Tanzania haya yametokea!!!!

Mtu wa Pwani

JF-Expert Member
Dec 26, 2006
4,184
671
•
Nesale : Polisi waliamuru nimuage mume wangu kabla hawajamuua


Na Seif Mangwangi,Ngorongoro

MIEZI sita baada ya kuuawa aliyekuwa kiongozi wa kimila wa jamii ya kimasaai ( Laigwanan), marehemu Shangai Ole Putaa, mke mdogo wa kiongozi huyo Bi.Nesale Putaa amedai kabla mumewe kuuawa askari walimwamuru amuage kwani hatamwona tena.

Kiongozi huyo wa kimila aliuawa kwa kupigwa risasi na askari polisi wilayani Ngorongoro kwa kile kilichoelezwa kuwakimbia askari hao baada ya kudaiwa kuonesha silaha aliyokuwa akiikodisha kwa majambazi.

Akizungumza na waandishi wa habari waliotembelea nyumbani kwake katika kijiji cha Soitsambu, Bi. Nesale alisema kabla mumewe hajauawa Novemba 7 mwaka jana, askari walifika nyumbani kwake wakiwa na mumewe baada ya kumchukua katika sherehe za kimila ( Manyata) na kumfikisha nyumbani huku wakimwamuru kutoa silaha aliyokuwa akiikodisha kwa majambazi.

Alisema hata hivyo mumewe marehemu Putaa alidai kutokuwa na silaha yoyote na hata askari walipopekua nyumba yake walikosa silaha waliyokuwa wakidai kuwepo ndani ya nyumba hiyo, badala yake walimuita na kumtaka kumuaga mumewe kwa kuwa hatamuona tena.

" Walipokosa silaha hiyo wakaniita na kuniambia nimuage mume wangu kwa kuwa sitamuona tena, baada ya kukaa siku nzima bila kurudi nyumbani zikaja taarifa kuwa mume wangu kapigwa risasi na wale askari ndipo wazee wakaanza kufuatia hadi hospitali ya Wasso na kukuta mwili wake mochwari,"alisema.

Alisema tangu kutokea kwa kifo hicho hakuna taarifa yoyote aliyoipata kutoka serikalini licha ya wazee wa jamii hiyo kujaribu kufuatili mauaji ya kiongozi huyo na kwamba hivi sasa maisha yake yamekuwa magumu kufuatia kutokuwa na mtu wa kumuhudumia.

Bi. Nesale mwenye mtoto mdogo wa mwaka mmoja alisema mke mwenzake Bi.Meeyu Putaa hivi sasa ni mjamzito wa mimba ya miezi nane hivyo maisha yao yamekuwa ya kubahatisha kufuatia kutoweza kuendesha famili zote mbili zenye zaidi ya watoto kumi walioachwa na marehemu.

Kwa mujibu wa Mwenyekiti wa kitongoji cha Soitsambu yalipotokea mauaji hayo, Bw.Loota Nyaaruu, walipata taarifa za kuundwa kwa tume ya kuchunguza kifo cha kiongozi huyo wa kimila lakini walipofuatilia ili wajumbe wa tume hiyo wafike nyumbani kwa marehemu ili kupata taarifa za kifo chake walikatazwa na viongozi wa wilaya kuwasiliana na tume hiyo.

Alisema mauaji ya kiongozi huyo ni ya uonevu na kwamba madai ya askari kuwa marehemu alikuwa akificha silaha taarifa walizopata kutoka kwa majambazi wawili waliokuwa wamekamatwa wilayani humo si za kweli kwa kuwa kiongozi huyo ambaye pia alikuwa Mwenyekiti wa Kitongoji cha Soitsambu hakuwahi kusikika kujihusisha na uhalifu wowote na badala yake ndie aliyekuwa mstari wa mbele kupinga uhalifu wilayani humo.

Aliiomba Serikali kufuatilia suala hilo ili askari waliofanya mauaji hayo wabainike na kuchukuliwa hatua za kisheria na kwamba endapo tume iliteuliwa kuchunguza kifo hicho ni vema ikafanya uchunguzi kwa mara nyingine kwa kuwa haikuweza kuwahoji ndugu wa marehemu pamoja na viongozi wa kitongoji hicho.

Akizungumzia mauajia hayo Mkuu wa Wilaya ya Ngorongoro Bw. Jowika Kasunga alikiri kuundwa kwa tume hiyo na Mkuu Jeshi la Polisi nchini, Bw. Saidi Mwema lakini alikiri kutofika katika familia ya marehemu na badala yake alidai huenda majibu yatatolewa hapo baadae.


majira
 
Back
Top Bottom