Yalikuwa ni mapenzi haramu yaliyomwaga damu

Mtambuzi

Platinum Member
Oct 29, 2008
8,810
15,398
attachment.php


Mchungaji Andras Pandey na mwanae Agnes

201003201233-1_gemeente-gaat-huis-andras-pandy-afbreken-.jpg
Mchungaji Andras Pandey


_1827312_pastor_300_afp.jpg
Mchungaji Andras Pandey akifikishwa mahakamani

pandy_463.jpg
Mchungaji Andras Pandey

media_l_974920.jpg
Agnes Pandey


Wakati mwingine yapo madai yanayoweza kufikishwa kwenye vyombo vya usalama kwa ajili ya kufanyiwa uchunguzi lakini kutokana na kutoyachukulia madai hayo kwa umakini hatimaye huonekana kama hadithi ya kufikirika. Na hivi ndivyo ilivyotokea nchini Ubelgiji. Mnamo mwaka 1992 mwanamke mmoja aliyekuwa na umri wa miaka 34 wakati huo aitwae Agnes Pandy, binti wa mhamiaji wa Kihangari ambaye ni mhubiri wa Kiprotestant aitwae Andras Pandy, alikwenda Polisi na kuwaeleza kwamba, yeye na baba yake mzazi wamekuwa kwenye uhusiano haramu wa kimapenzi tangu akiwa na umri wa miaka 13.

Alizidi kuwaeleza Polisi kwamba, katika kipindi chote walichokuwa kwenye uhusiano huo wa kimapenzi walihusika na mauaji ya ndugu zao wapatao 6 ambao ni mama yake mzazi, mke wa pili wa baba yake na kaka zake, pamoja na dada zake wa kufikia. Taarifa zile hazikupokelewa kwa uzito unaostahili na Polisi, kwani walimwona yule binti kama mtu aliyechanganyikiwa. Hata hivyo polisi waliamua kufanya uchunguzi ambao pia hawakuupa uzito wowote. Wapelelezi hao wa Polisi walikwenda nyumbani kwa mchungaji na Andras Pandy na kumhoji kuhusiana na madai ya binti yake. Mchungaji huyo alikanusha madai hayo ya binti yake kwa kuwaeleza Polisi kwamba, watu wote waliotajwa na mwanaye kuwa wameuawa siyo kweli kwani wako hai na salama salimini. Akifafanua zaidi alisema, watu watatu kati ya hao waliotajwa, walirudi nchini Hangari na wengine wako nchini Amerika ya kusini wakifanya shughuli za kimisionari. Ili kuthibitisha madai yake mchungaji Pandy alitoa lundo la barua zinazoonyesha kwamba alikuwa akiwasiliana na hao wanafamilia wake. Mnamo Septemba 1997 Polisi waliamua kumhoji kwa mara nyingine Agnes Pandy ambaye kwa wakati huo alikuwa anafanya kazi katika maktaba ya Albert Royal, kama mkutubi. Katika hali isiyotarajiwa Agnes alithibitisha kutokea kwa mauaji hayo ingawa likiri kwamba taarifa zake za awali hazikuwa sahihi kwa sababu idadi ya ndugu zake waliowauwa yeye na baba yake haikuwa kubwa kama alivyoeleza.

Kwa maneno yake mwenyewe Agnes aliwaambia Polisi, ‘nitawaeleza namna mimi na baba tulivyo wauwa ndugu zetu watano.' Katika maelezo yake Agnes alisema , mnamo mwaka 1986 aligundua kwamba Timea dada yake wa kufikia aliyekuwa na umri wa kiaka 22 wakati huo alikuwa na uhusiano wa kimapenzi na baba yake, kama yeye, ambapo pia alipata ujauzito na hatimaye kujifungua mtoto wa kiume. Hivyo katika hali ya kuona wivu, Agnes alitaka kumuuwa Timea kwa kumtwanga kwa nyundo kichwani, lakini Timea alinusurika katika jaribio hilo na hivyo akatorokea kwanza, Canada na baadae Hangari akiwa na kichanga chake. Baadaye yalifuatia mauaji yaliayoanzia mwaka huo huo wa 1986 na kukoma mwaka 1989.

