Riwaya: Doa

Riwaya: Doa

winston20

JF-Expert Member
Joined
Jun 21, 2020
Posts
1,116
Reaction score
2,319
RIWAYA; DOA
-----1-----

Ulikuwa ni muda sahihi kwa kila mmoja
kurejea nyumbani, muda ambao jua lilikuwa
limeanza kuiacha Mashariki yake na kwenda
kwa mchepuko wake bi. Magharibi. Harakati
za hapa na pale zilianza kufungwa, watu
walianza kujipa uchovu ili mradi tu, warejee
majumbani mwao kupambana na masimango
ya nyumba zao. Wale wenye gubu, ilikuwa ni
wakati wa majuto kwa panya na mbu ambao
huishia kuona na kusikia vibweka usiku kucha,
kiasi cha kuwanyima uhuru wa kubarizi
kwenye vyandarua na kuta za baridi.

Muda huu ni muda ambao huko mwituni,
wanyama wakali nao walikuwa wanafunga
hesabu za mawindo, huku wanyonge wa pori
wakipumua na kulishukuru jua kuzamia kwa
mchepuko wake, huku wakilaani ukali wa mke
halali mashariki; licha ya kuwapa kula,mwanga
na virutubisho, ila aliwachosha kwa kuwapa
adhabu ya hekaheka za kunusuru uhai wao.
Lakini licha ya kushukuru huko, wapo
wanyama ambao muda huo kwao, ndio muda
sahihi wa kuingia mawindoni, kuvizia na
kujipatia shibe.
Hali hii ilikuwa ni furaha kwa bwana jua,
ambae alifurahi kuona kwake na, mchepuko
wake kunafaidisha viumbe wa Mungu kwa
namna tofauti, hivyo kufanya iwe ni ratiba
yake ya kila siku na wakati wote.

Wakati jua anazidi kujichimbia nyumba
ndogo, Duniani kulikuwa na mambo mengi
yanatokea, usiku huu wa rasharasha, usiku
ambao haujaenda eda, kulikuwa na
mwanamichezo mmoja, akijaribu kumalizia
muda wake wa mazoezi ndani kwake.
Hakuonekana kuwa na wasiwasi hata kidogo,
alipiga balizi, kisha akapiga miinuko kadhaa,
alojinyoosha na kujipinda kwa utalaamu, huku
akiacha viungo vyake vikubali kwa kutoa sauti
ya mvunjiko.

Mwanamichezo huyu, alikuwa ni kocha wa
timu ya vijana ya Azan, timu ambayo ilikuwa
inafanya vyema chini ya mkufunzi huyo raia
wa Burundi. Makazi yake yalikuwa Sinza.
Alikuwa akiishi kwenye nyumba ya waajiri
wake ambao walikuwa ni kampuni ya Azan.
Ilikuwa nyumba nzuri yenye hadhi yake,
nyumba iliozungushiwa ukuta mrefu na juu
yake kukapita nyaya za umeme.

Kocha huyu licha ya kuishi nyumba nzuri na
kubwa, lakini hakuwahi kuwa na mke wala
mtoto na, hakuna aliewahi kujua kuhusu
familia yake.

Aliishi peke yake.

Aliendelea na mazoezi yake, lakini kwenye
ukuta wake wenye nyaya za umeme, kulikuwa
na kiumbe mwenye moyo wa nyama na miguu
miwili yenye vidole vitano. Mtu yule alikuwa
anamalizia kuhifadhi mkasi mdogo aliotumia
kukata nyaya zile na sasa alikuwa amesimama
wima akitizama upande wa mlango wa
nyumba ile.

Mtu yule alikuwa amevaa mavazi meusi,
kuanzia juu hadi chini kwenye raba zake.
Alipokwisha kuhakikisha hakuna anaemuona
pale ukutani, aliruka sarakasi moja kavu na
kutua chini bila kutoa ukelele, kisha alipiga
hatua fupi fupi kama vile alitarajia kuona
jambo uani pale. Mtu yule hakunyoosha
upande wa mlango uliokuwa wazi, bali alipita
upande wa nyuma wa nyumba ile, kisha
alitumia mlango wa jikoni kuingia ndani ya
nyumba ile.

Muda wote huo, kocha hakujua yanayojiri,
wala kuhisi kuna mtu wa ajabu atakuwa
kamtembelea ndani kwake. Aliendelea kupiga
zoezi jepesi, aliporidhika alielekea chumbani
kwake na alipotoka, alikuwa amevaa taulo tu
akielekea bafuni.

Wakati yeye akielekea bafuni,mgeni wake
yeye alielekea sebuleni,ambapo alichukua
simu iliokuwa mezani na kuipachika kwenye
chaji na kuwasha,kisha alikaa nyuma ya jokofu
kubwa na kutulia kimya.

Kwa nini alifanya vile, hakuna aliejua.

Kocha wa timu ya Azan alipotoka kuoga,
alipitiliza chumbani kwake, huko hakukaa sana
alirejea sebuleni, ambapo alianza kutafuta
kitu, mara akasita na kushangaa.

Hakuwa ameweka simu yake kwenye chaji,
alishangaa imejiweka vipi pale na yeye anajua
aliiacha mezani.

Ajabu hii!.
Aliifuata simu ile, nayo ikaanza kuita. Kocha
aliruka nyuma na kutoa macho kama teja
aliefumaniwa.

Aliiogopa simu yake mwenyewe.

Simu ile iliita na kukata.

Kocha bado alikuwa anajaribu kuweka
kumbukumbu zake sawa, hakuwa yeye
alieweka pale ile simu. Taratibu alianza
kuisogelea tena, mara ikaita tena.

Wakati huu aliamua kuipokea, ilikuwa simu ya
mmoja wa waajiri wake.

Kocha alikuwa katikati ya maongezi, hata
wakati mgeni wake alipotoka mafichoni, yeye
hakuwa na habari kabisa, aliendelea kupanga
mikakati ya timu yake kusafiri mkoani kwa ajili
ya mchezo wa kujipima nguvu na timu moja
maarufu.

Kocha alistuka akishikwa nyuma ya shingo na
mkono ambao ulikuwa umevaa glavu.
Alipojaribu kujitikisa, alipigwa teke la mgongo
na kumfanya abinukie mbele, na hilo likawa
kosa, mana mgeni alimbinua shingo na kukaa
kama mtoto analazimishiwa uji wa chumvi.

Kila alipojaribu kujitikisa, hakupata sehemu ya
kushika ili ajinasue na kabali ile matata.

Kocha alianza kuvuta pumzi kwa nguvu, hilo
ndilo lilitegemewa na mgeni, kwani alizidi
kumbinua kocha kwa kumwekea goti katikati
ya uti wa mgongo.

Kocha alishindwa kuhimili kabali ile ya aina
yake, aliaza kuishiwa pumzi huku macho yake
yakianza kuona kiza kizito, huku masikio yake
yakianza kusikia kelele za kuzomea za
mashabiki wa timu alizozifunga.

Dakika mbili badae, mgeni alikuwa anamlaza
chini taratibu, kisha alichukua simu na
kuirejesha tena kwenye chaji, kisha alimvuta
kocha hadi karibu na simu, kisha alimuinua na
kumshikisha simu ile na kuipachika sikioni.

Alipohakikisha maiti ya kocha imeshika vyema
simu ile, aliingia mfukoni mwake na kutoa kitu
kidogo mithili ya punje ya mtama na
kuipachika kwenye spika ya simu. Alipomaliza
alisogea pembeni kidogo na kubonyeza saa
yake, punde ukatokea mlipuko wa kiasi
kidogo, lakini ulikuwa ni mlipuko uliobomoa
kichwa cha kocha kuanzia upande wa kushoto
kwenda juu na kufanya awe kama papai
lilokatwa kipande.

Damu ilianza kutoka, na kusambaa hovyo pale
ndani. Mgeni muuaji alianza kuondoka ndani
ya nyumba ile, huku akiwa ameua bila kuacha
alama ya ushahidi na hiyo ilikuwa ni sheria
namba moja. Na kwa kifo cha kocha, maofisa
wangeishia kujua alilipukiwa na simu wakati
anaongea na simu ikiwa chaji. Muaji akiwa
mbali na hisia feki za maaskari.

Wakati muuaji anaondoka ndani ya nyumba
ya kocha, kulikuwa na mtu mwingine anaingia
pale, akiwa amevaa sawa na yule alietoka,
mtu huyu yeye alikuwa ni mfupi tofauti na
yule wa mwanzo. Aliingia ndani ya nyumba ile
kupitia dirishani,alipofika aliishia kukutana na
maiti ya kocha ikiwa na simu iliolipuka
pembeni yake.
Mtu yule alitoa simu janja yake na kupiga
picha moja, kisha alitoa kibahasha kidogo sana
na kukirusha chini ya uvungu.
Kibahasha kile kilikuwa kimeandikwa herufi
moja iliochanganywa na namba. Ilisomeka hivi
“F3”,Kisha aliondoka mle ndani kwa kupita
njia tofauti na alioingilia.

Nyumba ya kocha ilikuwa imetembelewa na
watu wawili, huku mmoja akiua na mwingine
akiacha ujumbe wenye maana aliojua yeye, na
dhahiri alieua hakujua kama ameonwa na mtu
alieacha ujumbe.

Lakini kwa nini huyu aue na huyu aache
ujumbe, kwanini?

Hakuna aliejua sababu zaidi ya wao wahusika
wenyewe.

Mtu wa pili kuingia nyumbani kwa kocha,
ambae ndie mtu wa mwisho kutoka nyumbani
kwa kocha, yeye aliamua kuendelea na ziara
yake jirani na maeneo yale. Kulikuwa na
nyumba moja ambayo alihitaji kuitembelea
usiku ule. Mtu huyu ni kama hakujali kabisa
kile alichokiona nyumbani kwa kocha.

Mtu huyu alipofika usawa wa nyumba
alioikusudia, aligeuka kushoto na kulia
kutazama kama kuna mtu yeyote aliekuwa
anamfuatilia. Alipohakikisha hakuna mtu,
alijongea taratibu na kuufikia ukuta,
aliutazama kwa sekunde kadhaa, kisha akatoa
glavu na kuzivaa. Alipomaliza alizijaribu kwa
kuushika ukuta, alipohakikisha zinafaa kwa
kazi alioikusudia, alianza kuukwea ukuta ule
huku akisaidiwa glavu zile maalumu kwa
kupandia kuta na miamba mirefu.

Tofauti ya ukuta huu na ule wa kocha, ukuta
huu ulikuwa unavipande vingi vya chupa kwa
juu, hivyo alipofika juu, alitulia kidogo na
kujivuta kwa kasi hadi alipotua chini na
kuachia ukelele mdogo usiostua. Alifanya vile
kukwepa kudhurika na chupa zile.

Alijinyanyua na kutembea bila wasiwasi,
macho yake yalikuwa sambamba na dirisha
moja alilokuwa amelikusudia kabla na baada
ya kuingia pale. Ni dhahiri aliijua nyumba ile.
Hakuhangaika na kukwepa taa zilizokuwa
zinawaka sebuleni, wala hakutaka kuhadaika
na kelele za watoto waliokuwa wakitizama
filamu za Tom na Jerry.

Yeye alikusudia kuingia bila kuwastua wale
watoto ama mtu yeyote aliekuwa pale
sebuleni.

Alipolifikia dirisha lile, alijaribu kusukuma kioo
lakini kilikuwa kimefungwa kwa ndani, haraka
alingiza mkono mfukoni mwake na kutoa
chuma kidogo chenye muundo wa bikari, kisha
alikapachika kwenye kioo na kuzungusha kwa
duara, aliporidhika alikirudisha mfukoni
mwake na kukivuta upande wake kipande cha
kioo alichokata. Alipokwishakitoa, aliingiza
mkono na kufyatua kabali ya kioo na
kukisukuma pembeni, kisha alipita na kuingia
ndani, ambapo alijikuta akitokea jikoni na ndio
ilikuwa kusudio lake.

Kutokea pale jikoni, kushoto kwake kulikuwa
na korido ambapo ukiifuata utatokea kwenye
chumba kikubwa cha mmiliki wa nyumba ile.
Mtu yule alitembea kwa hatua za kunyata na
kisha aliishia mlangoni mwa chumba
alichokikusudia.

Alitulia kidogo na kusikiliza, aligundua kuna
mtu ndani ya chumba kile, ni kama ambavyo
alikuwa anajua kuhusu ratiba ya pale ndani ya
mtu aliemfuata.

Aligonga kidogo na kutulia. Kukawa kimya.

Aligonga tena na mara hii kwa nguvu kidogo.

Mara ikasikika sauti ya mwanamke pale ndani,
ikimruhusu aingie.

Ni dhahiri mwenyeji wa chumba kile alijua ni
watoto au mfanyakazi ndie anaehitaji kuingia.

Mgongaji alitabasamu kiupande, kisha
aliusukuma mlango taratibu na kuingia ndani,
ambapo alikutana na mwanamke mwenye
umri wa kukadiria miaka sitini kasoro moja
hivi. Mwanamke yule alionekana mrembo
licha ya ngozi yake kuanza kupukutisha nyama
za urijali.

Mwanamama yule alitoa macho ya kuhoji,
huku akiwa ameshika taulo lake akishindwa
kumalizia kuusitiri utu wake.

“Wewe ni nani na umeingiaje hapa!” Mama
alihoji kwa kigugumizi cha woga.
Badala yake hakupata jibu, bali mtu yule
alikisogelea kitenza mbali na kuwasha radio na
kuweka sauti ya juu kidogo.

Mama yule dhahiri alijua mambo si mambo,
haraka aliachia taulo lake hadi chini na kubaki
mtupu, lakini hakujali,mikono yake yenye kasi
ilikuwa inaiwahi bastola yake kitandani, lakini
kasi ya mgeni ilikuwa kubwa na kumsukuma
kidogo kumpotezea mwelekeo,mama
hakutaka kukubali kirahisi, alitaka
kujipambania, lakini aliwahiwa kwa kofi zito
usoni,kofi lilomtoa kwenye ufahamu wake
kwa sekunde kadhaa na hata aliporudi kwenye
utimamu alikutana na kitu ambacho
hakukitarajia. Mgeni wake alikuwa ameshika
chupa ya marashi anayojipulizia mwili mwake.
Mtu yule alikuwa anayapuliza marashi yale
usoni pake na kwa kuwa halikuwa tukio la
kutegemea, alijikuta akivuta pumzi nyingi ili
kukwepa kile alichohisi mgeni wake
alikikusudia, lakini alikuwa amechelewa sana,
kwani alipovuta pumzi, alivuta harufu kali ya
marashi. Alianza kukohoa hovyo huku
akijaribu kuzuia asivute harufu kali ya marashi,
lakini haikusaidia, alikuwa amevuta harufu
nyingi kiasi koo lilikauka na hata majimaji
yanayokaa puani kulainisha
vinyweleo,yalikuwa yamekimbia kwa adha ile.

Mgeni alikuwa na hakika na kazi yake, hivyo
hakutaka kuendelea kuhangaika na
mwanamke yule aliekuwa mtupu na utu uzima
wake mbele ya kijana yule mdogo aliekuwa
amefunika uso wake kwa kitambaa maalumu.

Mwanamke yule alizidi kupambania uhai
wake, huku dhahiri akionekana kuhitaji
kunywa maji ili kupooza koo lililokuwa
limekauka na pua zikiwa kavu na zilizoenea
harufu ya manukato ya bei kubwa.

Mtu yule alitoa kibahasha kidogo kilichokuwa
na sawa na bahasha aliokuwa ameiacha
nyumbani kwa kocha. Bahasha hii pia ilikuwa
na herufi moja na namba “F3”. Bahasha ile
aliitupa uvunguni mwa kitanda na alianza
kuondoka, lakini ni kama alikumbuka kitu,
haraka alirudi na kuinama uvunguni, ambapo
aliitoa ile bahasha, kisha aliandika namba
mbili tu na kuitupa tena kule uvunguni.
Alipomaliza aligeuka upande ule ambao
alikuwa mwanamke akijitahidi kukohoa ili
aweke sawa koo lake.

Jamaa aliona picha kubwa ikiwa ukutani, picha
ilikuwa ya mwanamama yule akiwa kwenye
mavazi ya kipolisi yaliojaa nyota begani.

Ni kama hakuijali picha ile, badala yake
aliondoka na kupitia njia ile ile aliokuwa
amekujia.

Lakini mtu yule alikuwa anajua kabisa, si rahisi
kujua yule mwanamke ambae alikuwa ni
mstaafu wa jeshi la polisi, atakuwa ameuawa.

Kitu kimoja alichohakikisha ni kuwa mauaji
ya kocha alioyashuhudia, yanaendana sawa na
mauaji alioyafanya yeye kwa msataafu yule na
afisa habari wa timu ya Azan.

Muuaji alitokomea huku nyuma akiacha msiba
mzito na wenye utata mwingi, lakini ulikuja
kuumiza vichwa vya watu kwa namna tofauti
tofauti. Kuna wale ambao hawakukitegemea,
lakini wapo waliokitegemea. Lakini ilikuwa ni
kizungumkuti zaidi kwa idara ya usalama,
ambayo ilishindwa kujua kama yale mauaji
yalikuwa yanahusiana ama ni tofauti, lakini pia
haikuonekana kuwa ni mauaji, ni kama kocha
alilipukiwa na simu huku mstaafu akivuta
hewa nyingi ya manukato kiasi alishindwa
kupumua vyema.
Screenshot_20220929-180353.jpg
 
02

Lakini kilichostua mamlaka za ulinzi na
usalama ni jumbe zenye mfanano, zilizokutwa
kwenye maeneo ya vifo vilipotokea, lakini pia
vifo kuwahusu viongozi wa timu moja.

Walakini ukajaa, utata ukaibuka, mauaji
yaliongezeka na fumbo likasilia kwenye herufi
na namba zinazoachwa na muuaji ama wauaji.

Suala likawa gumu kwa jeshi la polisi, hivyo
faili la kesi likatua kwa kutengo maalumu chini
ya kamishina Zenge wa Zenge na hapo ndipo
ukawa mchezo wa vipepeo.

------------

-VIOLIN PUB.-

Usiku huu kulikuwa na makutano yasio
rasimi ndani ya Violin Pub Masaki . Pub hii
ilikuwa ina umaarufu mkubwa ndani na nje ya
jiji. Umaarufu wake ulitokana na aina ya
muziki unaopigwa pale kila siku, mziki wa ala
fidla(violin), Zeze na piano.

Pub hiyo iliojizolea umaarufu mkubwa, ilikuwa
inapata wageni kutoka nchi mbalimbali, Afrika
na hata mabara mengine na, kubwa
lilowapeleka pale ni muziki wa ala uliopigwa
na wasanii waliojua kuvitumia vyombo hivyo
ipaswavyo.

Licha ya kuwa sehemu ya watu kupata
burudani, lakini kulikuwa na harakati nyingine
zinaendelea ndani ya Pub, hasa kulingana na
mazingira yake kutawaliwa na sehemu nyingi
zenye kiza na taa hafifu, huku kukiwa na
korido nyingi na maalumu kwa wateja
maalumu wa ile Pub. Huduma nzuri ilikuwa ni
moja ya kivutio kwa wateja waliofika pale kila
mara.

Katika korido moja iliojitenga na zingine,
kulikuwa na makutano ya dharura ya watu
watano, lakini hadi usiku huo wa saa nne
mmoja alikuwa hajafika ili kutimiza idadi
kamili ya watu watano.

Watu hawa walikuwa na umri ulioenda
miongo zaidi ya mitano. Kulikuwa na wale
waliopita miongo sita na wengine walikuwa
chini ya miongo mitano na nusu lakini si
mitano kamili. Wote hawa walikuwa ni
wastaafu kwenye serikali ya Jamhuri ya
muungano wa Tanzania, ambapo walikuwa
wameshika nyadhifa mbalimbali katika serikali
kuu.

Usiku huu kuna jambo la muhimu lilikuwa
limewakutanisha, lakini walikuwa wanazidi
kupata mashaka zaidi kuona mtu wa tano na
waliemtegemea, akiwa hajafika na simu yake
haipokelewi.

