Date::11/14/2008
Kiama cha mapapa mafisadi mwezi huu, hapatakalika
Na Waandishi Wetu
Mwananchi
WAKATI watuhumiwa wa ufisadi wa fedha za Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) wakiendelea kusotea dhamana kwenye Mahakama ya Kisutu, mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru) Dk. Edward Hosea amesema wale wanaobeza kuwa serikali inashughulikia "vidagaa", wasubiri mwezi ujao kwa kuwa itakuwa patashika kwa mafisadi vigogo.
Tangu serikali ianze kuwafikisha kortini watuhumiwa wa wizi wa fedha hizo za EPA, ni mfanyabiashara mmoja tu, Jayantkumar Chandubhai Patel, maarufu kama Jeetu Patel, ambaye anaonekana kuwa kigogo na hilo limefanya wananchi wengi kuibeza serikali kuwa inawalea vigogo waliohusika kwenye kashfa hiyo.
Lakini jana, Dk. Hosea aliamua kuondoa udhia katika kongamano la wadau wa mapambano dhidi ya rushwa kwenye ukumbi wa Karimjee wakati alipoeleza kuwa kiama cha mafisadi vigogo ni mwezi ujao.
Dk. Hoseah alilazimika kutoa kauli hiyo baada ya mwenyekiti wa Chama Cha Wananchi (CUF), Prof. Ibrahim Lipumba kusema kuwa serikali inasumbuka na watuhumiwa wa rushwa ndogo badala ya kubwa.
Dk. Hoseah alisema: "Si kweli kwamba serikali inakumbatia watuhumiwa wa grand corruption (rushwa kubwa), subiri mwezi huu utaona.
"Tunamwogopa nani sisi?, hakuna tunayemwogopa, maji yanachemka. Nakuthibitishia kama mkurugenzi wa Takukuru kuwa tuna uchungu wa mali ya nchi hii. Kuanzia mwezi huu angalieni, mtaona matendo kwa mafisadi."
Alisema serikali na taasisi yake zina dhamira ya dhati ya kupambana na rushwa zote ndogo na kubwa na kusisitiza kuwa mwezi huu itaonyesha kwa vitendo.
Awali Profesa Lipumba alisema wananchi hawaamini kama serikali ina dhamira ya dhati ya kuwashughulikia watuhumiwa hao wa ufisadi.
Profesa Lipumba alitoa mifano mbalimbali ya tuhuma za rushwa kubwa ambazo serikali haijachukua hatua za kuridhisha na kuzitaja kuwa ni pamoja na ununuzi wa rada, umiliki wa zaidi ya dola bilioni moja za Kimarekani kwa aliyekuwa Waziri wa Miundo Mbinu, Andrew Chenge katika akaunti nje ya nchi na wizi wa fedha za EPA.
Lipumba alisema hotuba anazotoa Rais Jakaya Kikwete zinamshangaza kwa kuwa hazionyeshi kama mtu mwenye usongo na wala rushwa.
Kwenye Mahakama ya Kisutu, washtakiwa wawili walimudu kutimiza masharti ya dhamana na kuachiwa huru, wakati mfanyabiashara maarufu, Jayantkumar Chandubhai Patel, maarufu kama Jeetu Patel alirejeshwa rumande baada ya kushindwa kutimiza masharti ya dhamana ya kesi zake zote kwenye sakata hilo la EPA.
Waliomudu kutimiza masharti kati ya watuhumiwa sita walioomba dhamana jana ni Manase Hezekia Mwakale na Eddah Nkoma Mwakale ambao ni wafanyakazi wa BoT, lakini Jeetu Patel na ndugu zake wanne, licha ya kupata dhamana katika kesi moja, walilazimika kurudi tena mahabusu kutokana na kushindwa kutimiza masharti ya kesi nyingine.
Wengine walionyimwa dhamana jana ni Johnson Mutachukurwa Lukaza na ndugu yake Mwesiga Rutakyamila Lukaza, ambao walitimiza masharti lakini Hakimu Euphemia Mingi alieleza kuwa hati za nyumba walizowasilisha zina pingamizi kutoka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Jeetu na ndugu zake waliachiwa huru kwa dhamana ya kesi moja kati ya nne tofauti zinazowakabili, baada ya kutimiza masharti ya dhamana katika kesi hiyo namba 1157 ya mwaka 2008.
Katika kesi hiyo pamoja na masharti mengine watuhumiwa hao kwa pamoja walitakiwa kutoa pesa kiasi cha Sh490 milioni kila mmoja ambazo kwa pamoja zingefanya jumla ya Sh1.8 bilioni kama nusu ya fedha wanazotuhumiwa kuziiba katika kesi hiyo, lakini wao kwa pamoja waliwasilisha hati ya mali yenye thamani ya Sh2.3bilioni.
Kutokana na kukabiliwa na kesi nyingine tatu, watuhumiwa hao licha ya kuachiwa huru kwa dhamana katika kesi hiyo, walirudishwa mahabusu hadi hapo watakapotimiza masharti kwa kesi nyingine zinazowakabili. Kesi yao itatajwa tena Novemba 20 mwaka huu.
Kabla ya Manase na mkewe kuachiwa huru, Hakimu Mkazi anayesikiliza kesi hiyo, Warialwande Lema alionyesha kuitilia shaka hati na vilelezo vya dhamana yao jambo lilisababisha kuhoji.
Kwa mujibu wa Hakimu huyo, picha ya nyumba ya Everist Njau, aliyemdhamimi Eddah Mwakale ilioonekana kutofautiana na maelezo na kudai kuwa katika maelezo nyumba hiyo ilielezwa kuwa ni ghorofa moja, lakini katika picha haikuonekana kama ghorofa.
Lakini baadaye hakimu huyo aliamua kutoa dhamana kwa mshitakiwa huyo na kuahaidi kufuatilia jambo hilo ili kupata uhakika na kwamba kama atapata tafsiri tofauti atafuta dhamana hiyo.
Wakati taratibu za dhamana zikiendelea ndani, baadhi ya ndugu wa watuhumiwa hao waliokuwa nje ya mahakama hiyo na kuendesha ibada ya sauti ya chini kuwaombea ndugu zao hao ili waweze kupata dhamana.
Ndugu hao waliokuwa ameshika Rozoli na Tasbir walifanya maombi hayo hadi kufikia hatua ya kutoa machozi.
Baada ya watuhumiwa hao kuachiwa huru kwa dhamana, ndugu na jamaa waliofika mahakamani hapo waliacha kusali na kuwakimbili ndugu zao na kuwakumbatia kwa wa furaha.
Watuhumiwa hao waliondoka Mmahakamani hapo saa 7.10 wakiwa ndani ya gari ndogo aina ya Toyota Carina huku wakiwapungia mikono ndugu zao.
Wakati watuhumiwa hao wakiondoka kwa furaha, mambo hayakuwa mazuri kwa Bahati John Mahenge baada ya kujikuta akikosa dhamana kutokana na mahakama kushindwa kupata tafsiri halisi ya neno lililotumika katika hati ya nyumba iliyowasilishwa.
Hali hiyo ilisababisha mvutano kati ya mtuhumiwa huyo na askari magereza waliokuwa wakimuongoza kurudi mahabusu baada ya mshitakiwa huyo kugoma.
Wakati huohuo, upande wa serikali umeiomba mahakama kuahirisha kuanza kusikiliza maelezo ya awali (PH), kutokana na kile ulichodai kuwa inakusudia kufanyia marekebisho maelezo hayo.
Kesi hii itatinga tena Mahakamani hapo Novemba 19 mwaka huu kwa ajili ya maelezo hayo ya awali.
Katika hatua nyingine watuhumiwa wawili katika kesi ya jinai namba 1156, Johnson Mutachukurwa Lukaza na ndugu yake Mwesiga Rutakyamila Lukaza walijikuta wakigomba mwamba katika maombi yao ya dhamana licha ya kutimiza masharti yote.
Kikwazo katika dhamana yao kilijitokeza katika hati za nyumba zilizowasilishwa Mahakamani hapo kutokana na Hakimu Euphemia Mingi kueleza kuwa hati hizo zina pingamizi kutoka kwa Mwanasheria Mkuu wa Serikali.
Watuhumiwa hao kwa pamoja wanatuhumiwa kuiba kiasi cha Sh 6.3bilioni kutoka EPA ndani ya BOT.
Habari hii imeandikwa na James Magai, Excuper Kachenje na Paulina Richard