Edward Hosea awashambulia wabunge

BAK

JF-Expert Member
Feb 11, 2007
124,789
288,020
Edward Hosea awashambulia wabunge

• Wabunge waja juu, wahoji uadilifu wake

na Mwandishi Wetu

Tanzania Daima~Sauti ya Watu

MKURUGENZI wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU), Edward Hosea, jana aliwashambulia wabunge katika semina ya kukabiliana na rushwa iliyoandaliwa na taasisi yake na kuwashirikisha wabunge wa Chama cha Kupambana na Rushwa (APNAC).

Akitoa mada katika semina hiyo, Dk. Hosea aliwashambulia wabunge hao hadharani, kwamba wamekuwa wakichangamkia posho za semina wakati hakuna uwajibikaji.

Katika mada hiyo iliyoonekana dhahiri kuwakera wabunge hao, Dk. Hosea alisema baadhi yao wamekuwa wakihudhuria na kusaini posho zaidi ya tatu katika semina tofauti kwa siku moja, huku wakishindwa kuwajibika, jambo ambalo alisema ni aina mojawapo ya rushwa.

“Wapo wabunge wanaohudhuria semina zaidi ya tatu kwa siku moja na kusaini posho, lakini hata baada ya kuwezeshwa kwa posho hizo, hakuna uwajibikaji. Kwa kweli kuna mambo mengi yanayotokea, lakini tunayafumbia macho,” alisema Dk. Hosea.


Mbali na kusaini posho kwenye semina tatu kwa siku, Dk. Hosea pia alisema wapo wabunge ambao wanatumia vibaya ubunge wao kwa kutokaa kwenye foleni wawapo sehemu za huduma kama benki.

Pia aliwapasha wabunge kuwa hivi sasa siri nyeti za serikali ziko wazi, na kwamba inatokana na ukosefu wa maadili miongoni mwao.

Hata hivyo, baada ya kumaliza kutoa mada hiyo, baadhi ya wabunge walionekana dhahiri kukerwa na mada hiyo na kutaka kujibu mapigo kwa kuhoji utendaji wa taasisi hiyo na mafanikio yake tangu ilipoanzishwa.

Mbunge wa kwanza kutoa dukuduku lake, alikuwa Dk, Raphael Chegeni (Busega-CCM) ambaye alihoji utendaji wa TAKUKURU na kueleza kutoridhishwa kwake.

Dk. Chegeni alianza kujibu mapigo kwa kuhoji uwajibikaji wa Dk. Hosea na taasisi yake kuwa, iliwahi kuchunguza kashfa ya zabuni ya kampuni ya kufua umeme wa dharura, Richmond, na kuitangazia jamii kwamba hakukuwa na rushwa katika zabuni hiyo.

Kama hiyo haitoshi, Dk. Chegeni alisema TAKUKURU pia ilishindwa kuchunguza kashfa ya minara pacha ya majengo ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT) na badala yake Kampuni ya nje ya Ernest & Young ilibua ufisadi mkubwa na hatimaye leo baadhi ya watuhumiwa wamefikishwa mahakamani.

Huku akishangiliwa na baadhi ya wabunge, Dk. Chegeni alihoji ujenzi wa gharama wa ofisi za TAKUKURU nchini pamoja na magari ya kifahari wanayotumia wakati haiwajibiki ipasavyo katika kukabiliana na rushwa.

“TAKUKURU mnawajibika nini? Mlisema kwenye Richmond hakuna rushwa, lakini baadaye Bunge lilibaini kuwapo kwa rushwa, kwenye ujenzi wa minara pacha ya BoT mmeshindwa kuchunguza hadi kampuni ya nje ndiyo iliyokuja kuibua kashfa hiyo,” alisema Dk. Chegeni.

Kutokana na hoja hiyo, Dk. Hosea alikuja juu na kuwataka wabunge hao kuacha kuhoji mambo hayo, kwani wakianza kuchambuana, hakuna atakayebaki salama.

“Hapa hatukuja kulumbana, tumekuja kwenye semina, si mahala pake, lakini nyie wabunge ndio mlioamua kupitia Kamati Teule ya Bunge na mapendekezo yenu yapo, kwa hiyo iulizeni serikali, lakini hatuko hapa kushambuliana,” alisema Dk. Hosea.


Hata hivyo, baada ya malumbano hayo makali, wabunge na maofisa wa TAKUKURU, waliendelea na semina yao inayofanyika katika ofisi ndogo za Bunge jijini Dar es Salaam, inayotarajia kumalizika leo.
 
