Riwaya: Yatima

muhi

Member
Joined
Nov 12, 2014
Posts
51
Reaction score
19
RIWAYA: YATIMA

MTUNZI :RAJU NUHADAMU
Simu : 0679296836

**SEHEMU YA KWANZA**

Mamu alikuwa ni msichana mzuri wa sura,mzuri wa umbo,na pia alikuwa ni mzuri wa tabia.
********************
Alizaliwa katika familia ya kimaskini,alikuwa ni mtoto pekee katika familia hiyo,kwa bahati mbaya wazazi wake walifariki akiwa na umri mdogo sana,baba yake alifariki akiwa na umri wa mwaka mmoja na mama yake Mamu akafariki,Mamu akiwa na umri wa miaka minne.

Mamu hakuwa na mtu mwengine wa kumlea zaidi ya bibi yake aliyekuwa akiishi kijijini,aliishi katika kijiji cha Nyamurunge mkoani tabora,kijiji kilichokuwa na hali ngumu ya kiuchumi.
Baada ya kumalizika harakati za mazishi ya mama yake Mamu,Mamu alichukuliwa na bibi yake kwa ajili ya kumlea,Mamu akaanza maisha mapya nyumbani kwa bibi yake.

Bibi yake Mamu alimpenda sana mjukuu wake,maana hakuwa na mjukuu mwengine zaidi ya Mamu,na pia alivutiwa na uzuri wa tabia ya Mamu,si hilo tu bali uwerevu wa Mamu pia ulimvutia,kwani Mamu alikuwa ni binti mwerevu. Kila alipofundishwa alifundishika na kila alichoelekezwa alielekezeka.

Maisha ya bibi yake Mamu yalikuwa ni magumu sana,alitegemea kilimo cha mkono,na mvua ya muumba,ukubwa wa umri wake ulichangia ugumu wa maisha yake kwa kiasi kikubwa. Rasili mali pekee aliyoona ampe mjukuu wake ni kumfunza kilimo,akiamini kuwa kilimo ndio kitakacho muwezesha kupambana na ugumu wa maisha.

Hakuwahi kufikiria suala la kumpeleka mjukuu wake shule,hata pale Mamu alipofikia umri wa kwenda shule. Na hata Mamu mwenyewe hakuwahi kufikiria suala la yeye kwenda shule.
Hata ile siku alipomuuliza bibi yake baada ya kuwaona watoto wenzake wakienda shule, bibi yake alimjibu hivi,
"Mjukuu wangu kipenzi,kwa sasa hivi mimi sina uwezo wa kukupeleka shule,hata hivo hakuna kitu cha maana utakachokipata huko shule,zaidi ya kupoteza muda,"
"Mbona nawasikiaga wakisema kuwa,ELIMU NI UFUNGUO WA MAISHA?"
"Mmh,mjukuu wangu,labda huo ufunguo huwa unatumikaga kufungia maisha,na si kufungua maisha,maana hao wanaoenda shule hatuoni cha maana wanachokipata",
Mamu alimsikiliza bibi yake kwa makini,
bibi akaendelea,
"wakati wenzako wakienda shule, wewe unalima mbogamboga na vitu vengine,baada ya muda unavuna na kuuza na kupata pesa,ambazo zinakusaidia kwa mahitaji mbalimbali",
"Kwani bibi, wao wakiendaga huko shule huwa hawapati pesa?"
"Subutu!!,labda wao ndio hutoa pesa",
"Bibi,huwa nawasikiaga wanasema,mtu akimaliza shule anapata kazi na analipwa mshahara kila mwezi",
"Hakuna kitu kama hicho mjukuu wangu,nani umemuona kamaliza shule akapata kazi?,wanahangaika hangaika tu huko mitaani,mtoto wa mama Angela,si kamaliza shule mwaka jana,kazi gani anafanya? zaidi ya kuwa hata kazi za shambani haziwezi?"
"Ni kweli bibi,tukiendaga nae shamba hata kulima hawezi, analima vibayavibaya."
"Sasa na wewe unataka kuwa kama yeye"
"Hapana bibi"
"Sasa hao wanaoenda shule,waache waende shule,wewe endelea kujifunza kulima,ukifika umri wa kumaliza shule,utakuwa mkulima hodari,utapata maendeleo mazuri."
Maongezi ya Mamu na bibi yake yalikomea hapo,Mamu aliamini sana mawazo ya bibi yake,aliendelea kujifunza kulima kwa juhudi zote,hakujua kusoma wala kuandika,wala hakuona madhara ya hilo,kikubwa alichokiweza ni kurudisha chenji halisi katika biashara zake za mbogamboga,kwa hilo alikuwa mahiri. Haikuwahi kutokea akaongeza au kupunguza chenji.
********************
Mamu aliendelea kuishi na bibi yake katika maisha hayo ya tabu kwa muda wa takriban miaka kumi,yalikuwa ni maisha ya tabu,lakini yalimkomaza Mamu kiasi cha kuwa na uwezo wa kutatua mambo kama mtu mzima.

