Haya ni machache tu kati ya mengi yaliyowakuta wagombea wa CCM kwenye uchaguzi mwaka 2010;
- WATU kumi akiwemo Waziri wa Maendeleo ya Jamii, jinsia na watoto, Magreth Sitta, wamekamatwa na kuhojiwa na Takukuru kwa tuhuma za kutaka kuwapa rushwa wajumbe wa Mkutano Mkuu wa UWT, mkoa wa Tabora. Naibu Mkuu wa Takukuru mkoa wa Tabora, Bruno Rwenyagira aliwaambia waandishi wa habari jana kuwa Takukuru iliwakamata watu hao juzi usiku, ikawahoji na kuwaachia huku ikiendelea na uchunguzi.
- Katika mchakato wa kura za maoni unaoendelea ndani ya CCM, mkuu wa wilaya ya Kasulu, Betty Machangu alinaswa akiwa na wajumbe wa UWT kwenye chumba katika nyumba ya kulala wageni na akakutwa akigawa fedha, nguo na asali. Machangu ambaye anawania ubunge wa viti maalumu kupitia CCM mkoa wa Kilimanjaro, alinaswa na maofisa wa taasisi hiyo ya kuzuia na kupambana na rushwa akiwa pamoja na viongozi waandamizi wa Jumuiya ya Wanawake wa CCM, ngazi ya mkoa na wilaya.
- Shija Felician anaripoti kutoka Bukombe kwamba Takukuru mkoani Shinyanga imemnasa mwenyekiti wa Mamlaka ya Mji mdogo wa Bukombe, Benedikitor Yohana na mkewe Veneranda Basima wakigawa fedha zilizotolewa na mgombea ubunge wa CCM katika jimbo la Bukombe kwa ajili ya kuwahonga wapigakura. Kamanda wa Takukuru mkoani Shinyanga Reonada Ngaiza alisema mwenyekiti huyo na mkewe walikamatwa juzi usiku nyumbani kwao wakiwa na pesa taslimu Sh 150,000 na doti mbili za vitenge.
- Anthony Mayunga anaripoti kutoka Mara kwamba, mmoja wa wanaCCM wanaoomba kuteuliwa na chama hicho kugombea ubunge katika jimbo la Tarime, amekimbilia ofisi ya CCM wilaya kukwepa kukamatwa na Takukuru. Habari kutoka Tarime zilisema kuwa tukio hilo lilitokea tukio hilo lilitokea jana majira ya saa 2:00 asubuhi wilayani humo.
- Zaina Malongo na Hussein Issa wanaripoti kutoka jimbo la Ubungo kwamba; wafuasi wa wagombea wa nafasi ya kuwania ubunge kupitia CCM, Shamsa Mwangunga na Nape Nnauye jana walipigana ngumi katika kampeni zinazoendelea jimboni humo. Habari zimeeleza kuwa ugomvi ulianza katika kata ya Ubungo Tanesco baada ya wafuasi hao kuchaniana vipeperushi vinavyoonyesha sura za wagombea hao wawili.
Vitendo kama hivi vilienea nchi nzima lakini hadi leo hakuna, narudia hakuna, hata mmoja kati ya hawa mafisadi aliyewajibishwa, TAKUKURU my foot! Kwa hakika naichukia CCM!