Lula wa Ndali Mwananzela na sakata la CHADEMA

Lula wa Ndali Mwananzela na sakata la CHADEMA

allydou

JF-Expert Member
Joined
Apr 16, 2009
Posts
1,603
Reaction score
1,065
KWELI bado lipo tumaini. Hata kwa watu ambao walitarajia kuwa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA) kingeweza kuvunjika vipande vipande na kila mtu kugawana mbao, inawapasa wavute pumzi kidogo na kuona kilichotokea na kukiri kuwa labda CHADEMA watasalimika. Kwamba kweli CHADEMA kitasalimika ni muda tu utaamua, lakini kwamba kimenusurika hadi hivi sasa licha ya mawimbi makali na pepo za msimu zinazopunga kila kona ni wazi kuwa CHADEMA kinapitia wakati wake mgumu kabisa wa mabadiliko na maisha yake, kuliko wakati mwingine wowote ule.

Ni katika kutafakari haya yote ambayo yametokea hadi hivi sasa naweza kusema kuwa yapo mambo mazuri, yapo mabaya, yapo ya kuudhi na mengine ya kuchekesha na kwa kweli yapo ya kusikitisha vile vile. Nina uhakika wasomaji wangu pia watakuwa wameona kwa upande wao mambo kama haya. Tutafanya makosa makubwa tukidhani tu kuwa kuna jambo moja zuri au moja baya au kuangalia kwa uamuzi wa rangi nyeupe na nyeusi tu, bila kuangalia labda kama kuna kijivu mahali fulani.

Mazuri katika sakata hili

Yapo mambo mazuri ambayo yametokea kutokana na sakata hili la CHADEMA. Kati ya mengi naweza kutaja machache tu. Kwanza, hatimaye lile joto lililokuwa limepanda kwa muda mrefu ndani ya chama hicho limepata mahala pa kutokea. Kwa muda mrefu kumekuwa na hali ya kutunishiana misuli, kuumana maneno na hata kutegeshana na kutegeana. Viongozi wa taifa wa chama walikuwa wanaonekana wamegawanyika, lakini kila mmoja akikana kuwa hakuna mgogoro ndani ya chama.

Ni kana kwamba walikuwa wameamua kuwa wote watakuwa mbuni vichwa mchangani lakini mwisho wa siku ilibidi kushughulikia kile ambacho kilikuwa kinasumbua chama. Kwamba chama kimeweza kukaa chini na kuwajadili na kuchukua hatua kali dhidi ya viongozi wake wa kitaifa ni jambo zuri. Ni jambo zuri kwa sababu moja kubwa, kwamba sasa wana CHADEMA na wapenda mabadiliko wote ni lazima waamini kuwa hakuna ‘superstar' ndani ya chama na yeyote ambaye ataleta matatizo atashughulikiwa. Kama wameweza kufanya hivi kwa Naibu Katibu Mkuu ni lazima wana CHADEMA wawe tayari kuamini kuwa maji yale yale yaliyotumika kumnyonyoa yeye yanaweza siku moja yakatumika kumng'oa Mwenyekiti, Katibu Mkuu au kiongozi mwingine yeyote. Huu ulikuwa ni mstari ambao ulisubiriwa kwa hamu, watu waone kama utavukwa.

Jambo jingine zuri ni kuwa viongozi waliovuliwa madaraka wangeweza kabisa kuja na hasira na kutoa kauli za kutotambua uamuzi wa kikao kile na kudai kuwa wao bado ni viongozi halali wa ngazi husika. Wangeamua kumwaga mboga na wao kwa vile wenzao wameshamwaga ugali! Hawakufanya hivyo na badala yake, walitoa kauli ambazo kwa kweli hazikuwa kali kama watu walivyotarajia kwani walichukua muda kupima na kutulia – ndio mwanzo wa hekima. Jambo hili ni zuri na ndio maana nimesema kwa hakika bado yapo matumaini. Utulivu huu walioonesha – japo sikupenda watoe matamko yoyote hadi watakapokuwa wamejibu maelekezo ya Kamati Kuu- umesaidia kwa kiasi kuonesha njia nzuri ya huko mbele. Jambo hili ni zuri.