Baada ya miaka kumi, bibi yake Mamu alianza kuumwa na hatimae akafariki,
"KAZI YA MUNGU HAINA MAKOSA"
yalikuwa ni maneno ya kumfariji Mamu yaliyosemwa na baadhi ya majirani. Ulikuwa ni msiba wa kuhuzunisha sana kwa Mamu,si tu kwa sababu ya kufiwa na bibi yake,bali bibi yake kwake alikuwa zaidi ya bibi,ni kama baba na mama yake. Hatimae Mamu akamzika bibi yake.



***SEHEMU YA PILI***

Mamu alijitahidi kuondoa mawazo juu ya bibi yake baada ya msiba ule lakini alishindwa,alijikuta akilia kila wakati,kila kitu cha pale nyumbani kilimkumbusha kipindi cha uhai wa marehemu bibi yake.

Alishindwa kuendelea na kilimo akiwa peke yake kutokana na udogo wake,na alishindwa kushinda nyumbani kwa sababu palikuwa panamuongezea huzuni.

Kila alipokiona chumba na kitanda cha bibi yake vilikuwa vinaurudisha msiba upya moyoni mwa Mamu.

Mamu akalazimika kuwa anatoka nyumbani nyakati za asubuhi,na kuzunguka zunguka bila ya mpangilio maalumu,au wakati mwengine alienda nyumba ya jirani yao aliyeitwa mama Angela,na kumsaidia kazi ndogondogo, na Jioni kurudi nyumbani.

Alifanya hivo ili kupunguza mawazo,lakini ilikuwa ni kama anatwanga maji kwenye kinu,kila aliporudi nyumbani nyakati za usiku alijikuta akilia mpaka akipitiwa na usingizi bila ya kujitambua.

Ikawa ndio ada yake,mchana kuzunguka na usiku kulia,kitu kilichopelekea mwili wake kuanza kupungua. Hakiba ndogo ya pesa na chakula alichoachiwa na marehemu bibi yake vilikuwa vinakaribia kuisha.

*******************

"Nitaishi hivi mpaka lini?"
Siku moja Mamu aliwaza baada ya kuamka kutoka usingizini. Aliinuka na kwenda kuangalia hakiba yake ya chakula akaiyona ni ndogo sana,kama angeibana sana isingezidi siku tano.
"Kila kukicha hapa nyumbani pananiongezea simanzi,chakula ndio kinaishia na pesa ndio inaishia,"Mamu aliwaza.
"Nikiendelea kukaa hapa sitaweza kufanya chochote cha maana,sitaweza kuendelea kulima maana msiba wa bibi unajirudiarudia kichwani kila kukicha,"
Mamu aliendelea kuwaza lakini alikuwa na kipindi kigumu cha kuamua nini cha kufanya. Pamoja na umri wa miaka kumi na nne aliokuwa nao, alikuwa na uwezo wa kufikiri kama mtu mzima tena aliyekomaa kimaisha,hii ni kutokana na kukomazwa na bibi yake kimaisha akiwa bado ni binti mdogo.

"Ni lazima nifanye jambo,itanibidi nihame hapa,siwezi kuendelea kukaa tena hapa",
Mamu aliwaza,kwa kupata wazo hilo alijikuta kana kwamba amepata suluhisho la tatizo lake. Lakini swali la msingi likazuka,"nikihama hapa nitahamia wapi?".

Lilikuwa ni swali gumu mno kwa Mamu,kwani hakukuwa na ndugu yake mwengine anemjua aliyebakia katika dunia hii. Aliendelea kutafakari kwa muda,mara akakumbuka kitu.

Akakumbuka kuwa, siku moja bibi yake aliwahi kumwambia kuwa alizaa watoto wawili,mmoja wa kiume na mwengine ni wa kike. Mtoto wa kiume ndie baba yake Mamu,na mtoto wa kike ni mdogo wake ambae ni shangazi yake Mamu.

Mamu alijikuta akichangamka ghafla baada ya kukumbuka kuwa alikuwa na ndugu aliyekuwa hai katika hii dunia ambae ni shangazi yake. Mamu alipata nguvu ya kupika na kufua nguo zake kwa kipande kidogo cha sabuni kilichobakia. Baada ya kumaliza kufua akala,kisha akaamua kupumzika huku akiendelea kutafakari kuhusu shangazi yake.

