Simulizi: Najisalimisha

Judithkaunda

Member
Aug 21, 2022
90
228
SIMULIZI: NAJISALIMISHA

MTUNZI:JUDITH KAUNDA

0682253906


STELLA

Kwenye hii Dunia kuna mambo ambayo kila mmoja wetu amelazimika kuwa nayo bila hiari yake, kama ambavyo maisha hayatupi nafasi ya kuchagua kuzaliwa jinsi tulivyo. Hakuna aliyechagua azaliwe na mzazi aliye naye. Kama ilivyo kwa wengine, hata mimi nimejikuta nimezaliwa Stella. Na nina pambana na stori ya kuwa Stella.


Ni mzaliwa wa Songea, lakini Chato mkoani Geita ndipo nyumbani kwetu. Ni mtoto wa kwanza kati ya watoto watatu wa mama ntilie maarufu mtaani kwetu. Mimi na wadogo zangu Wellu na Enock Katika makuzi yetu hatukubahatika kupata malezi ya baba.

Nimekulia kwenye familia ya kimaskini lakini yenye furaha na amani kwa sababu ya mama mwenye upendo, ambaye anapambana kwa ajili ya wanae.

Mama aliniambia baba yangu alifariki nikiwa mdogo sana. Ni kweli sikumbuki chochote kuhusu baba yangu. Hata hivyo mama hapendi kumzungumzia.

Lakini mjomba aliwahi kuniibia siri na kuniambia kwamba baba yangu alikuwa jambazi na alitengana na mama baada ya kukamatwa na kuhukumiwa kifungo cha maisha gerezani. Na hakuchukua muda mrefu akafariki.

Kuna kipindi nilitamani kwenda Songea kuwatafuta ndugu zangu, lakini mama akanizuia na nilipomuuliza sababu akasema ndugu wa baba walimchukia sana na walimnyang’anya mali zote za baba alizokuwa nazo na hata kumtishia uhai wake kama atazifatilia. Sikuona sababu ya kwendelea na mpango wangu nahisi hata wao hawakuwahi kunitafuta.

Sijui niseme mama yangu ana bahati mbaya au ana mkosi na wanaume!

Baba yao Wellu na Enock yupo hai lakini hawajibiki kwa lolote zaidi ya kupiga simu na kuwapa ahadi asizoweza kutimiza, na tatizo lingine ni mlevi kupindukia hata yeye mwenyewe hawezi kujihudumia.

Siwezi kumlaumu mama yangu namuona anavyojitahidi kusimamia nafasi zote mbili, ingawa kuna kipindi tuliishi maisha magumu sana lakini hakuwahi kututelekeza. siku zote amekuwa mtu wa kupambana sana kuhakikisha tunapata mahitaji yote muhimu ikiwemo Elimu.

Nilikuwa mtoto mzuri na mwenye adabu ambaye nilimfanya mama yangu ajivunie. Kwa juhudi zake amefanikiwa kunisomesha mpaka chuo cha ualimu Butimba Mwanza, ilikuwa ndoto yake kunifikisha pale. sikuwa na uwezo mkubwa darasani lakini nilisoma kwa bidii kuhakikisha namfurahisha mwanamke anayepambana kulipa marejesho ya deni alilokopa vikoba ili nisome.

Baada ya kumaliza chuo nikarudi nyumbani, nikaongezeka kwenye idadi kubwa ya wahitimu wanaosubiri ajira. Wakati huo nilishatuma maombi ya kazi sehemu mbali mbali. Sikukaa bure nyumbani nilikuwa namsaidia mama kwenye biashara yake ya kuuza chakula.

Nilikuwa mwenye mawazo sana kwa sababu vyeti vyangu havikubadilisha chochote pale nyumbani. Mdogo wangu Enock alikuwa amemaliza kidato cha nne na matokeo yake yalikuwa mazuri, alitakiwa kwenda kidato cha tano na wakati huo biashara ya mama haikuwa nzuri sana na hali ya afya yake ilianza kudhorota.

Nilijiuliza mara elfu, mimi kama dada wa familia nifanye nini, kusaidia familia yangu?

Kama bahati siku moja rafiki yangu Happy alinipigia simu nakuniomba ushauri ni biashara ipi afanye. Nilimshauri biashara nyingi na tukazichanganua na mwisho akachagua duka la Steshenari. lakini akaniambia hajui vitu vingi kuhusu kazi hiyo, hivyo aliniomba niende kumsaidia.

Happy ni rafiki yangu wa karibu sana tulifahamiana tukiwa chuo. Hakuwa mtu wa kujikweza licha ya familia yake kuwa nzuri kifedha. kwa kiasi flani anajua stori yangu na mambo ninayopitia aliahidi kunilipa kwa mwezi na ningeishi nyumbani kwao. Nilifurahi kwa sababu siku zote nilikuwa naamini nikiwa nje ya nyumbani ntajituma zaidi ili niweze kusaidia familia yangu.

Nikalazimika kumdanganya mama kuwa nimepata kazi kwenye shule binafsi. Nilitamani kumuona mama akifurahia matunda ya juhudi zake maombi yake alitamani kuniona nafanyia kazi kile nilichosomea. Mama alifurahi sana na kunipa Baraka zake bila kusahau maonyo kama mzazi.

Mama yangu ananiamini sana kwa sababu sikuwa na tabia za kutilia shaka. Na kati ya miaka mitatu niliyosoma chuo Mwanza, alipokea kesi moja tu iliyomtisha…

Ni ile siku aliyopigiwa simu na mke wa mjomba wangu niliyekuwa nikiishi nyumbani kwake, akidai natembea na mumewe. Hata mimi nilishazwa na taarifa hiyo nilikuwa nawaheshimu sana.

Na tatizo lilianzia pale alipomkuta mjomba kalala chumbani kwangu.

Ndio chumbani kwangu!

Najua hata wewe unashangaa lakini siku hiyo mjomba alirudi akiwa kalewa sana na mkewe aligoma kumfungulia mlango. chumba nilichokuwa natumia kilikuwa cha nje akaamua kulala chumbani kwangu.

Nilikuwa sikifungi kwa sababu kulikuwa na baadhi ya vitu vya yule mama na sikuwa na wasiwasi kwa sababu ni ndani ya geti.

Usinifilie vibaya sikuwepo siku hiyo nilikwenda msibani, mmoja wa rafiki zangu alikuwa amefiwa na baba yake. Msibani palikuwa mbali na muda ulikuwa umeenda sana hivyo ni kalala huko.

Namshukuru mama licha ya kuwa na wasiwasi na kunionya lakini alichagua kuniamini, tuachane na hayo.

Hata sasa hakuwa na wasiwasi aliniruhusu. Nilijiandaa na kabla sijaondoka niliwaaga wadogo zangu.

Nilimuhakikishia Enock lazima ataenda shule na mdogo wangu wa mwisho Wellu alikuwa darasa la saba kwa bahati mbaya alikuwa hapendi shule. Lakini alikuwa mzuri sana na tayari vijana walipishana pale nyumbani. Nilimuonya na kumwambia athari na matokeo ya mahusiano katika umri mdogo na kumtolea mifano hai ya marafiki na majirani zetu.

Mpaka wakati huo dada yake sikuyapa nafasi mapenzi au niseme sikumpata wakuisumbua akili yangu. kitu pekee nilihitaji ni kufanya kazi kwa bidii ili ni mpunguzie mama majukumu. Nadhani hili nimejifunza kutoka kwake.

Mama yangu amewahi kuwa kwenye mahusiano lakini hakuwahi kutuacha au kumtegemea mwanaume kutulea.

Wazo la kuolewa nililitafsiri kama kuzikimbia shida za nyumbani kwetu na mimi nilichagua kupambana nazo mpaka ziamue zenyewe kujitenga nasi.

Baada ya kufika Mwanza. Mimi na Happy tulianza biashara yetu kama tulivyopanga, kawaida mwanzo huwa mgumu lakini kadri muda ulivyoenda tukaanza kuzoeleka na kupata wateja wengi. Happy alipenda uchangamfu wangu kazini nilijitoa kweli kweli kwa sababu sikuwa na mbadala ilikuwa tofauti kwake, alifanya kazi kama sehemu ya kujishughulisha tu na kama angehitaji kitu angeweza kupata kwa wazazi wake au mchumba aliyenae.

Alikuwa akinilipa hata kama hatujapata pesa nzuri. Kwa namna nilivyokuwa nimedanganya ikabidi nilipie uongo wangu. kila mwisho wa mwezi nilimtumia mama pesa nikimwambia ni sehemu ya mshahara wangu na kumuomba amuhifadhie Enock kwa ajili ya shule.

Nilipozoea mazingira nikapata wazo la biashara nyingine ya kuuza juice na baets pale dukani. Rafiki yangu Happy hakuwa na hiyana alikubali nikafanya ili kupata pesa zaidi. Hii biashara ndogo ilikuwa ya kwangu nayo ikaenda vizuri na nikapata pesa. Enock alipiga simu kunishukuru baada ya kupata mahitaji yote ya shule.

Mdogo wangu anajua namna ya kushukuru mpaka unalewa sifa, ili umkumbuke kwa mara nyingine. Alinitia nguvu za kwendelea kupambana zaidi.

Mambo yalienda vizuri mpaka pale Happy alipovishwa pete na kutangazwa tarehe ya ndoa yake. Happy alikuwa mwenye furaha sana na kwa vyovyote nilitakiwa kufurahia Ilikuwa habari njema kwa rafiki yangu. lakini ilikuwa tofauti kwangu nilishidwa kuficha simanzi niliyokuwa nayo.

Haukuwa wivu wala chuki bali uwoga wa maisha, ningewezae bila Happy?

Happy alikuwa ananifahamu sana na hakupenda unafki aliponiona tofauti akaniuliza si kuwa na budi kumwambia kuhusu hofu yangu.

Aliniambia baada ya kufunga ndoa angehama mkoa, tutatengana na kubwa lililonisumbua ni kazi, nilikuwa nimetafuta kazi baadhi ya sehemu bila mafanikio. Nilimweleza bayana akanipa moyo na kuniambia nisijali kila kitu kinasuruhisho isipokuwa kifo tu.


Happy ni zaidi ya rafiki kwangu. wengi walionifahamu kupitia yeye wanajua sisi ni ndugu na istoshe nlikuwa naishi nyumbani kwao. Kitu ambacho sikutegemea kutoka kwake kwa wakati ule alipokuwa bize na maandalizi ya harusi yake ni kunitafutia kazi. Na haikuwa rahisi kumshawishi binamu yake aniajiri.



****

Nilipata kazi kwenye studio kubwa ya kisas iliyokuwa katikati ya jiji la Mwanza. Ofisi yetu inawafanyakazi sita na wakike nilikuwa peke yangu. Kila mfanyakazi alikuwa na majukumu yake wapo wanao husika na mambo ya video na picha kwenye sherehe mbalimbali, kazi yangu ilikuwa kusafisha picha, mabango na kupiga passport hiyo nd’o kazi yangu sasa.. Na bosi wetu ni Photographer maarufu hapa mjini.