Mabaya katika sakata hili

Kati ya mambo mabaya yaliyotokea katika sakata hili ni kwamba lilifikia hapa lilipofikia. Hadi hivi sasa sijaelewa – japo nimejitahidi sana kujielewesha – kwa nini suala hili limefikia hapo lilipofikia hadi kulazimisha kuchukua hatua kali zaidi? Hivi hakukuwa na njia nyingine ambayo ingeweza kutumika mapema zaidi kudhibiti kile kinachoitwa uasi au kama wengine wanavyoona harakati za kutaka mabadiliko ndani ya chama?

Kwamba inafikia mahali watu wanatofautiana kiasi cha kuwa na uhasama wa wazi, kurushiana vijembe vya maneno, kweli watu hao wanaweza kusema wanataka kuongoza harakati za mabadiliko? Kuna msemo kuwa ‘nyumba iliyogawanyika haiwezi kusimama'; msemo huu ni wa kweli kwa maana nyingi sana. Muda ambao ndugu wanaweza wakakaa kugombana wenyewe kwa wenyewe na kuumizana ndio muda ambao adui anaweza kutumia kuwanyang'anya mali, kuwaibia na hata kuwadhuru. Tumeona hili vizuri sana kwamba CCM wananufaika mno na mgawanyiko ulioko ndani ya CHADEMA kiasi kwamba hawaoni tatizo kabisa kuunga mkono upande mmoja wakiamini kwa kufanya hivyo wanaongeza mgogoro. Na baya zaidi ni kweli wapo wana CHADEMA ambao hawaoni tatizo kuungwa mkono na CCM kwa kisingizio kuwa wanapigania maslahi ya taifa!

Kitu pekee ambacho hutaona wanaCCM wanakifanya ni kuwakaribisha hao wana CHADEMA waingie CCM ambako watapewa nafasi ya kugombea uongozi wa chama kitaifa au kuwa nyota wao. Kwa sababu wakiingia huko na huko nako tayari kuna mastaa wao na wao wenyewe pia wana migogoro yao ambayo kwa sababu ya mgogoro wa CHADEMA hatuisikii sana; lakini ipo.

Haya ya CHADEMA hayakupaswa kufika hapa na kuachwa kufika hapa. Yangeweza kabisa kumalizwa kidugu, kirafiki na kiumoja siyo sasa hivi ambapo watu wengine hata hawasalimiani tena! Na wote wanadai wanataka kuing'oa CCM madarakani!

Ya Kuudhi katika sakata hili

Kati ya mambo yanayoudhi ni ule ushabiki uliopitiliza wa wafuasi wa makundi mbalimbali ndani ya CHADEMA. Kwa sisi wengine ambao tunasoma mitandao na kufuatilia mambo haya kwa karibu, kwa kweli inachukiza kuona jinsi watu wanaodai kuwa wako chama kimoja na tena ni viongozi wakiwa wametengeneza kambi ambazo zinachukiana kupita kiasi. Kinachoudhi ni kuwa kambi hizi zimetengenezwa na viongozi wanaopenda wafuasi! Matokeo yake wafuasi wanajibizana, wanatambiana na wanatishana hadi inakera na kuudhi kwa wakati mmoja. Inaudhi kwamba makundi haya ya mashabiki wa watu (kumbuka si mashabiki wa itikadi fulani) wamekuwa watii kwa watu hawa hadi wamekuwa kama kasuku wanaorudia maneno ya wanaowafundisha! Wengine wamefikia mahali hadi wanazungumza kama viongozi wao! Wengine wanaigiza hadi sauti za viongozi wao.

Cha kuudhi ni kuwa kati ya hawa wapo ambao utii wao uko si kwa sababu wanaamini itikadi au maono ya viongozi wao bali kwa sababu matumbo yao na mifuko yao yanawategemea watu hawa. Hivyo, wamekuwa watetezi wa kimaslahi zaidi, siku minofu hiyo ikikatwa watatafuta mahali pengine pa kuegemea. Hili linaudhi!