Swali la kwanza alilojiuliza ni kuwa atawezaje kumpata shangazi yake,maana hakujua ni wapi anapoishi,na hata angejua anapoishi, angempataje maana hajawahi kumuona hata kwa mara moja na wala hamjui hata jina lake.

Alijikuta akipata kibarua kipya cha kufikiria namna ya kumpata shangazi yake huyo asiemjua kwa sura wala kwa jina. Alitafakari kwa muda mrefu akitarajia labda anaweza kupata angalau mwanga wa ufumbuzi lakini hakufanikiwa,alijikuta akipitiwa na usingizi bila ya kutarajia.

Aliposhtuka ilikuwa ni nyakati za usiku sana,akaamka, akaenda chooni kujisaidia na kisha kurudi kitandani ambapo alikaa kitandani kwa muda mrefu akitafakari mpaka mwanga wa jua la asubuhi ukaanza kuonekana.

Alihisi njaa sana wakati ule wa asubuhi,aliinuka na kupiga mswaki kisha akakiendea kiporo chake cha ugali na kachumbri ya jana ya nyanya tupu na akaanza kukishambulia. Alipomaliza alimshukuru Muumba kwa riziki ile, kama alivofundishwa na marehemu bibi yake.

Ulikuwa ni mlo aliouzoea katika maisha yake, tangu kipindi cha uhai wa marehemu bibi yake,baada ya kushiba alijikuta kichwa chake kikichangamka kidogo. Baada ya kutafakari kwa muda kidogo akakumbuka kitu. Kuna siku bibi yake alimwambia ,
"Shangazi yako anakusalimia",Mamu akamuuliza bibi yake,
"Umeonana nae wapi?"
Bibi akamjibu
"Hapana mjukuu wangu sijakutana nae,nimewasiliana nae,huwa nawasiliana na shangazi yako japo mara mojamoja sana".
Mamu alipoyakumbuka maongezi hayo yaliyojiri baina yake na bibi yake alijikuta anaanza kupata wepesi wa jambo lake.

Pamoja na kuyakumbuka maongezi hayo,alibakiwa na kitendawili kigumu alichoshindwa kukitegua ambacho ni,"njia gani bibi aliitumia kuwasiliana na shangazi?",alijaribu kurudisha kumbukumbu zake kwenye maongezi aliyoyakumbuka muda mchache uliopita pengine bibi yake aliwahi kumuambia njia ya mawasiliano aliyokuwa akitumia,lakini hakuambulia kitu. Alijaribu kuifikiria njia ya simu,lakini akaona haiwezekani. Hiyo ni kwa sababu kijiji kizima simu iliyokuwapo ilikuwa ni moja tu,na mtu aliyekuwa nayo alikuwa ni mwalim mkuu wa shule ya msingi.

Mwalimu huyo alikuwa ni mtu mwenye roho mbaya sana,na ikitokea akakupa simu yake, jiandae kudhalilishwa vilivyo.Mamu alikumbuka vizuri kuwa bibi yake hakuwa tayari kudhalilishwa na mtu yoyote kutokana na umaskini wake.

" hata siku moja sitoenda kuomba simu,sipo tayari kudhalilishwa na kijana mdogo kama yule,hata hivo sina mtu wa kumpigia simu"
Mamu aliyakumbuka vizuri maneno hayo ya bibi yake,akajikuta anazidi kupata mkanganyiko,
"kama bibi hakuwa akitumia simu kuwasiliana na shangazi,ni njia gani nyengine aliyokuwa akitumia?au alinidanganya".

Mamu alijiona mjinga sana kwa kutomuuliza bibi yake njia aliyokuwa akitumia kuwasiliana na shangazi yake,lakini angewezaje kumuuliza kipindi kile wakati bado alikuwa mdogo,hata hayo mawasiliano hakuyajua vizuri kipindi hicho kuwa ni kitu gani?.
Mamu alijikuta yupo kipindi kigumu mno,kila anapopata mwanga kinafuatia kiza kizito mno kuliko hata kiza kilichotangulia.

Alijikuta akianza kujuta kumkumbuka shangazi yake,hakuona faraja aliyoitarajia zaidi ya msongo wa mawazo kuongezeka.

Ghafla aliona machozi yakimtoka, hakujua ni machozi ya hasira au ya huzuni au mchanganyiko wa hasira na huzuni. Machozi yalifuatiwa na kilio cha kwikwi,alilia kwa muda mrefu mpaka akahisi kichwa kinamuuma. Aliendelea kulia kwa muda mrefu mpaka alipitiwa na usingizi.

Alipoamka ilikuwa ni Jioni,akainuka kutoka kitandani na kuamua kutoka nje ya nyumba ili angalau apate jua la Jioni. Akaamua kukaa nje kwenye kigogo cha mti ambacho alikitumia kukaa wakati akiosha vyombo tangu enzi za uhai wa marehemu bibi yake.