Niliipenda kazi hii na kufanya kwa bidii. Nimefanya kazi hapa zaidi ya mwaka na nimeaminika na bosi.

Nilianza kuona mshahara haunitoshi tena bosi wangu hakuwa na hiyana kama binamu yake pale nilipo muomba aliniruhusu niuze juice na bites pale ofisini muda wa chakula.

Lakini bado majukumu yaliongezeka, baada ya Happy kufunga ndoa nilihama nyumbani kwao. Happy alikuwa mtoto wa mwisho kwenye familia yao na ndugu zake wote walikuwa na familia zao. Pale nyumbani walibaki wazazi na msaidizi tu. wazazi wake walinizoea sana nilipowaaga wakanihimiza nibaki lakini niliona ni vema kuwapisha nilijua mazingira yatakuwa magumu bila Happy na sikutaka yanikute kama yale yaliyonikuta kwa mjomba wangu.

Dunia ilinikaribisha rasmi kwenye mbio zake, nyumba ya kupanga ikanifundisha uchugu wa kulipa kodi na wakati huo Enock aliendelea kufanya vizuri kwenye masomo yake.

Namuamini mama yangu ni mbishi sana asingeshindwa lakini haya yalikuwa majukumu mazito sana kwake na hakutaka nisumbuke lakini ningewezaje kupuuzia kama hakuna kitu?

Wakati nafahamu mama anasumbuliwa na mgongo na daktari alimshauri apumzike.

Mdogo wangu Enock alijua dada yake ni mwalimu mwenye mshahara hakusita kuniambia shida zake na mimi sikutaka apotee, nikajitwika jukumu la kumsomesha.

Ilikuwa ni kawaida yangu mambo yaliponizonga nilikwenda kwa bosi na kumuomba anikopeshe pesa na ningerudisha mara tu ntakapo pokea mshahara wangu.

Lakini awamu hii bosi alinipa msaada mwingine baada ya kumwambia ukweli pesa nayohitaji ni kwa ajili ya kodi.

“Stella nyumba yangu sio kubwa lakini kuna chumba kimoja kiko wazi unaweza kuishi, sintakuchaji chochote na hiyo pesa ambayo ungelipia kodi ukaendelea kumsaidia ndugu yako.” Alisema akinitazama usoni ni kama aliyasoma mawazo yangu.

Nilishusha pumzi ndefu hakika nilikuwa nimelemewa. Kwa kiasi Flani nilihisi amenitua mzigo mgongoni mwangu.

Wazo lake lilikuwa zuri ilikuwa ngumu kukataa kwa hali niliyokuwa nayo nilihitaji pesa zaidi kwa sababu ya ahadi niliyoweka kwa Enock.

Nilitafakari kwa muda kisha nikamkubalia, Shida zikanifanya nidhalau kilichonikuta kwa mjomba wangu, nikajiaminisha hakutakuwa na tatizo hata hivyo alikuwa hajaoa, nikajidanganya eti kama akiamua kuoa basi ntaondoka haraka.

Bosi wangu anamiaka zaidi ya thelathini, lakini muonekano wake ni kama kijana mdogo. Ni mtanashati mrefu kiasi na mwili wake unafaa hata angeamua kuwa model wa kutembea jukwaani kila nguo aliyovaa ilimkaa vizuri, Ni mkalimu na mcheshi sana ni rahisi kumvutia mwanamke yoyote aliye karibu yake.

Nakiri tangu siku ya kwanza nilipoanza kazi hapa ofisini nimefuatwa na wanaume wengi lakini hakuna aliyenivutia kama bosi wangu. Nilimuona kama mwanaume aliyekamilika machoni kwangu.


Bahati mbaya hakuna binadamu mkamilifu bosi wangu alikuwa muhuni kupindukia.

Happy anamjua vizuri binamu yake, kabla sijaanza kazi alinionya juu ya tabia zake, alitaka niwe makini nae sana. lakini hakuniambia namna binamu yake alivyo mtanashati.

Kwa muda niliofanya kazi hapa nimeshuhudia uchafu wake mwingi sana wanawake na mabinti walipishana ofisini kwake na wengi niliwashuhudia wakijipendekeza nadhani hakuwa na haja ya kuwatongoza.

Alikuwa mwanaume mwenye kiburi cha pesa aliwatumia wanawake atakavyo. Mwanzo niliamini hisia ninazohisi kwake ni tamaa tu na zingeondoka baada ya muda nilikuwa siamini kabisa kama moyo wangu ungeweza kumpenda mchafu wa tabia kama yeye.

Nilisahau kwamba mapenzi ni upofu na moyo unachagua wa kuwa naye, eti ukamuona yeye kati ya wote.

Kwa zaidi ya mwaka nafanya kazi hapa nimejitahidi kuficha hisia zangu, ilikuwa rahisi kutokana na tabia zake alinichukulia kama mdogo wake wa mwisho hata hakunionea aibu nilipomfuma studio na mabinti wakishikana.

Lakini hili la kuamia nyumbani kwake lilinipa mawazo sana ntawezaje kwendelea kuficha hisia zangu? Kuwaza kuwa mpenzi wake hiyo ni stori ya kufikirika isiyoleta maana kabisa. huyu mtu ni wa ajabu hakuwahi kuwa na mahusiano ya kudumu na mwanamke hata kwa week moja tu.



****



DANKAN

Kwenye maisha kila kitu kina faida na hasara zake. Ni asili yetu binadamu kutopenda changamoto au matatizo lakini katika hizo nyakati ngumu tunazopitia huzaa vitu vikubwa au jambo zuri. Najua hutaki kuniamini lakini tafakari ni mambo gani mazuri ambayo usingeweza kuyapata kama tu usingepitia jaribu flani?

Naitwa Dankani Moric Bilali. Ni mtoto wa pili kwenye familia yetu. tumezaliwa wawili Dada yangu ameolewa anaishi Arusha na familia yake. Nimekulia kwenye familia inayoongozwa na baba na mama mwenye upendo. nilikuwa kijana mzuri mwenye kujua thamani ya upendo ilikuwa hivyo kabla sijatendwa.

Nilipokuwa chuo katika mahusiano nilitokea kumuelewa Lucy binti wa kinyamwezi. wote tulikuwa mwaka wa pili huyo binti alikuwa mgeni wa jiji la Dar nikamkarimu, na kwa pesa za wazazi wangu nilijitahidi kumfurahisha nilijisifu kidume Lucy alikuwa ni pisi kweli kweli.

Sura yake ya kuvutia iliyopambwa na tabasamu zuri iliuteka moyo wangu na kwa mapenzi aliyonionyesha nikaamini yalikuwa ya dhati. Shepu yake ya Kinyarwanda iliwatesa vijana wengi lakini bahati ikawa upande wangu, nikajiona mwamba nimeokota dodo chini ya mpera,

Sikujua!
Sikujua kama bahati itaniletea balaa!

Nilimpenda na sikujali wala kusikia lolote hata kutoka kwa wazazi wangu, niliamini ni Mungu pekee ndiye angeweza kunitenganisha nae.

Kama kuna kitu nilitamani kukisahau kwenye maisha yangu, basi ni aibu na fedheha niliyoipata siku alipoamua kufunga ndoa. Lucy aliniacha kikatili sana kwa sababu ya pesa alijeruhi moyo wangu na kuugawanya vipande vipande.

Lucy alinifanya niwaone wanawake kama viumbe wakutisha nikaamini kuna nyakati shetani anajifunza kutoka kwao. Baada ya maumivu makali ya kujeruhiwa moyo, niliapa sitakuja kupenda tena kwa dhati maishani.

Lakini yule mwanamke namshukuru sana maumivu aliyosababisha yalinifunza jambo. Pesa sio kila kitu, lakini kila kitu kinahitaji pesa. Na hizo pesa zinafanya vitu vingi viwezekane.

Nikaondoka nyumbani na kuamia jijini Mwanza kwa binamu yangu nikimfanyia kazi kwenye studio yake. sikutaka kutegemea pesa za wazazi tena. Nilijiwekea mikakati ya kutafuta pesa.

Imepita miaka nane bado sijatimiza baadhi ya malengo yangu lakini sipo kama nilivyokuwa. Nina nyumba na gari la kutembelea namiliki studio ya kisasa na nimeajiri vijana wenzangu, na mimi kama Photographer ninaifanya vema kazi yangu.

Sijafanikiwa vya kutosha lakini pesa niliyonayo imenifanya kuwa rijali kwa kila msichana mzuri niliyemuhitaji.

Siwachukii tena wanawake lakini tukio lile liliniathiri sana. Siwezi kusema pesa zimenibadilisha lakini zilinisaidia kuwatumia wanawake nitakavyo na sikusita kuwaacha ikiwa ni sehemu ya kupunguza hasira yangu. Mwanzo ilikuwa kama mtindo wangu wa maisha lakini mazoea yakaibadili na kuwa tabia yangu. Kidume nikajionea sifa kweli kweli.

Imekuwa kawaida kuvutiwa na mwanamke na baada ya kuwa nae usiku mmoja nisitake zaidi kutoka kwake.

Nimeanza kuichukia hali hii!

Umri unakwenda sina mpango wa kuoa hali hii imeleta shida kwa wazazi wangu. sasa wanataka nioe.

Sina mtoto hata wakusingiziwa kwa sababu nilichagua kutowaamini wanawake na kwenye starehe zangu zote nilikuwa makini sikuwahi kuacha zana nyuma. Hata walionililia na kusema hisia zao na wengine walikuwa tayari kunizalia bila ndoa, sikuwa tayari kwa sababu nilifurahia maisha ya ukapera.

****


Leo nimetoka mapema kazini kwa sababu nina ugeni nyumbani kwangu. Kabla sijaenda nyumbani nilipitia sokoni kununua baadhi ya mahitaji namjua vizuri mgeni wangu lazima angehitaji kupika.

Mara baada ya kuingia ndani na kukaribia jikoni nikapokelewa na harufu nzuri ya chakula, nilipiga hatua kumfuata jikoni. Nilipomuona yuko bize nikanyata na kuweka mifuko chini taratibu na kumsogelea bila yeye kujua,

“Hivi huwezi kupika chakula bila kubadilisha hali ya hewa humu ndani?” nilimtania wakati mikono yangu ikizunguka mabega yake na kumkumbatia.

“Umenishtua… umekuja muda gani hata nisikusikie?” Alisema akinitoa mikono yangu na kunigeukia, akanitazama usoni na kuanza kunikagua.

Siku zote mama alinifanyia kama mtoto mdogo lakini bado alitaka nioe haraka. Najua lengo la safari yake huyu mwanamke akiamua jambo lake atalisimamia mpaka afanikishe. kuhusu kuoa hakutaka tena kuzungumzia kwenye simu kaamua kufunga na safari.