Mtu wa kwanza kuingia kwenye orodha yao ya mauaji alikuwa ni mke wa pili wa baba yake aitwae Edith Fintor ambaye alifuatiwa na binti yake aliyekuwa na umri wa miaka 14 aliyekuwa akiitwa Andrea ambaye Edith alimzaa katika ndoa yake ya kwanza kabla hajaolewa na Mchungaji Andras Pandy.
Mtu mwingine aliayefuatia, Agnes aliwaeleza Polisi kwamba alikuwa ni mama yake mzazi, Ilona Sores ambapo Agnes alikiri kwamba alimuua kwa mkono wake mwenyewe kwa kumpiga risasi kichwani. Baadae kwa kushirikiana na baba yake waliwauwa kaka zake waliozaliwa tumbo moja walioitwa Daniel aliyekuwa na umri wa miaka 27 na Zoltan aliyekuwa na umri wa miaka 22. Dada yake mwingine wa kufikia aitwae Tunde alitoweka katika mazingira ya kutatanisha ambapo Agnes alikanusha kujua lolote kuhusiana na kutoweka kwake.

Watu wote waliouawa, Agnes alibainisha kwamba waliuawa kwa kuwapigwa risasi ama kwa kuwatwanga na nyundo kubwa kichwani. Pia Agnes aliwajulisha Polisi kwamba mauaji yote aliyoyafanya, yalikuwa yakiratibiwa na baba yake ambapo pia ndiye aliyekuwa na jukumu la kuzika miili ile.
Akieleza namna yeye na baba yake walivyokuwa wakiifanya miili ile ya watu waliowauwa, Agnes alisema kwamba walikuwa wakiikatakata kwa kutumia visu vya jikoni na shoka na kisha kuiweka kwenye mifuko ya nailoni ya kuhifadhi uchafu na kwenda kuitupa jirani na eneo la machinjioni na mabaki mengine ya miili hiyo ilikuwa ikitumbukizwa kwenye pipa la lita 25 lilowekwa kemikali ya kusafishia vyoo ambayo inaweza kuyeyusha mwili wa binadamu na kuacha mifupa peke yake. Baada ya kupata maelezo yale, Polisi waliridhika na maelezo ya Agnes na moja kwa moja Mchungaji Andras Pandy na mwanae walikamatwa na kuwekwa ndani ili uchunguzi zaidi ufanyike. Hatua ya kwanza waliyochukuwa Polisi ni kuchunguza nyumba zake tatu ambazo zilikuwa katika wilaya ya Molenbeek.

Walipofika katika nyumba ya kwanza walikuta chumba ambacho kilikuwa na mlango wa chuma, kilikuwa kikionesha kama kilitelekezwa na hakitumiki tena.
Walivunja ule mlango wa chuma na kuingia ndani na kuanza uchunguzi wao ,ambapo walikuta kikasha kidogo ambacho kilikuwa na majivu ambayo yalikuwa yanaonyesha dhahiri ni ya mwili wa binadamu. Pia ndani ya chumba hicho walikuta jokofu mkubwa ambalo ndani yake kulikuwa na nyama mbichi zilizogandishwa kwa barafu ambazo nazo pia zilikuwa zikionesha kuwa ni za binadamu. Polisi waliondoka na ushahidi ule na kuhamia katika eneo lingine la ghorofa ya chini (basement) la nyumba hiyo huku wakiwa na rada maalum ya kuchunguzia mabaki ya binadamu yaliyozikwa chini ya ardhi. Kwa msaada wa rada ile waliweza kugundua eneo yalipozikwa mabaki ya miili ya binadamu, walipochimba walikuta mifupa na mafuvu ya vichwa vya binadamu ambavyo vilikuwa vinaonesha kuwa siyo vya mtu mmoja bali watu watatu.

Msemaji wa Polisi aitwae Joe Coplin aliwaeleza waandishi wa habari kwamba, uchunguzi hauhusishi tu watu wa familia ya mchungaji Andras Pandy peke yake, bali pia wanachunguza uwezekano wa kuwepo kwa mabaki ya miili ya watu kumi wa miongoni mwao wakiwepo waumini wa kanisa lake pamoja na washiriki wake walioripotiwa kutoweka katika mazingira ya kutatanisha nchini Hangari na Slovakia, akiwepo mtoto wake wa kufikia kwa mama mwingine aliyekuwa na umri wa miaka 12 aliyeitwa Adi Berta, ambaye naye alitoweka katika mazingira ya kutatanisha akiwa shuleni kwao mwaka 1993, ikiwa ni wiki moja tu tangu Andras Pandy na mama wa mtoto huyo kutengana.
Nchi ya Ubelgiji ilizizima kwa mshtuko baada ya gazeti moja nchini humo liitwalo Le Soir, kuandika habari za kukamatwa kwa mchungaji Andras Pandy kwa tuhuma za mauaji ya kutisha yakihusisha watu wa familia yake.