Alipokaa pale kwenye kigogo mara akakumbuka kitu,akakumbuka tukio lililotokea miaka kadhaa iliyopita,lilikuwa ni tukio muhimu sana kwake kwa kipindi kile,tukio lenyewe lilikuwa hivi,

Siku moja Mamu alikuwa nje anawasha moto nyakati za Jioni kwa ajili ya chakula cha usiku baada ya kutoka shamba. Mara akatokea kijana wa makamo,
"Bibi yako yupo?",yule kijana aliuliza,
"ndio yupo",Mamu alijibu,"mwambie anaitwa na mwenyekiti nyumbani kwake",yule kijana akaagiza.

Mamu akaingia ndani haraka na kumpa bibi yake ujumbe wa wito aliopewa na yule kijana. Bibi yake akamuuliza,"huyo kijana yuko wapi?",
"Nimemuacha hapo nje",Mamu akajibu. Bibi akatoka haraka kumuwahi yule kijana,alipofika nje akamuona yule kijana akimsubiri,
"Wewe mtoto,ni kweli umetumwa na mwenyekiti uje uniite?",bibi alimuuliza yule kijana,
"Ndio",yule kijana alijibu kwa mkato.

Bibi akamgeukia Mamu akamwambia,
"nawa mikono yako haraka tuondoke",
"Kwani bibi kuna nini?"
"Itakuwa ni shangazi yako tu"
"Shangazi amekuja?"
"Fanya haraka twende,utaona huko huko". Mamu na bibi yake wakaondoka haraka wakaelekea nyumbani kwa mwenyekiti.

Walipofika wakakaribishwa vizuri na mke wa mwenyekiti. Mara akaingia mwanaume mmoja ambae ni mtu mzima wa makamo asiyekuwa mzee.
Yule bwana akamsalimia bibi yake Mamu,"Shikamoo mama","Marahaba mwanangu,nimesikia unaniita, nimekuja kuitikia wito".

Mwenyekiti na bibi yake Mamu wakaanza mazungumzo. Kipindi chote cha mazungumzo Mamu alikuwa akipepesa macho huku na huko,hakuwa makini na chochote kilichokuwa kikiendelea pale.

Kikubwa alichotarajia ni kuwa baada maongezi yale atatokea shangazi yake ili wamchukuwe waondoke nae nyumbani kwao. Alikuwa na hamu sana ya kuonana na shangazi yake,hasa pale alipokumbuka kuwa bibi yake aliwahi kumwambia kuwa shangazi yake amefanana sana na kaka yake yaani baba yake Mamu,na pia aliwahi kuambiwa kuwa yeye Mamu amefanana na baba yake. Kwa hiyo alijua fika kuwa yeye amefanana na shangazi yake.

"Twende Mamu",bibi yake Mamu alimwambia mjukuu wake baada ya kumaliza maongezi yake na mwenyekiti.
" Bibi,shangazi yuko wapi? mbona hatujamchukua?" Mamu alimuuliza bibi yake,
bibi akamjibu
"Mamu,shangazi yako hajaja",
Mamu akauliza,
"kwani bibi tulienda kule kufanya nini?"
" shangazi yako alikuwa ametuma barua"
"Barua ndio nini bibi?"
"Barua ni maadishi, yanaandikwa kwenye karatasi kisha yanatumwa kwa yule anaetumiwa barua"
"Inatumwaje?"
"Kama sehemu kuna sanduku la barua,wanatuma kupitia sanduku la barua. Kama hapa kwetu hakuna sanduku la barua kwa hiyo huwa zinatumwa kwa njia ya treni, mwenyekiti anapoenda stesheni iliyopo hapo kijiji cha jirani huzichukua na kuja kumpa kila mtu barua yake. Lakini kwa wale wasioweza kusoma kama mimi huwa wanaitwa nyumbani kwa mwenyekiti,na mwenyekiti huwasomea barua zao. Kama mtu hahitaji kuijibu barua yake anamshukuru mwenyekiti na kuondoka. Lakini kama mtu anahitaji kuijibu barua yake kama mimi leo anasema maneno anayotaka kutuma na mwenyekiti anamuandikia kwenye karatasi na kuituma kama barua"
Tukio hilo liliishia hapo.

Kumbukumbu ya tukio hilo iliamsha uchanagamfu mpya kwenye kichwa cha Mamu.
ITAENDELEA......


Riwaya hii itakuwa itakujia hapa jukwaani mara mbili kwa wiki,itakujia jumamosi saa 5:00 asubuhi(11:00 am) ,na jumapili saa 10:00 Jioni (04:00 pm).
 
