Tuchambue Kitita Madai cha Huduma ya Afya cha NHIF 2023.

Kurunzi

JF-Expert Member
Jul 31, 2009
9,285
9,922
By Godlisten Malisa

Kuanzia tar.1 March 2024, vituo binafsi vya huduma za afya nchini vimekubaliana kutokupokea wateja wa NHIF. Maana yake ni kwamba wagonjwa wanaotibiwa kwa NHIF wako hatarini kukosa huduma. Kumbuka, takwimu zinaonesha zaidi ya 80% ya wagonjwa mahospitalini ni wanachama wa NHIF. Ni chini ya 20% tu ndio wanaotumia bima za makampuni binafsi au kujilipia cash. Kwahiyo 80% ya wagonjwa wote nchini hawajui hatma zao.

KIINI CHA MGOGORO
Kiini cha mgogoro ni vifurushi vipya vilivyopendekezwa na NHIF kwenye utoaji huduma. Vifurushi hivyo vimepunguza bei kwenye huduma nyingi na za msingi na vimeongeza bei kwenye huduma chache na zisizotumika mara kwa mara.

Kwa mfano, huduma ya kujifungua kwa upasuaji (C-section) kwenye hospitali za wilaya imepunguzwa kutoka 300,000/= hadi 130,000/=. Hospitali za mikoa 180,000/= na za Kanda 220,000/=. Maana yake ukipata changamoto za kujifungua na ukatakiwa kufanyiwa upasuaji kwenye hospitali binafsi yenye hadhi ya wilaya, NHIF itakulipia 130,000/= tu. Vituo binafsi vimesema haviwezi kutoa huduma kwa bei hii.

Procedure kama hii inahitaji timu ya watu angalau 6 au zaidi. OBGY, Assistant Surgeon, Anesthetist, Surgical Technologist, Delivery Nurse, Supporying staff. Hapo bado vifaa tiba kama mitungi ya Oxygen, sindano, madawa, nyuzi, gauze etc. Sasa kwa 130K utafanyia nini? Utanunua gauze? utamlipa daktari? utalipia umeme? utanunua vifaa tiba? Utalipia Oxygen?

Ikumbukwe hata 300,000/= iliyokuwa inatolewa awali bado ilikua haitoshi. Maana yake ni kwamba vituo binafsi vilikua vinatumia rasilimali zake za ndani kuongezea kwenye kiasi kinachotolewa na NHIF ili mama mjamzito asikose huduma. Hii inaitwa Corporate Social Responsibility. Yani unachukua faida kidogo unayopata kwenye huduma zingine, una-topup kwenye huduma ambazo hazina fungu la kutosha. Hospitali nyingi binafsi zinafanya hivyo. Sasa unapokuja kushusha tena kutika 300K hadi 130K unataka hospitali zijiendesheje?

Hakuna hospitali itakubali kufanya hii procedure. Unless otherwise wacompromise quality na kufanya procedure ambayo ni substandard. Yani badala ya chumba cha upasuaji kuwa na wataalamu 6 wawe watatu. Badala ya kumtumia Anasthesiologist atumike Nurse. Badala ya kutumia mashine ya Oxygen, wafungue madirisha 😀. Inachekesha lakini huku ndipo serikali dhaifu ya CCM inapotaka kutupekeka. Na mwisho wa siku muathirika ni mwananchi maskini. Hawa ndio watafia kwenye vitanda vya upasuaji. Hao viongozi walioshusha bei wao hata wakiugua malaria, wanaenda India.

MAPITIO YA VIFURUSHI YALIFANYIKA LINI MARA YA MWISHO?
Mara ya mwisho bei za vifurushi vya NHIF zilipitiwa mwaka 2016. Kwahiyo hadi leo ni miaka 8 imepita. Sasa jiulize miaka 8 gharama za maisha zinapanda au zinashuka? Kama mwaka 2016 NHIF ilikua inalipa 300K kujifungua kwa upasuaji, kwanini leo wanataka kulipa 130K? Yani kila kitu kimepanda, halafu wewe unashusha bei?. Oxygen imepanda, bei ya gauze imepanda, madawa yamepanda, umeme umepanda, vifaa tiba vimepanda. Hata gharama za kuwalipa watoa huduma zimepanda. Msingi wa kushusha bei unatoka wapi? Nilitegemea baada ya miaka 8 NHIF iongeze fungu kwenye huduma, na sio kushusha.

