Mrithi wa Regia atajwa
Na Richard Makore
21st January 2012
Ni Diwani wa kata moja wilayani Karatu
Alishika nafasi ya 26 Viti Maalum Chadema
Chama cha Demokrasia na Maendeleo (Chadema), kimesema mwanamke aliyeshika nafasi ya 26 katika majina 102 yaliyopelekwa Tume ya Taifa ya Uchaguzi (Nec), mwaka 2010 kwa ajili ya kufanyiwa uteuzi wa ubunge wa viti maalum, ndiye atakayemrithi marehemu Regia Mtema, aliyefariki dunia wiki iliyopita.
Katibu Mkuu wa Chadema, Dk. Willibrod Slaa, alisema hayo alipotakiwa na NIPASHE kutoa ufafanuzi kuhusu nafasi iliyoachwa wazi baada ya kifo cha marehemu Regia.
Habari zilizopatikana kutoka makao makuu ya Chadema, zinaeleza kuwa mwanamke aliyeshika nafasi ya 26 katika majina 102 yaliyopelekwa Nec, mwaka 2010 kwa ajili ya kufanyiwa uteuzi wa ubunge wa viti maalum, ni Cecilia Daniel Pareso.
Cecilia ni Diwani wa Kata ya Qurus, iliyoko katika Halmashauri ya Wilaya ya Karatu, mkoani Arusha.
Habari nyingine zinaeleza kuwa awali, mwanamke aliyekuwa akishika nafasi ya 26 ni aliyekuwa Mwenyekiti wa Baraza la Wanawake wa Chadema (Bawacha), Leticia Mosore, ambaye baadaye alihamia chama cha NCCR-Mageuzi.
Dk. Slaa alisema utaratibu wa kuwapata wabunge wa viti upo wazi kwa mujibu wa sheria na kwamba Chadema hawana mamlaka ya kuongeza wala kupunguza kitu chochote.
Alisema Chadema imeishamuandikia barua Spika wa Bunge, Anne Makinda, kumuarifa rasmi kwamba kuna nafasi iliyo wazi, ambapo naye ataiandikia barua Nec kwa ajili ya kufanya uteuzi rasmi.
Dk. Slaa alisema kuwa kama kutakuwa na mabadiliko ya mtu aliyeshika nafasi hiyo ya 26, ikiwamo mtu huyo kupoteza sifa ya kuwa mbunge kwa kuhama chama ama kuonekana na upungufu mwingine ambao unamnyima sifa, Chadema itaiandikia barua Nec ili achukuliwe mtu mwingine aliyeshika nafasi ya 27.
Alisema kama namba 26 na 27 wote hawatakuwa na sifa, Nec itachukua jina litakalofuata namba 28 ili kufanya uteuzi wa kiti hicho.
"Sisi kwa hili tulishalimaliza mwaka 2010 na tunachoweza kufanya kwa Nec ni kuisaidia itakapotaka maelezo yetu juu ya jina linalotakiwa kufanyiwa uteuzi," alisema Dk. Slaa.
Alisema mwaka 2010 walifanya kazi kubwa na kupata majina 102 ambayo yote yana sifa za kuwa wabunge wa viti maalum na kwamba, Nec ndiyo yenye mamlaka yote ya mwisho na sio Chadema.
Chadema kina wabunge wa viti maalum 25 katika Bunge la 10.
CHANZO: NIPASHE