Wakubwa sasa matumbo joto; Mali zao kutangazwa hadharani Desemba

nngu007

JF-Expert Member
Aug 2, 2010
15,862
5,797
Mwandishi Wetu - Raia Mwema


228_jk_img_0.png



Rais Jakaya Kikwete

Mali zao kutangazwa hadharani Desemba,
sheria kufumuliwa


Wengi serikalini wajipanga kukwamisha
utekelezaji


Kikwete aiga mfumo huo kwa Rais Obama




KILIO cha muda mrefu cha wadau mbalimbali wa utawala bora nchini, wakiwamo wanaharakati waliokuwa wakipinga usiri katika taarifa za mali za viongozi wa umma kinaweza kupata ufumbuzi. Raia Mwema imepata waraka maalumu unaotaka kuwapo kwa mabadiliko ya Sheria ya Maadili ya Viongozi, ambamo mali zao zitawekwa hadharani.


Waraka huo unaozungumzia utekelezaji wa mpango wa ubia katika kupanua uwazi serikalini (Tanzania Open Government Partnership), unaanza kutekelezwa mwaka huu hadi mwakani, ukifanana na uamuzi uliokwishafanywa na Rais wa Marekani, Barack Obama, pamoja na nchi ya Brazil.

Kwa upande wa Marekani, mpango huo unahusisha Ikulu ya Marekani (White House) kuweka wazi katika tovuti hadi mishahara ya watumishi wa Ikulu hiyo na taarifa nyingine za mali za watumishi wake, taarifa zao za maadili na hata rekodi za wageni wanaoitembelea Ikulu hiyo.


Lakini kwa upande wa mpango wa Tanzania ambao unatokana na mpango huo wa Marekani, ambayo itasaidia katika maandalizi ya mpango wa hapa nchini katika eneo la uwajibikaji na uadilifu (accountability and integrity) , Tanzania itazingatia maeneo sita.


Suala mojawapo linahusu kufanya mabadiliko ya sheria inayohusu utangazaji wa mali za viongozi wa umma, ili taarifa husika ziwe wazi hata kwenye tovuti ambako mtu yeyote anaweza kuzisoma.


Kipengele hicho kinaeleza: "Kuandaa marekebisho ya sheria na kanuni ili kuimarisha mchakato wa kutangaza mali za viongozi wa umma, ziweze kufikiwa na wananchi wengi kupitia mtandao hadi itakapofika Desemba mwaka huu."


Hata hivyo, taarifa zaidi zinaeleza kuwa mapendekezo hayo hususan kipengele hicho cha kuweka hadharani taarifa za umiliki wa mali za viongozi, kimeanza kupata upinzani ndani ya serikali.


Vyanzo vyetu vya habari serikalini vinaeleza kuwa wapo baadhi ya viongozi wanaopinga mpango huo kwa maelezo kuwa utaweza kuibua mtafaruku kati ya viongozi wa umma na wananchi, lakini wale wanaouunga mkono wanasisitiza kuwa hakuna sababu ya hofu kwa mtu mwenye mali alizopata kihalali.


Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais-Utawala Bora, Mathias Chikawe, amekaririwa akishangazwa na wenye kuhofia hatua hiyo.


Mbali na eneo hilo, katika suala hilo la uwajibikaji na uadilifu, eneo jingine litakaloboreshwa katika mpango huo wenye ubia wa kimaitaifa unaohusisha Marekani na nchi ya Brazili ni kuboresha tovuti ya Ofisi ya Taifa ya Mkaguzi na Mdhibiti Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), ili iweze kufikiwa na kila mwananchi anayetaka kusoma taarifa mbalimbali za ukaguzi wa hesabu. Kipengele hicho pia kimepangwa kutekelezwa ndani ya mwaka huu, kama ilivyo kwa kipengele cha kuweka hadharani mali za viongozi.


Eneo jingine maalumu la mpango huo linahusu uwazi (transparency) ambamo sasa hadi kufikia Julai mwaka huu, katika bajeti ijayo, taarifa zote za misamaha ya kodi zitakuwa zikiwekwa hadharani kwenye tovuti ya Wizara ya Fedha na taarifa hizo kuongezewa upya (update) angalau kila baada ya miezi mitatu.


Faida za mpango huo

Kwa mujibu wa taarifa zilizopo, kati ya athari za mpango huo hasa wa kufichua mali za viongozi wa umma kwa wananchi ni pamoja na wananchi kuweza kufuatilia ukweli wa taarifa za mali za viongozi hao.

Hali hiyo inatajwa kuweza kuondoa udanganyifu unaoaminika umekuwa ukifanyika kwa muda mrefu sasa na baadhi ya viongozi wa umma. Imeelezwa kuwa baadhi yao wamekuwa hawatangazi mali zao zote, na kwamba udhaifu huo umekuwa ukiwawezesha kuendelea kujilimbikizia mali kwa kutumia ofisi za umma bila hofu.


Wapo ambao wanaotumia mfano wa Rais wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa, ambaye wakati anaingia madarakani, alikuwa na ujasiri wa kutaja mali anazomiliki ikitarajiwa kuwa angefanya hivyo pia wakati anang'atuka.


