua gari na kuondoka nalo huku watoto wakiwa humo,” alisema Hamisi maneno ambayo yalimfanya Cassian kuinuka kwenye kiti huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Unasemaje?” aliuliza, akasimama, mwili ulikuwa ukimtetemeka na kijasho chembamba kumtoka.

Cassian hakuamini alichokuwa amekisikia kutoka kwa mlinzi, alimuuliza tena na tena na jibu lilikuwa lilelile kwamba dada wa kazi za ndani, Sikujua aliyekuwa akimwamini sana aliondoka na watoto nyumbani kwake, na alipokuwa ameelekea, hakukuwa na aliyepafahamu.
Alichanganyikiwa, haraka sana akakata simu na kuwapigia polisi, alipowapa taarifa, wakamwambia kwamba wangefika nyumbani kwake kwa ajili ya kuzungumza, ilikuwa ni lazima wajue ni kitu gani kilitokea mpaka mfanyakazi huyo kuondoka na watoto.
Yeye mwenye akaondoka ofisini, hakutaka kumpigia simu mke wake kwa kuona kwamba angemchanganya, ilikuwa ni lazima apambane yeye kama yeye kuona ingekuwaje ndipo amwambie mkewe kilichokuwa kimetokea.
Njiani, alionekana kuwa na mawazo mengi, alishindwa kabisa kuyazuia machozi kumtoka, moyo wake uliuma na kuchoma, kile kilichokuwa kimetokea kilikuwa kama ndoto kwake, hakuamini kama Sikujua angeweza kufanya kitu kama hicho.
Hakuchukua muda mrefu akafika nyumbani kwake, hakuliingiza gari, akateremka na kumfuata mlinzi, hata kabla hajamfikia tayari polisi wakafika mahali hapo na wote kumfuata mlinzi ambaye alianza kuhadithia kila kitu kilichokuwa kimetokea.
Ulionekana kuwa uzembe mkubwa, ilikuwaje nyumbani kwa bilionea mkubwa kama Cassian kutokee na mfanyakazi kufanya jambo kama hilo, utekaji uliokuwa umefanyika ulikuwa ni wa kizembe sana ambao hawakuamini kama ungeweza kutokea sehemu yoyote ile.
“Inawezekana vipi?” aliuliza polisi mmoja, maelezo ya mlinzi yalionyesha tukio hilo lilikuwa la kizembe.
Kila mmoja alishangaa, walihisi kulikuwa na kitu kilichokuwa kimetokea. Walianza na mlinzi, walihisi kwamba alikuwa akijua mambo mengi kuhusu tukio hilo lililokuwa limetokea.
Alijitetea kwa upande wake kwamba hakuwa akifahamu kitu chochote kile na kwa sababu Cassian na Naseku walikuwa wakimwamini sana Sikujua, hakuwa na la kuuliza lolote lile kwa kuamini kwamba kwa kila kitu alichokuwa akikifanya kilikuwa sahihi.
“Nitamwambia nini mke wangu? Huu ni mtihani mkubwa sana kwangu!” alisema Cassian huku akionekana kuumia mno.
Simu zikapigwa, polisi wa kila kituo wakapewa taarifa juu ya kilichokuwa kimetokea. Kitu cha kwanza kabisa ambacho kwao kilionekana kuwa na uhakika wa kujua mahali watoto walipokuwa kilikuwa ni kulitafuta gari lake.
Polisi walikimbizana, kutekwa kwa watoto wa Cassian, bilionea mkubwa ilikuwa ni sawa na kutekwa kwa watoto wa rais. Polisi wakaondoka katika vituo vyao na kuingia mitaani, wakasaidiana na trafki kulitafuta gari hilo.
Hawakutaka watu wengine wafahamu kilichokuwa kimetokea, ulikuwa ni msako wa kimyakimya ambao waliamini kwamba usingeweza kuwashtua watu wengi.
Ilipofika saa 10:15 jioni, gari la Naseku likaanza kuingia mahali hapo. Kwanza hali aliyokutana nayo nyumbani ilimshtua, hakukuwa na mlinzi, geti alifunguliwa na mume wake, alibaki akijiuliza maswali mengi pasipo majibu yoyote yale.
Alimfahamu Cassian, alikuwa mwanaume mwenye furaha tele lakini kwa siku hiyo alivyokuwa akimwangalia alionekana kabisa kuwa na kitu kilichokuwa kikimtatiza moyoni mwake kwani hata tabasamu ambalo alijitahidi kumuonyeshea lilionekana kutokutoka moyoni mwake.
“Mume wangu! Kuna nini?” aliuliza Naseku huku akionekana kuwa na hofu kubwa.
“Hakuna kitu!” alijibu Cassian.
“Unajua ni kwa jinsi gani sipendi kudanganywa mpenzi. Niambie kuna nini! Hata kama kuna kitu kinachouma mno, wewe niambie tu kwanza,” alisema Naseku huku akimwangalia mume wake huyo ambaye bado hakuonyesha furaha yoyote ile.
“Tuingie ndani kwanza!”
“Hakuna tatizo?”
“Hakuna!”
“Na mlinzi yupo wapi?”
“Tuingie ndani, tutaongea.”
Cassian akamshika mkono Naseku na kuingia naye ndani ya nyumba hiyo, walipofika sebuleni, macho ya mwanamke huyo yakatua kwa polisi wanne waliokuwa sebuleni. Hilo lilimuogopesha zaidi, akahisi kulikuwa na tatizo kwani haikuwa kawaida kwa polisi kufika nyumbani kwake hapo.
Alitaka kujua, alihisi mapigo yake ya moyo yakiongezeka kudunda, aliogopa, aliyafumba macho yake kwa sekunde kadhaa, akamuomba Mungu amtie nguvu kwa lolote ambalo angelisikia mahali hapo.
“Mke wangu...” aliita Cassian huku akimwangalia Naseku ambaye hakujua kilichokuwa kimetokea lakini cha ajabu kabisa akaanza kulia.
Hakuweza kumwambia mke wake, moyo wake ulimuuma, alijiona yeye kuwa chanzo kwa kile kilichotokea, polisi mmoja aliyekuwa mahali hapo ndiye aliyemwambia Naseku kila kitu kilichokuwa kimetokea.
Mwanamke huyo hakuamini alichokisikia, yaani watoto wake aliowapenda kwa moyo mmoja wawe wametekwa, tena na mfanyakazi wa ndani ambaye walimwamini kupita kawaida?
“Haiwezekani!” alisema Naseku huku akilia.
Ilikuwa kazi kubwa kumbembeleza mwanamke huyo, alilia kwa uchungu mno na ni Cassian ndiye aliyekuwa mfariji wake kwa ajili ya kumbembeleza katika kipindi kigumu kama hicho alichokuwa akipitia.
“Nyamaza mke wangu! Nyamaza bebi,” alisema Cassian huku akiwa amemkumbatia Naseku aliyekuwa akilia kama mtoto mdoo.
“Watoto wangu! Watoto wangu wao wapi?” aliuliza Naseku huku akiendelea kulia m,no.
Wakati wakiwa hapo, polisi wakapigiwa simu na kuambiwa kwamba gari aina ya Range SUV lililokuwa na namba za usajili T768NYC lilikutwa katika Ufukwe wa Coco huku likiwa limetekelzwa, walihisi kwamba kama wangeanzia huko wangejua mahali watoto walipokuwa.
“Tunakuja hukohuko” alisema polisi mmoja. Wakawaambia kilichokuwa kimetokea na hivyo wote kuondoka ndani ya nyumba hiyo. Naseku naye hakutaka kubaki, alitaka kujua kilichokuwa kikiendelea hivyo naye kuungana nao na kuelekea huko.
Njiani, hakuwa amenyamaza, bado aliendelea kulia tu. Hakukuwa na kitu alichokuwa akikipenda moyoni mwake kama watoto wake, alikuwa tayari kupoteza kila kitu lakini si kuwapoteza watoto wake aliokuwa akiwapenda mno.
Hawakuchukua muda mrefu wakawa wamefika katika ufukwe huo ambapo moja kwa moja wakaanza kulifuata gari hilo lililozungukwa na watu wengi ufukweni hapo.
Walipolifikia, wakalisogelea na kuufungua mlango wa mbele huku wakiwa na glovusi mikononi mwao, macho yao yalipotua ndani ya gari hilo hawakuweza kuamini, kulikuwa na damu nyingi katika kiti cha pembeni na nyuma picha ambayo ilionyesha kulikuwa na mauaji yaliyokuwa yamefanyika ndani ya gari hilo.
“Wamewaua watoto wangu...” alisema Naseku na kuanza kulia upya, kilio kikubwa kilichowashtua watu wote waliokuwa mahali hapo.
“Damu! Wamewaua hawa watoto,” alisema polisi mmoja, kama ilivyo kwa Naseku na Cassian, hata na yeye moyo ukaanza kuuma, ulikuwa ni ukatili mkubwa ambao hawakutakiw akufanyiwa watoto wadogo kama hao.

Evelyne alikuwa chumbani kwake, kichwa chake kilikuwa kikimfikiria Cassian ambaye bado aliendelea kuumiza moyo wake kupita kawaida. Maumivu aliyokuwa nayo moyoni mwake hayakuisha na ndiyo maana kitu pekee alichokuwa akikihitaji kwa kipindi hicho ni kuwaua watoto wa mwanaume huyo.
Aliwatuma watu ambao walimwambia kwamba iwe isiwe ilikuwa ni lazima kufanikisha kile alichokuwa kikihitaji. Hilo halikuwa tatizo kwani baada ya siku kadhaa, akapewa taarifa kwamba tayari watoto walikuwa waekwishatekwa.
Moyo wake ukawa na furaha tele, akamwambia Mwajuma kwamba tayari kazi aliyokuwa akitaka kwa kipindi kirefu ilikuwa imekamilika, watoto aliokuwa akiwataka walikuwa mikononi mwake.
Mwajuma akafurahia, akaona kwamba mtihani mgumu waliokuwa nao kipindi chote ukawa umekamilika na kwa kuwa alihitaji rafiki yake awe na furaha tele siku zote, akamwambia kwamba kwamba bado alikuwa naye bega kwa bega.
“Wapo wapi tukawaue?” aliuliza Mwajuma huku akionekana kuwa na hasira kali hata zaidi ya alizokuwa nazo Evelyn.
“Subiri! Wanasema wapo njiani!” alisema Evelyne.
Alichukua simu yake na kuwapigia watu wake kwa lengo la kuwaambia kwamba hawakutakiwa kuwaua watoto hao wao bali walitakiwa kumsubiria kwani yeye ndiye aliyekuwa na jukumu la kuwamaliza kwa mkono wake.
Kila alipokuwa akipiga simu, haikuwa ikipokelewa, moyo wake ulikuwa na presha kubwa, alikuwa na kimuemue ambacho hakuwa nacho kabla. Hakuacha, muda wote alikuwa akiwapigia simu lakini majibu yalikuwa yaleyale kwamba simu haikuwa ikipatikana.
Akahisi kulikuwa na tatizo, akahisi kwamba inawezekana watu hao walikuwa wamemgeuka na ndiyo maana walizima simu zao na hawakutaka kuziwasha kwa ajili yake.
Alihuzunika, ilipofika majira ya saa sita mchana akawapigia tena, wakati huo simu ilikuwa ikiita kuonyesha kwamba iliwasha, alisubiri, haikupokelewa kwa wakakati, alikuwa na hamu kubwa, baada ya sekunde kadhaa, simu ikapokelewa na sauti ya upande wa pili kusikika.
“Samahani simu iliisha chaji,” alisema mwanaume aliyesikika upande wa pili.
“Usijali! Imekuwaje huko?” aliuliza Evelyne.
“Sikujua aliwateka watoto, akaondoka na gari lao kisha kwenda kuwamaliza huko, kisha akaitupa miili yao baharini,” alisema mwanaume huyo.
“Mbona hamkuniambia nije kuwaua mimi mwenyewe?” aliuliza Evelyne huku akionekana kuumia sana.
“Alihisi kwamba alikuwa akifuatiliwa, si unajua yule ni bilionea alikuwa na mkono mrefu! Aliogopa na ndiyo maana aliwamaliza. Ngoja nikutumie picha,” alisema mwanaume huyo na kilichofuata ni kumtumia picha kadhaa zilizoonyesha wingi wa damu na kisu ndani ya gari hilo.
Kwa damu zilizoonekana tu, ilionyesha kwamba ni picha za kusikitisha, hazikuishia picha hizo bali kulikuwa na picha nyingine zilizoonyesha mfuko mkubwa wa nailoni huku ukiwa na damu nyingi kiasi kwamba hata yeye mwenyewe alisisimka.
Kilichokuwa ndani ya mfuko ule aliambiwa kwamba ni watoto, badala ya moyo wake kufurahi, akaanza kulia, picha ilimsisimua na hakuamini kwamba yeye ndiye aliyekuwa nyuma ya tukio lile.
Walikuwa watoto wadogo ambao aliamini kwamba Mungu alikuwa akiwalinda, kwa wivu wake, hasira zake akaagiza watoto hao wauawe, kweli wakauawa na kuwekwa kwenye mfuk wa nailoni.
Alishindwa kuyazuia machozi yake, akaanza kulia kwa maumivu makali kiasi kwamba hata Mwajuma akabaki akimshangaa, ilikuwaje alie na wakati yeye ndiye aliyeagiza watoto hao wauawe kama ilivyokuwa?
“Mbona unalia sasa?” aliuliza Mwajuma huku akimwangalia rafiki yake huyo.
“Inauma sana! Sikustahili kuwafanyia hivi watoto hawa. Hivi Mungu atanisamehe kweli?” aliuliza Evelyne huku akiendelea kulia kama mtoto.
****
Aliyekuwa akisubiriwa alikuwa ni Sikujua tu, aliwapa taarifa kwamba tayari tukio la utekaji lilikuwa limefanikiwa kwa asilimia mia moja hivyo kitu pekee walichokuwa wakitaka kukiona kwa wakati huo ni watoto kuletwa na kisha wampigie simu Evelyne na kwenda kuwaua kwa mikono yake.
Muda ulikwenda lakini Sikujua hakuwa amefika, walimpigia simu mara kwa mara lakini hakuwa akipokea, walikasirika sana lakini baada ya saa moja, akawapigia yeye na kuwaambia kwamba alikuwa kwenye hatua za mwanzo za kuwaua.
“Unawaua?” aliuliza jamaa mmoja.
“Ndiyo! Nimeanza kuwachinja kama kuku. Mtaona kwenye taarifa ya habari usiku jinsi damu zilivyotapakaa,” alisema Sikujua.
“Mmh! Sawa.”
“Nazileta maiti tu huko!”
“Hapana! Hutakiwi kuzileta, kama vipi nenda nazo baharini, zitupe huko, telekeza gari halafu njoo,” alisema jamaa kwa kutoa maelekezo.
“Haina shida!” alisema Sikujua na kufanya kile alichoambiwa.
Dakika arobaini na tano baada ya kuzungumza naye na kuwaambia kwamba alikuwa kwenye hatua za kwanza za kuwaua watoto hao, Sikujua akafika nyumbani hapo, kwa jinsi alivyoonekana, hakuonekana kuwa kawaida hata kidogo.
Mikono yake ilijaa damu, macho yake yalikuwa mekundu kama mtu aliyekuwa amelia sana, hiyo iliwaonyesha kwamba wakati Sikujua akifanya mauaji hayo, alikuwa akilia kupita kawaida.
“Pole sana! Ndiyo ukubwa huo,” alisema jamaa mmoja na kumkumbatia Sikujua.
“Ila picha inatisha sana. Ninaiona kichwani mwangu jinsi nilivyokuwa nikiwachinja, hakika picha hii haitotoka ubongoni mwangu! Kwa nini nimewaua kinyama hivi?” aliuliza Sikujua huku akilia kama mtoto kiasi kwamba kila mmoja alikuwa akimuonea huruma.
Walichokifanya ni kuwaruhusu watoto wa Mzee Marcus kuondoka mahali hapo kwani tayari walichokuwa wamekitaka kwa muda mrefu tayari walikippata.
“Wapelekeni hao watoto wa yule mzee kwake. Tayari mchakato umekamilika,” alisema jamaa huyo na hivyo watoto hao kuchukuliwa na kurudishwa kwa mzee huyo.
****
Cassian na mkewe, Naseku hawakuacha kulia, mioyo yao ilichoma kupita kawaida na hawakuamini kama walikuwa wakipitia maisha waliyokuwa wakipitia.
Walilia mno, picha ya gari iliyokuwa ikionekana mbele yao iliwaumiza mno. Polisi wakawatoa katika eneo la tukio na kuondoka nao. Kila mmoja alikuwa akihuzunika kwani Walter na Walker walikuwa watoto wazuri mno ambao hawakutakiwa kuuawa kikatili kama ilivyokuwa imetokea.
Wakiwa ndani ya gari ndipo kichwa cha Cassian kikakumbuka kuhusu Mzee Marcus, huyo ndiye mtu aliyekuwa amewaambia kuhusu huyo mfanyakazi na kumchukua. Waliambiwa kwamba alikuwa msichana mwema, aliyejua kukaa na watoto, sasa ilikuwaje msichana huyohuyo aondoke na watoto wao na kwenda kuwaua kikatili.
Hakutaka kupoteza muda, alichokifanya ni kuwasiliana na mzee huyo na kumwambia kila kitu kilichokuwa kimetokea na hivyo kutaka kuonana naye.
“Haina shida,” alisema mzee Marcus huku tayari akiwa amekwishapewa watoto wake.
Majira ya alasiri, mzee huyo akafika nyumbani kwa Cassian na kuanza kuongea naye, taarifa aliyokuwa akipewa ni kama hakuwa akiifahamu, alihuzunika mpaka machozi kumlenga, alimuonyesha Cassian kwamba kama kuchomwa kwa tukio hilo hata na yeye alikuwa amechomwa hivyohivyo.
“Yaani Sikujua ndiye amefanya haya?” aliuliza Mzee Marcus huku akionekana kutokuamini.
“Ndiyo!”
“Sikujua huyuhuyu ninayemjua?”
“Ndiyo!”
Akaanza kutokwa na machozi, maigizo aliyokuwa akiyafanya mahali hapo ilikuwa vigumu sana kugundua kwamba alijua mchongo mzima juu ya kile kilichokuwa kimetokea.
Yeye ndiye aliyetakiwa kutoa maelezo polisi juu ya msichana huyo ili polisi wajue ni kwa jinsi gani alikuwa amempata msichana huyo mpaka kumuamini na kumpelekea Cassian.
Hilo halikuwa tatizo, wakaelekea kituo cha polisi na kueleza kila kitu kuhusu msichana huyo. Kwake, alionekana kuwa mwema kwani aliwahi kuishi naye kwa miaka mingi na hakukuwa na kitu chochote kilichotokea.
“Inawezekana kuna mtu alimtuma kufanya hivi,” alisema Cassian.
“Sijui kwa kweli, ila cha muhimu ni kwamba moyo wa binadamu unaweza kubadilika muda wowote ule,” alisema Mzee Marcus.
Alikuwa akimheshimu sana, hakutaka kuwaambia polisi wamshikilie bali aliamua kuwaambia kwamba wafanye kila linalowezekana mpaka maiti za watoto wake zinapatikana ili kama kwenda kuzizika, basi azizike kwa mkono wake.
Wakaondoka, nyumbani, bado maombolezo yalikuwa yakiendelea, kila mmoja alikuwa akilia sana, walihitaji kuziona maiti hizo, walijua kwamba wangeumia sana lakini hawakuwa na jinsi, siku ya kwanza ikakatika, ya pili mpaka ya tatu bado maiti hizo hazikuwa zimeonekana.

Sikujua alikuwa ndani ya gari, watoto walikuwa pembeni yake, alikuwa akiwaangalia huku moyo wake ukimwambia kwamba siku hiyo alitakiwa kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha watoto hao wanauawa mikononi mwake.
Moyo wake ulidhamiria kuua kwa asilimia mia moja, kutoka hapo Mbezi Beach mpaka Mwenge hakukuwa mbali sana kwa kuwa tu hakukuwa na foleni kubwa, aliendesha huku akili yake ikijifikiria ni kwa namna gani alitakiwa kuwamaliza watoto hao ambao wala hawakuwa wakilia, ndiyo kwanza walikuwa wakicheka pale walipokuwa kana kwamba walikuwa wakienda kununuliwa nguo za sikukuu.
Gari lilipofika Makongo, likasimamishwa na msafara wa rais uliokuwa ukipita maeneo ya Mwenge. Alikasirika, alitaka kuwahi kuwamaliza watoto hao kwani iwe isiwe ilikuwa ni lazima kuwamaliza siku hiyohiyo.
Aliangalia huku na kule, magari mbalimbali yaliyokuwa katika msafara wa rais yalikuwa yakiendelea na safari ya kuvuka katika mataa ya Mwenge. Alitulia garini lakini alipoyarudisha macho yake kwa mapacha wale waliokuwa katika kiti cha mbele, kitu cha ajabu kabisa kikaukumba moyo wake, kitu ambacho hakuwahi kukifikiria kama kingemjia moyoni mwake hasa katika kipindi kama hicho.
Moyo wake wa kikatili, ukaingiwa na huruma nzito kiasi cha kumfanya kukosa amani kabisa. Kila alipokuwa akiwaangalia watoto wale, akahisi moyo wake ukisinyaa kabisa.
Akaanza kujuta kwa uamuzi aliochukua wa kukubali kuwateka watoto wale, akabaki akilengwa na machozi, mbele yake akawaona watu wengi wakiwa wamesimama wakimwangalia, wote hao walikuwa wakimlaumu kwa uamuzi aliotaka kuuchukua kipindi hicho.
Alijishangaa, hakuwa hivyo, hakuwa na hali hiyo tangu azaliwe, ni kitu gani kilichokuwa kikimfanya kuingiwa na huruma ya ghafla hivyo. Mbali na huruma hiyo akaanza kuisikia sauti moyoni mwake ikimlaumu kwa kile alichotaka kukifanya kwamba kwa nini aliuruhusu moyo wake kutaka kuwaua watoto wale, malaika wa Mungu ambao hawakuwa na hatia yoyote ile.
Alisakamwa moyoni mwake mpaka akahisi maumivu mazito, akabaki akisikitika kwa kile alichotaka kukifanya. Nguvu ya kutaka kufanya mauaji ikaanza kuondoka moyoni mwake na akajikuta akiingiwa na upendo wa hali ya juu kwa watoto wale.
“Siwezi kuwaua! Siwezi kuuawa watoto wasio na hatia,” alisema Sikujua.
Aliendelea kusubiri mpaka msafara uishe ndipo waliporuhusiwa akaliondoa gari lake mahali hapo na kuondoka. Aliambiwa kwamba ni lazima aende akawaue watoto hao, hakutaka kufanya hivyo hata kidogo hivyo alichokifanya ni kuondoka mpaka katika soko la Mwananyamala ambapo akanunua kuku wawili na kisu kisha kuingia ndani ya gari.
Kwanza hakutaka kuondoka kuelekea baharini, alichokitaka ni kwenda kwa rafiki yake aliyekuwa akiishi Magomeni, alipofika, akamuachia watoto hao kwa lengo la kuwafuata baadaye.
“Wewe! Ndiyo watoto gani hawa?” aliuliza rafiki yake huyo huku akishangaa.
Sikujua hakuwa na jinsi, akamwambia rafiki yake huyo kila kitu kilichotokea kwamba hakutaka kuwamaliza watoto hao, alikuwa kwenye harakati kubwa ya kuokoa maisha yao hivyo ilikuwa ni lazima amsaidie kwa ajili ya kuwa nayo kwa muda wakati yeye akielekea Coco Beach kufanya kile alichotaka kufanya.
“Usichelewe,” alisema rafiki yake huyo na kuondoka.
Kidogo moyo wake ukajisikia amani, akafurahi, akawaangalia kuku wale, walikuwa wakilia, aliondoka nao mpaka alipofika Coco Beach ambapo kwa muda huo hakukuwa na watu wengi, akawachukua wale kuku, akawachinja kisha kunyunyizia damu zile ndani ya gari lile, hakuishia hapo, akawaweka katika mfuko mweupe wa nailoni ambao ulionyesha jinsi ulivyolowa damu huku ndani kukiwa na kitu, akaupiga picha, akaliacha na yeye kuondoka zake kutoa taarifa kwamba mauaji aliyokuwa ameambiwa, yalikuwa yamefanyika.
****
Kila mmoja alikata tamaa, wakajua kwamba watoto wao walikuwa wameuawa kwani damu zilionekana ndani ya gari na kila mmoja aliamini kwamba huo ndiyo ulikuwa mwisho wa kuwaona mapacha hao.
Walikuwa na pesa, kuwapoteza watoto wao kuliwafanya kutokuwa na furaha ya utajiri ule, kuliwafanya kuona kwamba kila kitu walichokuwanazo mikononi mwao kupotea, utajiri huku watoto wako wakiwa wameuawa hakika yalikuwa ni zaidi ya maumivu.
Siku ziliendelea kukatika, Cassian alimuonea zaidi huruma mke wake, alionekana kuwa mwanamke mnyonge ambaye kila siku alikuwa akilia tu, moyo wake ulikuwa na maumivu makali mno na aliamini kwamba kama asingemfariji basi mwanamke huyo angeugua ugonjwa wa moyo na mwisho wa siku kufariki dunia.
Ilipofika siku ya nne huku kila mmoja akiwa na huzuni tele Cassian akaletewa taarifa na daktari ambaye aliichukua damu ile na kwenda kuipima, taarifa ilionyesha kwamba damu ile haikuwa ya binadamu bali ilikuwa damu ya kuku.
Alishindwa kuamini, hapohapo akamfuata mke wake na kuanza kuzungumza naye, akamwambia kuhusu ripoti hiyo aliyopewa na daktari kwamba damu waliyoikuta ndani ya gari haikuwa damu ya watoto wao bali ilikuwa damu ya kuku.
“Unasemaje?” aliuliza Naseku huku akiyafuta machozi yako.
“Ni ripoti ya daktari!”
“Sasa watoto wetu wapo wapi?”
Hilo lilikuwa swali ambalo kila mmoja hakuwa na majibu nalo. Walishindwa kujua mahali walipokuwa watoto wao, mpaka kufikia hatua hiyo, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumshukuru Mungu kwa kuwa watoto wao hawakuwa wameuawa kama walivyokuwa wakihisi kabla.
Mbali na swali kuhusu mahali walipokuwa watoto wao lakini pia kulikuwa na swali jingine kwamba kama Sikujua aliwateka watoto wao na kuondoka nao, kwa nini hakuwamaliza? Je, hakuwamaliza kwa kuwa aliuawa yeye au ni kitu gani kilikuwa kimetokea.
Wakawasiliana na polisi na kuwapa taarifa hizo. Wao wenyewe hawakuamini, walijaribu kutafuta kila sehemu, tena wakati mwingine wakiwatumia hata wapelelezi wao lakini hakukuwa na mtu aliyejua mahali walipokuwa.
Kazi ikaanza upya, haikuwa kuzitafuta maiti bali kilichokuwa kimetokea ni kutafuta mahali watoto walipokuwa. Walimwambia kwamba wangempa taarifa kwamba watoto wake walikuwa mahali fulani hivyo kumtaka kuwa na matumaini juu ya hilo.
“Kweli watapatikana?” aliuliza Naseku, muda wote alionekana kuwa na hofu tele.
“Wala usijali! Tumuombe Mungu, naamini watapatikana,” alisema Cassian huku akimkumbatia mke wake.

