Toa maoni yako juu ya wagombea hawa wa BAVICHA (Chadema) taifa

Ben Saanane

JF-Expert Member
Jan 18, 2007
14,581
18,124
TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Kuwania uenyekiti wa taifa wa Baraza la Vijana
CHADEMA (BAVICHA) APRILI 28, 2011

UTANGULIZI


Ndugu wanahabari
,


Awali ya yote, nawashukuru kwa dhati kwa kuitikia kwenu wito wangu wa kushiriki mkutano huu.Natambua kwamba vyombo vya habari ni Mhimili Muhimu na wa Kipekee katika kuburudisha, kuelimisha, kupokea na kutoa taarifa kwa wananchi.


Mimi ni mwanachama kijana wa Chama cha Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA). Kitaaluma, ni mwanauchumi na pamoja na masuala ya uhusiano wa kimataifa. Ni mwanaharakati na ni mwanasiasa.


Lengo la mkutano mkuu ni kutangaza nia yangu na kueleza sababu na malengo yaliyonisukuma kuwania uenyekiti wa Baraza la Vijana la Chadema (BAVICHA) ngazi ya Taifa. Uchaguzi wa BAVICHA utafanyika tarehe 28 Mei, 2011.


Ndugu wanahabari, nimeamua kugombea nafasi hii kwa kusukumwa na uzalendo wangu kwa taifa langu na chama changu; Na pia nimesukumwa na dhamira yangu ya kutaka kutumia ujuzi na uzoefu wangu wa kitaaluma, kisiasa na kiharakati kuhakikisha naliongoza BAVICHA katika kufanya mambo makuu mawili;


Kuishinikiza serikali, mamlaka husika na wadau wengine kupitisha na kutekeleza maamuzi ya kuboresha maisha ya vijana na mustakabali wa taifa.

Nitafafanua.


Kuwaandaa vijana wa Chadema kuwa tayari kukihakikishia chama ushindi katika uchaguzi wa serikali za mitaa wa mwaka 2014 na uchaguzi wa mwaka 2015.

Nisisitize, kwamba nimeamua kuwania wadhifa huu baada ya kujitathimini kwa kina sana, kuanzia kwenye dhamira iliyoko ndani ya nafsi yangu hadi kwenye ujuzi, uzoefu na utashi wangu wa nje.

Sijasukumwa na mtu yeyote wala kikundi chochote, nimesukumwa na nafsi na uwezo na utayari wangu wa kuwa mtumishi wa watu katika uongozi. Dhamira yangu kuu ni kuchangia harakati za Chadema kuchukua dola ifikapo mwaka 2015.


KWANINI NAGOMBEA?


1.
Jukumu la jumla la yeyote anayetaka kuwa kiongozi wa BAVICHA, ni kuhakikisha anatoa mchango wake wa kiuongozi kuliwezesha baraza letu kutekeleza malengo yaliyowekwa kama ifuatavyo.

·
Kutambua, kusimamia, kuendeleza na kuhamasisha ushiriki wa vijana katika masuala ya siasa
· Kubuni na kutekeleza mikakati ya kueneza sera za chama kupitia vijana ndani ya jamii.
· Kubuni na kupanga mafunzo ya vijana kuhusu masuala ya kiuchumi na kijamii.
· Kuhamasisha vijana kugombea uongozi ndani ya chama na katika chaguzi za serikali.
· Kuanzisha na kurutubisha ukuaji wa vikundi vya sanaa na michezo kwa vijana.
· Kubuni na kueneza mipango na mikakati ya kudhibiti uenezaji wa magonjwa mbalimbali yanayo athiri vijana matharan UKIMWI.
· Kuwa chemchem ya ushauri kwa chama kuhusu masuala yote yanayohusu vijana ndani ya chama.
· Kushiriki harakati mbalimbali za vijana ndani na nje ya nchi.
· Kushiriki kikamilifu katika timu za kampeni kwa kushirikiana na uongozi wa chama katika kila ngazi husika.

Nimejitathimini na kujiridhisha kwamba ninao uwezo, ujuzi na uzoefu wa kuniwezesha kuliongoza baraza kutekeleza na kuyafikia malengo yote hayo yaliyowekwa, ambayo kwa ujumla wake yatarahisisha harakati zetu za kuchukua dola mwaka 2015.