Nimetolea mfano mmoja wa C-section, lakini huduma nyingi zimeshushwa bei. Kwa mfano ukivunjika mguu NHIF watakulipia 12,000/= tu kuwekewa POP. Maana yake ni kwamba ukikuta gharama za POP ni 50,000/= utalazimika kuongezea 38,000/= kutoka mfukoni kwako. Sasa hapa mwananchi ataonaje faida ya bima?

Zipo huduma chache zimepandishwa (eg Consultation kwa Specialist) lakini nyingi zimeshushwa bei. Na hiki ndio kiini cha mgogoro wa serikali na hospitali binafsi. Ikumbukwe kwamba hospitali za serikali zinapewa ruzuku, kwahiyo haziwezi kulalamika hata kama zinaumia. Lakini hospitali binafsi zina haki ya kulalamika maana hazipewi ruzuku.

Na hizi binafsii zimegawanyika makundi mawili. Zile za mashirika ya dini na zile binafsi kabisa. Zile za mashirika ya dini angalau zinasamehewa kodi. Lakini hizi binafsi kabisa zinatozwa kodi maana zinaambiwa zinafanya biashara. Na ukihesabu wanalipa jumla ya kodi 32 kuanzia kodi za TRA, Halmashauri, mabaraza mbalimbali, TBS, NEMC, OSHA, TMDA etc.

Sasa jiulize mtu analipa kodi 32 kwenye serikali yako, halafu unataka afanye C-section kwa 130K kweli? Hiyohiyo alipe mishahara, ununue umeme, maji, vifaa tiba na bado alipe kodi zote 32 kwenye hela hiyohiyo? Mna wazimu?

Ikumbukwe NHIF ilileta mapendekezo ya vifurushi hivi December mwaka jana, wadau wakavikataa. Kamati ya bunge ya afya na masuala ya UKIMWI ikaingilia kati, ikasema vifurushi vya zamani viendelee kutumika wakati hivi vipya vikifanyiwa marekebisho. Bunge likaagiza iundwe kamati ya kupitia upya vifurushi hivyo itakayoshirikisha wizara, NHIF na watoa huduma, kwa maana ya hospitali za umma na zile za binafsi.

Lakini hospitali binafsi hazikushirkishwa. Kamati iliyoundwa ilihusisha wataalamu wa wizara, TIRA na NHIF tu. Mbaya zaidi Sekretarieti yote ya Kamati iliundwa na wajumbe kutoka NHIF tu. Maana yake ni kwamba NHIF waligeuka mahakimu kwenye kesi yao wenyewe, contrary to cardinal principles of Law. Kwahiyo NHIF walizuga kufanya review na kurudi na bei zilezile za awali zilizokataliwa na wadau, japo walifanya marekebisho kidogo sana.

Lakini wadau wa sekta binafsi kwa maana ya APHTA, CSSC na BAKWATA hawakushirikishwa kuunda Kamati, badala yake waliitwa kwenye kikao cha wizara tar.19 February 2024 kwenda kuelezwa kile ambacho kamati imeamua. Hapa maamuzi ya bunge kwamba hospitali binafsi zishirikishwe yalipuuzwa.

Lakini pia bunge lilizuia bei mpya kuanza kutumika mpaka pale sheria iliyoanzisha NHIF itakapopitiwa upya na kufanyiwa marekebisho ili kuaccomodate watoa huduma binafsi. Lakini wakati sheria ikuwa bado haijapelekwa bungeni ili kufanyiwa marekebisho, tayari NHIF inalazimisha bei mpya zianze kutimika leo. Huku ni kulidharau bunge kwa viwango vya juu.

Kwanini NHIF wanashinikiza bei mpya zitumike haraka haraka? Ni kwa sababu mfuko upo hoi bin taabani na unakaribia kufilisika. Kwa akili zao "finyu" wanadhani bei za huduma ndio zinafanya mfuko ufilisike, ndio maana wanajarjbu kuzipunguza. Lakini si kweli. Hata wapunguze bei, kama hawatashughulikia chanzo cha tatizo bado mfuko utafilisika tu.