“Unajua sielewi mambo haya jama”
Alizungumza mzee mmoja aliekuwa amevaa
pensi kubwa na sendo nyeusi, huku akiwa
amefunika kitambi chake na tisheti nusu, ni
dhahiri haikuwa yake.

“Acha kupagwa Masawe, bado mapema na
uzuri alituambia anakuja” Alisema Mzee
mwingine, ambae yeye alikuwa amevaa suti
iliokuwa inatoa harufu fulani ya uchafu
usiotisha, ni dhahiri aliitoa kwenye rundo la
nguo chafu.


“Kwa hiyo naona ushaniona mi kanyaboya wa
kupagawa hovyo sio.!” Masawe alimaka na
kumkata jicho aliempa ushauri.

“Sasa kama hujapagawa kwa nini umevaa
kimelembe?” Alihoji yule Mzee mwenye suti
chafu.

Kauli ile ilimfanya Mzee Masawe ajitazame,
kisha akatikisa kichwa na kusikitika.

“Kweli nimepagawa, yani na heshima yote
nimevaa hivi kweli!!” Masawe alijishangaa.

“Tatizo lako unapagawa sana na haraka,
wakati mambo madogo haya” Mwenye suti
chafu aliendelea kunanga.

Masawe alimtizama, kisha akacheka kivivu.

“ Haya mimi napagawa kizembe, vipi wewe
ulievaa msuti mchafu kama kikagula!”
Masawe nae alitoa dongo.

Wote waliokuwa mle walicheka, akiwemo
Mzee Kihengu ambae alikuwa amevaa suti
chafu.

“Jamani kila mtu kapagawa kwa kifo cha bi
Mwendampya, hakuna alietegemea kabisa
bwana” Alizungumza Mzee mmoja aliekuwa
amekaa kimya muda mwingi.

Wakiwa bado wanajadili, mara kuna mtu
alitokeza na kuwafuata wale wazee.

“Walau sasa tutahema, tulikuwa tuna
wasiwasi na afya yako bwana” Masawe
alimwambia alieingia.

“Nimechanganyikiwa kiasi nimesahasu simu
yangu mezani” Alijibu bwana yule.

Ulipita ukimya wa sekunde kadhaa, kila
mmoja akijaribu kuwaza lake.

“Jamani hili jambo limekaaje kwani, mana
naona kaondoka mtu ambae hatukuwa
tumepanga iwe hivyo.” Mzee kihengu
alianzisha mjadala.

“Kifupi hakuna ambae anajua kitu gani
kimetokea, lakini halina ubishi nae kauawa”
Mzee Mazengo ambae alikuwa kimya muda
mwingi, alitoa hoja yake.

“Lakini kwa nini auewe muda ule ule aliokufa
kocha? Aina ya kifo chake ni ya kitalaamu sana
jama” Masawe alitoa hoja yake.

“Kiukweli hakuna anaejua jambo hili
limetokeaje, lakini naamini Bi. Mwenda
kauawa, japo hatuna uthibitisho wa ripoti
kamili” Mzee alieingia mwishoni alisema.

“Lakini mnamwini mtu tuliempa kazi?”
Masawe alihoji.

“Aah, hilo halina ubishi, jamaa anajua bwana,
sifa zake zipo na ameonesha kwa wale
tuliotaka awaondoe” Mzee Kihengu alijibu.

“Unajua Masawe Unataka kukosea, unaanza
vipi sasa kukosoa utendaji wake mapema
namna hii?” Mazengo aliongea kwa ukali
kidogo.

“Sio kama ninahofu ya kazi yake, lakini huyu
mtu kumbukeni ni Psycho na watu wa namna
hii wanapenda sana kuuwa, tena kwa akili
nyingi sana na wao wanafurahia hali hiyo,
asije kuwa anataka kutoka na sisi ohoo”
Masawe alilalama.

“Unaogopa kifo kwani?” Aliuliza Kihengu.

“Naogopa vipi, wakati lazima nife, lakini sio
kwa mateso ya jitu lenu lile” Masawe alijibu.

“Sema jitu letu, au umesahau wewe ndie
uliempokea uwanja wa ndege?” Mzee
Mazengo alihoji.

“Sasa nani kamuuwa Mwendampya?”
Masawe alirudi kuhoji.

“Hakuna anaejua, kikubwa tusiogope kufa,
mana mchezo wetu ni wa kifo asilimia tisini”
Mzee alieingia mwishoni alisema.

“Afu Masawe usijisahaulishe kama wewe ni
muuaji” Kihengu alimwambia Masawe.

“Nani muuaji, sema sisi wauaji bwana.”
Masawe alihamaki.

“Aah, kwa hiyo tushakuwa wauaji tena”
Mazengo alishangaa.

“Kwani ulimlipa nani pesa? Si ulilipa muuaji,
kwa hiyo wewe nae muaaji.” Masawe alimaka.

“Aah kwa hiyo tunahatia sio!” Mazengo alizidi
kushangaa .

“Sio hatia tu, tuna kesi ya kujibu
mahakamani!” Masawe alikazia.

“Masawe usitutishe bwana, polisi hawawezi
kujua.!” Kihengu alipozea hamaki ya Mazengo.

“Wee thubutu, nimekuwa RPC, zaidi ya miaka
thelathini, najua serikali inachelewa tu, ila
inatakufikia tu, kikubwa jambo hili tulifanye
haraka, tuhame nchi kwa muda.!” Masawe
alizidi kutetea hoja zake.

“Aisee! Kweli bwana, nimekuwa muuaji eti”
Mazengo alizidi kuhamaki.

“Sio muuaji tu, muaji wa kutisha..hebu…”
Masawe alikatishwa na Mzee aliengia
mwishoni.

“Hebu Masawe, acha kututisha bwana, wote
tumehudumu huko, na tunaouwezo wa
kukwepa msala huu, ndio mana tulimuita yule
jamaa mtalaamu wa kupanga mauaji bila
kustukiwa na lengo ni kuondoa wote
wanaojua jambo hili kwanza.”

“Tatizo hawa wanataka tujadili hili jambo
kama watakatifu, ndo mana nimewambia
tusijitoe kwenye hatia kwanza.” Masawe
alijibu.

“Sawa, lengo ni kutaka kujua Bi Mwendampya
amekufaje na kwa nini na ni nani alimuua!”
Mzee alieingia mwishoni aliwarejesha wenzie
kwenye lengo la kukutana.

“Wakati nakuja hapa, yule bwana mdogo
alinambia kuna vitu wamevikuta sehemu zote
na vinafanana, kiasi inaonekana imewastua
maofisa na kuhisi ni mauaji ya kupangwa.”
Masawe aliwambia wenzie.

“Wamekuta vitu gani tena” Kihengu alihoji.

“kuna bahasha ndogo isio na kitu ndani, ila
kwa juu ina herufi moja na namba na
inasomeka “F3”…”

“F3?” Walijikuta wote wakishangaa kwa
pamoja.

“Vipi mmetambua lolote?” Masawe aliwahoji
wenzie.

“Afu huwa unajitia utoto Masawe, tungejua
tungeshangaa?” Mzee kihengu alimaka.

“aaah, naona unaleta uzuzu, nitakumbushia
enzi yangu bwana we, yani nauliza unaniita
mtoto ebo!” Masawe alimaka.

“Hebu tulieni bwana, mambo gani hayo sasa!”

“Sikia Nzaya, unajua Kihengu, ananichukulia
mimi wa kuokota tu, aisee mi nachafua si
mchezo ohoo!” Masawe alitupia mkwara
mwingine.

“Haya Mwakinyo, tumekusikia RPC wa
zamani.” Nzaya alimtuliza Masawe.

Nzaya ndie Mzee alieingia mwishoni.

“Sasa niliwambia huyu mtu atakuwa
anahusika mkanikatalia, kwa nini kwa Kocha
kuwe na bahasha sawa na ile iliokutwa kwa
Mwendampya?” Masawe alihoji wenzie.

“Lakini hii inafikirisha sana ujue. Kwani kijana
anasemaje yeye!” Mazengo nae alihoji huku
akimtizama Kihengu.

“Kuhusu Zozo kuuwa nakataa, mana
alipomaliza kwa Kocha, alinitaarifu, kisha
akasema anaenda kupumzika hadi apewe kazi
nyingine” Kihengu alijibu.

“Hata mimi naungana na Kihengu, hawa
wauaji wa kulipwa huwa wanaheshimu sana
mikataba yao, sio rahisi kuuwa mshirika wake
hata kidogo” Nzaya aliungana na Kihengu.

“Unajua wakati tunachagua mtu sahihi, tuliita
serial killer, huyu sifa yake kuu ni mgonjwa
yani anamtatizo ya ubongo, kitalaamu
Psychology, anafurahi akiua, anapanga
mipango yake kwa umakini, na kuwapa polisi
ugumu wa kuamua kesi, hivyo kumbukeni
hapa na tuna serial killer, hatuna Hitman wala
mamluki, hapa tumeita mgonjwa wandugu.”
Masawe aliwambia wenzie.

Ukimya ulichukua hatamu.

“Pamoja na yote, lakini hawezi kubadilika,
wala hana sababu ya kutugeuka bwana.”
Nzaya alikataa.

“Lakini unawajua watu wa aina hiyo kweli,
wao huwa wanafurahia kuua, afu wanaenda
kupiga selfie kituo cha polisi na polisi hawezi
mpata, furaha yao waone polisi
wanahangaika, au anaotaka kuwua
anahangaika…..” Masawe aliendelea
kuwazindua wenzie.

“Sasa kama ndie, kwa nini aache yale maneno
kwenye vibahasha?” Mazengo alihoji.

“Hapo ndo utata unaanzia, kwa nini aache
hicho kibahasha, ana maana gani?” Kihengu
nae alihoji.

“Sina hakika kama Zozo anatugeuka, mi
nadhani kuna jicho la mwewe linatuchora,
kiasi linataka kutuchanganya tu.” Mazengo
alizungumza.

“Unaweza kuwa sahihi, kuna kidudu mtu
anataka kutuharibia mipango” Nzaya aliunga
hoja.

“Hapa kuna mchezo wa danadana jamani,
tuwe makini na ikibidi tusitishe suala hili!”
Masawe aliwashauri wenzie.

“Aah wapi, haiwezekani hata kidogo, tuko
mwishoni kabisa, jambo tumelisubiri miaka
kumi, tunasitishaje kizembe namna hii”
Mazengo alimaka.

“Ila kweli, afu ujue tunakesi ya kujibu,
tumepanga mauaji ya kocha, na wale wawili,
kujitoa ni kujigeuza mbuni kuficha kichwa
mchangani huku mwili upo nje.” Nzaya nae
alishauri.

“Hapa babaya sasa!” Masawe alisikitika.

“Wewe si mstaafu na unatishia kucharaza
mkono, unakuwaje muoga sasa!” Kihengu
alimzodoa Masawe.

Vilifuata vicheko vya chini chini.
Watu waliokuwa kwenye dharura ile,
waliwafahamu vyema Kihengu na Masawe,
ambao ni marafiki wa kushibana na hakuna
aliewahi kumnunia mwenzake, zaidi
huzodoana na kuishia kucheka, hivyo haikuwa
mara ya kwanza wao kuzodoana.

Kikao kile kilivunjwa baada ya kuwepo
makubaliano fulani, mipango kabambe
ilipangwa, huku kila mmoja akiwa na jukumu
la kujilinda yeye kama yeye, kisha waliondoka
ndani ya Violin Pub.

Lakini wakati wanaondoka, kulikuwa na mtu
akiwasindikiza na macho makavu yenye hila
juu yao.

Ila wao hawakujua, waliamini kiza kilichokuwa
ndani ya Pub ile nzuri na ya kuvutia.

****
Ahsubuhi ilikuja ikiwa na mambo mengi,
lakini liloshika vichwa na masikio ya watu ni
kifo cha kocha wa timu ya vijana ya Azan.
Mashabiki wa timu hiyo waligubikwa na
simanzi, huku chanzof cha kifo chake,
kikihusanishwa na mlipuko wa simu wakati
alipokuwa anaichaji huku akiwasilana.
Magazeti yalipambwa na habari ile ya
kuhuzunisha.
Mashabiki waliumia zaidi kwa kuwa walipata
misiba miwili ndani ya klabu moja, alikufa
kocha na alikufa afisa habari wa timu ile
iliokuwa inazidi kujizolea mashabiki kila pande
ya nchi. Mtaani ukazuka mjadala kuhusu vifo
vile, lakini sababu za vifo zilitowesha kabisa
hisia za watu juu ya vifo vile.

Simanzi ilitanda, huku mwili wa kocha yule
raia wa Burundi ukiandaliwa kusafirishwa na
mwili wa afisa habari, Bi Mwendampya,
ukitarajiwa kuagwa kwa heshima za kiaskari
kwa kuwa alikuwa ni mstaafu wa cheo cha juu
kabisa ndani ya jeshi la polisi.

Ahsubuhi hiyo wakati hayo yakiendelea,
kulikuwa na jambo lingine linaendelea sehemu
fulani ndani ya jiji la Dar es laam.

Kulikuwa na mtu amekaa juu ya jengo fulani
akisubiri kitu, huku akiwa ameshika bunduki
kubwa ya kudungulia. Mtu yule alikuwa
amevaa nguo nyeusi, usoni akiwa amefunga
na kitambaa cheupe, alikuwa ni mrefu kwa
wajihi.

Mtu yule alikuwa amekaa pale zaidi ya saa
mbili, huku kila mara akitizama geti la nyumba
fulani. Nyumba ile ilikuwa kando ya barabara.

Ndani ya nyumba ile, kulikuwa na kijana
mwenye umri wa miaka kama thelathini hivi,
kijana yule alikuwa anamalizia kuvaa nguo
zake za kazi na mezani kwake kulikuwa na faili
lililokuwa limeambatanishwa vibahasha viwili.

Alikuwa ni ofisa wa jeshi la polisi mwenye
cheo cha koplo.

Koplo ndie aliekuwa ameshika jalada la
uchunguzi wa vifo vya kutatanisha vya kocha
na afisa habari wake. Alikuwa amekusanya
taarifa kadhaa za muhimu kuhusu vifo vile.

Koplo huyu hakuwa koplo wa kawaida,
alikuwa ni zaidi ya koplo na alikuwa ndani ya
kitengo cha operesheni maalumu chini ya
kamishina Zenge wa Zenge.

Koplo Juli tangu aingie kwenye uchunguzi
ule,ndani ya saa chache alikuwa amefanikiwa
kubaina mambo yenye kutia ukakasi, hivyo
haraka aliwasiliana na kitengo chake na kutoa
taarifa, kisha akatuma baadhi ya nyaraka
muhimu kwa njia ya mtandao, kisha alipiga
picha bahasha zile ndogo na kutuma kwa
kamishina Zenge wa Zenge.

Hivyo ahsubuhi hiyo alikuwa anajiandaa
kwenda kuripoti kituoni kwake, kisha
aendelee na uchunguzi wa kipolisi huku akitoa
taarifa kitengo maalumu .

Koplo Juli alitoka ndani ya nyumba yake,
akiwa amebeba mkoba wenye nyaraka zote
kuhusu kesi ile.

Wakati koplo Juli anafungua geti lake,
mdunguaji alikuwa ametulia akimtizama;
koplo alitulia getini huku akitizama saa yake.

Alikuwa anangojea Uber. Ilikuwa ni kawaida
yake kutumia usafiri huo kila siku, hakutaka
kununua gari, wala pikipiki, akiwa na nia ya
kukaa mbali na hisia za watu juu ya kazi yake
halali.

Kitu ambacho hakujua, hata mdunguaji nae
alikuwa anangojea Uber, ili akamilishe kazi
yake, mazingira yaliruhusu kufanya kile
alichotaji kufanya.

Dakika kumi baadae, kulikuwa na taxi
inasogea mitaa ile, mdunguaji alipoona nae
aliweka sawa bunduki yake.

Kutokea kule ilikokuwa taxi, hadi getini kwa
koplo Juli, kulikuwa na mteremko wa kiasi,
hivyo wakati gari inakaribia mdugunguaji
alilenga tairi ya mbele, kiasi gari ilianza
kuserereka kwa kasi kubwa huku ikipoteza
mwelekeo. Koplo alipokuja kutahamaki,
alijikuta akiwa amejaa kwenye taxi ile, kisha
alirushwa juu na kutupwa chini kwa nguvu na,
bahati mbaya hakuinua hata uso wake kuona
lolote lililofuatia.

Dakika moja iliofuata, kuna pikipiki ndogo
ilipita mitaa ile na kuuchukua mkoba wa
koplo, kisha ulikaguliwa kidogo na kurejeshwa
chini haraka sana, kisha pikipiki iliondoka kwa
kasi sana eneo lile.

Yote yalitokea kwa sekunde chache sana, kiasi
ilihitaji mtu mwenye elimu kubwa kuelewa
kilichotokea.

Mdunguaji alikunja bunduki yake, kisha
akaiweka kwenye begi na kuondoka juu ya
jengo lile na kutokomea anakojua.

Watu walianza kusogea eneo la tukio na
taarifa zilifika trafiki kwa kuwa ilikuwa ni ajali
ya gari kumgonga ofisa wa jeshi la polisi.

Wakati watu wanazidi kusogea, ilitokea
pikipiki moja na kusimama, aliekuwa juu yake
alishuka na taratibu alifika eneo lile na kuanza
kushangaa. Lakini mtu yule kuna kitu alitoa
mfukoni mwake na kukirusha karibu na tairi
ya taxi ilioleta ajali, kisha alipanda pikipiki
yake na kuondoka kwa kasi kubwa.

Hakuna raia alieona tukio lile, lakini mdunguaji
aliekuwa sambamba na raia wale akitaka
kuhakikisha kazi yake, aliona tukio la mtu yule,
lakini bahati mbaya sana hakumuona sura
yake.

Mdunguaji alipigwa na butwaa.

Kwa nini!.
Kwa sababu alitumwa kumuua koplo, ili
asifikishe vibahasha vile kwa uongozi wake,
lakini vibahasha vilishachukuliwa na wale
waliokuwa kwenye pikipiki, lakini kinaletwa
kibahasha kingine tena.
Ile ilikuwa ni maana mbaya kwa mdunguaji,
lakini ilikuwa ni hatari kwake, kwa sababu
aliona kila tukio analotumwa kufanya, yule
anaeacha vibahasha anajua, tena anajua hadi
eneo la kufanyia tukio.

Mdunguaji alibaki kujiuliza, kama jamaa
anajua mipango yake, kwa nini hazuii na
badala yake anaacha afanye kisha yeye
anaenda kuacha bahasha?.

Hakika lilikuwa ni swali gumu kwa mdunguaji
yule, alietumia akili nyingi kufanikisha tukio
lile.

Alipiga hatua ili aokote bahasha ile, lakini
aligundua kuna watu zaidi ya wawili
wanamtizama na walikuwa ni maofisa wa
jeshi la polisi waliofika pale haraka.

Mdunguaji alilaani kitendo kile, badala yake
alioendelea kusogea mbele na kulipita gari lile
taratibu kama vile hakuwa na nia na jambo
fulani.

****
 
03
****

Kifo cha koplo Juli, kilimwamsha Kamishina
Zenge wa Zenge.
Aliipokea taarifa ya kifo cha koplo kwa namna
ya tofauti kabisa. Aliona kuna hujuma
zitakuwa zimefanyika, sio rahisi eneo lile
kutokea ajali ya kuweza kumtoa mtu uhai.

Haraka alimwagiza Honda aliekuwa nae
ofisini, alihitajika mtu makini aina ya Honda,
kuchunguza kwa kina zaidi. Ilihitajika jicho
pana, hatua kwa hatua ili kufanikisha kujua
hila ya aina yoyote iliotumika.

Haraka Honda alichukua pikipiki yake na
kuelekea eneo la tukio.

Honda hakuchukua muda murefu kufika eneo
la tukio. Aliegesha pikipiki yake mbali kidogo,
kisha alitembea kwa miguu kuelekea eneo la
tukio, eneo ambalo watu walikuwa bado
wanashangaa kilichotokea.
Honda alikuta askari wa barabarani
wakimalizia kuchora ramani ya tukio la ajali.
Honda aliamua kujichanganya na watu ili aone
kinachofanywa na askari wale. Subira yake
hiyo, haikwenda bure, macho yake yalikuwa
yanacheza kama yale ya kinyonga. Kucheza
huko hakukuwa na bahati mbaya, yaliona kile
alichostahili kuona kwa wakati ule.