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA TANO

Sikujua alikuwa na mawazo tele, aliwachukua watoto wale na kuishi nao huku kila mmoja akijua kwamba walikuwa wameuawa ufukweni. Hawakuwa watoto wasumbufu, hawakuwa watoto wa kulia na kwa sababu walikuwa wamemzoea sana, muda wote walionekana kuwa na furaha mno.
Moyo wake ulimuuma mno, alijua ni kwa jinsi gani CAssian na mkewe, Naseku walikuwa wakiumia, walilia na hivyo alichokifanya ni kutamani kuwasiliana nao kwa lengo la kuwakabidhi watoto wao.
Hakutaka kuchelewa, haraka sana akachukua simu na kumpigia Cassian, simu haikuita sana, ikapokelewa na sauti ya mwanaume huyo kuanza kusikika upande wa pili.
“Sikujua!” aliita Cassian, kwa jinsi alivyosikika, msichana huyo akajua kwamba aliwekwa loud speaker, ila hakutaka kujali.
Hakutaka kupindisha maneno, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumuomba msamaha kwa kila kitu alichokuwa amekifanya, alijua kwamba aliwaumiza na kuwafanya kulia lakini aliyafanya yote hayo kwa kuwa nyuma kulikuwa na mtu aliyemlazimisha kufanya hivyo.
Hakutaka kuficha, alimwambia Cassian kwamba mtu aliyekuwa amemtuma alikuwa Evelyne ambaye alilipa kiasi kikubwa cha pesa kuhakikisha watoto hao wanauawa haraka iwezekanavyo kwa kuwa tu siku za nyuma aliumizwa hivyo na yeye alitaka kuwaumiza.
Cassian aliposikia maneno hayo, mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda kwa kasi, hakuamini alichokisikia, ilikuwa msichana huyo aendelee kuwafuatilia na wakati walikuwa wamekwishamalizana tangu kitambo? Moyo wake ukawaka kwa hasira, hakutaka kuona akibabaishwa na msichana huyo hivyo ilikuwa ni lazima kupambana naye.
“Watoto wangu wapo wapi?” aliuliza Cassian huku akitetemeka, pembeni alikuwepo mke wake aliyekuwa akisikia kila kitu, machozi yalikuwa yakimtoka kwa furaha kwani aliamini kwamba angewapata watoto wake.
“Ninao!”
“Unao hapo? Niambie upo wapi nikufuate,” alisema Cassian.
“Naogopa!”
“Unaogopa nini?”
“Utanikamata!”
“Sikujua! Umenisaidia, uliagizwa kuwaua watoto wangu, hukufanya hivyo, kwa maana hiyo umenisaidia, siwezi kukumata. Nakuahidi hata kuja huko nakuja na mke wangu tu. Usiogope, niambie upo wapi,” alisema CAssian.
Alimaanisha, alichokuwa akikihitaji kilikuwa ni watoto wake tu, japokuwa Sikujua alikuwa akiogopa lakini hakuwa na jinsi, akawaambia mahali alipokuwa na mwanaume huyo kwenda huko kuwachukua watoto wake.
Njiani, hakukuwa na aliyeamini, hawakujua ni kwa namna gani walitakiwa kumshukuru Sikujua ambaye alitumwa kuwaua lakini hakutaka kufanya hivyo kwa kuwa tu moyo wake ulijikuta ukishikwa na upendo wa ajabu, huruma ambayo haikuwahi kumpata kabla.
“Mke wangu! Usilie, ngoja tukawachukue watoto wetu,” alisema Cassian huku akiendesha gari kuelekea Magomeni.
Hawakuchukua muda mrefu wakafika huko, kwa maelekezo ya msichana huyo, wakatokea nyumbani kwake alipokuwa akiishi na kuingia ndani. Hawakuamini, waliwakuta watoto wao wakiwa kwenye kochi sebuleni huku kukiwa na chupa ya maziwa pembeni.
Haraka sana Naseku akawasogelea, akawabeba kisha kuwakumbatia. Huzuni aliyokuwa nayo moyoni, kilio alichokuwa amelia kwa siku tatu mfululizo kikapotea, furaha ya ajabu ikamuingia moyoni mwake.
Cassian akamsogelea mke wake na kumkumbatia. Wakati hayo yote yakiendelea, Sikujua alikuwa pembeni, alionekana kuwa na hofu nzito moyoni mwake, aliteteka, hakujiamini, aliona kama mwanaume huyo angemfanyia jambo lolote lile baya.
“Hutakiwi kuogopa Sikujua,” alisema Cassian huku akimwangalia msichana huyo.
Walimshukuru msichana huyo kwa wema wake, hawakuwa na cha kumlipa kwani kwa kuwaokoa watoto wao walimaanisha kwamba hiyo ilikuwa ni zaidi ya pesa, kilikuwa kitu kikubwa ambacho hata kama wangemlipa milioni mia moja bado isingelingana na kile alichowafanyia.
“Unataka tukufanyie nini?” aliuliza Cassian huku akimwangalia Sikujua.
Msichana huyo hakuhitaji kiasi chochote cha pesa, kitu pekee alichokihitaji ni kuwa huru tu. Hiyo haikutosha, Cassian akamuahidi kwamba angemlipa kiasi cha shilingi milioni hamsini, angemfungulia biashara kwanii kwa jinsi maisha aliyokuwa akiishi hapo nyumbani kwake, hayakuwa mazuri hata kidogo.
“Halafu mimi niache nidili na huyu msichana,” alisema Cassian kisha kuondoka nyumbani hapo huku Sikujua akiwa na amani tele moyoni mwake.
Huo ndiyo ukawa mwanzo, kupatikana kwa watoto hao ilikuwa siri kubwa, aliamini kwamba kama wasingewaficha basi hali ya Sikujua kule alipokuwa ingekuwa mbaya, inawezekana wenzake ambao walikubaliana wawamalize wakajua kwamba walidanganywa na hivyo kumuua yeye.
Akamuhakikishia ulinzi na hivyo kuendelea na maisha yao kama kawaida. CAssian alipanga kumtafuta Evelyne, alitaka kummaliza kwa kile alichokiona kwamba kingemfanya kuwa na amani moyoni mwake, akamwambia mke wake alichotaka kukifanya kwamba amtafute msichana huyo na kumuua lakini mkewe akamsihi kwamba hakutakiwa kufanya hivyo.
“Ila alitaka kuwaua watoto wetu!” alisema Cassian.
“Bado si sababu!”
“Kwa hiyo tumuache?”
“Ikiwezekana!”
“Ila atarudi tena na kuwaua endapo atajua kwamba wapo hai!” alisema Cassian.
“Tuongeze ulinzi, uwe mkubwa zaidi na tusimwamini mtu,” alisema Naseku.
Mkewe akaubadilisha moyo wake, maneno mazito yakamuingia na kumwambia kwamba hakutakiwa kulipa ubaya kwa ubaya bali alitakiwa kulipa ubaya kwa wema, akaamua kuachana na msichana huyo na kufanya mambo yake.
Familia ikawa ya furaha tena, siku zikakatika, kila mtu aliyafurahia maisha yake. Kuwa na watoto hao ndani ya nyumba ilikuwa siri kubwa, cha ajabu kabisa hata polisi hawakujua kama watoto hao walipatikana.
Ulinzi ukawa mkubwa, hakukuwa na mtu aliyeruhusiwa kuingia ndani ya nyumba hiyo kiholelaholela, Cassian na mkewe wakaishi kama jinsi ambavyo mabilionea walivyokuwa wakiishi. Siku zikakatika, miezi ikakatika mpaka watoto hao, Walter na Walker walipofikisha umri wa miaka miwili.
Walikuwa wameungana kama ilivyokuwa. Japokuwa walikuwa hivyo lakini hawakutaka kabisa kwenda kuwatenganisha, waliungana sehemu mbaya, walichangia sehemu ya ubongo, kwa kuwaangalia, walionekana kuwa na furaha tele, hawakuonekana kuumizwa na hali waliyokuwa nayo.
Japokuwa walikuwa wameungana lakini watoto hao walikuwa wazuri wa sura, hata wazazi wao walipokuwa wakiwaangalia, walionekana kuwapenda, walivutia na walikuwa na uhakika kwamba wangemvutia msichana yeyote ambaye angewaangalia.
Walipofikisha umri wa miaka mitatu wakaanza kusoma katika shule ya chekechea ya Amazon Day Care iliyokuwa Mikocheni B, shule iliyokuwa ikisomwa na watoto wa mawaziri na matajiri mbalimbali Tanzania. Mbali na watoto wa matajiri, pia kulikuwa na watoto wa mabalozi wa nchi mbalimbali.
Siku ya kwanza kufika shuleni hapo kila mtu alikuwa akiwashangaa, walimu hawakuamini kama wangeweza kuwaona watoto walioungana kama hao, walizoea kuwaona katika televisheni na sehemu nyingine lakini hawakuamini kama ingetokea siku wangewaona kwa macho yao.
Waliwashangaa lakini wakati mwingine waliamini kwamba Mungu alikuwa wa ajabu sana kwani pamoja na kuungana huko watoto hao walikuwa wazuri mno, sura zao zilionyesha kabisa kwamba huko mbeleni wasichana wangechanganyikiwa nao sana.
“Jamani hawa watoto wazuri sijawahi kuona,” alisema mwalimu Getrude huku akiwaangalia watoto hao, alitamani hata wangekuwa watoto wao.
“Kweli kabisa. Ningepata watoto wenye sura nzuri kama hawa, nadhani ningewaambia wazazi wa watoto wa kike mtaani kwangu wawe makini na mageti yao,” alisema mwalimu Susan na wote kuanza kucheka.
Walimu walikuwa wakiuzungumzia uzuri wa watoto hao, walikuwa na uzuri wa ajabu mno. Shuleni hapo walikuwa wachangamfu mno, japokuwa kwa siku za kwanza watoto wengine walikuwa wakiwaogopa lakini mwisho wa siku wakawazoea na kucheza nao kiasi kwamba kila mmoja alifurahia uwepo wa watoto hao shuleni hapo.
“Jamani! Nina wasiwasi, wale Jackline na Rosemary, nahisi baadaye huko kutakuja kutokea jambo,” alisema mwalimu Susan ofisini.
“Wale watoto wa mabalozi?”
“Ndiyo! Yaani naona wamezidisha ukaribu na watoto hawa. Wakiendelea kuwa karibu hivi kila siku, miaka na miaka, kuna jambo linaweza kutokea,” alisema mwalimu huyo na wengine kuanza kucheka.
Jackline alikuwa mtoto wa Balozi wa Marekani, Bwana Godluck Puff huku Rosemary akiwa mtoto wa Balozi wa Uingereza, Bwana Emmanuel Sinclair. Wawili hao walianza kusoma kutika shule hiyo, walikuwa watoto wa Kizungu waliokuwa wazuri mno.
Walikuwa watoto wakimya sana, hawakuwa wazungumzaji lakini tangu Walter na Walker wahamie shuleni hapo, watoto hao wakaanza kuonyesha uchangamfu wa ajabu kiasi kwamba hata walimu walikuwa wakiwashangaa.
Walikuwa wakicheza pamoja, kula pamoja na kufanya vitu vingine pamoja. Katika kipindi ambacho watoto hao walipokuwa wakifuatwa na wazazi wao kurudi nyumbani ilikuwa ni kilio, hawakutaka kuachana, hawakutaka kuona wakitenganishwa, kila siku walitamani kuwa pamoja.
Kutokana na ukaribu wa watoto wao, Cassian na mkewe wakajikuta wakiwa karibu na wazazi wa watoto hao wa kike, kwa kuwa walitambua kwamba walizoeana, wakaanza kuwapeleka nyumbani kwao na kuanza kucheza pamoja na wakati mwingine kutoka nao pamoja kitu kilichowafanya watoto hao kuwa na furaha tele.
Ilikuwa ni kama wamegawana, Jackline akawa karibu sana na Walter huku Rosemary akiwa karibu sana na Walker, kwa kifupi walikuwa na urafiki wa ajabu, urafiki uliomshangaza kila mtu aliyekuwa akiwaangalia. Walikuwa watoto hivyo kila mmoja kuhisi kwamba ni utoto tu lakini cha ajabu kila walivyozidi kukua, ukaribu ukaongezeka zaidi

Watoto wao ndiyo walikuwa furaha yao, kila walipokuwa wakiwaangalia, mioyo yao ilijisikia faraja na kuona kwamba Mungu aliwabariki kwa kuwapa watoto hao waliokuwa na sura nzuri kupita kawaida.
Kila siku ilikuwa ni lazima kwa Naseku kuwapeleka watoto wake shuleni kwa gari lake, hakutaka kumwamini mtu na kitendo hicho kilionekana kuwa sahihi kwa kuwa kilimfanya kuwa karibu na watoto wake.
Walter na Walker waliendelea kukua, walikuwa watoto wenye furaha tele kiasi kwamba mpaka watu wengine walikuwa wakishangaa kwani walijua kwamba wangekuwa kwenye huzuni tele kutokana na hali ya kuungana lakini ndiyo kwanza kila siku walikuwa watoto wa kucheka tu.
Siku zikaendelea kukatika, watoto Catherine na Jackline waliendelea kuwa pamoja nayo, kwenye kila hatua waliyokuwa wakikua, walikuwa pamoja huku ukaribu wao ukiongezeka kila siku.
Baada ya miaka minne, wakaanza kusoma darasa la kwanza katika shule hiyohiyo. Ilikuwa ni furaha kwao, walisoma kwa bidii, walipendwa kila kona, kwa darasani, hawakuwa na akili nyingi lakini kila siku walionekana kupenda sana kusoma.
Watu waliwapenda kwa kuwa walikuwa na sura nzuri. Katika kipindi hichohicho cha darasa la kwanza ndipo walimu wakagundua kwamba mapacha hao walikuwa na vipaji vikubwa mno.
Walter alikuwa na uwezo mkubwa wa kuimba, kila alipokuwa akiambiwa aimbe wimbo wowote ule, sauti yake iliwashangaza watu wengine, wakabaki wakishangaa, hawakuamini kama duniani kulikuwa na mtoto aliyekuwa na sauti kali ya kuimba kama ilivyokuwa kwa Walter.
Kwa Walker, hakuwa muimbaji, yeye alikuwa na uwezo wa kuchora. Tangu alipokuwa chekechea, hakukuwa na kitu alichokipenda kama kuchora, alijua kuchora sana zaidi ya watoto wengine.
Vipaji vyao havikujificha, kwa kuwa vilikuwa vimeonekana, walichokifanya Cassian na mkewe ni kuwaendeleza katika vipaji hivyohivyo walivyokuwa navyo. Kwa Walter, akatafutiwa mwalimu wa kwaya kwa ajili ya kumfundisha namna ya kuimba na kupangilia sauti yake.
Uwezo wake ulikuwa mkubwa mno, kila alipokuwa, maisha yake yalikuwa ni kuimba tu. Kanisani alikuwa gumzo, japokuwa alikuwa na miaka saba lakini kila mmoja alipenda kusikia namna alivyokuwa akiimba, aliwafurahisha watu wengi kiasi kwamba kanisani hapo akawa muimbaji kiongozi, kwenye kila ibada ya kusifu na kuabudu, alikuwa akichaguliwa yeye.
Wakati Walter akiwa muimbaji, Walker hakuwa na uwezo wowote wa kuimba, yeye alikuwa mchoraji, alikuwa na uwezo mkubwa wa kuchora kiasi kwamba mpaka watu wengine walikuwa wakishangaa.
Walter alikuwa mzungumzaji, alipenda sana kuongea, alikuwa na uwezo wa kuongea maneno mengi kwa wakati mmoja lakini Walker alikuwa mkimya, hakuwa mzungumzaji, mpole ambaye muda wote alionekana kuwa siriazi kupita kawaida.
“Who do you want to be?” (unataka kuwa nani?) aliuliza Cassian huku akiwaangalia watoto wake.
“A Pop star like Michael Jackson,” (niwe staa wa Pop kama Michael Jackson) alijibu Walter harakaharaka.
“What about you?” (vipi kuhusu wewe?) aliuliza Cassian huku akimwangalia Walker.
“I want to be a greatest picture artist ever in the world,” (nataka kuwa mchoraji bora kuliko wote waliowahi kutokea katika dunia hii) alisema Walker huku akimwangalia baba yake.
Waliishi katika ndoto, kila siku ilikuwa ni lazima kufanya mazoezi kwa kile walichokuwa wakitaka kuwa. Bado vipaji walivyokuwa navyo viliwashangaza watu wengi, hawakuamini kama kungekuwa na watoto waliokuwa na uwezo mkubwa kwa vile walivyokuwa nacho kama wao.
Kwenye mashindano mbalimbali shuleni, walipewa zawadi nyingi, waandishi wa habari waliposikia kuhusu wao, wakaanza kuwatafuta kwa lengo la kuzungumza nao na kuandika mengi kuhusu watoto hao.
Kuwapata halikuwa jambo jepesi, kila walipokwenda shuleni hapo, walikataliwa kuonana nao kwani ulinzi wao ulikuwa mkubwa kutokanma na heshima kubwa aliyokuwanayo baba yao.
Waandishi hao hawakukoma, kila kona walipokuwa waliendelea kusikia sifa za watoto hao, walikuwa wakiwashangaza kila mtu aliyekuwa akisikia kuhusu wao, juu ya vipaji vikubwa walivyokuwa navyo.
Kwa mwaka mzima walikuwa wakiwatafuta lakini hawakuweza kuwaona. Walipofikisha umri wa miaka kumi, baba yao akawafungulia chaneli katika Mtandao wa Youtube kwa ajili ya kuionyesha dunia kwamba kulikuwa na watoto waliokuwa na vipaji vya hatari ambao walikuwa wameungana.
Kwa kutumia pesa zake, akaanza kuitangaza chaneli hiyo, watu wengi wakaiona na kuangalia vipaji vya watoto hao. Kila mmoja aliyekuwa akiangalia alishangaa, hakuamini kama katika dunia hii kungekuwa na watoto waliokuwa na uwezo kama Walter na Walker.
Wakaanza kupata umaarufu wakiwa wadogo kabisa. Katika kila kona ya dunia walikuwa wakizungumziwa wao tu. Watu wengi wakataka kufahamu mahali walipokuwa, walitaka kujionea kwa macho yao uwezo mkubwa waliokuwa nao watoto hao.
Waandishi kutoka BBC, CNN na vituo vingine vya habari vya kimataifa vikasafiri mpaka nchini Tanzania kwa lengo la kuonana na watoto hao. Halikuwa jambo jepesa kuwapata, walikuwa watoto wa ndani tu na hata walipokuwa shuleni, ilikuwa vigumu mno kuwaona.
Waandishi hao wakatumia majina ya vituo vyao, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumtafuta Cassian, hakuwa mwepesi kuonana na watu hasa alipokuwa ofisini kwake, waandishi hao walihangaika kwa muda wa wiki nzima ndipo wakakutana naye na kuanza kufanya naye mahojiano.
Walimwambia wazi jinsi walivyokuwa wakishangazwa na vipaji walivyokuwanavyo watoto hao, kila mtu alishangaa, haikuwa Afrika tu bali dunia nzima ilikuwa ikistaajabu kwa kile kilichokuwa kikiendelea.
Moyo wa Cassian ukajisikia faraja, watoto wake wakawa maarufu, hilo ndilo alilitaka kwa kipindi kirefu, alijua kwamba walikuwa wameungana, alijua kwamba kama wangeendelea kuishi hivyo tu ilikuwa ni lazima kukata tamaa na kujiona kwamba hakukuwa na tumaini jingine na wakati mwingine hata kumlaumu Mungu na ndiyo maana alikuwa akipambana kuhakikisha kwamba wanakuwa na furaha hata kama wanakuwa kwenye hali ya kuungana.
“Wana miaka mingapi?” aliuliza mwandishi wa BBC.
“Miaka kumi ila mwaka huu katikati watakuwa na miaka kumi na moja,” alisema Cassian.
“Na una watoto hawa tu?”
“Ndiyo! Ila mama yao ni mjauzito. Natumaini kupata mtoto mwingine mwaka huu,” alijibu Cassian.
Alikuwa akiulizwa maswali mengi kuhusu Walker na Walter, baada ya kumalizana naye wakataka kuwaona watoto hao na kufanya nao mahojiano kitu ambacho hakikuwa na tatizo lolote lile.
Wakaondoka na kuelekea nyumbani huko, walitakiwa kuwasubiri mpaka watakaporudi kutoka shuleni. Hilo halikuwa tatizo, walisafiri kutoka nchini Marekani, Uingereza mpaka Tanzania kwa ajili ya watoto hao tu, hivyo wakawasubiri, na baada ya saa mbili, watoto hao wakafika nyumbani na kuanza kuwahoji baadhi ya maswali huku wakiwaonyeshea jinsi vipaji vyao vilivyokuwa hatari.
Dunia ikazidi kuwatambua, waliendelea kujulikana kila kona. Wazungu hawakutaka watoto hao wakae Tanzania, walichokifanya ni kuandaa matamasha na hivyo kuwaomab wazazi hao ruhusa ya watoto hao kushiriki katika matamasha mbalimbali yaliyokuwa yakifanyika humo.
Pesa zikazidi kuongezeka katika akaunti ya Cassian, akawaongezea pesa watoto wake, nao, wakaanza kupata utajiri mkubwa, kwenye kila tamasha walilokuwa wakihudhuria, watu walikuwa wakilipia sana kwa ajili ya kuona miujiza waliyokuwa nao watoto hao.
Mbali na kupokea pesa za waandaaji wa matamasha, pia wamiliki wa YouTube wakaanza kuwalipa pesa nyingi kwani chaneli yao ilikuwa ikitazamwa na watu wengi, mpaka kufika idadi ya watu bilioni moja, idadi ambayo ilikuwa ikiwafukuzia Justin Bielber kwa video yake ya wimbo wa Sorry na Adele kwa wimbo wake wa Helo.
They have received cheque of twenty milion dollars from YouTube,” (wamepokea cheki ya dola milioni ishirini kutoka Youtube) alisema jamaa mmoja aliyekuwa akiangalia kwenye mtandao kuhusu watoto hao.
“Sure?” (kweli?)
“Yeah! Check this out,” (ndiyo! Angalia hii)
Kwa kuwa walikuwa wakiishi sana katika nchini za huko, baba yake, Cassian akaamua kuwaanzisha masomo katika shule ya St. Monica iliyokuwa Washington nchini Marekani, shule ambayo ilikuwa ikikuza sana vipaji vya watoto waliokuwa mahali hapo.
Hapo, kulikuwa na waimbaji wengi lakini kitu cha ajabu kabisa kila mmoja alikuwa akimshangaa Walter, alikuwa akiimba kiasi kwamba wengine wakampa jina la malaika, waliamini kwamba sauti yake ilikuwa nzuri hata ya hao malaika waliokuwa na kazi kubwa ya kumsifu na kumwabudu Mungu.
Kwa Walker kila mtu alikuwa akishangaa, alikuwa mchoraji mkubwa, alijua kuchora picha za kila aina, kila mtu aliyekuwa akiziangalia picha zake alikuwa akipigwa na butwaa, alikuwa hatari katika uchoraji wake.
Waliishi nchini Marekani, wazazi wao walikuwa wakienda kuwaangalia mara kwa mara. Na baada ya miezi kadhaa baba yao akawaambia kwamba mama yao alijifungua salama mtoto wa kike na kuamua kumpa jina la Ester.
“Is this the one?” (ndiye huyu?) aliuliza Walter huku akiangalia picha ya Ester.
“Yes! She is!” (Ndiyo! Ndiye yeye)
“We look alike,” (tumefanana sana) alisema Walker huku naye akiiangalia picha hiyo.
Miaka saba baadaye, walikuwa watu maarufu kuliko wote nchini Marekani. Majina yao yaliongoza kutafutwa katika tovuti ya Google kitu kilichomaanisha kwamba kwenye kila kona watu walikuwa wakitaka kufahamu mambo mengi kuhusu hao.
Katika kipindi hicho ndipo wakakumbuka kitu. Kipindi walichokuwa wadogo kulikuwa na wasichana wawili waliokuwa marafiki zao sana nchini Tanzania, wasichana hao walikuwa Catherine na Jackline.
Hawakujua mahali walipokuwa, waliondoka nchini Tanzania zamani sana na hawakujua kama wasichana hao walikuwa hai au walikufa.
Walichokikumbuka ni kwamba mmoja alikuwa mtoto wa balozi wa Uingereza nchini Tanzania na mwingine mtoto wa balozi wa Marekani nchini Tanzania hivyo kuanza kuwatafuta katika mitandao ya kijamii.
“I’ve got her,” (nimempata) alisema Walker huku akiiangalia kompyuta yake, alikuwa amempata rafiki yake wa utotoni, Rosemary.
“How about Jackline? Did you find her?” (vipi kuhusu Jackline? Umempata?) aliuliza Walter huku akiwa na hamu ya kujua mahali alipokuwa msichana huyo.
“Give me one sec,” (nipe sekunde moja)
Haraka sana Walker akaanza kuangalia kwenye tovuti ile, alikuwa akimtafuta msichana huyo kwa kumsaidia ndugu yake huyo. Alichukua dakika zaidi ya tano kuangalia kila kona, kila alipoona jina lililofanana na la rafiki wa ndugu yake, alikuwa akiliangalia kuona kama alikuwa yeye au la.
“I’ve found her!” (nimempata) alisema Walker huku akimwangalia ndugu yake, japokuwa alikuwa akimwambia habari nzuri, uso wake ulionyesha kuwa na shaka kupita kawaida.
“Let me see,” (acha nione) alisema Walter na kisha kuanza kuangalia, alitaka kujua sababu iliyomfanya ndugu yake kuwa katika hali hiyo.
Haraka sana akaichukua iPad aliyokuwa nayo ndugu yake na kuanza kuangalia. Kile alichokiona hakuonekana kuamini, aliliona jina la msichana huyo, picha yake lakini habari ambayo ilimshangaza ni kwamba msichana huyo alikuwa amepata ajali mbaya ya gari alipokuwa akielekea chuoni Oxford nchini Uingereza.
Walter hakuamini alichokuwa akikiangalia, akahisi kama kitu chenye ncha kali kikiwa kimeuchoma moyo wake, baada ya sekunde kadhaa, machozi yakaanza kumtiririka mashavuni mwake.
Hakutaka kukubali, hakutaka kuona rafiki yake huyo akiteseka kitandani na wakati yeye alikuwa hai. Alichokifanya ni kumwambia Walker kwamba ilikuwa ni lazima kusafiri na kuelekea nchini Uingereza kwa ajili ya kumuona msichana ambaye alihisi kumpenda kwa penzi la dhati moyoni mwake.
Wakawasiliana na wazazi wao na kuwaambia kwamba ilikuwa ni lazima kusafiri kuelekea nchini Uingereza kwa ajili ya kumuona msichana huyo aliyekuwa hoi kitandani.
“Hamuwezi kwenda peke yenu! Nisubirini!” alisema Cassian kwenye simu.
“Utachelewa baba!” alisema Walter.
“Siwezi kuchelewa, nakuja baada ya siku mbili.”
“Sawa.”
Moyo wa Walter ukakosa amani, muda mwingi alikuwa akimfikiria msichana huyo. Alimpenda kutoka moyoni mwake, alijua kwamba kilikuwa kimepita kipindi kirefu sana lakini bado moyo wake ulikuwa kwa msichana huyo aliyekuwa hajitambui kitandani.
Aliona baba yake akichelewa kuja, alichokuwa akikihitaji ni kumuona msichana huyo tu. Baada ya siku alizoahidi baba yake kutimia, wakaondoka nchini Marekani na kwenda Uingereza ambapo huko wakapelekwa moja kwa mja mpaka katika Hospitali ya Queen Elizabeth kwa lengo la kumuona msichana huyo.
Walipofika hospitalini, umati mkubwa wa watu ulikuwa ukiwashangaa, wengine wakawasogelea kwa lengo la kupiga nao picha. Walikuwa maarufu, walipendwa na kila mmoja alitamani sana kuwa nao karibu kwani vipaji walivyokuwa navyo vilimshangaza kila mmoja.
Hawakuwa na haja ya kujitambulisha walikuwa wakina nani bali walikuwa na haja ya kuuliza mahali alipolazwa msichana huyo. Kwa kuwa ulikuwa muda wa kuona wagonjwa, walipoambiwa mahali alipokuwa, haraka sana wakaondoka na kuelekea huko.
Wakafungua mlango na kuingia ndani. Msichana Jackline alikuwa kitandani, alikuwa kimya, pembeni yake walikuwa wazazi wake, kwa jinsi walivyoonekana tu walikuwa wamekata tamaa, hawakuamini kama binti yao angeweza kuzinduka na kusimama tena.
Kila walipomwangalia, waliona kabisa huo ndiyo ungekuwa mwisho wake kitandani pale. Walter aliumia mno, alimwangalia Jackline huku akihisi akichomwa na kitu chenye ncha kali, hapohapo machozi yakaanza kumtoka. Mbali na wazazi wa Jackline waliokuwa chumbani humo, pia pembeni yao kulikuwa na kijana mwingine, huyu aliitwa Edmund, kijana aliyekuwa mpenzi wa Jackline aliyekuwa kitandani.