CHANZO CHA NHIF KUYUMBA KIFEDHA
1. Fedha za NHIF kutotumika sawa na makusudio. Ripoti ya CAG ya mwaka 2022 inaonesha kuwa wanafanyakazi wa NHIF wamekopeshana zaidi ya Bilioni 41 ambazo ni michango ya wanachama. Yani unakatwa pesa kwenye mshahara wako ili ukiugua utibiwe, kumbe mmewapa watu mtaji wa kukopesha bila riba. Yani wamegeuza mfuko kuwa KIKOBA, halafu haohao leo wanashanga kwanini mfuko unafilisika? 😀

2. Serikali kutoa huduma bure kwa wazee bila kufidia gaharama. Sera ya wazee kutibiwa bure ni nzuri sana. Lakini serikali inatakiwa kufidia gharama. Kwa mfano mzee akienda hospitali kutibiwa macho. Gharama zake zikawa 50,000/=. NHIF wanamlipia huyu mzee. Lakini serikali haitoi fedha kurudisha NHIF. Hii ni moja ya sababu ya huu mfuko kufilisika, hata ripoti ya CAG imeeleza kuwa seeikali inadaiwa na NHIF.

3. Centralization ya huduma za bima ya afya kwa watumishi wa umma. Zamani baadhi ya tasisi za serikali ziliruhusiwa kuwa na bima binafsi. Baadhi ya taasisi hizo kama BOT, NSSF, TRA, TANAPA, TANROADS, TANESCO etc zilikua zinatumia bima za makampuni binafsi kama AAR (currently Assemble), Jubilee, Strategies, etc. Lakini Magufuli akalazimisha watumishi wote wa umma kutumia NHIF. Na hapa ndipo mfuko ulipozidiwa., kwa sababu wengi walipohamia NHIF ilibidi watengenezewe vifurushi vyao vya VIP ili kuendana na huduma za kule walikotoka. Matokeo yake NHIF ikawa na mzigo mkubwa uliowashinda kubeba.

UJINGA WA SERIKALI
Jana baada ya hospitali binafsi zote kupitia umoja wao wa APHTA, kutangaza hazitapokea wagonjwa wa NHIF, tulitegemea serikali itakaa nao chini kutafuta suluhu kwa maslahi mapana ya afya za watanzania. Lakini mtu mmoja akaniambia ukitaka kujua serikali ina watu wajinga, wataanza kuzitisha hospitali binafsi na kuzifanyia surbotage ili kulazimisha zitoe huduma kwa bei zilizopendekezwa na NHIF.

Na hiki ndicho kilichotokea. Leo serikali imetoa onyo kwa hospitali za Agha Khan, Kairuki na Regency kwamba eti zinakiuka mkataba baina yao na NHIF. Kumbuka tamko la APHTA jana lilisema hospitali zote binafsi zitasitisha huduma leo. Sasa kwanini zitishwe hizo tatu tu? Hapa lengo ni devide and rule theory. Wakizitisha hizi hospitali kubwa wanajua nyingine zitafyata mkia. Yani ukiona Agha Khan ametishiwa akasurrender, wewe na hospitali yako huko Tandahimba utathubutu kukataa, hata kama unaumizwa?

Na hawataishia kuzitisha tu, wataenda mbali zaidi kufanya surbotage. Utaanza kusikia hospitali zinafanyiwa ukaguzi, mara zimekwepa kodi, mara zimeajiri watu bila mikataba, mara zimejenga majengo mapya bila kibali. Yani ili mradi kuzifrustrute ili tu zikubaliane na vifurushi vipya. Hii ndio mbinu pekee iliyobaki na inatumiwa sana na serikali za kiimla, zilizoshindwa kutatua changamoto kwa kutumia akili.

ATHARI ZAKE NI ZIPI?
1. Kwanza kuna watu watapoteza maisha kwa sababu ya huu mvutano wa NHIF na vituo binafsi vya kutolea huduma. Mtu amekosa huduma Peramiho, mpaka aende Songea mjini kama ni dharura anaweza kupoteza maisha.

2. Mgogoro huu utasababisha usumbufu usio wa lazima kwa wagonjwa. Umetoka huko Mpiji Magohe, unaenda Kairuki unaambiwa hamna huduma, unalazimika kukanyaga hadi Mwananyamala. Ukifika unakuta muda wa huduma umeisha, hadi kesho tena.

3. Vituo vya umma vitaelemewa sana na kushindwa kutoa huduma. Takwimu zinaonesha kuwa hapa Dar peke yake vituo binafsi ni 79% na vya serikali ni 21%. Na kwa nchi nzima vituo binafsi ni 42% na vya umma ni 58%. Hivi unawezaje kuhudumia watu wote kwenye vituo vya umma kama si kujimwambafai kwa ujinga?