Watoto wawili walikuwa wameshika bahasha
ndogo wakiishangaa, bahasha ile waliiokota
mbali kidogo na walipokuwa maofisa
wanaopima ajali. Macho yake yaliwafuata
hatua kwa hatua, hadi walipoiacha chini na
kuwahi shule. Taratibu alipiga hatua na
kuisogelea, kisha akainama na kuikota.


Hakika macho yake hayakumdanganya, ile
ilikuwa ni bahasha yenye herufi moja na
namba, yani “F3”. Honda aliona inafanana
sawa na zile walizokuwa wametumiwa na
Koplo Juli.
Lakini ile bahasha kuna kitu cha ziada alikiona,
kitu kile alikuwa amekiona kwenye zile picha
za bahasha alizokuwa ametumiwa na Koplo.
Japo kulikuwa na ufanano, lakini haukuwa
ufanano sawa.

Honda aliichukua na kuifutika mfukoni
mwake, kisha aliendelea kuwa shuhuda wa
yale aliokuwa ameyakuta pale.

Alichagua sehemu nzuri ambayo ilimwezesha
kuona mengi kwa wakati mmoja. Macho yake
yalicheza kama njiwa pori aliekoswa na
mtego.

Bado bahati ilikuwa kwake, macho yake
aliyapeleka pale ilipokuwa gari ilioleta ajali.
Kuna cha ziada aliona na haikuwa rahisi kwa
mtu wa kawaida kugundua kasoro ile.

Kuna kishungi cha risasi kilikuwa kimenasa
karibu na rimu ya gurudumu, kishungi kile
kilikuwa kimesababisha tairi kupasuka na
kukiacha kikiwa kimenasa pale kutoka.

Honda alitoa simu yake mfukoni, na kwa
uficho alipiga picha eneo lile, kisha alisogea
sehemu iliokuwa na mkusanyiko wa watu.
Alipowafikia, aligundua walikuwa
wanamsikiliza dereva wa gari ilioleta mauti ya
ofisa wa jeshi la polisi. Dereva alikuwa
anajaribu kutoa maelezo ya awali kwa ofisa
wa jeshi la polisi kuhusu namna alivyoanza
kukosa mwelekeo, baada ya gurudumu moja
la upande wa kushoto kupasuka na akiwa
kwenye mwendo wa kawaida sana.

Honda alitathimini namna ambavyo ajali
ilitokea, kisha akahusanisha na kishungi cha
risasi alichikiona, hapo akihitaji ofisa aulize
swali muhimu sana ambalo binafsi lingempa
mwanga fulani.

Kwa sababu wakati wote huo, alikuwa hajui ni
namna gani risasi ile ilipigwa, je ilipigwa na
mtu wa karibu au mtu wa mbali, na ni nini
lengo la huyo mtu kupiga risasi gurudumu la
gari.

Hatimae ofisa mmoja aliuliza lile swali
ambalo lilikuwa muhimu kwa Honda.

“Ulihisi gurudumu la gari yako limepasuka
ukiwa eneo gani?” Ofisa alihoji.

“Ni wakati nakianza kile kibonde pale!!”
Dereva alijibu huku akionesha kidole eneo
aliloanzia kupata hitilafu.

“Je! Kulikuwa na mtu mitaa hiyo, ama kisiki
ama kitu gani ulichokuwa umeona kabla
hujapata hitilafu.” Ofisa alihoji swali lingine
zuri lenye manufaa kwa Honda.

“Hakukuwa na kitu chochote maeneo yale.!”
Dereva alijibu, kisha ofisa alimuelekeza
kupanda ndani ya karandinga, ili taratibu
zingine zifuate.

Honda aliondoka taratibu, akiwa anaungana
na watu wengine waliokuwa wanatawanyika
eneo la ajali. Hatua zake ziliishia kwenye
kiteremko alichokisema dereva, alijaribu
kuona ni wapi aliepiga risasi alijibanza, lakini
eneo lile na maelezo ya dereva, kusingeweza
kuwepo na mtu mwingine na dereva
asimuone, lakini alipojaribu kupima maneno
ya dereva, hakuona kama dereva anahatia
kabisa, ni dhahiri hata yeye alikuwa hajui
kilichotokea hadi apate ajali ya namna ile na
kumuua mteja wake wa kila siku.

Honda aligeuza macho yake kila pande na
hatimae aliingiwa na shaka na jengo moja refu
lilokuwa linatazamana na barabara ile. Honda
alijaribu kutumia hisia zake kumweka
mdunguaji eneo lile, kisha akaipitisha gari
maeneo yale, akapiga hesabu za namna koplo
alivyokuwa amekaa getini.

Honda alishusha pumzi nyingi, kisha
akajiwazia.

“Huyu mtu alikuwa na uwezo wa kumuua
koplo, lakini aliamua kutumia gari ili ionekane
ni ajali ya kawaida…” Honda aliguna baada ya
mawazo hayo.

“Ni serial killer, alietumwa kama mamluki,
analipwa pesa, japo binafsi yake anapenda
kuua… Nani anampa pesa na kwa nini aue?”
Honda alizidi kujiweka kwenye maswali mengi
yasio na majibu.

Aliendelea kuwaza kifo cha koplo, hakuona
kama ni kifo cha bahati mbaya, ni cha
kupangwa na lengo ni kuzima juhudi za
kutambua mauaji ya kocha na msitaafu Bi.
Mwendampya.

“Kwanini kocha auae siku moja na afisa habari
wake?” Honda alizidi kujiuliza,mara akili yake
ikakumbuka vibahasha vyenye herufi moja na
namba, kisha kwa wino hafifu kunaonekana
namba mbili nyingine.

Je muuaji anaweza kuwa ni mmoja? Na kwa
nini anaacha vibahasha, anataka kuacha
ujumbe gani?.... Honda alizidi kujipa maswali
zaidi.

Aliona eneo lile pekee, haiwezi kumpa majibu
aliyotaka, alielekea kwenye pikipiki yake na
kisha aliondoka eneo lile taratibu sana.

Kitu alichoamini ni kuwa, hakuna muuaji
duniani, aiseacha nyayo zake nyuma. Hivyo ni
lazima wauaji ama muuaji huyo, atakuwa
anaacha alama zake nyuma yake, japo
inahitaji umakini mkubwa kujua kosa lake na
ukalitumia kumtafuta hadi akapatikana.

****

Safari ya Honda iliishia nyunbani kwa kocha
wa timu ya Azan. Aliegesha pikipiki yake mbali
kidogo, kisha alitembea kwa miguu hadi
getini. Alikutana na utepe wa njano,
uliomuonya yeyote asiehusika, kuingia eneo
lile.

Alitizama pande tatu za dunia, huku ile ya nne
ikiwa imekingwa na nyumba ya kocha,
hakuona mtu katika pande hizo alizofanikiwa
kuziona.

Utulivu aliokutana nao pale, ulimhakikishia
hakukuwa na mtu yeyote katika nyumba ile.

Alisukuma lango la na kuingia ndani. Nyumba
ilikuwa kimya kabisa, alipiga hatua zake na
kuelekea ndani.

Alipoingia ndani, alianza ukaguzi wake hatua
kwa hatua, alianzia chumbani, kisha alielekea
jikoni.

Macho yake yalitua kwenye dirisha lilokuwa
wazi upande wa kulia wa jiko.

Honda aliingiwa na mashaka, alisogea hadi
karibu na dirisha lile, aliona linatosha
kupitisha mifupa 206, hivyo muuaji alipita pale
wakati wa kuingia na kutoka. Lakini Kama
alipita upande ule, ina mana hakupita getini,
alipita wapi sasa wakati anaingia pale ndani!.

Honda alirejea sebuleni, alikutana na damu
ikiwa imetapakaa chini na hakukuonekana
kufanyika usafi wa aina yoyote. Alitizama kwa
makini ili aone kama kulifanyika nguvu yoyote,
lakini hakuna sehemu alioona. Honda alisogea
hadi kwenye jokofu kubwa lilokuwa pale,
aliangalia namna swichi zake zilivyokaa, kisha
akaenda hadi nyuma ya jokofu lile.

“Yawezekana muuaji alikaa eneo hili, ikawa
rahisi kumuua kocha kwa kupitia nyuma na
kisha alimlaza hapa chini” Honda alizidi
kujiwazia.

Aliondoka sebuleni na kuelekea kwenye
chumba, alichohisi ndicho kilitumiwa na
marehemu kulala, alitulia kwa dakika kadhaa
na kukizoea, kisha alianza kufanya upekuzi
tena, mara hii akienda hadi maliwatoni, huko
macho yake yalimwonesha kitu kingine kabisa
ambacho hakukitarajia.

Dirisha la maliwato, lilikuwa ni dirisha kubwa
kidogo, lakini halitoshi kupitisha mtoto wa
miaka saba, lakini yeye alikuwa na hakika
anaweza kupita kwa kutumia ujuzi wa
mafunzo maalumu.

Kioo cha dirisha kilikuwa kimevunjwa, pia
kulikuwa na tope pale maliwato, kuashiria
alipita mtu mwenye viatu.

Honda alibaki na swali lenye utata.

Je alieuwa alipitia pale, ama alipitia kule
jikoni, na kama alipitia jikoni, ni nani aliepita
pale dirishani?

Likabaki swali bila jibu.

Honda alitoka nje ya nyumba ile, kisha
akaelekea upande aliohisi muaji alipita na
kutokea jikoni.

Macho yake yaliona kile alichotarajia, nyaya
zilikuwa zimekatwa, muuaji alikata na
kudondoka ndani ya ua.

Honda hakuridhika, alielekea upande ule
aliohisi mtu alipita na kuingia kupitia
maliwato, napo viashiria vilionesha kuna
mbabe alipita pale.

Kulikuwa na mti mkubwa uliodondoshea
matawi yake pale uwani kwa kuufunika ukuta,
lakini pia aliona majani yakiwa yamedondoka,
kuashiria alishuka nayo wakati anatua ama
anapanda juu ya mti ule.

Honda alishindwa kujua mahusiano ya watu
wale, lakini alishindwa kujua umuhimu wa
kocha yule katika sakata lile, kiasi afuatwe na
watu wawili kwa nyakati sawa ama tofauti.

Kama ana umuhimu, basi kifo chake kitakuwa
sawa na kifo cha bi Mwendampya.

Hakika Honda alitatizika.

Aliamua kuondoka mazingira yale, huku
akutarajia kwenda nyumbani kwa Bi.
Mwendampya.

Na huko alikutana na jambo jipya tena.

---------

Kutoka nyumbani kwa kocha, hadi nyumbani
kwa Bi. Mwendampya, hakukuhitaji usafiri
zaidi ya hatua zako chache tu.

Honda aliingia nyumbani kwa Bi
Mwendampya akiwa kama mwombolezaji.

Aliungana na kundi kubwa la watu mbalimbali
waliokuwa pale; viongozi wa serikali na
maofisa kadhaa wa jeshi la polisi na Magereza,
wanajeshi wa vyeo vya juu nao walikuwa
sambamba na waombolezaji wengine pia.

Honda alikuwa na kazi moja tu, kuhakikisha
anaona kile ambacho mtu mwingine hawezi
kuona.

Wachezaji wa timu ya Azan na baadhi ya
viongozi, nao walikuwa wamejumuika kwa
ajili ya mazishi.

Honda alijaribu kuzungusha macho yake kila
pande, lakini hakuna jambo geni wala jambo
la kutisha aliloona linampa shaka.
Aliendelea kukaa pale kwa dakika kadhaa,
kisha alipitisha shauri azunguke maeneo
mengine zaidi ili aweze kuona kile alichohisi
anaweza kuona.

Alijichanganya na kundi la wachezaji lilokuwa
nyuma ya nyumba.

Alitulia akisikiliza maongezi ya wachezaji,
katika mazungumzo yote hakuna jambo geni
alilosikia na, wachezaji walikuwa wanajadili
hatima ya uongozi wa timu yao.

Masikio ya Honda yakiwa yanasikia
malumbano yale macho yake yaliona jambo
alilotilia shaka.

Kulikuwa na dirisha lilokatwa kidwara. Ni
dhahiri kilitumika kitu maalumu kukata kioo
cha dirisha lile. Aliamua kutizama upande wa
juu wa ukuta.

Aliona nyaya zikiwa zimekatwa, hiyo ilimpa
jibu ya kuwa hata Mwendampya nae
amehujumiwa uhai wake,lakini kwa nini
wahujumiwe viongozi wa timu ile?

Hakuwa na jibu, alihitaji kulipata jibu lenye
maana na kumuondoa kwenye kiza
alichoingia.

Honda alitamani kuingia ndani ya nyumba,
lakini umati wa watu ulimfamya asite kufanya
vile.

Akiwa bado anatafakari ujuzi wa muuaji, mara
alihisi kuna jambo halikuwa sawa maeneo
aliokuwapo.

Alihisi kuna mtu anamtizma kutoka mahali
fulani.

Alizungusha macho yake taratibu, hatimae
aliona yule aliemhisi anamtizama.

Kweli kulikuwa na mtu akimtizama na, mtu
yule alipogundua anatizamwa na Honda nae
aliamua kuondoka eneo alilokuwapo.
Honda hakutaka kumwacha mtu yule, nae
aliamua kumfuata taratibu sana bila
kumpoteza.

Mtu yule alianza kugeuka kila mara, dhahiri
alijawa na wasiwasi mwingi.
Honda alilitambua hilo.

Mtu yule alitoka nje ya ua, alianza kuambaa
na magari yaliokuwa yameegeshwa kwa wingi
pembezoni mwa barabara. Honda nae alizidi
kumkaribia zaidi na, hatimae mtu yule alianza
kutimua mbio kutoka eneo lile.


Honda nae aliamua kumfuata kwa nyuma
huku akijaribu kujipa kasi zaidi kuliko
anaemkimbiza.

Mbio za Honda zilizaa matunda chanya,
alifanikiwa kumfikia mtu yule, kisha akajirusha
mzima mzima na kumpiga kikumbo mtu yule
aliekuwa amevaa koti zito licha ya kuwa na jua
kali.

Honda alimpa konde zito lilomtoa kamasi yule
mtu. Mtu yule nae hakuonekana kuwa na ujuzi
wa kukwepa wala kurusha kofi na alikuwa
analia kama mtoto mdogo huku akiomba
radhi.

Honda alisimama na kumshangaa mtu yule
aliekuwa amejikunyata chini huku akijaribu
kuziba sura yake kwa mikono yake.

“Wewe ni nani?” Honda alihoji kwa ukali.

“Nisamehee kaka, nisamehe” Mtu yule alijibu
kwa kuombeleza huku akiomba msamaha.

“Sawa, nikusamehe kwa lipi na wewe ni nani!”
Honda alihoji tena.

“Naitwa Kindo kaka.!” Alijibu yule mtu.

“Nikusamehe kwa lipi sasa!” Honda alihoji.


“Nilitumwa kukufuatilia.”

“kunifuatilia!!?, kwa nini ulinifuatilia.”

“Sijui, mimi nilitumwa tu.”

“Nani alikutuma”

“Simjui kaka”

Honda alishangaa.

“Kwa nini usimjue mtu aliekutama?” Honda
alimhoji.

“Nilikutana nae leo tu na hakunambia jina
lake”

“Ulikutana nae wapi?”

“Pale alipopatia ajali afande Juli”
Honda alinyamaza kwa sekunde kadhaa.

“Kwa hiyo ulinifuatilia tangu kule?” Hatimae
alihoji.

“Ndio” Alijibu Kindo.

“Alikwambia kwa nini unifuatilie!”

“Hapana, ila alinambia nimfuatilie yeyote
atakae okota bahasha ndogo na kuifadhi.

Honda alinyamaza kidogo, alikuwa anayapima
maelezo ya yule mtu, hakika alikuwa sahihi na
hakuonekana kuwa na udanganyifu wowote.

“Baada ya kunifuatilia, alipanga mkutane
wapi?” Honda alihoji.

“Alinambia nitamkuta kwenye gari jeupe lenye
namba T580,litakuwa limeegeshwa nje
kwenye msiba wa Bi Mwendampya.” Alijibu
Kindo.

Honda alitafakari, akaona kwa kuwa
alikurupushan na Kindo, basi aliemtuma
atakuwa ameshatoweka, la sivyo atakuwa
kajichanganya na watu wengine na sio rahisi
kumuona.

Honda alimwinua Kindo kisha akamuomba
wafuatane kurudi kwenye maegesho ya
magari ya watu walioko msibani.

Kindo alimwongoza Honda kukitafuta gari
lenye zile namba alizopewa na mtu asie
mfahamu.

Macho yao yalikuwa makini na kila gari jeupe
waliloliona.

Hatimae waliipata gari yenye namba za usajili
T580. Honda alitizama kwa makini gari ile,
lakini hakuona kama kuna mtu ndani yake,
alipojaribu kuzungusha macho yake pande
kadhaa, hakuona mtu yeyote aliefaa kutiliwa
shaka.

Honda alimgeukia Kindo.

“Ukimuona utamfahamu?” Honda alihoji.

“Kama atakuwa kavaa yale mavazi, naweza
kumkumbuka, japo sio sura yake” Kindo
alijibu.

“Nifuate!!” Honda alimuamuru Kindo,
walielekea ndani ya uzio wa nyumba ya Bi
Mwendampya.


Honda na Kindo walizunguka pande zote za
nyumba ile, lakini hakuna sura ambayo Kindo
aliitambua wala kuifananisha na sura ya mtu
aliempa kazi ya kumfuatilia Honda.

“Sasa tunafanya nini?” Kindo alihoji.

Honda alimtizama kwa tuo, kuna jambo
lilimwijia kichwani mwake na aliamua kuuliza.

“Kwa nini unanisaidia!”

“Kwa sababu wewe ni askari na naogopa
kuingia matatizoni kwa ukaidi”

“Umejuaje kama mimi ni askari”

“Unanekana tu, lakini alienituma alinambia
niwe makini mana wewe ni askari”

Honda alimtizama sana Kindo, lakini hakuna
hisia yoyote iliompa hatia kijana yule.

“Unafanya kazi gani!” Hatimae Honda
alimuuliza.

“Mi ni Shanta” Kindo alijibu.

“Shanta ndo nani ama kazi ya aina gani!”

“Yani sina kazi maalumu, yoyote nafanya bila
kujali mazingira, wala kujali ugumu wake, kitu
pekee Shanta asichofanya, ni wizi” Kindo
alimjibu Honda.


Honda hakuona kama ni busara kuendelea
kuzunguka na Kindo, aliamua kuachana nae
kisha alirejea eneo la maegesho, pale
ilipokuwa gari aliooneshwa na Kindo.


Aliisogelea, lakini macho yake yaligundua
kuna tofauti fulani imejitokeza,tofauti na
alivyoiona mwanzo.

Gari ilikuwa imeshuka upande mmoja.

Alisogea taratibu hadi ule upande, alikuta
gurudumu moja halina upepo na dhahiri
lilitobolewa makusudi.

Honda alishangaa, hakujua ni nani aliefanya
tukio lile, lakini pia aligundua adui yake
anamfahamu na, anapiga hatua sambamba
nae na hiyo haikuwa hatua nzuri kwake, wala
haikuwa busara kuendelea kucheza na mtu
anaemchezesha bila kujua.

Alijaribu kuangaza kila pande lakini hakuona
mtu wa kumtilia shaka, watu wachache
waliokuwa pale, walikuwa wanaingia ama
kutoka ndani ya magari yao.

Honda alihisi mtu yule anampa ujumbe kwa
njia za aina ile, lakini hayupo mbali na eneo
lile, si ajabu yuko kwenye moja ya magari
yalioegeshwa pale na anamtizama kila
anachofanya.

Honda alitaka kuanza kuondoka pale, mara
akili yake ilimkumbusha kama aliona kitu
nyuma ya gurudumu lilotoboka.

Alirudi taratibu na kuchungulia; kweli
kulikuwa na kibahasha kidogo chenye ukubwa
sawa na bahasha aliokuwa nayo mfukoni.

