Namuombea Rais Magufuli Afanikiwe Katika Mipango yake ya Kuijenga Tanzania

Mipangomingi

JF-Expert Member
Mar 16, 2011
2,713
2,058
Wiki chache zilizopita mwana JF mmoja mzoefu sana hapa jukwaani alipaza sauti yake akimuombea Rais Magufuli ashindwe (kwa baadhi ya mambo ambayo yeye angependa Rais asifanikiwe). Mimi niko na mtizamo tofauti. Ningependa Rais wetu ashinde katika mipango yake YOTE hasa ya kujenga uchumi imara na kuondoa umaskini wa watanzania. Nasema kwa sababu zifuatazo:-

1. Kushinda kwa Rais katika mipango yake ya uchumi ni kushinda kwa Tanzania, ni kushinda kwa watanzania. Hili liko wazi halihitaji maelezo mengi.

2. Hatua za kuimarisha uchumi zilizochaguliwa na Mhe. Rais (hasa katika uchaguzi wa vipaumbele na sera za kodi), zimelenga katika kuleta matunda baada ya miaka zaidi ya 20 (kama zitaleta matunda). Hata hivyo, katika siasa ya uongozi wa njia ya kuchaguliwa (Demokrasia), mipango ya maendeleo na utekelezaji wa vipaumbe imegawanyika katika makundi matatu; mipango ya muda mfupi (Short Term Plan), mipango ya muda wa kati (Medium Term Plan) na mipango ya muda mrefu (Long terma Plan). Mtiririko huu wa mipango ya maendeleo unatokana na ukweli kwamba, uchaguzi ni jambo la muda mfupi na wapiga kura ili waamini kuna mazuri yanakuja baada ya miaka 20, wanataka waone mazuri yakiyofanywa katika miaka mitano na mazuri yenye dalili za kutekelezwa katika muda wa kati ili waweze kutoa ridhaa kwa wachaguliwa. Kwa msingi huu, kiongozi wa kisiasa, (na ieleweke, hakuna kiongozi yoyote ambaye ni wa kuchaguliwa halafu asiwe mwanasiasa). Ukitaka kuchaguliwa, automatcally ushakuwa mwanasiasa.

Sasa hapa ndipo kwenye kiini cha kumuombea Rais wetu huyu afanikiwe kwenye kuboresha maisha ya Watanzania kwa mujibu wa matamanio na ahadi zake za wakati wa kampeni. Sasa kwa kuwa anaonekana kutoa msisitizo zaidi kwa wapiga kura wa miaka 20-30 ijayo (Kumbuka Emirates ilihitaji zaidi ya miaka 20 ili kujiimarisha na kuwa kama ilivyo leo), nina wasiwasi wapiga kura wa leo hawatampigia. Ndiyo, kama wananchi hawataona mipango iliyowanufaisha wao ndani ya miaka mitano, hawatakuwa na imani ya kuendelea kumuamini kwa mafanikio ya miaka 30 ijayo. Binadamu hayuko hivyo na Siasa haiko hivyo.

Akifanikiwa hasa kwa muda mfupi, najua 2019 au 2020 atafanya tena ziara Kagera na kueleza kuwa Serikali ilikuwa na malengo mazuri kutowajengea nyumba au kutowapa misaada binafsi mwa juzi na kutokana na nia hiyo nzuri, leo Serikali inajenga Magorofa ya National Housing na wana Kagera wote hakuna tena kuishi kwenye vijumba vyenu vinavyoanguka kwa vitetemeko vidogo kama kile cha mwaka juzi. Wananchi, pamoja na kuwa rekodi zinaonyesha huenda walinua huko nyuma, lakini watakuwa wameelewa nia nzuri aliyokuwa nayo Rais wao, na sasa (2020) wanakula matunda yake. 2019-2020 Serikali itakuwa imejijenga vya kutosha na kuwa na mapato makubwa yatakaotoa mikopo ya elimu ya juu kwa wanafunzi wote (100%) wa Divisheni 1-3 na Diploma wenye sifa za kujiunga na vyuo vikuu. Kwa kanuni ileile ya wana BKB, wanafunzi na wananchi wataelewa nia nzuri ya Serikali iliyokuwa nayo miaka mi 3 iliyopita hata haikuweza kuwalipia baadhi ya wanafunzi hususana wa masomo ya Sanaa.

