JamiiTalks
JF Advocacy Team
- Aug 7, 2018
- 693
- 1,158
Katika mazingira yenye ushindani wa kisiasa, kijamii na kibiashara, waandishi wa habari wanakumbwa na changamoto kama shinikizo kutoka kwa wenye mamlaka, upendeleo wa vyombo au wahariri na ushawishi kutoka kwa wafadhili au wamiliki wa vyombo vya habari
Katika yote haya, ukweli na haki ya wananchi kupata taarifa sahihi vinapimwa kila siku. Je, ni taarifa zote zinahitaji mizania? Tunawezaje kuhakikisha kuwa habari haipindishwi kwa maslahi binafsi au ya taasisi fulani?
Kufahamu haya na mengine, usikose kujiunga nasi kwenye Mjadala wa Mizania kwenye uandishi wa habari, tutachambua maeneo muhimu yanayohitaji mizania, namna ya kukabiliana na shinikizo la moja kwa moja au na ulinzi wa uhuru wa habari
Kujiunga bofya https://jamii.app/MizaniaSpaceJune26th
Ni leo Alhamisi Juni 26, 2025 kuanzia Saa 12 jioni hadi 2 Usiku
========================================
MAONI YA WACHANGIAJI WALIOPO KWENYE MJADALA
PETER ELIAS (Mhariri Mwananchi):
Mizania bado ni changamoto katika tasnia ya Habari Nchini hasa katika Vyombo vya Habari vya Mtandaoni, ni mara chache unaweza kukuta kuna Mizania sawa.
Matukio kama yale ya kujibiwa kwa Askofu Gwajima yanaonesha kunakosekana kwa Mizania ya usawa, kwa kuwa kila upande unastahili kupata Haki sawa
Wakati huu wa kuelekea katika Uchaguzi kunakuwa na mashinikizo mengi, hasa kutoka kwa Wanasiasa ambao wanakuwa na nguvu ya Ushawishi, ni vema Wadau wa Habari wakawa makini kwa hili
Moja ya kitu au hali ambayo Vyombo vya Habari vinahitaji kusimamia au kuweka mkazo zaidi, ni suala la Wanasiasa wenye Ushawishi kutumia nguvu waliyonayo ndani ya Vyumba vya Habari kwa lengo la kunufaika wao au kwa maana ya kupata maslahi binafsi.
ELIAS MSUYA (MWANAHABARI):
Vyombo vya Habari vilirekodi mkutano wa Waandishi wa Habari na Askofu Josephat Gwajima, baadaye kukawa na shinikizo kwa Vyombo vya Habari vikitakiwa kuondoa taarifa hiyo.
Siku kadhaa baadaye kukawa na Watu mbalimbali wakiwemo Wanasiasa ambao walimjibu (Gwajima) lakini hakukuwa na shinikizo la kwamba hayo majibu nayo yasiwekwe hewani.
Kuelekea kwenye Uchaguzi ni vema Watu wote wanaohusika kwenye Vyama wakapewa Haki sawa, hii isiwe kwa Vyombo vya Habari Binafsi bali vyote.
ERGON (MDAU):
Vyombo vingi vya Habari vimekuwa vikiendesha shughuli zao vikiwa katika Mazingira ya hofu kutokana na uhalisia wa hali ilivyo
Vyombo vya Habari vimekuwa visemeo vya Wanasiasa na wanashindwa kuwa Wasemaji wa Jamii ya kawaida, ndio maana hata taarifa nyingi zinazotawala kwenye ‘Media’ utaona zinahusu nini ambacho Wanasiasa walikuwa wanakisema au wanatarajia kukisema
EDWARD CHAINA (MDAU):
Kuelekea Uchaguzi Mkuu ni kama tayari baadhi ya Vyombo vya Habari vimeshachagua upande, na hilo linaonekana wazi kutokana na kile ambacho wanakifanya
Inapotokea Chombo au Vyombo vya Habari vinapochagua upande, inamaanisha Wananchi hawatapata taarifa kwa Usawa.
Juzi nilikuwa nasikiliza chombo kimoja cha Habari, kuna mwandishi mmoja alikuwa akimlazimisha mwenzake kukubaliana na Serikali kwa kile ambacho wanakijadili, hiyo inaweza kuchangia ushabiki na kukosekana kwa Maadili ya Mizania katika Chombo husika.
KENNETH SIMBAYA (Mkurugenzi Mtendaji UTPC):
Mizania inasaidia kuongeza thamani ya Mwanahabari na Chombo cha Habari ikiwa kutakuwa na usawa na itazingatiwa.
Ukiniuliza mimi, sidhani kama Waandishi wa Habari hawaelewi Mizania kwenye Uandishi wa Habari, swali linakuja, kama wanajua kwanini hawalizingatii hilo?
Tukijibu hilo swali kwanini inakuwa hivyo, Wanahabari tutapata majibu kwanini kuna umuhimu wa kuwa na Mizania.
Kuna hoja ya maslahi ya Wanahabari nayo inachangia suala la Mizania katika Taaluma, wapo ambao hawajalipwa kwa Miaka kadhaa, wanategemea ‘sosi’ ndio awape
Hapo tayari inatengeneza ushawishi kwa yule aliyeandika, hawezi kuandika tofauti na kile ambacho aliyetoa hela hatakipenda.