Hebu sasa tujiulize, je huyu Andras Pandy ni nani? Kwa nini alihusishwa na mauaji ya kutisha ya watu wa familia yake mwenyewe? Na kwa nini kutoweka kwa wanafamilia yake katika mazingira ya kutatanisha hakujaripotiwa sehemu yoyote ambapo huenda kungekomesha mauaji hayo ya kutisha na kuokoa maisha ya watu wengine?

Taarifa za kumbukumbu zinaonesha kwamba, Mchungaji Andras Pandy alikuwa ni mhubiri wa dhehebu la Kigiriki la Orthodox na yeye na mkewe Ilona Sores ambaye baadaye alikuja kuuawa na mwanae wa kumzaa mwenyewe Agnes Pandy wakati huo akiwa na miaka miwili waliondoka nchini Hangari mnamo mwaka 1956 baada ya kutokea mapinduzi ya kupinga Ukomunisti.

Familia hiyo ilihamia nchini Ubelgiji na kuweka makazi yao katika jiji la Brussels. Miaka miwili baadae mchungaji Andras Pandy akawa ni mchungaji wa Kiprotestant na mwalimu wa dini katika kanisa hilo. Katika miaka yote ambayo mchungaji Andras Pandy alikuwa nchini Ubelgiji hadi kukamatwa kwake kwa tuhuma za mauaji , alipata kuwa na wanawake watatu ambapo alifanikiwa kupata watoto nane ambao miongoni mwao watoto watatu ndio walioko hai na ambao wanaishi nchini Ubelgiji.
Watu wa karibu wanaomfahamu mchungaji huyo walimwelezea kama mtu aliyekuwa na mamlaka na msiri mkubwa aliyekuwa na tabasamu la muda mfupi lilofananishwa na la waumini wa Budha, kama alivyoelezea mwanafunzi wake wa dini Ludovicusvan Makat.

Pia walimwelezea kama mtu katili katika familia yake na aliyekuwa akiendesha nyumba yake kwa mkono wa chuma. Lakini suala moja lililokuwa likiwaumiza Polisi vichwa ni kwamba, ni kwa nini mchungaji huyo alikuja kuwa muuaji wa watu wake mwenyewe?
Kwa mujibu wa watafiti wa masuala ya kihalifu walisema kuwa kuna uwezekano mkubwa kwamba, kila mauaji aliyofanya Andras Pandy ni katika kuficha mauaji aliyofanya awali na hiyo ilisababisha muendelezo wa mauaji hadi wakajikuta wanabaki peke yao, yeye na bintiye. Watafiti hao pia walibainisha kwamba, sababu nyingine iliyochangia kuwepo kwa mauaji hayo ni kutokana na athari za kisaikolojia zinazotokana na mahusiano ya kimapenzi kati ya baba na bintiye wa kumzaa mwenyewe.

Mara baada ya kesi ya Mchungaji Andras Pandy kuripotiwa kwenye vyombo vya habari vya nchini Ubelgiji kwa mara nyingine idara ya Polisi ya Nchini Ubelgiji ilianza kunyooshewa vidole vya lawama na wananchi kwamba, ilizembea kwa kutochukua hatua madhubuti tangu awali baada ya Agnes Pandy kutoa taarifa ya mauaji waliyoyafanya na baba yake. Wananchi hao hawakusita kuufananisha uzembe huo na ule wa kesi mtekaji nyara wa watoto wa kike na kuwauza kwa wafanyabiashara wa madanguro katika nchi za Ulaya Marc Dutroux.
Polisi kwa upande wao hawakusita kujitetea. Hata hivyo walisema kwamba hakuna uwiano wowote kati ya kesi ya Andras Pandy na Marc Dutroux, ingawa walikiri kwamba kulikuwa na uzembe uliofanyika.