****SEHEMU YA TATU****

Mamu baada ya kulikumbuka tukio lile ambalo lilipita kichwani mwake kama mkanda wa video,alijikuta amekuwa mwepesi sana.
" itabidi niwasiliane na shangazi kama bibi alivokuwa akiwasiliana na shangazi,kwanza nimpe taarifa ya msiba wa bibi,maana hakuna mtu wa kumpa taarifa zaidi yangu,pili nimwambie aje anichukuwe"
Mamu aliwaza.

Mamu aliinuka taratibu kwenye kile kigogo alichokuwa amekalia na kuingia ndani. Alijitupa kwenye kitanda na kupitiwa na usingizi.

Kulipokucha asubuhi aliamka mapema sana. Akasafisha na akafagiafagia pale nyumbani na baada ya kumaliza usafi wa pale nyumbani alienda kwa mwenyekiti.
"Shangazi yako anaitwa moza na anakaa Dar es salaam",hayo yalikuwa ni baadhi ya maneno ya mwenyekiti ambayo alimwambia Mamu

****************
Mamu alifanikiwa kumuandikia barua shangazi yake kwa msaada wa mwenyekiti, na hatimae barua ikatumwa.

***************

Jijini Dar es salaam,
Mama mmoja mnene wa wastani alikuwa chumbani kwake amekaa kwenye kigoda chake akisonga ugali kwa ajili ya chakula cha mchana.
"Hodi"
Mlango wa chumba cha mama huyo uligongwa,
"Nani?",aliuliza
"Mimi Tina" mgongaji alijibu,
"Karibu,ingia tu mlango uko wazi"akamkaribisha,na yule mgongaji akaingia.
"Vipi hali dada moza", yule mgeni alimuuliza hali mwenyeji wake,
"Nzuri tu mdogo wangu,za huko shule",
"Tabu tupu,lakini tushazizoea,tutazivumilia tu",
"Sasa wewe muajiriwa ukilalamika sisi tusemeje?"
"Hapana dada,hiyo kazi tunafanya tu kwa sababu hatuna nyengine,kwanza mitoto yenyewe haifundishiki,haielewi,mibichwa migumu utadhani ina mawe kichwani,halafu mishahara wanatucheleweshea kweli",
"Mmh,haya mwaya,tuyaache hayo ya shule,naona umekuja kunitembelea,au ndio umeniletea nauli?"
"Hapana dada,wanatuzingua kweli na hiyo mishahara,lakini kama nilivokuahidi dada yangu,nikipokea tu mshahara,breki ya kwanza ni hapa kwako","yaani nitakushukuru sana mdogo wangu,maana nilivokuwa na hamu ya kumuona mama yangu siwezi hata kusimulia"
"Kwani dada una muda gani tangu utoke tabora?"
"Mmh,mdogo wangu,inafika miaka kumi na tano"
"Mmh,pole sana dada,nitajitahidi nikupe nauli ya kwenda na kurudi"
"Yaani,nitakushukuruje!"
"Kwani wamesema wanatoa lini hiyo mishahara?"
"Ilikuwa watupe leo,lakini mhasibu amesafiri,anarudi leo Jioni,kwa hiyo kesho ni uhakika dadaangu,na vile keshokutwa ni ratiba ya treni,ikiwezekana kesho hiyo hiyo ukakate tiketi"
"Yaani,furaha yangu sijui niielezeje,tena usiku huu huu nitaanza kupanga nguo",
"Hilo la kwanza dada"
"Lapili ni lipi?"
"Kuna barua yako,nahisi bimkubwa wako atakuwa amekukumbuka",
"Mmh,mbona leo nitaota,maana mama huwa hana kawaida ya kuanza kunitumia barua,mpaka mimi nimuanze ndio anajibu,au kaniota kwa sababu nataka kwenda kumtembelea?",
"Labda kuna tatizo dada",
"Mmh,huenda kukawa na tatizo na pia inaweza ikawa ni salamu tu,maana ni siku nyingi mno sijamsalimu,tena imekuwa vizuri,nitamfanyia suprise,yeye katuma barua mimi naenda mwenyewe",
"Haya dada,barua yako hii hapa",
"Haya Asante",
"Sasa dada, mimi acha nikukimbie",
"Wewe nawe,haraka zote za nini,subiri basi angalau ule kidogo",
"Haya dada,maana wewe ukimng'an'gania mtu ale hawezi kuchomoka"
"Subiri kidogo tu mdogo wangu,mboga inaiva sasa hivi,mimi acha nianzage kusoma hii barua maana mama yangu nimemmisi sana,nina hamuje nae?"