Mkurugenzi wa Takukuru aumuka baada ya wabunge kuhoji uadilifu wake

Felix Mwagara na Ellen Manyangu
Mwananchi

MKURUGENZI wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hosea jana alikuwa kwenye wakati mgumu baada ya wabunge kumhoji uhalali wake wa kuiongoza taasisi hiyo wakati akikabiliwa na tuhuma za kusafisha kashfa ya zabuni ya mitambo ya kuzalisha umeme wa dharura.

Mkurugenzi huyo, ambaye alitajwa kwenye taarifa ya tume teule ya bunge iliyochunguza kashfa hiyo na serikali kutakiwa kumchukulia hatua, alikumbwa na mtafaruku huo katika semina ya Miundombinu ya Uadilifu iliyoandaliwa na Takukuru na Chama cha Wabunge wa Afrika (APNAC) na kufanyika kwenye hoteli ya Whitesands jijini Dar es salaam.

Ilifikia wakati Dk Hosea alionekana kukerwa sana na maswali kiasi cha kulazimika kuwaonya kuwa anao uwezo wa kuwachafua kama wakiendelea kufanya mambo yanayoonekana kumvua nguo.

Mbunge wa Busega, Raphael Chegeni ndiye aliyeanzisha kizaazaa hicho baada ya kumhoji Dk Hosea akisema ilikuwaje taasisi yake iliisafisha kampuni tata ya kuzalisha umeme wa dharura Richmond Development (LLC) iliyokuwa inakabiliwa na kashfa ya kushinda zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura wakati kamati teule ya Bunge iliyoundwa kuchunguza mkataba wake, iligundua kuwepo kwa mazingira ya rushwa.

“Inakuwaje wakati wa mjadala wa Richmond, wewe mkururugenzi wa Takukuru ulikanusha kuwapo rushwa na uchunguzi wa kamati ya bunge ulibaini kuwepo rushwa ndani ya kampuni hiyo? Je ni nani mwenye dhamana ya kukuadhibu wewe na taasisi yako kuhusu rushwa’’ aliuliza Chageni.

Swali hilo halikutegemewa na Dk Hosea na lilionekana kumuudhi na kulazimika kuchukua kipaza sauti na kusitisha maswali na kuanza kujibu kwa ghadhabu.

“Hapa siyo jukwaani hivyo tusilete siasa. Nipo hapa kwa ajili ya kufundisha na kama ni suala la Richmond waziri mkuu alishaliongelea na ndiyo mwenye dhamana ya kujibu hilo. Mimi sina jibu kwa hilo na kama mtu hapendi kuvuliwa nguo kwanini umvue mwenzako,” alisema Dk Hosea.

"Mjadala huu aachiwe Waziri Mkuu Mizengo Pinda na aliyeuliza swali hilo hanitendei haki kwani hakuna hoja nyingine ya maendeleo kwa jamii ambalo inaweza kujadiliwa... mbona mnang’ang’ania kujibu hilo pekee.

“Najua kuna watu wanatumiwa ili niongee halafu nibabaike katika kujibu na nishindwe kufanya kazi yangu. Mbona mnang’ang’ania jambo hilo tu wakati kuna hoja nyingine za maendeleo kwa jamii. Kuhusu suala la Richmond sijibu ng’o.”.


Baada ya wabunge kuona hoja hiyo imepingwa kwa nguvu na mkurugenzi huyo, kulitokea minong’ono ya chini iliyosababisha kutokuwepo kwa usikivu katika ukumbi ndipo mwenyekiti wa APNAC, Dk Zainabu Gama alisimama na kuomba usikivu kwa wabunge hao akisisitiza wafuate kilichowapeleka pale.

“Jamani naomba tusikilizane, mimi kama mwenyekiti naomba tuzingatie suala lililotuleta hapa na maswali yatakayoulizwa yaendane na mada inayotolewa na si vinginevyo,” alisema Dk Gama.

Hata hivyo, Dk Gama alisema Takukuru kwa kushirikiana na wabunge wanachama wa APNAC wasaidiane kuandaa mafunzo na semina kama hizo kwa wananchi katika majimbo yao.

“Sisi ni muhimu sana na tunaamini kwamba kiongozi, mwanasiasa au mtendaji yoyote akiingia madarakani kwa rushwa, hataweza kusimamia mapambano dhidi ya rushwa kwa uhakika. Sisi wabunge wanachama wa APNAC tuwe ndio mfano,” alisema Dk Gama.