Aliinama kuikota, kisha aliisoma ilivyokuwa
imeandikwa.

Hakukuwa na tofauti, kuliandikwa herufi moja
na namba “F3” kisha kulikuwa na namba mbili
nyingine zilizokuwa zimeandikwa kwa mkono.

Bahasha ile ilikuwa na kitu kwa ndani, Honda
aliifungua na kukutana na karatasi nyeupe.
Karatasi ile ilikuwa imechorwa ndege, kisha
ikawekwa alama nyekundu na kulifuatilia
maneno “JNIA”.

Honda alishindwa kuelewa kwa haraka,
aliweka mfukoni mwake huku akizungusha
akili yake kwa tabu kubwa, kila alichojaribu
kufikiria, aliona ni kama hakihusiani na kile
alichokisoma kwenye karatasi ile.

“Ndege na uwanja wa ndege, sasa ina maana
gani hii na kwa nini huyu mtu ananizingusha
namna hii!” Honda alijiwazia, huku akiondoka
maeneo yale na kuelekea kule alikoacha
pikipiki yake.

“Alama nyekundu,… anamanisha kuna tukio
huko bila shaka, tukio gani sasa…” Alizidi
kujiwazia bila kupata jibu sahihi.
Hakika Honda alitatizika, alizidi kuicheza
ngoma ya mtu asiemjua, asiejua lengo lake
hasa ni lipi.
Hakika ulikuwa mtihani mgumu.

***

Honda hakutaka kupuuza mawazo yake, bila
shaka kulikuwa na ujumbe muhimu huko
uwanja wa ndege, alijipa msemo wa “Mwenda
bure si sawa na mkaa bure”. Alihitaji kuelekea
huko ili walau apate kile ambacho muuaji
alitaka kumuonesha..
Lakini Honda alibaki na swali moja la msingi
sana.

“Muaji anau kwa sababu gani, analipiza visasi
ama kuna kitu anachihitaji kutoka kwa watu
anaowaua na asipofanikiwa basi huwamaliza,
ama anaua kwa sababu tu, amejisikia kuua.”
Lakini wakati anajiuliza hayo, aliona haiwezi
kuwa ni visasi ama muaji anaua tu, kuna kitu
cha muhimu muuaji anakifanya na kitakuwa
na masilahi kwa aliemtuma, lakini pia kuna
kitu kilimfikirisha sana.

Kwa hatua aliofikia, ni wazi muuaji hakuwa
mmoja, na alieua nyumbani kwa Kocha, sie
aliua nyumbani kwa Bi Mwendampya...

Kwa nini!

Kwa sababu alieua nyumbani kwa kocha,
alijitahidi kutokuacha alama nyuma, lakini
alipoingia mtu wa pili aliacha alama zake kwa
kupasua dirisha la choo, pia alipofika
nyumbani kwa Bi Mwendampya, aliacha
alama kwa kuvunja kioo cha dirisha, japo
alivyoua ni kama anaiga uuaji wa mtu alieua
nyumbani kwa Kocha.
.
Honda aliona kifo cha Bi Mwendampya, kina
walakini mwingi, kuliko kifo cha kocha, kwa
sababu kocha anaeweza kuwa kauwawa kwa
visasi tu, lakini Bi Mwendampya, ni zaidi ya
kisasi bali muaji alitaka kumpa kesi alieua
nyumbani kwa kocha..
Honda aliyawaza hayo yote akiwa juu ya
pikipiki yake, safari yake ikiwa ni uwanja wa
ndege wa JNIA.

Wakati alipokuwa anakaribia Tazara, kuna
kitu kilimjia kichwani, haraka aliamua
kuegesha pikipiki yake pembeni na kushuka,
kisha aliitoa tena ile bahasha yenye mchoro
wa ndege na alama nyekundu.

Alifuangua na kutoa karatasi ile, kisha aliirudia
kuitizama kwa makini zaidi.

Kuna jambo lilimtatiza kidogo; ile alama
nyekundu ilikuwa imechorwa karibu na
upande wa kushukia, kwa namna mchoro
ulivyoonesha.

Honda alibaki na viulizo vitatu muhimu na
vyote vilizidi kumpa tabu katika maamuzi
yake.

Alijiuliza; kama ni kuhusu ndege, je!
Inatunguliwa? Na kama inatunguliwa ni ndege
ya shirika gani na ina kitu gani hadi kufikia
hatua ya kuihujumu?. Lakini alijiuliza ni vipi
kama kuna abiria muhimu ndani ya hiyo ndege
na ndie anaewindwa na anakitu gani kikubwa
hadi awindwe kuuwawa na ni nani mtu huyo
na anahusika vipi katika mkasa ule ambao
ulikuwa unaanza kuchukua sura mpya kila
wakati.

Honda alipumua kwa nguvu huku akitizama
barabarani na kuona namna dereva wa gari la
IST anavyojaribu kuwapiku wenye BMW na
Aud waliokuwa mbele yake.

Honda alitabasamu, alijifananisha na dereva
yule anaejaribu kukimbizana na magari yenye
hadhi na garama kubwa, alijiona ni kama
anaejaribu kufuatilia jambo kubwa na lenye
hadhi, likiwa na watu makini na wenye kuijua
kazi yao kuliko yeye.

Lakini tena alishusha pumzi baada ya
kuwapuuza wale wenye magari ya garama,
kwa sababu aliamini dereva ndie anaeweza
kukipa hadhi chombo chake, anaweza kuwa na
IST lakini akawa na ujuzi na staha kubwa
kuliko alieko kwenye Aud au BMW na mwisho
wa siku dereva wa gari dogo akaonekana wa
maana.

Honda aliona si busara kwenda uwanja wa
ndege akiwa hajui ni ni ni hasa anachofuata
huko.

Simu yake ilipopekelewa, aliomba
afahamishwe kama kuna mtu mkubwa yeyote
anaeutumia uwanja wa ndege kuondoka ama
kutua JNIA.
 
04
Baada ya kuomba taarifa hiyo, alitulia juu ya
pikipiki yake akijaribu kuwaza hili na lile.

Punde ujumbe ukaingia kwenye simu na,
alipoufungua alikutana na picha na jina la
aliewahi kuwa mwenyekiti wa bunge la Africa,
bwana Eli Sasi.
Bwana Eli Sasi alikuwa amekumbwa na
ugonjwa wa tezi dume, upasuaji wake ulikuwa
unaenda kufanyika nchini India na baada ya
kukaa huko zaidi ya nusu mwaka, siku hiyo
alikuwa anarejea nchini na ujio wake
ulitangazwa na vyombo mbali mbali vya
habari. Eli Sasi alisifika kwa misimamo yake
ndani na nje ya bunge la Africa, kiasi watu
wengi walimuona shujaa na hata alipostaafu
kulitumikia bunge, miaka kadhaa nyuma, bado
aliendelea kuwa na umuhimu mkubwa katika
siasa za Africa na hakuwahi kupungua
umaarufu wake, huku watu mbalimbali
wakichukua mfano wake.

Bwana Eli Sasi, wafuasi wake walianza
kumpigia chapuo agombee urais wa jamhuri
ya muungano wa Tanzania.

Honda alipoipokea taarifa ile, haraka
alielekea uwanja wa ndege, ambapo zilibakia
dakika chache kabla ndege haijatua.

Kwa kuwa alitumia usafiri wa pikipiki,
hakukawia kufika na kutafuta eneo maalumu
kwa wanendesha pikipiki kuegesha, nae
aliegesha kisha alitembea taratibu hadi
sehemu iliokuwa na taxi.

Alienda pale kwa lengo la kukaa eneo zuri
ambalo lingwezesha kuona watu
wanaotoka,pia lilikuwa eneo zuri ambalo
lingetosha kumwezesha kuona nyendo za mtu
yeyote asie na wema.

Honda alimfuata dereva taxi mmoja, alimlipa
kiasi kadhaa cha pesa kisha aliomba kukaa
kwenye gari yake. Baada ya makubaliano
hayo, Honda aliingia ndani ya gari na kutulia.

Akiwa kwenye gari, aliona watu wachache
wakiwa na mabango yaliondikwa jina la Eli
Sasi.

Macho yake yalikuwa yakizunguka kila kona,
lakini hakuwa amefanikiwa kabisa kuona mtu
yeyote ambae alihisi anaweza kuwa na tatizo
ama jambo lenye kutia shaka.

Saa ya Honda ilionesha muda umewadia kwa
ndege kuwasili, alikaa vyema kwenye kiti cha
gari huku mlango ukiwa wazi na mkono wake
wa kushoto ukiwa tayari kwa lolote.

Wapambe wa bwana Eli Sasi, waliendelea
kujikusanya pamoja, huku watoto wachache
walioandaliwa kwa ajili ya kumpa maua,
wakisogezwa karibu.

Kulikuwa na mtoto mmoja aliekuwa
anakimbia kujumuika na wenzie, mtoto yule ni
kama alichelewa na alikuwa anawahi kujiunga
pamoja na wenzake huku akiwa ameshika ua
jekundu.

Honda alimsindikiza kwa macho makavu bila
kupepesa, hakujua kwa nini alimwangalia sana
mtoto yule wa kiume ambae alikuwa amevaa
nadhifu, pengine kulilo watoto wote pale.

Kuna jambo jingine ambalo lilimchanganya
Honda, ni kama wale wapambe nao walikuwa
wanamshangaa yule mtoto, lakini umakini
wao kwa yule mtoto ulipungua baada ya
kuona msafara wa watu watatu ukitokea.
Wamama walianza kupiga vigelegele na
waandishi wa habari walianza kumzonga
bwana Eli Sasi.

Honda alimtizama Eli kwa kushangaa kidogo,
haiwezekani mgonjwa wa tezi, aliekaa
hospitali miezi sita, atoke akiwa na afya yake
timamu, ilikuwa inshangaza ila hakuna aliejua
ukweli zaidi ya ule wa kuambiwa bwana Eli
Sasi alikuwa amefanyiwa upasuaji wa tezi
dume nchini India.

Umakini wa Honda ulipungua, kwa kuwa
alikuwa anamtafakari mgonjwa kuliko lile
lilokuwa limempeleka pale.

Na hilo ndilo likawa kosa lake kubwa pengine
kuliko wakati wowote..

Honda akiwa anamshangaa Eli Sasi
alivyonawiri, mara aliona yule mtoto akimpa
ua bwana Eli Sasi, Eli nae alilipokea kwa furaha
na kumbusu mara kadhaa, kisha mtoto yule
alianza kujitoa katikati ya kundi dogo la watu.

Lakini kabla hajamalizia jitihada zake,
kulitokea kitu ambacho kilizua taharuki pale
uwanja wa ndege.

Ulitokea mlipuko wa kawaida, lakini uliondoka
na uhai wa Bwana Eli Sasi.

Ua alilokuwa amepewa na yule mtoto nadhifu,
lilikuwa limelipuka, ni dhahiri lilikuwa na
bomu dogo lenye madhara kwa mtu husika tu.

Wakati watu wanatawanyika ili kuokoa
maisha yao, kuna kitu kingine Honda aliona.
Yule mtoto akipaa juu na kuanguka chini;
Honda alirejewa na ufahamu wake, haraka
alijitoa ndani ya gari na kukimbilia pale
alipoangukia yule mtoto.

Kufuani kwa mtoto yule kulikuwa na tundu,
alikuwa amehujumiwa uhai wake kwa
kupigwa risasi mtoto yule.

Macho ya Honda yalitembea kwa kasi ule
upande ambao kulikuwa na magari ya watu
binafsi, aliyapeleka upande ule ambao aliacha
pikipiki yake,lakini kote huko hakuona kitu
chochote.

Polisi walianza kusogea eneo la tukio, Honda
hakuona kama ni busara kujitambulisha kwa
polisi mapema, hajui adui ni nani na anacheza
mchezo gani na kwa lengo gani.

Alisimama na kuondoka pale haraka, lakini
kuna sehemu aliona kuna na nafasi na bila
shaka mwenye gari kaliondoa muda mfupi
uliopita.

Haraka alizunguka upande wa pili wa eneo
lile, kulikokuwa na chumba cha kuongozea
kamera za usalama pale uwanjani.

Bahati mbaya ilikuwa kwake, alikutana na
askari wengi wakiwa wamesimama karibu na
chumba kile, hivyo ujanja wowote, ungempa
hekaheka asioitarajia.

Aligeuza na kurudi pale kwenye maegesho,
alikuta gari nyingine nayo ikijiandaa kutoka,
gari ile ilikuwa nyuma ya gari ilioacha nafasi na
kutoweka.
Honda alimuuliza dereva wa ile gari.

Dereva alifikifikiria kidogo, kisha alimtajia
namba ya gari kama alivyokuwa amehitaji.

Namba alioyatajiwa, ilimchanganya akili yake.

Ilitajwa namba T580, namba sawa na ile
aliotajiwa na Kindo, kisha waliitafuta na
kuipata.

Lakini gari hii iliokuwa pale uwanjani, haikuwa
na rangi nyeupe kama ile alioona mwanzo,
gari hii ilikuwa na rangi nyeusi na ilikuwa ni
V8,tofauti na ile iliokuwa Aud.
Ilikuwa ni ajabu, lakini ndivyo ilivyokuwa,
namba moja, ilikuwa inatumika na gari mbili
tofauti, kwa nini, hilo hakujua.

Honda aliona kuna umuhimu wa kuondoka
pale, alihitaji kuifanyia kazi namba ile.

Alikimbia haraka kuelekea kule alikokuwa
ameacha pikipiki yake, kisha alitaka
kuchomeka ufunguo pahala pake, lakini alisita
kufanya hivyo, kulikuwa na karatasi fupi ikiwa
imekunjwa na kuwekwa sehemu ile na kuwa
kama imekinga sehemu ya kutia funguo, ikiwa
na mana ya kuwa alitakiwa auone ujumbe ule
haraka na kabla hajatoka uwanja wa ndege.

Aliichukua karatasi ile, aliifungua na kukutana
na maneno ya kingereza, yasio leta mana ya
moja kwa moja, lakini ulikuwa ni ujumbe
fulani ulioeleweka vyema na Honda
mwenyewe, ujumbe ambao ulimwacha
akijitathimini kujiweka pande gani katika
mkasa ule.

“You decode, otherwise it’s not a menu you
deserve….my public IP….”

Honda aliurejea ujumbe ule kwa mara
nyingine tena, alijiona ni mtu alieshindwa
jambo fulani na kudhihakiwa na mtu
anaemwekea ujumbe kila mara, lakini hata
yeye alijiuliza..

Ni nini lengo la mtu yule, na kwa nini
alimwandikia ujumbe wa mafumbo, na kwa
nini alipenda kutumia zaidi code ngumu
ambazo sio rahisi kuzivunja!

Honda alibaki njia panda, hakujua mbivu wala
mbichi, aliona anazidi kuingia kwenye mchezo
wa adui alieficha sura yake .

Lakini je!, adui yule ndie anaeyafanya hayo
mambo yote, ama adui huyo anamsaidia tu ili
afikie lengo ambalo adui anaamini hawezi
kulifikia?

Hakika Honda alijiona amejaa kwenye dharau
kubwa ya mtu asiemjua na ilikuwa ni kama
kuchomwa kidole na kahaba ukiwa na mkeo.

Alirudia tena kusoma ujumbe ule, ikiwa ni
mara ya tatu kufanya hivyo, hapo ndipo
alizingatia maneno ya mwisho kabisa
yaliokuwa kwenye ile karatasi…

“My Public IP…”

Honda aliguna,kisha aliigeuza ile karatasi
upande wa nyuma, lakini hakukuwa na jipya…

“Sasa ataandikaje IP address afu asiiweke, na
anajiamini nini hadi kunitaarifu utambulisho
wake.

“Ina maana kama nikishindwa kuelewa zile
namba, basi ujumbe utakuwa haunihusu?”
Honda alitikisa kichwa na kuwasha pikipiki
yake, akiwa bado hajapiga hatua yoyote zaidi
ya kushuhudia mauaji ya bwana Eli Sasi na
mtoto mdogo.

Alienda ofisini, ambako alitarajia kukutana na
wengine wajadili kwa kina swala hilo.

Wakati Honda anaelekea ofisini, muuaji
mfupi na anaeacha bahasha zenye herufi moja
na namba moja, alikuwa amekaa karibu na
makutano ya barabara fulani ndani ya jiji la
Dar.

Kuna jamboa alikuwa analisubiri, jambo
ambalo lilimweka pale kwa zaidi ya saa moja
na dakika kadhaa.

Hakuna mtu yeyote aliemtilia shaka, wala
hakuna mtu alihisi kuna kitu kikubwa
anachokisubiri eneo lile.

Pembezoni kidogo ya makutano yale,
kulikuwa na kituo cha kujaza mafuta(sheli).
Ndani ya kituo, kulikuwa na fuso moja
iliokuwa inapakia mafuta na baada ya kupakia,
ilienda kuegesha kwenye gereji ya msaada
ilioko kituoni pale.

Macho ya mtu mfupi, yalikuwa yanatembea
kila hatua na ukarabati wa fuso ile, hata
wakati dereva wake anashuka na kuelekea
maliwato huku akiacha mlango wazi, mtu yule
alikuwa anaona yote hayo.

Mtu yule alitizama saa yake, kisha alipiga
hatua za haraka kuelekea kwenye gereji ya
msaada ndani ya kituo kile cha mafuta, hesabu
zake alitaka awahi kabla dereva hajarudi.

Hilo alifanikiwa, kwani aliwahi na kupanda
kwenye ile fuso kwa kasi kubwa, kisha
aliwasha na kuiondoa kwa kasi, kiasi ambacho
mafundi na watu wengine, walibaki
wakishangaa tukio lile bila kuchukua hatua
yoyote ile.

Alipolitoa kwenye gereji, alielekea upande ule
wa makutano ya barabara; macho yake
yakiwa makini na mshale wa saa yake,
ilipotimia dakika alioihitaji, alianza kuongeza
mwendo, kisha alikunja kulia ambako
kulikuwa na moafisa wawili wa jeshi la polisi
ambao walikuwa wamezuia magari kupita
upande huo kwa muda, hata pale walipojaribu
kumsimamisha wala hakujali, alizidi kuelekea
kule ambako gari zilikuwa zinatoka na si
kwenda kama alivyokuwa anafanya yeye.

Macho yake yaliona kile alichotaka kuona,
aliona pikipiki ya kuongoza msafara ikiwa
inamuwashia taa kuashiria apishe, lakini
hakusikia, alizidi kuongeza mwendo wa gari
lake la kuiba.

Mbele yake kulikuwa na msafara wa kamanda
wa polisi mkoa wa Ilala, bwana Luke Machage.

Dereva wa fuso alianza kuyumbisha gari lake
kushoto na kulia, lengo lake likiwa ni kuwapa
kimuhemuhe madereva wa msafar a ule
uliokuwa na magari matatu.

Ilikuwa ni ajabu kwa kiongozi yule kuwa na
msafara wa aina ile, lakini kwa siku hiyo
kwake ilikuwa ni muhimu kutembea na
msafara ule, kuna sehemu alikuwa anaenda,
sehemu ambayo mwizi wa fuso alikuwa
anaijua na hakutaka kamanda yule afike huko.

Kuyumba hovyo barabarani, hatimae kukawa
na matunda chanya kwa mwizi wa fuso.
Kwani madereva wa msafara, walikuwa
wanajaribu kumchanganya yeye kwa
kupokezana nafasi, lakini mwizi wa fuso
alikuwa na hesabu kali zaidi na alilifahamu
vyema gari la kamanda yule wa mkoa wa
kipolisi Ilala.

Kuyumba kwake alikuwa na malengo
maalumu, ambayo yalifanikiwa na hatimae
alikutana na gari iliokuwa imembeba kamanda
Luke Machage.

Mwizi wa fuso alikuwa na uwezo wa ajabu
kwenye usukani, kwani alipobakiza hatua
chache alikata kona kali na kwa mwendo ule
ule bila kupunguza kasi, gari iliombeba
kamanda, ilijigonga ubavuni mwa fuso
iliokuwa imebadili uelekeo gafla na kuwa
kama inajaribu kugeuka na kurudi ilikotokea.