Walikuwa na umri mdogo lakini walionekana kuwa na mapenzi ya dhati, kila siku walikuwa pamoja huku mtoto Catherine akijitahidi kumuonyeshea Walter kwamba kweli alikuwa akimuhitaji kama rafiki katika maisha yake.
Siku ziliendelea kukatika, wakaendelea kukua zaidi na zaidi, ukaribu ule ukaongezeka kiasi kwamba Catherine akawa haoni wala hasikii kwa Walter, kila siku ilikuwa ni lazima awe mtu wa kwanza kuzungumza naye shuleni wakati anaingia na awe mtu wa mwisho kuzungumza naye wakati akiondoka.
Ilikuwa hivyo, wazazi waliendelea kuwashangaa, haikuwa rahisi kuona watoto waliokuwa wakipendana kiasi hicho, walishindwa kuwatenganisha na kwa jinsi walivyokuwa wakiwaona walivyopendana, walihisi kabisa hapo baadaye kungekuwa na ugumu mkubwa kuwatenganisha.
Siku zikaendelea kukatika, baada ya miaka mitano, baba yake, Bwana Gordon Smith akamaliza muda wake wa kuwa balozi wa Uingereza nchini Tanzania hivyo kurudi na familia yake nchini huko.
Hilo likawa pigo kubwa kwa Catherine, siku za kwanza zilikuwa ni ngumu sana kwake, alikuwa akilia kila wakati, alikosa furaha na muda mwingi alikuwa mtu wa huzuni tele. Wazazi wake wakajaribu kumletea marafiki wengi wa kukaa naye lakini hakubadilika, bado kichwa chake na moyo wake ulimfikiria mtu mmoja tu, Walter aliyekuwa nchini Tanzania.
Baada ya miaka mingine mitano kukatika, Catherine akafanya vizuri katika masomo yake na hivyo kuchaguliwa kusoma katika Chuo Kikuu cha Oford kilichokuwa hapohapo Uingereza.
Bado hakuacha kumfikiria Walter, alimkumbuka mwanaume huyo, alipata marafiki wengi lakini kwa Walter ilikuwa ni tofauti kabisa, alikuwa rafiki aliyejali na kumsikiliza, aliufurahisha moyo wake na muda mwingi alitamani kumuona tena mbele yake, alitamani kumwambia kwamba katika maisha yake yote hakika asingepata rafiki wa kweli kama alivyokuwa yeye.
Wakati kichwa chake kikimfikiria sana ndipo akaamua kumtafuta katika mtandao. Hakupata kazi kumpata kwani mapacha hao walikuwa maarufu mno nchini humo kutokana na vipaji walivyokuwanavyo.
Moyo wake ukaridhika, alifurahi kumuona Walter, mwanaume aliyekuwa akimpenda kupita kiasi. Alitamani kusafiri kuelekea nchini Tanzania kwa ajili ya kuonana naye lakini masomo yalikuwa yakimbana na kuwa na ratiba ndefu mno.
Siku zikakatika, mwanaume huyo aliendelea kuishi moyoni mwake. Kila siku ilikuwa ni lazima kuingia katika chaneli yao iliokuwa YouTube na kuanza kumwangalia jinsi alivyokuwa akiimba, sauti yake nzuri ilimtetemesha, hakuhisi kama kungekuwa na mtu aliyekuwa na sauti nzuri kama ilivyokuwa kwa mwanaume huyo.
Wakati kichwa chake kikimfikiria Walter ndipo mwanaume mwingine akaanza kujisogeza. Huyu aliitwa Edmund, mwanaume aliyekuwa akisomea masuala ya IT hapo Oxford.
Siku ya kwanza Edmund alipomuona Catherine moyo wake ulitetemeka mno, hakudiriki kuyatoa macho yake kwa msichana huyo, alikuwa mzuri wa sura, alikuwa mrembo mno kiasi kwamba kila alipokuwa akimwangalia, hakuisha hamu kabisa.
Akaanza kujipendekeza, kitu cha kwanza alichokuwa akikihitaji ni kuwa rafiki yake, wazungumze kama marafiki lakini mwisho wa siku amwambie ukweli kwamba alikuwa akimpenda kupita kawaida.
Kwa msichana kama Catherine halikuwa jambo jepesi hata kidogo, alikuwa msichana mgumu kuzoeleka lakini kwa Edmund naye hakuwa mwanaume aliyekuwa na moyo mwepesi wa kukata tamaa.
Aliendelea kumfuatilia msichana huyo huku kila alipokuwa akimuona, alimfuata na kupiga naye stori. Catherine hakuwa akipenda ukaribu na mwanaume huyo lakini kwa kuwa alianza kumng’ang’ania sana mwisho wa siku akajikuta akiwa karibu naye.
Kichwa chake kilifikiria urafiki zaidi lakini kichwa cha Edmund kilifikiria mapenzi zaidi. Walikuwa karibu kiasi kwamba mpaka watu wengine wakahisi kwamba wawili hao walikuwa wapenzi.
Edmund hakutaka kukaa kimya, alijua kwamba kama wangezoeana zaidi basi suala la kaka na dada lingeingilia kati kitu kilichomfanya kuanza kumchombeza msichana huyo kwa maneno ya hapa na pale.
Siku za kwanza ilikuwa ngumu kwa msichana huyo kuelewa lakini baada ya Edmund kung’ang’ania zaidi, mwisho wa siku akampata msichana huyo na kuanza kuwa wapenzi.
“Edmund!” aliita msichana huyo.
“Unasemaje mpenzi!”
“Naomba nikuombe kitu!”
“Kitu gani?”
“Kuna mwanaume ninampenda. Tena zaidi ya ninavyokupenda wewe. Kama utataka tuendelee kuishi pamoja, sawa, ila tukubaliane kwamba kama mwanaume huyo akija tena maishani mwangu, naomba tu tuachane kwa amani,” alisema Catherine huku akimwangalia Edmun.
Edmund akakaa kimya kwa muda, akamwangalia Catherine, maneno aliyozungumza msichana huyo yalikuwa ni yenye kuumiza mno, hakuamini mtu kama Catherine angemwambia maneno hayo kwamba wawe wapenzi wa muda na kama mwanaume aliyekuwa akimpenda angerudi maishani mwake basi huyo ndiyo ungekuwa mwisho wao.
Hilo halikumuingia akilini hata kidogo lakini aliamini kwamba kama angemkatalia Catherine basi huo ndiyo ungekuwa mwisho wao hivyo alichokifanya ni kumkubalia ili aone huyo mwanaume alikuwa nani ambaye alitaka kulikatisha penzi lake kutoka kwa msichana huyo.
“Haina shida!”
“Una uhakika umekubali kutoka moyoni?”
“Ndiyo mpenzi!”
“Kabisa?”
“Kabisa.”
Catherine akamkumbatia mwanaume huyo, machozi ya furaha yalikuwa yakimtoka kwani hakuamini kama Edmund angekubaliana naye katika hilo.
Siku zikaendelea kukatika, moyo wa mwanaume huyo ulimkereketa, alitamani sana kumfahamu mwanaume huyo, alikuwa wapi, aliishi wapi na alikuwa akifanya ni kipindi hicho.

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA SITA

Alijaribu kumdadisi sana Catherine ili amwambie kuhusu mwanaume huyo lakini Catherine alikuwa mgumu kufanya hivyo, alichoambulia ni kujua jina lake tu kwamba aliitwa Walter.
“Jina tu linatosha,” alisema Edmund huku akionekana kuwa na hasira kali mno.
Edmund hakujiskia raha hata kidogo, kila alipokuwa akikaa, jina la Walter ndilo lililokuwa likimjia kichwani mwake. Akatokea kumchukia mwanaume huyo hata kabla hajamtia machoni mwake, alijua kwamba huyo ndiye alikuwa mtu pekee ambaye angelikatisha penzi lake kutoka kwa msichana huyo mrembo.
Hakuwa tayari kuona hilo likitokea, hakuwa tayari kuona akimkosa Catherine kwa kuwa kulikuwa na mwanaume aliyeitwa Walter katika dunia hii.
Hakuwahi kufikiria kama mwanaume huyo alikuwa Mtanzania, alichohisi ni kwamba alikuwa Muingereza hivyo kuanza kufuatilia chini kwa chini huku wakati mwingine akiuliza kama kulikuwa na mwanaume aliyekuwa na jina hilo.
Baada ya miezi minne kupita huku akiendelea kuwa katika penzi na Catherine ndipo akapewa taarifa kwamba mpenzi wake huyo alikuwa amepata ajali ya gari baada ya kugongwa na hivyo kukimbizwa katika Hospitali ya Queen Elizabeth.
Alichanganyikiwa, kama kichaa akaondoka nyumbani kwao na kuelekea katika hospitali hiyo. Alipofika, akauzuiliwa kwa kuwa msichana huyo alikuwa katika chumba cha upasuaji akipewa matibabu.
“Ilikuwaje?” aliuliza Edmund huku macho yake yakiwa mekundu mno na machozi kumtiririka mashavuni mwake.
“Alipata ajali ya gari!”
“Aligongwa au?”
“Alikuwa ndani ya gari lake, likagongwa na mgongaji kukimbia,” alijibu kijana aliyeishuhudia ajali hiyo ambaye ndiye alishughulika na watu wengine kumkimbiza msichana huyo katika hospitali hiyo.
Moyo wake ukachoma sana lakini hakuwa na jinsi. Siku hiyo hakuweza kumuona msichana huyo na hata wazazi wa msichana huyo walipofika, walimsifu Edmund kwa moyo wake kujitolea kuwa mtu wa kwanza kufika hospitalini hapo.
Siku iliyofuata ndipo wakaruhusiwa kumuona msichana huyo. Alikuwa ameumia vibaya kichwani mwake huku akiwa amefungwa bandeji kubwa kichwani na kwa maelezo ya madaktari waliwaambia kwamba fuvu la kichwa chake lilikuwa limepata ufa ambapo kwa kitaalamu lilijulikana kama skull fracture.
“Atapona?” aliuliza Bwana Gordon.
“Ndiyo! Kwa kawaida fuvu la kichwa likipata ufa, maumivu huwa kwa siku saba mpaka kumi, baada ya hapo mgonjwa atakuwa kwenye hali ya kawaida na ili fuvu lirudi katika hali ya kawaida, itamchukua miezi zaidi ya ishirini na nne, ila akiwa chini ya uangaliazi,” alisema Dk. Wayne.
Hizo zilikuwa ni kama siku za mateso kwa msichana huyo, alikuwa kimya kitandani na hata baada ya kuyafumbua macho yake hakuweza kuzungumza lolote lile, alikuwa kimya huku akiwaangalia watu waliokuwa katika chumba chake.
Siku ziliendelea kukatika, msichana huyo aliendelea kupatiwa matibabu hospitalini pale na baada ya siku tatu, Walter na Walker wakafika hospitalini hapo. Siku hiyo ilikuwa kizaazaa, kila mtu aliyekuwa akiwaona, alitaka kupiga nao picha, walikuwa maarufu, watu waliokuwa na vipaji ambavyo havikuwa vya kawaida kabisa.
Kwa kuwa muda wa kuona wagonjwa ulikuwa umefika, wakaruhusiwa kwenda moja kwa moja katika chumba kile. Edmund aliwaona lakini hakuwajua, alikuwa bize na masomo na hakuweza kufuatilia mambo ya habari au yale yaliyokuwa yakiendelea katika mitandao ya kijamii.
Aliwashangaa wanaume hao lakini wazazi wa Catherine walikuwa wakiwakumbuka vizuri, walikuwa marafiki wa binti yake. Kidogo Walter alipomuona Catherine kitandani pale moyo wake ukafurahi, wakamsogelea na kisha kumshika mkono.
Edmund alikuwa kimya akifuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Catherine aliposhikwa mkono, akayafumbua macho yake, tabasamu pana likamjia usoni mwake.
“Walter! Atlast you have come to see me,” (Walter! Hatimaye umekuja kuniona) alisema msichana huyo huku tabasamu pana likiendelea kuonekana usoni mwake. Edmund aliposikia jina la Walter tu, akashtuka, mapigo yake ya moyo yalikuwa yakidunda kwa nguvu, hakuamini kama mmoja wa mapacha wale walioungana alikuwa Walter ambaye Catherine alisema wangeachana kama tu mwanaume huyo angerudi maishani mwake.

Kupatikana kwa Walter kulimaanisha kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa uhusiano wake na msichana Catherine aliyekuwa kitandani. Moyo wa Edmund uliuma na kuchoma sana, kila alipokuwa akimwangalia mwanaume huyo ambaye aliungana na pacha mwenzake kulimaanisha kuwa huo ndiyo ungekuwa mwisho, yaani alitakiwa kusahau kila kitu kilichokuwa kimetokea.
Hakutaka kukubali, kwa wakati huo alikuwa tayari kupoteza kila kitu isipokuwa kumpoteza Catherine ambaye kila alipokuwa akimwangalia, kila siku uzuri wake uliongezeka maradufu.
Japokuwa alikuwa kitandani lakini kitendo cha kumuona Walter akiwa amefika mahali hapo, Catherine akaonekana kuwa na furaha mno, furaha ambayo Edmund mwenyewe alikiri moyoni kwamba hakuwahi kumuona msichana huyo akiwa kwenye furaha kama siku hiyo.
“Nilikukumbuka sana,” alisema Catherine huku akimwangalia Walter machoni.
“Nilikukumbuka pia. Sikutaka nione ukiendelea kuwa kwenye matatizo halafu mimi nipo. Nitahakikisha nakulinda maisha yangu yote,” alisema Walter.
Wazazi wa pande zote tatu walibaki wakiwaangalia watu hao, kadiri muda ulivyozidi kwenda mbele ndivyo ambavyo Edmund alivyozidi kuumia. Hakukuwa na mtu aliyefahamu kile walichokuwa wameongea zaidi ya wao wawili tu.
Alivumilia tu kukaa na hata alipokuwa akitambulishwa, alijibaraguza kwa kuonekana kuwa na tabasamu pana na wakati moyo wake ulikuwa ukiwaka moto kwa wivu.
Hakutaka kubaki mahali hapo, akaondoka na kurudi nyumbani. Ndani ya gari, alikuwa akilia kama mtoto, hakuamini kilichokuwa kikiendelea. Uwepo wa Walter ulimaanisha kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa maisha yake.
Alipofika nyumbani, akajifungia chumbani na kuanza kulia. Alipenda mpaka kufikia hatua ya mwisho kabisa, hatua ambayo aliona ikivuka hapo angekuwa kichaa, mapenzi yaliuendesha moyo wake, yalimsumbua kupita kawaida na ndiyo maana alipogundua kwamba mwanaume aliyekuwa amemuona alikuwa Walter, alihisi kitu chenye ncha kali kikiuchoma moyo wake.
“I must kill him,” (ni lazima nimuue)
Huo ndiyo ulikuwa uamuzi alioufikia kipindi hicho, hakutaka kuona akimkosa Catherine kwa sababu ya Walter, alitamani kuendelea kulilinda penzi lake lakini si kuona likipotea na kuchukuliwa na mtu mwingine.
Alichokifanya ni kuanza kufikiria ni watu gani ambao angewatumia kwa ajili ya kumuua Walter. Ilikuwa ni lazima afe kwani aliamini kwamba kama asingemuua basi ingekuwa ngumu sana kwake kuendelea na msichana huyo.
Wazo ambalo lilimjia kichwani lilikuwa ni kuwamaliza kwa kuwekea sumu ndani ya gari alilokuwa akilitumia. Alijua kwamba ilikuwa ni lazima kwa mwanaume huyo kufika hospitalini hapo mara kwa mara hivyo kama angeweka sumu, wakati wanaingia ndani ya gari, kuwashwa na kiyoyozi kuwashwa basi sumu ienee ndani ya gari na mwanaume huyo kufa.
“Yeah! I can use Hydrogen Selenide to kill him through air condition,” (Yeah! Naweza kutumia Hydrogen Selenide kumuua ndani ya gari lake)
Huo ndiyo ulikuwa mpango wake, hakutaka kujua ni watu wangapi angewaua mara baada ya kuweka sumu hiyo katika gari hilo, kitu alichokuwa akihitaji ni kuona anammaliza mwanaume aliyetokea kuumiza moyo wake.
Kuipata sumu hiyo kali halikuwa jambo jepesi, kulikuwa na ugumu sana na ilihitaji kupata barua maalumu kutoka serikali ambayo ingeeleza sababu ya yeye kuihitaji sumu hiyo ili kama kutaonekana hakukuwa na msingi wowote wa kupewa, basi asipewe na kama angepewa wakati wa kutumia ilikuwa ni lazima mtu wa serikalini awepo mahali husika.
Aliuona ugumu huo hali iliyomfanya kuwasiliana na rafiki yake, Thomson ambaye baba yake alikuwa daktari mkuu katika Hospitali ya The Royal London, alihitaji Thomson afanye kila linalowezekana mpaka baba yake ampe sumu hiyo ya gesi na kwenda kuitumia kumuua Walter.
“I will talk to him,” (nitazungumza naye)
“I just need your help Thom,” (ninahitaji msaada wako Thom) alisema Edmund huku akionekana kweli kuhitaji msaada.
“I will give you a hand,” (nitakusaidia)
Wakakubaliana na kuondoka mahali hapo. Thomson hakutaka kwenda kumuomba baba yake sumu hiyo kwani aliamini kuwa ni lazima amkatalie, alichokifanya ni kufanya kila liwezekanalo kuhakikisha anaiiba sumu hiyo hospitalini kwa kuchukua mtungi mdogo na kuondoka nayo.
Hilo ndilo alilolifanya, siku iliyofuata akaenda katika hospitali aliyokuwa akifanya kazi baba yake kwa lengo la kumsaidia kumbe upande mwingine alikuwa na jambo jingine kabisa alilotaka kulifanya.
Alipofika huko, akasalimiana na baba yake na muda wa kuondoka, akaanza kwenda maabara ambapo aliamini kwamba ni lazima gesi hiyo ingekuwa mahali huko.
Hakuonekana kuwa na hofu, hata madaktari waliokuwa wakimuona akielekea katika maabara ile hawakuwa na hofu naye kwani hiyo haikuwa mara ya kwanza kwenda huko, alikuwa akifika mara kwa mara na kuingia katika maabara hiyo.
Alisalimiana na watu mbalimbali mpaka alipoufikia mlango na kuingia ndani. Humo akakukatana na watu zaidi ya thelathini ambao walikuwa wakisomea uuguzi na walikuwa humo kwa ajili ya kuonyeshwa vitu mbalimbali kwa vitendo.
Naye akajifanya kuungana nao, macho yake hayakutulia, yalikuwa yakiangalia huku na kule, alipoiona mitungi ya gesi na mingine midogo kama fire extinguisher zile zinazokaa kwenye pikipiki, akaona kwamba hiyo ndiyo ilikuwa nafasi yake.
Wanafunzi wale walichukua dakika arobaini, walipomaliza wakaondoka na haraka sana Thomson kwenda kule kulipokuwa na mitungi ile. Kabla ya kuichukua, akaanza kuisoma ili kuipata gesi ya Hydrogen Selenide.
“Haipo!” alisema mara baada ya kuangalia sana.
“Nitrogen trioxide, Nitrosyl chloride, sasa nichukue ipi kama Hydrogen Selenide haipo?” alijiuliza, lakini hata kabla hajajijibu, akaichukua Nitrosyl chloride na kuuingiza ule mtungi mdogo ndani ya begi lake na kuondoka ndani ya maabara ile.
Akamfuata Thomson na kumkabidhi, akamwambia jinsi ambavyo ilitakiwa kutumika. Alimpa maelekezo kwamba ni lazima achukua mpira, aitoboe na haraka sana aingize mpira katika tundu la gesi ile kisha kuanza kuichukua kwa kuiweka katika kiyoyozi cha gari na kukaa humo, kiyoyozi kama kingewashwa, basi gesi hiyo ingetoka na kummaliza audui yake ndani ya gari.
“Nashukuru sana!” alisema Walter na kumpa Thomson zawadi ya paundi elfu mbili ambazo ni zaidi ya milioni nne kama shukrani kwa kile alichomfanyia.
****
Kila Muingereza alijua kwamba Walter na Walker walikuwa nchini Uingereza. Watu wengi walijazana katika Hospitali ya Queen Elizabeth kwa ajili ya kuwaona mapacha hao waliokuwa gumzo kila kona duniani.
Wale waliokuwa katika miji mingine kama Liverpool, Newcastle, Manchester na sehemu nyingine wakaondoka kuelekea jijini London kwa ajili ya kuwaona mapacha hao waliokuwa na vipaji visivyo vya kawaida.
Walikuwa ndani ya hospitali hiyo huku watu wengi wakiwa nje. Kila mtu alitamani kwenda kuwaona lakini hakukuwa na mtu aliyepewa nafasi, wengi wakaambiwa kwamba walitakiwa kusubiri mpaka watu hao watakapoondoka, wawapige picha kwa mbali lakini si kuwasogelea.
Polisi walikuwa makini, kuwalina Walter na Walker haikuwa kazi ndogo hata kawaida. Watu walisumbua, walipata kazi kubwa ya kuwalinda kuhakikisha hakuna mtu mbaya yeyote ambaye anawasogelea na kuwafanya kitu chochote kile.
"Tunataka kuwaona! Mbona jana nasikia watu waliowaona hapa hospitali ila leo mnatukatalia?” alihoji jamaa mmoja, alionekana kuwa na hasira.
“Nyie subirini! Jana ni jana na leo ni leo!”
“Haiwezekani bwana. Yaani kuwaona mnataka mpaka tufanye fujo?” alihoji jamaa huyo.
Ilikuwa kazi ngumu kuwaona watu hao. Walter na Walker waliendelea kukaa hospitalini huku wakimfariji Catherine aliyekuwa ameanza kupata nafuu, ilipofika majira ya saa kumi na moja jioni, kama kawaida wakatoka tayari kwa kuondoka mahali hapo.
Walipotoka nje, polisi wakafanya kazi ya ziada kwani kila mmoja alitaka kuzungumza nao huku wengine wakiwa na vitu vyao kwa ajili ya kusainiwa. Kwa mwendo wa taratibu, wakaanza kusogea kule watu walipokuwa na kuanza kusaini vitabu vyao huku wengine wakiwapiga picha.
Waliwafurahisha watu, walipomaliza, wakaanza kupiga hatua na wazazi wao kuelekea katika maegesho ya magari kwa ajili ya kuondoka mahali hapo. Dereva alikuwa ndani ya gari hilo, alikuwa amelala, wakaufungua, hawakujali sana, walichokifanya ni kuufungua mlango wa gari hilo lililokuwa limefungwa vioo, hata kabla ya kuingia ndani, hapohapo wakaanguka chini, wakaanza kutoka mapovu na miili kuwatetemeka.
Kila mtu aliyekuwa mahali hapo alishangaa, wazazi wao wakasogea kuangalia kulikuwa na kitu gani kilichokuwa kimewapata lakini nao waliposogea, wakaanza kusikia kivunguzungu, nao hapohapo wakaanguka kitu kilichomshtua kila mtu aliyekuwa mahali hapo, hakukuwa na mwingine aliyelisogelea gari lile kwani tayari kukaanza kusikika harufu fulani ambayo haikuwa ya kawaida.