Moza akaanza kuifungua barua,na kuanza kuisoma. Mara Tina akamuona dada yake wa hiyari Moza akitoa macho, mara akaanza kutokwa na mchozi,Tina akaanza kumshangaa dada yake,lakini ghafla akaanza kumuona mikono ikilegea barua ikadondoka chini na yeye akaanza taratibu kwenda chini akapoteza fahamu. Tina akawahi kumdaka dada yake yule wa hiyari na kumuweka chini taratibu,asijue ni nini kilichomsibu.

Kwa haraka haraka akampigia simu dereva texi aliyemzoeya kumtumia,akamuelekeza wapi aje, na baada ya hapo akaepua chungu kilichokuwa jikoni ambacho hata hivo kilishawiva, kisha akamuweka vizuri dada yake. Mara akasikia honi ya gari ikilia kutoka nje ya nyumba ile ikiashiria kuwa dereva texi alishafika,kwani hakuwa mbali na pale alipokuwa Tina.

Tina aliinuka na kutoka nje,alipofika nje alimkuta dereva texi akiifuta texi yake vumbi kwa kitambaa. Tina akamwita dereva texi kwa kutumia ishara. Dereva texi akaja, Tina akamwambia asogeze texi yake mlangoni na dereva texi akafanya kama alivoambiwa.

Baada ya hapo, Tina akamuonesha ishara dereva texi ya kuwa amfuate ndani, dereva texi akamfuata Tina. Wote wakaingia mule chumbani na kumkuta Moza akijigeuzageuza. Tina akamkimbilia haraka dada yake na kumuuliza anavojisikia, Moza hakujibu chochote zaidi ya kuendelea kujigeuza geuza. Tina akamwita dereva texi na kumuomba amsaidie kumbeba dada yake,wakambeba wakamtoa nje na kumuingiza kwenye texi.

Safari ya kuelekea hospitali ikaanza, walielekea hospitali ya private kwani ndio iliyokuwa karibu.

Walipofika hospitali Tina alimuangalia dada yake na kumkuta amepoteza tena fahamu. Walivyopaki gari,akatoka haraka haraka akaenda kuomba kitanda cha kubebea wagonjwa. Akakumbana na nesi njiani,wakapigana vipushi bila kukusudia kwani kila mmoja alikuwa na haraka zake, hakuna aliyekuwa makini na njia.

Tina na nesi waliangaliana kwa hasira kama majogoo wawili wanaotaka kupigana. Kila mmoja alikuwa ni kama anajiangalia kwenye kioo. Ghafla nyuso zile mbili zilizokuwa zikiangaliana kwa ghadhabu zilianza kubadilika na kuzaliwa tabasamu la ajabu,tabasamu lenye huzuni ndani yake,mara wote wawili wakaanza kulengwa na machozi.

****************
Ghafla Tina na nesi walirukiana kwa haraka ya ajabu na kukumbatiana huku kila mmoja akishindana na mwenziwe kutoa machozi mengi,lakini kama yalikuwa ni mashindano Tina alikuwa mshindi.

Kwa kweli walilowanishana nguo zao kwa machozi yale,walikuwa wamekumbuka miaka mingi iliyopita. Walikuwa ni mapacha waliopotezana miaka mingi sana,mmoja aliitwa Tina na mwengine aliitwa Tunu. Tina alitangulia kuzaliwa kwa robo saa kabla ya Tunu.

Walikuwa wakipendana mno walipokuwa wadogo, kiasi cha kugawana hata bakora za kuchapwa pindi mmoja alipofanya kosa walipokuwa wadogo. Walitengana kwa kutengana na wazazi wao. Tina alichukuliwa na baba yake na Tunu akachukuliwa na mama yake.

*******************

Watu walioona tukio lile la Tina na nesi(Tunu) tangu mwanzo walipopigana vikumbo walibakiwa na mshangao,wale waliokuwa mbali kidogo walifikiri Tina na nesi wamekabana kutokana na hasira za kupigana vipushi. Lakini walishangazwa na mkabano ule usio na kurupushani yoyote.

Wale watu waliokuwa karibuni yao walishangazwa na mabinti wale wazuri waliofanana kila kitu, tofauti yao ilikuwa ni moja tu,ni mavazi waliovaa mmoja alivaa nguo za uuguzi huku mwengine akivaa nguo za nyumbani.

Tina na Tunu walikumbatiana kwa muda mrefu kidogo huku kila mmoja akisahau alikokuwa anaelekea.

"Nilijua umeshakufa dadaangu" Tunu alianza kutoa ukimya huku aliendelea kutoka machozi. Ilikuwa ni kawaida ya Tunu kumwita Tina 'dada' japo wamepishana robo saa.
" Hapana mdogo wangu Mungu ni mwema,japo niliponea kwenye tundu ya sindano",Tina alijibu.