2. Kama mwanauchumi nitatumia ufahamu katika tafiti na takwimu kuliongoza baraza kisayansi katika kufikia malengo yake. Mathalan, vijana waliokuwa na umri wa kuanzia miaka 13 hadi 17 mwaka 2010 hawakuweza kupiga kura kwa sababu walikuwa chini ya umri wa miaka 18 ambao ndio umri wa kikatiba unaomruhusu kujiandikisha na kupiga kura. Vijana hao ndio watakaokuwa wapiga kura wapya mwaka 2015 kama wakijiandikisha. Kwa hiyo, kwa mahesabu yangu ifikapo mwaka 2015 inatarajiwa kuwa watu milioni 28 hadi milioni 32 ndio watakaokuwa na umri wa kupiga kura.


Kwa mantiki hiyo, ninaposema tutachukua dola, namaanisha kuwa tuna kazi ya kuvuna kura hizo, milioni 28 hadi milioni 32, ambazo nyingi zitakuwa ni kura za vijana. Nitahakikisha mikakati na mipango yote ya baraza la vijana inalenga katika kukiwezesha chama kuvuna na kulinda kura hizo.


Pia natambua idadi ya waliojitokeza kupiga kura mwaka 2010 ilikuwa takribani wapiga kura Milioni 8, yaani watu takribani milioni 12 hawakujitokeza kwa sababu mbalimbali, zikiwemo sababu haramu na sababu halali. Hivyo ni jukumu langu mimi pamoja na baraza la vijana kuhakikisha tunakisaidia chama kuifikia idadi hii na kuhakikisha wanajiandikisha na kupiga kura 2015


3. BAVICHA ni sehemu muhimu ya kukuza vipaji vya uongozi na kulea viongozi wa sasa na wa siku zote wa taifa hili. Nitahakikisha baraza linahamasisha vijana kushiriki siasa kwa kugombea nyadhifa mbalimbali za kiserikali.

Katika hili nitachangia pia ujuzi na uzoefu wangu wa kikazi na kitaaluma kuliwezesha baraza kubuni programu na miradi ya kuhamasisha na kuwajengea vijana uwezo na fursa zote zinazohitajika kwa wao kuwania uongozi kupitia Chadema. Huu ni mpango wa kati na wa muda mrefu kuhakikisha vijana wengi wanaingia kwenye uongozi kuanzia ngazi za chini (serikali za mitaa) hadi Bungeni mwaka 2015. Lengo letu ni kulidhibiti pia Bunge.


4. Nitaliongoza baraza kuwa chombo cha kukosoa, kupika na kushawishi sera na misimamo ya kitaifa na kidiplomasia ili kujenga na kuimarisha mahusiano yenye manufaa kati ya Tanzania na nchi za nje. Uzoefu na ujuzi wangu wa kitaaluma kama mwanazuoni wa siasa za kimataifa kulisaidia baraza katika hili.


5. Kuliongoza baraza kushinikiza uanzishwaji wa Baraza Huru la Vijana la Taifa. Baraza hilo halipo na uwepo wake ni muhimu sana kwani ndilo litakaloweza kuwaunganisha vijana wote wa kitanzania kuwa kitu kimoja bila kujali tofauti zao za kisiasa, kikabila, kiuchumi na nyinginezo.

Kama baraza hili lingekuwepo na lingekuwa na viongozi makini basi lingeweza kuchukua wajibu wa kuishauri na kuishinikiza serikali kupitisha na kutekeleza maamuzi ya kisera na hata kisheria yenye maslahi kwa vijana.

Kwa kuwa halipo na kwa kuwa lengo la Chadema ni Tanzania kwanza, basi kupitia uongozi wangu kama ninavyoamini kuwa nitapewa ridhaa hiyo, tutafanya kila jitihada kuhakikisha linakuwepo na linatimiza wajibu wake. Vijana wa Tanzania wamenyimwa fursa ya kuwa na chombo hiki kutokana na ghiliba na hofu ya watawala wasiowajibika kwa wananchi wao.


6. Ni jukumu la BAVICHA kuwasemea vijana wanaonyimwa haki zao kwani hawana mahali salama pa kukimbilia kutokana na ukweli ulio dhahiri kuwa Umoja wa Vijana wa Chama cha Mapinduzi (UVCCM) hauwezi kuwapigania.

