Halisi
JF-Expert Member
- Jan 16, 2007
- 2,802
- 613
Mafisadi EPA waruka kiunzi
na godfrey dilunga
WIKI chache kabla ya Timu Maalumu iliyoundwa na Rais Jakaya Kikwete kuchunguza wizi wa mabilioni ya fedha kupitia Akaunti ya Madeni ya Nje (EPA) ya Benki Kuu ya Tanzania (BoT), imebainika kuwa baadhi ya watuhumiwa hawatafikishwa mahakamani.
Timu hiyo ilipewa muda wa miezi sita kukamilisha kazi ya kuifanyia uchunguzi ripoti ya EPA Januari 9, mwaka huu kwa nia ya kurejesha fedha zilizoibwa pamoja na kuwafikisha mahakamani watu wote waliohusika katika ufisadi huo.
Ripoti ya kampuni ya ukaguzi ya kimataifa ya Ernst and Young, iliorodhesha majina ya makampuni 22 ambayo yalihusika kwa namna moja au nyingine katika wizi wa fedha hizo mali ya walipakodi wa Tanzania. Vyanzo vya habari kutoka ndani ya Timu hiyo, vinaeleza kuwa baadhi ya watu waliohusika katika ufisadi huo mkubwa kuwahi kutokea Tanzania, hawatafikishwa mahakamani kutokana na kulindwa na sheria zilizopo.
Sheria zinazotajwa kuwalinda mafisadi hao ni pamoja na ile ya Udhibiti wa Biashara ya Fedha Haramu ya Mwaka 2006 na ile ya Udhibiti wa Mali zilizopatikana kwa Njia ya Uhalifu ya mwaka 1991.
Kwa nafasi kubwa, sheria hizo zinasisitiza urejeshaji wa fedha na mali ambazo ndio msingi wa uhalifu.
Kwa sasa upelelezi kuhusu ufisadi huo wa Sh bilioni 133, unafanywa na timu maalumu ya Rais Jakaya Kikwete. Timu hiyo inaongozwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali (AG) Johnson Mwanyika, Mkuu wa Jeshi la Polisi (IGP) Saidi Mwema, Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali (CAG), Ludovick Utouh na Mkurugenzi wa Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU), Edward Hosea.
Kwa mujibu wa vyanzo hivyo vya habari, ikiwa ni pamoja na Kitengo kipya cha Udhibiti wa Fedha Haramu (FIU), katika Wizara ya Fedha na Uchumi, msisitizo wa Sheria ya Udhibiti wa Fedha Haramu ni urejeshaji wa fedha na mali.
Mojawapo ya misingi muhimu ya sheria hii mpya (ya Udhibiti wa Fedha Haramu) ni msisitizo wa kurejesha fedha na mali ambazo ni msingi wa uhalifu. Msingi huu unapunguza hasara ambayo Serikali inapata kutokana na uhalifu, inasema sehemu ya taarifa kwa umma iliyotolewa na FIU katika gazeti moja la kila siku, wiki hii.
Pamoja na mambo mengine, taarifa hiyo inaeleza kuwa ukiukwaji wa taratibu mbalimbali za kifedha, sio lazima uwe kosa la jinai, ambalo ndilo pekee linaloweza kuwafikisha mahakamani watu waliohusika na ufisadi huo.
Mteja wa benki ambaye amepata mkopo kwa kushirikiana na mtumishi wa benki bila kuweka dhamana, yeye na mtumishi huyo watakuwa wamevunja utaratibu wa kutoa na kupata mkopo lakini hawatakuwa wametenda kosa la jinai, inaongeza sehemu ya taarifa hiyo kwa umma na kuongeza;
Benki husika ikiamua kumkamata aliyepata mkopo na ofisa wake aliyehusika na kuwapeleka mahakamani, itabidi ithibitishe madai yake.
Hata hivyo, taarifa hiyo inasema endapo benki husika itapata fursa ya kurejeshewa fedha zake, itapata ahueni katika mtaji wake na hivyo kuendelea na shughuli zake kama kawaida wakati huo huo wahusika wakiwa hawana tena mamuzi juu ya fedha hizo.
Hata hivyo, si wahusika wote wa EPA watakaonusurika. Watakaobainika kuhusika katika kughushi watafikishwa mahakamani kwa sababu ni dhahiri kuwa kughushi ni kosa la jinai.
Hata hivyo, pale ambapo hati ya kughushi imetumika katika kutoa mkopo, suala hili linaweza kuwa kosa la jinai, inasema taarifa hiyo.
Vyanzo vyetu vinazidi kudokeza kwamba huenda maelezo yaliyomo katika taarifa hiyo ya FIU kwa umma, ndiyo yatakayojitokeza katika taarifa ya mwisho ya Timu ya Rais Kikwete, kuhusu uchunguzi wa ufasadi BoT.
MTANZANIA ilipomtafuta jana Msemaji wa Ofisi ya Mwanasheria Mkuu wa Serikali, Omega Ngole, ambaye amekuwa akiwasiliana na wanahabari kuhusu kazi za timu hiyo, alisema anachofahamu ni kwamba timu inaendelea na kazi vizuri.
Alisisitiza kuwa, timu hiyo kwa sasa haina taarifa yoyote inayoweza kutolewa kwa umma.
Kwa sasa Timu inaendelea na kazi yake na naomba tuipe nafasi ifanye kazi yake vizuri na ikimaliza naamini mtapata taarifa, alisema Ngole alipoulizwa kuhusu habari hizo mpya jana asubuhi.
Tangu Mwanyika alipotangaza kuwa timu yake imefanikiwa kukusanya Sh. bilioni 60 kutoka kwa baadhi ya watu na makampuni yaliyotajwa kuhusika katika kashfa hiyo miezi miwili iliyopita, timu hiyo haijawahi kutangaza tena hadharani maendeleo ya upelelezi wao unaohusisha mtandao wa fedha hizo duniani kote.
SOURCE: Mtanzania 14.05.2008
http://www.newhabari.com/mtanzania/habari.php?id=4929§ion=kitaifa
http://www.newhabari.com/mtanzania/habari.php?id=4929§ion=kitaifa