Mambo unayohitaji kujua katika ndoto unazoota sehemu ya tatu(jambo la 3) by Christopher Mwakasege

Principal Focus

JF-Expert Member
Jan 4, 2013
925
548
Bwana Yesu asifiwe sana!
Leo tuangalie jambo la 3, katika yale ambayo ni vyema ukayafahamu juu ya ndoto, ili uweze kufanikiwa kimaisha.
Jambo hilo la 3 ni hili: “Zijue Ishara zitakazokuonyesha ya kuwa ni ndoto ipi uliyoota inayohitaji ufuatiliaji wa haraka”
Hizi zifuatazo ni baadhi ya ishara, nilizoweza kukukusanyia toka katika biblia, zitakazokusaidia kujua ikiwa ndoto uliyoota, inahitaji ufuatiliaji wa haraka, na wa makini.
Ishara ya 1: Kuiota ndoto ile ile zaidi ya mara moja! Yusufu alimwambia Farao hivi: “Na ndoto ya Farao kwa vile ilivyokuja mara mbili, ni kwa sababu neno hilo Mungu amelithibitisha, na Mungu atalitimiza upesi”. (Mwanzo 41:32).
Hii haina maana yaliyomo katika ndoto huwezi kuyabadilisha – la hasha! Ukiota ndoto ile ile au zinazofana zaidi ya mara moja, ni ili ujue umuhimu wa kuyafuatilia yaliyomo kwenye ndoto hizo – kwa haraka na kwa makini. Wazo hili unalipata ukisoma Ayubu 33:14,15.
Ishara ya 2: Ndoto kukutia hofu – ambayo hata baada ya kuamka hofu hiyo unajikuta bado unaisikia! Mfalme Nebukadreza aliwahi kusema hivi juu ya ndoto aliyoota: “Nikaota ndoto iliyonitia hofu ….” (Danieli 4:5).
Kabla ya kuota ndoto ile, hakuwa na hofu. Ndoto aliyoota ilibeba roho ya hofu – iliyomwingia Nebukadreza wakati akiiota ndoto ile! Na alipoamka – alijikuta amejaa hofu kutokana na ndoto aliyoota.
Ishara ya 3: Kujisikia umefadhaika moyoni baada ya kuota ndoto! Tunasoma katika Danieli 2:1 ya kuwa: “Nebukadreza aliota ndoto; na roho yake ikafadhaika, usingizi wake ukamwacha”.
Je, umewahi kusikia hali ya namna hii, mara tu baada ya kuzinduka usingizini baada ya kuota ndoto? Ikiwa hali ya namna hii imewahi kukupata – basi ujue ndoto hiyo ina ujumbe wa muhimu unaohitaji kuufahamu! Soma Danieli 2:28.
Ishara ya 4: Hali ya kufadhaika iliyoambatana na kitu kingine! Nebukadreza katika Danieli 2:1 – aliposikia kufadhaika baada ya kuota ndoto aliyoota – kuna hali nyingine zaidi iliyojitokeza kwake! Biblia inasema ya kwamba: “ na roho yake ilifadhaika, usingizi wake ukamwacha”!
“Mnyweshaji na mwokaji wa mfalme wa Misri waliofungwa gerezani” na Yusufu, waliota “ndoto wote wawili, kila mtu ndoto yake usiku mmoja, kila mtu kwa tafsiri ya ndoto yake” (Mwanzo 40:5).
Biblia inasema, si tu kwamba Yusufu “akawaona wamefadhaika” (Mwanzo 40:6); lakini pia akawaona mfadhaiko ule waliokuwa nao, uliambatana na “nyuso” zao kukunjamana (Mwanzo 40:7).
Farao alipoota ndoto mbili mfululizo katika usiku mmoja, asubuhi yake “roho yake ilifadhaika” (Mwanzo 41:8). Ule mfadhaiko uliambatana na mahangaiko ya kutaka kupata tafsiri ya ndoto zile, bila kujali hali za kiroho za wale aliokuwa anawaulizia tafsiri zake (Mwanzo 41:8).
Mahangaiko ya Farao yalipokwama kupata tafsiri, ndipo Mungu alipomkumbusha mkuu wa wanyweshaji wake juu ya Yusufu, na akamkutanisha Farao na Yusufu. Yusufu akampa Farao tafsiri za ndoto zake, na maelekezo ya kufanya.