UVCCM haiwezi kusimamia mambo yenye maslahi kwa taifa tena. Vijana wasio na ajira, vijana wa mitaani, wafanyabiashara ndogo ndogo (wamachinga) wamebaki wakiwa na wahanga wa mfumo mbovu wa elimu na utawala. Wale wa shule za kata wapo mitaani, ni nani wa kuwasemea na kuwapigania? Ni lini watajua jukumu lililopo mbele yao la kulijenga taifa lao ilhali uzalendo wao unatumika vibaya?


UVCCM wamegeuka kuwa makuwadi wa Uzembe na Ufisadi. UVCCM wamekuwa madalali wa fitina za siasa chafu na mbeleko ya watawala walioshindwa. UVCCM kimekuwa ni kijiwe cha watoto wa vigogo.

Vijana maskini wanahitaji chombo chao, na chombo hicho ni BAVICHA. Wananfunzi wa shule za msingi,sekondari na vyuo vikuu wamekosa chombo cha kuwaunganisha,wanafunzi wa Vyuo ni sehemu muhimu katika kujenga maono na mtazamo wa Taifa kwa siku za Mbele.Nitahakikisha BAVICHA inakuwepo kwa ajili yao, inakuwa sauti yao, mtetezi wao na tumaini lao. Zama za utumwa sasa tunazimaliza.


Kwa moyo wa dhati kabisa,na kwa hisia za pekee nilizo nazo kuhusiana na hatima ya vijana wenzangu hawa,kwa dhati kabisa nitafanya kazi usiku na mchana kuhakikisha makundi haya tunayaunganisha katika harakati za kudai mabadiliko ikiwa ni pamoja na kujiandikisha kupiga kura na kuzilinda, kwani matatizo yao yanatokana na mfumo mbovu uliowekwa na CCM.

7. Tatizo kubwa la vijana ni ukosefu wa mitaji, elimu ya ujasiriamali na uwezo mdogo wa kuchanganua miradi ya kuwaingizia vipato. BAVICHA tutashirikiana na asasi za kiraia kuhakikisha vijana wengi iwezekanavyo wa maeneo mbalimbali nchini wanajengewa uwezo huo. Elimu yangu ya uchumi, biashara na fedha pamoja na ujuzi wa vijana wengine, nitahakikisha vinatumiwa ipasavyo kuliwezesha baraza kutimiza wajibu huu.


8. Nitaliongoza baraza kuhakikisha chama kinafika katika kila kona ya nchi yetu kwa kuunda mtandao wenye sura ya mfumo wa majimbo ili kurahisisha ugawanyaji wa raslimali za kuliendesha baraza katika ngazi zote na kulisogeza karibu zaidi na wananchi (Decentralization).

Hili ni vuguvugu la nguvu (Aggressive Movement) lenye lengo la kukabiliana na chama dhalimu (Brutal party) kama CCM chenye fursa za ziada (Added advantages) za kumiliki raslimali za taifa kwa maslahi yake tangu enzi ya mfumo wa chama kimoja, katika kipindi ambacho Chama na Serikali vilikuwa haviwezi kutenganishwa.

Hii ni ajenda nyingine, inahitaji mjadala lakini nitaifanyia kazi.


9. Ili kutimiza malengo yote haya na mengineyo tunahitaji raslimali za kutosha.Tanzania ya enzi za Mwalimu J.K Nyerere, ilitumia raslimali nyingi katika kupigania uhuru wetu na ule wa mataifa mengine. Mabadiliko tunayoyapigania leo ni sawa na kupigania Uhuru mpya wa Taifa letu (Second Liberation struggle).

Kwa ufahamu wa kuridhisha nilionao kitaifa na kimataifa nitashirikiana na Asasi Rafiki za kitaifa na Kimataifa kuwezesha baraza kupata raslimali na ushauri wa kufanikisha harakati hizi. Tunao marafiki wanaoongoza mabaraza ya vijana ya vyama vya siasa nchini India, Afrika Kusini, Msumbiji, Ghana, Zambia, Mauritius, Canada na Nigeria.Hawa wote tutashirikiana nao vizuri.


Nitaliongoza pia baraza kuimarisha na kuendeleza mikakati ya uchangishaji wa fedha na raslimali nyingine iliyoanzishwa na Kurugenzi ya Vijana ya Chadema miaka michache iliyopita, mathalan kuendeleza programu ya Mfuko wa Vijana na Ubunge.