Ilikuwa ni ajali mbaya sana, ajali ambayo
ilichukua dakika tano kuoenekana ya kawaida
mbele ya mashuhuda.

Gari ilikuwa imebondeka hovyo, huku damu
ikitoka na kuchanganyikana na mafuta
machafu yalioanza kuvuja.
Kishindo kikubwa kiliwafanya hata walioko
mbali kusogea ili kuona kilichotokea.


Wakati watu wakishangaa, mwizi wa fuso
alishuka haraka na kwenda kwenye gari
iliopata ajali, macho yake yalikuwa
yameshaona ni hatua ngapi atapiga kabla gari
zilizokuwa kwenye msafara hazijafika na
askari waliokuwamo kumpa bugudha.

Aliifikia ile gari, kuna kitu alikuwa anakitafuta
na moja kwa moja alielekea upande ambao,
aliamini kamanda Luke Machage, alikuwa
amekaa.

Bahati ilikuwa kwake, kwani upande ule
ulibondeka, lakini nafasi ilikuwa imebaki
kuweza kuchubgulia ndani, kiasi ambacho
aliweza kuona vyema namna vyuma vya gari
vilivyoweza kumsurubu kamanda yule.

Yeye hakuwa na shida nae tena, kuna kitu
alikihitaji, alitupia macho yake harakahara na
kuona mkoba wa kiofisi, aliingiza mkono
haraka na kunyakua mkoba ule, kisha
aliifungua kwa tabu kidogo mana nao ulikuwa
umekutana na dhoruba, kisha alipofanikiwa,
alitoa diski mweko iliokuwamo huku akiacha
nyaraka zingine ambazo hakuwa na kazi nazo.

Aliufunga ule mkoba, kisha alitoweka maeneo
yale kwa kasi kubwa huku akiacha maofisa
wengine waliokuwa kwenye magari mengine
ya msafara wakishuka kwenye gari zao na
wasijue kama kuna mtu kawahujumu. Wao
walikuwa wameelekeza akili kwa kamanda wa
polisi wa mkoa kipolisi Ilala.

Mwizi wa fuso, alizidi kutokomea mbali na
maeneo yale, huku akiwa amefanya
mawasiliano na mtu mmoja, ambae alimtuma
kazi ile, alihitaji usafiri wa haraka kuwahi
sehemu fulani kabla hajaifikisha diski ile kwa
aliemtuma.
 
05
Ndani ya Violin Pub, kulikuwa na burudani
inaendelea, watu waliendelea kuburudika kwa
kula, kunywa na kucheza. Lakini sio wote
waliokuwa wamefika mle kwa usiku huo,
walikuwa na furaha, la hasha, kulikuwa na
kundi la watu watano likiwa na majonzi, woga
na hasira kwa wakati mmoja.

Kundi hili liliongozwa na Mzee Masawe,
aliewahi kuwa RPC ndani ya mkoa wa Dar es
laamu kisha alimpisha Bi Mwendampya na
kisha akaenda kuwa balozi wa Tanzania nchini
Canada.
Pembeni yake alikaa Mzee Nzaya, aliewahi
kuwa mkurugenzi mkuu wa Bandari ya Dar es
laam; kulikuwa na Mzee Kihengu aliewahi
kuwa Kanali wa jeshi la wanachi Tanzania,
kisha alihudumu kama Mkurugenzi mkuu wa
Usalama wa Taifa,kulikuwa pia na Juma Lilo,
ambae aliwahi kuwa mkemia mkuu wa
serikali.

Wote hawa walikuwa ni wastaafu wa jeshi la
wengine wakiwa ni wastaafu walioongoza
kurugenzi mbalimbali ndani ya serikali.


Mbali na watu hawa, kulikuwa na mtu wa
tano, mtu huyu alikuwa amesimama kwenye
kona moja ndani ya korido ile iliokuwa imekaa
kama chumba kisicho na mlango ndani ya
Violin Pub.

Kikao hiki hakikuwa kikao cha dharura,bali
kilikuwa ni kikao ambacho kilipangwa tangu
ahsubuhi. Usiku huu kikao kilikuwa kimeingia
doa baada ya mtu muhimu sana kukosekana,
mtu huyo alikuwa na ujumbe muhimu sana
kwa watu wale, lakini sasa mtu yule alikuwa
hajafika, na hajutarajiwa kufika siku hiyo wala
siku zijazo.

Mtu wao alikuwa amekufa kwa ajali, ajali
ambayo kwa haraka ilikuwa ni ya kupangwa.

Kwa nini walijua ni ya kupangwa, kwa sababu
ilikuwa imeondoka na uhai wa mtu wao, na
kitu muhimu sana alichokuwa nacho mtu yule.

Hakika iliwachosha hali ile.

“Watu ambao hawahitajiki kufa, wanakufa kila
siku jamani…” Hatimae Mzee Masawe alivunja
ukimya uliokuwa umetamalaki pale ndani.

“ Hakika hili ni pigo na, ni pigo ambalo hatujui
kabisa linalenga nini” Mzee Kihengu alisema
huku akikuna kichwa chako.

“Ninaanza kuwa na mashaka na ukanali wako,
unawezaje kuona huu mpango na usiujue?”
Mzee Masawe alimjia juu Mzee Kihengu.

“Ni lazima tujadili kwa kina bila kuingiza hisia
bwege wewe ebo!” Mzee kihengu nae alifoka
kwa sauti kubwa.

“Tulieni wazee, sio muda wa vijembe huu,
kumbukeni adui yetu anazidi kuweka mipango
yake sawa” Nzaya aliingilia kati sakata lile.

“Jamani mwanzo tuliona kama huyu bwana
anatuhujumu, lakini leo Kamanda Luke
Machage, amehujumiwa tukiwa na huyu
bwana, hakika inafikirisha sana” Alizungumza
Juma Lilo huku akimuonesha kidole mtu yule
aliekuwa amekaa kwenye kona akiwa kimya.

Mtu yule alikuwa ndie muuaji wao
waliemtegemea na ndie aliemuua Bwana Eli
Sasi uwanja wa ndege.

Mtu yule aliitwa Zozo, raia wa Africa Kusini,
alieogopwa na mwenye sifa ya kuuwa bila
sababu na aliipenda kazi yake.

Bwana Zozo hakuwahi kulipwa kuua, bali aliua
pale alipojisikia, lakini Bahati mbaya
alikamatwa miezi kadhaa huko, lakini
alitolewa kwa makubaliano maalumu, ambayo
yalifikiwa baina ya Mzee Masawe, Nzaya na
Kihengu, ambao walilipa pesa nyingi kama
hongo kwa maofisa kadhaa nchini Afrika
kusini, ambao walimwachia Zozo kisha
kumsafirisha hadi Tanzania na kuanza
kuwatumikia watu wale kwa malipo, lakini
akiwa katikati ya kazi yake, anaibuka mtu
mwingine tena ambae anasifa na uwezo kama
wake, mtu yule alikuwa anajua kile
kilichoenda kufanywa na Zozo.

Jambo lile si wale wazee tu, hata Zozo
lilimchanganya sana, kiasi alianza kuona hatari
kubwa sana mbele yake.

Lakini hakuwa na namna, alikuwa kibaruani na
sheria alizijua vyema, hakutakiwa kukimbia na
kuacha kazi yake.

“Hakika hata mimi nimeanza kuona hujuma
ya wazi juu ya jambo hili” Nzaya aliunga
mkono hoja iliotolewa na mjumbe mmoja.

“Unajua mimi nimefanya kazi kama mkuu wa
idara ya usalama, kuna kitu nakihisi kwenye
hili sakata letu na tunachezewa kabisa” Mzee
Kihengu alisema na wenzie walikaa kimya
wakimtizama, walihitaji aendelee na hoja yake
ili wamuelewe.

“Kuna mtu miongoni mwetu ni double Dave”

Ukimya na miguno ilichukua hatamu kwa
kupishana kidogo.

“Una maana gani komredi” Nzaya aliuliza
huku akiwa kama anaepaliwa na mate yake.
Kisha alikohoa kidogo kujiweka sawa.

“Unajua double dave, ni nyoka wa vichwa
viwili lakini mwili mmoja, katika vichwa hivyo
kila kimoja huwa na ulimi wake na kila ulimi
una kazi mbili tofauti, lakini zinaufadisha mwili
mmoja” Kihengu alifafanua.

Ukimya ulipita kwa sekunde kadhaa.

“Umezungumza jambo zito kidogo, lenye
maana fulani hivi!” Juma lilo aliungana na
Kihengu.

“Sitaki kuamini unachosema, japo inafikirisha
hasa kwa matukio haya yanayoendelea
kutokea hivi sasa” Nzaya nae aliongezea.

“Kibaya zaidi ni ngumu kushika mkono wa
baradhuli, mana wote hapa tumefanya kazi
kitengo aisee!” Masawe aliongea kwa upole
sana, ishara ya kuwa mbali kifikira kuhusu
wazo la Kihengu.

“Hapo ndo pagumu zaidi, lakini naamini hata
kama hatoki miongoni mwetu, basi kuna mtu
miongoni mwetu aliwahi kuuza mchoro wetu
huu” Kihengu alizidi kutoa mashaka yake.

“Kusema kuliuzwa mchongo, isingewezekana
kila tunachofanya basi kinagundulika kirahisi
na kuishia kuacha majonzi juu yetu” Masawe
alisisitiza zaidi.

“Ni kweli, mana tulioko hapa, tulikubaliana
kuwaondoa wengine ili tusije kustukiwa
kizembe,pia tuishie kupata mgao mnono, sasa
inakuwaje kila tunaemtaka afe, na mtu wa
upande wetu anakufa?” Masawe alihoji tena.

“Na hapo ndio tunaishia kusema kati yetu
wanne kuna mmoja ni Dave!!” Kihengu
alisema.

“Ni nani sasa!” Nzaya alihoji.

“Kila mtu atauliza hilo swali, lakini kila mmtu
pia atakuwa na jibu moja ya kuwa, hahusiki”
Juma Lilo alizungumza na kila mmoja alitikisa
kichwa chake kwa kukubaliana na jambo lile.

Wakati wao wanaendelea kujadili, Zozo
alikuwa makini sana akiwasikiliza licha ya
kutoelewa lugha, lakini alikuwa anaona
namna waajiri wake walivyo katika tafakuri na
majadiliano makubwa.

Lakini yeye jicho lake lilikuwa kwa Nzaya,
hakujua kwa nini, lakini alijikuta akimwaga
maji tumboni, kila alipomtizama Nzaya,
angefanya nini wakati hajui majadiliano yao
yalihusu nini, yeye aliitwa pale kudumisha
ulinzi na kisha alitakiwa kumsindikiza Masawe
nyumbani kwake na huko angepata mgao wa
pesa yake kwa kazi aliokuwa amefanya siku
hiyo.

“Hakika naanza kujuta kuipanga hii kitu, mana
naona kuna mjanja anataka kuilalia na bila
shaka anausaka uhai wangu kwa nguvu zote ili
apate anachotaka” Masawe alizungumza kwa
utaratibu sana.

Ukimya ulikuwa mkubwa, hakuna aliemjibu
mwenzie wala kutaka kuzungumza tena, kila
mmoja aliwaza kuhusu diski mweko iliopotea,
ilikuwa ni muhimu sana kwenye hilo swala, na
kupotea kwake, ilimaanisha wanarudi nyuma
na kupoteza tena kila kitu walichokuwa
wamekipigania, zaidi ya miaka kumi iliopita.

Lakini kubwa lilowapata shaka, ni namna
serikali ilivyokuwa imelichukulia suala la kifo
cha msitaafu, Bi Mwendampya, ambae ripoti
ilipotoka, ilionesha alikufa kwa kuwa alivuta
kiwango kikubwa sana cha harufu ya marashi
makali, kiasi koo lake lilikauka na kumpa kiu
kali, iliopelekea yeye kukosa uwezo wa
kupumua vizuri na damu kutembea kwa kasi
kubwa, huku mapigo ya moyo yakienda kasi
na kupelekea kifo chake.

Dhahiri sababu hiyo, ilipelekea serikali kuona
kuna jambo ambalo halikuwa sawa sehemu
fulani, lakini pia bastola yake ilikutwa ikiwa
imeondolewa usalama, huku uchunguzi wa
awali ukionesha, kulikuwa na mparangano
kidogo ndani ya chumba chake.

Wao waliamini kuendelea kusubiri jambo
lisiloisha, ni kama kujiweka pabaya zaidi ,hasa
ikija gundulika kuna mkono wa mtu, tena
watu ambao waliwahi kupata wadhifa
mkubwa serikalini; Sio wadhifa tu, waliwahi
kuwa maofisa usalama wa taifa, wakihudumu
katika migongo ya nyadhifa walizokuwa nazo
na zilizotambulika na watu wengi.

Hakika walijikuta wakiishiwa hamu na
kushikwa na hatia ya kulisaliti taifa lao
kizembe, kwa kile walichokuwa wamekifanya.

“Huyu anaetula migongo, nitapambana nae
kwa njia anazotaka, naombeni kila mtu
aondoke, niacheni, hii diski nitaipata na
msaliti nitamwanika hadharani kabla ya
kuondoka na kichwa chake.” Masawe
aliwambia wenzake, kisha walianza kusambaa
mmoja mmoja, lakini Masawe aliomba
Kihengu asalie pale ndani.

Juma Lilo na Nzaya, waliondoka na kumwacha
Kihengu; Masawe na mlinzi Zozo.

“Naamini huwezi kunidanganya, wala huwezi
kupindua meza yenye vinywaji, hapa kati ya
Juma na Nzaya, unahisi yupi ni dede?”
Masawe alimuuliza Kihengu baada ya kusalia
wao wawili na Zozo, ambae hakuwa anajua
lugha ya kiswahili.

“Hata wewe najua huwezi kukengeuka, lakini
sina hakika kama Juma anaweza kufanya
hivyo, Nzaya kawa mjanja mjanja sana, uso
wake unasadifu hujuma hii, ukizingatia
akaunti zote zinataka sahihi yake, hivyo ni
rahisi sana kutugeuka” Kihengu alimjibu
Masawe.

“Nakuamini sana, na huwa sina shaka na
mawazo yako, ukizingatia umekuwa kanali wa
jeshi, kisha ulikuja kuwa mkurugenzi wa
usalama, naamini unahisia za mlango wa
saba.” Masawe aliongea.

“Hakuna namna, lazima tumweke kikaangoni,
kuanzia usiku huu” Kihengu alimwambia
Masawe

“Najua unao vijana makini, ambao wanaweza
kumfuata bila kujua, vijana hao waliwahi
kukutii wakati ukiwa mnene wao, hivyo basi
fanya hivyo” Masawe alimwambia Kihengu.

“Usijali, kila kitu kitakuwa sawa, kisha tutajua
cha kufanya” Kihengu alijibu.

“Poa komredi, ila hawa wajinga wamefanya
nisiende kwa mchepuko wangu, sina hamu
kabisa!” Masawe alisema huku akinyanyka
kivivu.

“Huna hamu, au siku hizi hupandi milima,
usisingizie bwana!” Kihengu aliongea huku
akianza kupiga hatua kuondoka ndani ya
korido ile tulivu.

“Vipi mkeo aliwahi kukusimulia mtanange
wangu lakini!” Masawe alimjibu Kihengu kwa
utani.

“Kwa sura gani ulionayo hadi umvue mke
wangu nguo, yani wewe hata akipewa bilioni
moja, hawezi kukuvulia” Kihengu alijibu huku
akiweka sawa koti lake.

“aah, nijaribu leo!” Masawe alihoji huku
akitabasamu.

“Naona umesahau kama nina namba za mkeo,
shauri yako!” Kihengu alijibu huku akiondoka
na kumwacha Masawe akicheka kwa masihara
yale.

“Huyu mjinga ananifurahishaga, hata kama
nimenuna, lazima nicheke… a true friend.”
Masawe alijisemea mwenyewe, huku
akimgeukia Zozo na kumpa ishara waondoke,
Zozo alielewa.

Wakati anatoka, alipita karibu na jukwaa la
wanamuziki na, kulikuwa na mpiga fidla
mmoja akitumbuiza.

Mpiga fidla alikuwa amevaa sweta lenye kofia
kichwani, ilikuwa ni vazi lake la kila siku na
pub ile ilikuwa na wapiga fidla wawili tu,
mmoja alikuwa havai sweta na kila mara
alibadili mavazi, lakini huyo aliekuwa anapiga
wakati huo, hajawahi kubadilisha sweta lake
hilo lenye kofia na kila alipopanda jukwaani,
huwekwa taa hafifu, kiasi inakuwa ngumu
kutambua mpigaji.

Mpigaji yule alikuwa anajua namna ya
kuitumia fidla ile, alikuwa anapangilia vyema
ala bila kukosea, kila muziki alikuwa anaweza
kuupandishia ala yake.

Masawe alitumia dakika mbili kutazama
mpigaji yule, alijikuta akijiwa na wazo fulani la
kipuuzi, kisha alimuita Zozo na kumuomba
waongozane kuelekea kwenye ofisi ya meneja
wa Violin Pub.

Walitumia dakika mbili kufika kwa meneja,
Masawe hakubisha hodi, aliishia kuusukuma
mlango na kuingia, nyuma yake alifuata Zozo.

Walikuta Meneja akiwa na binti mmoja
wakinyonyana ndimi, kuingia kwao
kuliwagutusha meneja na hamimu wake.

“Nikikufukuza utanilaumu?” Masawe alimhoji
meneja.

“Nisamehe Boss, ni bahati mbaya tu!” Meneja
alojitetea.

“Bahati mbaya, wakati unaona upo ofisini?,
bahati mbaya huwa chumbani tu!” Masawe
alifoka.

Meneja alikaa kimya.

“Ukimwi nao hauna bahati mbaya matege
yako wewe!!” Masawe alizidi kufoka na
meneja alikaa kimya.

“Hili tutazungumza kesho, saivi nataka kujua
jina na sura ya mpiga fidla wa zamu ya usiku!”
Masawe alimwamuru meneja.

Meneja aliguna..

“Nini!” Masawe alihoji.

“Huyu jamaa anaitwa Kado, ila sikuwahi
kuipata sura yake na kwenye mikataba ya
wafanyakazi, hatukuwahi kujaza mi na yeye.

“Aisee!! Yani unazidi kunipa sababu za
kukupuga hapa Pub, unawezaje kufanya kosa
kama hilo?, akipata tatizo tutamsaidia vipi
kama hana mkataba na uongozi wa Pub hii?”
Masawe alifoka.

Meneja aliomba radhi.
Masawe alimuangalia kwa dakika moja bila
kusema kitu, kisha aliuliza.

“Ulimpata wapi huyu mpiga fidla?”

“Aah, aliletwa na rafiki yako Nzaya!” Meneja
alijibu.

“Whaat!” Masawe alishangaa.

“Ndio, alimleta na kumkabidhi kwangu na
nilipomwambia ashike fidla, aliishika
kucharaza kama unavyosikia bosi”

“Alikwambia anapoishi?” Masawe alihoji.

Meneja alitikisa kichwa, kuwa hajui.

“Aisee!!” Masawe alisema huku akimwangalia
meneja wake.

“Nenda umwambie aje, aachie wapiga piano
waendelee!” Masawe aliagiza.

Meneja alitoka na kuwaacha, Masawe na
Zozo ambao walikaa kimya bila kusemeshana,
lakini Zozo aligundua Masawe ndie mmiliki wa
Pub ile kubwan na ya kisasa ilioitwa violin
pub, pub ambayo ilisifika kwa buruduni ya ala
pekee, huku sifa nyingi zikienda kwa wapiga
fidla(violin) ambao umaarufu wao ulifanya
pub ibadilishwe na kuitwa violin pub.

------
 
06
Dakika tano zilipita, ndipo meneja aliporudi
akiwa peke yake bila mpiga fidla.

“Nimeambiwa alishuka jukwaani, lakini
hakumuaga mtu anapoelekea”Meneja alimpa
taarifa Masawe.

Masawe alibaki akishangaa, hakujua aseme
nini ili apate jibu la mpiga fidla.

“Kwa nini aondoke?”

“Sijui bosi, lakini nimebiwa hajamuaga mtu!”