Sakata la Richmond liliibuka mwaka 2006 wakati nchi ilipokumbwa na ukame mkubwa uliosababisha mgawo wa umeme na hivyo kuchukuliwa hatua za kutafuta kampuni ya kuzalisha umeme wa dharura. Katika mchakato wa kutafuta kampuni hiyo, ndipo Richmond iliposhinda zabuni hiyo kwa njia ambazo zilitia shaka kubwa.

Lakini Takukuru ilipofanya uchunguzi wake, iliibuka na ripoti kuwa hakukuwepo na mazingira ya rushwa katika utoaji wa zabuni hiyo na kwamba sakata hilo halikuiingizia serikali hasara. Suala hilo lilipoibuka tena bungeni, iliundwa kamati teule iliyokuwa chini ya mbunge wa Kyela, Dk Harrison Mwakyembe ambayo ripoti yake ilisababisha Edward Lowassa kujiuzulu uwaziri mkuu, huku ikipendekeza baadhi ya watendaji, akiwemo Dk Hosea, kuchukuliwa hatua.

Waziri Mkuu Mizengo Pinda, katika taarifa yake ya utekelezaji wa mapendekezo ya bunge, alisema tayari Dk Hosea na wengine wameshaandikiwa barua ya kutakiwa kujieleza kuhusu kuhusika kwake kwenye kashfa hiyo. Bunge lilishauri Dk Hosea achukuliwe hatua na mamlaka husika.

Kuhusu semina hiyo, Dk Hosea alisema ina malengo ya kutoa elimu kwa wabunge wote kuhusu suala la rushwa na kuongezea kuwa utaratibu huu umekuja baada ya mkutano mkuu uliofanyika Kigoma ukishirikisha halmashauri za wilaya 103.

“Hivi sasa ofisi zetu zipo katika halmashauri 103 za wilaya na kwamba jambo la msingi na kuzingatiwa ni kuwa Takukuru pekee haiwezi kupambana na rushwa isipokuwa kwa kushirikiana na jamii nzima,” alisema Dk Hosea.

Alisema semina hiyo itatoa mafunzo mbalimbali ikiwa ni pamoja na kuhakikisha fedha za serikali zinafika mahali panapohusika bila ya kufanyiwa ujanja au hujuma yoyote.

Pia baadhi ya wabunge walisema rushwa sio kwa watumishi wa serikali pekee bali hata kwa baadhi ya wananchi waomba rushwa na kwa kudhihirisha hilo mbunge wa Magu, Dk Festus Limbu (CCM) alionyesha baadhi ya ujumbe aliotumiwa na baadhi ya wapigakura wake.

“Mimi nimetumiwa ujumbe na mwananchi ambaye hakutaja jina lake akinitaka nimtumie fedha na ujumbe unasema hivi ‘wewe mheshimiwa tunakubipu hutaki kutupigia, wewe si mheshimiwa nitumie hela Sh6,000 mimi ni mtu wako wa Magu I WISH U BEST’ na ujumbe mwingine ulisema ‘hautapata kura 2010 tunakuomba hela hautaki,’” alisema Dk Limbu.

Maoni yake yaliungwa mkono na wabunge wengine walioelezea kuwa pamoja na kutoa huduma nzuri kwa wananchi, bado baadhi ya wananchi wanadai kupewa fedha na kuwatishia mambo mbalimbali, likiwemo la kutajwa katika kura za maoni za wahusika wa mauaji ya walemavu wa ngozi, wauzaji wa dawa za kulevya na majambazi.
 
Hosea anatakiwa ajiuzulu,ujasiri huo wa kushambulia kaupata wapi?Wabunge mshinikize huyo mtetezi wa mafisadi anang'oka kwani elimu yake anaitumia visivyo.
 
Maoni ya Wasomaji






mtu said:
BUNGENI NAKO KASHILILAH KATIBU WA BUNGE KACHUKUA WANAFUNZI WA ST.AUGUSTINE WOTE WALIOMALIZA DARASA MOJA HAWANA SIFA ZA KAZI KAWAJAZA NA KUACHA WATU WANAOSTAHIKI.SABABU NI WAKATOLIKI WENZAKE.HUYU JAMAA ANA PhD.kama HOSEA.NAE FAILURE MKUBWA.


 
KAMA alivyo na Kiburi RA sasa Hosea, hii inaonyesha dharau kwa Walipa kodi ambao tunamchangia mshahara wake na leo anatulipa mateke.
 
Basi tena ... hawatarudia tena.