Waliachiana wakangaliana kwa sekunde kadhaa,
"Umefikajefikaje huku?"
Tunu alimuuliza Tina.
Nae Tina akajibu
"Ni stori ndefu Tunu,tutaongea muda mwengine. Nimekuja hapa hospitali kwa matatizo, nashukuru sana kukukuta hapa naomba msaada wako Tunu"
"Matatizo gani hayo tena Tina?"
"Dadaangu Tunu,dadaangu kapoteza fahamu"
"Dadaako gani tena huyo Tina?"
"Dadaangu wa hiyari,dadaangu aliyenilea tangu nifike hapa Dar,dadaangu aliyenilea mpaka leo nimekuwa mtu Tina mie,ni stori ndefu sana Tunu,kwanza tuangalie uzima wake, mengine yatafuata baadae".

"Yuko wapi huyo mgonjwa mwenyewe,mbona uko peke yako?"
"Nimekwambia kapoteza fahamu ,kwa hiyo nilikuwa nimekuja kuomba kusaidiwa kitanda cha kubebea wagonjwa,mgonjwa nimemuacha kwenye texi pale nje ya geti"

"Wewe nenda hapo nje ya geti,mimi naenda kuchukua kitanda"

Baada ya maongezi hayo Tina na Tunu wakaachana,Tina akarudi alikoiacha texi na Tunu alienda kufuata kitanda cha wagonjwa. Tina alivofika kwenye texi haikuchukua muda na Tunu nae akawa amefika na kitanda cha kubebea wagonjwa.

Tina na Tunu wakishirikiana na dereva texi, walimbeba na kumtoa Moza kwenye texi na kumuweka juu ya kitanda kile cha wagonjwa. Tunu akakiburuza taratibu kile kitanda akielekea ndani ya hospitali ile wakati Tina akimlipa dereva texi na kuagana nae.

Baada ya kuingia hospitali,Tunu alimpeleka moja kwa moja mgonjwa yule wodini na kumtoa kwenye kitanda cha matairi na kumuweka kwenye kitanda cha kawaida
ITAENDELEA............
 
****SEHEMU YA NNE****

MIAKA 10 ILIYOPITA.

Moza alikuwa ameamka mapema sana kama kawaida yake, kwa lengo la kwenda kufungua biashara yake ya siku zote,biashara ya mama ntilie.

Alipofika kwenye banda lake akashangaa kumuona mtu amelala kichakani pembeni kidogo ya banda lake,haikuwa jambo la kawaida.

Moza alikaribia ili amuone vizuri, kwani bado kulikuwa hakujakucha vizuri. Alipigwa na yowe la ghafla baada ya kukuta mwili wa msichana mzuri ukiwa inavuja damu, alishindwa kujua kuwa alikuwa hai msichana yule au amefariki.

Alimsogelea karibu zaidi akagundua kuwa anavuja damu sehemu za siri,nguo zake zilikuwa chafu mno. Aligwaya kidogo asijue cha kufanya, akili ilimruka kwa dakika kadhaa,iliporudi alishapata maamuzi ya kufanya.

Cha kwanza alichofanya alikwenda kwenye kifua cha yule binti na kupima mapigo ya moyo. Aliyahisi mapigo ya moyo yakipiga kwa mbali sana.

" bado yupo hai huyu",Moza alijisemea kimoyomoyo. Hakutaka kuchelewesha muda alimbeba begani kama wanavobebwa watoto wadogo,kwani binti yule alikuwa amekonda sana na kwa hiyo alikuwa ni mwepesi kumbeba.

Alimbeba na kumfunika tenge mwili mzima ili asionekane,alimuekea kanga na kumshika vizuri ili damu isichuruzike chini,hakuwa mbali sana na hospital,ni kama mwendo wa robo saa. Kutokana na ukakamavu wake alijikaza,akambeba binti yule mpaka hospitali.

Bahati nzuri alipofika tu hospitali alikutana na mtu aliyetamani sana kukutana nae,alikuwa ni daktari kijana aliyezoea kula chakula kwenye banda la mama ntilie la Moza.

"Za asubuhi dada,vipi salama?" Yule dokta aliuliza,
" si salama docta,naomba msaada wako wa haraka sana"
" nini tatizo?"
"Nimeleta mgonjwa huyu hapa niliyembeba".
"Nifuate"
Dokta akamuingiza wodi ndogo na kumuonesha Moza kitanda cha kumuweka mgonjwa wake.

Moza akamshusha yule mgonjwa na kumuweka juu ya kitanda, dokta akashikwa na mshangao wa ghafla baada ya kumuona Moza amerowa damu kwenye dera lake.
"Huyu ni nani yako? Halafu amepatwa na nini?mbona nguo zake chafu mno?mbona anavuja damu?" Dokta alijikuta akiuliza maswali mfululizo bila kukusudia.