“Mzee anaendeleaje?”

“Hajambo lakini madawa anayotumia yanamchosha sana, vipi wewe unaendeleaje?”

“Naendelea vizuri kabisa.”

“Baba yako amekuwa mpweke sana hivi unajua anavyotamani kupata mjukuu?

Nilitikisa kichwa kukataa, alianzisha mada hii mapema sana angalau angeniacha nipumzike kidogo nilihitaji sababu ya kubadili mada lakini sikupata.

“Nilipomuaga nakuja kwako akaniambia nije kukuuliza kama una mtoto unayemficha nimpeleke akamuone.”

“Lakini mzee haliziki kabisa si tayari anawajukuu kutoka kwa dada,”

“Ni tofauti na watakaotoka kwako, kwanini unasahau wewe ni mtoto pekee wa kiume tuliyenae.”

“Mama sina mtoto yoyote na kama angekuwepo sina sababu ya kumficha"

“Dankan mwanangu, mpaka lini utaishi maisha ya upweke namna hii?”

“Mimi sio mpweke mama, na sitaki kuona unahuzunika na kwenda kubadili nguo kisha ntarudi kukusaidia.” Alitikisa kichwa kukubali huku akiendelea kuchambua mchele.

Nilikwenda chumani kwangu nikavua nguo kisha nikaingia bafuni kuoga ili kutoa uchovu wa siku nzima baada ya kazi. Maji yalipokuwa yanateremka kwenye mwili wangu nilikuwa nikitafakari maneno ya mama.

Baada ya kuvaa nguo nikarudi jikoni. Nikachukua matunda kwenye jokofu ili kuyaandaa. Nilikuwa natafuta mada ya kuanzisha ili asigusie kile ambacho sikutaka kusikia, bahati mbaya nilichelewa yeye akawa wa kwanza kuzungumza

“Kwanini uliacha kwenda kwa Daktari wako?” aliuliza bila kunitazama machoni.

Aliendelea kuangalia kile alichokuwa anapika lakini nilifahamu umakini wote ulikuwa kwangu. Nilitakiwa nitafute namna nzuri ya kumdanganya.

Bimkubwa ameshafanya juhudi nyingi sana baada ya kujua tatizo langu.Alinikutanisha na mtaalamu wa saikolojia akanieleza mambo mengi na kubwa alilotaka nifanye ili nirudi kwenye hali yangu ya kawaida. Eti niruhusu moyo wangu kupenda tena. Mapenzi yale yale nisiyotaka hata kuyasikia si kuweza Kukubaliana nae, kupenda kwangu ni kama kukubali maumivu na mateso. Huo ukawa mwisho wa kwenda kwenye matibabu hayo.

“Niko sawa mama sina tatizo tena, ntaoa muda ukifika.”

“Unaongea kama kijana mdogo, ngoja nikukumbushe unamiaka thelathini na tatu huna hata mtoto. Sawa ni maisha yako lakini ni lini utakuwa na familia yako? Hauwezi kuishi hivi maisha yako yote tunapokwambia uoe ni kwa faida yako.”

“Sawa mama ntaoa mwaka huu kama mtakavyo,” sikutaka kwendelea kubishana nae tena.

Aliacha alichokuwa anafanya alionekana kuumizwa na hali yangu yakushidwa kupenda tena lakini aliamini ntakua sawa kama ntapata mwenza. Mama akasogea nilipo akanishika mikono yangu na kunitazama.

“D mwanangu, haya ni maisha yako hakuna anaekulazimisha kuoa. Je, nimakosa kwa mzazi kutamani kushuhudia kijana wake akioa kabla hajamaliza muda wake hapa duniani?”

“Mama...” Nilimuita kinyonge hakuniruhusu niendelee kuzungumza akaongeza neno.

“Basi niweke wazi kama bado unampenda yule mwanamke?” Mama aliuliza kiugwana kabisa lakini niliweza kuiona hasira machoni mwake.

Swali lake lilinishangaza nilijua wazi anamuongelea Lucy nami nilitakiwa kumhakikishia jambo, na mimi nikamtazama bila kupepesa macho yangu.

“Unanifahamu vizuri mama, hivi ukiniangalia unaona bado naweza hata kumkumbuka yule mwanamke?” Mama alitikisa kichwa kukataa. “Basi na wewe jitahidi ufanye hivyo,” baada ya kumwambia hivyo niliona tabasamu jepesi usoni mwake angalau alianza kuipata amani.


Mama alimchukia Lucy zaidi yangu. Huwezi kuamini yule mzee aliyemuoa Lucy alikuwa baba yake mzazi.

Ndio! usijifanye hujaelewa. namaanisha Lucy aliolewa na babu yangu.

Kuna wakati tunaowapenda ndio wanaongoza kutuumiza. Lucy alivuruga maisha yangu na hakuishia kunidhalilisha peke yangu hii ilihusu familia yangu. Na kama ningeandika hadithi basi ingesisimua wengi hata kwa chapter yake tu ingesomeka

‘mchumba wangu mtarajiwa kuolewa na babu yangu’

Tulikuwa kwenye mahusiano zaidi ya miaka miwili lakini sikujua kama anatamaa kiasi hicho. Babu yangu alikuwa Mzee na dhaifu sana alikuwa mgonjwa wa moyo na kisukari, nauhakika hakuwa na uwezo wa kumburudisha kitandani hiyo haitoshi kusema alifata mali zake? Na kwa bahati mbaya hakufanikiwa baada ya mama na ndugu zake kuingilia kati. Hata kabla ya babu kufariki alikwisha kimbia na sikujua alikwenda wapi hiyo sio biashara yangu kwanini nijue?

Niliendelea kuandaa matunda kwa ajili ya juice, wakati mama akiniuliza kuhusu maendeleo ya ofisi yangu. Stori zilikatishwa na kelele za mlango ukigongwa.

“Ulitarajia kupata mgeni leo?”

“Ndiyo. Atakuwa Stella,” nilisema kwa shauku nikifuta mikono yangu kwenye kitaulo kidogo.

“Umeniahidi utaoa lakini bado hujaacha tabia yako.”

“Sio hivyo mama. Stella ni mfanyakazi wangu.”

“Sasa mfanyakazi wako amefata nini nyumbani kwako tena usiku?"

“Tutaongea badae, unachotakiwa kufahamu ataishi hapa,” nilisema nikitoka jikoni, bila shaka nilimuacha na maswali ambayo ningemjibu baadae.

Nilitoka haraka nikaenda kumfungulia.

Stella alikuwa ni mmoja wa wafanyakazi wangu. Nimefanyanae kazi zaidi ya mwaka. kwangu ni mfanyakazi bora anajituma na ninaiona bidii yake nani mwenye kuaminika. Utofauti wake na mabinti wengine niliyowahi kuwaajiri yeye anajiheshimu.

Ni mrefu wastani na mnene kiasi hakuwa na mambo mengi alilizika na uzuri wa asili aliyobarikiwa hata nywele zake natural mara nyingi alizibana kidoti.

Unajiuliza kama nimewahi kuvutiwa nae? jibu ni ndiyo! lakini sitaki kuchukua hatua yoyote kwa sababu najua matokeo yake, na siko tayari kumpoteza mfanyakazi mwaminifu kama yeye.


STELLA

Ilikuwa mida ya saa tatu usiku nilipofika nyumbani kwa bosi wangu. Ilikuwa maeneo ya Nyakato.

“Waooh pazuri sana…” Nilishangazwa na muonekano wa nyumba yake sikuwahi kufika hapa kabla.. alisema kweli nyumba yake sio kubwa lakini ilivutia kila kona. Bosi wangu alikuwa mbunifu sana nje kulikuwa na bustani ndogo ya maua yenye rangi za kuvutia. Na ndani thamani zake na stika ukutani zilionekana za gharama na zilikuwa kwenye mpangilio mzuri. Kama ningekuwa simfahamu ningeamini amewahi kuoa na mkono wa mwanamke umehusika kufanya yote haya.

Nilijitahidi kuficha mshangao niliyopata ili nisionekane mshamba. Baada ya kunikaribisha ndani nilipoteza amani yangu aliponitambulisha kwa mama yake.

Jamani, mama yake tena? Mie nilidhani anaishi peke yake sijui nilitegemea nini?

Alikuwa mwanamke wa makamo kiasi, niligundua bosi wangu amefanana sana na mama yake naliona hilo kila akitabasamu.

Sikuwa na vitu vingi Dankan alinisaidia na hatukutumia muda mrefu tukawa tumemaliza kuingiza vyote.


Nikiwa chumbani natoa vitu kwenye box na kuvipanga, bosi wangu alikuwa akimalizia kufunga kitanda akaweka godoro na kujirusha juu yake kukijaribu kama kipo sawa. nilihisi ajabu kidogo bosi wangu juu ya kitandani changu mawazo ya kijinga yalipita kichwani mwangu, alinitazama tukakutanisha macho, niliona aibu nikageuza shingo yangu haraka.

Na uhakika ameniona asije tu kuropoka na kuniuliza kwanini nilikuwa namwangalia. Zilipita sekunde kimya ‘nashukuru hakusema kitu’ nikashusha pumzi na ili kupotezea nikamtupia swali.

“Mbona hukunifahamisha kama unaishi na mama yako?”

“Ungependa tuishi peke yetu?” alinijibu kwa swali huku akitabasamu.

Niliona aibu, huyu mwanaume alijua namna ya kuivuruga akili yangu, najuta kumuuliza ni bora ningekaa kimya.

Na hakutakiwa kutabasamu vile mbele yangu hajui ni kiasi gani tabasamu lake linavyonipa shida.

“Sizani kama amependa mimi kuwa hapa?” nilisema

“Hapa ni nyumbani kwangu hakuna wakunipangia nani nimkaribishe kuwa na amani hata hivyo amekuja leo na ataondoka hivi karibuni. Usimuogope ni mtu mzuri.”

Nadhani alinijibu maswali yangu yote na kunitoa hofu.

“Kumbe na wewe unapenda kusoma vitabu?” aliuliza baada ya kuona box nililokuwa nimepanga vitabu vyangu, hakusita kuanza kuvikagua.

“Nadhani hatufahamiani vizuri,” nilisema nikimaanisha hajui chochote hata namna anavyoutesa moyo wangu.

“Bila shaka ntakufahamu vizuri muda si mrefu,” nilinyanyua uso wangu kumtazama baada ya kusikia vile nikamkuta ameshika albamu yenye picha zangu. Tena kulikuwa na kumbukumbu za tangu utotoni ambazo sikuwahi kuzipenda.

“Dankan usiangalie na kuomba,” sikutaka azione picha za utoto wangu sikupenda namna nilivyokuwa nilinyanyuka haraka nikamfata nikitaka kumnyang’anya asizione.