Ya Kusikitisha katika sakata hili

Jambo kubwa la kusitikisha kutokana na sakata hili ni kuwa CCM na serikali yake wanaendelea kutawala wapendavyo. Wakati CHADEMA wanafukuzana wenyewe, wanatafunana na kung'atana CCM wao wanaendelea kumkamua ng'ombe aitwaye ‘Mtanzania' kama wapendavyo. Tumesikia juzi kuwa serikali imekubali kupandisha bei ya umeme na wakati huo huo, tayari tumeona jinsi sera mbovu zilizoshindwa za CCM zilivyoharibu taifa. Kuanzia kwenye elimu, maji, ulinzi na usalama na kwingine kote sera za CCM zimekuwa na madhara makubwa zaidi kuliko kitu kingine chochote. Sera pekee ambayo inaonekana kufanikiwa ni ile ya ‘uwekezaji wa wageni'. Serikali imejitahidi kwa kila namna kuwavutia wawekezaji wa kigeni kiasi kwamba watendaji wake wanapokebehi wawekezaji wa ndani hakuna anayeshtuka; nani anawahitaji wa ndani kama wa nje wanaleta yote wanayohitaji.

Lakini hili pia tunaweza kuliona kama ni ubovu wa sera ya uwekezaji wa kigeni – kama sera yenyewe ipo kweli. Sasa wakati CCM inaweza kufanya lolote CHADEMA kama chama kikuu cha upinzani kinasubiri kikao cha Bunge ili waonekane wanapiga kelele, wagome na kutoa hotuba motomoto. Wanafanya hivyo huku wenyewe wakiwa hawapatani na mwisho inaonekana wanachozungumza kila mmoja ni maoni yake na siyo mkakati wa kichama (party strategy). Matokeo yake juhudi za wabunge mbalimbali wa upinzani zinaonekana kutukuza majina yao zaidi kuliko kukijenga chama. Imefikia mahali wao wenyewe tena hawapatani hadi bungeni! CCM wanagongagonga meza tu na kuitikia ndiyo!! Nani atawazuia! Nani ataonesha ubaya wa sera zao? Kweli kuna mpinzani anayeamini kuwa sera za CCM ni mbaya na ni janga kuu la taifa letu? Hili linasikitisha!

Ya kuchekesha katika sakata hili

Yapo pia mambo ya kuchekesha, kubwa zaidi ni lile linalotokana na hayo yote hapo juu. CHADEMA inaamini kuwa inaweza kuvuruga kwa kiasi chochote kile na watu bado wataendelea kusimama nyuma yake na kusema "people's power". Hisia hizi zinatokana na kupendwa. Wakati mwingine mtu anayependwa anaweza kabisa asijue kabisa ameharibu kwa kadiri ya kwamba watu wanaendelea kumpamba kwa maneno mazuri na kumfanya ajione ni muhimu. Mtu wa namna hiyo anaweza kuchelewa sana kujijua kuwa kaharibu na hata siku akija kujua kuwa ameharibu, atakuwa amekwishachelewa sana.

Tatizo la mtu wa namna hiyo ni kiburi cha kupendwa. Kuna msemo kuwa mtu anayependa ‘haoni wala hasikii'; hili ni kweli pia kwa mtu anayependwa hasa akijua anapendwa na mtu ambaye katika mazingira mengine asingeweza kupendwa. Mtu huyu anayependwa siku atakapokuja achwa hawezi kuamini; na anaweza kuumia kweli kweli na hata kuwa mtu wa kisasi. Kwa sababu hakuwahi kuamini mtu aliyemuonesha mapenzi namna hiyo kweli anaweza kumuacha solemba.

CHADEMA isipoangalia itajikuta iko katika hali ya namna hii – kama haiko tayari – kwamba kwa vile inajua inapendwa na watu wengi basi viongozi wake hawaamini kuwa wana matatizo ndani yao au katika uongozi wao. Binafsi naamini tuliyoyashuhudia siku hizi chache zilizopita ni kilele cha ulevi huu wa mapenzi; wahusika wote wanaamini wanapendwa! Wote wamezungukwa na watu wanaowaimbia nyimbo za kuwapenda na kuwafanya wajisikie ‘spesho'! Kwa baadhi yetu tuliosoma Saikolojia watu wa namna hii ni vigumu sana kujiangalia na kubadili tabia kwa sababu wakibadili tabia na watu wakaacha kuwapenda itakuwaje? Kwa kadiri ndugu zetu hawa wataendelea kuzama katika hizi hisia za kupendwa ndivyo itakavyokuwa vigumu zaidi kwa wao kujipima na kubadili tabia, mitazamo na matendo yao. Kwa nini wabadili wakati wao wanapendwa? Hili linachekesha. Ama linatisha.