"Huyu ni mdogo wangu,naomba kwanza mshughulikie, hayo maswali mengine nitakujibu baadae"
Docta hakutaka maongezi zaidi, kwanza alimpima mapigo ya moyo. Alipoona bado yupo hai akamtundikia dripu ya glucose na kisha akamchoma sindano kwa ajili ya kuzuiya damu kuendelea kutoka,na mwisho akamchoma sindano ya kupunguza maumivu. Akamuangalia damu yake na kukuta imepungua.

"Inabidi aongezewe damu"
Docta akamwambia Moza
"Aongezewe damu kiasi gani?"Moza akauliza.
Dokta akamjibu akamwambia
"Chupa moja tu itatosha"
"Basi nitoeni mimi hiyo damu ,nina group O ,cha muhimu tu ni kupima usalama wa damu yangu japo mimi mwenyewe nina uhakika kuwa damu yangu ipo salama". Docta akacheka kidogo kisha akasema,
"Ngoja niongee na wahusika wenzangu,wewe nenda pale kafungue file la mgonjwa,kisha nitakuita"
" Sawa docta,lakini ujue wewe ndio ninaekuamini, hao wengine mimi siwajui"
"Usihofu dadaangu"

Baada ya muda mfupi Moza aliitwa na dokta,akaenda nae kupima damu na damu yake ikaonekana inamfaa mgonjwa. Moza akatolewa damu na damu akawekewa mgonjwa.

********************

Yule mgonjwa alipoteza fahamu kwa muda wa wiki mbili. Kipindi chote hicho Moza alifunga biashara yake kwa muda,kwa ajili ya kumuuguza mschana yule asiyemjua hata kwa jina,kikubwa kilichomsukuma kufanya vile ni moyo wa ubinaadamu aliokuwa nao. Hakiba yake ndogo ya pesa iliishia kumuuguzia mgonjwa,hata hivo hakuwa na wasiwasi sana,alijuwa mgonjwa akipona ataendelea na biashara yake ya mama ntilie amabayo ndio inayomuweka mjini.

Baada ya wiki hizo mbili yule mgonjwa alizinduka.
"Mdogo wako ameamka",dokta alimwambia Moza aliyekuwa amejiinamia kwenye benchi.
" kweli dokta au unanitania",Moza aliuliza.
"Ni kweli, siwezi kukutania katika jambo zito kama hili"

Moza aliinuka kwa furaha mno kwenye benchi na kuingia wodini. Alinyoosha moja kwa moja mpaka kwenye kitanda cha mgonjwa wake huku dokta akiwa nyuma yake. Alipofika alimkuta mgonjwa wake akiwa amekaa kitako anashangaashangaa.

"Hujambo mdogo wangu?",Moza alimuuliza yule mgonjwa huku akimwita 'mdogo wangu' ili ampoteze maboya yule dokta. Yule mgonjwa hakung'amua hilo, lakini aliitikia bila tabu kwa kuona wazi kuwa yule anaemuuliza ni mkubwa kwake kiumri.

Kisha Moza akamgeukia dokta akamwambia," sasa dokta niache niongee kidogo na mdogo wangu"
Dokta akajibu ,"Sawa lakini haturuhusu maongezi marefu kutokana na hali ya mgonjwa, bado anahitaji mapumziko",Moza akajibu
"Sawa dokta nimekuelewa",
Dokta nae akaingiza maneno ya utani kidogo "hivi nimekuingiza huku kwa heshima yako tu,pengine utapata faraja kidogo urudi kazini maana tumeyamisi sana mapishi yako"
Wote wawili wakacheka na dokta akaondoka kuwapisha Moza na mgonjwa wake waongee kidogo.
Moza akamgeukia mgonjwa wake na kuanza kumwambia kwa sauti ya chini,
"Nisikilize mdogo wangu kwa makini sana,maana hakuna muda wa kutosha wa kuongea hapa,zaidi tutaongea tukitoka,ila cha msingi nilichokuwa nataka kukuambia ni kuwa mimi ndio niliyekuleta hapa hospitali,na nimekutaja kama mdogo wangu, kwa hiyo chochote utakachoulizwa waambie dadaangu ndio anajua zaidi,ukiulizwa dada yako anaitwa nani sema Moza,na wewe nimekuandikisha kwa jina la mwajuma Athumani,umenielewa?"
Yule binti akajibu kwa kutikisa kichwa kuwa ameelewa.

Baada ya Moza kumaliza kumwambia mgonjwa wake yale maneno alianza kumuuliza hali ya maendeleo yake,
"Naendelea vizuri ila tu nahisi kichwa ni kizito sana"
ITAENDELEA................
 
SEHEMU YA TANO
******""*************
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…