Dankan alikuwa mjanja alijua nachotaka, akanyanyuka haraka na kuanza kunikwepa. Tulianza kukimbizana mule ndani kama watoto wakigombania toy. Saa ngapi Dankan asifungue mlango na kutoka hadi sebuleni.

Angekuwa mtu mwingine ningemwacha azione lakini sio Dan na dharau zake najua atanitania na itachukua week kusahau hili.

“Namna unavyonifuata ndivyo unaniongezea shauku ya kutaka kuona zaidi.” Alisema akiendelea kutembea kinyume nyume wakati ananitazama alikaribia ukutani.

“Tafadhali usifanye hivyo,” nilimuomba nikiwa bado namfata mpaka nilipo mbananisha kwenye konanilikuwa mfupi kwake na bado alinyoosha mkono uliyokuwa na albamu hivyo nikaanza kuruka ili kuichukua.

Wakati naruka kwa bahati mbaya nikawa nimemshika kifuani ili kupata balance, niliona akinitazama kwa namna ambayo alinishangaza nikatoa haraka mikono yangu. ghafla akanishika kiuno kwa mkono mmoja huku mwingine ukiwa bado juu, akanivuta karibu yake kiasi cha kusikia namna alivyopumua hata mimi mapigo ya moyo yangu yakabadilika yalipiga kwa nguvu sana, macho yetu yakagongana ukimya ukatawala kwa sekunde kadhaa sijui nilipatwa na nini? sikuweza hata kusogeza miguu yangu.

Wakati hisia zikitawala na kuchukua akili zetu. Dankanaling’ata mdomo wake wa chini kwa namna ya kutamani kufanya jambo flani, taratibu akaanza kusogeza uso wake kwangu. Ni kama nilikuwa nimepigwa ganzi nilitumbua macho yangu nisiamini kile anachotaka kufanya.

“Paah…”

Ilikuwa sauti ya sahani iliyobamizwa mezani wakati mama yake anaandaa chakula, bila shaka alifanya makusudi. Nilistuka nakutoa mkono wa Dankan aliyekuwa bado amekamata kiuno changu nikamsukuma ukutani.

Nikafanikiwa kuchukua albam nakukimbilia chumbani kwa aibu.



DANKAN

Jaribio langu la kumbusu Stella halikukamilika lakini hisia nilizopata zilinifurahisha. Wakati nasogea kwenye meza ya chakula nilitoa simu kwenye mfuko wa suruali yangu nikaandika ujumbe mfupi na kumtumia Stella. Nikasogeza kiti na kukaa. Sikuweza kuficha tabasamu langu nikachukua sahani na kuanza kupakua chakulamuda wote mama alikuwa akinitazama.

“Mmhmm….” Niliguna baada ya kuweka kijiko cha chakula mdomoni na kuanza kutafuna. “Hujawahi kukosea siku zote chakula chako ni kitamu sana mama angu” nilisema baada ya kumeza.

“Sina uhakika kama chakula kimekufurahisha zaidi ya kile ulichotaka kukifanya na mfanyakazi wako.”

“Sijafanya chochote… angalau ungesubiri mpaka mwisho, kuliko kujaribu kuvunja sahani yangu.”

“Utaoa hivi karibuni ningependa uwe makini na kupunguza hayo mambo yako.”

“Ona sasa umefanya aogope hata kuja kula, nakuomba usimfanye akakose amani,” nilisema baada ya kusoma ujumbe aliotuma kwenye simu yangu.


“Kama kweli angekuwa na aibu asingekuja kuishi na bosi wake akijua kabisa ni mseja,” mama alionyesha kutofurahishwa na uwepo wa Stella na labda kile kitendo kilichochea zaidi.

“Haujui chochote kuhusu yeye hivyo acha kuhukumu.”

Nilisema nikiendelea kuchat na Stella tabasamu halikuisha kwenye pembe za midomo yangu kila nilipopokea ujumbe.

“Huyo binti bado mdogo na….”

“Ana miaka ishirini na nne,” nilimkatisha

“Usiniambie ndiye utakaye muoa?” alisema kwa sauti ya ukali, “Anaonekana hajatulia kabisa na wala hamuendani,” alisema kunikatisha tamaa utazani nilimwonyesha dalili za kumuoa mfanyakazi wangu.

“Umefika mbali sana mama, sijafikilia bado nani wakumuoa.”

Ukimya ukatawala nilikuwa bado na chat na mama anaendelea kula huku ananitazama, nadhani alikuwa anatafakari jambo najua punde tu atanieleza huyu mwanamke hajui kukaa na kitu moyoni.

“Mara ya mwisho umewasiliana lini na Reyna?” hatimae alisema la moyoni nilijua huyo ndiye binti pekee alitamani nimuoe.

“Mmh mwezi mmoja uliopita. Nilimpongeza baada ya kushida kesi yake ya kwanza. Unajua ameanza kufanya kazi kama mwanasheria,”

“Nilijua tu atafanikisha malengo yake ni binti mwelevu sana. Na unafahamu anavyokupenda nadhani ni mwanamke sahihi unayepaswa kumuoa.”

Reyna ni binti wa aliyekuwa bosi wake wa zamani. Namzidi mwaka mmoja ni mwanamke msomi na mrembo sana. kweli Reyna alinipenda sana ni moja ya wanawake niliyowahi kuwaumiza kwa matendo yangu. Alipambana sana kunibadilisha lakini hakufanikiwa nilidhani angekata tamaa baada ya kwenda kusoma nje ya nchi. Lakini ikawa tofauti hata akiwa huko tuliendelea kuwasiliana bado nilimchukulia kama rafiki na sikuwahi kumpa matumaini ya kuwa kwenye mahusiano naye. sikutaka kumuumiza zaidi na kumpoteza rafiki yangu.

Lakini baada ya kurudi amekuwa tofauti hanitafuti mara kwa mara kama zamani sizani kama ubize ndiyo sababu au amependana na mtu mwingine? Nachoshukuru ni kuepukana na malalamiko yake kuhusu tabia yangu.

Mama anampenda sana Rey, alipolitaja jina lake tu nilijua alichotaka kuongelea.

“Baada ya muda wote huo sizani kama bado atakuwa na hisia na mimi, huenda tayari anampenzi,” nikamdokeza.

“Rey sio mtu wakuficha mahusiano yake, kama ingekuwa hivyo mama yake angeniambia. Unabahati mwanangu angalau yupo mwanamke mzuri anayekusubiri.” Alisema akichukua jagi la juice na kujimiminia kwenye glass.

Nilimtazama mama alionekana mtu aliyekwisha dhamilia na alitaka tu kusikia uthibitisho kutoka kwangu na sio vinginevyo.


STELLA

Nikiwa chumbani kwangu nilikuwa nikizunguka kama mwendawazimu, hakuna nilichoweza kufanya kila nikikumbuka kilichotokea nilijitahidi kuvuta pumzi na kuishusha kutuliza presha yangu.

‘Umefanya nini Stella…’ nilisema nikijipiga piga mashavuni.

Huu ni mwanzo mbaya sana ni siku ya kwanza lakini tayari nimeonyesha udhaifu wangu. Jana nilikuwa na pesa ambayo nilitaka kuongezea ili kulipa kodi lakini nilimtumia Enock kwa ajili ya mitihani, ntafanya nini sasa? na pesa niliyobakinayo ni ndogo.

Nilikuwa kwenye dibwi la mawazo nikamkumbuka rafiki yangu aliyenisisitiza nirudi kuishi nyumbani kwao. Nikachukua simu na kutafuta jina la Happy. nikampigia baada ya kulipata nilitaka kumweleza kilicho nikuta najua angenilaumu lakini angenisaidia namna ya kukabiliana na aibu niliyokuwa nayo. Sikuwa na mtu mwingine wa kumweleza hali yangu. Simu yake iliita bila kupokelewa, nilijua atakuwa bize na mtoto mara kadhaa amenieleza namna anavyomsumbua usiku. Nikaweka simu pembeni nikiamini atanitafuta.

Sauti ya ujumbe mfupi ilisikika kwenye simu yangu haraka nikaichukua kuifungua.

<Boss Dan> Hey, we dogo njoo ule, sintajaribu kukung’ata tena.

Maneno yale yalifanya joto lipande mwilini.

Hana wasiwasi kabisa sijui kapata wapi nguvu za kunitania baada ya kile alichotaka kufanya…

Lakini kwanini na mimi nilielekea kukubali? Bila shaka mama yake atatafsiri vibaya, hii hali inanivuruga naelekea kuwa kichaa,

Nilikuwa najilaumu mwenyewe nadhani kuishi hapa haita kuwa rahisi kama nilivyodhani.

<Mimi> Mama yako kasema nini?

Hatimae nikamtumia ujumbe, hakuchelewa kurudisha.

<Boss Dan> Kasema uje tuendelee tulipoishia.

What.. nilishtuka nikakaa vizuri kitandani nikitafuta jibu la kumpa


<Mimi> Jaribu kuwa siriuos.

<Boss D> Kwanini sasa, inamaana wewe hutaki?

<Mimi> Kutaka nini?

<Boss D> Kumalizia tulichoanzisha.


Huyu mpuuzi ndo anazidi kunichanganya.

Ni kweli bosi wangu nimcheshi sana lakini haya mazoea yaliyoanza baada ya kuhamia hapa sizani kama yatakuwa na mwisho mzuri.


<Mimi> Samahani bosi hilo halikupaswa kutokea.

<Boss Dan> Usijali dogo nakutania utatoka kwa muda wako, hakikisha unakula vizuri.

Nilijikuta natabasamu nikatoka sehemu ya ujumbe. Nikanyanyuka kitandani nikajitengeneza vizuri.

‘Siwezi kukaa humu ndani milele lazima nitoke, natakiwa niwe kawaida kama hakuna kilicho tokea hata hivyo hakufanya chochote.’

Nilitabasamu baada ya kukumbuka namna alivyonishika kiuno changu nilipata msisimko wa ajabu. Nimewahi kuwa kwenye mahusiano lakini sikuwahi kupata hisia za namna hii niliposhikwa.

Nadhani itakuwa ngumu kwendelea kuficha hisia zangu nahisi malazi ya moyo yataniumbua mwenzenu.


Nilishindwa kutoka, nikarudi kukaa kitandani nikachukua moja ya kitabu changu nikafunua mahali nilipoishia nikaanza kusoma. Nilihitaji kupoteza muda kidogo ili nitoke tena labda watakuwa wameshaingia vyumbani mwao kulala.

Sijui nilisinzia muda gani? nikashtuka saa kumi na moja alfajili baada ya kuangalia muda kwenye simu yangu. hata majogoo yalikuwa hayajaanza kuwika. Nilikuwa na njaa sana, nikaamka kitandani nikijinyoosha.