Kaazi kweli kweli .... yaani hakuna mbunge msafi hata mmoja ... yanashambuliwa hivi halafu yanakaa kimya!! Mafisadi.
 
Safi sana Hosea!Umewapa fact wanajua sana kuangalia kwenye "majicho"ya wenzao kabla hawajatoa boriti zao!
 
Safi sana Hosea!Umewapa fact wanajua sana kuangalia kwenye "majicho"ya wenzao kabla hawajatoa boriti zao!

siawakamate basi, yeye si ndiye aliyeshika mpini...
dada acha kutetea ufisadi ameulizwa swali ajajibu
atuambie kwa nini richmond inatesa mpaka leo, na athibitishe gharama za ofisi yake na sio kumtoa kafara liyumba peke yake
 
Hakyamungu hii sinema imepata waigizaji kweli. Tena hawafuati maelekezo ya muongozaji.
Anyway tunashukuru sana waandishi wa habari kwa kuyaweka pembani matatizo mengine ya wanajamii, naona la rushwa ndo ajenda ya kuuza magazeti yenu. Mtaulizwa nyakati zikifika kwa fursa mlizopewa, tufanyeni biashara tu, au ndo shinikizo la waajiri wenu? andikeni basi hata tafiti kuhusu kero za wananchi.
 

Nakupongeza Bubu kwa kututumia habari mbili za tukio moja. Kwangu mie nimefaidika kwa njia mbili;
Ya kwanza ni ile ya kufahamu jinsi waandishi wanavyotuchezea katika kufata maslaha yao. Kwa mujibu wa mwandishi wa kwanza inamuonyesha kuwa Hosea ni shujaa kwa kuwapasha Wabunge wakati habari ya pili inaonyesha Wabunge ndio waliompasha Hosea. sasa tutapata wapi habari sahihi? Muda na wakati vinazuia kwetu kusoma magazeti yote na kupambanua ipi habari sahihi.
Jambo la pili ni kule kuthibitishiwa kuwa hakuna wasafi miongoni mwa viongozi na vyombo vyetu. Wabunge wanamshutumu Hosea kwa kuwabeba mafisadi na lawama zinamstahiki kwani amekubali kuwa anaficha ufisadi unaofanywa na Wabunge.
Ama kwachombo kama Bunge kuwa na wahujumu wa Taifa ni jambo la kusikitisha sana. Wapi tuende tupate viongozi safi? Wabunge wasifikiri kuwa Ufisadi ni ule wa kina Rostam peke yao na wao wao wa kuhujumu Taifa huku hawatekelezi wajibu si ufisadi.
 

Nimewahi kuona mashahidi mahakamani wakitoa ushahidi wa tukio ambalo waliliona kwa macho yao na wakatoa ushahidi tofauti kabisa! Wengine hata rangi ya nguo alizovaa mtuhumiwa huwa tofauti kabisa. Labda uwezo wa kuweka kumbukumbu ya tukio lilitokea unatofautiana kati ya mtu na mtu.
 
Safi sana Hosea!Umewapa fact wanajua sana kuangalia kwenye "majicho"ya wenzao kabla hawajatoa boriti zao!

Mimi naona Hosea anazidi kuchemka.
1. Anataka kupigana na Rushwa huku akiwa na tuhuma nzito za RICHMOND, ambapo nae hawezi kutenganishwa na rusha
2. Anajua kuwa hili doa ni kibwa lakini hataki kujibu hoja badala yake anatumia ubabe na jeuri ya madaraka kuwatisha wabunge, kwani kupandikiza kesi ya rushwa kwa raia yeyote tanzania sio kazi kubwa.
3. Anaonekana kufahamu fika jinsi watu maarufu wanavyojishughulisha na vitendo vya rushwa, ila kwa kuwa wao ni wateule hawaulizwi, ila pale ambapo wanaonekana kumuingiza kidole jichoni.

Mimi sioni sababu ya msingi, pia kwa majibu yake hana sifa zozote kuendelea kuwa kiongozi Takukuru. Ila Tanzania, teuzi hizi zipo kulinda masilahi ya wenye meno ya kula nchi. Hebu Hosea abishe tukusikie.
 
This Hosea guy is a failure in his own way. Nikikumbuka clean up ya Richmond nakosa hata raha kabisa!! Mpuuzi mpumbavu kabsaaa
 
Tanzania moto ! Ccm moto! CCm inawenywe !!serekali inawenywe .wabunge nao ???inaonesha sasa ndio ule mwisho wa njia(end of the road ) kwa wabunge kuonesha kuwa wao ndio watetezi wa nchi alhali wanamaovu mazito kutokana na kauli ya mr horse wabunge hao huyaficha maovu yao kwa kutumia neno kuikosowa serekali kwa maana hii serekali mpaka ubungeni kumeoza ni sawa kusema la kuvunda halina ubani.
 