Masawe alianza kuhisi kitu kibaya kwa mpiga
fidla, lakini pia alianza kuona swahiba wake
ndie anaewala kisogo, lakini suala la mpiga
fidla na Nzaya kuwa wana mahusiano,
lilimwacha njia panda.

“Kwanini aondoke? au kwa kuwa
nilimwangalia sana muda ule?” Masawe
alijiuliza peke yake, kisha alinyanyuka na
kuanza kuondoka pale ofisini, nyuma yake
alifuata Zozo.

***
Baada ya kutoka jukwaani, mpiga fidla alienda
sehemu fulani yenye kiza katikati ya jiji la Dar.
Alienda kukutana na mtu waliekubaliana
kukutana ndani ya muda huo wa usiku.

Yalikuwa ni makutano yao ya kila mara, lakini
usiku huu yalikuwa ni makutano ambayo
hayakupangwa tangu mapema, hivyo yalikuwa
ya dharura.


“Sina hakika kama ni busara kuniita wakati
unajua nipo kazini!” Alizungumza mtu
aliekuwa amesimama kwenye kona moja
ndani ya chumba kwenye jengo pweke.

“Kado, ukiona nimekuita ujue kuna dharura!”
Aliongea mwingine aliekuwa kona nyingine
ndani ya chumba kile chenye giza.

“Hawa jamaa wameanza kushitukia mchezo
bwana!” Alisema yule bwana.

“Kivipi yani!” Alihoji Kado.

“kikao chetu hakijamalizika vizuri, kila mmoja
anamshuku mwenzie kuhujumu mpango!”
Alijibu yule bwana.

“Kwa hiyo tunafanya nini sasa!” Alihoji Kado.

“Sina wazo zuri kwa sasa, mana wote ni
wahusika muhimu kwa hatua iliobaki, pesa
zingine zipo kwenye mzunguko unaowahitaji,
hivyo sio rahisi kuchukua maamuzi magumu
kwa sasa!” Alijibu yule bwana.

“Ukihitaji kufanya lolote, nistue nami
nitafanya inavyowezekana ili ubaki kuwa
salama” Kado aliongea.

“Usijali, lakini kuwa makini kuanzia sasa, mana
Zozo anadai alikuona wakati ukiwa kwenye
tukio la ajali ya koplo Juli, lakini hakufanikiwa
kukariri vyema!”

“Umefanya vizuri kunipa taarifa, lakini
waonaje kama nikumuondoa haraka huyo
jamaa?” Kado alihoji.

“Usijali, muda ukifika nitakutaka ufanye
hivyo” Alimjibu yule bwana.

Baada ya mazungumzo yao hayo, Kado
aliondoka na kurejea kazini kwake pale Violin
Pub, huku mtu wake nae akiondoka kuendelea
na majukumu yake mengine usiku huo.

Wakati Kado na mgeni wake wakiachana,
huko posta katika jengo moja la siri, kulikuwa
na kikao cha watu watatu, kikao hicho
kilikuwa kimedumu zaidi ya saa moja na
muafaka ulikuwa haujapatikana kabisa.

Kikao kilijumuisha watu wenye weledi na
wajanja wa kila kitu katika nyanja ya ujasusi,
lakini usiku huo walikuwa wamekwama
kwenye jambo dogo lakini lenye masilahi
makubwa sana.

Kilikuwa na Kobelo, Honda pamoja na
mwanadada pekee ndani ya idara ile ya siri,
mwanadada Mina.

“ Hizi bahasha zote zimeandikwa “F3” kisha
kila bahasha, ina wino wa kalamu uliondikwa
kwa mkono na ni namba mbili kila bahasha,
lakini hizi zipo nne!” Kobelo alizungumza.

“Kwa hiyo unadhani hapa alitaka kumaanisha
nini, mana zote zimetokea sehemu tofauti
katika matukio ya aina moja!” Mina nae
alisema.

“Na hapo ndipo hatujajua lengo lake hasa ni
nini!” Honda nae alisema.

“Hakuna lengo zaidi ya kutupatia ujumbe
fulani, lakini tatizo hatujui ujumbe gani!”
Kobelo aliwambia wenzake.

“Hapo ndo pagumu sasa!” Mina alisema.

“Ujumbe wake wa mwisho, alitoa haya
maneno “my public IP …” bila kuweka wazi ni
namba ngapi,lakini pia aliandika ‘decode,
otherwise it’s not a menu you deserve’. Bila
shaka inaleta picha fulani” Honda aliwambia
wenzake huku akiwapa bahasha alioikuta
kwenye pikipiki yake.

“ina maana tukishindwa kuelewa code hizi, sio
ujumbe unaotuhusu!” Mina aliongea huku
akiishika ile bahasha.

“Ndio mana yake!” Honda alijibu.

“Kwa nini!” Kobelo alihoji.

“Kwa sababu alinipa ujumbe kwenye msiba
wa Mwendampya, lakini nilifika uwanjani na
bado mtu aliuwawa mbele yangu, hivyo
ilitakiwa nimwachie mtu aliestahili!” Honda
alijibu.

Kobelo na Mina walishangaa.

“umezungumzia ujumbe wa uwanjani, vipi
umefanikiwa kujua mmliki wa gari yenye hizo
namba?” Kobelo alimuuliza Honda.

“gari inamilimikiwa na timu ya mpira ya Azan,
Azan football club.” Honda alijibu.

“ Ukitizama vizuri, matukio haya yameanzia
hapo, alianza kocha na kufuata afisa habari,
huoni kama ni mipango ya timu?” Kobelo
alitoa hoja.

“Tatizo sio mipango ya timu, tatizo ni hizi code
za huyu jamaa, lakini pia anahusikaje na
mambo haya?” Honda alirejesha mjadala.

“Hebu tuanze kuzipanga hizi bahasha, kuanzia
ya kwanza hadi hii ya mwisho!” Mina
aliwambia wenzake.

“Zile mbili za kwanza, tunapicha zake, mana
koplo aliuwawa na zikapotea, uzuri alikuwa
ameshatutaarifu mapema.!” Kobelo aliongea
huku akifungua simu janja yake na
kuwaonesha bahasha zile.

“Ndo tuzipange sasa, kisha tujue hii ndo
inaweza kuwa IP yake na kama ni IP, ina
maana amewahi ama amehudumu ndani ya
idara ya usalama wa taifa.” Mina aliongea
huku akianza kunakili zile namba zilizokuwa
zimeandikwa kwa mkono juu ya bahasha.

Alipomaliza kuandika, alikutana na namba
zikiwa nane, huku zikitenganishwa na alama
ya kituo, kila baada ya namba mbili, hivyo
kufanya kuwe na makundi manne yenye
namba mbili mbili.

Ilikuwa hivi…

69.44.24.17

“Ina maana ujumbe wake wote, upo kwenye
hizi namba.” Honda aliongea huku akizitizama
kwa makini sana.

“Usihahau kuna ile ‘F3’,” Kobelo
aliwakumbusha.

“Hapana, mi nadhani ili uifikie F3, lazima
uelewe ujumbe ulioko hapa kwenye hizi
namba.!” Mina nae aliongea.

“Bado nakubali kwamba, hizi ni namba za
utambulisho, lakini zimezidi namba halisi
zitolewazo idarani” Honda aliwambia
wenzake.

“Upo sahihi, hebu tuzigawanye katika
makundi mawili.” Kobelo aliongea huku
akichukua kalamu na karatasi, kisha aliandika
hivi…

69.44 kundi la kwanza.

24.17 kundi la pili.

Alipomaliza, aliwatizama wenzake.

“hapa nadhani tutakuwa tumegawanya vyema
hizi namba, na taratibu tunaanza kuingiza
maana katika utambulisho wake!” Kobelo
aliongea huku akisogeza karibu laptop yake.

Aliingiza namba za kundi la kwanza, alijaribu
kutafuta mmiliki wa namba zile katika idara ya
usalama wa taifa, lakini laptop, ilionesha
hakuna mtu katika mfumo wa malipo mwenye
zile namba, hata alipojaribu kwa wana
usalama walioacha, kufa na wengine kustaafu,
huko kote aliambulia patupu.

Aliingiza namba za kundi la pili, napo
aliambulia patupu, kulikuwa hakuna namba za
aina ile katika utambulisho wa wana usalama
wote.

Kobelo hakukata tamaa, aliamua
kuzibadilisha zile namba, ambapo; namba za
kundi la kwanza alizichanganya na namba za
kundi la pili, kwa kuchukua namba mbili za
kundi la kwanza, na namba mbili za kundi la
pili.

Lakini hadi anazimaliza namba zote, hakuwa
amefanikiwa kuambua lolote lile.

“Hii ngoma si ya kitoto hata kidogo” Kobelo
aliwambia wenzake.

“Zimegoma!” Honda alihoji. Kobelo alitikisa
kichwa kukubali.

“Hebu jaribu kuzipindua” Mina alishauri.

“Nimepindua na kubinua, lakini haijaleta
jawabu!” Kobelo alijibu.

Mina alishusha pumzi.

Honda alifikiria kwa muda wa dakika tano,
kisha aliomba karatasi na kalamu, ambapo
alipewa na kisha alianza kuandika tena zile
namba kwa mtindo tofauti, aliandika kwa
kushuka chini, huku akizibadilisha, kwa
kuchukua za namba za kundi la kwanza zilizo
mwisho na kuziweka mwanzo, na zile za
mwanzo, akiziweka mwisho.

Yani 69.44, yeye aliandika 44.69. Huku zile za
kundi la pili nazo akiziandika hivyo hivyo, kisha
aliandika kwa kushuka chini katika mpangilio
ule ule, na kuziweka pamoja namba za
makundi yote.

Aliandika hivi …

44
69
17
24.
Kisha alichukua namba za upande mmoja
zikiwa zote nne, na kuzitenganisha na namba
za upande wa pili zikiwa zote nne, ambapo
alipata namba hizi..

4612 kundi la kwanza na 4974 kundi la pili.

Kisha akampa Kobelo azitafute.

Kobelo alianza kwa kuchukua namba za kundi
la kwanza na kuziingiza, hapo aliambulia
patupu.

Aliingiza namba za kundi la pili na hapo
alipata majibu ya kile walichokihangaikia.

“Done!” Kobelo aliongea huku akishugulika na
kicharazio kwa kasi kubwa, kisha akawageuzia
wenzake nao waone kile alichokiona.

Kulikuwa na picha ya kijana mwenye umri,
yapata miaka thelathini na tano, alikuwa ni
usalama wa taifa miaka kumi iliopita, lakini
kulikuwa na alama ya mkasi sehemu iliohitaji
kuoenekana uhai wake ndani ya idara, na hiyo
ilimaanisha, alikuwa hayupo tena kwenye
mfumo na pia hakuwa hai, mana angelikuwa
hai na si mfanyakazi, ilimaanisha alitakiwa
awekewe alama nyeusi tu.

“Alishafariki huyu jamaa!” Honda alisema
huku akiitizama kwa makini sura ile.

“Sasa nani anaetumia namba yake? Au
ujumbe una maana ya kumtafuta huyu
jamaa?” Kobelo nae aliongezea.

“Hapana, huyu hatafutwi, bali kuna ujumbe
muhimu yupo nao, au anaweza kuwa taarifa
za msaada.” Honda alijibu.

“Kwa nini sasa tumewekewa mkasi?” Mina
alihoji.

“Kitengo kina mengi, huwezi jua.” Honda
alizungumza huku akiendelea kupekua taarifa
kadhaa kwenye laptop.

“Reason behind, naambiwa Dismissed” Honda
aliwambia wenzake.

“Sasa kama ni kupotea, kwa nini aandikiwe
hayupo hai!” Mina alihoji.

“Yawezekana faili lilifungwa, kwa kuwa
hawakumuona, au walimpoteza wenyewe kwa
kwa sababu walizozijua!” Honda alitoa maoni
yake.

“Jina lake ndo hilo Sospita Kado!” Mina alihoji.

“Ndo jina lake! Kobelo alimjibu.

“it’s sounds like he’s alive!” Mina aliongezea.

“Yes, na yawezekana hiki kinachoendelea
kikawa kina mhusu moja kwa moja.” Honda
aliongea.

“Yote yanawezekana” Kobelo alisema.


Ulipita ukimya mfupi, kila mmoja alikuwa
akiwaza lake.

“Sasa turudi kwenye hii F3, ina maana gani
sasa!” Kobelo aliwakumbusha wenzake.

Ni ngumu sana kuilewa hii kitu kwa haraka
namna hii, bora nianze na huyu Kado kwanza”
Honda alimwambia Kobelo.

“No, mi naona kama uende Patandi hivi!”
Mina alimwambia Honda.

Honda alishituka na kumkazia macho.

“Una maanisha chuo cha ualimu na kwaya?”
Honda alihoji.

“yes, chuo cha lugha za alama” Mina alijibu.

“Ooho mbona mnataka kuniacha njiani
ndugu!” Kobelo aliingilia.

“Tuna maanisha hiyo F3 ni tone ya muziki.!”
Mina alimwelewesha Kobelo.

“Kati yenu yupo, manamuziki?” Kobelo alihoji,
hakuwa na imani na mawazo ya Mina.

“Miezi sita nilikuwa ndani ya Tanzania house
of Talent!” Mina alimjibu Kobelo.

“Ulikuwa unafanya nini!” Kobelo alimhoji
Mina.

“Muda mrefu na ilikuwa ni kazi, ikanibidi
nijifunze muziki ili kupata lengo kirahisi!” Mina
alimjibu.

“Basi upo sahihi, kama waujua muziki inabidi
Honda aende Patandi, avunje code hiyo ya
Muziki.” Kobelo aliongea huku akimtizama
Honda.

“Kama ndivyo, huyu jamaa somo la code
alilifaulu vyema sana aisee!” Honda alisema
huku akitikisa kichwa chake.

“Hii F3 haiwezi kutumika sehemu zaidi ya ala
ya muziki na huwa ni note muhimu sana
kwenye ala yoyote!” Mina alizidi kuwafunua
wenzake, kulinganana mafikirio yake.

“Kwa hiyo tuseme huyu jamaa ni muhimu
sana kumpata?” Kobelo alisema

“Bila shaka, mana hawezi kuwa hana jipya
katika mkasa huu” Honda alimjibu.

“Nadhani tunahitaji kujua zaidi hii F3, ili tujue
tunachoweza kuhusanisha hapa” Honda
aliongea huku akimwangalia Mina.

“Kwenye muziki kunakitu kinaitwa STAFF
NATION, ambayo ni mchanyanyiko wa alama
mbali mbali, za muziki zinazojenga lugha kwa
kuimba au kuisikia katika sauti ya chombo..
Alama hizo ni kitambulisho cha sauti za juu
ndani ya chombo cha muziki, kwa kitalaamu
tuinaita Treble au G Clif na kitambulisho hiki,
kinaanzia kwenye note ya G.” Mina
alinyamaza kidogo huku akimtizama wenzake.

“Sasa hii F3 inatabia ya kutumika kutengeneza
mduara kwenye treble clef, ambayo ndio
tunapata not G…” Mina alinyamaza baada ya
kuona Honda anataka kuzungumza jambo.

“ Najua hapa tutatoka kapa, lakini
nimegundua huyu jamaa pia ni mjuzi wa
muziki, na anajua kabisa tukiifunua hii code
yake, basi ni rahisi sisi kujua wahusika wa hizi
hujuma za rejareja..” Honda alizungumza.

“Lakini kuna kitu nimeelewa, kwamba hii F3
inatengeneza marudio kwenye not G, naona
kuna ujumbe hapa jamani.” Kobelo alisema
huku akijaribu kufikiria.

“Sasa huyu G, tuseme ni mkubwa kwa F3 sio!”
Honda alihoji.

“Hapana, ili G awepo, anahitaji muundo wa
F3,ili kujizungusha katika not mbalimbali
ikiwemo bass clef” Mina alijibu.

“Sasa tuseme, huyu mtu ni mpiga ala za
muziki, lakini anategemea wengine kupata kile
anachohitji, lakini watu wenyewe anawapata
kwenye huo huo mzunguko…” Honda alijaribu
kuhusanisha matukio na maana ya ile F3.

Tuseme ndo hivyo, lakini bado jibu linabaki
kwa Kado, yeye anajua yote haya…” Kobelo
aliunga hoja, huku akirudisha mjadala kwa jina
la Kado.

Honda alitizama saa yake..

“Hivi sasa ni saa tano kamili usiku, utanibidi
nitembelee sehemu nyingi zenye miziki ya ala”
Honda alisema huku akianza kujiweka sawa
kwa kuondoka pale ofisini.

“Naona uanzie Violin Pub.” Mina alimshauri
Honda.

Honda aligeuka ili ahoji, lakini Mina aliwahi
kuelewa na kumwelewesha.

“Hapa kuna gari, namba zake zinamilikiwa na
timu ya mpira ya Azan, lakini mmoja ya
wamiliki wa Azan ni Balozi na Rpc msataafu
Masawe; Violin Pub nayo inamilikiwa na
Masawe akiwa na swahiba wake D. G
msataafu, Kihengu ambae nae anaimiliki Azan
football club…. Huoni maana hapo?” Mina
alimalizia kwa kuhoji.

“Duh, kama inaleta maana hivi” Honda aliitikia
huku akianza kuondoka ndani ya ofisi ile ya
siri.

******

Honda akiwa kwenye operesheni yoyote,
huwa anapenda sana kutumia pikipiki,
akiamini inarahisisha zaidi na kumuwahishia
muda, kutokea sehemu moja kwenda
nyingine.

Hata usiku huo alitumia pikipiki yake, pia
ilikuwa ni usiku na barabara nyingi zilikuwa
wazi, hivyo alitumia dakika chache kufika
Violin Pub, kisha alishuka na kuacha pikipiki
yake ikiwa eneo maalumu la maegesho na
chini ya uangalizi wa walinzi wa kampuni
fulani.

Honda aliungana na watu wengine ambao
walikuwa wanaingia ndani ya Pub, huku
wakipishana na watu kadhaa waliokuwa
wametosha burudani, ama walikuwa
wanahamia viwanja vingine vyenye burudani
zaidi ya ile waliokuwa wanapata ndani ya
violin pub .

Honda alipoingia ndani ya Pub, alikutana na
taa zenye mwanga hafifu, lakini pia aliona
baadhi ya maeneo yakiwa giza kabisa licha ya
kuwa na watu waliokuwa wakifurahia ulabu
na burudani kutoka kwenye spika zilizofungwa
kila kona na kuunganishwa na jukwaa la
wapiga ala za muziki kufuatisha nyimbo
maarufu, ndani na nje ya nchi.

Honda alitafuta sehemu nzuri alioona inamfaa
kwa muda huo, sehemu ambayo alihakikisha
kila aneingia ama kutoka, anamuona. Pia
sehemu ambayo hawezi kupitwa na tukio
lolote linaloendelea kwenye jukwaa la wapiga
ala, ambapo wakati huo kulikuwa na mpiga
fidla maarufu kwa uvaaji wake wa sweta na
kufunika kichwa chake, huku akiwa
amezimiwa taa zenye mwanga mkali na kubaki
zile zenye mwanga hafifu.

Kwa muda mchache ambao Honda alikuwa
amekaa pale, aligundua mpiga fidla anakonga
nyoyo za watu wengi, mana kila mara watu
walikuwa wanaenda kumtuza na wengine
kujumuika kucheza na baadhi kupiga vifijo
pale ambapo mpigaji aliwakuna hisia zao.

Hilo ndilo jambo lilomfanya Honda awe
makini zaidi, mana mpiga fidla alionekana
kuijua vyema kazi yake, lakini pia aina yake ya
uvaaji.

Jamaa hata alipokuwa akiruka kutoka sehemu
moja kwenda nyingine, kofia iliokuwa
imeungana na sweta, haikuweza kuvuka
kabisa na haikuwa rahisi kumuona sura yake.

Honda aliwaza jambo, alihitaji kumuona
bwana yule, hivyo aliamka na kwenda
kumtuza mpiga fidla, akiwa na lengo la
kumsogelea karibu zaidi.

Alishika noti ya shilingi elfu tano, alijiunga na
wadada wawili waliokuwa wanayarudi, huku
wakipunga noti zao hewani kwa nia ya
kwenda kutuza jukwaani.