Edmund alidhamiria kufanya mauaji, hakutaka kufikiria utu, aliamini kwamba kama Walter angekufa basi ingekuwa rahisi kwake kuendelea kuishi na Catherine ambaye alikuwa akimpenda kwa mapenzi ya dhati.
Sumu yake aina ya Nitrosyl chloride alikuwa nayo chumbani kwake, ilikuwa ni lazima kwenda kwenye gari la mapacha hao walioungana kwa ajili ya kuiweka na kisha kuondoka zake.
Hakutaka kuchelewa, kwa kuwa siku hiyo Walter, Walker na wazazi wao walikuwa wakienda hospitalinikatika Hospitali ya Queen Elizabeth kwa ajili ya kumuona Catherine, naye akapanga kwenda huko kwa muda wake.
Aliamini kwamba huko kungekuwa na watu wengi, hakutaka kwenda kikawaida, alifahamu jinsi polisi walivyokuwa wakivaa, suala la kutafuta sare wala halikuwa gumu kwani aliwasiliana na rafiki yake ambaye alikuwa akishona sare hizo kwa ajili ya kuigiza filamu mbalimbali nchini Uingereza, yeye akampelekea mavazi ya polisi ambayo kwa kuyaangalia kwa mbali, hayakutofautiana mpaka pale utakapoyachunguza zaidi.
Akaingia ndani ya gari lake na kuondoka huku akiwa na mtungi huo mdogo. Hakuchukua muda mwingi akafika katika hospitali hiyo, ni kama watu walijua kwamba mapacha hao walioungana wangefika hapo, wengi walikusanyika kwa ajili ya kuwashuhudia tena.
Edmund hakuteremka katika gari lake, alitulia huko huku moyo wake ukichoma kupita kawaida, baada ya kukaa kwa saa moja, akayaona magari yakianza kuingia hapo, akabaini kwamba gari moja lilikuwa limewabeba mapacha wale, hivyo akaanza kufuatilia.
Watu wakaanza kusogea kule kulipokuwa na magari yale huku wakiwa na simu zao mikononi na wengine wakiwa na kamera, walitaka kupiga picha kila kitu kilichokuwa kikiendelea mahali hapo.
Baada ya dakika kadhaa, mapacha hao wakateremka huku wakiwa na ulinzi mkubwa, kama kawaida yao wakaanza kuwapungia watu mikono huku wakipiga hatua kuelekea ndani.
“Can you sign an autograph on my book, pleaseee?” (unaweza kusaini kwenye kitabu changu?) aliuliza msichana mmoja kwa sauti ya upole kabisa, japokuwa kulikuwa na ulinzi mkubwa, yeye alifanikiwa kupenya, na walinzi walipotaka kumtoa, Walke akawazuia.
“Mine or his?” (yangu au yake?) aliuliza Walker.
“Both of you,” (nyie wote)
“Okey.” (sawa)
Hilo halikuwa tatizo, wakafanya kama msichana huyo alivyotaka na kisha kupiga naye picha na kuanza kuelekea ndani ya hospitali hiyo. Bwana Cassian na mkewe, Naseku walikuwa na furaha kupita ajabu, hawakuamini kama watoto wao walikuwa wakikubalika kiasi hicho japokuwa walionekana kuwa na matatizo.
Wakati watu wakiwa bize, haraka sana Edmund akateremka kutoka kwenye gari lake na moja kwa moja kuanza kusogea kule gari lililokuwa limewabeba mapacha wale lilipokuwa huku mkononi akiwa na mtungi wa gesi.
Alipofika, akaangalia ndani, akamuona dereva akiwa anavuta sigara, akaanza kulisogelea gari zaidi, alipolifikia, akakigonga kioo, dereva akafungua.
“Unajua kwamba unavunja sheria?” aliuliza Edmund huku akimwangalia dereva.
“Sheria gani?”
Akamuonyeshea bango dogo lililoandikwa kwamba hakukuwa na mtu aliyekuwa akiruhusiwa kuvuta sigara katika eneo la watu wengi likiwemo hospitali kama hiyo.
Haraka sana dereva akaizima sigara yake kwani kwa jinsi Edmund alivyoonekana, jinsi alivyokuwa amevaa sare za bandia za kipolisi, aliamini kwamba mwanaume huyo alikuwa polisi.
“Samahani sana.”
“Hebu teremka, nenda nyumba ya gari nikukute huko. Nataka nipekue, unaweza kuwa na bangi au madawa ya kulevya humu,” alisema Edmund, kwa kuwa alikuwa amefanya kosa, haraka sana dereva akafungua mlango na kwenda nyuma, Edmund akaingia ndani, akachukua sumu ile na kuanza kuipulizia katika sehemu ya kiyoyozi, aliipulizia kwa wingi huku kiyoyozi hicho kikiwa kimezimwa, alipomaliza, akafunga mlango.
“Una bahati sikukuta kitu. Sijakukataza kuvuta, kama utaendelea, hakikisha unafunga vioo, washa kiyoyozi na ndipo uvute, vinginevyo sitokuelewa,” alisema Edmund huku akiwa anamwangalia dereva huyo.
“Haina shida.”
Dereva akaingia ndani, kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kufunga mlango, kioo kikashushwa, akachukua sigara nyingine, akaiwasha na kuanza kuivuta.
“Alisema na kiyoyozi,” alisema na hapohapo kuwasha kiyoyozi.
Hilo likaonekana kuwa kosa kubwa kwani hapohapo sumu iliyokuwa imepuliziwa humo ikaanza kutoka mfululizo. Ilikuwa sumu mbaya ambayo ilikuwa ikiingia mwilini mwa binadamu kwa haraka na kuharibu ini huku ikianza kuusimamisha moyo na kuziba mishipa ya damu.
Dereva hakuchukua hata dakika moja, palepale alipokuwa, akatulia tuli, mwili ukaanza kukakamaa, mapovu yakaanza kumtoka mdomoni na hatimaye kutulia tuli.
***
Kila mtu aliyekuwa ameliona tukio lile aliogopa, wote wakasogea nyuma kwani hali ilionekana kutokuwa nzuri. Watu walibaki wakiwaangalia Walter na Walker walivyokuwa wakihangaika pale chini walipokuwa na wazazi wao.
Hakukuwa na mtu aliyetoa msaada zaidi ya watu hao kuanza kupiga picha kana kwamba walikuwa waandishi wa habari. Kwa kuwa ilionekana kama kulikuwa na gesi iliyokuwa imewadhuru, hapohapo wanaume wawili wakajifunga vitambaa puani na mdomoni, wakasogea kule walipokuwa watu wale na kuanza kuwasaidia, machela zikaletwa, wakapakizwa na kuanza kuingizwa ndani.
“Nini kimetokea?” lilikuwa swali la kwanza alilouliza nesi.
“Saidia kwanza. Tunahisi ni sumu!”
“Sumu?””Ndiyo! Husikii harufu ya Nitrosyl chloride? Ni sumu hatari sana hii,” alisema mwanaume mmoja aliyekuwa akitoa msaada.
Kila mtu akashtuka, dunia ikaingiwa na majonzi mazito, hakukuwa na aliyeamini kile kilichokuwa kimetokea. Kila mtu alikuwa na hofu, wengi wakaona kwamba huo ndiyo ulikuwa mwisho wa mapacha wale.
Lawama zote zilikwenda kwa Waingereza, ilikuwaje washindwe kuzuia jambo hilo na wakati walijua kabisa kwamba watu hao walikuwa maarufu hivyo kungekuwa na watu wengi waliotaka kuwaua kwa kuwa tu waliwaoneka wivu?
Kila mmoja akahisi kwamba kulikuwa na kiongozi mkubwa serikalini alikuwa amehusika katika tukio hilo la mauaji. Waziri mkuu nchini humo, Bwana Sinclaire hakutaka kuchelewa, haraka sana akawaita waandishi wa habari na kuwaomba msamaha kwa lililotokea lakini pia ilikuwa ni lazima kuhakikisha kwamba mtu aliyefanya tukio hilo akipatikana haraka iwezekanavyo.
“Na hali zao?” aliuliza mwandishi mmoja.
“Bado sijajua chochote kile kwa kuwa baada ya kupewa taarifa nikawaita kwa ajili ya kuzungumza nanyi,” alisema Bwana Sinclaire huku akiwaangalia waandishi waliokuwa wamemzunguka.
Hospitalini hakukukalika, kila mtu alikuwa na hofu, sumu ambayo walikuwa wamepuliziwa ilikuwa ni sumu hatari ambayo ilikuwa ikitumika kuulia wanyama wakubwa msituni na samaki baharini.
Kitendo cha kuwapata kidogo tayari ilionyesha nguvu zake kiasi kwamba walianguka na kupoteza fahamu huku hali ya miili yao ikianza kubadilika ghafla pamoja na wazazi wao.
Madaktari walikuwa na kazi kubwa kuokoa maisha ya mapacha hao na wazazi wao. Haraka sana wakawapeleka katika chumba cha upasuaji na kuanza kuwahudumia haraka sana. Ilikuwa kazi kubwa kwani walitakiwa kwanza kuondoa sumu ile ambayo ilikuwa ikisambaa taratibu katika miili yao.
Wakawatundikia dripu zilizokuwa na maji yaliyotiwa dawa ambazo zilikuwa na uwezo wa kuruhusu matone kumi na tano kwa dakika moja tu.
“Hii itawasaidia!” alisema daktari mmoja.
“Kweli?” aliuliza nesi.
“Ndiyo! Ila hatutakiwi kuamini sana kwani kadiri dakika zinavyozidi kwenda mbele, mapigo yao yanazidi kushuka,” alisema daktari huyo.
“Kwa hiyo wanaweza kufa?”
“Uwezekano wa kupona ni asilimia thelathini na kufa ni asilimia sabini. Cha msingi ni kumuomba Mungu tu,” alisema daktari huyo, pamoja na utaalamu wake mkubwa lakini kwa sumu waliyokuwa wamepuliziwa watu wale, ilionekana kumshinda.
Serikali ikaamua kuongeza madaktari wengi kumi kutoka katika hospitali nyingine. Ilikuwa ni lazima wapambane usiku na mchana kuokoa maisha ya watu hao kwani kama wangekufa katika ardhi yao ingekuwa aibu sana dunia nzima hivyo iwe isiwe ilikuwa ni lazima kupambana kuokoa hali zao.

Polisi jijini London walichanganyikiwa, hawakuamini kile kilichotokea kama kweli kilitokea katika ardhi ya Uingereza. Kila mtu alikuwa akizungumza lake, wengi waliona nchi hiyo ikiwa na uzembe mkubwa kiasi kwamba walishindwa kuweka ulinzi wa kutosha kuhakikisha vijana hao wanakuwa salama mpaka pale ambapo wangeondoka nchini humo.
Haraka sana, mkuu wa jeshi la polisi nchini humo, Bwana Simon Pegg akazungumza na kitendo cha Usalama wa Taifa, Military Intelligence Section 6 kwa lengo la kutaka kujua kila kitu kilichokuwa kimetokea.
Haraka sana maofisa wa Usalama wa Taifa wakaanza kufanya kazi hiyo. Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kwenda mpaka katika hospitali hiyo kwa lengo la kuangalia kwenye kamera kila kitu kilichokuwa kimetokea.
Walipofika huko, wakapelekwa katika chumba kilichokuwa na televisheni ambacho kiliunganishwa na kamera thelathini na sita zilizokuwa katika hospitali hiyo.
Walitaka kujua kila kitu kilichokuwa kimetokea tangu mapacha hao walipofika katika hospitali hiyo mpaka tukio la kuupatwa na sumu lilivyotokea. Hilo halikuwa tatizo, kila kitu kilikuwa kimerekodiwa na kilichofanyika ni kuonyeshwa kila kitu kilichotokea.
Walianza kufuatilia. Dakika kumi kabla ya mapacha hao kufika mahali hapo wakaanza kuangalia mazingira jinsi yalivyokuwa. Hakukuwa na mtu yeyote ambaye walimtilia shaka, kila aliyekuwa mahali hapo alionekana kuwa na hamu kubwa ya kuwaona mapacha hao na ndiyo maana kila mmoja alishikilia simu yake tayari kwa kupiga picha.
Baada ya dakika kadhaa, wakayaona magari yaliyokuwa kwenye msafara mfupi wa mapacha hao ukianza kuingia ndani ya eneo la hospitali hiyo. Kila mmoja alikuwa akiyaangalia kwa makini mpaka pale yalipokwenda kupaki.
Waliwaona walipokuwa wakiteremka, lengo lao halikuwa kuwaangalia mapacha hao bali lengo lao kubwa ni kuangalia ni nani alikuwa amekwenda katika gari lile baada ya mapacha hao kuteremka.
Wakati wameelekea ndani, wakamuona polisi mmoja akiteremka katika gari lake huku mkononi akiwa na kitu ambacho hawakuwa wakikifahamu kwa kuwa ilikuwa ni picha ya mbali kabisa.
Polisi yule akaanza kutembea mpaka lilipokuwa gari lile walilokuwa mapacha wale na kuanza kuzungumza na dereva. Hawakujua walizungumza kitu gani lakini baada ya dakika moja wakamuona dereva akiteremka na kuelekea nyuma ya gari na polisi yule kuingiza kichwa kwa ndani.
“Hebu vuta kwa karibu, vuta zaidi,” alisema Bwana Pegg ambaye naye alifika kwa ajili ya kuangalia.
Picha ya karibu ikavutwa zaidi, halafu akamwambia arudishe nyuma na kisha kutakiwa kuvuta kile kitu kilichokuwa mkononi mwake, walitaka kujua kilikuwa kitu gani. Kilipovutwa, hakukuwa na mtu aliyeamini, ulikuwa mtungi mdogo wa gesi kali aina ya Nitrosyl Chloride iliyokuwa ikitumika kuulia samaki baharini na wanyama wakali.
“Huyu ndiye aliyeweka hiyo gesi ambayo imekuwa sumu. Hebu mvute karibu. Ni polisi kweli huyu?” aliuliza.
Jamaa aliyekuwa ameshikilia kipanya akaanza kuvuta picha kwa karibu zaidi. Walikuwa wakitaka kuona kama kweli huyo alikuwa polisi au la. Alipovutwa, waliangalia sare zake, hazikuwa origino kama za polisi wengine kitu kilichomaanisha kwamba mwanaume huyo ndiye aliyefanya tukio hilo la kuwamaliza mapacha hao.
“Vuta sura yake, piga picha halafu anza kupeleka sehemu zote. Nahitaji ndani ya nusu saa mtu huyo awe amekamatwa,” alisema Bwana Pegg na hapohapo picha ya Edmund kuchapishwa na kuanza kupelekwa sehemu mbalimbali, hasa katika vituo vya polisi.
Na kwa sababu waliipata picha ya sura yake, walichokifanya ni kutaka kupata data zote kuhusu mwanaume huyo ambaye waliamini kwamba kama alikuwa ni rais wa Uingereza basi ilikuwa ni lazima kujiandikisha kama rais wa nchi hiyo na hivyo kuwa na data zake zote.
Wakaiingiza picha ile katika kompyuta ambayo ilikuwa na taarifa ya raia wote wa Uingereza na kuanza kumtafuta mwanaume huyo. Zaidi ya picha elfu moja zilikuwa zikipita ndani ya sekunde sitini na baada ya dakika tano, picha yake ikasimama na neno kubwa lililosomeka Match 100% likionekana vizuri kwamba picha ile iliyokuwa imeingizwa ilifanana kwa asilimia mia moja na picha iliyokuwa ikionekana.
“Anaitwa Edmund Jefferson. Anaishi hapa Londo katika Mtaa wa Camberwell nyumba namba 297. Kikosi cha askari ishirini wanatakiwa kwenda huko haraka sana,” alisema Pegg na hivyo kikosi cha kwenda huko kupigiwa simu na kutumiwa picha ya mtu aliyekuwa akitakiwa na maelezo yote kuhusu yeye.
***
Kidogo moyo wa Edmund ukajisikia amani, akahisi kwamba alifanikiwa kwa asilimia mia moja kufanya jambo lile lililompa uhakika kwamba mbaya wake, Walter alikufa katika gesi ile kali.
Akaondoka hospitalini hapo, njiani, redioni ni taarifa za mapacha hao ndizo zilzokuwa zikisikika kila kona kwamba walikuwa wamekufa. Wakati dunia ikihuzika na kulia, kwake hali ilikuwa ni tofauti kabisa kwani moyo wake ulikuwa na furaha kupita kawaida.
Alipofika nyumbani, hakutaka kubaki mahali hapo, ilikuwa ni lazima kuondoka nchini humo kwa kuamini kwamba mara baada ya kugundulika ilikuwa ni lazima kutafutwa kila kona. Akachukua baadhi ya vitu vyake na kuondoka zake huku lengo lake kubwa likiwa ni kuelekea nchini Ireland ambapo aliamini kwamba huko angeishi kwa amani kabisa.
Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumpigia simu rafiki yake, Thom na kumshukuru huku akimwambia kwamba alikuwa akijiandaa na safari ya kuelekea nchini Ireland.
“Nimefanikisha. Nashukuru sana,” alisema Edmund, akachukua begi lake lililokuwa na baadhi ya vitu na kuondoka mahali hapo.
Akaingia ndani ya gari lake, akaliwasha, hakutaka kuaga, alipoingia barabarani tu, akasikia ving’ora vya polisi kwa mbali, akapishana nao, yaani wakati yeye akiondoka nyumbani kwao, nao ndiyo walikuwa wakiingia.
“Hamuwezi kunipata!” alisema Edmund huku akitoa tabasamuu pana ambapo alipokuwa akiangalia nyuma kupitia kioo cha gari cha pembeni, akawaona polisi wakiingia katika eneo la nyumba yao. Akaongeza gia na kukanyaga moto. Akapotea eneo hilo.

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA SABA

Kidogo moyo wa Edmund ukajisikia amani, akahisi kwamba alifanikiwa kwa asilimia mia moja kufanya jambo lile lililompa uhakika kwamba mbaya wake, Walter alikufa katika gesi ile kali.
Akaondoka hospitalini hapo, njiani, redioni ni taarifa za mapacha hao ndizo zilzokuwa zikisikika kila kona kwamba walikuwa wamekufa. Wakati dunia ikihuzika na kulia, kwake hali ilikuwa ni tofauti kabisa kwani moyo wake ulikuwa na furaha kupita kawaida.
Alipofika nyumbani, hakutaka kubaki mahali hapo, ilikuwa ni lazima kuondoka nchini humo kwa kuamini kwamba mara baada ya kugundulika ilikuwa ni lazima kutafutwa kila kona. Akachukua baadhi ya vitu vyake na kuondoka zake huku lengo lake kubwa likiwa ni kuelekea nchini Ireland ambapo aliamini kwamba huko angeishi kwa amani kabisa.
Kitu cha kwanza kabisa kilikuwa ni kumpigia simu rafiki yake, Thom na kumshukuru huku akimwambia kwamba alikuwa akijiandaa na safari ya kuelekea nchini Ireland.
“Nimefanikisha. Nashukuru sana,” alisema Edmund, akachukua begi lake lililokuwa na baadhi ya vitu na kuondoka mahali hapo.
Akaingia ndani ya gari lake, akaliwasha, hakutaka kuaga, alipoingia barabarani tu, akasikia ving’ora vya polisi kwa mbali, akapishana nao, yaani wakati yeye akiondoka nyumbani kwao, nao ndiyo walikuwa wakiingia.
“Hamuwezi kunipata!” alisema Edmund huku akitoa tabasamuu pana ambapo alipokuwa akiangalia nyuma kupitia kioo cha gari cha pembeni, akawaona polisi wakiingia katika eneo la nyumba yao. Akaongeza gia na kukanyaga moto. Akapotea eneo hilo.
*
Ilikuwa ni lazima kuondoka kuelekea nchini Ireland, hakutaka kuonekana kwa kuhisi kwamba ilikuwa ni lazima kutafutwa na polisi kwa kile alichokuwa amekifanya. Edmund hakuwa na uhakika kama angegundulika, hakuwa ameziona kamera ndogo za CCTV zilizokuwa zimefungwa kila kona hospitalini hapo.
Aliendesha gari lake kwa mwendo wa kawaida kabisa, hakutaka kushtukiwa na polisi ambao mara nyingi magari yao yalikuwa mitaani yakitembea huku na kule kuhakikisha usalama kila kona hapo London.
Wazo lake kwa wakati huo lilikuwa ni kwenda Olympia London ambapo huko angenyoosha moja kwa moja mpaka Twickenham, huko angepumzika kidogo kabla ya kuelekea katika Jiji la Reading, angeingia Swindon, Bristol ambapo hapo angechukua treni ya chini ya maji mpaka nchini Ireland.
Akaliingiza gari mpaka katika Barabara ya Brixton na kuanza kuelekea Upande wa Kusini huku lengo lake likiwa ni kufika West Noorwood ambapo hapo angechukua barabara nyingine ya Tooting Bec ambayo ingempelekea Upande wa Mashariki mpaka Battersea, huko angechukua Barabara ya S Circular ambayo ingempeleka mpaka Twickenham.
Kuanzia hapo Camberwell alichukua saa tatu mpaka kufika huko. Kila alipopita, hakukuwa na tatizo lolote lile, alihisi kwamba hakukuwa na mtu yeyote aliyekuwa akimfuatilia. Hapo Twickenham akaendelea mbele na baada ya saa moja akafika Felthman ambapo hapakuwa mbali kutoka katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Heathrow.
Hapo ndipo kulipokuwa na barabara mbili zilizoungana, moja ilikuwa ikienda upande wa Kaskazini ambayo ilikwenda mpaka Harmodsworth ambapo kama angekata kulia basi angekwenda mpaka Dorney na kushuka kwa kuelekea chini.
Ilikuwa ni njia ndefu ambayo aliamini angetumia zaidi na saa tano. Kwake, njia hiyo haikuwa salama hata kidogo, kwa kukubali kwenda huko kulimaanisha kwamba ilikuwa ni lazima angekamatwa na polisi kama tu wangekuwa wakimtafuta kwa kuwa barabara hiyo haikuwa mbali na uwanja wa ndege.
Akaamua kuichukua Barabara ya ya Engham ambayo ilimpeleka mpaka Thorpe alipokutana na barabara nyingine ambayo ndiyo ilikuwa ikimpeleka mpaka Bristol.
Katika kila njia alizopita kulionekana kuwa na nafuu kwake, na kwa sababu ilikuwa ni siku ya Jumamosi, siku ambayo mashabiki wa timu za mipira, raga na kriketi walikuwa wakienda viwanjani, njiani alikuwa akipishana na watu wengi kiasi kwamba kwa mhalifu kama yeye ilikuwa rahisi sana kwenda bila kukamatwa.
Aliendesha gari mpaka katika kituo cha mafuta cha Shell ambapo haraka sana akateremka na kuchukua kadi yake, akaiingiza katika kitundu kidogo, akaandika lita alizotaka na kuweka mpitra katika mdomo wa gari lake, akajaza, akaichukua gari lake na kuondoka mahali hapo.
Wakati hayo yote yakiendelea, hakujua kama alikuwa akitafutwa na polisi. Wakati akikaribia Bristol ndipo alipoamua kufungua redio kusikiliza kilichokuwa kikiendelea. Katika kila redio taarifa ambayo ilikuwa ikitangazwa sana ilikuwa ni kuhusu tukio lile lililotokea hospitalini.
Alisikiliza kwa makini, alitaka kujua kama mapacha hao walikufa au la. Kila aliposikiliza, alisikia kwamba walikuwa kwenye hali mbaya m,no ambapo muda wowote ule wangefariki dunia.
Hakuhuzunika, ndiyo kwanza akafurahia kwa kuona kwamba alimkomoa na kama kukosa basi wakose wote. Wakati akiendelea kusikiliza ndipo akapokea taarifa kwamba tayari mtu aliyefanya tukio hilo alijulikana, na mpaka jina lake likatajwa.
Hakushangaa kwani hata alipoondoka nyumbani aliwaacha polisi wakiingia hapo. Aliendelea mbele mpaka kufika Bristol huku akiwa amechoka. Wazo lake kwa kipindi hicho lilikuwa ni kuendelea na safari kwa gari lake mpaka katika kituo cha treni cha Bristol Packway.
Akalipaki gari lake nje ya kituo hicho katika sehemu husika na kisha kuelekea ndani. Alipoanza kushusha ngazi, kitu cha kwanza kabisa alichokutana nacho kilikuwa ni picha zake nyingi zilizobandikwa kwenye kuta mbalimbali.
Alishtuka, hakuamini kama kwa saa chache angekuwa kwenye kila kona nchini Uingereza. Haraka sana akafungua begi lake, akatoa kofia yake nyekundu na kuivaa, baada ya hapo akaanza kutembea kwa kujiamini mpaka sehemu kulipokuwa na watu wengi ambapo walikuwa wakiweka sarafu kwenye kifaa kimoja na chuma kujifungua.
Alipofika, naye akaweka, chuma kikapanda na kuingia ndani. Kwa mwendo wa haraka sana akaanza kuelekea kulipokuwa na watu wengi waliokuwa wakisubiri treni na kusimama hapo.
“Treni itafika baada ya dakika chache, ndiyo inaondoka katika kituo cha Reading, baada ya dakika chache itaingia mahali hapa,” ilisikika sauti nyororo ya msichana kwenye spika zilizokuwa humo.
Moyo wake ulikuwa ukimuomba Mungu, alitaka kuondoka mahali hapo salama kwani kama angeendelea kubaki nchini Uingereza ilimaanisha kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wake.
Wakati akiwa amesimama mahali hapo, akasikia watu waliokuwa nyuma yake wakilizungumzia suala la mapacha wale kupuliziwa gesi ndani ya gari. Akajificha zaidi lakini ghafla watu wale wakanyamaza kana kwamba waliambiwa wanyamaze, wakati akijiuliza kuhusu ukimya huo wa ghafla, akashtukia akishikwa bega kwa nyuma na kutakiwa kugeuka.
“Turn around, please...” (geuka tafadhali) ilisikika sauti ya mwanaume mmoja nyuma yake.
****
Catherine alikuwa akilia, hakuamini kilichokuwa kimetokea, kitendo cha kuambiwa kwamba rafiki yake, Walter alikuwa amepuliziwa gesi yenye sumu moyo wake ulimuuma mno na kumfanya kulia kila wakati.
Alijiona kuwa yeye ndiye mtu aliyesababisha lile lililotokea, alijihukumu moyoni mwake na muda wote alikuwa akiwaambia wazazi wake kwamba yeye ndiye alikuwa chanzo kwani bila yeye aliamini mapacha hao wasingeweza kupata tatizo walilokuwa wamelipata.
Kwa kuwa alikuwa akijisikia nafuu, hakutaka kubaki katika chumba kile alicholazwa, aliomba sana aende katika chumba walichokuwa mapacha wale ili aone walikuwa wakiendeleaje. Hilo lilikuwa gumu kuruhusiwa kwa kuwa tangu tukio la kupuliziwa gesi iliyokuwa na sumu hakukuwa na mtu yeyote aliyeruhusiwa kuingia ndani ya chumba kile.
Kila kona duniani ni stori za mapacha hao ndizo zilizokuwa zikisikika. Watu waliichukua picha ya Edmund na kuiweka katika mitandao ya kijamii, Watanzania hawakuwa nyuma, wao ndiyo walikuwa watu wa kwanza kuichukua picha hiyo na kuisambaza kwa nguvu zote kwani hakukuwa na mtu aliyehitajika mikononi mwa polisi kama ilivyokuwa kwa Edmund.
Mbali na mapacha hao, Walter na Walker pia wazazi wao walikuwa hoi kitandani. Tangu walipolazwa, mpaka inaingia siku ya pili hakukuwa na yeyote aliyerudiwa na fahamu.
Mapigo ya mioyo yao ilikuwa ikidunda kwa mbali sana hali iliyoonyesha kwamba muda wowote ule watu hao wanne wangefariki dunia.
Wakati hayo yote yakiendelea, tayari taarifa za kwanza zilionyesha kwamba polisi walikwenda nyumbani kwa Edmund siku ileile lakini hawakufanikiwa kumpata na hivyo kuhitaji msaada wa kamera za CCTV. Ilikuwa vigumu kumpata kwa siku hiyo kwa kuwa tu mitaani kulikuwa na idadi ya watu wengi kutokana na Jumamosi kuwa siku ya mechi mbalimbali nchini humo.
Picha zilipigwa, gari lake lilionekana sehemu nyingi likipita, hawakujua mahali lilipokuwa likielekea lakini baada ya kufika Bristol, hakukuwa na mtu aliyejua mahali gari hilo lilipokuwa.
“Lilikwenda wapi?” aliuliza jamaa mmoja.
“Hatujui! Au aliondoka kwenda kwenye kituo cha treni kupanda treni?” aliuliza mwanaume mwingine.
“Ni vigumu! Inawezekanaje ukatafutwa halafu ukaenda kupanda treni? Hakuna kitu kama hicho,” alisema mwanaume mwingine kabisa.
Kila mtu hakujua mahali alipokuwa Edmund, alionekana kama mzimu kwani kwa nchi kama Uingereza ilikuwa vigumu sana kumkosa mtu aliyekuwa akitafutwa kutokana na teknolojia yao kuwa juu sana.
Mpaka inafika wiki ya kwanza, hakukuwa na mtu aliyejua mwanaume huyo alipokuwa. Kila mmoja akajiuliza kwamba kama mwanaume huyo aliondoka nchini Uingereza, alipitia wapi mpaka kwenda kwenye nchi nyingine? Kila walipojiuliza, walikosa majibu.