Huu ulilenga kukusanya fedha kwa njia ya harambee ili kutunisha mfuko wa kuwawezesha vijana kugharamia kampeni zao wanapowania nyadhifa za kiserikali kama ubunge, udiwani na nyadhifa za serikali za mitaa.


10. Ili kujenga uwezo wa kudumu wa BAVICHA kujitegemea kiraslimali, nitahakikisha nashirikiana na viongozi wenzangu na wataalam mbalimbali kuanzisha vitega uchumi au miradi mikubwa ambayo mapato yake yataliwezesha baraza kujiendesha na kurahisisha harakati za kulikomboa upya taifa letu.


WASIFU WANGU KITAALUMA


Kwanza kabisa mimi ni kijana mwenye umri wa miaka 27. Kanuni zinamtaka kijana mwenye umri usiozidi miaka 30 kujitokeza na kugombea.Kwa kigezo cha umri na sifa nyinginezo nimetimiza


Mimi ni mhitimu wa wa Shahada mbili za Uzamili (Masters) katika fani mbili tofauti kutoka vyuo vikuu viwili tofauti vya nchini India. Ninayo Shahada ya Uzamili katika Uchumi yaani "Masters of Arts in Economics" kutoka chuo kikuu cha Allahabad nchini India.


Pia, nimehitimu Shahada ya Uzamili ya Uhusiano wa Kimataifa nikiwa nimebobea katika sera za mambo ya nje hasa kwa mataifa yenye nguvu duniani kama Marekani - (Masters of Arts in International Relations specializing in Foreign Policy of Major Powers) kutoka chuo kikuu cha Annamalai nchini India


Nimehitimu Shahada ya kwanza katika uongozi wa Biashara nikiwa nimejikita katika Masuala ya Fedha (BBA Hons) kutoka chuo kikikuu cha Allahabad nchini India. Nimehudhuria semina na makongamano mbalimbali ya ujasiriamali na vijana


WASIFU WANGU KIUONGOZI


Nimekuwa Mwenyekiti wa Serikali ya Wanafunzi wa Kimataifa wa Chuo Kikuu cha Allahabad. Kwa nafasi hiyo niliongoza wanafunzi kutoka nchi zaidi ya 40 Duniani. Nilikabiliana na changamoto kubwa ya kuunganisha jamii yenye watu wenye tabia, tamaduni na hulka tofauti duniani. Kupitia Baraza la vijana la taifa nitautumia uzoefu nilioupata kufanikisha malengo yote tuliyojiwekea.


Nimeshiriki harakati za kisiasa za Chadema kupitia mikutano ya hadhara, kampeni na makongamano mbalimbali. Nilishiriki kutafuta kura za chama katika baadhi ya majimbo ya hasa ya mkoa wa Morogoro na Dar es Salaam.


Nimekuwa kiongozi tangu nikiwa shule ya msingi hadi vyuo vikuu.Nikiwa chuo kikuu nilikuwa kiongozi wa Jumuiya ya watanzania katika mji wa Allahabad kwa muda wa miaka 2 kuanzia mwaka 2006-2008 .Nilipata fursa ya kuwaunganisha watanzania na jamii ya wanafunzi wengine kutoka kona mbali mbali za Dunia pamoja na kutetea maslahi ya wanafunzi wa Kitanzania katikati ya changamoto mbali mbali nchini India


UZOEFU WANGU KIKAZI


Nimewahi kufanya kazi kama Afisa Utawala na Fedha (Administrative and Financial officer) wa kampuni ya Reliance ya nchini India kupitia mfumo wa kuongeza ufanisi wa kampuni kwa muda wa ziada mwaka 2006/2008


RAI YANGU KWA TAIFA KWA WAKATI HUU TULIONAO


Ndugu Wanahabari,
naomba mnifikishie ujumbe huu kwa umma.