Honda macho yake yalikuwa makini sana,
lakini kitu ambacho hakujua ni kuwa, mpiga
fidla alikuwa amemuona tangu alipojiunga na
wadada, hivyo alipofika karibu ni wakati
mpiga fidla alipogeuka gafla kuwatizama
wapiga dram waliokuwa nyuma yake, lakini
aligeuka kwa mbwembwe nyingi kiasi zilisikika
sauti za watu wakishangilia.

Honda akawa amekosa lengo lake, lakini
kuna kitu alikiona na kilimfanya atimize lengo
zaidi ya alivyotegemea.

Honda aliona kitako cha fidla kikiwa na herufi
moja na namba, yani F3.

Lakini alipozidi kulikagua jukwaa, aligundua
vyombo vingi vilikuwa vimeandikwa alama
mbali mbali za kimuziki.

Lakini bado alibaki kwa ile fidla alioiona, alijua
kabisa ina mahusiano na ile F3 ya kwenye
vibahasha.

Honda hakujua kwa nini aliwaza hivyo, lakini
aliamini kabisa yupo kwa mtu sahihi.

Honda alituza pesa, kisha aligeuka na
kuondoka na kwenda kukaa kwenye kiti
alichokuwa amekalia mwanzo.

Macho yake hayakubanduka kwa mtu mpiga
fidla, hapo tena alifahamu jambo ambalo
hakuwa amelitilia shaka mwanzo.

Miondoko na midondoko ya kiuchezaji ya
yule mpiga fidla, haikuwa kama ile ya mpigaji
wa kawaida, alieamua kutia mbwembwe.
Huyu alikuwa anaondoka na kusimama kwa
mtindo maalumu, lakini pia alikuwa anauwezo
wakutunza pumzi na bila kuchoka, mikono
yake ilikuwa kwenye ubora ule ule wa
kucharaza fidla, bila kuonesha mchoko wala
viungo vingine havikutetereka kabisa.

Honda aliyaona yote hayo na hapo akawa
makini sana na kutazama aina ya uchezaji wa
mpiga fidla.
 
07
Dakika tano badae, Honda alikuwa
anahitimisha kwa kumuona bwana yule si wa
kawaida, ni mtu mwenye ujuzi mkubwa zaidi
ya upigaji fidla.

Honda aliendelea kumtizama, hakutaka
kubandua uso wake kwa mtu yule.

Honda aliamini kuna kitu cha ziada kwa mtu
yule.

***

Honda aliendelea kuvuta subra ambayo
ilimletea heri; mtu yule alishuka kwenye
jukwaa na kuelekea upande fulani, upande
ambao Honda aliona watu wengi wakienda na
kutoka,hivyo alijua kule ni maliwato na ndiko
mpiga fidla alikuwa anaenda, jukwaani
alikuwepo mpiga piano na aliendelea
kucharaza piano na kuzidi kuwakonga nyoyo
wageni kutoka nchi za magharibi, ambao
walipenda aina ile ya muziki, huku wenyeji
kutokea nchi zetu za kiafrika wakiwa
wamepoa kwa kutoelewa midundo ya piano
na utamu wake.

Honda alinyanyuka na kuelekea kule
maliwato, alipishana na watu kadhaa ambao
walikuwa wanaingia na kutoka.

Honda alikutana na korido pana ya kupitisha
watu zaidi ya wanne, korido ile ilitenganisha
vyoo vya wanawake na wanaume, ambapo
upande wa kulia kulikuwa na vyoo vya
wanaume upande wa kushoto kulikuwa na
vyoo vya wanawake. Mbele ya korido ile,
kulikuwa na vyoo vilivyokuwa vimebainisha
kutumika kwa wahusika na wafanyakazi wa ile
Pub.

Honda alijua mpiga fidla atakuwa kwenye vile
vyoo vinavyomhusu.

Honda alipiga hatua zake kwa utulivu
mkubwa, akiruhusu akili yake inase tukio
lolote, kutokea upande wowote.

Alipofika kwenye mlango wa vyoo vya
wafanyakazi, alikunja kulia ambako
kulibainisha kutumiwa na wafanyakazi wa
kiume.

Alianza kukutana na milango upande huo,
mara macho yake yaliona choo kimoja kikiwa
na tangazo “Hakitumiki”. Honda alitizama
choo kile, hadi alipoona hakuna jipya ndani ya
vyoo vile kwa kuwa alikuwa ameona hakuna
mtu kwenye vyoo vile, kulikuwa kimya sana.

Alitaka kukata shauri kuondoka, lakini alihisi
kusikia sauti ya mdondoko wa kitu kwenye
choo kile kisichotumika.

Atega sikio vyema, lakini alisikia miguno zaidi
na vishindo vya hapa na pale.

Honda hakuwa mgeni wa vishindo vya namna
ile, alijua kuna watu wameweka mchapo huko
maliwatoni.

Honda aliusukuma mlango kwa nguvu na
kuingia ndani kwa kasi kubwa, kisha aliruka
sarakasi moja na alipotua chini, aliserereka
kwenye vigae vilivyolowa maji na kuwapita
watu wawili waliokuwa wamepigwa na butwa
kwa uvamizi ule.

Mtu mmoja alikuwa nj yule mpiga fidla, huku
mwingine akiwa ni mgeni kabisa machoni
mwake, alikuwa amevaa prova nyeusi na
usoni akiwa ameziba na kitambaa
cheusi,mikononi alivaa glavu nyeusi; kifupi,
alikuwa amevaa mavazi meusi kuanzia juu
hadi chini.

Honda alisimama na kuwatizama vijeba wale,
ambao walionekana kutoana jasho kwa muda
kidogo.

Licha ya Honda kuingia kwa mbwembwe,
lakini alishindwa kujua amshambulie yupi,
mana alikuta watu wanachapana, lakini
hakujua sababu ya wao kufanya hivyo.

Honda alipiga akili ya haraka, aliona kama
mpiga fidla ni muhimu zaidi, lakini pia alitaka
kuthibitisha kama anaweza kuwa na msaada
kwake na kama anajua elimu ya code.

Honda alitaka kujua kati ya mpiga fidla na
mwenye nguo nyeusi, ni nani alikuwa ana
msaada zaidi, hivyo alipanga kutamka maneno
fulani, ambae angejibu ndie alistahili kupewa
msaada.

“Black or white!” Honda alisema, huku akiwa
makini na matendo ya wale jamaa, wasije
kumhujumu.

“White with benefits!” Mpiga fidla alijibu.

Yes, ndio jibu alilohitaji Honda, na hiyo
ilidhihirisha mpiga fidla ndie haswaa,
aliemfikisha pale na kama ndivyo, basi alihitaji
msaada na si ajabu mwenye nguo nyeusi
alitaka kumhujumu tu.

Honda alielekeza macho yake kwa mtu
alievaa nguo nyeusi, mpiga fidla nae alielekeza
macho yake kwake, hapo ndipo aligundua
hayuko sehemu salama, hivyo alifanya tukio
gumu kusimulika, lakini alilenga kujiokoa.

Bwana yule alimtizama Honda kisha
alimtizama mpiga fidla. Aliona walivyomakini,
hivyo akataka kuwapotezea umakini; alijifanya
kama anataka kumfuata Honda, hapo aliona
namna mpiga fidla alivyomakinika, lakini
alimwona Honda alivyojipannga kumpokea, ila
yeye aliamua kufanya kinyume cha matarajio
yao, kwani aliachana na Honda, akapaa
hewani huku akimkanyaga mpiga fidla kifuani,
kisha alijirusha kwenda choo cha pili.(vyoo vile
vilikuwa wazi upande wajuu) huko alitua
salama, kisha alifungua mlango kwa kasi na
kutoka nje.

Honda na mpiga fidla walitoka kwa kasi
kubwa, lakini walikuta yule bwana
ameshakutana na giza la Pub na wasimuone
tena.


Mpiga fidla alimshika mkono Honda ambae
alikuwa anataka kumfuata bazazi yule.

“Huwezi kumpata, na hata ukimpata, sio
chakula chako kile!” Mpiga fidla alipmwambia
Honda.

“Naitwa Kado, najua hadi umefika hapa,
umelijua jina langu, tuonane nje baada ya
dakika mbili, kaa kwenye pikipiki yako” Mpiga
fidla alimwambia Honda huku akipiga hatua
na kuishia kwenye ngazi za jukwaa.

Honda aliondoka pale ndani na kuelekea
alikoacha pikipiki, huko hakuhitaji kujificha,
bali alikaa akimsubiri Kado.

Umakini wake ukiwa mara dufu, ili asije
kuhujumiwa, hakuwa ameweka imani kubwa
kwa kado.

****

Baada ya dakika mbili, Kado alitokea huku
akiwa amevua lile sweta lake, alivaa shati
jeupe na tai huku akiwa amevalia suruali
nyeusi na viatu vyeusi.

“Umefanya kazi kubwa, unastahili kuitwa
jasusi hodari!” Kado alimwambia Honda huku
akirekebisha tai yake.

Honda alikaa kimya..

“Kunipata mimi kwa njia ile, basi unazistahili
hizo sifa, mimi nadhani nikuache umalizie kile
nilichokianza.” Kado alizidi kuongea na Honda.

“Twende kwangu, tumia usafiri wako.” Kado
alimwelekeza Honda.

Honda nae alipanda kwenye pikipiki na
kuiondoa kwa kasi kubwa.
Njia nzima, hakuna aliemsemesha mwenzake,
zaidi ya mara chache Kado kumwelekeza njia
ya kupita.

Baada ya mwendo wa dakika kumi na tano,
hatimae Kado alimwelekeza Honda sehemu ya
kuegesha pikipiki, kisha walitembea kwa
miguu kuelekea nyumbani kwa Kado.

Ilikuwa ni nyumba ya kawaida, kulikuwa giza
nyumba nzima.

“Huwa nakuja hapa mara chache sana, lakini
ni sehemu sahihi kuwepo muda huu” Kado
alimkaribisha Honda kwa maelezo hayo, huku
akiwasha taa ya ndani.

Ajabu haikuwa nyumba yenye vyumba, bali
ilikuwa ni nyumba ilio kama gala, kwa kuwa
haikuwa na chumba hata kimoja.

Lakini ukutani, kulikuwa na picha za watu
kumi na mbili, na baadhi yao walikuwa
wamemewekewa alama za mkasi, kwa rangi
nyekundu.

Honda alisogea hadi pale kwenye ubao
uliokuwa na picha, alizitizama zile picha kwa
tuo, watu wote kwenye zile picha
aliwafahamu.

Kuna watu nane walikuwa wamekufa vifo
tata, na kuna watu wanne walikuwa wapo na
waliwahi kuwa viongozi wakubwa serikalini.
Honda aliachana na ubao wa picha, aligeuka
kuangalia mazingira ya gala lile, ambalo kwa
nje ni kama nyumba ya kawaida.

Aliona kuna kiti cha mbao, begi la nguo
lilokuwa limetundikwa ukutani, kulikuwa na
sanduku la chuma likiwa chini.

“ Kama kuna vitu vya muhimu, huoni kama
unaviuza kwa bei rahisi?”Honda alimuuliza
Kado.

“Sijawahi kuwa mjinga kiasi hicho kamanda!”
Kado alijibu.

Honda alibaki akimtizama, kisha alimuuliza.

“Kwa nini ulinilenga mimi?”

“Sikukulenga wewe, bali yeyote atokae
kwenye kitengo chenu, ambae angekuja
kushugulika na zile bahasha.” Kado alijibu.

“Umeweza vipi kuniamini” Honda aliuliza.

“Kwa sababu ulianza harakati za kufuatilia
vibahasha, pia nilipokufuatilia ndio nikakujua
kiundani zaidi, sifa zako zipo Dunia nzima”
Kado alimwambia Honda.

“Yule jamaa mliewekeana mchapo ni nani?”
Honda alihoji.

“Utamjua nikishakukabidhi kazi rasmi” Kado
alijibu huku akujishugulisha kuweka sawa,
karatasi fulani mkononi mwake, kisha alimpa
Honda.

Honda alianza kuzisoma karatasi zile,
alipomaliza ni kama hakuelewa hivi.

“ Hapa naona balozi wa Canada, balozi wa
Tanzania, hii inahusu nini zaidi.” Honda
alimhoji.

“Ulichosoma ni mkataba, mkataba ambao
ulizua uovu mioyoni mwa wanene serikalini.”
Kado alimwambia Honda.

“Kwa hiyo kontena ndio chanzo!” Honda
alihoji.

“Yes ndio chanzo.” Kado alimjibu Honda huku
akianza kumpa dondoo kamili za mkasa ule,
uliokuja kuondoka na uhai wa watu kirejareja.

*Miaka Kumi nyuma

Balozi wa Tanzania nchini Canada, bwana
Werema Masawe, alikuwa nchini Tanzania
kwa likizo ya mwezi mzima.

Likizo yake hii Ilikuwa inaenda kidogo kidogo
na hakuona kama inaisha, kwa kuwa alikuwa
na jambo ambalo aliona lina manufaa
makubwa sana kwake. Jambo lililozua tamaa
moyoni mwake.

Kila siku, bwana Masawe alikuwa anafungua
mkoba wake na kutoa nyaraka fulani
zilizohitaji muhuri wa rais ili zirudi Canada
kushugulikiwa.

Bwana Masawe alipiga akili yake vizuri, kisha
alinyanyuka kwenye kiti na kwenda chumbani
kwake. Alichukua simu yake na kuchagua jina
fulani,jina lile lilikuwa na namba za mtu
kutoka Rwanda.

Masawe alizipiga.

“Muda mrefu sana hatujawahi kuongea
Masawe” Alisema mtu upande wa pili.

“Hakika bwana Rugera!” Masawe nae alisema.

“Bila shaka ni habari njema hizi!” Rugera
alimwambia Masawe.

“Ni njema, lakini zina msafara kidogo!”

“Kivipi Masawe!”

“Nina karatasi hapa za moto sana, lakini naona
kama sitazintendea haki hivi!”

“Karatasi!? Hebu nifafanulie”

“Kuna mzigo wa silaha na unga wa kuunda
mabomu, lakini nataka nikugawie, mana
uliniomba siku nyingi sana, tangu nikiwa Rpc!”

Rugera alinyamaza kidogo, kisha
alizungumza…

“Huo mzigo unatoka wapi?”

“Canada!!”

“Ooh my God, Tanzania inapata modified
weapons!?” Alishangaa Rugera, mana
hakutegemea kusikia Canada ambayo
imekuwa maarufu siku za karibuni, kwa
kutengeneza silaha zenye ubora mkubwa
katika soko la silaha. Alishagaa kusikia nchi
jirani ya Tanzania ndio inayotarajiwa kupewa
silaha na serikali ya Canada.

Hakika haikuwa vizuri, aliona ni kama
Tanzania inazidi kupiga hatua kwa misaada ya
kijeshi.

“Kwa hiyo ulitaka ngapi vile!” Rugera alihoji.

“Ni kontena sita, lakini kontena moja
nakupatia na lina unga wa mabomu mazito.
Hivyo nipe Bilioni mia tatu.” Masawe aliongea.

“Unaonaje nikikupa bilioni mia tano na wewe
ukanipa kontena mbili za aina hiyo?” Rugera
alimshawishi Masawe.

“Tutazungumza zaidi, ngoja niendelee
kuliweka sawa jambo hili.” Masawe alijibu.

Yalifuata mazungumzo machache, kisha
Masawe alikata simu.

Alikuwa anaongea na waziri wa ulinzi wa
Rwanda.

Masawe alipotoka chumbani kwake, aliamua
kwenda kwenye mgahawa mmoja nje kidogo
na nyumbani kwake.

Huko alitaka kwenda kuonana na Mkurugenzi
wa usalama wa taifa, bwana Wambura
Kihengu.

Alipanga kumshirikisha katika suala lile,
walikuwa marafiki wa kushibana, hivyo
aliamini hatoweza kumripoti kwa rais hata
kama wasipoelewana.

Masawe alifika kwenye ule mgahawa na
kuagiza supu ya kongoro na chapati nne.

Wakati anaendelea kula, swahiba wake wa
siku nyingi, bwana Wambura Kihengu, alikuwa
anaingia kwenye mgahawa ule.

Masawe alimkaribisha, kisha ulifuata utani wa
hapa na pale, kisha Masawe alitoa karatasi
alizokuwa ameziweka kwenye mkoba na
kumpa Kihengu.

Kihengu alizipokea na kuzisoma, kisha
alimtizama Masawe.

“Mzigo huu kwa nini unatembea nao?”
Kihengu alihoji kwa ukali kidogo.

“Tulia bwana,unadhani mimi ndo sijui
umuhimu wake?” Masawe alimjibu.

“Kama ungejua umuhimu wake, wala
usingezurura na nyaraka nyeti kama hizi!”
Kihengu aliendelea kushikilia misimamo wake.

“Unyeti wake naujua mimi, wewe sikiliza
nilichokuitia hapa bwana!” Masawe alimjia
juu Kihengu.

“Hivi unajua unaongea na nani?” Kihengu
alimhoji Masawe.

“Najua, Mkurugenzi wa usalama wa taifa, ndo
mana nimekuita kwa kulijua hilo” Masawe
alimjibu Kihengu.

“Naona unaanza kuwa kichaa sasa!” Kihengu
alimwambia Masawe.

Masawe alitazama kushoto na kulia, aliwaona
walinzi wa Kihengu, kisha aliongea kwa sauti
ndogo ili wasisikie.

“Wewe ndo kichaa, mana unatembea na
waangalizi, ili ukizingua tu, Milembe.”

Kihengu alicheka kwa sauti, huku akiwatizama
vijana wake, waliokuwa hatua mbili nyuma
yake, na wengine walikaa meza za jirani
kuhakikisha usalama wa bosi wao.

“Umeniitia nini sasa, mana naona karatasi tu.”
Kihengu alihoji huku akiwa ameweka mbali
masihara.

“Mi naona hizo zikisainiwa na rais, ni pesa
kubwa tunapiga Kihengu” Masawe alianza
ushawishi.

“Sijakuelewa Masawe”

“Namaanisha, kwenye hizo kontena saba za
silaha na unga wa kutengenezea mabomu,
tunaweza kuzuia kontena mbili na kupiga pesa
nyingi sana”

“Tangu lini umaeanza upigaji?”

“Mi nimepiga sana tu,tangu niko Rpc na mali
zote unazoona ni za upigaji, mshahara
unadhani ningemiliki hata bajaji?”

“Aisee! Mbona hatari hii, kama na wewe
mpigaji…”

“Sikia Kihengu, kuna bilioni mia tano kwa hizo
kontena, je unaona ni vyema ususbiri kiinua
mgongo au unataka uneemeke,acha ujuha
bwana”
Kihengu alinyamaza akimtizama Masawe.

Mbona kontena mbili hazin thamani kubwa
kiasi hicho?” Kihengu alihoji.

“Hapa zinapanda thamani kwa matumizi yake,
mana zinaenda kubadilishwa na dhahabu ya
Congo.” Masawe alijibu huku akibugia pande
la mnofu.

“Una maanisha, tunawauzia waasi ili tupate
vipande vya dhahabu?”

“Hapana, tunamuuzia jamaa fulani kutoka
Rwanda, ila yeye ndie anaezipeleka huko
Congo”

“Rwanda?” Kihengu alishangaa.

“Ndio, Rwanda” Masawe alijibu.

“Huoni kama tunafanya jambo la hatari kiasi
fulani?” Kihengu alionesha wasiwasi.

“We achana na wasiwasi, yule anafanya hii
biashara miaka mingi sana, hivyo sio rahisi
kabisa, kufanya unachofikiria”

“Lakini Warwanda hawaaminiki, na kuwauzia
silaha zetu, ni kama kuwapa ramani ya kila
kitu kinachohusu usalama wetu” Kihengu
aliendelea kutia ngumu.

“Hapana, mi nikikufikishia dili, ujue lina
usalama mkubwa sana, kikubwa tujadili bilioni
mia tano na namna ya kuzipata sasa!”

“Kwa hiyo rais akitia saini, huo mzigo
unasafirishwa?”

“ Ndio, tena mapema tu”

“Lakini huoni kama tunatakatisha pesa?”
Kihengu aliongea,Masawe alistuka.