Polisi walikuwa wakihangaika kila kona kumtafuta Edmund ambaye mpaka muda huo hawakujua mahali alipokuwa. Kwenye kamera zao, waliliona gari lake lakini baada ya muda likawapotea. Wakahakikisha wanaweka ulinzi kila kona kuhakikisha mwanaume huyo hatoki kuelekea sehemu yoyote ile.
Polisi waliokuwa katika Kituo cha Treni cha Bristol walikuwa wametulia kuhakikisha ulinzi unakuwa salama mahali hapo. Walimwangalia kila mtyu aliyepita ili kuona kwamba ni lazima wahakikishe kwamba ndani ya kituo hicho, mwanaume huyo haingii kabisa kwani kama wangemkosa mahali hapo na kuondoka kuelekea nchi nyingine basi wasingeweza kumpata tena.
Wakiwa hapo, ghafla polisi wawili wakamuona mwanaume ambaye kwa muonekano alifanana kabisa na Edmund japokuwa alijaribu kuvaa kofia ambayo aliamini kwamba ni lazima ajifiche na asionekane kwa watu wengine.
Hawakutaka kuchelewa, wakaanza kumfuata kule alipokuwa. Kwa jinsi alivyokuwa akitembea huku akiangalia huku na kule, ikawapa uhakika kwamba mwanaume huyo alikuwa Edmund, na alipokwenda na kusimama sehemu kwa ajili ya kupanda treni, wakasimama kwa mbali nyuma yake na kuanza kumwangalia vizuri.
“He is the one, let’s arrest him,” (ndiye yeye, tukamuweke chini ya ulinzi) alisema polisi mmoja.
Wakaanza kumfuata, walipomkaribia, mmojawapo akamshika begani kwa lengo la kumtaka ageuke ili kama ni yeye basi wamuweke chini ya ulinzi lakini kama si yeye, wamuombe radhi.
Edmund alihisi kabisa mtu aliyemshika bega kwa nyuma alikuwa akimfahamu na ndiyo maana aliamua kumfuata na kumtaka ageuke ili atambulike na kukamatwa.
Wakati mapigo ya moyo yakimdunda kwa nguvu tena huku akitetemeka, mara zikaanza kusikika kelele kutoka kwa binti mmoja aliyetoka chooni, alikuwa akikimbia kwa mwendo wa kasi.
“A bomb....a bomb...” (bomu...bomu...) alisema msichana huyo huku akikimbia kutoka chooni.
Vichwa vya Waingereza wengi vilikumbuka tukio ambalo lilitokea mwezi uliopita jijini Manchester ambapo kituo cha treni kililipuliwa kwa bomu lililowekwa na Waarabu kutoka Mashariki ya Kati. Waliposikia hivyo, hakukuwa na mtu aliyebaki, kila mmoja akaanza kukimbia kwa hofu kuyaokoa maisha yake. Pale polisi wale waliposimama, wakashtukia wakikumbwa na watu waliokuwa wakikimbia, walipoinuka, Edmund hakuwepo, naye aliungana na watu wengine kukimbia.
Ilikuwa ni balaa ndani ya kituo hicho, watu wakatawanyika, si wale wanaosimama kwenye kizuizi, bali kila mtu aliyekuwa ndani ya kituo hicho ambao walikuwa ni zaidi ya elfu tatu, walikimbia kuelekea nje.
Edmund hakutaka kurudi, pale alipofika, akalikuta gari lake lakini hakutaka kulifuata, akahisi kwamba kulikuwa na watu waliokuwa wakilifuatilia na kutaka kuona ni mtu gani ambaye angeingia ndani ya gari hilo.
Alichokifanya ni kutembea kwa mwendo wa kasi huku watu wengine wakiendelea kukimbia hovyo. Alipofika umbali fulani, akasimamisha teksi, akaingia na kuondoka.
“Kuna nini?” aliuliza dereva teksi, alishangaa kuona watu wakikimbia huku na kule.
“Kuna bomu!”
“Kuna bomu! Wapi?”
“Kituoni!”
“Acha utani!”
“Kweli! Kuna bomu humo!”
Edmund akamshukuru Mungu kwa kumuwezesha kuondoka salama katika kituo kile pasipo kugundulika. Safari iliendelea, alipokuwa akielekea, hakupajua, wakati mwingine alijisikia kumwambia dereva kwamba wazunguke tu mpaka pale ambapo giza lingeingia.
Wakati wakiwa wanaendelea kuzunguka ndipo akapata wazo kwamba aondoke mpaka nchini Ireland kwa kutumia gari kwani wangepitia katika daraja kubwa lililokuwa likipita kutoka Uingereza mpaka Wales ambapo huko kusingekuwa na kazi kubwa ya kwenda huko.
Wazo hilo lilionekana kufaa, akamwambia dereva kwamba walitakiwa kuanza safari ya kuelekea nchini Wales kitu ambacho hakikuwa na ugumu hata kidogo.
“Kwa hiyo twende Wales?”
“Ndiyo! Twende huko!” alijibu Edmund.
Hakukuwa na tatizo lolote lile, katika muunganiko wa Uingereza, pia kulikuwa na nchi nyingine kama Scotland na Wales ambapo kwa Muingereza kwenda huko hakuhitaji viza kwa kuwa ilionekana kama kutoka sehemu moja na kwenda nyingine.
Ilikuwa ni safari ndefu lakini Edmund hakutaka kujali. Muda wote ambao safari ilikuwa ikiendelea, masikio yake yalikuwa katika redio aliyokuwa akiisikiliza humo garini. Hakutaka kupitwa na wakati, ilikuwa ni lazima kufuatilia kila kitu kilichokuwa kikiendelea ili ajue msako mkubwa wa kumtafuta yeye ulikuwa ukifanyika mahali gani.
Baada ya saa tano, saa mbili usiku wakafika katika eneo ambalo ilikuwa ni lazima magari yaangaliwe kama kulikuwa na kitu cha hatari ambacho kilikuwa kikitoka nchi moja kwenda nyingine.
Hapo kulikuwa na msururu mkubwa wa magari na yote ambayo yalikuwa yakiingia nchini Wales ilikuwa ni lazima kupekuliwa kwanza. Hapo, Edmund akawa na hofu, akahisi kabisa kwamba angeweza kuonekana kitu kilichomfanya kuanza kuzungumza na dereva yule.
“Ninahitaji kupita hapa salama,” alisema Edmund huku akimwangalia dereva huyo.
“Hakuna tatizo! Hatujabeba kitu cha hatari, tunapita bila tatizo lolote lile,” alisema dereva yule kwa kujiamini.
“Najua! Ila hatuwezi kufanya kitu chochote tukapita salama?” aliuliza Edmund.
“Hapa lazima tupite salama! Mbona unakuwa na wasiwasi sana?”
“Yeah! Nataka unifiche. Unajua ninatoroka nyumbani!”
“Kivipi?”
“Baba yangu kanizingua. Ninakwenda kuonana na mpenzi wangu. Familia yetu ni Wazungu, mchumba wangu ni mtu mweusi. Baba hataki niwe naye, amenizuia, nimetoroka nyumbani na ninajua tu kwamba ametuma polisi kunitafuta ili wanirudishe nyumbani kwani hapendi kweli ngozi nyeusi,” alidanganya Edmund.
“Baba yako nani?”
“Steven Powell.”
“Huyu mkuu wa jeshi la polisi?”
“Ndiyo! Naomba unisaidie nipite salama. Sitaki kurudi nyumbani, ninampenda Vanessa, naomba unisaidie katika hili nivuke salama,” alisema Edmund huku akionekana kuomba sana. Na kwa sababu dereva alikuwa na roho nzuri kama papa Francis, akakubaliana naye kwamba iwe isiwe ilikuwa ni lazima kumvusha salama mahali hapo.

“Mom! Where are we?” (mama! Tupo wapi?) lilikuwa swali la kwanza kabisa alilouliza Walter kwa sauti ya chini kabisa.
Aliyafumbua macho yake, mbele yake alisimama mwanamke mnene, aliyevalia nguo nyeupe ya kinesi, kutokana na kutokuona vizuri, hakujua kama mwanamke huyo hakuwa mama yao, alimfananisha.
Mwanamke huyo hakuzungumza kitu zaidi ya kutoka na kwenda kumuita daktari. Walikuwa wamekaa kwa wiki moja hospitalini hapo na hawakuwa wamerudiwa na fahamu kitu kilichoonekana kuwa kibaya kwa afya yao.
Nesi yule hakuchukua muda mrefu, akarudi chumbani hapo akiwa na daktari ambaye uso wake ulionyesha tabasamu pana kwani hakuamini kama vijana hao wangeweza kuyafumbua macho yao, kila mmoja alikata tamaa na kuhisi kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wao.
“Where are we?” (tupo wapi?) aliendelea kuuliza Walter huku akiangalia kwa macho yake mazito.
Kwa kuwa bado hali zao hazikuwa nzuri, daktari akaagiza wawekewe dripu iliyokuwa na dawa ya Morphometip ambayo ilikuwa na kazi ya kuyaamsha zaidi mapigo yao ya moyo. Kidogo baada ya kuwekewa dripu hiyo, wakapata nguvu na hapohapo Walker naye kuyafumbua macho yake na kuanza kuangalia huku na kule.
Kutokana na hali iliyokuwepo mahali pale, wakagundua kwamba walikuwa hospitalini, hawakujua walifikaje mahali hapo, hawakujua mahali walipokuwa wazazi wao, walishangaa lakini baada ya kukaa kwa dakika kadhaa, wakakumbuka kila kitu kilichokuwa kimetokea kwamba walikuwa wakiingia ndani ya gari na ghafla wakahisi wakiishiwa nguvu na kuanguka chini.
Walihitaji kuwaona wazazi wao, hawakujua mahali walipokuwa, walitaka kuwaona kwani wao ndiyo walikuwa watu muhimu katika maisha yao.
Waliwaulizia lakini madaktari hawakutaka kuzungumza kitu chochote kile, kila walipokuwa wakiulizwa, waliruka na kuliacha swali hilo kitu kilichowafanya kuwa na hofu kwamba inawezekana walikuwa wamefariki dunia ila madaktari hawakutaka kuwaambia ukweli.
Waliendelea kubaki hospitalini hapo, mtu aliyekuwa akiwajulia hali zaidi alikuwa msichana Catherine ambaye hakukuwa na siku iliyokuwa ikipita pasipo kufika katika chumba walichokuwa wamelazwa na kuzungumza nao.
Hakuwaambia ukweli juu ya kile kilichokuwa kimetokea, alijua kwamba ni Edmund ndiye ambaye alisababisha hayo yote, alihofia kuwaambia ukweli kwa kuwa alihisi kwamba wangemchukia kwa kuwa mwanaume huyo alikuwa karibu naye.
Kila siku walikuwa wakiwaulizia wazazi wao, walitaka kujua ukweli kama walikuwa wamekufa au walikuwa hai, na kama walikuwa hai walikuwa mahali gani. Hakukuwa na mtu aliyewaeleza ukweli mpaka pale ambapo walipopewa taarifa kwamba wazazi wao nao hawakuwa katika hali nzuri, walikuwa hapo hospitalini kwani sumu iliyokuwa imewapata, ilikuwa mbaya sana.
“Sumu?” aliuliza Walker huku akionekana kushtuka.
“Ndiyo! Mliwekewa sumu!” alijibu Dk. John.
“Nani alifanya hivyo?”
Hakukuwa na mtu aliyejibu hilo, kila mtu alihofia kwamba kama wangejibu basi wangewafanya mapacha hao wamchukie Catherine ambaye alionekana kuwa karibu na mwanaume aliyekuwa amesababisha hayo yote.
Siku ziliendelea kukatika mpaka pale walipoanza kupata nafuu. Kila mmoja alionekana kuwa na furaha na baada ya siku mbili, wazazi wao ambao hawakujua mahali walipokuwa kipindi cha nyuma, wakakutana nao hospitalini hapo na kuanza kuzungumza nao.
Sumu ile haikuwapata sana kama ilivyowapata wao, katika kipindi chote hicho hata nao walikuwa wakifichwa juu ya hali waliyokuwa wakiendelea nao watoto wao. Walipokutana, wakashindwa kuvumilia, wakakumbatiana kwa furaha, kila mmoja hakuamini kwamba hatimaye familia hiyo iliungana kwa mara nyingine.
Watu wakapewa taarifa kwamba hatimaye mapacha hao walikuwa wameinuka kitandani, kila mtu aliyeziangalia picha zao alibaki na furaha tele kwani kwa kipindi hicho hakukuwa na watu waliokuwa wakipendwa kama ilivyokuwa kwa Walter na Walker.
Hawakuambiwa juu ya mtu aliyewafanyia hivyo ila baada ya kusikia habari na kuona matangazo, wakajua kwamba mwanaume aliyekuwa amefanya hivyo alikuwa Edmund.
Hilo liliwasikitisha, walimfahamu mwanaume huyo kwa kumuona tu, hawakuwa wamezoeana sana, sasa ilikuwaje mpaka kuamua kuwafanyia unyama mkubwa kiasi hicho?
“Kisa?” aliuliza Walter na hapo ndipo Catherine alipoanza kusimulia kila kitu kilichokuwa kimetokea kati yake na mwanaume huyo.
Hapo ndipo wakajua ukweli kwamba Edmund alidhamiria kufanya mauaji hayo kwa sababu tu alihisi kwamba Walter alikuwa mpenzi wa Catherine. Hilo lilimuumiza mno, hakuamini kama kungekuwa na mwanaume ambaye angeweza kufanya jambo kama hilo kwa ajili ya mapenzi tu.
Waliendelea kukaa hospitalini hapo huku kila siku wakifuatilia kuhusu kufuatiliwa kwa Edmund. Kidogo dunia ikatulia, kitendo cha mapacha hao kupona kilimfanya kila mmoja kuwa na furaha tele.
Nchini Marekani, kila mtu akatamani kuwaona watu hao wakielekea huko. Kulikuwa na mashindano makubwa ya America Got Talent ambapo waliombwa kuwa majaji katika shindano hilo lililokuwa kubwa duniani ambalo lilikuwa maalumu kwa watu kuonyesha vipaji vyao mbalimbali.
Ilikuwa nafasi kubwa kwao, hawakuwa na jinsi, kwa kuwa walikuwa watu wa watu, wakapanga kwenda huko ambapo wangekuwa katika siku zote za shindano hilo ambalo lingechukua miezi mitatu.
Wakapanda ndege, Catherine hakutaka kubaki nchini Uingereza, maishani mwake, hakukuwa na mwanaume aliyekuwa na thamani kubwa kama Walter, alimpenda mwanaume huyo, kwake, ngono halikuwa tatizo, alichokuwa akikifikiria ni kumuona mwanaume huyo kila wakati kitu alichoamini kingemfanya kuwa mwanamke mwenye furaa duniani kote.
“Are you going to Las Vegas?” (utakwenda Las Vegas?) aliuliza Walter.
“Yeah! I lost you, I don’t wanna lose you again,” (ndiyo! Nilikupoteza, sitotaka kukupoteza tena) alisema Catherine huku tabasamu pana likiwa usoni mwake.
***

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA NANE

Siku nzima polisi walikuwa barabarani kuhakikisha kwamba mtu aliyekuwa akitafutwa, Edmund anapatikana kwa hali na mali. Hakukuwa na polisi aliyejua kwamba gari moja miongoni mwa magari yaliyotaka kuingia nchini Wales lilikuwa na mtu aliyekuwa akitafutwa kwa udi na uvumba.
Kila mmoja alichoka, hawakuamini kama kweli mwanaume huyo alikuwa njiani kuelekea huko, walichokijua ni kwamba aliendelea kuwa Uingereza hivyo hata kwa jinsi walivyokuwa wakiyakagua magari mpakani hapo, hawakukagaua kama ilivyotakiwa kuwa.
Edmund akapewa kofia kama ya Malboro na dereva yule, akaivaa na kuanza kulisogeza gari kule walipokuwa polisi. Kila mmoja alichoka, walihitaji kuondoka kuelekea nyumbani kwani tangu asubuhi walikuwa mahali hapo, walizikumbuka familia zao, umakini wa kupekua magari uliwatoka na hivyo kuruhusu magari hata kama hawakufanya ukaguzi ambao ulitakiwa kufanyika.
Polisi alimuona Edmund akiwa na kofia, hakumjua, hakutaka kumkagua sana, ilikuwa ni usiku na mwili wake ulichoka mno. Hata kumwambia kuvua kofia ile ili amwangalie vizuri hakuwa na muda huo, akamulika tochi ndani ya gari kizushi, tena kwa haraka na kuliruhusu gari hilo kupita.
Edmund mwenyewe hakuamini, alihisi kama yupo ndotoni, alimwangalia polisi yule kwa makini, hakuamini kama kweli yeye ndiye aliyeliruhusu gari hilo kupita pasipo kufanyika ukaguzi kwa makini kama ambavyo ulitakiwa kufanyika.
Wakapita kirahisi kabisa, na baada ya dakika kadhaa gari likasimishwa nje ya hoteli kubwa ya Wales King ambapo Edmund akateremka, akaelekea mapokezi na dereva yule, akachukua chumba kwa ajili ya kwenda kupumzika.
“Utachukua chumba nikulipie?” aliuliza Edmund huku akimwangalia dereva, bado alimuhitaji, walikuwa na safari ndefu ya kuelekea katika Kituo cha Treni cha Bravein kwa ajili ya kupanda treni na kuelekea nchini Ireland.
“Haina shida. Nichukulie cha chini kabisa, ila kwanza ngoja niende baa kunywa,” alisema dereva huyo na Edmund kufanya hivyo.
Dereva yule akaelekea baa na kuanza kuunywa, nusu ya kiasi cha pesa alicholipwa kama malipo kilimfanya kujiona tajiri, aliamini kwamba kama angemfikisha mwanaume huyo huko alipokuwa akienda basi angepata kiasi kikubwa zaidi.
Kulikuwa na watu wengi ndani ya baa hiyo, kila mmoja alikuwa na chupa ya pombe, wengine waliongea kilevi, wapo walikuwa bize kuwashika makalio wahudumu, na wengine kuwa bize na mambo yao.
Macho ya dereva yule yalikuwa yakiangalia kila kitu kilichokuwa kikiendelea mahali hapo. Baada ya dakika chache alipoyahamishia macho yake kwenye televisheni, akashangaa kuiona sura ambayo haikuwa ngeni kabisa machoni mwake.
Haraka sana akasimama na kuisogelea televisheni ile ili kuiangalia vizuri. Ilikuwa ni sura ya Edmund ambayo ilikuwa kwenye tangazo lililosema kwamba alikuwa akitafutwa na dau la paundi milioni moja iliandaliwa kwa yeyote ambaye angefanikisha kukamatwa kwake.
Moyo wake ukamlipuka, hakuamini kile alichokuwa akikiona. Akaisogelea televisheni zaidi, kile alichokiona akiwa mbali ndicho alichokiona akiwa karibu. Haraka sana akatoka ndani ya baa, nje, kulikuwa na walinzi wawili waliokuwa wakihakikisha usalama mahali hapo, akawasogelea.
“Oya! Mnataka pesa?” aliuliza dereva huku akiwaangalia mabaunsa hao.
“Ndiyo! Kiasi gani?”
“Paundi elfu kumi kila mmoja!”
“Ndiyo! Zipo wapi?” aliuliza, kiasi hicho kilikuwa kikubwa mno.
“Twendeni. Mnamjua yule jamaa anayetafutwa kwenye televisheni?”
“Nani? Edmund? Yule aliyewafanyizia mapacha?”
“Ndiyo!”
“Yupo huku!”
“Wapi?”
“Nyie twendeni acheni presha!” alisema dereva na kuwachukua mabaunsa hao na kuanza kuelekea nao katika hoteli ambayo haikuwa mbali kabisa kutoka hapo. Aliamini kwa kutumia nguvu za watu watatu, wasingeshindwa kumkamata Edmund ambaye kwa kuwangalia tu alionekana kuwa goigoi.
Wakavuka barabara na kuanza kuelekea katika hoteli hiyo ambapo baada ya kufika, wakawaambia polisi waliokuwa mahali hapo pia kuongozana nao kwenda katika chumba alichokuwamo kwani kila waliposikia jina la Edmund, waliziona akaunti zao benki kujaa pesa.