4. Maelfu ya watu watapoteza ajira. Ili vituo viweze kujiendesha kwa hizi bei mpya, itabidi vipunguze idadi ya wafanyakazi na matikeo yake wengi watapoteza ajira. Serikali itakosa kodi (PAYE) na mzigo wa watu tegemezi utaongezeka.

5. Huduma nyingi zitatolewa chini ya kiwango ili kupunguza gharama za uendeshaji.

6. Vituo vingi vya kutolea huduma vitafungwa. Wamiliki wataona bora wabadilishe biashara ili kuepusha mgogoro na serikali.

NINI KIFANYIKE?
1. Jambo la kwanza kabisa, Serikali isitishe vifurushi vipya, na badala yake vile vya zamani viendelee kwanza wakati suluhu ikitafutwa.

2. Kamati ya kureview bei mpya ya vifurushi ihusishe wadau wote kwa usawa. Wawepo watu wa wizara, NHIF, hospitali za umma, hospitali binafsi (APHTA, CSSC, BAKWATA) na wananchi ambao ndio beneficieries.

3. Bunge liharakishe mapitio upya ya sheria iliyoanzisha NHIF ili hospitali binafsi na vituo binafsi vya kutolea huduma viweze kutambulika kisheria kama wadau wa NHIF.

4. Serikali ihakikishe fedha zote zilizokopwa NHIF zinarudishwa kama ilivyoelezwa kwenye ripoti ya CAG. Haiwezekani watu wajikopeshe hela kwenda kununua magari, viwanja, nyumba halafu usumbufu waje kupata wagonjwa. Hatukatwi mishahara yetu ili watu wakanunue magari, tunakatwa ili tutibiwe.

5. Serikali ihakikishe inalipa madeni yote yaliyotokana na huduma bure kwa wazee. Na uwekwe utaratibu rasmi wa kuendelea kulipia wazee matibabu yao badala ya kuacha mzigo huo kwa NHIF pekee.

6. Baadhi ya taasisi za umma ziruhusiwe kutumia bima za makampuni binafsi ili kupunguza mzigo kwa NHIF. Taasisi kama BOT, TRA, TANAPA, TPA, TANESCO etc zinaweza kabisa kulipia watumishi wake bima kwenye makampuni binafsi na kupunguza mzigo NHIF.

7. Bodi ya Wakurugenzi na Menejimenti ya NHIF ifumuliwe na kusukwa upya kwa kugeuza pesa za wananchama kuwa KIKOBA cha kukopesha watumishi badala ya kulipia huduma za matibabu kwa walengwa.!

Kuhusu Kauli ya Waziri wa Afya Ummy Mwalimu

Mhe.Ummy punguza jazba tafadhali. Hii si kauli ya kutolewa na mtu mwenye dhamana ya Waziri. Unawezaje kubeza mchango wa vituo binafsi kwenye sekta ya afya? Si kweli kwamba vituo vya serikali vinajitosheleza. Huu ni uongo mtupu. Mwambie PS wako akupe takwimu za uwiano wa vituo vya serikali na binafsi halafu ujenge hoja kwa facts bila mihemko.

Hapa Dar peke yake, vituo binafsi ni 79% na vya serikali ni 21%. Kwa lugha rahisi vituo binafsi vikiacha kutoa huduma, sekta ya afya inacollapse Dar nzima. Dar ndio lango la nchi, lakini serikali haimiliki hata robo ya vituo vya afya. Halafu unajisifu mpo vizuri? Kivipi? Acha kujilisha upepo dada mkubwa.

Takwimu za kitaifa zinaonesha nchi nzima vituo binafsi ni 42%, ambayo ni karibia nusu ya vituo vyote. Sasa unawezaje kubeza mchango mkubwa hivi wa sekta binafsi kwenye afya? Bila sekta binafsi serikali pekee haiwezi kubeba mzigo wa kuhudumia afya za watanzania.

Hujui huko vijijini jinsi ambavyo sekta binafsi imechangia kuokoa maisha ya watu. Nenda Igunga waambie Nkinga Hospital haina mchango kwao, usipopigwa mawe. Nenda Peramiho ufunge hospitali ya misheni Peramiho uone Wangoni watakachokufanya. Nenda Moshi ongea "blahblah" kuhusu KCMC usiponywesha mbege kwa karai.