Akizungumza na waandishi wa habari, msemaji wa Polisi alisema kuwa Andras Pandy ameshahojiwa na kukiri kuhusika na mauaji hayo, lakini hata hivyo Polisi hawakusita kuwanyooshea vidole majirani wa Andras Pandy pamoja na watu wake wa karibu kwamba, iweje ndani ya miaka kumi tangu watu wa familia ya Mchungaji huyo waanze kutoweka mmoja mmoja katika mazingira ya kutatanisha asiwepo hata mmoja wa kutilia shaka na kuwajulisha Polisi!
Msemaji huyo aliandelea kudai kwamba, kama wangejulishwa japo hata kutoweka kwa mtu mmoja huenda wangeyachukulia maelezo ya Agnes Pandy kwa umakini wa hali ya juu katika kukusanya ushahidi zaidi. Polisi wa nchini Ubelgiji kwa kushirikiana na Polisi wa nchini Hangari walikuja kugundua kuwa katika hali ya kuficha tuhuma za mauaji aliyoyafanya, mchungaji Andras Pandy alidanganya kwa kuandika historia ya uongo kuhusu maisha katika mfumo wa kutengeneza filamu (Scripts) na kuajiiri vijana wawili waishio nchini Hangari waliokuwa na umri wa kati ya miaka 22 na 24 ambao aliwapa majina ya Andrea na Tunde kama majina watakayotumia katika kuigiza filamu hiyo.

Aliwadanganya vijana hao kwa kuwaambia kwamba anataka kuengeneza filamu inayohusu maisha yake na familia yake kwa ujumla, kuhusu maiasha yake tangu alipokuwa nchini Hangari hadi alipohamia nchini Ubelgiji. Aliwakabidhi wale vijana zile script za filamu na katika hali ya kuzifanyia mazoezi walikuwa wakiwasiliana kwa barua wakitumia yale majina ya bandia aliyowapa mchungaji Pandy. Kwa kufuata mfumo wa zile script kulikuwa na wakati wale vijana walilazimika mkusafiri kutoka nchini Hangari na kwenda nchini Ubelgiji kama vile walikuwa wakimtembelea baba yao na wanapofika nchini ubelgiji walikuwa wakitumia yale yale majina waliyopewa na mchungaji Pandy.
Zile barua za bandia walizokuwa wakiandikiana kati ya mchungaji Pandy na wale vijana ndizo zilizomsaidia kuwadanganya Polisi mwaka 1992 wakati kwa mara ya kwanza, Agnes aliporipoti Polisi kuhusu mauaji aliyoyafanya kwa kushirikia na na baba yake.

Hata hivyo, Polisi katika uchunguzi wao kwenye nyumba ya Andras Pandy waligundua pia mihuri ya bandia ya Posta za Miami nchini Marekani, Brazili na Israel, mihuri ambayo alikuwa akiitumia kughushi barua mbalimbali ili kuonesha kwamba wanae aliokuwa amewauwa, walikuwa hai wakiishi katika nchi hizo.
Polisi wa nchini Hangari pia walibainisha kwamba mchungaji Pandy alikuwa ameanzisha vituo kadhaa vya kulelea watoto yatima nchini Humo ambapo alikuwa akikusanya misaada kutoka kwa wafadhili mbalimbali. Misada hiyo ndiyo inayohisiwa kwamba, ndiyo aliyoitumia katika kununua nyumba tatu nchini Ubelgiji ambazo alikuwa akizimiliki. Ushahidi mwingine uliokusanywa ulitoka kwa mchungaji mwenzake ambaye alikuwa anawafahamu vizuri Pandy na mkewe Fintor ambapo aliielezea ndoa yao kuwa ilikuwa ni kama ya mtu na mtumwa wake, kwa jinsi Pandy alivyokuwa akimnyanyasa mkewe huyo wa pili ambaye alimuoa baada ya mkewe wa kwanza Ilona kuuawa na mwanae Agnes.