Kila mmoja alikuwa na uhakika kwamba Edmund alikuwa ndani ya hoteli hiyo hivyo kuanza kupandisha juu, polisi mmoja na dereva walipanda kwa kwenda huko kwa kutumia lifti huku wengine wakienda kwa kutumia ngazi.
Tayari walikwishazungumza na dada wa mapokezi ambaye aliwaambia kwamba mwanaume waliyekuwa wakimuulizia ambaye aliingia na dereva huyo muda mchache uliopita alichukua chumba namba 62 kilichokuwa katika ghorofa ya saba.
Walikwenda mpaka katika ghorofa hiyo aliyokuwa mwanaume huyo katika chumba hicho, wakaanza kuangalia huku na kule kabla ya kwenda katika chumba hicho. Walipohakikisha kwamba hakukuwa na mtu yeyote yule, wakamtaka mhudumu waliyekuwa naye kuufungua mlango kwa kutumia kadi ya masta.
"Mna uhakika yupo humu?' aliuliza mhudumu yule.
"Ndiyo dada. Fungua haraka asije kuruka dirishani," alisema dereva huku akiwa na presha kubwa.
Yule mhudumu akaufungua mlango huo kwa kutumia kadi ile, wakaingia ndani kwa pamoja huku polisi wale wakiwa na bunduki zao mikononi. Wakaanza kuangalia huku na kule kwa lengo la kumuweka chini ya ulinzi mwanaume huyo lakini kitu cha ajabu kabisa, Edmund hakuwepo chumbani.
"Au chooni," alisema dereva na hivyo kwenda huko.
Hakukuwa na kitu walichoambulia, huko napo hawakufanikiwa kumuona, kila kona chumbani humo palikuwa peupe kitu kilichomfanya dereva yule kushangaa kwani si muda mrefu mwanaume huyo alikuwa ameingia ndani ya hoteli hiyo.
"Au alibadilisha chumba?" aliuliza polisi.
"Sidhani! Hakubadilisha chumba, nina uhakika huo," alisema dereva huku akionekana kuwa na presha kubwa.
Kwa maelezo ya dereva yaliwapa uhakika kwamba bado Edmund alikuwa ndani ya hoteli hiyo, hawakutaka kuishia hapo, walichokifanya ni kuomba ruhusa kwa uongozi wa hoteli na kuanza kuingia kwenye kila chumba. Ilikuwa kazi kubwa sana lakini hawakuwa na jinsi, walikwenda kila chumba na kuangalia kama mwanaume huyo alikuwepo huko lakini hawakupata jibu.
Baada ya dakika arobaini na tano wakateremka mpaka chini, walishangaa, hawakujua mahali alipokuwa Edmund, wakamuuliza mlinzi kama alimuona mtu yeyote aliyetoka ndani ya hoteli hiyo, wakaambiwa kwamba hakukuwa na mtu yeyote.
"Au waulizeni wale vijana," alisema mlinzi huku akiwaonyeshea wanaume wawili waliokuwa wakiingiza takataka kwenye gari la taka.
"Hatujamuona. Kwani alikuja huku? Labda alitoka wakati tumekwenda kuchukua takataka kule," alijibu jamaa mmoja.
"Basi sawa. Popote mtakapomuona, tupeni taarifa," alisema polisi huku akiwaachia namba yao.
Hakukuwa na mtu aliyechanganyikiwa kama dereva, hakuamini kile kilichotokea, alikaa chini huku akiwa ameshika kichwa chake. Kilichomuuma ni kwamba Edmund alikimbia huku akiwa hata hajammalizia malipo yake.
Alikasirika, hakutaka kuondoka, aliamini kwamba mwanaume huyo alikuwa ndani ya hoteli hiyo, kwa kuwa yeye ndiye alikuwa amempeleka mule, akaelekea ndani ya gari na kusubiri humo kwa kuamini kwamba Edmund angerudi na kuendelea na safari kwa kutumia gari lake.
***
Edmund alikuwa chumbani kwake hotelini, kichwa chake kilikuwa kikifikiria mambo mengi yaliyopita, hakuamini kama alifanikiwa kuwamaliza mapacha wale kwani hata alipokuwa akiangalia kwenye televisheni, taarifa pekee ambayo aliipokea kipindi hicho ni kwamba walikuwa kwenye hali mbaya sana.
Moyo wake ulifarijika, hakuamini kama kweli alifanikiwa katika hilo. Hakuwa tayari kupoteza penzi lake, alimpenda sana Christina kiasi kwamba alikuwa tayari kufanya kitu chochote kile lakini si kumuona mwanaume mwingine akimchukua na kuondoka naye.
Alitulia kwa muda, alijiuliza maswali mengi kama alifanya jambo la maana sana kujificha ndani ya gari kwa kisingizo cha kutafutwa na baba yake. Alikuwa na machale, ni kweli alikuwa amezungumza na dereva yule kuhusu kutafutwa kwake na baba yake lakini kwa upande mwingine alikuwa na hofu kubwa kwamba inawezekana dereva huyo akataka kutafuta kile kilichokuwa kimetokea mpaka kuamua kujificha wakati polisi walipokuwa wakipekua kila gari lililokuwa likipita.
Wakati akiwa anafikiria hayo yote akiwa ndani ya chumba kile, akasimama na kwenda dirishani, alitaka kuhakikisha kwamba kila kitu kinakuwa salama na hata pale ambapo alipokuwa kunakuwa salama kabisa.
Akiwa hapo, bado alikuwa akijifikiria mambo mengi mno na baada ya dakika kumi nzima, akamuona kijana mmoja akiwa na mabaunsa wawili wakivuka barabara kuelekea kule hoteli ilipokuwa.
Alimfahamu dereva yule, alipomwangalia, alikuwa na uhakika kwamba alikuwa yeye. Alikuwa akitembea kwa mwendo wa kasi kuelekea katika upande kulipokuwa na hoteli ile. Hofu ikamjia, akahisi kabisa kwamba kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea, hakutaka kujiuliza, hapohapo akatoka dirishani, kwa haraka sana akachukua kila kitu alichokuwa nacho kwa lengo la kuondoka mahali hapo.
Alijua fika kwamba kama angepitia mapokezini basi kungekuwa na urahisi wa kukutana na watu hao, alichokifanya ni kupanda ngazi na kuelekea juu ya ghorofa kabisa na kupanga mikakati ya kuondoka hotelini hapo.
"Nitaondoka kwa kuruka! Hapana! Nitaweza kuvunjika! Au nishuke kule kule mapokezi? Hapana! Nitakamatwa," alisema huku akizungukazunguka huku na kule.
Alikuwa akitafuta njia ya kuteremka kutoka ghorofani mpaka chini. Hakuona sababu ya kuendelea kubaki kwani hapo hotelini hakukuwa salama tena. Wakati akiwa hapo, akaona bomba kubwa la maji machafu likiwa limeshuka mpaka chini nyuma ya hoteli hiyo, bomba hilo lilikuwa na kazi ya kukusanya mamji ya mvua yaliyokuwa yakikaa huko juu na kuteremka chini.
Hiyo ndiyo ilikuwa nafasi yake, kitu cha kwanza kabisa akalishika bomba hilo na kulitikisa kuona kama lilikuwa imara, halikuonekana kuwa na tatizo na hivyo kuanza kuteremka kuelekea chini.
Alilidandia na kuanza kuteremka kwa kasi kubwa, hakutaka kuchelewa, alijua dhahiri kwamba kama watu wale wangemkosa kule chumbani basi ilikuwa ni lazima kwenda kumtafuta katika vyumba vingine na hata kujaribu kupanda kule ghorofani.
Aliteremka, baada ya dakika tano, akafanikiwa kufika chini kabisa huku akiwa hoi. Hakusimama, alichokifanya ni kuanza kupiga hatua kuelekea sehemu iliyokuwa na parking ya magari ambapo hapo akaliona gari kubwa la takataka likiwa limefika hapo kwa kuondoa taka usiku huo.
"Nitakwenda nalo hilihili," alisema Edmund na kuingia ndani ya garti hilo ambapo kulikuwa na mifuko mingi myeusi, akaichambua na kujificha katikati ya mifuko hiyo na kutulia.
"Nahisi nitaondoka salama mahali hapa," alijisemea huku akiendelea kujichimbia zaidi.

Watu walijaa katika Uwanja wa Ndege wa JFK uliokuwa jijini New York nchini Marekani. Watu wote waliokuwa mahali hapo walitaka kuwaona mapacha walioungana ambao walikuwa na vipaji vya aina yake, Walter na Walker waliokuwa wameiteka dunia kwa kipindi hicho.
Watu waliwaona sana kwenye televisheni, walitaka kuwaona tena na tena. Walijua kwamba siku chache zilizopita walikuwa nchini humo kabla ya kwenda nchini Tanzania, siku hiyo walitaka kuwaona zaidi, kwa wale ambao hawakuwahi hata kuwagusa, walitaka kuwagusa na hata wale ambao hawakuwa wamesainiwa vitabu vyao, walitaka kuona hilo likitokea.
Muda wote watu hao walikuwa wakiangalia saa zao, waliambiwa kwamba ndege hiyo ingewasili mahali hapo majira ya saa tisa jioni lakini cha ajabu, kila mmoja aliona kama muda ulikuwa umefika ila watu hao hawakuwa wameingia nchini humo.
“Jamani! Mbona wanachelewa hivi?” aliuliza msichana mmoja huku akiangalia saa yake, ndiyo kwanza ilikuwa saa 8:17 mchana lakini waliona kama saa tisa ilikuwa imekwishafika.
Uwanjani hapo hawakuwa peke yao, walikuwa na Waziri Mkuu, Bwana Gordon na mkewe ambao nao walitaka kuwaona mapacha hao ambapo kila kona duniani walikuwa wakizungumziwa wao tu.
Dakika zilizidi kwenda mbele na ilipofika majira ya saa tisa jioni, ndege ndogo ya kukodi, Flight 1789 WC ikaanza kuonekana angani, watu wakaanza kujiandaa kwani walijua fika kwamba hiyo ndiyo ilikuwa ndege iliyokuwa imewabeba watu waliokuwa wakiwasubiri uwanjani hapo, ndiyo ilikuwa ndege iliyowabeba watu waliowafanya kuacha shughuli zao na kufika uwanjani hapo.
Ndege ikasimama na watu hao kuanza kuteremka, kila mmoja akaanza kupiga kelele za shangwe, waandishi wa habari waliokuwa na kamera zao wakaanza kusogea kule ndege ile ilipokuwa na kuanza kupiga picha kwa kila kitu kilichokuwa kikiendelea mahali hapo.
Kila mmoja alitaka kuwagusa, hakukuwa na kipindi ambacho walinzi walipata wakati mgumu kama kipindi hicho. Ni kama shughuli zote za ndege zilikuwa zimesimama mahali hapo kwani kitendo cha kuwaruhusu watu kuingia katika ardhi ya uwanja wa ndege tu ilikuwa shida tupu.
“Please Walter! Sign my book,” (naomba usaini kitabu changu Walter!) alisema msichana mmoja huku akikiweka kitabu chake mbele.
Kila mmoja kipindi hicho alitamani kuwa karibu na watu hao, kila mmoja alitaka japo kuguswa na mapacha hao. Hakukuwa na mtu aliyetamani kuwaona watu hao wakiondoka pasipo kufanya jambo lolote lile kwa ajili yako.
Kwa kuwa kila mmoja alikuwa na kiu nao, walichokifanya ni kusaini vitabu vyao na kisha kuingia ndani ya gari na kuondoka mahali hapo. Bi Naseku na mumewe, Cassian walikuwa hawaamini walichokuwa wakikiona, hawakuamini kama vijana wao walikuwa mastaa kiasi hicho, walifurahi, muda mwingine walikuwa wakimshukuru Mungu kwani waliamini kwamba bila watoto wao kuungana namna hiyo basi wasingekuwa mastaa kama walivyokuwa.
Wakafikia katika Hoteli ya Nyota Saba ya 3 Pyramids iliyokuwa hapo New York. Chumbani, kila mmoja alikuwa na furaha, mbali na umaarufu waliokuwa nao lakini pia walikuwa na utajiri mkubwa wa dola milioni 600 katika akaunti yao.
“Shindano no keshokutwa! Nini cha kufanya baada ya hapo?” aliuliza Walker huku akimwangalia ndugu yake.
“Ni kurudi Tanzania! Baada ya hapo, tutafanya mambo mengine mengi,” alisema Walter.
“Na vipi kuhusu Catherine?”
“Nitamuoa. Ila nitaona siku ukioa, tutafunga ndoa pamoja. Umekwishapata msichana wa maisha yako?” aliuliza Walter.
“Bado.”
“Na vipi kuhusu Jackline? Bado hujafikiria kumtafuta?”
“Bado! Ila kuna siku nitamtafuta. Kuna mambo mengi sana. Kuna mchoro nitahitaji kuuchora, wa yule msichana Patricia!” alisema Walker.
“Yupi? Nikuumbushe!”
“Tuliyekutana naye kwenye ndege. Umemsahau?”
“Ooh! Yule Mfaransa?”
“Yeah! Ninatamani sana nimchore kisha nimtumie. Ni msichana mzuri sana. Kiukweli nimetokea kumpenda,” alisema Walker huku akionekana kumaanisha alichokuwa akikizungumza.
“Safi sana. Sema naye.”
Japokuwa alikuwa amekutana na wasichana wengi wauzri lakini Walker alikuwa amekufa na kuoza kwa msichana mmoja tu, Patricia ambaye alikutana naye ndani ya ndege katika kipindi walichokuwa wakitoka nchini Tanzania kwenda Marekani.
Alizoeana na msichana huyo na mara nyingi walikuwa wakichati, walikuwa wakizungumza mengi na kushauriana mambo mengi mazuri. Hakukuwa na mtu aliyemwambia mwenzake, kila Walker alivyotaka kufanya hivyo, alijiona akishindwa kabisa na kitu pekee ambacho aliamini kwamba kingezungumzia hisia zake juu ya msichana huyo kilikuwa ni kumchora tu.
Alikuwa na mawazo tele, hakumfikiria rafiki yake wa utotoni, Jackline ambaye hakujua kipindi hicho alikuwa wapi, mtu pekee aliyekuwa akimfikiria sana alikuwa msichana Patricia tu. Alimwambia ndugu yake, alitamani sana kuona akiwa na msichana huyo zaidi na zaidi ili hata kama ingetokea siku ndugu yake, Walter angekuwa anaona, basi waweze kuoa pamoja.
“Ukichelewa, nitaoa kabla yako!” alisema Walter.
“Huwezi kuoa kabla yangu. Tutaoa pamoja. Wala usijali,” alisema Walker huku akiwa na uhakika wa kumpata msichana huyo.
***
Maisha yalikuwa tofauti, kile alichokuwa amekifanya hakikuleta matokea chanya, akawa mtu wa kuhangaika huku na kule. Edmund alikuwa ndani ya gari la takataka, alifunikwa na taka hizo na kulisikia gari likianza kuondoka mahali hapo.
Hakuamini kama yeye ndiye aliyekuwa akiishi maisha hayo ya digidigi, yaani kisa mapenzi tu leo hii alikosa amani kabisa, na mbaya zaidi kile alichokuwa amekikusudia hakikuwa kimetimia.
Alijuta lakini wakati mwingine aliamua kusonga mbele, alikuwa tayari kuendelea kuishi hivyo na ndiyo maana alikuwa ameondoka kuelekea nchi nyingine kabisa kwa kuamini kwamba angekuwa salama hapo Wales.
Aliikumbuka familia yake, alimkumbuka mpenzi wake, aliwakumbuka marafiki zake, kila kitu alichokiacha nyuma yake huo ndiyo ulikuwa wakati wa kukikumbuka.
Safari ille iliishia katika sehemu iliyokuwa na jumba kubwa ambalo ndani yake kulikuwa na eneo maalumu pa kuchomea takataka. Wakati gari likiwa limesimama kwa lengo la watu kuja kutoa takataka, naye akatoka na kuanza kuelekea sehemu iliyokuwa na mlango mkubwa wa kutokea.
Hakukuwa na watu wengine, humo ndani, watu waliokuwa na zamu ya kuleta gari hilo ndiyo waliokuwa wakiingia humo kwa ajili ya kuzichoma moto taka hizo. Alipofika nje ya jengo lile, akaanza kupiga hatua kuelekea mitaani.
Hapo palikuwa Stonford Pelrr, sehemu iliyokuwa karibu na pori dogo la kutengenezwa la Jumanji. Alitembea kwa mwendo wa haraka katika kipori hicho mpaka alipofika sehemu iliyokuwa imetengwa kwa ajili ya wazazi kuwapeleka watoto wao kwenda kucheza.
Alichoka, alihitaji muda wa kupumzika, pale, hakukuwa na mtu yeyote, palikuwa pamefungwa kwa muda, akayafuta mabenchi yaliyokuwa mahali hapo na kutulia.
Moyo wake ulikuwa na mawazo tele, hapo alipofika, akatamani kuwasiliana na wazazi wake, alitaka kuwaomba msamaha kwa kila kitu kilichokuwa kimetokea kwani hakuwa amekusudia bali kulikuwa na nguvu kubwa iliyokuwa imemuingia ambayo ilimuongoza kufanya jamboo la kipumbavu kama lile.
Akaichukua simu yake iliyokuwa mfukoni mwake ambayo aliizima kitu kiitwacho location na kuizima kabisa, akaiwasha na kuanza kumpigia simu baba yake ambapo baada ya sekunde chache, simu ikapokelewa.
“Baba! Aliita baada ya simu kupokelewa!
“Edmund! Upo wapi?”
“Nimeondoka nyumbani. Baba! Naomba unisamehe, nimefanya jambo la kijinga sana, ninajutia kile nilichokifanya, naomba unisamehe, najua umeumia, sikuwa na cha kufanya, nilifanya hivyo kwa kuwa nilihitaji kulilinda penzi langu, nilimpenda sana Catherine, sikuwa na sababu ya kumpoteza na ndiyo maana niliamua kufanya hayo yote kwa kuamini kwamba ningeweza kulilinda penzi langu kwake,” alisema Edmund huku akitokwa na machozi ya uchungu, aliusikia moyo wake ukichomwa na kitu chenye ncha kali.
“Pole sana. Usijali! Upo wapi?”
“Nimeondoka! Nimekuja huku....” alisema Edmund lakini hata kabla hajamaliza sentensi yake, akasikia vishindo vya watu wakija kwa kasi kule alipokuwa, hapohapo akageuka, macho yake yakatua kwa polisi waliokuwa na bastola viuononi mwao na virungu mikononi mwao.
“Mikono juu! Weka mikono tuione vizuri,” alisema polisi mmoja huku wakimsogelea, hapohapo Edmund hakuwa na jinsi, akaiachia simu na kunyoosha mikono juu huku machozi yakimtoka.
“Halo...halo..” ilisikika sauti ya baba yake kwenye simu.

Kiuhalisia huo ulionekana kuwa mwisho wa Edmund, alinyanyua mikono yake hewani huku akiwa na hofu kwamba hatimaye alikuwa amekamatwa na polisi waliomfikia hapo bustanini na kumnyooshea bastola huku wakimtaka kutulia kama alivyokuwa.
Baba yake aliyekuwa upande wa pili aliendelea kuita pasipo mafanikio yoyote yale. Polisi wale wakazidi kumsogelea, walipomfikia, wakamuweka chini ya ulinzi na kumuuliza maswali juu ya kitu alichokuwa akikifanya mahali pale.
"I was looking for my wife," (nilikuwa namtafuta mke wangu) alisema huku akilala chini.
Walikuwa na taarifa ya mtu aliyejulikana kwa jina la Edmund kutafutwa nchini Uingereza lakini hawakujua kama yule waliyekuwa naye ndiye kijana aliyekuwa akitafutwa kwa udi na uvumba.
Mahali hapo kulikuwa na mwanga hafifu hivyo hata walipomwangalia usoni iliwawia vigumu sana kugundua kwamba alikuwa yeye na maneno ambayo aliwaambia kwamba alikuwa akimtafuta mke wake yaliwafanya kumuonea huruma kwamba alikuwa kwenye matatizo makubwa.
"Where is she?" (yupo wapi?)
"She came here with my son, I don't know where they are!" (alikuja hapa na mwanangu, sijui wapo wapi) alisema Edmund huku akiwa amelala chini, sauti yake kwa jinsi ilivyosikika ilikuwa ni kama ya mtu aliyetaka kulia.
"Did you try to call here?" (ulijaribu kumpigia simu?)
"I tried many times but I didn't reach her!" (nilimpigia mara nyingi lakini sikumpata) alijibu.
Hiyo haikuwa mara ya kwanza, ni mara nyingi watu waliokuja wakija mahali hapo walikuwa na malalamiko mengi kuhusu kupotea kwa watoto wao na hata mume na wake zao. Kitendo cha Edmund kuwaambia hivyo, hapohapo wakamfungua pingu na kumuweka kwenye benchi.
Hakutaka kugundulika hivyo kujifanya kulia huku akiuinamisha uso wake. Alijifanya kuwa kwenye tatizo kubwa kiasi kwamba wote wawili wakaanza kumuonea huruma kwa kuona kwamba kweli mwanaume huyo alikuwa kwenye matatizo makubwa hivyo kuhitaji msaada.
Wakamwambia achukue simu yake, akajiandikia namba na kupiga. Simu haikuwa ikipatikana, akawaambia polisi kwamba namba haikuwa ikipatikana hivyo alitakiwa kurudi nyumbani kuona kama mkewe huyo alikuwa amefika nyumbani.
Hawakuwa na jinsi, wakamruhusu, akaondoka mahali hapo kinyonge. Polisi wale walibaki wakimsinidkiza kwa macho mpaka alipopotea na kutokomea zake huku akiwa amenusurika kukamatwa na polisi hao. Moyoni mwake akajiona kuwa na bahati, alimshukuru Mungu zaidi na zaidi kwamba alimuokoa kutoka katika mikono ya polisi hao.
Alipofika barabarani, akasubiri basi la abiria na kuondoka mahali hapo. Alipokuwa akielekea, hakuwa akipafahamu, basi liliendelea mpaka alipofika sehemu ambapo alihisi ndiyo mwisho wa basi hilo, akateremka na kuelekea katika kitu kupumzika. Wakati akiwa hapo, simu yake ikaanza kuita. Haraka sana akaipokea.
"Edmund...You are a superstar," (Edmund...wewe ni supastaa mkubwa) alisikika mwanaume aliyekuwa upande wa pili.
"How?" (kivipi?) akajifanya kuuliza.
"I see you in my television! You about to win an Oscar award!" (nakuona kwenye televisheni yangu, unakaribia kutwaa Tuzo ya Oscar) alisikika mwanaume wa upande wa pili.
Huyo alikuwa rafiki yake wa karibu, Mark aambaye mara nyingi sana walikuwa wakitaniana pasipo kujua ni kwa namna gani mtu fulani alikuwa kwenye hatari ya kupoteza maisha yake. Baada ya kumtania ndipo akauliza kilichokuwa kikiendelea, Edmund hakutaka kumficha, alimwambia kwamba kile alichokuwa akikiona kwenye televisheni ndicho kilichokuwa kimetokea hivyo kutaka msaada kwani alikuwa nchini Wales.
"Hakuna tatizo! Ngoja nimpigie mjomba wangu akusaidie kukupokea," alisema Mark.
Hilo halikuwa hata tatizo, kipindi hicho kitu alichokuwa akikihitaji Edmund ni msaada wa hali na mali kwani ilikuwa ni lazima kuhakikisha kwamba anaondoka salama na kwenda mbali kuishi maisha yake. Mark akawasiliana na mjomba wake huyo ambaye alimwambia kuhusu rafiki yake aliyekuwa akihitaji msaada mkubwa.
Akamwambia sehemu alipokuwa kisha kumpigia simu Edmund na kumwambia juu ya msaada aliokuwa akiuhitaji kupatikana. Akamshukuru rafiki yake huyo na kumsubiri mjomba huyo ambaye aliingia hapo baada ya dakika kadhaa.
"Wewe ndiye Edmun?" aliuliza mjomba huyo.
"Yeah! Ndiye mimi!"
"Ingia twende!"
Hakuwa na hofu yoyote ile, akaingia ndani ya gari na kuondoka mahali hapo. Kidogo moyo wake ukawa na furaha mno, akaamini kwamba kwa kitendo cha rafiki yake huyo kuwasiliana na mjomba wake na hatimaye kumsaidia, kwake ilimfanya kumuona Mark mtu wa maana mno.
Hawakuchukua dakika nyingi wakafika mahali kulipokuwa na nyumba chache ambapo hapo ndipo alipokuwa akiishi huyo mjomba, wakateremka na kuingia ndani, akamuonyesha chumba cha kulala na kumwambia kwamba kuanzia siku hiyo angelala mahali hapo mpaka pale ambapo angetaka kuondoka mwenyewe.
"Nashukuru sana!" alisema Edmund, akaingia ndani na kupumzika.
Mjomba aliyeitwa Vonn alitulia sebuleni. Kitendo cha kwenda kumpokea Edmund na kumuona, hakuamini kabisa kama huyo ndiye alikuwa yule mwanaume aliyetakiwa kwenda kumpokea.
Alimjua, hiyo haikuwa mara ya kwanza kumuona, alimuona kwenye televisheni na kipindi chote hicho mwanaume huyo alikuwa maarufu mkubwa, alionekana kwenye kila kituo cha televisheni huku kukiwa kumetolewa donge nono la pesa ambalo angepewa mtu yeyote ambaye angefanikisha kupatikana kwake.
Sebuleni hakutulia, alikuwa akihangaika, moyo wake ulikuwa ukifukuta, hakutulia, alitamani sana kuwa mwaminifu kwa Mark lakini kila alipokuwa akizikumbuka zile pesa alizokuwa ameahidiwa mtu yeyote ambaye angefanikisha kupatikana kwake, udenda wa tamaa ukamtoka.
"Ni pesa nyingi sana! Hizi zitanifanya kutoa mizigo Ujerumani na kuileta hapa kuendelea na biashara zangu! Siwezi kuziacha pesa hizi," alijisemea huku akiwa sebuleni hapo.
Hakutaka kuchelewa, ilikuwa ni lazima kwenda kituo cha polisi na kutoa taarifa kwamba mwanaume aliyekuwa akitafutwa kila kona alikuwa nyumbani kwake. Akaelekea chumbani, akabadilisha nguo zake, kila kitu alichokuwa akikifanya chumbani humo aliona akifanya taratibu sana kwani alitamani kuondoka haraka sana na kuelekea polisi na kutoa taarifa juu ya mwanaume huyo aliyekuwa chumbani.
Alipomaliza, hakutaka kuchelewa, hapohapo akaelekea sebuleni, akachukua simu yake, akaufuata mlango, alipoufungua tu, macho yake yakakutana na bunduki zaidi ya kumi zilizoshikwa na wanaume waliokuwa wamevalia mavazi meusi ambapo usoni mwao walikuwa wameficha sura zao na kwa nyuma kukiwa na gari lililoandikwa S.W.A.T.
"Don't movie! Hands on your head," (usitingishike! Mikono kichwani mwako) alisema mwanaume mmoja kwa sauti ya chini ambayo hakutaka mtu yeyote ndani asikie chochote kile, hapohapo Vonn akafanya kama alivyoambiwa.
"Where si he?" (yupo wapi?) aliuliza.
"Who?" (nani?)
"Edmund!"
"Who is that?" (ndiye nani huyo?) aliuliza huku akiwaangalia wanaume hao.
Hawakutaka kumwambia ukweli, walichokifanya ni kuanza kuelekea ndani kwa ajili ya kumtafuta mwanaume huyo huku wakiwa na uhakika kwamba alikuwa humo.
Vonn alibaki pale mlangoni, hakuamini kilichokuwa kimetokea, ilikuwa watu hao wajue kama Edmund alikuwa nyumbani kwake na wakati hakumwambia mtu? Wakati mwingine alihisi kwamba Mark alikuwa amewataarifu polisi kwamba mwanaume huyo alikuwa nyumbani kwake.
Zile pesa zilizokuwa kichwani mwake, zikaanza kupotea na kuona kuwa hao polisi wangemuona Edmund ambapo wangemchukua na kuondoka naye bila yeye kupata kitu chochote kile kwani hakuwa ametoa taarifa kama mwanaume huyo alikuwa ndani ya nyumba hiyo.
"Freeze...freeze...frezeeeeee..." ilisikika sauti za watu hao huko ndani.