Ni siku mpya nikiwa ndani ya nyumba ya bosi wangu.
Baada ya kutandika kitanda na kusafisha uso na meno yangu nikatoka mpaka sebuleni ambapo nilikuta chakula mezani nikatabasamu baada ya kukifunua.

“Waooh kumbe kweli niliachiwa chakula,” ulikuwa wali na rosti ya kuku kilionekana kitamu kabla sijaweka mdomoni.

Mwanamke anapaswa kuwa mgeni siku ya kwanza tu, hili alinifundisha mama yangu nikabeba vyombo na kupeleka jikoni. nilitakiwa nifanye usafi haraka niende kazini kabla hawajaamka.

Nilimaliza kufanya usafi nikachemsha chai na kile chakula cha jana. Kula kipolo kwangu sio tatizo siku zote hasili ya mtu haijifichi.

Tatizo lilitokea wakati nakula nilipaliwa na chakula baada ya kumuona mama Dankan akiingia jikoni.


Mungu wangu… amefata nini jikoni mapema yote hii? kwanini aamke muda huu jamani? Maswali mfululizo yalipita kichwani kwangu.

Kitu ambacho sikutegemea kikatokea. Akanipatia maji ya kunywa nikapokea nikanywa baada ya kumeza nikashusha pumzi huku kijasho chembamba kikinitoka. Ile hali ya kukohoa ikaisha, alikuwa bado ananitazama nikamshukuru.

“Usijali unatakiwa kuwa makini, wakati mwingine usile chakula kilicholala kuna mikate na mayai unaweza kutengeneza.” Alisema wakati anasogea kuchukua jagi la kuchemshia maji.

Aisee… hawa watu tabia zao zinafanana wanafanya nijisikie aibu muda wote. Sasa kupaliwa kunahusiana nini na kiporo? Yeye nd’o sababu.

“Jana sikuweza kula baada ya kupitiwa na usingizi, ndio maana nikaona haipendezi kukimwaga, hata hivyo bado kizuri.” Nilijitetea kwa uchangamfu sana nikiamini atanielewa.

“Kwanini uko hapa binti?” aliniuliza akinitazama bila shaka alisubiri kwa hamu jibu ntakalompa.

Nilishtuka baada ya kusikia lile swali, “Nii..kwasa..babu..” sijui kilitoka wapi kigugumizi cha ghafla kilinivamia.

“Nakuelewa, haina haja kujielezea,” alinikatisha baada ya kuona napata shida kujibu swali lake.

“Umefanya kazi kwake kwa muda gani?”

“Mwaka mmoja mpaka sasa,” nilijibu kwa utulivu.

“Inamaanisha unamjua vizuri bosi wako?”

Swali lake lilinichanganya nikabaki namtazama kwa mshangao alitaka kusema nini huyu mwanamke?

“Nimependa ujasiri wako,” alisema akimimina maji ya moto kwenye kikombe.

“Sijakuelewa?” haya mazungumzo yalianza kuninyima amani nilikuwa natamani kuondoka.

“Huelewi nini binti? Unataka niseme kitakacho kukuta baada ya kutumika na bosi wako?” alisema kwa sauti ya chini lakini ya kuonya.

“Ha..hapana, sio hivyo.” sauti inakauka.

“Kama tatizo ni pesa…” alisita kwendelea akaingiza mkono kwenye mfuko wa suruali aliyokuwa kavaa akatoa kiasi cha pesa, sikujua ni shilingi ngapi lakini ilikuwa nyingi nadhani ilizidi laki moja, akanyoosha mkono kunipatia,

“Nadhani itakusaidia kuliko kupoteza muda ukijaribu kumvutia bosi wako atakaye kuacha baada ya usiku mmoja tu.”

Nimewahi kuyaona matukio mengi kama haya kwenye muvi na tamthilia na siku zote nilimlaumu sana muhusika kukataa pesa na kufanya maamuzi ya niliyohisi ya kijinga. Nadhani leo ni zamu yangu nilaumu utakavyo. Ni kweli nazihitaji sana lakini sikuwahi kutumia mwili wangu ili kuzipata. Kuna hela za moto jamani…. kwa maneno ya huyu mwanamke kupokea ile pesa maana yake nikuthibitisha alichosema ni kweli.

Maumivu niliyosikia moyoni ni kama kiwembe butu kina kwangua. Niling’ata mdomo wangu kwa ndani nikizuia machozi nayo yasipate nafasi ya kuniaibisha. Miguu yangu nayo ilinisaliti nilipogeuka kuondoka, ilikuwa ikitetemeka sana nilijikaza na kupiga hatua zisizo eleweka, nilipanga kulia nitakapofika chumbani kwangu.

Ndicho nilichofanya baada ya kuingia na kufunga mlango nikasogea karibu na kitanda nikakaa chini huku kichwa na mikono vikiinama kitandani nilishidwa kuzuia machozi. nililia hata nisijue kinachoniliza kama ni maneno ya huyo mwanamke au uamuzi wangu wa kijinga kuhamia kwa bosi wangu.

Mama Dankan alikuwa sahihi baada ya lile tukio la jana.

Nina sababu ya kuwa hapa na sikuhitaji pesa kutoka kwa bosi wangu. Hata hivyo Dankan ni mwanaume mbahili kuwahi kumjua, ni kweli amekuwa mwema kwangu na amenisaidia mara nyingi lakini kila aliponikopesha nilirudisha pesa yote na hakusita kupokea. zaidi alichofanya kunipoza baada ya kugawana mshahara wangu nikuninunulia chakula.

Huyo nd’o Dankan bila shaka utakubaliana na mimi hakuwa na sifa ya kuitwa Danga.

Ni kweli nampenda bosi wangu lakini sio kwa sababu ananisaidia. hapana, ni kwa sababu uwepo wake unanipa hisia ambazo sikuwahi kuzipata, bahati mbaya nafahamu hatuwezi kuwa pamoja.


Kila chenye mwanzo hakikosi kuwa na mwisho, siwezi kulia milele nikanyanyuka na kuelekea bafuni. Nilioga kisha nikajiandaa kwenda kazini.

Nilipofika ofisini nikafanya usafi na baada ya hapo nikaanza na kazi niliyobakiza jana.

Masaa mawili badae karibu wafanya kazi wote walikuwa wameshafika na bosi pia, nilipanga kuwa serious atakapo nisemesha lakini alinipita kwa kasi akinisalimia kwa mkono tu, sikutegemea yeye ndio awe serious vile.

Ilipofika saa sita kasoro nilikuwa napanga picha za harusi kwenye albam kwa mtililiko wa matukio. Wazo la kuhama lilininyima raha lakini nisingeweza kuishi hapo tena. Nilitamani muda wa lunch ufike haraka nikaonane na Happy nilipanga kumwambia kila kitu nikiamini ntapata nafuu.

Nilipokuwa naendelea na kazi kuna mwanamke alitoka ofisini kwa bosi alikuwa mwanamitindo alikuja pale kwa ajili ya picha za mavazi anayotangaza. Akapita kwa mwendo wa madaha huku akitabasamu, na mimi nikatabasamu kinafki alipotoka nikapindisha mdomo pembeni.

“Anajikuta nani huyu? Miss world au kitu gani? Hata hanishtui nimeshaona wengi kama yeye,”

Haikupita hata dakika moja bosi nae akatoka, nilikuwa mwenye mawazo lakini hayakuzuia macho yangu kuona namna bosi wangu alivyopendeza leo. Huyu mtu nikimuona hata macho yananisaliti kabisa. Akasogea kwenye meza yangu nikavunga niko bize sitaki hata kumwangalia.

“Muda wa lunch umekaribia unaonaje tukale pamoja?” alisema akiweka mikono juu ya meza huku akinitazama.

“Hapana nashukuru..” nilijibu haraka sikutaka kutafakari mara mbili.

“Unaonekana hauko sawa kuna tatizo?”

“Hakuna tatizo nimepanga kwenda sehemu,”

“Wapi?”

“Haikuhusu,”

“Nimeuliza tu kama kaka anayejali, sasa hasira za nini?”

Alifanya nione aibu nikaima kwendelea na kazi “Kwanini unajali. hiyo lunch ulitakiwa ukale na yule model,” baada ya kuropoka nikamtazama usoni nilidhani atakasirika lakini akatabasamu

“Stella, unawivu?”

“Kwanini niwe na wivu?” nilitoa macho kama sijaelewa.

“Ok sawa kuwa makini huko uendako”

Akageuka na kuondoka wala hakujisumba kunibembeleza tena bila shaka ningekubali. Ona sasa jeuri yangu imenifanya nipoteze ofa.

Alikuwa sahihi ulikuwa wivu na hasira pia. Nakumbuka muda mchache uliopita wakati nampelekea lisiti za malipo ya umeme ofisini kwake. Nilimkuta yule model amemkalia mapajani na yeye akimpapasa huku wanazungumza kimahaba na sasa anataka kutoka na mimi kweli inakera sana nimefanya maamuzi sahihi kukaa karibu na mchafu lazima utanuka tu.

Muda wa lunch nilikwenda dukani kwa Happy hapa kuwa mbali na ofisini.

Happy ni rafiki mwema niliyebahatika kuwa naye maishani mwangu. Kama nilivyowaambia awali alikuwa hapendi unafki kabisa hiyo ilimfanya kuwa na marafiki wachache sana. Aliamini kwenye mapenzi ya kweli alitaka mwanaume atakaye mpenda kwa dhati bila kumuongopea. Najua kila mwanamke anapenda hivyo lakini yeye alimaanisha,

‘Pasipo uaminifu hakuna mapenzi’

Hata aliyekuwa mume wake alijifanya mwema mwanzoni lakini baada ya ndoa akaonyesha makucha yake. Ndoa yao ilidumu ndani ya mwaka mmoja tu. Happy alikuwa mtu wa ajabu sana alipogundua mumewe anamsariti lile kosa lilivunja ndoa yake bila kujali ujauzito wake, hakujali hilo sembuse watu watasema nini? hakuiamini ile kauli ya ‘cha peke yako kaburi’

Baada ya kurudi kwao akaendelea na ile biashara ya steshenari. Alipata flemu karibu na ofisi yetu na biashara iIienda vizuri.

Nilipofika dukani kwake nilimkuta na mfanyakazi wake na mtoto wake Criff mwenye miezi mitatu, aliyekuwa anamlisha chakula. Baada ya kusalimiana nikakaa nje sehemu ya viti vya wateja nae akanifuata akiwa na mwanae.

“Jana wakati unapiga simu nilikuwa hoi nimelala eeh niambia kuna jipya gani?”

“Nimehamia kwa Dankani...."

“Nini....Siamini kama umefanya hivyo!” alishangaa huku akinitazama kama mtu wa ajabu.