Source:
Raia mwema
 
EPISODE 1.
Takribani miaka kumi iliyopita, kijana mmoja mwembamba alisimama katika mojawapo ya kumbi zilizopo ndani ya viwanja vya sabasaba jijini Dar es Salaam. Alikuwa akiomba nafasi ya kuchaguliwa kuwa mjumbe wa Baraza kuu la CHADEMA.
Baadaye aliniambia kwamba hadi wakati ule hakuwahi kuvaa suti maishani mwake. Suti kwake ilikuwa ishara ya ubepari. Watu aliokuwa akiwapenda wakati akiwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM); Profesa Chachage Seith Chachage, Profesa Issa Shivji na Dk Azaveli Feza Lwaitama hawakuwa wapenzi wa suti.
Lakini kwenye siku hiyo, Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, alijitolea kununua suti mpya ili walau kijana wake huyo kipenzi wakati huo aonekane vema mbele mbele ya wajumbe.
Kijana huyo akaja baadaye kupata ujumbe wa Baraza kuu. Baadaye akifanya kazi kwa karibu sana na Mbowe, alipanda ngazi hadi kufikia kuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho. CHADEMA haikuwahi kuwa na kijana mdogo namna ile kwenye nafasi kubwa namna ile.
Kijana huyo ndiye huyu Zitto Kabwe ambaye leo hii yuko kwenye mgogoro na chama chake alichojiunga nacho tangu akiwa na umri wa miaka 16….
(Hii ni sehemu ya makala ya E.Kamwaga kwenye gazeti la Raia Mwema yenye kichwa ‘’Utatu wa Tofauti Kati ya Zitto, Mbowe na Slaa’’ )
 
Huu ukweli upande wa wafahidhina hawatakubali lakini zzk kawashika pabaya
 
Watanzania wameshajua kuwa chadema ni chama cha kilaghai na kihuni
 
We kalikanye acha ushamba. Jadili mchango wa Lula mwananzila. Zitto ameishika Chadwma pabaya
 
Ndugu naomba nitofautiane na wewe. Huu sio msukosuko mkubwa uliowahi kukipata Chadema kuliko wakati wote. Kumbuka mtajwa mkuu ni naibu katibu mkuu wa chama. Chadema kimewahi kwa uthubutu mkuu kabisa kuwaondoa makamu wenyeviti wa chama taifa wawili. Mkumbuke wangwe na kabouru. Kwa hiyo kitila na zitto na mwigamba bado hawana uzito kama wa makamu mwenyekiti wa chama taifa. Chadema kilipita na kimeendelea kuyashinda mawimbi yote makali yaliyowahi kukipata. Ni chama pekee kilichowahi kuwaondoa makamu mwenyekiti wa chama mara 2 na kubaki salama. Naibu katibu mkuu, mwigamba na kitila hilo ni wimbi dogo tu. Chadema kama taasisi iliyokomaa imepita salama hata katika kawimbi haka ka kusafisha chama. Wanaoshangaa sana ni wale wa upande wa pili ambao hawajazoea kufanya maamuzi magumu.
 
Niseme ukweli nilikuwa nasubiri sana muono wa huyu bwana kuhusu yanayoendelea.Nimemwelewa sana lakini nadhani bado hatujafikia mahali watu bila woga,bila unafiki,bila kuhofu kupoteza urafiki na pengine baadhi ya fursa kwa kuwa mkweli na muwazi.

Wengine wanabeza kutengeneza hoja kwa kutaja majina ya watu lakini naamini kwa aina ya matatizo ya CDM yalipoanzia hadi kufikia kama wanaharakati wote hasa wale wenye heshima na wanaoweza kusikilizwa sauti zao kama mwenye makala hii walipaswa kusema wazi matatizo ya hawa viongozi kwa kusema wazi pengine ingewashtua kidogo wahusika.

Dr Lwaitama amekwenda kwenye inner core ya tatizo na ametaja hadi majina na makala yake hadi sasa ndio pekee nionayo itakuwa imestua hata wahusika wa pande zote na ndivyo inavyopaswa ili kugusa wahusika moja kwa moja bila kuwaachia kazi watu kutegua mitego ya kundi gani limeguswa au halijaguswa.