Unapopata stori ambayo inakuwa ya upande mmoja na ukaitumia, uwezo wako wewe Mwandishi unakuwa unafifishwa
Jamii ikielewa kuwa Chombo chako cha Habari kina mwelekeo fulani inakuwa inashusha thamani ya Biashara yako
Unaporipoti taarifa ya upande mmoja, unawanyima Haki wale wanaotaka kusikia upande wa pili unasema nini
MAXENCE MELO (Mwananchi):
Suala la Mizania bado ni changamoto katika sekta ya Habari, hilo lipo wazi
Unaweza kuzungumzia Habari za Serikali katika Chombo chako na Watu wakakuona bado wewe uliyeandika au kuripoti ni Mtu wa maana na mwenye thamani kubwa, inategemea na Wewe umeitengeneza vipi taarifa yako
Mwanahabari anatakiwa kuelewa yeye anaishi katika Jamii, unachokiandika na kukiripoti ni kile ambacho kinatakiwa kuendana na Jamii husika, usipofanya hivyo ni rahisi Mwananchi kutafuta njia nyingine ya kufikisha ujumbe wake. Ndio maana Watu wengi wanakimbilia kuwasilisha ujumbe wao kupitia njia mbalimbali za Mtandaoni
Sisi JamiiAfrica tumekuwa tukiwapa nafasi Wananchi kueleza hisia zao ikiwemo Kero zao, kufanya hivyo haimaanishi tunaichukia Serikali bali tunaonesha uhalisia wa kile kilichopo kwenye Jamii na ambacho kinahitajika
NEVILLE MEENA (Mjumbe Kamati TEF):
Tunapokwenda kwenye Uchaguzi, Vyombo vyote vya Umma huwa vinatakiwa kuwa chini ya Tume ya Uchaguzi ili vitoe Mizania sawa
Wakati wa Uchaguzi kumekuwa hakuna Mizania ya Usawa kwa Vyombo vya Umma ambavyo vinaendeshwa kwa Kodi za Wananchi, vingi vimekuwa vikiegemea upande mmoja
Suala la kusukumwa kuandika kwa upendeleo ni jambo ambalo lipo kwenye Vyombo vya Habari wala siyo siri, hilo jambo lipo na linatokea, mimi mwenyewe nimekutana na hali hiyo mara tatu katika Vyombo vikubwa hapa Nchini
Wakati wa Uchaguzi nimewahi kukutana na suala la kupata maelekezo kutoka kwa Viongozi wangu kuwa suala hili liende hivi, kulikuwa na maelekezo unatakiwa ufanye hivi kama unaona haifai unaambiwa uchague ubaki au uondoke
Kuna wakati imewahi kutokea Mwenye chombo aliwahi kunishinikiza, nikamshauri kwa Kitaaluma, baadaye akakubali kwa kusema "Haya bana endelea na mambo ya Taaluma yenu", baadaye mmiliki huyo alikuja kukubali kuwa kile ambacho tulimshauri na kukiandika kilikuwa sahihi zaidi
Hao "Content Creators" wao Vyombo vyao havisajili kama ilivyo Vyombo vya Habari, yule anayekupa usajili akikupa maelekezo na akakwambia usifanye hiki, ukifanya anaweza kukufutia usajili
Katika Chombo ninachofanya kazi, tuliwahi kupata barua ya #TCRA ikitutaka kushusha taarifa ambayo licha ya kuwa ilikuwa na Mizania sawa lakini walielekeza hivyo na tukatii kwa kuwa walisema ina vimelea vya uchochezi
CAEJAY (MDAU):
Ikionekana Chombo cha Habari fulani kinaripoti taarifa ambazo haziwafurahishi waliopo katika Utawala, kunatengenezwa Mazingira ya kuonekana hicho kilichoripotiwa sio sahihi
Kuna hii falsafa ya "No Reforms, No Election", inaonekana kuwa ni ya Kichama lakini kuna mambo ambayo ni ya Kitaifa, mambo kama hayo yalitakiwa kuwa katika Vyombo vya Habari ili kujadiliwa na kupatikana kwa Usawa
Baadhi ya Vyombo vya Habari navyo vimeingia katika ombwe la kusifia na kutukuza kutokana na Mazingira
Kinachofanyika kwa sasa katika Vyombo vya Habari ni kuua Uzalendo wa Watanzania, kwani kusema mambo kwa maslahi ya Taifa sio kulichukia Taifa lako
FREDYHERBET (Mdau):
Moja kati ya jambo ambalo linawatatiza au kuwaweka njia panda Wanahabari ni wanapoona urafiki kati ya Mmiliki wa Chombo chao na Mwanasisasa
Mwanahabari anapoona hivyo anaweza kupata hofu ya kuamini kuwa hawezi kuandika taarifa ya pande zote kwa kuwa anajua atamkasirisha bosi wake
Mizania ni ngumu kupatikana inapotokea Mwandishi au Waandishi wanahudumiwa Kiuchumi na mtoa taarifa kwenye kuripoti Habari fulani, inapokuwa hivyo usitegemee kuona Mizania