Hata hivyo, kinyume cha matarajio ya wengi, Mkapa aliamua kufanya taarifa zake za mali siri alipong'atuka, hatua ambayo kama Sheria ya sasa ya Maadili ya Viongozi wa Umma itafanyiwa marekebisho na taarifa za mali za viongozi kuwekwa kwenye tovuti kila mwaka, fursa ya namna hiyo aliyoitumia Mkapa haitakuwapo tena.


Hali ya utawala bora nchini

Taarifa mbalimbali, yakiwamo maoni ya wananchi wengi, zinabainisha kuwapo kwa hali ya mwenendo usioridhisha katika eneo la uwajibikaji, utawala bora na uwazi.

Wakati hali hiyo ya kutoridhishwa ikiwa bayana miongoni mwa wananchi, zipo hatua ambazo zimekwisha kuchuliwa na serikali, ingawa matokeo ya hatua hizo hayajawa na ufanisi wa kujivunia.


Hatua hizo pia zinahusisha uamuzi wa Bunge la tisa, chini ya Spika Samuel Sitta, kufikia uamuzi wa kuanzisha Kamati za Kudumu za Bunge, kamati maalumu zinazoongozwa na wabunge wa Kambi ya Upinzani, zikitajwa kuwa ni kamati za uangalizi (watchdog committees).


Kamati hizo ambazo zinatajwa katika mpango-mkakati huo kama hatua za awali zilizopata kutekelezwa na nchi ni pamoja na Kamati ya Hesabu za Serikali Kuu, ambayo kwa sasa inaongozwa na Mbunge wa Bariadi Mashariki, John cheyo (kutoka UDP), Kamati ya Hesabu za Mashirika ya Umma, inayoongozwa na Kabwe Zitto, Mbunge wa Kigoma Kaskazini (CHADEMA) na Kamati ya Hesabu za Serikali za Mitaa inayoongozwa na Mbunge wa Vunjo, Augustine Mrema.


Ingawa kwa sasa uamuzi huo wa kuanzisha kamati hizo maalumu za Bunge umewekwa kama masuala ya msingi yaliyokwisha kufanyika, lakini itakumbukwa kuwa Spika wa Bunge la tisa, Samuel Sitta, alipata upinzani mkali kutoka kwa baadhi ya viongozi wa Chama cha Mapinduzi, akitajwa kuongoza Bunge katika mtindo wa kuhujumu Serikali.


Sitta kwa wakati huo alikuwa akiweka bayana kwamba anataka Bunge liwe na meno katika kutekeleza wajibu wake kwa mujibu wa Katiba, wa kuisimamia na kuishauri Serikali, lakini alipingwa na baadhi ya wabunge wenzake, hadharani na katika vikao vya faradha, kwamba "meno" aliyokuwa akiyatengeneza katika Bunge yalikuwa yanaitafuna Serikali. Ni Sitta huyo huyo aliyetishiwa kuvuliwa uanachama wake ili hatimaye apoteze uspika, lakini zikatumika mbinu nyingine za kumng'oa kutoka kiti hicho.


Ushindi kwa wanaharakati

Iwapo mkakati huu utafanikiwa kwa kufanyiwa marekebisho kwa Sheria ya Maadili ya Viongozi wa Umma, namba 13, ya mwaka 1995, hatua hiyo inaweza kutafsiriwa kuwa ni ushindi kwa baadhi ya wanaharakati nchini, ambao wakati fulani walifungua kesi kupinga usiri uliomo ndani ya sheria hiyo.

Wanaharakati hao kutoka baadhi ya asasi za kiraia walifungua kesi, huku wakiwa na kumbukumbu za kuwahi kufutwa kwa sheria ya "takrima", iliyokuwa ikiruhusu wagombea wa nafasi za uongozi wa dola, nyakati za Uchaguzi Mkuu, hasa ubunge kutoa "takrima" ambayo kimsingi ni rushwa kwa baadhi ya wapiga kura.








 
Oh Wow hii kama itafanikiwa itakuwa Vizuri kweli, tutajua ni kinanani wanatufilisi nchi yetu, kina nani wameshiba na kina nani wameshashiba hawahitaji Ubunge... Kama Abdallah Kigoda sijua kwanini anakaa na Ubunge labda ni kwa sababu ya kujilinda maslahi yake; alikuwa ndiye mkuu wa Investment ndani ya serikali ya Mkapa.

Ndiye aliyempa Mkapa hayo Machimbo ya Makaa ya Mawe...
 
Aanza yeye kuweka hadharani mali zake. Tena afanye hivyo kabla hajazificha kwa majina ya ndugu zake na washikaji wake.

Tunataka kudanganyana sasa. Hamna uzalendo.
 
Aanza yeye kuweka hadharani mali zake. Tena afanye hivyo kabla hajazificha kwa majina ya ndugu zake na washikaji wake.

Tunataka kudanganyana sasa. Hamna uzalendo.
Kupotezana muda bure, wenyewe ndiyo wataorodhesha, wenyewe ndio watakaosema, yote yanafanywa na wao kwaajili yao. Hakuna lolote hapo.
 
Back
Top Bottom