Tuna umri sawa lakini Happy tangu alipoolewa na kupata mtoto ananiona kama mdogo wake. Sikuwa na namna nikamwelezea kilichotokea kwa binamu yake,

“Happy nimefanya hivi sio kwa sababu nataka kuwa mpenzi wake. Nahitaji kusave pesa unajua Enock anahitaji kwa ajili ya mitihani nielewe, na kitu kingine ni kwamba napenda tu kuwa karibu yake,” nilisema kauli yangu ya mwisho nikitabasamu.

“Kwahiyo umefurahi baada ya kilichotokea? Hivi unafikiri utaweza kumshawishi akupende?”

“Nimekosa amani kabisa na siwezi kumkaidi shangazi yako itabidi nihame haraka,” nilisema kinyonge.

”Nilikwambia urudi nyumbani ukakataa, sasa angalia kutosikiliza kwako kulipokufikisha siku zote mwana kulitafuta mwana kulipata.”

Happy alitaka nirudi kwao tena baada ya yeye kurudi. hapana siwezi tutaonekana waajabu sana. Natamani ningekuwa kama Happy asiyejali nani atasema nini.

“Bado una ile namba ya dalali? nataka anitafutie chumba maeneo ya karibu,” nilimwambia wakati nachezea simu yangu.

“Unatafuta chumba… wakati ungependa kwendelea kuishi nyumbani kwake,” alisema akinitazama alikuwa sahihi lakini sikuwa na njia nyingine.

“Unanishangaza hivi unawezaje kumpenda huyo mwanaume wakati unajua atakuumiza?”

“Happy, huu ni upendo na nimeshindwa kuzuia hizi hisia, niambie kama kuna kitufe cha kubonyeza ili nimalize haya?”

Happy alihisi nimechanganyikiwa hakutaka kunielewa kabisa, akanyanyuka na kuingia dukani na aliporejea alikuwa na kikapu mkononi. Wakati huo nilikuwa namuendesha Criff wake kwenye babywalker huku namuongelesha kitoto.

“Niambie kuhusu Lucas mmewasiliana?” Happy alianzisha maongeza tofauti na yale.

“Kwanini tuwasiliane?”

“Stella shoga angu unachezea shilingi chooni, yani Yule kaka anavyokupenda, anakujali na alivyompole unatakanini tena?”

“Happy hivi ulishawahi kupenda kweli wewe? Sijakataa Lucas anasifa zote za mwanaume rijali lakini sina hisia nae sasa kwanini ni mdanganye?”

“Hukuwahi kumpa nafasi hata ya kuhuge, utajuaje kama huna hisia nae?”

Nilitabasamu nikagundua Happy bado hajawahi kuzama kwenye bahari ya mapenzi, nadhani kwake mapenzi ni mazoea tu.

“Naweza kupata hisia na Dan hata akiwa mbali na mimi, ninaposikia sauti yake au hata nikihisi harufu ya marashi yake moyo wangu unadunda kwa speed hata nikimfikilia tu”

Happy alinishangaa.. “Lazima utakuwa na njaa nawa tule,” alisema wakati anafungua hotpot ya chakula aliyotoa kwenye kikapu.

Ni kweli nilikuwa na njaa na nilipanga kula sambusa na juice ninazouza pale ofisini, ningeweza kukataa kama angekuwa mtu mwingine lakini sio Happy. Nikanawa mikono na kuanza kula huku stori zikiendelea Criff alikuwa anatabasamu na kucheka kila nilipomwangalia kwa kumkonyeza na kumchezea miguu yake, kwake ulikuwa mchezo wa kufurahisha.

“Criff mwanangu achana na Stella hakufai mwali gani anaamka na kula viporo asubuhi asubuhi…” Happy alisema kwa utani akikumbushia stori niliyompa nakufanya wote tucheke.


DANKAN

Ilikuwa majira ya saa nne usiku. siku ya leo nilikuwa na kazi nyingi ofisini nilitamani kumpa lift Stella lakini aliondoka mapema baada ya kazi zake kuisha. Stella anajitahidi sana kunikwepa, lakini hawezi kuficha tena tunaishi nyumba moja, kwani vina muda basi.. atajisalimisha mwenyewe.

Nilikuwa kwenye gari naendesha kuelekea nyumbani. Natabasamu kila nikimfikilia namna anavyojifanya havutiwi na mimi.

Nilipofika nyumbani, kama kawaida mama yangu alikuwa amepamba meza kwa vyakula vizuri nadhani hii nd’o sababu naweza kumvumilia huyu mwanamke tofauti na hapo ningemwambia arudi kwa mumewe haraka.

Wakati namsalimia mama nilisikia sauti ya binti jikoni nilimuuliza ni nani kwa sababu nilitambua haikuwa sauti ya Stella.

“Otea anaweza kuwa nani?” mama aliongea kwa uchangamfu sana.

Kabla sijatafakari nilimuona Rey akitokea jikoni.

“Mashalaa unazidi kuwa mrembo,” nilimwambia

Rey alinikimbilia na kunikumbatia kwa nguvu kidogo tudondoke huku akinimiminia mabusu, kwa mbali nilimuona Stella akitoka msalani ni kama hakujali maana alipita kwa kasi akielekea chumbani kwake.

Nyumba yangu inavyumba vitatu vya kulala na viwili vinamaliwato kwa ndani lakini chumba nilichompa Stella aishi hakikuwa hivyo. Nilifanya makusudi niliwaza mbali sana namna ntakavyopata burudani ya kutazama makalio yake kila akitoka kuoga. Lakini Stella alikuwa na pigo za kienyeji sana alijua kujistili mpaka wakati wa kwenda kuoga. Lakini hilo halinisumbua nimegundua anavutiwa na mimi ntampata kwa vyovyote.

Hata sijui nini kimenipata tangu amehamia hapa akili na mwili wangu vinamzingatia sana, si kuwa hivi kabla yeye sio aina ya mwanamke nayetamani aniburudishe. Sijui nini kinaendelea kwenye ubongo wangu hii tamaa imevuka viwango.

“Nilikumiss sana rafiki yangu,”

“Mimi pia Rey, niambie kazi zinaendaje?”

Tuliendelea na stori. Wakati mawazo yangu yapo kwa Stella nataka atoke nimuone atakavyopata shida kunitazama nikiwa na mwanamke.

Rey alikuwa mchangamfu na muongeaji sana, robo saa ilitosha kunieleza kila kitu kuhusu kazi yake, kesi zote alizowahi kushiriki tangu akiwa mwanafunzi na changamoto anazopitia.

Mama alikuwa mwenye furaha sana akituona tukiwa pamoja,

“Basi mle kwanza chakula stori zitaendelea baadae.”

Wakati Rey amechukua sahani nakuanza kupakua nikamkumbuka Stella, nikanyanyuka kwa lengo la kumfata,

“D. unakwenda wapi tena?” Rey aliuliza

“Hatuwezi kula wenyewe Stella yupo ndani,”

“Amerudi muda si mrefu atakuwa ameshakula,” mama alizungumza najua lengo lake nikunizuia lakini sikujali.

Nilitembea koridoni na hatua chache tu zilibaki kuufikia mlango wa chumba cha Stella, alikuwa hajaufunga vizuri, kabla sijagonga nikasikia sauti yake akiongea. alikuwa anazungumza na mtu kupitia simu.

Sina tabia ya kusikiliza kwa siri maongezi ya mtu lakini alichoongea Stella kilinishtua nikatega sikio na kusikiliza kwa makini labda nilisikia vibaya.

Nilishindwa kuvumilia nikaingia bila hata kubisha hodi.

“Kwanini anataka kuha…ma?”

“Mungu wangu!” nilichokiona kilinifanya nitoe macho kama mjusi kabanwa na mlango nilishidwa kugeuza shingo pembeni.

Hata kama wewe nd’o ungekuwa macho usingeweza kujizuia kutazama nilichokiona. Jamani Mungu fundi nakili sikujua kama Stella kapendelewa kiasi hiki labda kwa sababu nilizoea kumuona kwenye jinsi na matisheti makubwa.

Nina kila sababu ya kulekebisha maneno yangu. Stella ni aina ya mwanamke anayefaa kwa matumizi.

Stella alikuwa amejilaza kitandani akiwa amevaa kigauni cha kulalia chepesi chenye rangi nyekundu ilikuwa rahisi kuona namna alivyo umbika na karibu nusu ya mwili wake ilikuwa wazi na lile pozi na uhakika alifanya makusudi kabisa.

Lakini baada ya kuniona akajifanya kushtuka na kutafuta nguo ya kufunika maungo yake.

“Mtu mstarabu hugonga mlango kabla ya kuingia,” alisema wakati amejifunika upande wa khanga.

Nilikuwa bado namkodolea macho nilirudisha akili yangu baada ya kuniita zaidi ya mara moja. Nikajiweka sawa kabla ya kuuliza

“Stella kwanini unataka kuhama?”

“Nadhani sikufanya maamuzi sahihi nitahama siku si nyingi,”

“Na unatarajia ntakuruhusu uende?”

“Dan. mimi sio mtoto naweza kufanya maamuzi yangu.”

“Nimependa ulivyoniita inaonyesha kweli umekuwa,” nilisema nikimsogelea,

“Nikusaidie nini?” alisema akirudi nyuma,

“Mimi…?” eti nilisahau hata kilicho nileta ikabidi nitafakari kwanza,

“Wewe ndiyo, sizani kama hicho nd’o kilicho kuleta”

“Aaah nimekuja kukuita tukale,”

“Asante nimeshiba tayari,”

“Wewe ni sehemu ya familia yangu lazima tule pamoja ni Sheria ya nyumba hii na kuhusu kuhama usifikirie kitu kama hicho tena,”

“Sawa unaweza kwenda nataka nivae kwanza,”

“Hata hivyo umependeza,” nilimkonyeza nakumfanya ainame kwa aibu.

“Mlango upo upande huu” alinionyesha kwa kidole baada ya kuhisi sina mpango wa kutoka.

“Ni nyumba yangu lakini siwezi kukaa sehemu ninayotaka”

Nilifungua mlango nikinung’unika sikutamani kutoka sijui nilikuwa na shida gani?


STELLA

Baada ya bosi wangu kutoka chumbani kwangu nilishusha pumzi ndefu. Nampenda lakini naogopa sana kuwa karibu yake nahisi uvumilivu unaweza kunishinda nikajikuta nimefanya kosa lingine. Nilipogeuka nikatazama kitandani nikagundua simu ilikuwa bado hewani,

“Oooh Jamani Happy sio vizuri, nauhakika salio langu limeisha”

“Umefanya vizuri angalau hujajirahisisha kwake,”

“Napata wapi nguvu za kufanya hivyo baada ya kumuona akikumbatiana na mwanamke?”

“Tofauti na hapo ungemkaribisha kitandani?”

“Happy unanijua, mimi sio msichana wa aina hiyo,”

“Niahidi kile ulichofanya jana hakitajirudia tena,”

“Sawa nakuahidi dada mkubwa,” alicheka akakata simu.