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA TISA

Patricia alikuwa msichana mrembo aliyekuwa akiishi katika Jiji la Lyon nchini Ufaransa. Alikuwa msichana mwenye mchanganyiko wa rangi, sura ya kitoto na kila alipokuwa akitabasamu au kucheka vishimo vilionekana mashavuni mwake kitu kilichomfanya kuonekana mzuri maradufu.
Katika kipini ambacho alikuwa na mapacha walioungana kwenye ndege alikuwa akitoka Dubai kuelekea nchini Marekani. Walikutana ndani ya ndege na kuzungumza na Walter, kwa jinsi alivyokuwa akiwaona kila siku katika mitandao ya kijamii na hata magazeti, kitendo cha kuonana nao na kuzungumza pamoja kilimchanga.
Alifurahi na mwisho wa siku kupiga nao picha. Hakutaka kuondoka pasipo kuwaomba namba ya simu, alipoomba, mtu wa kwanza kabisa kutoa alikuwa Walker. Alichukulia kila kitu kuwa kawaida japokuwa kwa upande mwingine alijiona kuwa mtu mwenye bahati kubwa mno.
Aliwajua masupastaa, walikuwa watu waliojiona, walioishi maisha yao ambapo hawakuwa radhi kutoa namba zao za simu. Kwa Walker, alishangaa, ilikuwaje mwanaume huyo awe mwepesi kumpa namba ya simu, kuweka ukaribu kitu ambacho kilionekana kuwa kama ndoto katika maisha yake.
Njia nzima alikuwa akijibaraguza kwa Walker, walikuwa wakizungumza mambo mengi huku Walter akiwa amechuna kabisa, yeye alikuwa bize na Catherine aliyekuwa katika upande mwingine kabisa.
Ndege ilipofika Marekani, akateremka huku akimwambia Walker kwamba kesho yake alitakiwa kuondoka kuelekea Ufaransa alipokuwa akisoma ambapo huko ndipo alipokuwa akiyaendesha maisha yake.
Kitendo cha kubadilishana namba za simu kikawafanya kuwasiliana mara kwa mara. Walker alijua kuzungumza na mwanamke, alijua kusifia, alijua kubembeleza kitu kilichomfanya Patricia kujiona kama malkia wa mbingu aliyeshushwa duniani kwa bahati mbaya.
“Unajua kama wewe ni mzuri sana?” aliuliza Walker kwenye simu.
“Mmh! Mimi?”
“Ndiyo! U mzuri sana. Kama ungekuwa gari, basi wewe ungekuwa Lamborghini au Ferrari,” alisema Walker.
“Mmh! Una maneno wewe!”
“Kweli tena. Nilipokuona kwa mara ya kwanza, moyo wangu ulibabaika, nilishindwa kukuangalia mara mbili. U mzuri sana, unapokasirika, uzuri wako haupotei, unapokuwa kimya, bado u mzuri mno, unapokasirika, uzuri wako unazidi kuonekana maradufu. Patricia, hivi ulizaliwa muda gani?” aliuliza Walker baada ya maneno mengi yalimfanya msichana huyo kutabasamu kila wakati.
“Hahah! Unanichekesha!”
“Sidhani kama ulizaliwa hospitalini! Nahisi ulizaliwa supamaketi, tena karibu kabisa na friji lililokuwa na chokolate. U mrembo sana, sina mtu wa kukufananisha nawe,” aliendelea kusema Walker huku akichukua maneno mengi kutoka katika Kitabu cha Romeo And Juliet kilichoandikwa na mwandishi wa Kiingereza, William Shakespear.
“Walker! Hujakutana na wazuri!”
“Nimekutana nao, ila moyo wangu umekukubali zaidi wewe! Unajua kutabasamu, unajua kuringa, unajua kupetika, kwa kifupi wewe ni malkia wa nyuki, acha kidume niwe mtafuta maua.”
“Hahah! Nashukuru sana!”
“Hebu rudia tena! Nataka niisikie sauti hiyo tena!” alisema Walker huku akitoa kicheko cha mbali kabisa.
“Kwani sauti yangu ipoje?”
“Hebu rudi kwanza. Kidogo tu!”
“Niambie kwanza ikoje!”
“Jamaniiiii! Rudi basi mpenzi! Rudia basiiiii...”
“Nashukuru!”
“Patricia, nimekwambia una sauti nzuri sana, kwa sauti yako ina uwezo wa kulifungua daraja la London, kwa sauti yako ina uwezo wa kuufanya mnara wa Eifel jijini Paris ukapinda na hata kuanguka,” alisema Walker.
“Hahah! Utanifanya nisikie aibu!”
“Hakuna bwana! Unajua nashindwa kuvumilia, nashindwa kuongea lolote lile. Nahitaji nikuchore, picha moja matata sana,” alisema Walker.
“Kweli?”
“Haswaa! Nitakuchora. Haiwezekana nikutane na msichana mrembo kama wewe halafu niache kumchora. Patricia, ninakupenda mno!” alisema Walker huku simu ikiendelea kuwa sikioni mwake, Waltr alishindwa kuzungumza lolote lile kwani kwa jinsi ndugu yake alivyokuwa akiendeshwa kwa nguvu kubwa ya mapenzi, hata kwake ilikuwa hivyohivyo.
Walizungumza mengi, Patricia akajisikia raha moyoni mwake, alipenda kupendwa, alijihisi kuwa msichana aliyekuwa na bahati kubwa mno maishani mwake.
Hakutaka iwe siri, alichokifanya ni kuwaambia wazazi wake kwamba alipata mwanaume wa kweli na alipowaambia kuhusu mwanaume huyo, wao wenyewe hawakuamini. Walimfahamu Walker, alikuwa mwanaume mzuri wa sura japokuwa alikuwa ameungana na ndugu yake, Walter. Walijisikia fahari mno na kumsisitizia kwamba kitu cha kwanza kabisa alitakiwa kusoma na kuhakikisha anapata digrii yake ya kwanza ya mambo ya uchumi.
Walker hakutaka kuchelewa, bado penzi lilikuwa changa na alikuwa na presha kubwa, alichokifanya ni kumchora msichana huyo na picha yake kumtumia katika barua pepe. Patricia alipoipata, hakuamini macho yake, aliishangaa kwani kwa jinsi ilivyoonekana, ilikuwa kama si picha ya kuchorwa.
Kwa jinsi alivyokuwa na furaha, akaanza kububujikwa na machozi na kumpigia simu Walker na kuanza kuzungumza naye. Moyo wake ulijisikia furaha mno, walizungumza kana kwamba hawakuwahi kuzungumza kabla.
“Nakuja Marekani!” alisema Patricia huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Unasemaje?”
“Nakuja Marekani! Siwezi kuvumilia!” alisema msichana huyo.
“Mmh! Mbona ghafla hivyo?”
“Najua! Nina hamu ya kukuona, siwezi kubaki Ufaransa, naomba nije, tena kesho!”
“Kesho?”
“Ndiyo!”
Huo ndiyo ulikuwa uamuzi wake, moyo wake ulichanganyikiwa, hakutaka kusikia kitu chochote kile, kitu pekee alichokitaka muda huo ni kumuona mwanaume huyo tu. Hakutaka kubaki Ufaransa, alichokifanya siku iliyofuata ni kupanda ndege kuelekea Marekani.
Njiani, moyo wake ulikuwa na mawazo tele, alikuwa na kiu ya kumuona mwanaume huyo kwa mara nyingine tena. Baada ya saa kadhaa ndege ikatua katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa JFK na kuteremka. Akampigia simu na kumwambia kwamba alikuwa amekwishafika.
“Mbona sikuoni mpenzi?” aliuliza Patricia.
“Nimekuja kusaini mkataba wa American Got Talent! Umekwishafika?”
“Ndiyo!”
“Chukua teksi! Nimekwishakuchukulia chumba katika Hoteli ya Caspean Ville! Chumba namba 79. Ukifika hapo chukua ufunguo, nimekwishaacha maagizo. Nitakuja mpenzi nikimaliza kazi ya huku!” alisema Walker.
“Sawa. Nashukuru! Utanikuta huko.”
“Haina shida. Nakupenda mpenzi!”
“Nakupenda pia!”
Patricia hakutaka kubaki mahali hapo, alichokifanya ni kuchukua teksi na kuanza kuondoka mahali hapo huku akionekana kuwa na furaha tele. Wakati gari likiwa limeingia katika Barabara ya St. Louis IV, ghafla honi nyingi zikaanza kusikika, dereva alikuwa amejisahau kuzembe kabisa, hakuangalia vizuri taa zilizokuwa zikiwaka na hivyo kuingia katika barabara hiyo iliyokuwa ikiruhusu magari yaliyokuwa yakikimbia kuanzia kasi ya 100 mpaka 150. Ni mlio mmoja mkubwa ndiyo uliosikika mahali hapo.
“Puuuuuuuu!” Teksi ile ikagongwa, ikaruka angani, ikabingirika mara tano, watu wakashika vichwa, ilipotua chini, damu tu ndizo zilizokuwa zikionekana kwenye lami. Patricia akatulia kwenye kiti kama alivyokuwa huku akitokwa na damu mfululizo.

Hakukuwa na siku ambayo Walker alikuwa na hamu ya kuzungumza na Patricia kama siku hiyo. Wakati wakiwa kwenye mkutano kwa ajili ya kusaini mkataba huo ambao ungewafanya kuwa majaji katika Shindano la American Got Talent, kichwa chake kilikuwa kikimfikiria msichana huyo mrembo.
Wakati mwingine alitamani asimame na kuondoka, aliona kila kitu kikiendelea taratibu sana, alitamani yeye ndiye angekuwa msimamizi wa mkutano huo mdogo ambao angeamua ni muda gani walitakiwa kuondoka humo ndani.
Muda ulizidi kwenda mbele, baada ya dakika kadhaa, akapokea notification ya CNN ambayo ilimwambia kwamba kulikuwa na ajali mbaya iliyokuwa imetokea katika Barabara ya St. Louis.
Hilo wala halikumtisha, kwake, lilionekana kuwa jambo la kawaida akaendelea kukaa kwenye kikao mpaka kilipokwisha ambapo kitu cha kwanza kabisa akachukua simu yake na kumpigia Patricia ambaye alimwambia atangulie hotelini.
Simu ikaanza kuita pasipo kupokelewa, hilo halikumtia hofu sana kwani alihisi kwamba msichana huyo alikuwa bafuni akioga hivyo kusubiri zaidi na baada ya dakika kadhaa kumpigia tena. Majibu hayakubadilika, yaliendelea kuwa vilevile kwamba simu haikupokelewa.
Hilo likaanza kumtia hofu, akaanza kuhisi kwamba kulikuwa na kitu kilichokuwa kikiendelea huko alipokuwa. Alichokifanya ni kupiga simu katika hoteli aliyomuwekea chumba kwa lengo la kusikia kama msichana huyo alikuwa amefika humo au la.
“Hajafika,” sauti na msihana upande wa pili ilisikika.
“Hajafika?”
“Ndiyo!”
Hilo likamchanganya zaidi, likamfanya kuipiga simu ya msichana huyo zaidi lakini majibu yalikuwa yaleyale kwamba simu haikupokelewa kitu kilichomfanya kuwa na hofu kubwa.
Akamwambia Walter kile kilichokuwa kikiendelea, jinsi alivyokuwa na hofu kwamba inawezekana kulikuwa na jambo baya limemtokea mpenzi wake kwani kila alipokuwa akimpigia simu haikuwa ikipokelewa kitu ambacho hakikuwa kawaida kabisa.
“Sidhani kama kuna jambo baya limetokea. Au amelala hotelini baada ya kuchoka na safari,” alisema Walter manano ambayo aliamini kwamba yangemfariji ndugu yake huyo.
“Walter! Nahisi kuna tatizo!” alisema Walker.
“Hakuna tatizo! Usihofu braza, hakuna kitu chochote kile, niamini!” alisema Walter.
Japokuwa alifarijiwa vya kutosha lakini Walker hakufarijika, bado moyo wake ulimwambia kwamba kulikuwa na kitu cha hatari kilichokuwa kimetokea. Hakuacha kumpigia simu, kuna kipindi kila alipokuwa akipiga simu, haikuwa ikiita, ilionyesha kabisa ilikuwa imezima.
Hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya. Wakati akiendelea kuwa katika hali ya mawazo huku akiwa hajui ni kitu kilimtokea Patricia mpaka kuamua kuzima simu, akasikia tena mlio kwenye simu yake kuonyesha kwamba kulikuwa na notification ilikuwa imeingia. Haraka sana akaifungua, ilitoka katika akaunti ya CNN ambayo ilionyesha kwamba jina la mtu aliyekuwa amepata ajali hatimaye alijulikana kwa jina baada ya kupatikana kwa vitambulisho vyake kwenye gari.
“Ni Patricia...” alisema Walker huku akiwa ameshutuka.
Akahisi kama moyo wake ukipigwa ganzi, hakuamini kile alichokuwa amekiona, msichana aliyekuwa akimpenda kwa moyo wote, aliyemuona kuwa kila kitu katika maisha yake alikuwa amepata ajali mbaya ya gari.
Hakukukalika tena, machozi yanaanza kumtoka na kububujika mashavuni mwake, hakutaka kubaki mahali hapo, akamwambia Walter kwamba ni lazima waelekee hospitalini kwani Patricia alipata ajali mbaya ya gari.
Kazi ya Walter ilikuwa ni kumbembeleza ndugu yake huyo, alimuonea huruma, alikuwa akibubujikwa na machozi tu kitu kilichomfanya kuumia mno moyoni mwake kwani hakupenda kumuona Walker akiwa kwenye hali hiyo, ila kwa kuwa alimpenda sana Patricia, hakuwa na jinsi.
Wakaondoka mpaka katika Hospitali ya St. Monica iliyokuwa hapohapo New York. Walipofika, kama kawaida watu wakaanza kuwazunguka, kila mtu alitaka kusainiwa kitabu na nguo zake kwani kitendo cha kukutana na watu maarufu kama hao lilikuwa jambo moja adimu sana.
Wakatembea pasipo kuzungumza na mtu yeyote mpaka walipofika katika chumba walichoambiwa wasubiri. Muda wote huo Walker alikuwa akilia, moyo wake ulimuuma, hakuamini kama msichana aliyekuwa akimpenda kwa moyo wote alikuwa hoi hospitalini hapo.
Madaktari walikuwa bize wakihangaika na hali yake, walimtibu kwa nguvu zote kuhakikisha kwamba msichana huyo anapata nafuu na kurudi katika hali yake ya kawaida. Muda ulizidi kwenda mpaka baada ya saa tatu ndipo mlango ukafunguliwa na kuchukuliwa kupelekwa katika ofisi ya daktari.
Huko, wakapewa taarifa ambazo hazikuwa nzuri, Patricia alikuwa ameumia vibaya mno, ubongo wake ulipata ufa huku uti wa mgongo ukiwa umevunjika mara moja hali iliyomaanisha kwamba hata kama angerudiwa na fahamu, angepooza mwili mzima.
“Unasemaje?” aliuliza Walker huku akimwangalia daktari.
“Hatoweza kusimama! Amepooza mwili mzima. Cha msingi tumuombe Mungu tu,” alisema daktari maneno yaliyomfanya Walker kulia mno.
Walter akaanza kumbembeleza ndugu yake aliyekuwa ameumia sana, alilia kama mtoto, hakubembelezeka wala kunyamaza, kitendo cha Patricia kupata matatizo hayo kilimfanya kuumia moyoni mwake na kujiona kwamba yeye ndiye alikuwa sababu kubwa ya msichana huyo kupata matatizo hayo kwani pasipo kumwambia kwamba aelekee nchini Marekani, asingepata ajali hiyo.
“Pole sana Walker! Huu si mwisho wa Patricia,” alisema Walter huku akimpigapiga ndugu yake huyo mgongoni kama njia ya kumfariji.
Daktari alinyamaza, mbali na taarifa hiyo pia alikuwa na taarifa nyingine kuhusu msichana huyo, taarifa ambayo aliamini ingekuwa mbaya zaidi, kila alipotaka kuwaambia, alinyamaza kwani kama kwa taarifa hiyo tu Walker alilia hivyo, ingekuwaje kama angempa taarifa nyingine ambayo aliamini ingemuumiza zaidi?
Hakutaka kunyamaza, ilikuwa ni lazima kumwambia ukweli juu ya kila kitu kilichokuwa kikiendelea. Akawaambia kwamba mbali na tatizo hilo, pia kitendo cha ubongo wake kupata ufa uliufanya kutikisika na kupata tatizo jingine ambalo lingeonekana kuwa la hatari kama lilivyokuwa lile la kupooza.
“Kitu gani?” aliuliza Walter.
“Hatoweza kukumbuka kitu chochote kile. Kumbukumbu zake zimefutika, zimekuwa kama za mtoto aliyezaliwa leo. Yaani hatoweza kumfahamu mtu yeyote yule, hatowafahamu wazazi wake, hatowafahamu nyie, hatokumbuka kitu chochote kile, ila yote hayo yatatokea kama tu atarudiwa na fahamu,” alisema daktari aneno yaliyomfanya Walker kulia zaidi.
Huo ndiyo ulikuwa ukweli wenyewe, hakukuwa na kilichobadilika, msichana Patricia alikuwa kimya kitandani, uti wa mgongo ulivunjika na mbaya zaidi alipata matatizo kichwani yalioupelekea fuvu lake kupata ufa na ubongo kutikisika.
Yalikuwa ni maumivu makali kwa Walker, hakuamini kama kweli mpenzi wake angepatwa na tatizo kama hilo. Hakuacha kulia, alibembelezwa lakini hakubembelezeka, alihisi kama huo ndiyo ungekuwa mwisho wa msichana huyo mrembo aliyekuwa akimpenda kwa moyo wake wote.
Baada ya kuzungumza na daktari, wakatoka na kuelekea nje ya chumba ambacho Patricia alikuwa amelazwa kwa ajili ya mapumziko baada ya kufanyiwa upasuaji. Wakatulia hapo, hakukuwa na mtu aliyewasogelea kwani kwa jinsi walivyoonekana, haukuwa muda mzuri wa kuomba kupiga nao picha au kuomba kusainiwa vitabu vyao.

Edmund alikuwa akitafutwa kila kona, watu waliangalia mitaani, kila mtu waliyekuwa wakimtia hofu kwamba alikuwa yeye walimchukua. Hawakujua mahali jamaa huyo alipokuwa, japokuwa matangazo yalibandikwa kila kona lakini bado mwanaume huyo hakuonekana.
Hilo likawapa wasiwasi watu wengi na kuhisi kwamba inawezekana mwanaume huyo akawa amepotea sehemu fulani na hivyo alitakiwa kutafutwa kwa nguvu zote. Walipambana, walimtafuta lakini matokeo yaliendelea kuwa yaleyale kwamba hakuonekana sehemu yoyote ile.
Baada ya kuona kuwa wasingefanikiwa, M16 wakaamua kuanza kumtafuta kupitia simu yake, waliamini kwamba huko alipokuwa ilikuwa ni lazima kuwasiliana na familia yake hivyo kufanya hivyo.
Walipomtafuta kwa kutumia simu yake, waliona kabisa kwamba jamaa alikuwa akiondoka kutoka sehemu moja kwenda nyingine. Walimfuatilia kwa nguvu zote, waliona akiondoka Uingereza na kuingia Wales, hawakutaka kubaki nyuma, wakawasiliana na polisi wa huko na kuwaambia uwezekano wa kumkamata Edmund.
Wakati akiwa ameondoka katika sehemu ya kuchezea watoto, dakika tatu mbele polisi wakafika mahali hapo na kuanza kuangalia kila kona, waliamini kwamba alikuwa hapo lakini kitu cha ajabu kabisa hawakuweza kumuona.
Kifaa cha GPS ndicho kilichokuwa msaada kwao, wakaanza kuangalia ili kuona kama alikuwa mahali hapo amejificha au la, walipoangalia, wakaona kwamba alikuwa amekwishaondoka mahali hapo na kuanza kumfuatilia kwa kutumia kifaa hicho.
Hilo lilifanyika kwa nguvu kubwa, wakafanikiwa kuifikia nyumba ambayo alikuwepo, kifaa kile kiliwaonyeshea kwamba Edmund alikuwa ndani ya nyumba hiyo na hivyo kuanza kuelekea humo.
Walipoufungua mlango, Mzee Vonn akatoka, kitu cha kwanza wakamuweka chini ya ulinzi na kuingia ndani ambapo huko, pamoja na kumtafuta sana, wakamkosa kabisa.
“Yupo wapi?” aliuliza polisi mmoja.
“Sijui! GPS inaonyesha yupo humu. Mungu wangu! Kumbe ameacha simu na yeye kukimbia,” alisema polisi mmoja huku akishangaa.
Waliifuatilia simu hiyo kwa kipindi kirefu, waliamini kwamba wangempata lakini mwisho wa siku waliweza kuipata simu na Edmund hakuwepo mahali hapo. Walichanganyikiwa, wakatoka ndani, wakamtafuta hata kwa nje na sehemu nyingine lakini hawakufanikiwa kumpata.
****
Japokuwa Edmund alikaribishwa kwa upendo mkubwa ndani ya nyumba ya Bwana Vonn lakini moyo wake haukuwa na amani hata kidogo. Alimwangalia mzee huyo, alionekana kuwa na furaha mno kwa yeye kuwa hapo na hakuona dalili zozote za mzee huyo kumkamata au kumfanyia mchezo mchafu wowote ule.
Akapelekwa chumbani kwake na kutulia huko. Usingizi haukuja, alijaribu kulala lakini usingizi ulikataa kabisa kitu kilichomfanya kuwa na hofu kwamba inawezekana kungekuwa na kitu kibaya ambacho kingemtokea mahali hapo.
Akatulia chumbani, muda ulizidi kwenda, usingizi ukakata na kutulia kitandani. Macho yakeyalikuwa dirishani, alikuwa akiangalia nje kuona kama kungekuwa na mtu yeyote ambaye angefika nyumbani hapo.
Muda ulizidi kwenda, baada ya dakika kadhaa akasikia muungurumo wa gari kutoka nje, haraka sana akainuka na kuangalia nje, alichokiona ni gari kubwa lililoandikwa SWAT ubavuni, gari ambalo alifahamu kabisa kwamba lilikuwa ni la polisi waliokuwa na silaha nzito.
Hakutaka kujiuliza sababu ya watu hao kufika mahali hapo, akajua kwamba walifika hapo kwa kuwa walikuwa wakimtaka yeye, hivyo akasimama na kuanza kufikiria ni kwa jinsi gani angeweza kuondoka nyumbani hapo pasipo kuonekana.
“Ni lazima niondoke!” alijisemea.
Wakati hajajua hata kitu gani alitakiwa kufanya, akasikia mlango wa sebuleni ukifunguliwa, hakutaka kujiuliza, alijua dhahiri kwamba huyo alikuwa Vonn ambaye bila shaka ndiye aliyewaita polisi hao kwa kuwa yeye alikuwemo ndani ya nyumba hiyo.
Kwa haraka sana akachomoka chumbani, akaelekea jikoni, huko, akakuta mlango mwingine wa kutoka nje, hakutaka kujiuliza, akaufungua taratibu na kuangalia kama kulikuwa na mtu.
Polisi walionekana kufanya uzembe mmoja tu, ni kweli walifika nyumbani hapo, mtu wao alikuwa ndani lakini uzembe waliokuwa wameufanya ni kutokuizunguka nyumba ile. Kitendo cha kumpata Vonn pale mlangoni walikuwa na uhakika kwamba Edmund alikuwa ndani na hivyo kuingia.
Hakukuwa na mtu, waliangalia kila kona, kabatini, chini ya kitanda na sehemu nyingine lakini hawakufanikiwa kumuona mtu yeyote yule.
Wakati wao wakiangalia huku na kule, Edmund alikuwa mbali kabisa na nyumba hiyo, alikuwa akikimbia kwa mwendo wa kasi, kubaki ndani ya nyumba hiyo kulimaanisha kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wake.
Alikimbia mpaka sehemu moja aliyokuta nyumba kubwa iliyokuwa imezungushiwa fensi kubwa huku kwa pembeni kukiwa na mti. Alichokifanya ni kuufuata mti na kuupanda na kutulia huko, sehemu ambayo aliamini kwamba ingekuwa salama mpaka asubuhi yake ambapo angeamua ni kitu gani angetakiwa kufanya.
Kwake, alijiona kutokuwa na rafiki, aliamini kwamba inawezekana Mark alimfanyia ujanja ili akamatwe na kuvuna kiasi cha pesa kilichokuwa kimewekwa au mjomba wake, Vonn aliingiwa na tamaa na hivyo kutaka kumkamatisha na kuvuna kiasi hicho cha pesa.
Hakutakiwa kumwamini mtu yeyote yule kwa kipindi hicho. Alihitajika kupambana na hali yake mpaka kuona kwamba anafanikiwa kuwakimbia polisi hao kwa maisha yake yote.
Macho yake hayakutoka kule ilipokuwa nyumba ya Bwana Vonn, alikuwa akiiangalia kwa kuyaweka majani pembeni. Akaona mzee huyo akichukuliwa na kupakizwa ndani ya gari kisha kuondoka mahali hapo huku polisi wengine wakibaki kuhakikisha kwamba hatoki kama tu alikuwa ndani amejificha.
***

ITAENDELEA

CHANZO : BURE SERIES
 
SEHEMU YA KUMI .... MWISHO

Walker alitia huruma, moyo wake ulikuwa ukimfikiria mpenzi wake, Patricia, alimpenda, kwake, msichana huyo alikuwa kila kitu. Bado hakuamini taarifa za madaktari kwamba mpenzi wake asingeweza kukumbuka kitu chochote wala kusimama kama ilivyokuwa zamani, wakati mwingine alihisi kwamba alikuwa kwenye ndoto mbaya na ya kusisimua ambapo baada ya muda fulani angeshtuka na kujikuta akiwa kitandani.
Kama kulia, alilia sana lakini hakukuwa na kitu kilichobadilika. Siku ziliendelea kukatika, kila siku alikwenda hospitalini hapo akiwa na pacha wake, Walter. Alihitaji kumuona mpenzi wake kitu ambacho baada ya siku tatu kuukatika, madaktari wakawaruhusu kuwaona.
Macho yake yalipotua kwa msichana huyo aliyekuwa kitandani hoi, hakuamini, alimsogelea na kumwangalia vizuri, hakuonekana kama alikuwa mzima, alionekana kama mfu kitandani pale. Alilia zaidi, akamsogelea na kumkumbatia.
Alijiona kuwa kwenye wakati mgumu, alijihukumu kwamba yeye ndiye aliyesababisha hayo yote kwani bila yeye Patricia asingesafiri mpaka nchini Marekani na kupata ajali hiyo.
“Patty! Wake up and talk to me,” Patty! Amka na uzungumze nami) alisema Walker huku akiendelea kulia.
Siku hiyo ilikuwa kimya, siku ziliendelea kukatika huku kila siku wakifika mahali hapo. Kwenye magazeti, mitandao ya kijamii na sehemu nyingine kila kona walikuwa wakiwazungumzia watu wao. Kila mmoja alimuonea huruma Walker, kwa jinsi alivyokuwa na pacha wake walipaswa kupata fulana maisha yao yote lakini kitu cha ajabu kabisa kilichokuwa kikiendelea kilikuwa ni maumivu makali.
Baasa ya siku kumi na sita kupita ndipo Patricia akayafumbua macho yake na watu wa kwanza kabisa kuwaona walikuwa mapacha hao hata kabla ya wazazi wake.
“Patricia! Hatimaye umeamka,” alisema Walker huku akitabsamu.
Msichana huyo alinyamaza, hakukumbuka kitu chochote kile, alikuwa akiwashangaa, hakujua watu hao walikuwa wakina nani na walihitaji nini kutoka kwake.
Wazazi wake waliokuwa na nyuso za furaha hasa baada ya kumuona akiwa amefumbua macho wakamsogelea na kumwangalia, hata nao pia, Patricia hakuwa akiwakumbuka, alibaki akiwashangaa tu.
“Nyie ni wakina nani? Nipo wapi hapa?” aliuliza Patricia huku akimwangalia kila mmoja.
Swali hilo likawapa maumivu makali zaidi mioyoni mwao, hawakuamini walichokuwa wamekisikia kutoka kwa binti yao, alikuwa amepoteza kumbukumbu zake zote na kitandani pale hakuwa akikumbuka kitu chochote kile.
Patricia alipojaribu kunyanyuka kitandani pale, alishindwa kabisa, akahisi mwili wake ukiwa umekufa ganzi, hakujua ni kitu gani kilichokuwa kimetokea kitu kilichompelekea kuwauliza watu wale waliokuwa mbele yake kwamba ni kitu gani kilikuwa kimetokea mpaka kuwa hivyo.
Hakukuwa na mtu aliyemjibu kitu chochote kile, msichana huyo aliendelea kushangaa na hata wakati mwingine kulia. Daktari akaingia, alipomuona yupo katika hali hiyo, akawaomba watoke chumbani humo kwani mgonjwa alitakiwa kupumzika zaidi kitu ambacho hakikuwa tatizo lolote lile, wakatoka chumbani humo.
Nje, Walker akaanza kulia, aliumia mno moyoni mwake. Alibaki nje ya chumba kile akiuangalia mlango wa kuingia ndani. Alimwambia Mungu kwamba mtu aliyekuwa akimuhitaji kwa kipindi hicho alikuwa msichana wake tu, hakuhitaji pesa, hakuhitaji umaarufu, kwake, Patricia alionekana kuwa kila kitu.
Alimuomba Mungu afanye muujiza lakini hilo halikuwezekana, msichana Patricia akaendelea kuwa kitandani pale huku akiendelea kushangaa sababu za kutokusimama na hata watu wale waliokuwa chumbani mule, kilichokuwa kikiendelea, hakukielewa kabisa.