Na hapo nimetaja facility chache tu zenye hadhi ya hospitali za kanda. Lakini huko vijijini zahanati zinazookoa watu ni za binafsi, na nyingi ni za mission. Usfikiri wananchi ni wajinga kiasi cha kuacha huduma vituo vya umma na kwenda private? Wewe mwenyewe huwezi kutibiwa Mwananyamala, wala mtoto wako hawezi kutibiwa Temeke, pamoja na kutuambia kwamba mpo vizuri. Sasa mko vizuri how?

Ukweli ni kwamba NHIF ipo hoi. Na sababu mojawapo ni kwamba Michango ya wanachama imetumika vibaya. Wewe kama kiongozi tafuta suluhu kwa busara. Punguza kiburi cha madaraka. Ulijenga heshima kubwa kwenye hii Wizara lakini unataka kuipoteza unnecesarily. Nakushauri tulia kwanza. Usikimbilie kujibu kila kitu. Jipe muda, na usikilize zaidi kuliko kuongea. Wanaoumia kwa kukosa huduma ni wananchi, sio nyie mnaolumbana. Tumia busara tafadhali.!

UHALISIA
Huduma ya kujifungua kwa upasuaji (C-section) NHIF watakulipia 130,000/= tu kama itafanyika kwenye hospitali yenye hadhi ya wilaya. Hebu jiulize is that realistic? 130K uwalipe hawa watoa huduma wote unaowaona hapa, ulipie vifaa tiba kama Oxygen, sindano, madawa, nyuzi, gauze etc. Ulipie umeme na maji. Pia uhakikishe una "standby" jenereta lenye mafuta ili umeme kikatika tu, liunge fasta bila kuathiri huduma. Yote hayo yafanywe kwa 130K? Huku ni kufanya mzaha na maisha ya watu. Halafu hao wanaotaka kukulipia 130K ufanyiwe upasuaji, wao wamejikopesha Bilioni 41 bila riba ambazo ni michango yako. Hii serikali ya CCM haina tofauti na jinamizi.!

Tuendelee kuchambua kitita kipya cha huduma cha NHIF. Ukivunjika mguu au mkono, gharama za kuwekewa POP kwenye hospitali yenye hadhi ya wilaya ni TZS 12,000/= kwa mtu mzima na 10,000/= kwa mtoto. Sasa jiulize POP gani la 12K? Wewe kama mtoa huduma hiyo 12K utafanyia nini? Yani ununue plain weave, gauze fabric, crepe bandage, calcium sulphate hemihydrate etc. Hapo bado hujamlipa daktari na nurse. NHIF hebu acheni futuhi kwenye maisha ya watu.

POP ya buku ten kweli? Halafu hawa "wanasiasa" wanaotaka watoto wetu wafungwe POP za buku ten, wao watoto wao wakivunjika wanawapeleka India au Nairobi. Si mnamkumbuka yule mtoto wa "mheshimiwa" aliyevunjika mguu akaenda kutibiwa Afrika kusini na akakaa huko karibu mwezi mzima? Kwanini hakupelekwa Mwananyamala akawekewe POP la buku 10?

Aisee CCM chezeni na mambo mengine lakini sio afya za watu. Afya ndio kila kitu kuhusu maisha ya mwanadamu. Maisha hayana maana yoyote bila afya njema. Mmevuruga kwenye mambo mengi wananchi wamewavumilia, lakini kwenye hili la afya mtatokea dirishani. Bata, Wahed.!
 

Attachments

  • VID_1709380782965.mp4
    25.9 MB
Hapo kwenye 'NINI KIFANYIKE' nakazia kwenye pointi namba 4 na nashauri wahusika wa ubadhirifu huo wakamatwe na kushtakiwa.
 
Hongera Kwa kuandika vizuri sana inaonekana una taarifa ya kutosha ( Insider).

Naishauri serikali ichukue ushauri wako..
 
Umeandika vizuri.
Nakukumbusha tu kuwa unaweza kushauri bila kutoa matusi.

Mgomo wa hospitali binafsi kutokupokea wagonjwa haukubaliki.
 
Umeandika vizuri.
Nakukumbusha tu kuwa unaweza kushauri bila kutoa matusi.

Mgomo wa hospitali binafsi kutokupokea wagonjwa haukubaliki.
Anzisha ya kwako ndo ujui ugomu wa kuendesha huopsitali acha na huyo chiriko mwenye mdomo kama ... badala ya kuwa waziri wa afya amekuwa msemaji wa wizara
 
CCM ni zaidi ya Shetani.
Wanaiba huku wanawatesa Raia bila huruma.
 
Back
Top Bottom