Watawala wanajichimbia kaburi lao wenyewe kuhusu hili suala la Dowans. Ni dhahiri kuwa Rais Kikwete alitoa maagizo kwa Waziri Mkuu, Mwanasheria Mkuu wa Serikali na Waziri wa Nishati na Madini wawalipe Dowans. Ngeleja asingekuwa na ujasiri wa kufanya maamuzi makubwa ya kuwalipa Dowans $65 million za walipa kodi bila kupewa amri/ruhusa na Kikwete. Sasa ofisi ya Rais kupitia waziri wake wa utawala bora, Mathias Chikawe, imeibuka kuwakemea Sitta na Mwakyembe kwa kupinga malipo kwa Dowans. Haya yote ni maagizo kutoka kwa Rais. DK. WILLIBROD SLAA alikuwa sahihi kabisa kusema Kikwete anamiliki Dowans, ndiyo maana amekaa kimya wakati kuna national crisis juu ya Dowans.
SAKATA LA DOWANS
Mafaili ya serikali yachomwa moto
* Vigogo wizarani wateketeza nyaraka nyeti kwa siri usiku
* Serikali yaingia kiwewe kuhusu malipo kwa Dowans
* Baraza la Mawaziri kukutana Januari 18 hali ikiwa tete
MWANDISHI WETU
Dar es Salaam
SAKATA la malipo ya fidia kwa kampuni tata ya Dowans Holdings SA/Dowans Tanzania Limited limeingia katika hatua mpya baada ya kuibuka kwa taarifa kuwa maafisa waandamizi serikalini wamechoma moto nyaraka nyeti kuhusu suala hilo ili kuficha ushahidi.
Taarifa zilizoifikia KuliKoni zinasema kuwa baadhi ya maafisa wa Wizara ya Nishati na Madini waliteketeza mafaili kadhaa usiku wa tarehe 11 Januari (Jumanne wiki hii).
"Tukio hili limetokea Jumanne usiku saa 3.30 kwenye nyumba ya mmoja wa maafisa waandamizi wa Wizara ya Nishati na Madini eneo la Oysterbay jijini Dar es Salaam," mtu aliyeshuhudia jambo hilo ameiambia KuliKoni.
"Kuna vigogo wakubwa kutoka wizarani walikuja na magari yao binafsi madogo kwenye nyumba hiyo. Waliagiza mafuta ya taa na yakachomwa moto mafaili matatu ya serikali yanayohusika na Dowans."
Taarifa zinasema kuwa watumishi watano wa Wizara ya Nishati na Madini, wakiwemo vigogo watatu na maafisa wawili, walikuwepo nyumbani kwa afisa mmoja wa wizara hiyo ambaye anatunza nyaraka nyeti za serikali wakati mafaili hayo yakichomwa moto.
Wakati mafaili ya serikali yanachomwa moto, Baraza la Mawaziri linatarajia kufanya kikao chake jijini Dar es Salaam Januari 18 chini ya uenyekiti wa Rais Jakaya Kikwete.
"Haijulikani kama suala la Dowans litakuwepo kwenye agenda ya Cabinet (Kikao cha Baraza la Mawaziri). Lakini huenda mawaziri wakatangaziwa kuwa Dowans tayari wameshalipwa na serikali," alisema mwanasheria mmoja aliyekaribu na serikali.
Serikali imewekwa mahali pagumu na sakata hili kutokana na kuwa na mgawanyiko mkubwa kwenye Baraza la Mawaziri juu ya uhalali wa malipo kwa Dowans na wananchi walio wengi kupingana na uamuzi wa serikali.
Wananchi wa kila kada hawakubaliani na malipo kwa Dowans na kumekuwa na tishio la kufanyika kwa maandamano makubwa ya kitaifa ambayo yanaweza kuisambaratisha serikali, kwa mujibu wa wadadisi wa masuala ya kijamii na kisisasa nchini.
"Nchi nzima sasa hivi imetikiswa na hili suala la Dowans. Serikali isipokuwa makini inaweza kupoteza imani ya wananchi juu ya dhamira yake ya kupambana na ufisadi na kuhakikisha kuwa kunakuwa na utawala wa sheria," alisema afisa mmoja wa serikalini.
Mahakama ya ICC ilitoa hukumu Novemba kuitaka Tanesco iilipe Dowans takriban shilingi 97 bilioni, lakini jitihada zikafanywa ili kuzidisha shilingi bilioni 88 zaidi kwenye kiasi kilichoamuliwa na majaji.
Mbinu hizo za kifisadi kutaka kuongeza malipo kwa Dowans mpaka ziliichanganya Ikulu ya Rais Jakaya Kikwete ambayo ilitoa taarifa kimakosa kuwa Dowans wanatakiwa kulipwa 185 bilioni/- badala ya 97 bilioni/-.
Wanasheria wa kujitegemea kutoka kwenye mashirika kadhaa makubwa yasiyo ya kiserikali wametangaza kusudio la kufungua kesi kwenye Mahakama Kuu jijini Dar es Salaam kupinga uamuzi wa baadhi ya watu serikalini kukubali kuilipa Dowans.
Wanaharakati hao wameikosoa serikali kwa kukubali haraka haraka tuzo iliyotolewa na mahakama ya usuluhishi wa magomvi ya kibiashara (ICC) iliyopo jijini Paris, Ufaransa, ambayo imeitaka TANESCO iwalipe Dowans kutokana na kuvunjwa kwa mkataba baina ya pande hizo mbili.
Wataalamu wa masuala ya kisheria kutoka Kituo cha Sheria na Haki za Binadamu (LHCR), Chama cha Waandishi wa Habari Wanawake Tanzania (TAMWA), Mtandao wa Jinsia Tanzania (TGNP) na mashirika mengine wanapinga kusajiliwa kwa tuzo hiyo Mahakama Kuu kwa sababu mikataba ya awali ilipatikana kwa rushwa na kukiuka maslahi ya umma.
"Kwa taifa maskini kama letu lenye matatizo mengi kama ukosefu wa umeme, mfumko wa bei na mengineyo, kutumia hela nyingi hivyo kulipa kampuni ambayo iligundulika kwa uchunguzi sahihi kuwa ni hewa, inatia shaka kwenye umakini wa serikali," alisema Mkurugenzi wa LHRC, Francis Kiwanga, mapema wiki hii.
Wanasheria hao wa kujitegemea wameitaka Tanesco, ambalo lina matatizo makubwa ya kifedha, kutokubali kuilipa Dowans kwa kuwa shirika hilo la umma lililazimishwa kuingia mkataba na Richmond/Dowans kinyume na sheria ya nchi.
Walisisitiza kuwa kwa kuwa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilithibitisha kuwa Richmond ni kampuni hewa, mkataba uliorithishwa kwa Dowans nao pia ni batili.
Wanaharakati hao walionesha wasiwasi wao kwa Waziri Mkuu Mizengo Pinda, Mwanasheria Mkuu wa serikali Frederick Werema na Waziri wa Nishati na Madini William Ngeleja kudai kuwa serikali lazima iwalipe Dowans kwa vyovyote vile, wakati malipo hayo yanakinzana na sheria za nchi.
Ili hukumu ya mahakama ya ICC iwe na nguvu ya kisheria hapa nchini, ni lazima Mahakama Kuu ya Tanzania itoe amri ya kukazia utekelezaji wake.
Sheria ya Tanzania ya mapatano, The Arbitration Act, inatamka wazi kuwa Mahaka Kuu ya Tanzania lazima iridhie hukumu ya ICC kabla haijaweza kutekelezwa.
Hata hivyo, wanasheria wa kujitegemea wanasema kuwa Mahakama Kuu ya Tanzania haiwezi kuridhia hukumu ya ICC kwa kuwa inakinzana na sheria ya Tanzania ya Manunuzi ya Umma (Public Procurement Act of 2004).
Kifungu cha 15 cha sheria ya "The Arbitration Act" kinaipa Mahakama Kuu ya Tanzania mamlaka ya kutupilia mbali hukumu ya ICC.
"TANESCO ilivunja mkataba na Dowans kwa kuwa mkataba huu ni kinyume na sheria ya Manunuzi ya Umma, ICC ilifanya makosa ya kisheria kwenye hukumu yake ilipoutambua mkataba wa Richmond/Dowans na TANESCO," alisema mwanasheria mmoja wa serikali.
"Mahakama Kuu ya Tanzania kamwe haiwezi kubariki hukumu ya ICC kwa vile hukumu hiyo inapingana moja kwa moja na tafsiri ya sheria ya Manunuzi ya Umma ya Tanzania."
Kwa mujibu wa sheria hiyo ya Manunuzi ya Umma, mkataba kati ya Richmond/Dowans na Tanesco ni batili kisheria kwa vile mkataba huo haukutokana na bodi ya tenda ya Tanesco.
Wakati huo huo, kuna utata wa kisheria juu ya umiliki wa mitambo ya Dowans huku kukiwa na shinikizo kwa serikali kufanya malipo hayo makubwa kwa haraka.
Hivi sasa huko Texas, Marekani, kuna kesi kati ya kampuni ya Richmond na Dowans kuhusu umiliki wa mitambo hiyo.
Richmond inadai kuwa mtambo mmoja wa kuzalisha umeme aina ya TM2500 ni mali yake na iliinunua Marekani kwa gharama ya dola za Marekani milioni 7.5.
Kwa upande mwingine, Dowans inadai kuwa ilipokabidhiwa mkataba na Richmond, mtambo huo ulikuwa bado haujanunuliwa na ilitumia pesa yake yenyewe kuununua.
"Hii ina maana kuwa serikali kwa sasa haitakiwi kufanya malipo yoyote kwa Dowans kufuatia hukumu ya ICC kwa kuwa kuna utata juu ya umiliki wa mitambo yenyewe," alisema mwanasheria mmoja wa serikali.
"Itakuwa ni jambo ya hatari kama serikali itakimbilia kuwalipa Dowans wakati haijulikani kama mmiliki halali wa mitambo yenyewe ni kampuni ya Richmond ya Marekani au kampuni ya Dowans ya Costa Rica."
<Source: Gazeti la kila wiki, Kulikoni, toleo la Ijumaa, Januari 14, 2011>