HALI YA UCHUMI


Hivi sasa Watanzania tunakabiliwa na hali ngumu ya maisha.Mfumuko wa bei uko juu, Deni la Taifa limeongezeka.Kupanda kwa bei za vyakula kunatokana na serikali kutokuwa na dhamira ya dhati kwa miaka mingi ya kuwekeza kwenye kilimo cha umwagiliaji. Kupitia cha umwagiliaji kisichotegemea bahati ya mvua, taifa letu lingeweza kudhibiti mfumuko wa bei za vyakula kwani kingekuwa kinapatikana vya kutosha muda wote lakini pia wakati huo huo kilimo hicho uhakika kingetoa ajira kwa zaidi ya asilimia 80 ya Watanzania.


Siasa za kauli mbiu hazitatufikisha popote na sasa zimepitwa na wakati. Kauli mbiu au sera ya Kilimo kwanza haikupangwa vema na wala haiwezi kuwa na ufanisi kwa sababu serikali ilipaswa kuwekeza kwenye maji kwa kubuni mfumo mzuri wa kilimo cha umwagiliaji. Ingeanza na Maji kwanza ndipo suala la kilimo kwanza lifuate.


Kilimo kimeshawahi kupewa majina na kauli mbiu za kutisha kama Kilimo cha Kufa na Kupona,Siasa ni Kilimo,Kilimo ni Uti wa Mgongo nk.Ni tofauti gani iliyopo kati ya kauli mbiu zote hizi na zimekuwa na manufaa gani kwa Watanzania hadi tuje na kauli mbiu nyepesi ya Kilimo kwanza?


Mateso wanayopata Watanzania yamechangiwa kwa kiasi kikubwa na serikali isiyo na vipaumbele.Matumizi mabaya ya kodi ya Watanzania yangedhibitiwa, tungeweza kuwekeza kwenye kilimo cha umwagiliaji. Serikali ipunguze matumizi yasiyo ya lazima, ielekeze fedha hizo katika kutoa Ruzuku kwa bidhaa za vyakula au kupunguza kodi kwenye viwanda kwa masharti ya kuuza bidhaa za vyakula kwa gharama nafuu.

Viwanda vingi nchini vinajaribu pia kupandisha kodi katika jitihada za kupunguza au kufidia hasara iliyotokana na Mgawo wa Umeme hali iliyosababisha gharama za uzalishaji kupanda. Kwa hiyo serikali na bunge vihakikishe vinapitisha bajeti ya dharura ili kupunguza makali haya ya maisha.


Pia kwa mtazamo wa muda mrefu, ni muhimu tujenge viwanda vya ndani ili kukuza upatikanaji wa ajira kwa vijana na kutoa fursa zaidi kwa wakulima wetu kuuza mazao yao kwa thamani. Ajenda ya kilimo kwanza iende sambamba na viwanda vya usindikaji mazao (Processing Industries) ili kuongeza thamani (Value) ya bidhaa hizo na hasa zinazosafirishwa nje ya nchi


JUMUIYA YA AFRIKA MASHARIKI NA SERA YETU YA MAMBO NJE.


"Natoa onyo kuwa serikali isipochukua hatua ya kutazama mwenenndo wa misimamo katika siasa za kimataifa, basi upo uwezekano mkubwa wa heshima ya Rais na hadhi ya nchi kuchafuka katika medani za kimataifa".


Nitatoa mfano.


Serikali ya Kenya kupitia Rais wake Mwai Kibaki imekataa kupeleka kesi za watuhumiwa wa vurugu za baada ya uchaguzi mkuu wa nchi hiyo (post election violence) katika mahakama ya kimataifa ya wahalifu wa kivita (International Criminal Court –ICC).


Na izingatiwe kuwa katika jitihada za kutafuta kuungwa mkono, serikali ya Kibaki ilimtuma makamu wake wa Rais, Kalonzo Musyoka kufanya ushawishi wa kidiplomasia ili nchi za kiafrika ikiwemo Tanzania iwaunge mkono (Shuttle diplomacy).


Umoja wa nchi za Afrika (AU) umeunga mkono msimamo huo wa serikali ya Kenya wa kukataa watuhumiwa hao wa vurugu za uchaguzi kupelekwa mahakama hiyo ICC nchini Uholanzi na badala yake wanataka watumie mahakama maalum za ndani ya Kenya (Special Tribunal Courts) kushughulikia tuhuma hizo. Serikali yetu ya Tanzania nayo kupitia AU imeunga mkono msimamo huo wa kukataa watuhumiwa hao kupelekwa ICC.