Hii takururu takukuru whatever the name is ilipashwa kuvunjwa na kuanzishwa taasisi mpya kabisa. Tanzania inabidi tuendeshe kijeshi jeshi hii kuleana kama watoto wadogo au kuuguza kidonda ndugu tumechoka. Wabunge waongo wanafiki na Hosea vile vile wote mmeshindwa kazi mnajua kutetea maslahi yetu tu na si maslahi ya wananchi waliowaweke madarakani. Waangalie kinachotokea Moshi hii ni dhahiri wananchi wamechoshwa na mchezo wenu wa kuigiza. Wabunge na Hosea wote wanabebana tu hicho kikao ni kutuzuga watanzania hamna lolote kwendeni zenu. Mahakama za bongo ndio kabisaaaaaaa zimeoza kesi ya ufisadi miaka miwili jamani kwani ushahidi mnasubiri meli ije toka china au kisiwa cha kufikirika ndio muwahukumu hawa watu.
 
MKURUGENZI wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (Takukuru), Dk Edward Hosea jana alikuwa kwenye wakati mgumu baada ya wabunge kumhoji uhalali wake wa kuiongoza taasisi hiyo wakati akikabiliwa na tuhuma za kusafisha kashfa ya zabuni ya mitambo ya kuzalisha umeme wa dharura.

Mkurugenzi huyo, ambaye alitajwa kwenye taarifa ya tume teule ya bunge iliyochunguza kashfa hiyo na serikali kutakiwa kumchukulia hatua, alikumbwa na mtafaruku huo katika semina ya Miundombinu ya Uadilifu iliyoandaliwa na Takukuru na Chama cha Wabunge wa Afrika (APNAC) na kufanyika kwenye hoteli ya Whitesands jijini Dar es salaam.
Ilifikia wakati Dk Hosea alionekana kukerwa sana na maswali kiasi cha kulazimika kuwaonya kuwa anao uwezo wa kuwachafua kama wakiendelea kufanya mambo yanayoonekana kumvua nguo.

Mbunge wa Busega, Raphael Chegeni ndiye aliyeanzisha kizaazaa hicho baada ya kumhoji Dk Hosea akisema ilikuwaje taasisi yake iliisafisha kampuni tata ya kuzalisha umeme wa dharura Richmond Development (LLC) iliyokuwa inakabiliwa na kashfa ya kushinda zabuni ya kuzalisha umeme wa dharura wakati kamati teule ya Bunge iliyoundwa kuchunguza mkataba wake, iligundua kuwepo kwa mazingira ya rushwa.
“Inakuwaje wakati wa mjadala wa Richmond, wewe mkururugenzi wa Takukuru ulikanusha kuwapo rushwa na uchunguzi wa kamati ya bunge ulibaini kuwepo rushwa ndani ya kampuni hiyo? Je ni nani mwenye dhamana ya kukuadhibu wewe na taasisi yako kuhusu rushwa’’ aliuliza Chageni.

Swali hilo halikutegemewa na Dk Hosea na lilionekana kumuudhi na kulazimika kuchukua kipaza sauti na kusitisha maswali na kuanza kujibu kwa ghadhabu.
“Hapa siyo jukwaani hivyo tusilete siasa. Nipo hapa kwa ajili ya kufundisha na kama ni suala la Richmond waziri mkuu alishaliongelea na ndiyo mwenye dhamana ya kujibu hilo. Mimi sina jibu kwa hilo na kama mtu hapendi kuvuliwa nguo kwanini umvue mwenzako,” alisema Dk Hosea.


"Mjadala huu aachiwe Waziri Mkuu Mizengo Pinda na aliyeuliza swali hilo hanitendei haki kwani hakuna hoja nyingine ya maendeleo kwa jamii ambalo inaweza kujadiliwa... mbona mnang’ang’ania kujibu hilo pekee.
“Najua kuna watu wanatumiwa ili niongee halafu nibabaike katika kujibu na nishindwe kufanya kazi yangu. Mbona mnang’ang’ania jambo hilo tu wakati kuna hoja nyingine za maendeleo kwa jamii. Kuhusu suala la Richmond sijibu ng’o.”.
 
Cookies are required to use this site. You must accept them to continue using the site. Learn more…