Nilishusha pumzi ndefu nikakaa kitandani nakumbuka namna bosi wangu alivyokuwa akinitazama kwa matamanio, nikaanza kujitazama. “Imekuaje nikaacha mlango wazi, vipi kama angenikuta sijavaa kabisa? Na atahisi nimefanya makusudi.”

Nikanyanyuka kwenda kutafuta nguo kwenye begi langu, nilichagua gauni refu itakayostili mwili wangu sitaki matatizo zaidi.


Nilivaa kisha nikatoka mpaka sebuleni. Niliwakuta wameshaanza kula, nikasogeza kiti na kuketi kando ya mama yake. Muda wote mwanadada mgeni alinikazia macho.

Baada ya kukaa akanisalimia kwa kunipa mkono. Nikaupokea kwa tabasamu. Moyo wangu uliugulia kwa wivu, alikuwa mrembo sana na ukimtazama huwezi kujiuliza mara mbili familia aliyotoka, uvaaji wake na namna anavyozungumza vilimtambulisha moja kwa moja ni msomi.

“D. mbona umetumia muda mrefu chumbani kwa mfanyakazi wako, kuna usalama kweli?” aliuliza akitabasamu huku akijaribu kumdadisi.

kilichonishangaza hakuonekana kama anawivu, ikanifanya nipate ahueni nikaamini atakuwa rafiki tu.

Nikapakua chakula. licha ya kwamba Rey alikuwa akimpigisha stori bosi wangu, lakini muda wote macho ya Dankan yalikuwa kwangu huku anatabasamu ile hali ilifanya nikose amani kwa sababu mama yake alikuwa akitutazama najua anachukia hali hii.

Hakupenda namna mwanae anavyonitazama hatimaye akaamua kuchafua hali ya hewa.

“Kwanini msizungumzie mipango yenu ya kuvishana pete?”

Nini pete!?

Ile taarifa ilinishtua nikapaliwa na chakula, haraka nikalifikia jagi la maji lengo langu nimimine kwenye glass lakini mikono ilikuwa inatetemeka sana, nilivyokuwa na pupa hata sikuangalia vizuri glass ilikuwa na maji tayari, wakati na mimina yakajaa haraka na kumwagika mezani, wakati nahangaika kufuta na tishu niligundua wameacha kuzungumza na macho yote yananitazama mimi. Jambo ambalo sikutaka litokee sikutaka kuwa ruhusu waone jinsi nilivyokuwa na hofu.

“Samahani kwa kukatisha maongezi yenu mnaweza kwendelea,” nilijisikia vibaya najua nimeonekana kama kituko, nikajitahidi kuvunga kama sijapata mshtuko.

“Eti mpenzi ungependa ifanyikie wapi?” alisema Rey huku mkono wake mmoja ukiwa begani kwa Dani akiendelea kumpapasa mgongoni, wala hakujali mama yake anamtazama. Hawa watu ni kama wanaishi Dunia tofauti na yangu, au ndio wakishua yaani sipati picha huyu mzazi angekuwa mama yangu, lazima povu lingemtoka.

“Hilo na kuachia wewe utakapoona panafaa,” bosi alisema huku akinitazama ni kama alitaka kuhakikisha nimesikia alichosema.

Ili kumwonyesha kwamba sijali ni kawa bize na chakula, hasira yangu iliishia kwenye chakula.

Nusu saa baadaye Rey aliaga kuondoka na Dan ndiye alimpeleka nyumbani. Tukabaki wawili nilitamani kuondoka bila kutoa vyombo, lakini ingekuwa sio ustaharabu, sikutaka stori na huyu mama ingawa nauhakika yeye hawezi kunyamaza.

Nikiwa jikoni nasafisha vyombo alinifata nakuniuliza,

“Umeshapata chumba cha kupanga?”

“Ndiyo nimepata jioni na kesho naenda kukiangalia,” nilidanganya

“Nimefurahi kwa kunielewa, kama ulivyowaona Dankan na Reyna wataoana hivi karibuni,”

“Nimeona, ni jambo zuri”nilisema nikitabasamu kinafki hata yeye alijua hilo, Mambo asiyopenda Happy angekuwepo lazima angeniumbua. Nashukuru huyu hakujali akaondoka.





DANKAN

Tulipokuwa kwenye gari Rey aliniomba nimpeleke bar. tulifika bar tukaagiza vinywaji alikuwa mchangamfu kama kawaida yake. Lakini alinishangaza baada ya kuagiza Whisky na soda ya kuchanganyia alianza kunywa kwa pupa. Ni muda hatujatoka pamoja lakini najua hii sio kawaida yake, Rey alipendelea kunywa wine lazima kuna tatizo.


“D, hii pombe mbona haileweshi, kiukweli nataka kulewa”

“Rey uliyokunywa inatosha na tayari umeshalewa,” nilisema huku namnyang’anya glass, akaona nambuguzi akasogeza chupa nzima nakuifakamia.

“Chease kwa ajili yetu” alisema akinyanyua chupa juu huku ananitazama,

Alitaka tugongeshe chupa zetu, nikatabasam nikanyanyua na kugonganisha yake.

“Ni kwa ajili ya nini?” nilimuuliza

“Rasmi nimeamua kuachana na mapenzi,”

“Nini kimekukuta rafiki yangu?” nilimuuliza nikitabasamu utadhani ni habari ya kufurahisha.

“D, unajua kipindi kile nilikutafsiri vibaya lakini sasa nimekuelewa ulikuwa sahihi. tunaishi mara moja na siwezi kuishi nikiumizwa hivi ni uamuzi wa busara kufurahia maisha angali bado tupo Duniani,” aliongea na sauti yake ya kilevi

“Rey unaongelea nini?”

“Bora nikae single milele sitaki kuteseka na mapenzi, nataka kufurahia maisha”

“Unasikika kama vile umepitia mikasa mingi,”

“Ni kweli D. nimechoka hata sina muda na nguvu za kuanzisha mahusiano,”

“Sasa kwanini umemkubalia mama kuhusu ndoa?”

“Hahaha,” alicheka kilevi kabla hajanijibu,

“Unajua wazazi wangu wamekuwa wakiniuliza sana kuhusu mahusiano yangu. nimekuwa na siwategemea tena lakini wanalazimisha niolewe,”

“Na kwanini hujaolewa mpaka sasa?” Rey alitabasamu kilevi,

“Kwanini na wewe unaniuliza hivyo?"

"Nimeuliza tu hata sikulaumu".

"Kuna mpuuzi mmoja nilimpenda sana nikamwamini alikaribia kunioa, lakini sikujua kumbe muda wote ananidanganya kanichezea mwili mpaka akili yangu. yaani Yule mjinga kanipotezea muda alafu akaniacha. sasa hivi anaishi na mwanamke mwingine.” aliongea kwa uchungu akifakamia pombe.

“Basi Rey acha.... pombe uliyokunywa inatosha” nilisema nikimnyang’anya chupa.

“Mbaya zaidi huyo mwanamke aliyemuoa ukimuona,” alicheka kwa dhalau “D. sijisifii lakini yule mwanamke hanifikii kwa lolote sio elimu wala uzuri na amewahi kuolewa na hapo alipo anamtoto, kwa hiyo ex wangu analea mama na mtoto wa mwanaume mwenzie hivi unaweza kuamini?”

“Binafsi sikuwahi kuyaelewa mapenzi,”

“Mapenzi mapenzi sitaki hata kuyasikia,”

“Basi usihuzunike huyo hakuwa wako, utapata atakaye kupenda kwa dhati niamini mimi,”

“Hahaha...” alicheka kwa sauti mpaka watu waliokuwa karibu yetu pale bar wakageuka kumtazama,

“Rey unafanya nini? Umechanganyikiwa? embu nyamaza,”

Hata mimi alinishangaza muda si mrefu alikuwa mwenye huzuni sana kipi kimemfurahisha ghafla hivyo?

“…mmh..D, yani wewe ndo wakunishauri hivyo kweli? Siamini. aisee nimeanza kuamini fikra zangu.”

“Rey unaongelea nini?”

“Inaonekana rafiki yangu kipenzi amependa,” alisema kwa msisitizo

“Hakuna kitu kama hicho, ninachomaanisha wewe hutakiwi kuishi kama mimi, utaolewa na kuwa na familia yako.”

“Vipi kuhusu wewe D?”

“Kwangu inawezekana kama nikitaka mtoto naweza kuzaa na yeyote alafu nikamhudumia, lakini kwako itakuwa ngumu kulea peke yako,”

“Kwani lazima kuolewa? Sisi Waafrica sijui nani katuroga huwezi kuamini wazazi wangu hawajivunii Elimu yangu kama wanavyojivunia ndoa ya mdogo wangu. Asubuhi watanipongeza kwa kazi nzuri jioni wataniuliza ntaolewa lini nimechoshwa na kila kitu.”

“Ni kweli kabisa, ndoa imepewa heshima kubwa”

“Lakini sisi ni marafiki tunaweza kusaidiana”

“Unamaanisha nini..?”

“Tunaweza kuoana kwa ajili ya kuwafurahisha wazazi wetu alafu kila mtu akaishi maisha yake au unaonaje?”

“Rey hivi unahisi tuko kwenye filamu? haya ni maisha halisi na ndoa sio jambo la mchezo kiasi hicho. lengo la wazazi wangu nianzishe familia unajua maana yake?”

Nilitaka kumuweka sawa maana nilikuwa nauhakika ni pombe zinaongea,

“Usijali tunaweza kutengeneza filamu yetu ya kusisimua kwenye hayo maisha halisi,”

“Naona tuahilishe haya mazungumzo kwa sasa.”

Kulikuwa na mwanadada mrembo alikuwa meza ya jirani na yetu muda wote alinitazama na kutabasamu na mara kadhaa alijipitisha karibu yangu sikumjali kabisa. leo nilikuwa tofauti ni mwanamke mmoja tu aliyekuwa kwenye akili yangu na nilitamani kuwa nae. Nadhani kile nilichokiona kilinichanganya. Nataka kuwa nae najua usiku mmoja tu utatosha kumtoa akilini mwangu.

Rey pia aliona hilo licha ya kuwa amelewa.

“D, ninayemjua asingeacha fursa hii impite hivi hivi. Na uhakika rafiki yangu amependa,”

“Nani… Stella?”

“Ndiyo, ni wazi kuwa unamtaka,”

“Ni kweli na unafahamu nikishampata itachukua muda gani kumsahau.”

“Mmmh… natumai hivyo,”

“Muda umeenda hupaswi kwendelea kunywa inuka nikupeleke nyumbani,” nilisema nikisimama nilikuwa nimekunywa bia nne na bado nilikuwa fiti.