Lakini naomba itiliwe maanani kuwa msimamo huo wa serikali ya Kibaki si msimamo wa Wakenya walio wengi, kwani kwa mujibu wa matokeo ya kura rasmi ya maoni iliyopigwa hivi karibuni, asilimia zaidi ya 60 ya Wakenya wanataka watuhumiwa hao wakashitakiwe katika mahakama hiyo ya IC iliyoko The Hague nchini Uholanzi.


Pia hata Waziri Mkuu wa nchi hiyo, Raila Amolo Odinga, yupo upande wa Wakenya walio wengi akipinga uamuzi huo wa Kibaki na wenzake.


Tatizo ni nini?

Tatizo ni kwamba serikali yetu kupitia AU imeunga mkono uamuzi wa serikali ya Kibaki wa kutowapeleka watuhumiwa hao ICC na jitihada za serikali hiyo za kutaka kujiondoa kwenye mkataba wa kimataifa wa Roma (Rome Statue) wakati Wakenya walio wengi hawataki.

Ikumbukwe Tanzania ilipata fursa ya pekee ya kuwa msuluhishi wa mgogoro wa kisiasa nchini Kenya baina ya upande wa Kibaki na Odinga, heshima hiyo tulipewa kwa heshima ya kuaminiwa (Honest broker) katika kusimamia matakwa ya Wakenya.

Na kwa kutambua mchango wa nchi yetu, Rais alipewa zawadi ya kutunukiwa shahada ya udaktari wa falsafa wa heshima kutoka Chuo Kikuu cha Umma cha Jomo Kenyatta.


Kwa mantiki hiyo, kwa msimamo ambao serikali yetu imeonyesha, wa kutofautiana na Wakenya walio wengi (zaidi ya asilimia 60), ni dhahiri upo uwezekano kwa nchi yetu kujiingiza katika mgogoro wa kidiplomasia baina yetu na wananchi wa Kenya.


Upo uwezekano pia wa nchi yetu kujiingiza katika mgogoro wa kidiplomasia baina yetu na serikali ya Kenya katika siku za usoni kama Rais wa nchi hiyo atakuwa Raila Odinga wa chama cha ODM ambaye tayari ameshatangaza azima yake ya kuwania urais wa nchi hiyo katika uchaguzi mkuu ujao wa 2012.


Ninatoa wito wa kumtaka Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa, Bernard Membe pamoja na Waziri wa Ushirikiano wa Afrika ya Mashariki, Samuel Sitta, kutoa tamko la kuueleza umma wa Watanzania kwanini wameiingiza nchi yetu kwenye msimamo unaopingwa na Wakenya wengi ambao ni majirani zetu na ni ndugu zetu wa karibu. Je, waliona ni busara tu kumuunga mkono Kibaki na wenzake wachache na kupuuza matakwa ya
Wakenya walio wengi?

Je hawaoni kwa kufanya hivyo wanalichonganisha taifa na majirani zetu wa karibu?

Katika hali ya kawaida nilitarajia kuona serikali yetu ikiheshimu matakwa ya Wakenya na msimamo wetu wa awali ambao ulikuwa ni kusimamia maslahi ya Wakenya walio wengi.

Kimsingi, sera na misimamo yetu katika siasa za kimataifa, hasa diplomasia ya uchumi, vimekuwa vikiyumba, badala tumetilia mkazo diplomasia ya kuomba misaada na kushukuru. Tunahitaji mabadiliko makubwa ya kisera, mchakato wa kupata katiba mpya ni vema ukatumiwa kufanikisha mabadiliko hayo.


UJUMBE WANGU KWA CCM.


Natoa wito kwa CCM, kukaa chini na kuitumia sekretarieti yao mpya kuwaandaa wafuasi wake kisaikolojia, kwani mwaka 2015 wataingia katika dimbwi la maji taka ya historia.Waendelee kushirikiana na CUF ili kupata uzoefu wa siasa za upinzani ili ifikapo mwaka 2015 waunde kambi moja ya Upinzani badala ya kuwatumia vijana wao kuwahadaa na kuwapotosha Watanzania.

Ufisadi na ghiliba ndiyo uti wa mgongo wa CCM ya sasa kwa hiyo kujivua gamba ni hadaa tu.Natoa wito kwa Watanzania kuendelea kuwapuuza, hawana jipya, walichofanya ni mwendelezo wa vita yao ya kimaslahi.

