nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,860
- 5,803
16 APRIL 2012
*Kauli za wagombea zachochea uvamizi wa shamba
*Wananchi waharibu mali, nyumba za wawekezaji
*Wadai kuambiwa mashamba hayo ni mali yao
Na Queen Lema, Meru
ZAIDI ya wakazi 300 waishio Kata za Maji ya Chai na Maroroni, Wilaya ya Arumeru, mkoani Arusha, juzi walivamia shamba la mwekezaji zaidi ya ekari 6,000 lijulikanlo kama Doll Estate.
Mbali ya uvamizi huo, wakazi hao waliwavua nguo zote walinzi wa shamba hilo, kuharibu mali na kuiba vifaa mbalimbali.
Akizungumza na Majira jana, Msimamizi wa Idara ya Wanyama katika shamba hilo, Bw. Robson Peter, alisema wakazi hao walifanya uvamizi huo saa 11 jioni.
Alisema wakazi hao walidai kuwa, shamba hilo ni mali yao kama walivyoambiwa na baadhi ya wagombea ubunge katika uchaguzi mdogo Jimbo la Arumeru Mashariki.
"Wananchi waliovamia shamba hili ambalo linahusika na ufugaji wa wanyama mbalimbali kama twiga, swala, pundamilia na wengine walikuwa na silaha za jadi wakidai kuwa, hawataki kuona wawekezaji wa kizungu ndani ya shamba hili," alisema.
Bw. Peter alisema baada ya wananchi hao kuingia ndani ya shamba wakiwa wamevunja ukuta wenye urefu wa zaidi ya kilomita nne, waliwakamata walinzi, kuwavua nguo zote na kuwapa adhabu huku wengine wakiendelea kufanya uharifu wa mali katika nyumba za wawekezaji.
Alisema kutokana na uvamizi huo, walilazimika kutoa taarifa Kituo ch Polisi Meru ambacho kilituma askari ambao ndio waliofanya kazi ya kuwatawanya wavamizi hao kwa mabomu ya machozi.
Awali baadhi ya wawekezaji katika shamba hilo ambao hawakupenda majina yao yatajwe gazetini, walisema kilichofanywa na wananchi waliofanya uvamizi huo hasa kutoka Kijiji cha Kitefu si cha uungwana kwani walikuwa wakiishi kwa ushirikiano mkubwa.
"Sisi tupo katika shamba hili kwa mujibu wa sheria, tunashangaa wakazi wa kata hizi kusema hawataki kutuona wakati sisi tuna haki, leo hii wamevunja nyumba zetu na kuchukua mali, hatujapendezwa na hali hii hata kidogo," walisema wawekezaji hao.
Hata hivyo, baadhi ya wakazi wa kata hizo walisema kuwa, kuvamiwa kwa wawekezaji hao kunatokaa na kauli za siasa zilizotolewa na viongozi mbalimbali kwenye kampeni za uchaguzi mdogo jimboni humo.
"Juzi viongozi wa vyama viwili ambavyo vilikuwa vinachuana walidai haya mashamba ni mali ya wananchi ambao waliamua kwenda kufanya uvamizi ili kuchukua shamba hili, nguvu ya ziada inahitajika ili kukomesha tabia hii," walisema.
Diwani wa kata ya Maji ya Chai Bw. Loti Nnko, naye alijionea uharibifu wa mali za wawekezaji na kudai hadi sasa, thamani halisi ya uharibifu huo haijajulikana.
Kamanda wa Polisi mkoani hapa, Thobias Andengenye, amethibitisha kuwepo tukio hilo na kudai jeshi hilo linaendelea kufanya uchunguzi zaidi.