“Hapa umesema kweli, sasa tunafanyaje?”
Masawe alihoji.

“Ina bidi timu iongezeke, peke yetu ni rahisi
kustukiwa bwana”

“Kwa hiyo unashauri uri iweje?”
“Najua mzigo utakuja kwa meli za kijeshi,
lakini bandarini kuna taratibu zake, hivyo ili
mzigo ubaki, lazima tuwe na mtu bandarini,
pia lazima vyombo vya ulinzi na usalama
vitakuwa na taarifa, hivyo lazima bosi mmoja
au wawili wajue, lakini pia ni lazima huo unga
uhakikiwe, hivyo mkemia wa serikali na yule
wa jeshi, wanatakiwa wahusike mana
hatuwezi kuuza mzigo usiothibitishwa na
serikali haiwezi kupokea mzigo kama huo bila
kuthibitisha ubora wake.”

Masawe aliguna.

“Mbona kama watu wanakuwa wengi,
tutafanikiwa kweli kupata pesa nyingi?”
Alihoji.

“Bado watu wataongezeka, mana kuna kitu
inabidi kifanyike ili tusistukiwe, inabidi pesa
hiyo ipite sehemu nyingi kabla haijarudi
mikononi mwetu, hivyo timu inakuwa kubwa
sana na lazima tujue hatutaitumia kwa siku za
karibuni, inabidi tutumie miaka kadhaa badae,
kwa kuwa tutakuwa tumefanikiwa kuziingiza
kwenye mzunguko halali.”

“Duh, mbona tutagawana bilioni tatu tatu
aisee!”

“Hapana Masawe, tunatakiwa kucheza
mchezo fulani huko mwishoni.”

“Mchezo gani?”

“Baadhi ya watu tukiwatumia, inabidi
tuwaondoe ulimwenguni, hadi mwisho
tutabaki wawili tu kama tulivyoanza”

“Hahaahaaaa….. Wewe Kihengu…haaaahaaa..
Unamipango ya kiusalama haswaa, afu nawe
mpigaji vile vile tusidanganyane uzalendo.”
Masawe aliongea kwa kufurahi sana.

“We bwege sikia, hata rais huyu aliepo ni
mpigaji mkubwa tu, na ndio mana alinipa hiki
kitengo ili niwe karibu nae na nimpe mipango
madhubuti ya upigaji.” Kihengu aliongea
taratibu sana.

“Aah, kumbe nae mpigaji, walahi hao
wanyonge nao waone na watu wa kuwapigia
kura Hahaaa.” Masawe alimalizia kwa cheko
kubwa.

“Sasa hii timu tutaiundaje, mana inatakiwa
niwafahamu wote hawa wanaotakiwa kuwapo
kwenye huu mpango!” Masawe alimhoji
Kihengu
 
08
“Usijali, najua wapigaji ni kina nani kwenye
serikali hii na nitamtuma kijana wangu,
atawapa taarifa, kisha tutaenda kukutana”

“aah hapo sawa!”

“Lakini masawe, inabidi tuingie garama
kuanzia sasa” Kihengu alimwambia Masawe.

“Kivipi!”

“Unajua hizo pesa ni nyingi, hata tukizigawa
vipi, haiwezi kuepukika kujulikana, unaonaje
tukianzisha timu ya mpira, ambayo inatumia
pesa nyingi na tukaipa udhamini wa
kimagumashi ili kuingiza huo mzigo?”

“Wewe una mipango, naukubali huo mpango,
lakini ngoja kwanza tuuze mzigo.”

“Hapana, tukisubiri mzigo ipo siku
tutabwanwa kwa kuwa tutakuwa wamiliki wa
timu, na wataona tuihujumu ndo tukaanzisha
timu.”

“Unaona mbali sana, ngoja tutalijadili na
wajumbe wengine, ngoja niwasiliane na rais,
ili nimpelekee huu ujumbe”

***

Baada ya siku mbili kikao kiliitishwa, ambapo
kilihudhuriwa na Kihengu ambae alikuwa
mkurugenzi wa usalama wa Taifa, Bi
Mwendampya ambae alikuwa ni Rpc mkoa wa
Dar es laam (kabla ya kugawanywa katika
mikoa ya kipolisi). Kulikuwa na Masawe
ambae alikuwa ni balozi wa Tanzania nchini
Canada, kulikuwa na Juma Lilo, mkemia mkuu
wa serikali. Kulikuwa na Nzaya ambae alikuwa
ni mkurugenzi wa bandari ya Dar es laam na
wote hawa walikuwa wanafanya kazi usalama
wa taifa, lakini walikuwa wamegawanyika
vitengo tofauti kwa masilahi ya taifa.

Siku hii walikutana kwa lengo la kuhujumu
taifa, walitanguliza masilahi yao.

Kikao chao kilienda vyema na walikubaliana
mambo kadhaa.

Rejea Sasa*

Honda alitikisa kichwa kwa habari hiyo,
aliona kama utani vipepeo weusi kukengeuka
na kuingiwa na tamaa kubwa.


Lakini bado maswali yake, hayakuwa
yamejibiwa vyema na Kado.

“Sijaona uhusika wako hapo, pia sijaona kwa
nini kocha afe na huyu Sasi Eli.” Honda alihoji.

“Uhusika wangu upo hivi.. Wakati nayajua
haya, mi ndio nilikuwa mlinzi wa Kihengu na
mambo mengi alinitumia mimi, hata kuita
timu hii, niliita mimi na kwenye kikao
nilikuwepo na nilishiriki kuwandalia
mazingira.” Kado alinyamaza kidogo.

“Lakini mi na wao tulianza kukorofishana
baada ya kugundua wanataka kunihujumu”

“Kivipi yani!” Honda alihoji.

“Kuna siku moja, Nzaya alinifuata, alinambia
kuna mpango unasukwa kwa ajili yangu,
nilipotaka kujua, alinambia anataka nimfanyie
kazi na atanambia, mpango wenyewe ulikuwa
ni kuniua!”

“Kwa nini walitaka kukuua?”

“Nilifahamu mengi sana kuwahusu wao, lakini
pia hawakutaka nifike nao mwisho katika
safari ile, hivyo hawakutaka kuniamini.”

“Aisee!” Honda alishangaa..

“Yes, lakini pia Nzaya aliamua kunipa mipango
yake, ambapo nae alitaka kuwazunguka
wenzake, hivyo alitaka kunitumia kama kulipa
kisasi, lakini afanikishe malengo yake,lakini
binafsi nilitaka kuwakomesha wote, na ndicho
unaona nimekifanya na hapa nakupa taarifa
zao” Kado alimjibu Honda.

“Sasa ilikuwaje Kocha akafa?”

“Baada ya wao kuanzisha timu, walifanikiwa
kuuza mzigo wao, hivyo kupitia balozi wa
Tanzania nchini Canada, timu yao ilikuwa
inaenda kushiriki mashindano mbali mbali,
lakini mashindano mengi yalikuwa hewa,
hivyo zawadi za ushindi zilikuwa ni pesa
kutoka kwa balozi mwenyewe na zilitoka kwa
ile pesa haramu, ambayo ililipwa kwa akaunti
binafsi ya Masawe, akaunti hiyo iko Panama,
ambako kila mtu anajua ni sehemu ya kuweka
pesa haramu, hivyo kocha huyu aligundua huo
mchezo na alitishia kusema kwenye chama
cha soka nchini, kwa sababu waligeuka kuwa
watalii kila mara waliposafiri nje ya nchi” Kado
alijibu.

“Aisee! Inashangaza lakini” Honda alishangaa.

“Na kuhusu Eli Sasi, ni kuwa yeye alikuwa
anautaka urais, hivyo Kihengu alimfuata na
kumshirikisha, ambapo ili apate pesa za
kuanzia kampeni, ilibidi atangaze kuuguza tezi
dume, ambapo ilibidi aombe msaada, ambapo
watu kadhaa walijitokeza kumlipia garama za
matibabu, lakini watu wale walikuwa ni batili,
hivyo alilipiwa hotel na malazi, ambapo kwa
siku alitumia milioni mia mbili, sasa zidisha
kwa miezi sita, lakini pia zile pesa zilikuwa
zinaenda kwenye akaunti batili ya hospitali na
pia michango ilikuwa inaingizwa kwenye
akaunti yake, nae alikuwa anahamisha na
kuziweka kwenye ile akaunti, ambapo ilikuwa
ni akaunti ilioundwa kwenye diski mweko,
hivyo hakuna malipo, zaidi ya kuweka pesa
kwenye ile diski ili zirudi hapa nchini na
kuingizwa kwenye matumizi ya kutuo chake
cha kulea watoto yatima.” Kado alizidi
kumpasha Honda.

“Kwa hiyo aliuwawa kwa kuwa alikuwa
ameshatumika?” Honda alihoji.

“Yes, walikuwa wakikutumia, unageuka kama
kondomu, umeisha matumizi ni kutupwa”
Kado alijibu.

“Sasa wewe na Nzaya mipango yenu ilikuwa ni
ipi?” Honda alihoji.

“Kama upo makini, utagundua walikuwa
wanakufa wawili kwa siku, mmoja aliuwawa
kimkakati wa kikundi kile cha hujuma, lakini
mmoja aliuwawa kwa malengo ya kuzidi
kuwapunguza wote na mpango huu, upo chini
ya Nzaya, ambae ndie mtoa pesa na mpokea
pesa kwenye maeneo yote ambayo wanataka
na wameyatumia kuhifadhia pesa zao haramu,
lakini kitu kimoja ambacho Nzaya hajui, hata
yeye yupo kwenye hesabu na lengo la wote ni
kuwaondoa wote ili wabaki Kihengu na
Masawe.” Kado aliongea hivyo.

“Kwa nini sasa, faili lako linaonesha
ushakufa?” Honda alihoji.

“Yes, nilikufa. Mana waliichoma nyumba
yangu, na ndani alikuwemo mfanyazi wa
kiume, lakini bahati nzuri sikuwemo siku hiyo,
hivyo walijua nimekufa na tangu siku hiyo,
nikaishi nijuavyo hadi pale nilipopata kazi ya
kucharaza fidla kwenye ile Pub ya Masawe,
huku nikiwekwa pale na Nzaya kimkamkati.”
Kado alijibu.

“Kwa hiyo kila mtu, anajua umekufa?”

“Ndio, isipokuwa Mama yangu.”

“Sasa kwa nini kamanda wa Ilala ulimuua?”
Honda alihoji.
 
09
“Nzaya aliitaka hii diski, ambayo ina pesa
nyingi Sana, na pale alikuwa anaenda
kuikabidhi kwa Masawe ili utaratibu mwingine
ufuate, lakini Nzaya aliiona itamfaa, lakini
nilimpafeki, orijino ninayo na ndo hii.” Kado
alimwambia Honda, huku akibandua kitu
fulani ukutani na kutoa diski mweko na
kumkabidhi Honda.

“Mwanzo nilikwambia mi sio mjinga, hivyo
nani angejua kuna kitu ukutani?” Kado
alisema huku akicheka.

Wakiwa bado wanapeana habari, mara
mlango ukapigwa kwa nguvu na kufuatia risasi
mfululizo.

Honda aliwahi kuruka na kubiringita chini,
lakini Kado wakati anaruka alichelewa, risasi
kadhaa zilipita na bega lake na kwenda
kumrusha ukutani kwa nguvu.


Honda pale alipoangukia, aliachia risasi
ambazo zilikwepa kiufundi na mvamizi ambae
alimtabua kwa aina ya mavazi aliokuwa
amevaa.

Alikuwa ni yule aliekuta ameweka mchapo na
Kado chooni.

Honda aliishiwa risasi na yule bwana nae
risasi ziliisha.

Alikuwa ni Zozo, aliekuwa ametumwa
kuhakikisha mpiga fidla anaaga dunia.

Honda alichora ramani ya mchezo, Zozo nae
aliweka mchapo.

Ngumi zirirushwa kwa ufundi mkubwa, kila
mmoja akijaribu kukwepa na kurusha ngumi
kiustadi, hatimae dakika mbili zilikatika na
hakuna mshindi aliepatikana.

Honda aliamua kubadili aina ya mapigano .

Alianza kwa kumvizia Zozo, alimpiga kwa
umakini bila kuruhusu kushambuliwa, hadi
dakika mbili badae, Zozo alijikuta akishindwa
kuuzoea mchezo wa Honda, mana alikuwa
amepigwa maeneo nyeti na yenye kutia
udhaifu.

Zozo aliona akizubaa, atazikwa. Hivyo
alijipanga kisha akarusha teke ambalo lilienda
mbavuni mwa Honda na kumfanya ayumbe
kidogo, Zozo hakutaka kutoa nafasi, aliendelea
kurusha makonde kwa mfululizo, jambo
ambalo lilifanya Honda awe na wakati mgumu
kukwepa na makonde kadhaa yalimwingia
vyema mwilini mwake.

Zozo hakuwa wa mchezo, alijua aina nyingi za
mapigano, kiasi kumchanganya Honda kwa
aina hizo na jambo lile lilimuwia ugumu
Honda.

Lakini Honda nae huwa ana ujanja wake,
kwani alijua Zozo anatumia miguvu mingi,
hivyo alikubali kusurubika, ili amchoshe Zozo.

Hilo lilitimia, kwani alijisogeza pembeni na
kumwacha Zozo akitweta kutafuta pumzi
mpya.

Honda aliamua kutompa nafasi, alijirusha kwa
mtindo safi wa kimieleka, ulioitwa spear au
Roman spear. Ambapo alijiachia na
kumkumba Zozo kwa bega la kulia kisha
alimbwaga chini kama mzigo.

Zozo alivunjika mkono, hivyo kumfanya alie
kama mtoto mvivu.

Lakini licha ya kuvunjwa, bado alitaka kuleta
ubishi, hivyo Honda aliona akiendelea
kumchekea, atamachelewesha,
Haraka alimpa pigo moja katikati ya shingo,
lilikuwa pigo la kifo na Zozo hakuwa mbishi,
aliondoka na Uzozo wake, hakuwa na jambo
tena la kufanya duniani.

Honda alimgeukia Kado, aliekuwa amelala
chini na damu zikimtoka.

Alimuinua.

“Vipi, umeumia sana?” Honda kado, huku
akimtizama jeraha la risasi.

“Atakuwa kanivunja mifupa ya bega, hivyo
nahitaji tiba ya haraka” Kado alijibu huku
akigugumia kwa maumivu.

Haya twende basi” Honda alisema huku
akitaka kumbeba Kado.

“ Kuna bahasha ipo kwenye ule mkoba pale,
itakusaidia sehemu iliobaki, ambayo ni
kuwatia hatiani dhalimu wale” Kado
alimwambia Honda na Honda haraka alielekea
kwenye ule mkoba na kuichukua, kisha
akamrudia Kado.

“Niahidi kwamba hautafichua uwepo wangu
hapa duniani, nataka niishi kwa uhuru zaidi”
Kado alimwambia Honda.

“Usijali, kwa kazi hii unastahili kuishi utakavyo
na kwa mara ya kwanza kwenye uovu,
sijatumia nguvu kubwa, nadhani nastahili
kukulipa wema wako kwa nchi yako” Honda
alimwambia Kado huku akiondoka nae
kwenda nje ya nyumba ile na kumwacha Zozo
akiwa mzoga ndani ya nyumba ile katika nchi
ngeni.
 
10
***

Taarifa za kifo cha Zozo, kilimfanya Masawe
ashindwe kutulia, aliona kila kitu hakipo sawa,
na kibaya zaidi hakujua kama aliemuua ni yule
mpiga fidla anaefanya kazi kwa Nzaya ama ni
ofisa wa usalama wa taifa.

Aliona kama anazidiwa kete na karibuni
kitumbua chake kitaingia mchanga.alijiuliza ni
vipi kama dunia itatangaziwa ubaya wake.

Masawe aliwapigia washirika wake, kisha
aliwaomba wakutane ahsubuhi hiyo ndani ya
Violin pub.

Alipomaliza kuwataarifu, aliondoka kuelekea
huko.

Kitu kimoja ambacho hakujua, ni kuwa simu
yake ilikuwa imehakiwa, hivyo kila alichofanya
kilisikiwa vyema na Honda na wenzake.

Honda aliposikia wanaenda kukutana Violin
Pub, alijua anaweza kuwapata huko huko
wakiwa pamoja, ushahidi alikuwa nao wa
kutosha na walisitahili kupandishwa
kizimbani.

Honda aliwasiliana na kamishina Zenge wa
Zenge, ambae aliagiza Honda aongozane na
vijana kadhaa wa polisi, ambao wangeenda
kumsaidia jukumu la kuwatia pingu bazazi
wale.

---------

Masawe na Kihengu, walitangulia kufika,
kisha alifuatia Nzaya na Juma Lilo.

Kama kawaida walienda kukutana na kwenye
korido iliojificha ndani ya violin pub, ambayo
wakati huo haikuwa na kelele za muziki wa
ala.

Masawe aliwatizama wenzake kwa tuo, lakini
macho yake yaliishia kwa Nzaya.

“Kwa nini ulimleta yule mpiga fidla hapa
kwangu?” Masawe alihoji.

“Aah,nadhani tujikite kwenye suala letu
kwanza jamani” Nzaya alijitetea.

“ Hapa inabidi utujibu, mana haiwezekani
utuwekee mtu anetuua kila siku, hata sasa
kamuua Zozo!”

“What…!!” Juma alishangaa.

“Ndo hivyo Juma, Nzaya anatuzunguka, hata
ile diski ya hela anayo yeye..” Masawe
alimwambia Juma.

Nzaya aligwaya..

“Jamani naombeni tuwek..” Nzaya alitaka
kujitetea, lakini alijikuta akiangaliana bastola
kutoka kwa Masawe.

“Tulikubaliana, msaliti auwawe.. Sasa sijui
unataka kusema nini, naomba diski tafadhali”
Masawe alimwambia Nzaya.

“Nadhani upunguze jaziba, tunaihitaji diski,
afu tujue cha kumfanya huyu bwege” Kihengu
alimwambia Masawe.

Jamani mkiua hapa hadharani itakuwa ni doa,
doa la vipepeo, inatakiwa tufanye Mambo
kiweledi” Juma alishauri.

“Usijali Juma, huyu bwege, ameshatuweka
tatizoni Na vipepeo wote tushapata doa jeusi”
Masawe alimjibu Juma.

Nzaya alianza kunyanyuka ili kuwapa ile diski,
hakutaka kuleta ugumu, kwa kuwa alijua
ameshajulikana na hana cha kujitetea; wakati
huohuo kikosi cha askari kumi kiliingia
kikiongozwa na Honda .

“Naitwa Honda, ni ofisa wa jeshi la polisi,
wote mpo chini ya ulinzi, na Masawe weka
chini silaha yako” Honda aliwapa amri wazee
wale.

Tofauti na matarajio ya wengi, Masawe
aliachia risasi mbili zilizoenda kumchakaza
vibaya Nzaya na kumwangusha chini, muda
huohuo silaha ya ofisa mmoja ilikohoa na
kiganja cha Masawe kikasambaa na kuacha
bastola ikienda chini na kufuatiwa na kilio cha
maumivu.

Haraka askari waliwakamata na kuwatia
pingu, huku wengine wakiomba gari la
wagonjwa mana hali ya Nzaya haikuwa nzuri
hata kidogo.

***-
Baada ya wiki moja, Masawe; Kihengu na
Juma Lilo walipandishwa kizimbani na makosa
ishirini yalisomwa juu yao, huku yakiwemo
mauaji,kupanga njama za kuua, kuhujumu
uchumi na utakatishaji fedha.

Nzaya alifariki Dunia akiwa hospitali.

Kesi yao iliahirishwa hadi wakati mwingine
kwa kuwa mahakama haikuwa na uwezo wa
kusikiliza kesi ile, hivyo ilipelekwa mahakama
kuu.

Baada ya kupona, Kado aliendelea na maisha
yake akiwa hatambuliwi na watu wengi,
aliendesha maisha yake akiwa ni mvuvi wa
samaki kwa kutumia boti maalumu ziwa
Victoria.

-------TAMATI—
 
Hongera Sana ,story nzuri Sana..Endelea kuandika nyingi zitakuja kutumika kutengenezea movie huko mbeleni
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom