nngu007
JF-Expert Member
- Aug 2, 2010
- 15,862
- 5,797
BARAZA Baraza la Umoja wa Vijana wa Chama Cha Mapinduzi (UVCCM) Mkoa wa Arusha limemfukuza Mjumbe wa Baraza la Vijana Taifa anayewakilisha mkoa huo, Mrisho Gambo, kwa madai ya kukihujumu chama hicho.
Mrisho anatuhumiwa kuunga mkono vyama vya upinzani na kusababisha Jimbo la Arusha lichukuliwe na mbunge kutoka Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA).
Hatua hiyo ilitangazwa na Mwenyekiti wa Vijana Mkoa wa Arusha, James Millya, juzi usiku. Tangazo hilo lilipokewa kwa shangwe na wajumbe wenzake.
James alisema kuwa uamuzi wa kumfukuza Gambo umetokana na tuhuma na taarifa zenye ushahidi kuwa Gambo amekuwa ni kiini cha kukivuruga chama na kushawishi vijana wa CCM kuchagua upinzani.
Sisi wajumbe wa Baraza tumechoka na Mrisho Gambo, tunasema basi, inatosha, kama anataka kwenda upinzani aende moja kwa moja, hatutaki kuendelea kumuona anaendelea kutuvuruga, tunamwangalia, na hapa tunaandika barua rasmi kwa Baraza la Vijana Taifa kuwa hatumtaki na sisi ndiyo tuliomchagua na sasa hatumtaki, ushahidi tunao wa kutosha wa jinsi anavyohujumu chama, alisema Millya.
Kwa upande wake, Gambo alipoulizwa na MTANZANIA juu ya uamuzi wa kufukuzwa, alisema, Bado sijapata barua rasmi kuhusu suala hilo, lakini mimi ni mjumbe wa Halmashauri Kuu ya CCM Mkoa na mjumbe wa Baraza kuu la UVCCM Taifa, kwa mantiki hiyo uteuzi wangu wa mwisho unafanywa na Halmashauri Kuu ya CCM Taifa chini ya uenyekiti wa Mheshimiwa Jakaya Kikwete, na ambayo kwa mujibu wa Katiba ya CCM ndiyo yenye mamlaka ya kunivua uongozi.
Lakini lazima ujue kuwa nitaendelea kusimamia itikadi ya chama changu ya kusema ukweli daima na fitna kwangu mwiko.
Baraza hilo limesema linamtambua na kumjali Mwenyekiti wa CCM, Rais Jakaya Kikwete na kumtaka afanye kazi zake kwa biidi na asikubali kutishwa.
Rais Kikwete ni Rais imara, sisi tuko naye na tunamwambia asitishiwe nyau na mtu yeyote, alisema Millya
Vijana hao pia wametaka makundi ya kisiasa ndani ya CCM yafe na viongozi wasiendeleze malumbano ya nani atakayekuwa rais wa kipindi kijacho.
Millya alisema kuwa ni jukumu la wananchi kujadili na kuona ni nani anayefaa kuwa kiongozi wao.
Alisema ni wajibu wa wananchi kuamua ni nani awe rais wao ajaye hata kama atakuwa akitoka upande wa Kaskazini mwa nchi.
Katika hatua nyingine, vijana hao waliomba Serikali irejeshe huduma ya Kampuni ya Ndege Tanzania (ATCL), na kueleza kuwa ni aibu kwa nchi kukosa huduma hiyo.
Haiwezekani Rwanda na Burundi wakawa na huduma ya ndege zao wenyewe, sisi tukakosa huduma hiyo, tunamuomba Rais Jakaya Kikwete avalie njuga suala hili, alisema Millya.
Pia walipongeza huduma ya dawa inayotolewa na Mchungaji mstaafu Ambilikile Masapila, na kutaka Serikali isaidie kuboresha miuondombinu.
Wageni rasmi katika Baraza hilo walikuwa ni Mbunge wa Arumeru Magharibi Godluck ole Medeye, aliyefungua mkutano saa tano asubuhi; na Mkuu wa Wilaya ya Longido, James ole Milliya, aliyefunga mkutano huo saa tatu usiku.