Ishara ya 5: Ndoto zinazosababisha jambo uliloota lijitokeze katika mwili wako! Unaposoma Ayubu 4:12 – 16, utatambua ya kwamba, Elifazi aliota ndoto iliyomtia hofu, na mifupa yake yote ilitetemeka. Unapolitafakari jambo hili, unaona uwezekano mkubwa wa Elifazi kusikia maumivu ya mifupa yake alipoamka, baada ya kuota ile ndoto.
Kuna mtu aliyeniandikia ujumbe wa simu mwaka 2016 akiomba nimwombee, ambaye alikuwa na maumivu katika mwili wake, yalisababishwa na ndoto aliyokuwa ameota. Mwaka 2009 aliota amepigwa risasi kwenye paja lake, na katika ndoto alipokuwa anaota, alijua risasi ilikuwa imebaki kwenye paja na ilihitaji kutolewa. Lakini aliamka toka usingizini kabla risasi haijatolewa!
Mwaka 2013 mguu wake ukaanza kuuma, na kuwa na maumivu makali kwenye eneo lile la paja palipopigwa risasi! Kwa nini? Kwa sababu ile “risasi ya kiroho” iliyompiga katika ndoto ilikuwa haijaondolewa!
Pia kuna dada mmoja ambaye alinisimulia ya kuwa aliota akicheza mpira wa miguu na wenzake. Na alipoupiga mpira kwa mguu wake, mara ule mguu ukaanza kumuuma. Na mara akaamka toka usingizini.
Lakini alishangaa alipoona ya kuwa, baada ya kuamka toka usingizini – mguu ule uliokuwa unauma kwenye ndoto ulikuwa bado unamuuma! Na tokea usiku ule alikuwa hawezi kutembea bila kuchechemea, kwa kuwa mguu ule uliendelea kumuuma.
Tulipokutana alipotoka hospitali na aliponieleza shida ile, nilijua tatizo lililompata. Nikamwombea na akapona muda ule ule nilipomwombea!
Ishara ya 6: Imani yako kwa Mungu katika Kristo Yesu au/na utumishi wako kwake kuanza kuyumba na kuhangaika na kupoa – baada ya kuota ndoto!
Tukisoma Kumbukumbu ya Totati 13: 1 – 4, tutaona ya kuwa, kuna ndoto ambazo lengo lake, ni kumwondoa mtu kwenye imani aliyonayo, kwa Mungu huyu tunayemwabudu katika Kristo Yesu.
Tena – tunaposoma Yeremia 23:25 – 17, tunajulishwa ya kuwa, kuna ndoto ambazo lengo lake ni kutaka kumsahaulisha mtu jina la Bwana Yesu!
Kwa hiyo – ukiona baada ya kuota ndoto imani yako, na utumishi wako kwa Mungu katika Kristo Yesu, vinaanza kupoa na kuyumba – ni ishara ya kuwa unahitaji kuifuatilia hiyo ndoto kwa haraka, na kwa umakini mkubwa kwa njia ya maombi.
Wengine waotao ndoto zenye malengo kama hayo; wanajikuta au hawaendi kanisani bila maelezo yanayoeleweka, au nguvu za maombi zinapotea, au wanajikuta hawana msukukumo tena hata wa kusoma biblia.
Ushauri wangu kwako kuhusu ishara hizi:
1. Hizi ishara zikiwa kubwa (“Strong”), au nzito (“heavy”) moyoni mwako – ina maana ufuatiliaji ufanyike kwa haraka – maana muda umekaribia wa kutimia yote uliyoyaona kwenye ndoto, ikiwa utayanyamazia! Labda kama unataka yatimie kama ulivyoyaona kwenye ndoto uliyoota.
2. Iandike ndoto unayoona ishara nilizokushirikisha, zinakupa kujua inahitaji kufuatiliwa. Iandike hiyo ndoto hata kama bado hujui tafsiri yake, wala ujumbe wake. Soma Habakuki 2:2 na Danieli 7:1
3. Anza kuiombea hiyo ndoto, na usiache kuiombea, hadi hizo “ishara” zilizokusukuma kuanza kuomba zimeondoka moyoni mwako au mwilini mwako!
Ni maombi yangu ya kuwa Mungu atasikia kuomba kwako!
Na Mungu azidi kukubariki!
 
Back
Top Bottom