“Bado mapema sana mimi siondoki, wewe unaweza kwenda usijali kuhusu mimi kuna mtu namsubiri,”

“Siwezi kukuacha peke yako hapa nitaondoka akishafika,”

Haikuchukua muda akafika kijana mmoja kwa umri alionekana mdogo kwake, urefu wa wastani. Anaonekana anatumia muda mwingi gym akipasha misuli. aliinama karibu na Rey wakakiss, nilishangaa kwa sababu sikutegemea kama Rey anaweza kufanya hivi.

“Dulla huyu ni mume wangu mtarajiwa anaitwa Dankan huyu mwanaume amewahi kuivuruga sana akili yangu,”

Nilimuona yule kijana akishtuka baada ya utambulisho ule lakini nikamtoa hofu baada ya kumpa mkono. Rey hakuwa mtu wa pombe ndiyo maana akinywa kidogo inamvuruga.

“D huyu ni Dulla mwalimu wangu wa mazoezi. Nimemualika tubadilishe mazingira kidogo leo nataka kufurahia mazoezi nje ya Gym au unasemaje kipenzi?”

“Ndiyo bosi,” alijibu bila kujiamini nilitabasamu kumfanya aamini sina tatizo na hilo.

“Rey inabidi niende furahia usiku wako,” nikamgeukia yule kijana, “Oyii kuwa makini usimuache mwenyewe hakikisha anafika nyumbani salama,”

“Sawa bosi,”nikalipa bili nakuondoka.Nilijisikia mwenye hatia licha ya kujua sikuwa sababu lakini najua kwa kiasi flani nimechangia hali anayopitia.


STELLA
Nilikuwa kitandani najigeuza geuza nilishidwa kupata usingizi nikifikilia Dankan atakuwa na mwanamke usiku kucha na hivi karibuni atamvisha pete. Hayo mawazo yalivuruga tumbo langu, mama yake alikuwa sahihi itabidi niwapishe sitaweza kuvumilia hili.

Nahitaji maji, koo langu limekauka sana nataka nipate kitu cha kunituliza. Nikashuka kitandani na kutoka mpaka sebuleni nilikuwa na uhakika mama yake amelala na bosi hajarudi sikuwa na wasiwasi.

Taa za sebuleni zilikuwa na mwanga hafifu lakini niliweza kuona lilipo jokofu nikalifuata.

Nilipiga ukunga baada ya kumuona mtu, ilikuwa kidogo nidondoke mtu Yule alikuja kunidaka. Nilimpiga mangumi kifuani aniachie huku nimefumba macho,

“Usiogope dogo ni mimi,” alikuwa Dankan

“Umenishtua sana, kwani umerudi saa ngapi? nilijua utalala kwa mchumba wako”

‘Nimeongea nini sasa? Ona nimemfanya ajue nina wivu,

Tulikuwa tumesogeleana na namna alivyonishika macho yetu yalitazamana nilikumbuka mara ya mwisho kilichotokea wakati tunaangaliana nikajitoa mikononi mwake

“Kwanini uko hapa?” nilimuuliza

“Hata mimi nimekosa usingizi kama wewe,” alisema akitelemsha macho na kutazama mwili wangu

Mungu wangu nimevaa ile gauni tena na sikuwa na namna ya kujificha natakiwa kuikabili aibu yangu kwani tayari kaniona.

Na yeye alikuwa kifua wazi na chini alivaa bukta, nilibaki namtolea macho sikuwahi kumuona vile alinivutia sana alionekana mwanaume kamili mbele yangu. Nilitamani kumrukia kwenye kifua chake kilichojengeka vizuri na kumkumbatia lakini nilikumbuka natakiwa kujidhibiti na sitakiwi kufanya chochote kumuonyesha namtaka.

Nikapiga hatua mpaka lilipo fliji nikafungua na kuchukua kopo la maji, nikaona glass juu ya fliji lakini ilikuwa mbali kidogo kwa kimo changu nisingeweza kuifikia bila kusimamia viganja vya miguu yangu. Nilifanya hivyo lakini bado sikufikia, ghafla nikahisi mwili wake ukinigusa nyuma yangu akanyoosha mkono wake kuichukua kirahisi na kunipatia nauhakika alifanya makusudi kuivuruga akili yangu.

Na alifanikiwa tulitazamana tena, na kwa mara ya kwanza kwenye maisha yangu nilitamani kumkumbatia mwanaume na kumbusu lipsi zake kabla hajanitongoza wala kuniambia ananipenda.

‘Stella usifanye hivi jikaze,’ nilihisi shetani anataka kunitumia na ili kupotezea ile hali nikamimina maji na kunywa funda kubwa haraka nikameza.

“Unahitaji maji?” nilimuuliza

“Hapana nakuhitaji wewe,” kauli yake ilifanya joto la mwili wangu kupanda, alisema akipiga hatua kusogea karibu yangu zaidi kiasi niliweza kuhisi anavyonukia.

‘Jikaze Stella huyu ni mchumba wa mtu’ nilijiambia huku akili ikijitahidi kuudhibiti mwili wangu ulioingia tamaa.

“Wewe ni mrembo sana na uko vizuri kuficha hisia zako,” alisema akiweka mikono ukutani kwa namna ya kunidhibiti nisitoke. Nilihisi aibu kwa ukaribu huo nilishindwa kumtazama usoni nikaangalia chini.

Hakuwa mnyonge alijua hali nayopitia akashusha mkono mmoja nakunishika kidevu akakinyanyua nimtazame, alisogeza lipsi zake kwangu na akataka kunibusu mdomoni. nilifanikiwa kumkwepa na uso wake ukaangukia mabegani mwangu

“Unafanya nini?” nilimuuliza kwa upole, nilimsikia akishusha pumzi kwa nguvu

“Sasa mate ni kitu cha kumnyima mtu?” alinongona sikioni mwangu pumzi yake ilinisisimua mwili mzima na kauli yake ikafanya nikatabasamu, hakika alijua kuivuruga akili yangu nilihisi kuwa pale hali itakuwa mbaya zaidi nikamsukuma mbele na kupiga hatua, lakini akanishika mkono kunizuia nisiende.

“Stella nahitaji nafasi usiku wa leo, sitaki kulala na hizi ndoto mbaya,"

“Nafasi…?”

“Ndiyo ningependa…”

“Ungependa niwe kahaba wako?” nilimkatisha nakumalizia sentensi yake huku nimekunja sura,

“Hapana yaani uwe rafiki wa kufurahi nae, Stella kwanini tujipunje wakati nafasi ipo?”

Alifanikiwa kunitoa kwenye mood kweli nilikosea sijui nilitegemea nini kwa mtu huyu, nilijisikia vibaya nikamtazama kinyonge wakati huo machozi yako njiani

Nafsi iliniambia mwanaume ninaemtata hapa hayupo. Nilipotea kwenye mawazo mpaka Dan aliponishika

“Stella uko sawa?”

“Nawezaje kuwa sawa baada ya kuonekana kahaba?”

“Samahani sijamaanisha hivyo nilifikili una hisia kama zangu tufurahie na baada ya hilo tungebaki kama zamani yaani kama hakuna kilichotokea”

Ndivyo alivyo Dankan na ukweli wake unaniumiza sana. Niliminya midomo yangu lakini bado machozi yalinitoka na kuloanisha mashavu yangu, sikuwa tayari kusikia ukweli huu mchungu, nauhakika kama angenidanganya ningemkubalia.

“Samahani hatuna hiyo nafasi kwa sababu mimi sio mtu wakufanya hivyo bila kuwa na malengo mengine,” nilisema kwa uchungu.

Dankan alishangaa baada ya kuona nalia. Aliona namna maneno yake yalivyo ujeruhi moyo wangu.

“Stella samahani,” alisema akinisogelea nakuaribu kunifuta machozi. Nilitoa mkono wake na kumpita kuelekea chumbani kwangu na kufunga mlango nyuma yake. nikaegemea mlango nikilia kwa sauti.

“Stella fungua tuzungumze,”aliniita huku anagonga mlango

Sauti yake ilizidi kunichanganya nikanyanyuka pale mlangoni, nikakaa kitandani nikachukua simu yangu na kumpigia Happy ni kawaida yangu kumtafuta kila ninapokuwa na wakati mgumu. hakuchukua muda akapokea. Nilishidwa kuzungumza nikabaki nalia tu

“Bila shaka kuna tatizo haya niambie shida nini?”

“Dankan kaniomba niwe nae usiku wa leo eti tufurahishane kama marafiki,”

“Na wewe ukakubali?”

“Hapana lakini…”

“Sasa kinachokuliza kitu gani? Unajifanya kama humfahamu,”

“Kwanini aseme hivyo sasa…?”

“Ulitaka akudanganye? Akwambie anakupenda, akutumie alafu kesho umlaumu kwa kukupuuzia?”

“Nilitamani kusikia hivyo angalau kwa leo tu,”

“Stella, umechanganyikiwa?”

Happy aliongea kwa ukali na kama angekuwa karibu yangu nauhakika angenipiga kwenye bichwa langu akili ikae sawa.

“Stella, Tafadhali fungua tuzungumze” Dan alikuwa bado mlangoni akisisitiza,

“Bado yuko mlangoni, ananiita kiukweli natamani kutoka nataka kuwa nae,” nilimlalamikia Happy.

“Nahisi umerogwa, unahitaji maombi,”

“Happy niambie nifanyeje nakaribia kurukwa na akili,”

“Jitahidi kutulia hiyo ni mihemko ya muda tu,”

“Bado yuko mlangoni nawezaje kutulia?”

“Hakikisha umefunga mlango vizuri, rudi kitandani weka mziki kwenye simu yako na uvaa earphone masikio yote, hakikisha husikii sauti yake, weka mziki unaopenda na ukiweza imba. Acha leo ipite utafanya maamuzi kesho kama utakuwa tayari kuongezwa kwenye listi yake.”

“Sawa..” niliitikia kinyonge.

“Kama utakubali kutoka humo ndani jua siko upande wako na kesho utafute mtu mwingine wakumlilia. usije kuniambia huo ujinga sintokusikiliza.”

Nilisikia akishusha pumzi akaniita, “Stella…”

“Nimekuelewa” nilijitetea

“Najua rafiki yangu sio Malaya,” alisema kisha akakata simu.

Happy sio mtu wa kupindisha maneno amekuwa zaidi ya rafiki kwangu, namuona kama ndugu pekee niliyenae hapa mjini. Na haya nayopitia nisingeweza kumwambia mama yangu.

Nilifanya kama alivyoniambia. Nilivaa earphones nikaweka mziki kwa sauti kubwa nikafanikiwa kutosikia sauti ya Dan pale mlangoni. Lakini nilizidi kuumia baada ya kusikiliza mziki wa msanii Yami, alivyokuwa akilalamika Hapendwi, niliendelea kulia ni kama unaniongelea mimi.


Itaendelea....
Toa maoni yako kwenye Whatsapp no. 0682253906
Uwe miongoni mwa watakaotumiwa muendelezo wake Bureee...
 

Similar Discussions

Back
Top Bottom