2019/20, kwa kuwa serikali itakuwa imejikusanyia ukwasi mkubwa sana, kima cha chini cha Mshahara kinaweza kuwa mara 7-8 ya kilivyo leo, na kwa hakika wananchi ndugu zetu watumishi wataielewa Serakali kwanini miaka ya 2016/17...? Serikali haikuongeza mishahara na ikafuta posho zote. Nasema watumishi wataielewa tu Serikali na wataendelea kuiamini.

2019/20, Kwa kuwa Serikali itakuwa na ukwasi wa kutosha wa mapato, itamwaga ajira nyingi tu kwa ngazi zote na taaluma zote, wale 3000 na wengine wote wanaoendelea kumaliza katika vyuo vyetu, kwa hakika wataielewa tu Serikali kwamba ilikuwa na nia nzuri kabisa.

2019/20, Serikali itakuwa imevutia wawekezaji wa kutosha ambao wengi wao wataweza kuajiri makundi makubwa ya vijana wenye skills ndogo ambao kwa sasa wengi wao ni wabangaizaji mjini. Hili kundi kwa hakika litaielewa Serikali nia nzuri iliyokuwa nayo miaka 4 iliyopita na litaendelea kutoa ridhaa ya kuongoza dola;

2019/2020, Serikali itakuwa na uwezo mzuri sana na kuweza kutoa fidia kwa wale wote waliougua njaa miaka mitatu-minne iliyopita na Serikali haikuwa na uwezo wa kuwapelekea chakula kipindi hicho. Mimi naamini kwa asilimia 100, watu hawa wataielewa Serikali na wataishukuru sana na kupongeza nia nzuri iliyokuwa nayo hata haikutoa msaada wa chakula na baadhi ya jamaa zao wakafa. Lakini kwa sababu Serikali imekuwa imara na imetoa fidia, wataendelea kuiamini na kuipa ridhaa serikali iendelee.

Kuna makundi mengi sana ambayo kwa miaka minne nyuma (kumbuka hiyo na kwa 2019/2020) yalikwazika na harakati za maendeleo zilizochukuliwa Serikali kwa miaka hiyo, na sasa wataweza kula Bata kama kwingineko duniani (Brunei, Dubai, nk). Pembeje haitakuwa shida kwa wakulima, neno mlo mmoja tutalifuta kwenye kamusi zetu. Ni Tanzania mpya itakayokuwepo 2019/2020 iwapo tutamuombea Rais wetu.

Naendelea kumuombea kwani kinyume cha hapo, makundi haya hayataipa ridhaa Serikali hii kuendelea na miaka mingine ya madhila. Sasa hapa, ndipo OMBI langu kuu lilipo. Tukiiombea mabaya na isiweze kuyatimiza haya 2019/2020, na wanachi wakikataa kuiamini, itakubali kuwa imekataliwa? Na kama ikikataa halafu tukiingia kwenye rekodi mpya za Dunia, ya machafuko ya kisiasa kwa wachaguliwa "kufuta" matokeo, tutakuwa wageni wa nani?

Mimi nimewahi kusoma historia za nchi mpya zilizoendelea wanaziita (NIC) na hizi ndizo nchi ambazo zimefikia hatua ya kuendelea kwa kipindi kifupi sana (Miaka 50) kwa historia iliyopo. Lakini nchi hizi hazikuwa na uchaguzi wa kila baada ya miaka mitano, kipindi hicho dunia haikuwa busy na Demokrasia ila ilikuwa busy na Ukomunisti na Usoshalisti. 2020, tunaenda kubalisha historia ya Dunia kwa kuweka rekodi ya nchi iliyoendelea kwa haraka sana (miaka mitano) tena katika Demokrasia ya "asiyefanya kazi na asile na aisiyetimiza ahadi asichaguliwe"

Wanabodi, nauona ugumu wa Uchaguzi wa 2020, nahisi namna Tanzania isivyo kisiwa cha uvumilivu tena hivyo wacha niongeze maombi kwa Rais wetu kufanikiwa kwenye mipango yake ili wahanga hao niliowataja hapo juu wabadili nyoyo zao waipe ridhaa Serikali ya Lumumba ili tusiwe Kenya, Congo nk.
 
Back
Top Bottom