Naseku hakuwa na raha hata kidogo, kila alipokuwa akiwaangalia watoto wake alikuwa akilia tu. Walikuwa na umaarufu mkubwa, pesa nyingi lakini kitu cha ajabu kabisa maisha waliyokuwa wakipitia, yaliwapa maumivu makubwa mno.
Walter na Walker walikuwa watu wa huzuni tu, kila siku walikuwa wakipitia majanga mbalimba, kama walinusurika katika janga hili, kesho walikuwa wakitumbukia katika janga jingine kabisa. Hayo yalikuwa maisha yao, ni kama walikuwa wamezoea kumbe kwa jinsi walivyokuwa hawakutakiwa kabisa kupita katika maisha waliyokuwa wakipitia kila siku.
Yeye na mumewe, Cassian walikuwa na mtoto mwingine, Esta ambaye kipindi hicho alikuwa chuo kikuu lakini bado tu hawakuonekana kufurahia kabisa, walikuwa wakimuomba Mungu ili kila kitu walichokuwa wakipitia watoto wao hao yaishe ili waishi maisha ya amani na furaha kama ilivyokuwa zamani.
Machozi hayakuacha kutiririka mashavuni mwake, kila siku viganja vyake vilikuwa mashavuni akifuta machozi yaliyokuwa yakitiririka kila alipokuwa akiwaangalia watoto wake waliokuwa kwenye matatizo makubwa.
Walker hakuacha kulia, mpenzi wake aliyafumbua macho yake lakini hakuwa na furaha hata kidogo, alisahauliwa, msichana huyo hakukumbuka kitu chochote kile na kila alipokuwa akiwaangalia, alibaki akishangaa.
Hawakuacha kufika hospitalini hapo, Patricia aliendelea kuwa kitandani na hata pale alipopata nafuu, alichukuliwa na kuwekwa kwenye kiti cha walemavu kwani hakuwa na uwezo wa kufanya kitu chochote kile katika kiti kile alichokuwepo.
Walker na Walter ndiyo waliokuwa na kazi ya kumpeleka huku na kule, walihuzunika, wakati mwingine walikuwa wakilia, kwa Walker, alitumia nafasi hiyo kuzungumza naye maneno mengi na hata kumkumbusha yaliyopita lakini msichana huyo hakuwa akikumbuka kitu chochote kile.
“Mimi nilikuwa nasoma?” aliuliza Patricia huku akishangaa.
“Ndiyo! Ulikuwa nchini Ufaransa ukiishi na wazazi wako. Unakumbuka?’ aliuliza Walker huku akimwangalia msichana huyo.
“Hapana! Sikuwahi kuishi Ufaransa hata siku moja.”
“Unamkumbuka Annie?”
“Ndiye nani?”
“Rafiki yako chuoni!”
“Kwani mimi nimewahi kusoma?”
“Ndiyo! Tena ulikuwa na akili sana darasani,” alisema Walker.
Hakukumbuka kitu chochote kile, kila kitu alichokuwa akiambiwa kilionekana kuwa kipya katika maisha yake. Walker na mwenzake walijaribu kumkumbusha kila kitu kilichotokea lakini hakukumbuka kabisa.
Wazazi wake nao walikuwa wakilia tu, waliumia, hawakuamini kama binti yao angepitia maisha kama aliyokuwa akipitia. Ubongo ulicheza na uti wa mgongo kuvunjika, yalikuwa ni matatizo makubwa yaliyowafanya kulia kila siku.
Siku zikaendelea kukatika, baada ya miezi tisa, Walker na Walter wakaanza kujisikia hali ya tofauti vichwani mwao. Walikuwa wakipata maumivu makali ya kichwa kiasi kwamba wakati mwingine walihisi kama walibeba vitu vizito na kupoteza fahamu.
Lilikuwa tatizo kubwa lililowatesa kupita kawaida, Naseku na mumewe walishangaa, watoto wao hawakuwahi kupata tatizo kaka hilo, hawakujua kilichokuwa kimetokea hivyo kuwachukua na kuwapeleka hospitalini.
“Tatizo limeanza lini?” aliuliza daktari huku akiwaangalia.
“Ni ghafla sana, hatujui tatizo nini!” alijibu Cassian huku akimwangalia daktari.
Kilichofanyika ni vipimo, wakaangalia vichwani mwao, walihisi kwamba inawezekana fuvu la kichwa lilikuwa limepata majeraha hivyo kuangalia. Huko hawakugundua kitu, iliwashangaza, hakukuwa na tatizo lolote lile sasa kwa nini walikuwa wakizimia mara kwa mara.
Kilichofuata kilikuwa ni kuangalia mishipa na misuli yao pale ilipokuwa ikiwaunganisha vichwani. Hapo ndipo wakagundua kwamba walikuwa wameharibu mishipa na misuli kwa kuwa tu walikuwa wakitumia nguvu kubwa mno katika kufikiria na kulia hivyo mishipa mingi kulegea na kutanuka hali iliyoonyesha kwamba hali ingekuwa mbaya zaidi katika maisha yao kama hali hiyo ingeendelea.
“Tatizo kubwa ni nini?” aliuliza Cassian, Naseku hakuzungumza chochote kile, kazi yake ilikuwa ni kulia tu.
“Misuli na mishipa yao ina tatizo hasa katika sehemu hii waliyoungana, kuna tatizo kubwa la kuvimba na kusinyaa,” alijibu daktari huku akiwaangalia wazazi hao.
Lilikuwa pigo kubwa kwao, kitendo cha kufikiria sana na kuhuzunika ndicho kilikuwa sababu kubwa ya wao kuwa katika hali hiyo. Wakalazwa hosipitalini. Kila mtu duniani akajua kile kilichotokea, watu wengi wakaanza kutuma salamu zao za pole kwa mapacha hao ambao walilazwa katika chumba maalumu huku madaktari wakiendelea kuwahudumia.
Hakukuwa na mtu aliyeruhusiwa kuingia ndani ya chumba hicho zaidi ya manesi na madaktari ambao walikuwa kwa ajili ya kuwatibu tu. Siku ziliendelea kukatika huku wakiwa humo. Tatizo lile likaanza kukua na mwisho wa siku kuanza kutoka damu katika masikio yao na madaktari walipowapima, wakaonekana kuwa na tatizo jingine kabisa, mishipa na misuli iliyokuwa imevimba ilianza kuchanika.
“Nini?” aliuliza daktari mmoja huku akionekana kuchanganyikiwa.
“Ndiyo hivyo! Tatizo kubwa ni kuungana kwao, haya mengi hujitokeza mara chache sana, ni wawili kati ya watu elfu kumi. Chanzo kikubwa kabisa ni kuungana kwao,” alisema daktari ambaye alikuwa ametoka kuwachukua vipimo.
Ilikuwa taarifa mbaya ambayo hawakujua ni kwa namna gani walitakiwa kuwaambia wazazi wao. Pale katika kichwa ambapo waliungana kulipitia mishipa mingi ya damu na misuli kiasi kwamba hata ilipokuwa imevimba, ilikuwa rahisi kuchanika kwa kuwa tu ilikuwa imebanana sana na tena ilikuwa mingi kupita kawaida.
“Watakufa! Kama kweli tatizo limefikia hapa, watakufa,” alisema daktari mmoja huku akiwaangalia wenzake, kidogo akaonekana kukata tamaa, hakukuwa na mgonjwa aliyekuwa akichanika mishipa na misuli halafu akapona.
****
Edmund aliendelea kukaa kwenye mti mpaka asubuhi. Mwili wake ulichoka, hakulala usiku mzima, alikuwa na hofu kwa kuona kwamba angekamatwa na polisi. Akateremka na kuanza kupiga hatua kuelekea barabarani.
Siku hiyo hali ilionekana kuwa tofauti, kila alipokuwa akipita, hakukuwa na watu wengi kama ilivyokuwa siku nyingine hasa katika nchi hizo zilizokuwa zikitawaliwa na Malkia Elizabeth.
Alitembea kwa mwendo wa taratibu, uso wake ulikuwa chini, mawazo mengi yalimtawala na hakutaka kabisa kugundulika alionekana kuwa mnyonge kupita kawaida, alijuta, hakujua kama kuna siku angekuja kuishi katika maisha aliyokuwa akiishi kipindi hicho.
Alitembea mpaka alipofika katika kituo cha daladala ambapo hapo akatulia. Akaanza kuyafikiria maisha yake yaliyopita, japokuwa yalikuwa kwa kipindi kifupi sana hasa baada ya kutaka kuwaua mapacha walioungana lakini aliona kama ulikuwa mwaka mzima kwa jinsi alivyokuwa.
Wakati akiwa hapo, watoto wanne wakaletwa mahali hapo huku wakiwa wamevaa sare za shule na kusubiri hapo huku wakiwa na wanawake watu wazima wawili. Walimsalimia lakini mawazo ya Edmund hayakuwa hapo kabisa, alikuwa akifikiria mbali, maisha yake yalimchanganya kupita kawaida.
Hawakutaka kushughulika naye, wakasubiri gari la shule ambalo lilifika hapo baada ya dakika kadhaa na kuwaingiza watoto wale na kuondoka. Edmund hakusimama, bado kichwa chake kilikuwa kimechanganyikiwa, hakujua ni kitu gani alitakiwa kufanya, alikuwa na njaa, mwili ulichoka na hakujua ni kwa jinsi gani angeweza kula.
Wakati akiwa amekaa mahali hapo, kwa mbali akaliona lile gari la wanafunzi likaanza kurudi mahali hapo. Hakuliona, kichwa chake kilikuwa mbali kabisa, gari lile likasimama karibu naye, polisi wawili waliokuwa na bunduki mikononi mwao wakateremka na kumuweka chini ya ulinzi kwa kutaka aweke mikono yake kichwani.
Hakufanya hivyo, alikuwa akibubujikwa na machozi mfululizo na muda wote alihisi kama alikuwa akienda kufa kwa jinsi maisha aliyokuwa amepitia yalivyomchanganya.
Alibaki akiwa kama mtu aliyeganda, hakutingishika, kichwa alikiinamisha kidogo na hakuonekana kujua kitu chochote kilichokuwa kikiendelea. Kama kuzunguka huku na kule, alifanya hivyo kwa kipindi kirefu sana, akachoka, ilikuwa ni bora kukamatwa na polisi akapumzike lakini si kuendelea kuzurura kama alivyokuwa akifanya.
“Hands on your head,” (mikono kichwani mwako) alisema polisi mmoja huku akiwa amemnyooshea bastola lakini Edmund hakufanya hivyo.
Wakamsogelea na kumfunga pingu, hakufanya kitu chochote zaidi ya kulia, moyo wake ulibadilika na kuumia mno, hakuyapenda maisha yake, aliyachukia na kitu pekee alichokuwa akikihitaji kilikuwa ni kupumzika tu.
Kitendo cha kukamatwa, watu wakaanza kujaa na kutaka kujua kilichokuwa kimeendelea, dereva wa gari lile la wanafunzi ambaye ndiye aliyetoa taarifa kwa polisi hao baada ya kumuona katika kituo hicho akaambiwa kwamba gari hilo lilihitajika kumpeleka Edmund mpaka kituoni jambo ambalo halikushindikana kabisa.
Akachukuliwa, akapakizwa ndani ya gari huku akilia. Hakuzungumza kitu chochote kile, alikuwa kimya, watu waliogundua kwamba yule alikuwa Edmund, wakapigiana simu na kuwaambia wenzao kwamba hatimaye Edmund alikuwa amekamatwa, ili kuonyesha ushahidi, mpaka picha wakawatumia.
“Una uhakika ni yeye?” aliuliza jamaa mmoja kwenye simu.
“Ngoja nikutumie picha uone!”

Hakukuwa na kitu kilichobadilika, Walter na Walker waliendelea kuwa katika hali ileile, walikuwa kitandani huku wakiwa kwenye hali mbaya. Madaktari walikuwa wakihangaika kuhakikisha wanarudi katika hali zao za kawaida lakini hilo lilishindikana kabisa.
Damu zilizidi kuwatoka, mishipa ilipasuka hali iliyowafanya kuwa katika hali mbaya zaidi. Wazazi wao walikuwa wakilia, hawakuwa wakiamini kama mwisho wa kila kitu ungekuwa namna hiyo.
Vyombo vya habari viliendelea kutangaza kwamba watu hao walikuwa na dalili ndogo sana za kupona na kurudi katika hali kama zamani kwani hakukuwa na mtu ambaye mishipa yake ilipasuka halafu akapona.
Kipindi hicho ni kama dunia ilikuwa kimya, ilikuwa ikiomboleza kwa kile kilichokuwa kikiendelea. Kwenye mitandao ya kijamii, magazetini na hata mitaani watu walikuwa wakiwazungumzia wawili hao na jinsi walivyokuwa na nafasi ndogo ya kuweza kupona na kurudi katika hali zao kama walivyokuwa zamani.
“Wanakufa!” alisema mwanaume mmoja alipokuwa akiziangalia picha za mapacha hao waliokuwa hawajitambui katika kitanda kikubwa walicholalia.
“Ila nina uhakika Mungu atawaponya!” alisema mwanamke aliyekuwa pembeni yake, macho yake yalikuwa mekundu, japokuwa hawakuwa ndugu zake lakini alishindwa kujizuia, alikuwa amelia sana kwa ajili ya watu hao.
Watu wakaendelea kujazana hospitalini walipokuwa, kila mmoja alitaka kujua kile kilichokuwa kikiendelea. Wengi waliokuwa mahali hapo walionekana kukata tamaa, walijua kabisa kwamba baada ya saa chache zijazo wawili hao wangefariki dunia na kwenda kuanza maisha mapya baada ya kifo.
Naseku alilia sana, aliishiwa nguvu na kupoteza fahamu zaidi ya mara tatu, alikuwa na uchungu mno, moyo wake ulimuuma na kila alipokuwa akiwaangalia watoto wake, alisikia kitu chenye ncha kali kikiuchoma moyo wake.
Aliomboleza, mtu pekee aliyekuwa akimfariji kwa kipindi hicho alikuwa mume wake, Cassian. Kila alipokuwa akibembezwa, hakubembelezeka kwani alijua kabisa kwamba huo ndiyo ungekuwa mwisho wa kila kitu, watoto wake wangekufa palepale hospitalini walipokuwa.
Madaktari hawakuacha kuhangaika, walifanya kila liwezekanalo kuokoa maisha ya mapacha hao. Kila mtu aliwatumainia, wao ndiyo ulikuwa msaada wa mwisho waliokuwanao kipindi hicho, yaani wao ndiyo waliokuwa wameshililia uhai wa mapacha hao, wao ndyo wangeamua kama watu hao walitakiwa kufa au kuendelea kuishi.
Hawakuwa na mategemeo yoyote ya mapacha hao kupona, damu zilizokuwa zikiwatoka baada ya mishipa kuchanika ziliendelea kusambaa miilini mwao na hivyo kuwafanya kuwa kwenye hali mbaya zaidi.
Ilipofika tarehe 2/09/2016 majira ya saa 2:36 usiku ndiyo muda ambao Walter na Walker wakafariki dunia katika kitanda walichokuwepo.
Hiyo ilikuwa habari ya mshtuko, madaktari ambao walilitambua hilo wakaishiwa nguvu, hawakujua ni kwa namna gani wangeweza kuwaambia wazazi wao juu ya kile kilichokuwa kimetokea kwani kwa kipindi chote ambacho watoto hao walikuwa mahututi nyuso zao zilionekana kuwa kwenye maumivu makali, ingekuwaje kama wangewaambia kuwa walifariki dunia?
“Tutaitoaje miili hii na wakati wazazi wao wapo hapo nje?” aliuliza daktari mmoja.
“Labda tukawatoe!”“Tukawatoe? Tutaanzaje?”“Subiri! Nakwenda kuwachukua na kuwaambia twende kwa daktari kuongea nao. Wakati nimetoka nao, nyie watoeni haraka sana muwapeleke katika chumba maalumu kwanza,” alisema daktari mwingine.
“Sawa.”
Wakakubaliana, hakukuwa na muda wa kupoteza, hapohapo daktari yule akatoka, akaanza kuzungumza nao na kuwaambia kwamba walitakiwa kuzungumza nao katika ofisi yake hivyo awafuate.
“Wanaendeleaje?’ aliuliza Naseku huku akimwangalia daktari.
“Wanaendelea salama! Twendeni,” alisema daktari.
Wakasimama na kuanza kuondoka, walipiga hatua fupifupi huku kila mmoja akiwa na mawazo tele. Daktari alikuwa akiwaza ni kwa namna gani angeweza kuwaambia wazazi hao kile kilichokuwa kikiendelea kwani kwa jinsi walivyokuwa wakionekana, hawakuwa radhi kupokea taarifa kwamba watoto wao walikuwa wamefariki dunia.
Wakaondoka katika korido ile, haraka sana madaktari wale waliokuwa wamebaki ndani ya chumba kile walipoona wameondoka, wakaanza kuitoa miili ile iliyokuwa kitandani na kuipeleka katika chumba kingine.
Wakati Naseku na mumewe akipiga hatua, akajipekua, hakuwa na simu, alikuwa ameisahau pale alipokuwa amekaa kwani aliondoka kwa kushtukiza sana. Hakutaka kuendelea na safari ya kuelekea huko, akamwambia mumewe kwamba alisahau simu na hivyo kuirudia.
Alipofika katika korido ile, macho yake yakatua katika kitanda kikubwa kilichokuwa kikitolewa katika chumba kilekile walichokuwa watoto wake huku kikiwa kimefunikwa na shuka kubwa la kijani.
Moyo wa Naseku ukapiga paaa! Hakuamini alichokuwa akikiona, madaktari walipomuona, wakashikwa na hofu na kujua kwamba ile siri waliyokuwa wameitunza ilibumburuka. Haraka sana Naseku akaanza kupiga hatua za harakaharaka kuelekea kule wapokuwa wale madaktari, tayari akili yake ilimwambia kwamba wale walikuwa watoto wake, na kama walikuwa wamefunikwa shuka la kijani ilimaanisha kwamba walifariki dunia.
Hata kabla hajafika, madaktari wakamzuia, hakutakiwa kuangalia kile kilichokuwa kimefunikwa, hapo ndipo akaanza kulia. Alilia kama mtoto, alipiga kelele kiasi kwamba watu wengine wakafika kuona nini kilikuwa kikiendelea. Alilia kwa ajili ya watoto wake, alilia kwa kuwa walikuwa watu muhimu sana katika maisha yake.
“Walter...Walker...kwa nini mmekufa? Kwa nini mmetuacha...mbona hamkusema kama mtakufa...nitaishi vipi mimi....nitaishi vipi bila nyie wananngu?” alilia Naseku kama mtoto huku madaktari wakiwa wamemzuia pande zote, hakuchukua muda mrefu, akaanguka kama mzigo, akapoteza fahamu na hakujua ni kitu gani kiliendelea baada ya hapo.
***
Hali haikuweza kubadilika kwa Patricia, aliendelea kuwa vilevile kama alivyokuwa. Hakuweza kukumbuka kitu chochote kile, kila alipokuwa akitembelewa na watu alikuwa akiwashangaa, hakujua walikuwa wakina nani na wakati mwingine alijiuliza sababu ya kuwa hospitalini hapo lakini akakosa jibu.
Wazazi wake waliendelea kuhuzunika, hakukuwa na kipindi kigumu walichokuwa wakipitia kama kipindi hicho. Hakukuwa na kilichobadilika, mbaya zaidi wakati wakiendelea kumsubiri binti yao arudiwe katika hali ya kawaida, wakasikia kwamba Walter na Walker walikuwa wamefariki dunia.
Ilikuwa ni habari mbaya, ilikuwa ni zaidi ya kuchomwa na msumali wa moto mioyoni mwao, hawakuamini kile kilichokuwa kimetokea kwani mbali na pacha mmoja kutoka kimapenzi na binti yao, walikuwa wakiwapenda kupita kawaia.
Dunia ikashtuka, hakukuwa na aliyeamini kwamba mapacha hao walikuwa wamefariki dunia, kila mtu alikuwa akilia, wengi wakaelekea hospitalini hapo na kuweka mashada ya maua na picha mbalimbali katika eneo ambalo waliruhusiwa kufanya hivyo.
Hakukuwa na mtu aliyeamini kama wasingeweza kuwaona watu hao tena, vile vipaji vya kipekee walivyokuwanavyo wasingeweza kuviona au kusikia tena. Watu maarufu wakatuma salamu za rambirambi katika mitandao ya kijamii na wengine kwenda huko na kuwatia moyo wazazi wao waliokuwa watu wa kulia kila wakati, tena mpaka muda huo, Naseku alikuwa amepoteza fahamu zaidi ya mara nne, yote ilikuwa ni kwa sababu ya kuumizwa na msiba mzito aliokuwa ameupata.
Baada ya siku mbili, mapacha hao wakapelekwa katika Kanisa la St. John lililokuwa haohapo New York na kuagwa sura ya mwisho kabla ya kupelekwa nchini Tanzania tayari kwa maziko.
“Hivi ni kweli wamekufa?” aliuliza mwanamke mmoja, macho yake yalikuwa yamevimba huku mashavu yakiwa yamelowanishwa kwa machozi.
“Yaani siamini! Kweli mapacha hawa wamekufa?” aliuliza mwanamke mwingine, naye hakuwa ameamini kile kilichokuwa kimetokea.
Siku iliyofuatwa taratibu za kuwasafirisha mapacha hao zikafanyika na hivyo kupelekwa nchini Tanzania. Ndani ya ndege ilikuwa ni huzuni tele, kila wakati Naseku alipokuwa akiliona jeneza la watoto wake alikuwa akilia kwa uchungu, hakuwa akiamini kwamba mwisho wa kila kitu ungekuwa namna ile.
Zaidi ya watu elfu kumi na tano walikuwa wamekusanyika katika Uwanja wa Kimataifa wa Julius Nyerere kwa ajili ya kuipokea miili hiyo. Watu wengi waliokuwa mahali hapo walikuwa na fulana zilizokuwa na picha za mapacha hao huku wengine wakiwa na maua kama njia mojawapo ya kuomboleza kwa kile kilichotokea.
Ndege ilipotua, watu wakateremka, jeneza likashushwa, watu wakaanza kulia kwa sauti, kila mmoja alitaka kuligusa jeneza hilo ambalo lilipakizwa na kuanza kupelekwa katika uwanja wa taifa ambapo huko watu walitakiwa kuaga na kisha kuelekea kanisani, kufanyiwa ibada na kwenda kuzikwa katika makaburi ya Kinondoni.
Kila kitu kilichotakiwa kufanywa, kilifanywa na ilipofika majira ya saa kumi jioni, tayari msafara ukaanza kuelekea katika makaburi hayo na hivyo mapacha hao kuzikwa huko.
Ilikuwa ni huzuni, mapacha waliokuwa wameipatia Tanzania umaarufu walifariki, kila mmoja alihuzunika, japokuwa walikuwa wameondoka lakini kwenye akaunti yao waliacha utajiri mkubwa ambao wazazi wao wakaamua kutumia asilimia kumi ya utajiri huo kwa ajili ya kuwasaidia watoto waliokuwa kwenye matatizo mbalimbali.
Kwa msichana Patricia, aliendelea kuwa kwenye hali hiyohiyo kwa muda wa miaka mitano. Alikuwa akitibiwa kwa nguvu zote, pingili za mgongo wake ambazo ziliachia zikaanza kurudi na miaka miwili mbele, akafanikiwa kusimama na kuanza kutembea ila kumbukumbu zake hazikuweza kurudi tena.
Ubongo wake ulikuwa kama umeathiriwa, hakujua kilichotokea, hakujua kama aliwahi kuwa na mwanaume aliyekuwa akimpenda kwa moyo wake wote. Wazazi walijitahidi kumpeleka katika hospitali mbalimbali lakini kote huko waliambiwa kwamba binti yao asingeweza kukumbuka kitu chochote mpaka kifo chake.
Maisha yake yakaanza upya, akaanza kutengeneza urafiki na watu wengine, hata alipokuwa akiziona picha za Walter na Walker hakuwa akikumbuka kitu chochote kile, kwake, watu hao walionekana kuwa wageni kabisa ambao aliwaona mara kadhaa walipokuwa wakimfuata hospitalini kumuona.
Naseku hakuwa na furaha, alikuwa mtu wa huzuni, kila alipokuwa akiziona picha za watoto wake, alikuwa akilia, machozi yalitiririka mashavuni mwake na kuyafuta kwa kutumia viganja vyake.
Hakikubadilika kitu, kwa mtoto mmoja waliyekuwa naye, Esta, wakaendelea kumlea na baada ya miaka minne, akaolewa na kufanikiwa kujifungua watoto mapacha wa kiume ambao kwa kuwaenzi ndugu zake, akaamua kuwaita Walter na Walker.

MWISHO
TOA MAONI YAKO

CHANZO : BURE SERIES
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom