Mheshimiwa Spika, ninapenda pia kuungana na Kamati ya Uwekezaji na Biashara katika pendekezo la kuundwa kwa Kamati Teule ya Bunge ya kushughulikia suala la Richmond. Wako wenzetu ambao wamechangia awali ambao wamekuwa wakisema ni kwa nini pengine tumefika mahali tukapendekeza haja ya kuundwa kwa Kamati Teule ya kushughulikia suala hili. Kwanza ni vizuri ieleweke wazi kwamba Serikali ya Awamu ya Nne iliangalia tatizo lililokuwepo la dharura ya kukosekana kwa umeme na ikaona haja ya kuingia ubia au kuwatafuta wawekezaji wanaoweza kuwekeza katika upatikanajiwa umeme wa dharura. Lakini si Richmond peke yake wala DOWANS ambao walipewa, wengine walipewa kama AGGREKO na wengineo na waliweza kuzalisha umeme kwa wakati. Moja kati ya suala lililopelekea Kamati ya Uwekezaji na Biashara kuona haja ya kuundwa kwa Kamati Teule ya Bunge ni kukosekana kwa uwazi katika suala zima la Mkataba wa Richmond DOWANS.
Mheshimiwa Spika, Rais wa Jamhuri ya Muungano alipokuwa akifungua Bunge letu alisema maneno haya na ninaomba kunukuu:-
�Ninyi Waheshimiwa Wabunge ndiyo macho na masikio ya wananchi, mmeaminiwa na kuheshimiwa. Naomba kila siku mnapoingia na kutoka katika Bunge hili, mnapozungumza humu ndani au mnaposikiliza wengine wakizungumza, mnapokuwa macho au mnapofumba macho kwa kutafakari kwa kina, kila mmoja akumbuke imani na heshima hiyo kubwa mliyopewa na wananchi �.
Mheshimiwa Spika, tumepewa jukumu la kuwawakilisha Watanzania wenzetu kuwa macho na masikio yao na imani hii ni kubwa sana. Ttunapofika mahali pa kutumia haki yetu tuliyopewa kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika Ibara ya 63(2) ya kuweza kuisimamia na kuishauri Serikali ikiwa ni pamoja na kutaka kuona Mikataba hii, hii Serikali inapata kigugumizi. Walipata kigugumizi kwenye Kamati yetu na tukaona kwamba hapa ndiyo mahali pakee iundwe Kamati Teule ili haya mambo yaweze kufahamika kwa uwazi zaidi. Sababu nyingine zimeainishwa zaidi ya sababu sita na maswali sita ambayo yalitakiwa kujibiwa yapo pale kwenye ripoti ya Kamati ya Uwekezaji na naungana nazo kabisa. Lakini ukungu zaidi unazidi kuingia au utata pale ambapo baadhi ya ripoti nyingine za TANESCO zenyewe zinapobainisha mashaka zaidi wakati wa zabuni ya kupatikana kwa kutolewa kwa tendahii kwa Richmond na baadaye kwa dada yake DOWANS.
Mheshimiwa Spika, ukisoma ripoti ya TANESCO ya Procurement Contract and Perfomance Audit , utaona wazi kabisa kwamba wakati Bodi ya Zabuni ilipokuwa inakutana kulikuwa na kuingiliwa kwa uhuru wa Bodi yenyewe kufanya maamuzi. Ukiendelea zaidi ,wakati dharura ya umeme imekwisha na yule Richmond ameshindwa kutoa umeme kama ilivyokuwa inatakiwa bado iliwezekana kuhamisha mkataba kutoka Richmond kwenda DOWANS kinyume na mkataba wa awali inavyosemekana katika ripoti hii.
Mheshimiwa Spika, kwa ruhusa yako, naomba tu ninukuu baadhi ya maeneo katika report ya PPRA ili kubainisha utata uliokuwepo na ambao unalishawishi Bunge hili liunde Kamati Teule ili iweze kuujua ukweli na kuweza kuwaambia Watanzania ukweli juu ya Mkataba huu. Ripoti hiyo inasema hivi:-
�Emergency Power Supply - Richmond Development Company LCC, with regard to tender PC 010/2006 for emergency Power Supply from Rental Gas Base Generating Plant of 100MW in Dar es Salaam, the tender Board at its meeting held on 28 and 29th March, 2006, disqualified all bids and decided to retain to eight bidders who submitted bids and in addition include five new friends in the power rental business following non responsibleness of the previous eight bidders. But on 4th April, 2006, the Chairman of the Tender Board received instructions from the Board of Directors, in response to directives from the Government to recall for eight bidders and get clarification for the submission bids with the purpose of finding a possible bidder that could deliver same plan successful. This was clear interference with the tendering procedures and was not consistent with the Public Procurement Procedures�.
Mheshimiwa Spika, ukiendelea mbele kwa kuwa muda umekwenda, utabaini wazi kabisa kwamba inasema contract between Richmond Development Cooperation and TANESCO did not provide for reassignment of the contract to DOWANS but subtracting arrangement however political influence force TANESCO to waiver from the principles of the contract.
Mheshimiwa Spika, unahitaji nini zaidi ukishapata mashaka kama haya na hii ni ripoti iliyotolewa na TANESCO yenyewe ambayo ni Auditing Report.
Mheshimiwa Spika, baada ya kusema hayo, tulipowahoji Bodi ya TANESCO walibainisha wazi kwamba kulikuwa na mashinikizo. Lakini mbaya kuliko yote ni kwamba Richmond haikuwa na uwezo lakini ilipewa tender. Tunataka kujua ukweli juu ya jambo hili. Mbaya zaidi ni kwa Wizara kutotoa ushirikiano kwa Kamati ya Uwekezaji na leo kuiingiza Serikali na wananchi hasara ya kuundwa kwa Kamati ya kujua ukweli juu ya jambo hili ambalo lingeweza kuishia kwenye Kamati ya Uwekezaji na Biashara.
Mheshimiwa Spika, ningependa kuchukua nafasi hii kusema kwamba hatufurahii wala hatupendelei kuundwa kwa Kamati Teule, lakini tunalazimika ili kuweza kuunda wajibu wetu wa msingi wa kuiona mikataba ile kwa niaba ya Watanzania na kuwaeleza Watanzania ukweli.
Mheshimiwa Spika, nataka niunge hoja mkono kabla sijapigiwa kengele ya pili na niunge mkono pendekezo la kuundwa kwa Kamati Teule ya Bunge