vinasaba vitumike kutambua miil

ngoshwe

JF-Expert Member
Mar 31, 2009
4,131
931


Kwa wataalamu, hii kisayansi itafanyikaje na kuthibitishwa pasipo kuacha shaka?. kulinganisha nasaba za ndugu wanaoishi na zile za marehemu waliokwisha zikwa,!?..


--------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------------

Rais Kikwete aagiza vinasaba vitumike kutambua miili ya marehemu wa ajali ya MV Spice Islander
11/09/2011



Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Jakaya Mrisho Kikwete ameagiza sayansi ya vinasaba (DNA) itumike mara moja kusaidia zoezi la utambuzi wa miili ya watu waliopoteza maisha yao katika ajali ya kuzama kwa meli ya *Mv Spice Islander* katika Bahari ya Hindi kwenye pwani ya Kisiwa cha Zanzibar usiku wa kuamkia jana, Jumamosi, Septemba 10, 2011.

Aidha, Kamati ya Taifa ya Ulinzi na Usalama ilikuwa inakutana leo, Jumapili, Septemba 11, 2011, Ikulu, Zanzibar chini ya uenyekiti wa Rais Kikwete kutathmini hali ilivyo kufuatia ajali hiyo ambako watu wapatao 192 wamethibitishwa kuwa wamepoteza maisha hadi sasa.

Vile vile, Rais Kikwete ametoa shukurani kwa wanakijiji cha Nungwi, vyombo vya ulinzi na usalama nchini pamoja na taasisi nyingine nchini kwa jitihada zao katika kuokoa maisha ya watu waliokumbwa na ajali hiyo. Hadi usiku wa jana Jumamosi ilikuwa imethibitishwa watu 650 wameokolewa katika ajali ya meli hiyo iliyokuwa inasafiri kutoka Dar es Salaam kwenda Pemba kupitia Zanzibar.

Rais Kikwete ametoa agizo hilo la matumizi ya vinasaba leo, Jumapili, Septemba 11, 2011, wakati alipotembelea kituo na eneo la maafa la Nungwi kilichoko kwenye kijiji cha Nungwi ambako karibu watu wote waliokolewa katika ajali hiyo na miili ya wote waliopoteza maisha yao katika ajali hiyo ilifikia. *Mv Spice Islander* ilizama katika katika eneo hilo la Nungwi.

Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini, Unguja, Mheshimiwa Pembe Khamis amemweleza Mheshimiwa Rais Kikwete kuwa habari walizonazo ni kwamba meli hiyo ilianza kuzama kati ya saa sita na saa sita usiku wa Ijumaa na viongozi wa mkoa huo walipata habari kuhusu mkasa wa meli hiyo kiasi cha saa saba usiku na zoezi la uokoaji lilianza mara moja.

Mheshimiwa Pembe Khamis amesema kuwa kituo hicho cha maafa cha Nungwi kilipokea miili 134 na majeruhi kiasi cha 78 na kwamba zoezi la kutafuta waliookoka na waliopoteza maisha katika ajali hiyo lilikuwa linaendelea leo.

Akiwashukuru madaktari na wataalamu wengine wa afya na sekta nyingine ambazo wamekuwa wanashiriki katika zoezi la uokoaji, kuhudumia waliokolewa pamoja na kuziweka katika hali nzuri maiti za watu waliopoteza maisha yao, Rais Kikwete ambaye amekaa kwenye kituo hicho cha maafa kwa dakika karibu 40
amewaambia, "Nawashukuru sana kwa kazi kubwa mliyoifanya, kwa yote mliyoyafanya na kwa moyo nzuri mliouonyesha. Mimi nimekuja kuungana nanyi kuwashukuru kwa kazi hiyo."

Kuhusu kasi ndogo ya zoezi la utambuziwa maiti, Mheshimiwa Rais amesema kuwa kwa jinsi zoezi hilo linavyokwenda inawezekana kabisa kuwa siyo miili yote itatambuliwa na jamaa na ndugu zao kabla ya kulazimika kuizika na hivyo akaagiza itumike sayansi ya vinasaba kuweka kumbukumbu za waliopoteza
maisha yao, "Kila maiti ichukuliwe sampuli ya DNA (vinasaba) na ikitokea kuwa pengine ndugu zake wamechelewa kuja kuitambua basi akifika hata kama mwili tayari umezikwa aweze kutambua kuwa ndugu yake alipoteza maisha katika ajali ya meli hiyo."

Hata baada ya kuambiwa na mtaalam wa utambuzi wa magonjwa na uchunguzi wa magonjwa na vyanzo vya kifo, Dkt. Ahmad Makata kuwa walikuwa wanaipiga picha miili yote na kuhifadhi nguo za wote waliopoteza maisha kama namna ya kuweka kumbukumbu, Rais Kikwete bado ameelekeza, "Miili ya binadamu hubadilika na kuharibika haraka, kwa kasi kubwa na katika muda mfupi. Miili ile ya ajali ya MV Bukoba ilibadilika na kuwa myeupe katika kipindi kifupi sana. Hivyo, naagiza tutumie vinasaba katika kuweka kumbukumbu. Si mnao wataalam wa vinasaba katika timu yenu?" ameongeza Rais Kikwete: "Tufanya DNA profile ya miili yote ambayo haijatambuliwa. Huko mbele, hii itasaidia kuepukana na kuwa na makaburu ya watu wasiotambuliwa kabisa kwa sababu inawezekana kuwa baadhi ya ndugu ya wale waliopoteza maisha katika ajali hiyo wanaweza kuchelewa kufika kufanya utambuzi kabla ya miili kuzikwa."




source: http://www.wavuti.com/4/post/2011/0...ajali-ya-mv-spice-islander.html#ixzz1XlzJWtoL
 
Back
Top Bottom