UMUHIMU WA KITCHEN PARTIES NI KWA MABINTI TU?
Ndugu zangu kwa muda sasa nimekuwa ninajiuliza. Hivi hizi Kitchen parties wanazofanyiwa mabinti siku chache kabla ya kuolewa zinawasaidia kweli hao mabinti? Jibu ambalo nimelipata ni ndiyo na hapana. Ndiyo kwa sababu wananufaika na zawadi wanazopewa ambazo nyingi zinakuwa ni vifaa ambavyo vitatumika katika kuendesha jiko na nyumba atakayohamia baada ya kuolewa.
Hapana kwa sababu inapokuja kwenye kupewa mawaidha anayepewa ni yeye peke yake bila ya mume mtarajiwa. Mara nyingi binti hupewa mawaidha kama vile mume anayekwenda kuishi naye amekuwa nae kafuzu katika masuala ya kuendesha nyumba na kumwangalia na kumtunza mkewe. Kumbe sivyo. Matokeo yake baada ya muda kunatokea migongano kati yao wawili. Kwa sababu kile alichoambiwa yule binti kinahusu baadhi ya mambo ambayo mengi yanakuwa kwa upande wake kama mwanamke au mke. Walimu wake wanakuwa wamesahau ndoa japo ni ya mume na mke lakini pia yapaswa kuwa ni taasisi moja kwa maana ya umoja wa mume na mke. Na kama taasisi inakuwa na mfumo wake na mwenendo wake ambao hutokana na kuunganisha ujuzi wa mume na mke.
Nataka kusema nini. Ninachosema ni kuwa kwa kuwa mume mtarajiwa hakufanyiwa darasa wala maandalizi yoyote kwa maana ya jinsi ya kuishi na mkewe, anapoanza maisha ya ndoa kunakuwa na migongano iliyojaa mshangao kwa wao wote wawili. Kumbe mume nae angefanyiwa darasa kwa kweli ingelimsaidia kukabiliana na changamoto zinazojitokeza.
Pamoja na kwamba sijawahi kushiriki kwenye kitchen parties ila nimewahi kuona kanda za video kuhusiana na hilo. Ambalo nimeliona ni kuwa mawaidha anayopewa binti hayana maono. Yaani hayalengi kumsaidia kwa maana ya kuiona ndoa yake ni kitu ambacho kitadumu hadi kifo.
Mawaidha mengi yanagusa juu ya namna ya kumpikia mume na masuala ya tendo la ndoa. Yaani mambo ya sasa na yenye mahusiano ya kutuliza kiu ya mwili. Kama vile msosi na unyumba. Wanasahau kuwa kwamba ndoa kama taasisi hupitia hatua kadhaa kadiri miaka inavyoenda na wakati huo huo mwanaume na mwanamke pia hubadilika kutokana na umri unavyoongezeka. Kwa mfano wanaume wengi huwa hawaelewi kuwa mkewe akiwa mja mzito hubadilika kihaiba na hata kitabia. Wanawake wengine wanakuwa wakali hata kumuona mume hawataki na wengine kila wakati anataka awe na mumewe karibu na kadhalika.
Lingine ni kuwa mke akifikia miaka ya 50 na kuendelea huanza kubadilika kuelekea menopause. Hatua hii huwapumbaza na kuwashangaza wanaume wengi hadi wengine hufikia kuwatelekeza wake zao wakifikiri wamekuwa wakorofi au baridi au hawana mvuto, kumbe the woman is undergoing biological changes in her hormones. Sasa mume huyu angekuwa alifanyiwa darasa wakati wa ujana wake kabla ya kuoa na kuambiwa juu ya haya asingeshangaa. Kwani angeweza kujitayarisha hata kisaikolojia jinsi ya kukabiliana nalo. Hata katika nafasi za uongozi tabia ya mwanamke aliyemo kwenye menopause huwashangaza hata wanajamii. Sitaki kutaja majina ya watu. Unamkuta mwanamke ana madaraka ya juu sana katika Wizara au shirika kama kiongozi wa kufanya maamuzi. Kuna wakati unashangaa kauli au maamuzi anayoyatoa mnabaki hamuelewi au mnaamua na nyie kulumbana nae kwa kumshambulia. Kumbe masikini ya Mungu yule mama hajielewi na nyie mnaemsikiliza hamumwelewi.
Sasa ndugu zangu nini maoni yenu kuhusu suala hili. Hamuoni upo umuhimu wa wanaume nao kufanyiwa siyo kitchen party labda niite Managing the House Briefing au unyago na jando au??!!!!