Lula wa Ndali,huu mgogoro unaujua vizuri gonga penyewe kama nia yetu ni upinzani wa kweli na wenye nguvu na sio kuzunguka kuelezea matatizo kiujumla huku kila mhusika akijipima kwa nafsi yake tu na wananchi wasiojua ukweli wa chanzo cha haya kuendelea kubaki hewani na pengine kuchanganyikiwa zaidi.

Tuwaambie ukweli hawa wanasiasa ili wajue tumechukia na wasicheze na muda na support yetu kwao kwa namna yoyote.
 
Lula wa Ndali nimezidi kukuheshimu....ila umeongea mambo ya msingi sana laiti CDM wangekusikiliza.... najua hawapendi ushauri wako maana kuna kipindi uliwahi kuwaashauri ila MTENDAJI MKUU alikuja kukurukia kwa maashambulizi sana tu

Kama usemavyo CDM wasijidanganye kwamba mgogoro huu na maamuzi yake hayatakuwa na athari kwa pande zote, ukweli wote wataathirika na wafaidikaji ni CCM

Ona sasa badala ya kujipanga kukemea kupanda bei ya Umeme CDM inajipanga kupita mikoani kueleza 'uhalali' wa maamuzi yao
 
Hakuna demokrasia ndani ya chadema ila ni umwinyi, umangimeza na ushetani mtupu
 
Nilikuwa najaribu kutafuta nani ataandika kitu kinachomake sense, nafikiri huyu kafanya vizuri.
 
EPISODE 1.
Takribani miaka kumi iliyopita, kijana mmoja mwembamba alisimama katika mojawapo ya kumbi zilizopo ndani ya viwanja vya sabasaba jijini Dar es Salaam. Alikuwa akiomba nafasi ya kuchaguliwa kuwa mjumbe wa Baraza kuu la CHADEMA.
Baadaye aliniambia kwamba hadi wakati ule hakuwahi kuvaa suti maishani mwake. Suti kwake ilikuwa ishara ya ubepari. Watu aliokuwa akiwapenda wakati akiwa mwanafunzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam (UDSM); Profesa Chachage Seith Chachage, Profesa Issa Shivji na Dk Azaveli Feza Lwaitama hawakuwa wapenzi wa suti.
Lakini kwenye siku hiyo, Mwenyekiti wa CHADEMA, Freeman Mbowe, alijitolea kununua suti mpya ili walau kijana wake huyo kipenzi wakati huo aonekane vema mbele mbele ya wajumbe.
Kijana huyo akaja baadaye kupata ujumbe wa Baraza kuu. Baadaye akifanya kazi kwa karibu sana na Mbowe, alipanda ngazi hadi kufikia kuwa Naibu Katibu Mkuu wa chama hicho. CHADEMA haikuwahi kuwa na kijana mdogo namna ile kwenye nafasi kubwa namna ile.
Kijana huyo ndiye huyu Zitto Kabwe ambaye leo hii yuko kwenye mgogoro na chama chake alichojiunga nacho tangu akiwa na umri wa miaka 16….
(Hii ni sehemu ya makala ya E.Kamwaga kwenye gazeti la Raia Mwema yenye kichwa ''Utatu wa Tofauti Kati ya Zitto, Mbowe na Slaa'' )
Unataka kutuaminisha akinunuliwa suti asidai demokrasia? ama kweli "macho siyo kitu iwapo akili haioni'
 
Lula wa ndali unaposema angeamua kumwaga mboga kama alivyo mwagiwa ugali wake si kweli sababu hata ukiangalia press alilolifanya pale Serena ni kwamba amejitahidi kumwaga mboga ingawa bakuli alilokuwa ameshikilia lilikuwa sawa na tupu. Nakuhakikishia hata Chadema wangemfukuza kama mvua mwizi, kamwe huyu kijana ni kama ng'ombe dume lililohasiwa mbele ya jike lenye joto. Au ni kama mmbu dume anawasha tu lakini halileti malaria.

Kwenye press kaongea mambo madogo ila katumia lugha za kukuza ili yaonekane yana impact kubwa, ndani swala la kutonywa amejikakamua kutafuta hilo neno ili lionekane kubwa.

Ieleweke Chadema ilikuwa ikiwa na kina Zitto na wengine lakini sasa wao hawataki kupewa hizo heshima za kuitwa ma legendary kwa tamaa yao. Na wasijidanganye kama bila wao Chadema haitadumu, hawa watu waende wanakostahili wawaachie wenye nia njema
 
Back
Top Bottom