Jaji Bomani: ZEC imejipunguzia imani

Paul Alex

JF-Expert Member
Jul 14, 2012
4,240
9,527
Mwanasheria Mkuu mstaafu nchini, Jaji Mark Bomani amesema kitendo cha Tume ya Uchaguzi (ZEC) kutangaza marudio ya uchaguzi wa rais wa Zanzibar, wawakilishi na madiwani, kumepunguza imani ya wananchi kwa chombo hicho.

Bomani pia amesema huenda uamuzi wa kutangaza kurudiwa kwa uchaguzi huo Machi 20, hakikuishirikisha tume hiyo na hivyo lawama zinapaswa kuelekezwa kwa mwenyekiti wake, Jecha Salim Jecha.

Akizungumza katika mahojiano maalumu na gazeti hili ofisini kwake jana, Bomani alisema anahisi huenda uamuzi wa kufuta uchaguzi huo na kisha kutangaza tarehe mpya, haukuishirikisha ZEC.

“Hizo dosari hazikuwekwa kinagaubaga hii inaacha maswali mengi kuliko majibu,” alisema mtaalamu huyo wa katiba.“Yeye ndiye alifuta na leo ametangaza, je hizo dosari ameshatangaza kwamba zimerekebishwa?”

Bomani alisema kwa namna uamuzi wa kufuta uchaguzi huo ulivyofanywa, inaonyesha dhahiri kuwa maofisa wengine wa ZEC hawakushiriki, hivyo si sawa kutangaza marudio ya uchaguzi huo.“Kufuta matokeo ya uchaguzi bila ya maelezo yanayoridhisha au bila ya ushahidi kunaonyesha uamuzi huo haukutokana na tume.

Ni kama uamuzi wake Jecha kwa hiyo haitoshi yeye pekee kutangaza uchaguzi unarudiwa maana haitakuwepo imani,” alisema.Hata hivyo, alisema ili kutatua mgogoro wa Zanzibar njia pekee ni kuunda jopo la watu wachache wanaoheshimika chini ya uenyekiti wa mmoja wa majaji wakuu mstaafu nchini, ili wazingalie dosari za kufuta uchaguzi huo endapo zilikuwepo na kisha kutoa maoni au ushauri.

Kuhusu mchakato uliosimama wa kuandika Katiba mpya, Bomani alisema suala hilo ni zito na linapaswa kushughulikiwa baada ya Serikali ya Zanzibar kupatikana na si kuachwa hewani. Alisisitiza kuwa suala hilo linapaswa lifanywe kwa umakini kwa kuwa baadhi ya mapendekezo ya Katiba mpya tayari yalishafanyiwa kazi na Tume ya Mabadiliko ya Katiba iliyoongozwa na Jaji Joseph Warioba na Bunge Maalumu la Katiba (BMK).

Kuhusu serikali ya Rais John Magufuli, mwanasheria huyo alimpongeza kiongozi huyo wa nchi kwa jitihada za kupambana na rushwa na ufisadi na kumshauri arekebishe mfumo wake serikalini ili uweze kwenda na kasi yake.
 
Back
Top Bottom