Nawatakieni kila la kheri katika kazi yenu yenye manufaa kwa taifa.

Asanteni sana kwa kunisikiliza.


Mungu Ibariki Afrika
Mungu Ibariki Tanzania
Mungu Ibariki CHADEMA

Imetolewa na.
Bernard Saanane

Mgombea wa nafasi ya uenyekiti wa Baraza la Vijana la Taifa Chadema (CHADEMA)

 
Good Luck guy, let us see if it will make it happen to you.

After all umesomea India, that mean utakuwa unakautamaduni wa kifisadi kama wa kihindi kihindi Ben.

We have vijana wazuri waliosomea kwenye vyuo vya kwetu Tanzania, nao wamebobea kwenye taaluma zaidi kama si ya kwako.
John Heche is almost the best. Vote for him kama unaipenda CHADEMA

Good luck!
 
Hongera kwa kuonyesha nia na kutueleza wewe ni nani?wanao uliza who are you hawajasoma taarifa yako wasikukatish tamaa
 
Ben,

Ndo wewe? Hongera kwa kuonyesha nia kwa vitendo. Kama sio wewe mwambie aje hapa akomazwe. Pia patamuongezea umaarufu wa kukutana na vijana kama Heche, David.

Ole wenu mjenge makundi kwa faida ya chama cha magamba bila kujijua.
 
Hongera Ben,

Ushauri wangu ni kuwa unapotaka kugombea Chadema hakikisha unajishughulisha na masuala yanayohusu Chadema pekee. Kuwataja CCM kwenye mkakati wako huu ni kuwapa heshima wasiyostahili... wamepoteza heshima hiyo na hawatakiwa kuwepo kwenye mkakati wako wa kuingoza BAVICHA na Chadema kwenda 2015.

Nakushauri pia ukifanikiwa usaidie kuongeza kasi ya kufungua matawi ya chama ... watu wengi wanataka kujiunga na Chadema lakini changamoto kubwa iliyopo ni kupata ofisi ya Chadema (mimi ni miongoni mwa wanaotaka kujiunga kwa miaka miwili sasa)
 
Hongera sana Ben!

Personally nimefurahishwa na kujitokeza kwako hapa JF na kueleza nia yako.

Kama utashinda chondechonde makundi ni sumu kwa chama.Always simamia haki with time your price will be high and high.
 
karibu sana ben, ila hatujakusikia kwenye harakati za chadema wala kwenye uchaguzi mkuu ambapo tuliwaona vijana waliojitia muhanga na wakaonyesha uwezo wao katika anga za harakati na siasa za chadema na tz kwa ujumla wake, mashaka yangu ni kwamba wanachadema watakuamini vipi? Wapo vijana kama akina John Heche wa tarime, Joshua Nassari wa arumeru mashariki, Dadi igogo wa Rorya, Mwampamba wa mbozi e.t.c. Mimi nadhani ungejiunga kwenye harakati za chama kwanza, ukafanya harakati zikaonekana na baadaye fursa zikafata ukizingatia chama kinaendelea ku-accelerate siku baada ya siku.

Ushauri wangu kwako
 
Wanajamvi, haya ni baadhi ya majina niliyoyasikia yakitajwa kwenye nafasi mbalimbali za uongozi wa Baraza la Vijana la Chadema, toa maoni yako tafadhali.

NAFASI YA MWENYEKITI.
1. John Heche (rorya)
2. Silinde David (mbozi mbeya)
3. Mwampamba (mbozi mbeya)
4. Habib Mchange ( kibaha pwani)
5. Ben Saanane ( dar/morogoro)

MAKAMU.
1. Gwakisa Baton (mbeya)
2. Kinabo (moshi)
3. Shalifa (zanzibar)
4.

NAFASI YA KATIBU MKUU.

1. Nassari Joshua (arumeru mashariki)
2. Deogratius Munishi (moshi)
3. Steven Owawa (rorya)

NAIBU KATIBU MKUU.
1. Dadi Igogo (rorya)
2. Odero Oderos (rorya)


mengine nitaweka nikiconfirm. Wadau na wanachadema toeni maoni yenu.
 
Wanajamvi toeni mawazo yenu, mnaowafahamu vizuri vijana hawa embu wekeni wasifu na profiles zao tafadhali
 
Back
Top Bottom