Katika kipindi hicho hicho zilikuwepo taaarifa zilzofikishwa Polisi na watu waliokuwa wakijenga mfereji wa maji machafu karibu kabisa na nyumba ya Mchungaji Pandy ambapo walikuta mabaki ya mifupa ya binadamu wakati wanachimba mtaro. Katika hali ya uzembe ule ule wa Polisi, hakuna hatua zozote zilizochukuliwa katika kuchunguza uhusiano wa ile mifupa iliyookotwa na taarifa za kutoweka kwa wanafamilia wa Mchungaji Pandy. Katika hali nyingine isiyo ya kawaida mabaki yote ya miili iliyofuliwa nyumbani kwa mchungaji Pandy hakuna hata mabaki ambayo vipimo vyake viliwiana na watu wa familia yake. Hivyo kufanya kutambuliwa kwa mabaki yale kuwa kitendawili. Ilikuwa ni Februari 2002 ndipo mchungaji Andras Pandy na mwanane Agnes Pandy walipofikishwa mahakamani. Mchungaji Pandy alishitakiwa kwa makosa mawili ambayo ni kuwabaka binti zake na kosa la pili lilikuwa ni kuhusika na mauaji ya watu sita ya familia yake. Naye Agnes alishtakiwa kwa makosa mawili pia, kosa la kwanza liliwa ni lile la jaribio la kutaka kumuuwa dada yake wa kufikia aitwae Timea, jaribio ambalo lilishindwa. Na kosa la pili lilikuwa ni lile la kuhusika na mauaji ya watu watano wa familia yao.

Akitoa maelezo yake mahakamani, Agnes alieleza kwa kirefu jinsi baba yake alivyombaka akiwa na umri wa miaka 13 na kumgeuza kuwa mtumwa wake wa ngono kwa kipindi cha zaidi ya miaka 20. Aliendelea kuileza mahakama jinsi jaribio lake la kutaka kumuuwa dada yake aitwae Timea lilivyoshindwa na jinsi yeye na baba yake walivyofanya safari za kwenda nchini Hangari kumtafuta Timea wamuuwe na kupoteza ushahidi ambapo juhudi zao hazikufanikiwa. Pamoja na kwamba, mchungaji Pandy alifikishwa mahakamani kwa mauaji ya kutisha aliyoyafanya takriban miaka 20 iliyopita, lakini aliidhihirishia mahakama kuwa Polisi bado hawakuwa na ushahidi madhubuti wa kumtia hatiani. Akizidi kuishangaza Mahakama, mchungaji Pandy alidai kwamba, watu wote waliotajwa kuwa amewauwa, wapo hai wakiendela kuitumikia jamii mahali fulani.

Aliendela kusema, ‘ni jukumu la mahakama kuthibitisha kama ni kweli wamekufa, na ninaamini pindi nitakapoachiwa huru na mahakama hii, watakuja kunitembelea.'
Shauri hilo ambalo lilichukuwa takribani wiki mbili, lilimalizika kusikilizwa mnamo Machi 8, 2002, n iliwachukuwa saa 12 jopo la washauri wa Mahakama, kupitia ushahidi wote uliotolewa na mahakamani na kumtia hatiani mchungaji Andras Pandy kwa makosa ya kuhusika na mauaji ya watu sita likiwamo pia kosa la kuwabaka mabinti zake. Naye Agnes Pandy alitiwa hatiani kwa kosa la kuhusika na mauaji ya watu watano na pia alitiwa hatiani kwa kosa lingine la kujaribu kumuuwa dada yake wa kufikia aliyetajwa kwa jina la Timea. Kwa makosa hayo Agnes alihukumiwa kifungo cha miaka 21 jela na baba yake, mchungji Andras Pandy alihukumiwa kifungo cha maisha jela.
 

Attachments

  • phpThumb_generated_thumbnailjpg.jpg
    phpThumb_generated_thumbnailjpg.jpg
    24.7 KB · Views: 608
Haya Mtambuzi ni Ijumaa nyingine tena kama unavyotimiza ahadi yako siku zote
Nikimaliza kusoma nitarudi na koment
 
Mchambuzo tungo zako ndefuuuuuuuuuu!
Natamani kusoma mmmh muda hautoshi!
 
Kama kawaida ni Ijumaa nyingine tena, nimekuja na mkasa huu ambao ni wa kusikitisha na unatisha kwa kweli. Nashindwa kusema lolote kwa sababu mhusika alikuwa ni Mtumishi wa Mungu. Ni vyema ukiisoma habari hii ukiwa nyumbani mwishoni mwa Juma na familia yako.
 
Du hii picha kali ipo kwenye HBO au mm ntaipitia baadae unajua tena mitandao ya kulipia hata kwenye ka-modem asante sana mtafsiri
 
Huwezi kusoma ukiwa peke yako. Kama horror Movie. Lakin ni kweli ilitokea. Weekend njema Mtambuzi. Next time iwe hadithi ya furaha na sio ya masikitisho na mauwaji kama hii. Si nlikuambia?
 
Back
Top Bottom